Tangazeni Kotekote Sifa Bora za Yehova
1 “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima; kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako.” (1 Nya. 29:11) Upendo na uthamini wetu kwa Yehova unatuchochea kufanya nini? Unatuchochea ‘kutangaza kotekote sifa bora zake yeye aliyetuita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ (1 Pet. 2:9) Hatuwezi kuacha kuwaambia wengine kuhusu Mungu wetu mkuu! Tutakuwa na nafasi za pekee za kutangaza sifa bora za Yehova katika miezi ya Machi, Aprili, na Mei.
2 Kampeni ya Pekee ya Kutangaza Ukumbusho: Jumatatu, Aprili 2, tutakazia sifa bora za Yehova kwa kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Mwaliko wa pekee utagawanywa ulimwenguni pote kuanzia Machi 17 hadi Aprili 2. Wote wanatiwa moyo washiriki kwa ukamili. Huo utakuwa wakati unaofaa kwa wapya kuanza kuhubiri habari njema ikiwa wanastahili. Ikiwa una mwanafunzi wa Biblia au mtoto ambaye anaweza kustahili, zungumza na wazee kuhusu jambo hilo.
3 Kampeni hiyo itakuwa kama ile iliyofanywa wakati wa Makusanyiko ya Wilaya ya “Ukombozi Unakaribia!” Makutaniko yatatumiwa mialiko ya kutosha ili kila mhubiri apate nakala 50. Kila painia anaweza kupewa nakala 150. Zungumza kwa ufupi, labda ukisema tu: “Huu ni mwaliko kwa ajili ya tukio muhimu la kila mwaka. Unakaribishwa sana. Habari kuhusu tukio hilo zimeonyeshwa katika mwaliko huu.” Bila shaka, ikiwa mwenye nyumba ana maswali, tumia wakati fulani kuyajibu. Habari kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana kwenye nyongeza ya kitabu Biblia Inafundisha ukurasa wa 206 inaweza kusaidia kujibu maswali yake. Kwenye miisho ya juma, tutatoa magazeti ya karibuni pamoja na mwaliko huo wa pekee. Fuatia upendezi wowote unaoonyeshwa na upange kurudi.
4 Ikiwezekana, mwaliko huo wa pekee unapaswa kupewa mwenye nyumba moja kwa moja. Kwa hiyo, andikeni nyumba zote ambazo watu hawapatikani na mpange kurudi wakati mwingine. Ikiwa mialiko mingi imebaki kwenye kutaniko mnaweza kuiacha katika nyumba ambazo hamuwakuti watu. Hilo linapaswa kufanywa tu juma la mwisho kabla ya Ukumbusho lakini si kabla ya hapo. Pia hakikisha kwamba ziara zako za kurudia, wanafunzi wa Biblia, watu wa ukoo, wafanyakazi wenzako, majirani, na marafiki wengine wanapata mwaliko huo.
5 Upainia Msaidizi: Je, unaweza kutangaza zaidi sifa bora za Yehova kwa kuwa painia-msaidizi miezi ya Machi, Aprili, na Mei? Huenda ukahitaji kufanya mabadiliko fulani katika ratiba yako ya kila siku ili ufaulu. (Efe. 5:15-17) Uwe na hakika kwamba ukijitahidi kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova utapata shangwe na baraka ya Yehova. (Met. 10:22) Kwa kuwa majira ya Ukumbusho yanakaribia, sasa ndio wakati wa kuanza kufanya mipango.—Met. 21:5.
6 Dada mmoja mwenye umri wa miaka 90 alifurahia pendeleo la kufanya upainia msaidizi mwaka uliopita. Alisema hivi: “Ingawa ninapenda sana kulima nami nilitaka kuanza kazi hiyo katika kipindi hicho, nilitambua kwamba nilihitaji kuchunguza mambo ninayotanguliza. Nikiwa na tamaa ya kutanguliza masilahi ya Ufalme, niliamua kufanya upainia msaidizi mwezi wa Machi.” Je, alibarikiwa kwa jitihada hizo? Alisema hivi: “Ninajihisi nikiwa sehemu ya kutaniko, na hilo limenifanya nimkaribie Yehova zaidi.” Je, tunaweza kuchunguza mambo tunayotanguliza na kufanya mabadiliko yanayohitajika?
