Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 11/09 kur. 5-8
  • Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Kwenye Shule ya Bweni?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Kwenye Shule ya Bweni?
  • Huduma ya Ufalme—2009
Huduma ya Ufalme—2009
km 11/09 kur. 5-8

Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Kwenye Shule ya Bweni?

1. (a) Baadhi ya wazazi hukabili matatizo gani wanapowaelimisha watoto wao? (b) Kwa nini baadhi ya wazazi huwapeleka watoto wao kwenye shule za bweni?

1 Wazazi wote wanaowajali watoto wao wanataka wawe na mwanzo mzuri maishani. Kwa hiyo, elimu nzuri na yenye usawaziko ni muhimu. Mara nyingi elimu ya ulimwengu hutokeza fursa za kazi ya kuajiriwa na huwasaidia vijana wawe watu wazima walio na uwezo wa kujiandalia mahitaji yao wenyewe na baadaye ya familia zao. Hapa Afrika Mashariki, wazazi walio Mashahidi wanakabili hali ngumu sana katika kuwaelimisha watoto wao. Kwa kawaida watu wasio Mashahidi huwapeleka watoto wao kwenye shule za bweni, zilizo na viwango vya juu vya elimu na vifaa vizuri zaidi kuliko shule nyingi za mchana. Hata hivyo, wazazi fulani huamua kuwapeleka watoto wao kwenye shule za bweni hata ingawa katika eneo lao kuna shule za mchana zilizo na kiwango cha elimu kinacholingana na cha shule za bweni.

2. (a) Ni kanuni gani muhimu inayopatikana katika Marko 8:36, ambayo lazima ifikiriwe? (b) Andiko hili linaweza kutumiwaje kuhusiana na shule za bweni?

2 Huenda mtu akauliza: ‘Ikiwa shule ya bweni inandaa elimu nzuri, kwa nini nisitumie fursa hiyo?’ Ili kujibu swali hilo, wazazi Wakristo wanapaswa kusali na kufikiria jukumu lao zito la kutunza hali ya kiroho ya watoto wao. Yesu Kristo aliuliza hivi: “Kwa kweli, mtu anapata faida gani ikiwa ataupata ulimwengu wote na kuipoteza nafsi yake?” (Marko 8:36) Hatapata faida yoyote. Kwa hiyo, ni mambo gani ambayo wazazi Wakristo wanapaswa kufikiria kabla ya kufanya uamuzi kuhusu jambo hili? Ni hatari gani ya kiroho ambayo huenda watoto wetu wakakabili wakiwa katika shule ya bweni?

3. (a) Ni hali gani zilizo katika shule za bweni leo? (b) Hali hizi zinaweza kuwaletea watoto wetu shinikizo gani?

3 Ushawishi wa Wanafunzi Wengine: Huenda shule fulani za bweni zikawa na viwango vya juu vya elimu, lakini vipi kuhusu mwenendo wa wanafunzi na walimu wa shule hizo? Wanafunzi wengi hawaoni kama ni makosa kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa. Wizi, uwongo, na udanganyifu ni mambo yanayoonwa kuwa ya kawaida. Ngono kati ya watu wa jinsia moja, habari au picha chafu (ponografia), na kuwasiliana na pepo, ni mambo ambayo yameenea sana katika shule fulani za bweni. Kwa sababu watoto wa Mashahidi hawafanyi maovu hayo, wao huteswa, kudhihakiwa, na hata kushinikizwa kuyafanya.—1 Pet. 4:4.

4. (a) Shule za bweni na vyuo fulani vinatofautianaje na shule nyingine? (b) Jambo hili linaweza kuwaathiri watoto wetu jinsi gani?

4 Lakini, huenda mtu akasema kuwa hali hizi zinapatikana katika shule zote. Hata hivyo, hali ni tofauti katika shule za bweni na vyuo fulani. Shule hizi zinawatenganisha watoto na wazazi wao. Watoto wanalazimika kula, kukaa, na kushirikiana na watoto ambao hawamheshimu Yehova wala kanuni zake za uadilifu. Wanakabili hali hizo kwa saa 24 kila siku! Polepole, hali hizo mbaya zinaweza kuathiri imani ya watoto wetu, na mwishowe hata kuwaangamiza kiroho. (1 Kor. 15:33) Msaada wa kiroho ambao unatolewa na wazazi wenye upendo unapokatizwa, watoto wanaweza kuanza kuwa wanafiki, yaani, kujiendesha kwa njia moja shuleni na kwa njia tofauti nyumbani wanapokuwa pamoja na wazazi wao.—Zab. 12:2.

