Ujenzi wa Majumba ya Ufalme—Sehemu Muhimu ya Utumishi Mtakatifu
1 Tangu programu hiyo ilipoanza mnamo Septemba 1999, Majumba ya Ufalme 555 yamejengwa, mengine 21 yakafanyiwa ukarabati, na mengine 35 yakarekebishwa nchini Burundi, Kenya, Tanzania, na Uganda. Tunashukuru kwa moyo mweupe watumishi na wajitoleaji wa Majumba ya Ufalme, na wote waliowasaidia kwa ajili ya kazi ngumu waliyofanya. Ingawa kazi kubwa sana imefanywa, bado Majumba mengi ya Ufalme yanahitaji kujengwa. Sisi sote tunawezaje kuunga mkono sehemu hii muhimu ya utumishi mtakatifu tunaomtolea Yehova?—Ufu. 7:15.
2 Uwe Tayari: Ikiwa umebatizwa, tunakuomba ujitolee kufanya kazi pamoja na wajenzi wa Majumba ya Ufalme. (Zab. 110:3) Wote wanaojitolea wanapaswa kuwa tayari kufanya kazi na wawe na roho ya ushirikiano. (Zab. 133:1) Hata kama huna ujuzi wa kujenga, bado unaweza kusaidia sana katika ujenzi wa majumba. Pia huenda ukazoezwa na hivyo kutumiwa sana wakati ujao.
3 Ikiwa huwezi kujitolea, unaweza kuonyesha kwamba unaunga mkono mpango huo kwa kuwatia moyo wale wanaoweza kushiriki katika ujenzi. Unaweza kusaidia kwa kushughulikia migawo ya kutaniko ya wale wanaosaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Kwa kupanga mambo kimbele, wazee wanaweza kuhakikisha kwamba kutaniko linatunzwa vizuri baadhi ya wahubiri wanaposaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Bila shaka, Yehova anafurahi tunapofanya kazi kwa umoja ili kuendeleza mambo ya Ufalme.—Ebr. 13:16.
4 Uwe Mwenye Kutia Moyo: Kujenga majumba ya ibada kunahusisha wakati na kazi ngumu. Kwa hiyo, inaeleweka kwamba wale wanaopewa mwaliko wa kusaidia kujenga nyakati nyingine watakuwa mbali na makutaniko yao. Basi tusikose kuwapongeza na kuwatia moyo wale wanaojidhabihu kufanya ‘kazi hii ya lazima.’—Mdo. 6:3; Rom. 14:19.
5 Uwe Mwenye Usawaziko: Kazi yetu kuu inayohusiana na ibada yetu ni kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu. (Marko 13:10) Kwa sababu hiyo, wajenzi wa Majumba ya Ufalme hujitahidi kupanga kazi vizuri ili wale waliojitolea wasiwe mbali na makutaniko yao isivyo lazima. Vivyo hivyo, wajenzi hujitahidi kudumisha usawaziko wanapotimiza madaraka yao mengi. Wao hufanya mipango inayohitajiwa ili kuhakikisha kwamba migawo yao ya kutaniko itashughulikiwa na wengine wakati ambapo hawatakuwepo.
6 Mtume Paulo alisema kwamba washiriki wa kutaniko hufanya kazi pamoja kwa ushirikiano ‘kutokeza ukuzi wa mwili ili huo ujijenge wenyewe katika upendo.’ (Efe. 4:16) Kumpenda Yehova na ibada ya kweli hutuchochea tushirikiane pamoja ili habari njema ihubiriwe na tuunge mkono ujenzi wa Majumba ya Ufalme.
[Maswali ya Funzo]
1. Ni nini ambacho kimetimizwa kuhusiana na ujenzi wa Majumba ya Ufalme, lakini bado ni nini kinachohitaji kufanywa?
2. Tunawezaje kuunga mkono moja kwa moja ujenzi wa Majumba ya Ufalme?
3. Tunaweza kuonyesha kwamba tunaunga mkono mpango huo katika njia zipi nyingine?
4. Tunawezaje kuwatia moyo wale wanaoshiriki katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme?
5. Wale wanaojitolea kujenga wanawezaje kuwa wenye usawaziko?
6. Ni nini kinachotimizwa wote kutanikoni wanaposhirikiana ili kuunga mkono ibada ya kweli?