Mabadiliko Yenye Kusisimua Katika Mnara wa Mlinzi!
1 Mapema mwaka huu, makutaniko yalipokea tangazo lenye kupendeza sana: Kuanzia Januari 2008, kutakuwa na matoleo mawili tofauti ya Mnara wa Mlinzi, moja kwa ajili ya watu wote na nyingine kwa ajili ya undugu wetu wa Kikristo! Huenda umekuwa ukijiuliza: ‘Magazeti hayo mawili yatakuwa na tofauti gani? Kuna faida gani za kuwa na matoleo tofauti? Je, tunaweza kutazamia mambo mapya katika matoleo hayo?’
2 Tofauti: Toleo la tarehe moja la kila mwezi litaitwa Toleo la Watu Wote. Makala zote katika toleo hilo zitatayarishwa kwa faida ya watu wote. Toleo la tarehe 15 la kila mwezi litaitwa Toleo la Funzo, nalo halitatolewa katika utumishi wa shambani. Litakuwa na makala zote za funzo za mwezi mmoja na makala nyingine zinazowafaa Wakristo waliojiweka wakfu. Toleo la Watu Wote la Mnara wa Mlinzi litawavutia Mashahidi lakini pia litawavutia sana watu wasio Mashahidi ambao huenda wana imani katika Biblia. Kwa upande mwingine, Amkeni! litaendelea kutolewa kwa ajili ya watu wengi zaidi, kutia ndani watu wenye shaka kuhusu Biblia na watu wa dini zisizo za Kikristo.
3 Faida: Katika Toleo la Funzo, haitakuwa lazima tena kufafanua maneno kama vile “painia” kwa njia ambayo watu wasio Mashahidi wanaweza kuelewa. Toleo hilo linaweza pia kuwa na habari ya moja kwa moja iliyotayarishwa hasa kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova na mafunzo ya Biblia yanayofanya maendeleo ya kiroho. Vipi kuhusu Toleo la Watu Wote? Kwa kuwa habari na njia ya kuandika itaelekezwa kwa faida ya watu wote, mtu ambaye si Shahidi anaweza kufurahia kusoma gazeti hilo kutoka mwanzo hadi mwisho. Bila shaka, kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova atafaidika kwa kusoma kila toleo. Kwa kuwa tutatoa gazeti moja tu la Mnara wa Mlinzi pamoja na Amkeni! moja katika utumishi wa shambani kila mwezi, tutakuwa na mwezi mzima wa kujaribu utoaji wenye matokeo zaidi.
4 Mambo Mapya: Mambo fulani mapya yamepangwa kwa ajili ya Toleo la Watu Wote la Mnara wa Mlinzi. Makala moja itazungumzia mafundisho ya msingi ya Maandiko kwa njia rahisi sana. Nyingine itaonyesha jinsi Biblia inavyoweza kusaidia familia. Kutakuwa na miradi ya kujifunza Biblia ambayo itatolewa kwa ajili ya vijana. Kila toleo litakuwa na makala inayokazia masimulizi hususa ya Biblia yanayotufundisha kuhusu utu wa Yehova.
5 Tunasali kwamba Yehova atabariki mpango huo mpya wa Mnara wa Mlinzi. Gazeti hilo, pamoja na Amkeni! na liwafikie wengine wengi wanaostahili kwa habari njema.—Mt. 10:11.