5. Simulia kisa halisi kinachoonyesha hatari ya kuwapeleka watoto kwenye shule za bweni.

5 Fikiria kisa chenye kusikitisha cha mhubiri kijana aliyebatizwa, ambaye alisomea shule ya bweni. Katika mwaka wake wa kwanza, mwanafunzi mwenzake wa kike alionyesha anavutiwa naye kimapenzi. Alikataa urafiki wa msichana huyo na akawaeleza wazazi wake. Wazazi wake walimkumbusha kuhusu hatari anayokabili na wakamhimiza awe mwangalifu. Hata hivyo, kwa sababu ya kushinikizwa sana na msichana huyo na wanafunzi wenzake, mwishowe alikubali urafiki huo na akafanya uasherati kisiri. Inasikitisha kwamba aliendelea kufanya uasherati kwa muda wa mwaka mmoja na nusu hadi alipofunuliwa. Wazazi wake walihuzunika na kuumia hisia sana alipotengwa na ushirika wa kutaniko.

6. (a) Baadhi ya wazazi wanakuwa na maoni gani wanapowapeleka watoto wao kwenye shule ya bweni? (b) Kwa nini maoni haya hayafai? (c) Wazazi wanapaswa kujiuliza swali gani, na kwa nini?

6 Wazazi fulani wanafikiri kwamba watoto wao wanapojitambulisha kwa maneno na matendo kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova, hilo litawalinda na ushawishi mbaya wa wanafunzi katika shule za bweni. Wanafikiri kuwa huenda wasimamizi wa shule wasiwalazimishe watoto wao kushiriki katika ibada ya dini za uwongo au mambo mengine ya ulimwengu. Pia, wazazi hao wanafikiri kuwa wanafunzi wengine hawatawahusisha watoto wao katika mazungumzo machafu au hata mwenendo mbaya wakijitambulisha kuwa Mashahidi. Hata hivyo, mambo yaliyoonwa yanathibitisha kuwa hilo si kweli. Ni vigumu kwa kijana kufanya yaliyo sawa huku akiwa amezungukwa na vijana wasiofuata kanuni za Mungu. Kukaa pamoja na vijana wasio waamini, wenye mwenendo mbaya, na wenye roho ya ubinafsi, kunawaathiri watoto Mashahidi. Jiulize hivi: ‘Nikimpeleka mtoto wangu kwenye shule ya bweni, je, itakuwa rahisi au vigumu zaidi kwake “kuukimbia uasherati” na “matendo mengine ya mwili”?’ (1 Kor. 6:18; Gal. 5:19-21) Wazazi wanaomwogopa Mungu hufikiria jambo hili na kusali kulihusu.

7. (a) Walimu wanaweza kuwa na ushawishi gani juu ya watoto wetu? (b) Walimu huwafunza watoto wetu nini ambacho ni kinyume na andiko la Yohana 17:16?

7 Ushawishi wa Walimu: Katika shule yoyote ile, huenda kukawa na walimu walio na mwenendo mchafu, wanaotumia mamlaka yao vibaya, na hata wanaoweza kufanya ngono na wanafunzi. Katika shule za bweni huenda matendo ya walimu kama hao yasiripotiwe. Zaidi ya hayo, walimu wengi huwachochea watoto ‘wapende pesa’ na ‘waazimie kuwa matajiri.’ (1 Tim. 6:9, 10) Walimu wengine hujitahidi kwa moyo mweupe kuwafunza watoto kuwa watu wanaonufaisha jamii na wanaoweza kuchangamana vizuri na watu wa ulimwengu. Hapa pia kuna tatizo. Hiyo ni kwa sababu kanuni ambazo Wakristo huishi kulingana nazo zinatofautiana na kanuni za ulimwengu. Ingawa walimu wanawatia moyo wanafunzi wachangamane na watu wa ulimwengu huu, Yesu alisema kuwa wafuasi wake si “sehemu ya ulimwengu.”—Yoh. 17:16.

8. Ikiwa watoto wanapatwa na matatizo yoyote katika shule ya bweni, ni nini ambacho hawataweza kufanya?

8 Vipi ikiwa matatizo yanatokea shuleni wakati watoto wetu wanapojitahidi kufuata kanuni za Biblia? Ikiwa watoto wanasomea shule ya mchana na wanakaa nyumbani, wanaweza kuzungumzia matatizo hayo na wazazi wao. Wazazi nao wanaweza kuwashauri watoto wao na pia kuongea na mwalimu. Hivyo, kutoelewana na matatizo yanaweza kutatuliwa mara moja. Lakini hali ni tofauti katika shule za bweni. Katika shule hizo, nyakati zote watoto wetu wanakuwa chini ya mamlaka na mwongozo wa walimu, ambao si waabudu wa Yehova. Ikiwa watoto watasimama imara na kufuata kanuni za Kikristo, watalazimika kufanya hivyo peke yao, bila msaada wowote kutoka kwa wazazi wao.