7 Kutimiza takwa la saa 50 lililowekwa kwa ajili ya mapainia-wasaidizi si jambo gumu kama unavyoweza kufikiri. Kupitia sala chunguza utendaji wako wa kila siku, panga ratiba, kisha uiandike kwenye kalenda yako ya utendaji wa kitheokrasi. Wewe unajua hali zako vizuri. Ikiwa huna afya nzuri au nguvu, huenda ukashiriki katika huduma kwa saa chache kila siku. Ikiwa unafanya kazi kila siku au unaenda shuleni, huenda ukafaulu kufanya upainia msaidizi kwa kushiriki katika huduma wakati wa jioni au kwenye miisho ya juma.
8 Wengi wamefaulu kufanya upainia msaidizi wakiwa familia. Miaka fulani iliyopita, wenzi fulani wa ndoa walisita kujiandikisha kwa kuwa walihisi kuwa hali zao hazingewaruhusu kufanya upainia msaidizi. Walifanya nini? “Tulimwomba Yehova atusaidie kutimiza jambo ambalo tulitamani kwa muda mrefu sana.” Walipofanya mipango inayofaa walifaulu kutimiza mradi wao. Walisema hivi: “Hilo lilikuwa jambo la kupendeza sana. Tulifurahia baraka nyingi pamoja. Tunapendekeza kwamba ujaribu kujiandikisha. Ikiwa sisi tulifaulu, huenda wewe pia ukafaulu.”
9 Kwa nini msitenge wakati katika funzo lenu la familia linalofuata ili kuchunguza jinsi nyinyi nyote mnavyoweza kuongeza utendaji wenu katika miezi inayokuja? Hata ikiwa familia yote haiwezi kufanya upainia msaidizi, huenda mshiriki mmoja wa familia anaweza kufanya hivyo kupitia msaada na ushirikiano wa washiriki wengine wa familia yake. Ikiwa haiwezekani, huenda familia yenu ikajiwekea miradi ya kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma katika miezi hii ya utendaji wa pekee.
10 Saidianeni: Shauku yetu inaweza kuwaathiri wengine. Zungumza kuhusu tamaa yako ya kufanya upainia msaidizi. Huenda hilo likawatia wengine moyo wajiandikishe. Isitoshe, wale ambao wamekuwa mapainia hapo awali wanaweza kukupa mapendekezo ambayo yatakusaidia kupanga mambo yako na kupanga ratiba ili ufikie mradi wako. (Met. 15:22) Ikiwa utafaulu kufanya upainia msaidizi, mbona usimwalike mhubiri mwingine, hasa mtu aliye na hali kama zako, ajiunge nawe katika utendaji huu wenye kupendeza?
11 Wazee wengi hufanya mipango inayohitajika ili kushiriki katika utumishi huu wa pekee. (Ebr. 13:7) Kwa kweli, hilo ni jambo linalotia moyo sana kutaniko! Wazee vilevile huchochea kupitia mazungumzo yao na wengine. Huenda maneno machache tu ya kitia moyo au mapendekezo fulani yanayofaa yakawa tu jambo linalohitajika ili kuwachochea wengine kuwa mapainia-wasaidizi. Mwangalizi wa utumishi atapanga mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani ili wote waweze kushiriki katika mahubiri ya vikundi, hata baada ya kazi au shule. Mipango hiyo inapaswa kutangazwa kwa kawaida. Pia atahakikisha tuna eneo na vichapo vya kutosha.
12 Hata ikiwa hali hazikuruhusu kufanya upainia msaidizi, unaweza kuwatia moyo wote wanaojiandikisha, na unaweza kusali kwa ajili yao. (Met. 25:11; Kol. 4:12) Huenda ukafanya mipango ili kushiriki nao katika huduma siku ya ziada katikati ya juma au kuhubiri kwa saa nyingi kuliko unavyohubiri kwa kawaida.
