“Mwenye Furaha Ni Mtu Anayeendelea Kuvumilia Jaribu”
1 Lazima Wakristo wote wapatwe na majaribu. (2 Tim. 3:12) Majaribu yanaweza kuja kupitia magonjwa, hali ngumu ya kiuchumi, kishawishi, mnyanyaso, au kupitia njia nyingine nyingi. Majaribu yanayoletwa na Shetani yamekusudiwa kutufanya tupunguze mwendo, tupuuze huduma yetu ya Kikristo, au hata tuache kumtumikia Mungu. (Ayu. 1:9-11) Kuvumilia majaribu kunawezaje kutuletea furaha?—2 Pet. 2:9.
2 Jitayarishe kwa Ajili ya Majaribu: Yehova ametuandalia Neno lake la kweli, kutia ndani habari kuhusu maisha ya Yesu na mafundisho yake. Tunaposikiliza maneno ya Yesu na kutenda kupatana nayo, tunaweka msingi imara na hivyo kujitayarisha kwa ajili ya majaribu. (Luka 6:47-49) Pia tunapata nguvu kutokana na maandalizi mengine, kama vile undugu wetu wa Kikristo, mikutano ya kutaniko, na vichapo vinavyotegemea Biblia vya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Tunatumia kwa kawaida zawadi ambayo Mungu ametupatia ya sala.—Mt. 6:13.
3 Pia Yehova ametupa tumaini. Tunapositawisha imani yenye nguvu katika ahadi za Yehova, tumaini letu linakuwa “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Ebr. 6:19) Katika nyakati za Biblia, meli hazikuondoka bandarini bila nanga, hata hali ya hewa ilipokuwa nzuri. Dhoruba ikitokea ghafula, kutia nanga kungezuia meli isisukumwe na upepo hadi kwenye ufuo wenye mawe. Vivyo hivyo, kujenga imani katika ahadi za Mungu sasa, kutatusaidia kuwa imara dhoruba za matatizo zinapotokea. Hali ngumu zinaweza kutokea ghafula. Ingawa mwanzoni kazi ya kuhubiri ya Paulo na Barnaba ilipokewa vizuri katika Listra, hali ilibadilika haraka wapinzani Wayahudi walipowasili.—Mdo. 14:8-19.
4 Uvumilivu Hutokeza Furaha: Kudumu katika huduma yetu licha ya upinzani hutupa amani ya akili. Tunashangilia tunapohesabiwa kuwa tunastahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya Kristo. (Mdo. 5:40, 41) Kuvumilia majaribu hutusaidia kusitawisha zaidi sifa za unyenyekevu, utii, na uvumilivu. (Kum. 8:16; Ebr. 5:8; Yak. 1:2, 3) Kunatufundisha kumtegemea Yehova, ahadi zake, na kumkimbilia ili kupata ulinzi.—Met. 18:10.
5 Tunajua kwamba majaribu ni ya muda. (2 Kor. 4:17, 18) Majaribu hutupa nafasi za kuonyesha tunampenda Yehova kwa kiasi gani. Kwa kuvumilia majaribu hayo, tunaweza kujibu mashtaka ambayo Shetani anazusha. Hivyo, hatufi moyo! “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.”—Yak. 1:12.