9. (a) Kuna sheria gani katika shule za bweni ambazo watoto wetu wanalazimishwa kufuata? (b) Baadhi ya shule za bweni zimewalazimishaje watoto wetu washiriki katika ibada ya dini za uwongo? (c) Kwa nini jambo hili halikubaliki kwa wazazi Wakristo?

9 Sheria Kuhusu Kutoka Nje ya Shule: Katika shule za bweni na vyuo fulani, wanafunzi hawaruhusiwi kutoka nje ya shule. Kwa kuwa wasimamizi wengi wa shule hawaheshimu imani yetu, hawawaruhusu watoto Mashahidi wahudhurie mikutano au washiriki katika utumishi wa shambani pamoja na kutaniko lililo karibu. Mara nyingi, shule zinazoongozwa na mashirika ya dini, zinawalazimisha watoto wetu waende kanisani, na washiriki katika ibada ya dini za uwongo. Watoto hao wanalazimika kufanya mipango yao wenyewe ili kutimiza mahitaji yao ya kiroho kwa kuwa hawawezi kuhudhuria mikutano. Katika shule fulani za bweni, wanafunzi Mashahidi husoma Biblia na vitabu vingine kwa zamu. Hata hivyo, mzazi yeyote Mkristo asifikiri kuwa mpango huo unatosha kutimiza mahitaji ya kiroho ya mtoto. Lingekuwa jambo lisilo la busara kuwapeleka watoto wetu kwenye shule ambapo hawataweza kushiriki katika utendaji wa Kikristo au kufurahia ushirika pamoja na Wakristo wenzao. Pia, katika shule hizo huenda wakalazimishwa kushiriki katika ibada ndani ya kanisa la Babiloni Mkubwa, mara nyingi kinyume na mapenzi yao.—Ufu. 18:4.

10. (a) Wengine wanasema nini ili kutetea uamuzi wao wa kuwapeleka watoto katika shule ya bweni? (b) Gazeti la Mnara wa Mlinzi lilitoa onyo gani kuhusu jambo hili?

10 “Msipotoshwe”: Wazazi fulani huenda wakawa na maoni kama ya wazazi wengi wasioamini kwamba mtoto ananufaika anapoondoka nyumbani na kukaa katika shule ya bweni. Wanafikiri kwamba kufanya hivyo kutamsaidia mtoto asitawishe sifa zake mwenyewe na kujifunza kujitegemea. Ili kuonyesha kuwa ‘shule za bweni si mbaya sana,’ huenda wengine wakataja Wakristo fulani waliohudhuria shule za bweni na ambao sasa ni wazee wa kutaniko au mapainia. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1997, ukurasa wa 26, fungu la 3, liliwaonya wazazi hivi: “Paulo aliandika: ‘Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.’ (1 Wakorintho 15:33) Wazazi Wakristo hawapasi kuongozwa vibaya wafikiri kwamba watoto wao hawatapata madhara yoyote ya kiroho ikiwa wanashirikiana wakati wote na wale wasiomtumikia Mungu. Baada ya kipindi fulani cha wakati, watoto wanaomtumikia Mungu wanaweza kufanywa sugu kuelekea kanuni za Kikristo na wanaweza kupoteza uthamini wote kuelekea mambo ya kiroho. Nyakati nyingine hilo haliwi dhahiri kwa wazazi mpaka watoto wanapomaliza shule ya bweni. Mara nyingi wakati huo huwa ni kuchelewa mno kurekebisha mambo.”

11. (a) Tunawezaje kutii shauri la Waefeso 6:4 kuhusu suala la kuwapeleka watoto kwenye shule za bweni? (b) Wazazi wanawapa watoto wao ujumbe gani wanapowapeleka kwenye shule za bweni?