13 Mradi wa Mapainia-Wasaidizi 6,400 Mwezi wa Aprili: Idadi kubwa zaidi ya mapainia-wasaidizi ambayo imewahi kufikiwa nchini Burundi ni 792, nchini Kenya ni 2,601, nchini Tanzania ni 1,297, na nchini Uganda ni 455. Kwa hiyo, mradi wetu mwezi wa Aprili ni kuwa na mapainia-wasaidizi 1,000 nchini Burundi, 3,300 nchini Kenya, 1,400 nchini Tanzania na 700 nchini Uganda. Tunaweza kufikia mradi huo ikiwa kwa wastani 1 kati ya wahubiri 6 katika kila kutaniko atakuwa painia-msaidizi. Bila shaka, huenda katika makutaniko fulani kukawa na wahubiri zaidi ambao hali zao zitawaruhusu kuwa mapainia-wasaidizi. Makutaniko mengi yanaweza kutimiza mradi kama huo. Wazia msisimko ambao hilo litatokeza katika kutaniko lenu na matokeo mtakayopata mnapohubiri katika eneo lenu!
14 Kwa nini Aprili ni mwezi mzuri sana wa kufanya upainia msaidizi? Ukumbusho utakuwa mwanzoni mwa mwezi huo, hivyo tutakuwa na nafasi nyingi za kuwarudia wale waliohudhuria. Tutatoa magazeti tukiwa na lengo la kuacha kitabu Biblia Inafundisha kwenye ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia. Hivyo, kufanya upainia msaidizi mwezi wa Aprili kutaandaa nafasi nyingi za kuanzisha mafunzo ya Biblia. Isitoshe, mwezi wa Aprili una Jumapili tano na sikukuu ya kilimwengu. Hilo litafanya iwe rahisi zaidi kwa wale wanaofanya kazi na kwenda shuleni kujiandikisha.
15 Kila wakati majira ya Ukumbusho yanapopita tunakaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo. Wakati uliobaki wa kuwaambia wengine kuhusu Mungu wetu mkuu umepungua. (1 Kor. 7:29) Majira haya ya Ukumbusho yakipita, nafasi zenye thamani ambazo tulipata za kumsifu Baba yetu wa mbinguni zitakuwa zimepita milele. Basi na tufanye mipango sasa ili tufanye yote tuwezayo mwezi wa Machi, Aprili, na Mei ili kutangaza kotekote sifa bora za Yehova!
[Maswali ya Funzo]
1. Ni nini kinachotuchochea kutangaza kotekote sifa bora za Yehova?
2. Ni kampeni gani ya pekee iliyopangwa kutangaza Ukumbusho, na ni nani wanaoweza kushiriki?
3. Tunaweza kusema nini ili kuwakaribisha watu kwa ajili ya ukumbusho?
4. Mwaliko huo wa pekee kwa ajili ya Ukumbusho utagawanywaje?
5. Kwa nini tunapaswa kuanza sasa kufanya mipango kwa ajili ya kufanya upainia msaidizi?
6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo lililoonwa la dada mwenye umri wa miaka 90 ambaye alifanya upainia msaidizi mwaka uliopita?
7. Je, ni vigumu kufanya upainia msaidizi?
8. Ni nini kilichowasaidia wenzi fulani wa ndoa kufanya upainia msaidizi?
9. Mnaweza kufanya nini katika funzo lenu la familia linalofuata ili kujitayarisha kwa ajili ya miezi ijayo ya utendaji wa pekee?
10. Kwa nini tuzungumze na wengine kuhusu tamaa yetu ya kufanya upainia msaidizi katika majira haya ya Ukumbusho?
11. Wazee wanaweza kuchocheaje wengine wafanye upainia msaidizi katika miezi ijayo?
12. Unaweza kufanya nini ikiwa hutaweza kufanya upainia msaidizi?
13. Ni mradi gani ambao umewekwa kwa ajili ya nchi yenu, na kutaniko lenu linaweza kuchangiaje kutimiza mradi huo?
14. Kwa nini Aprili ni mwezi mzuri wa kufanya upainia msaidizi?
15. Kwa nini tunapaswa kuwa na hisi ya uharaka majira haya ya Ukumbusho yanapokaribia?
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Je, Tunaweza Kufikia Miradi Yetu ya Mapainia-Wasaidizi Mwezi wa Aprili?
Burundi 1,000
Kenya 3,300
Tanzania 1,400
Uganda 700
◼ Chunguza mambo unayotanguliza
◼ Zungumzieni miradi yenu mkiwa familia
◼ Zungumzeni na wengine kuhusu mipango yenu