11 Jukumu la Wazazi: Baadhi ya wazazi wamewapa watu wa ukoo au Mashahidi wengine jukumu la kuwaangalia watoto wao wanaosomea shule ya bweni. Wao hufikiri kuwa watu hao wanaweza kufuatilia utendaji na mwenendo wa watoto wao. Hata hivyo, Paulo aliwaandikia wazazi hivi: “Nanyi, akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Wazazi wanawezaje kufuata shauri hili la neno la Mungu, ikiwa watoto wao wanaishi na mtu mwingine, au wanasomea shule ya bweni ya mbali, ambapo wazazi wanaruhusiwa kuwatembelea mara moja au mara mbili tu kwa mwezi, au watoto hawaruhusiwi kuhudhuria mikutano kwa ukawaida? Wazazi wanawapa vijana wao ujumbe gani wanapowapeleka kwenye shule kama hizo? Wanawafundisha kuwa kupata elimu nzuri ni muhimu kuliko kukusanyika kwa ajili ya ibada na kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Jambo hili linaweza kuathiri sana imani ya mtoto na hata wakati wake ujao.—2 Tim. 1:5.

12. (a) Wazazi wote wana jukumu gani kuwaelekea watoto wao? (b) Kwa nini tunahitaji kuzungumza na watoto wetu kila siku? (c) Andiko la 1 Timotheo 5:8 linakaziaje uzito wa jambo hili?

12 Wazazi walio Wakristo wakomavu wanatambua kuwa hakuna mwalimu, shule, au mtu wa ukoo anayepaswa kujitwika jukumu la kuwafunza watoto wao kuwa watumishi waliojiweka wakfu kwa Mungu. Hili ni jukumu ambalo wazazi walipewa na Mungu! (Kum. 6:6, 7; Gal. 6:5) Watoto wetu wanahitaji msaada wakati wote ili wabaki kwenye barabara ya uzima. Wanahitaji kuwa na funzo la Biblia la kawaida, kushiriki katika utumishi wa shambani, na kuhudhuria mikutano yote. Wazazi wanahitaji kuwa na watoto wao kila siku ili watambue ishara zozote zinazoonyesha kwamba wameanza kuathiriwa na ulimwengu au kudhoofika kiroho. (Met. 20:11) Bila shaka, wazazi watakubali kuwa hii si kazi rahisi. Ikiwa wazazi wanapokuwa na watoto wao nyumbani wanahitaji kujitahidi sana kuwalea, kuwaimarisha kila siku, na kusali kwa ajili yao kila wakati, vipi ikiwa wako katika shule ya bweni iliyo mbali ambapo hawawezi kupata msaada wa wazazi? Uzito wa jambo hili unakaziwa na maneno haya ya Biblia: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.”—1 Tim. 5:8.

13. (a) Wazazi wanaoishi katika maeneo ambako hakuna shule za upili, wanaweza kufanya nini? (b) Kulingana na Waefeso 6:4 na 1 Timotheo 5:8, ni nini ambacho mzazi hataweza kufanya iwapo atampeleka mtoto wake kuishi na watu wengine? (c) Mtumwa mwaminifu ametoa mashauri gani kuhusu kuwaelimisha watoto wetu?

13 Je, Kuna Suluhisho Nyingine? Wazazi wanaweza kufanya nini ikiwa wanahitaji kuamua kama watampeleka mtoto kwenye shule ya bweni au kwenye shule ya mchana isiyo na vifaa vya kutosha? Wazazi fulani ambao wamejikuta katika hali hii, wameamua kupangia masomo ya ziada kwa ajili ya watoto wao. Wazazi wengine wameamua kutenga wakati ili kuwafundisha watoto wao wenyewe, au kuwapeleka kwenye vyuo vya ufundi. Baadhi ya wazazi wameamua kuhamia eneo lililo na shule nzuri za upili za mchana. Ikiwa hayo hayawezekani, na wazazi wamruhusu mtoto wao aishi na watu wa ukoo au na marafiki walio Mashahidi, basi wanapaswa kutambua kwamba wao ndio watakaowajibika kwa chochote kitakachotokea. (Efe. 6:4) Kabla ya kufanya uamuzi, itakuwa vyema kwa wale wanaoishi katika maeneo ambako hakuna shule za upili kufikiria kwa uzito mashauri hayo mazuri yanayotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45; 1 Tim. 3:2; w88 9/1 28-30; w82-SW 12/1 23; w70-E 12/1 732-735.

14. Wazazi wanaweza kufanya nini ikiwa ni lazima watoto wasomee shule ya mchana isiyo na vifaa vya kutosha?

14 Mambo yaliyoonwa yanaonyesha kuwa watoto wa Mashahidi hufanya vizuri shuleni wanapokuwa na tamaa na bidii ya kujifunza, hata ikiwa shule wanayosomea ni ya mchana na haina vifaa vya kutosha. Pia, watoto wanafaidika wazazi wanapohangaikia masomo yao. Wanaweza kufanya hivyo kwa kujuana na walimu na hata kuwaomba mashauri ya jinsi watoto wao wanavyoweza kuwa wanafunzi bora. Hata walimu wa shule ambazo hazina vifaa vya kutosha wanaweza kuchochewa kuongeza bidii ili kuwasaidia watoto wa Mashahidi.

15. Wakristo wakomavu wanaionaje elimu?

15 Wazazi wanaomtumikia Mungu wanataka watoto wao wapate elimu ili waweze kujitegemeza na pia kutimiza jukumu lao la Kimaandiko wakiwa watumishi wa Mungu. Kwa hiyo, wanataka watoto wao wawe na uwezo wa kufikiri, na waweze kuongea, kusoma, na kuandika vizuri. Pia, wanataka watoto wao wawe na uwezo wa kutumia vizuri Maandiko na vitabu vinavyotegemea Biblia ili waweze kufanya maendeleo ya kiroho na kushiriki kikamili katika huduma. (1 Tim. 4:15; 2 Tim. 2:15) Maelfu ya watoto wa Mashahidi wamefaulu kufanya hivi bila kusomea shule za bweni au vyuo, ambavyo vinaweza kuharibu hali yao ya kiroho.

16. (a) Mzazi anayeamua kuhatarisha hali ya kiroho ya mtoto wake kwa kumpeleka katika shule ya bweni, hudhihirisha nini? (b) Ni nini ambalo si jambo muhimu hapa? (c) Ni jambo gani lililo muhimu kuliko mapendeleo ya utumishi ambayo huenda Mkristo akapoteza kwa kuwapeleka watoto wake kwenye shule ya bweni?

16 Kwa kufikiria hatari zinazohusika, wazazi Wakristo hawaweki mfano mzuri wanapowapeleka watoto wao kwenye shule za bweni au vyuo fulani vinavyowanyima nafasi ya kuhudhuria mikutano ya kila juma na kushiriki katika utumishi wa shambani. Kufanya hivyo kunaonyesha ukosefu wa hekima na ukomavu, kwa hiyo, uamuzi kama huo unaweza kufanya Mkristo asistahili kuwa mzee, mtumishi wa huduma, au painia. (1 Tim. 3:1-5, 12, 13; Tito 1:5-9) Je, hilo linamaanisha kuwa Mkristo ambaye hana mapendeleo katika kutaniko anaweza kuwapeleka watoto wake kwenye shule ya bweni? La! Wazazi Wakristo waliokomaa wanaelewa kanuni za Kimaandiko zinazohusu jambo hili, na wanatambua kwamba jambo lililo muhimu hapa si kupata au kupoteza mapendeleo kwa sababu ya kuwapeleka watoto kwenye shule ya bweni, bali ni kulinda hali nzuri ya kiroho ya watoto wao. Wazazi Wakristo walio na “akili ya Kristo” wanahangaikia zaidi kuwasaidia watoto wao wapate uzima wa milele kuliko mapendeleo yoyote wanayoweza kupata katika kutaniko, au faida zozote za kifedha ambazo huenda wakapata baadaye kwa sababu waliwapeleka watoto wao kwenye shule hizo.—1 Kor. 2:16; Flp. 1:10.

17. Kuhatarisha hali ya kiroho ya mtoto ili apate elimu bora ni sawa na kufanya nini?

17 Utafanya Nini? Kwa kuwa, uzima wa milele wa watoto wetu unahusika, wazazi wanapaswa kufikiria kwa uzito na kusali kuhusu hatari zinazohusika kabla ya kuamua kama watawapeleka watoto wao kwenye shule ya bweni au la. Kufanya hivyo kunaweza kufananishwa na mtu anayeingia ndani ya nyumba inayowaka moto ili aokoe kitu fulani chenye thamani, lakini anakufa humo ndani. Halingekuwa jambo la busara hata kidogo kuhatarisha hali ya kiroho ya mtoto ili kupata faida ambayo huenda ikatokana na elimu ya shule ya bweni!—Mt. 16:26.

18. (a) Ni shauri gani lenye hekima linalopatikana katika Methali 22:3? (b) Tunaweza kufuataje shauri la andiko hilo?

18 Neno la Mungu linasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Met. 22:3) Wazazi wote Wakristo, na watumie hekima inayotoka juu na ‘kuona msiba’ ili kulinda hali ya kiroho ya watoto wao. Kwa kuwa, “mwisho wa mambo yote umekaribia,” wazazi Wakristo wanapaswa kufikiria kwa uzito na kusali kuhusu swali hili, Je, nimpeleke mtoto wangu kwenye shule ya bweni?—1 Pet. 4:7.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki