Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
DESEMBA 7-13
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 10-11
“Mpende Yehova Kuliko Familia”
it-1 1174
Haramu
Moto na Uvumba Haramu. Katika Mambo ya Walawi 10:1, neno la Kiebrania zar (jinsia ya kike, za·rahʹ; kihalisi, ajabu) hutumiwa kuhusu “moto haramu” ambao wana wa Haruni, Nadabu na Abihu, walimtolea Yehova “jambo ambalo hakuwaamuru wafanye” na kwa sababu hiyo akawateketeza kwa moto. (Law 10:2; Hes 3:4; 26:61) Kisha Yehova akamwambia hivi Haruni: “Msinywe divai au kileo chochote mnapoingia katika hema la mkutano, msije mkafa. Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu. Ili muweze kutofautisha mambo matakatifu na mambo yaliyo najisi, mambo safi na mambo yasiyo safi, na ili muwafundishe Waisraeli wote sheria zote ambazo Yehova amewaambia kupitia Musa.” (Law 10:8-11) Maneno hayo yanaonyesha kwamba huenda Nadabu na Abihu walikuwa wamelewa, hali iliyofanya watoe moto haramu ambao Yehova hakuwa ameamuru. Huenda moto huo ulikuwa haramu kwa sababu ya wakati uliotolewa, eneo, au jinsi ulivyotolewa, au huenda uvumba uliotumiwa haukuwa na viungo vinavyotajwa katika Kutoka 30:34, 35. Matumizi yao ya kileo hayakuwa kisingizio cha kutenda dhambi.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 111 ¶5
Wanyama
Maagizo kuhusu vyakula yaliwahusu wale wote waliokuwa chini ya Sheria ya Musa, kwa kuwa Mambo ya Walawi 11:8 inasema hivi: “Hao si safi kwenu,” yaani, kwa Waisraeli. Sheria ilipokoma kwa msingi wa kifo cha kidhabihu cha Kristo Yesu, vizuizi vyote viliondolewa, na kwa mara nyingine wanadamu wote wangeweza kustahili tena maandalizi aliyoambiwa Noa baada ya Gharika.—Kol 2:13-17; Mwa 9:3, 4.
DESEMBA 14-20
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 12-13
“Jifunze Kutokana na Sheria Kuhusu Ukoma”
it-2 238 ¶3
Ukoma
Katika mavazi na nyumba. Ukoma ungeweza pia kuathiri vazi la sufu au la kitani, au kitu chochote cha ngozi. Ugonjwa huo ungeweza kuondolewa kwa kuosha kitu kilichoathiriwa, na pia mipango ilifanywa ya kukitenga. Hata hivyo, ikiwa kiliendelea kuwa na doa lenye mchanganyiko wa rangi ya manjano na kijani au doa jekundu, basi kilikuwa na ukoma hatari na kilipaswa kuchomwa moto. (Law 13:47-59) Ikiwa ukuta wa nyumba ungekuwa na sehemu zilizobonyea zenye mchanganyiko wa rangi ya manjano na kijani au rangi nyekundu, kuhani angeifunga nyumba hiyo. Katika visa vingine, mawe yaliyoathiriwa yalibomolewa na sehemu ya ndani ya nyumba hiyo ilikwanguliwa, kisha lipu na saruji iliyoondolewa ilitupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi. Ikiwa ukoma ungeirudia tena nyumba hiyo, ilikuwa si safi na ilibomolewa, na vitu vyote vilivyotumiwa kuijenga vilitupwa mahali pasipo safi. Hata hivyo, nyumba ilipotangazwa kuwa safi, ilitakaswa kulingana na utaratibu uliowekwa. (Law 14:33-57) Inasemekana kwamba ukoma ulioathiri nguo au nyumba ulikuwa aina fulani ya ukungu au kuvu; hata hivyo, hakuna uthibitisho kamili kuhusu madai hayo.
DESEMBA 21-27
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 14-15
“Usafi Ni Takwa Katika Ibada Safi”
it-1 263
Kuoga
Waisraeli walipaswa kuoga ili kujitakasa kisherehe kwa sababu mbalimbali. Mtu yeyote aliyepona ukoma, mtu yeyote aliyegusa vitu vilivyoguswa na mtu yeyote “anayetokwa na umajimaji,” mwanamume aliyetokwa na shahawa, mwanamke aliyetokwa na damu ya hedhi au damu, au yeyote aliyefanya ngono, ‘hakuwa safi’ na alipaswa kuoga. (Law 14:8, 9; 15:4-27) Mtu aliyeingia katika hema iliyokuwa na, au aliyegusa, maiti ya mwanadamu ‘hakuwa safi’ na alipaswa kujitakasa kwa maji ya kujitakasa. Yeyote aliyekataa kutii sheria hiyo, alipaswa ‘kuuawa kutoka kutanikoni kwa sababu alichafua mahali patakatifu pa Yehova.’ (Hes 19:20) Hivyo, inafaa kwamba kujisafisha hutumiwa kwa njia ya mfano kumaanisha kuwa na msimamo safi mbele za Yehova. (Zb 26:6; 73:13; Isa 1:16; Eze 16:9) Kuoshwa na neno la Yehova la kweli, linalofananishwa na maji, kunaweza kutusafisha.—Efe 5:26.
it-2 372 ¶2
Hedhi
Mwanamke alionwa pia kuwa si safi kwa muda wote ambao angetokwa na damu wakati ambao si wa hedhi au “akitokwa na damu kwa muda unaozidi kipindi chake cha hedhi,” kitanda chochote alicholalia na kitu chochote anachokalia pamoja na watu waliogusa vitu hivyo watakuwa si safi. Baada ya damu kukoma kutoka kwa muda unaozidi wa kawaida, alipaswa kuhesabu siku saba, kisha angekuwa safi. Katika siku ya nane, mwanamke huyo angeleta njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga na kumpa kuhani aliyetoa dhabihu kwa niaba yake, ndege mmoja kama dhabihu ya dhambi na mwingine kama dhabihu ya kuteketezwa.—Law 15:19-30; tazama SAFI, USAFI.
it-1 1133
Mahali Patakatifu
2. Hema la mkutano na, baadaye hekalu. Mpango wote, kutia ndani ua wa hema la ibada na nyua za hekalu, yalikuwa maeneo matakatifu. (Kut 38:24; 2Nya 29:5; Mdo 21:28) Vitu vya msingi vilivyokuwa katika ua vilitia ndani madhabahu ya dhabihu na beseni la shaba. Vitu hivyo vilikuwa vitakatifu. Watu waliokuwa safi kisherehe ndio tu walioruhusiwa kuingia wakati wowote katika ua wa hema la ibada; vivyo hivyo, hakuna mtu ambaye hakuwa safi aliyeruhusiwa kuingia katika nyua za hekalu. Kwa mfano, mwanamke asiye safi hakupaswa kugusa kitu chochote kitakatifu au kukaribia mahali patakatifu. (Law 12:2-4) Inaonekana pia kwamba hema la ibada lilitiwa unajisi kwa sababu tu ya Waisraeli kuendelea kuwa wachafu kwa muda mrefu. (Law 15:31) Watu waliotoa matoleo ya kujitakasa ukoma wangeweza kuleta matoleo hayo hadi tu kwenye lango la hema la ibada. (Law 14:11) Mtu asiye safi hakupaswa kula dhabihu ya ushirika katika hema la ibada au hekalu, na yeyote aliyekataa kutii amri hiyo aliuawa.—Law 7:20, 21.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 665 ¶5
Sikio
Wakati wa sherehe ya kuwekwa rasmi kwa makuhani katika Israeli, Musa aliagizwa achukue damu ya kondoo dume na kuipaka katika ncha ya sikio la kulia la Haruni na la kila mmoja wa wana wake, na pia kwenye mkono wa kulia na mguu wa kulia, ili kuonyesha kwamba chochote walichosikiliza, kazi waliyofanya, na mwenendo wao ulipaswa kupatana na utumishi wao. (Law 8:22-24) Pia, katika kisa cha mtu aliyejitakasa ukoma, Sheria ilisema kuhani alipaswa kupaka kiasi kidogo cha damu ya kondoo dume aliyetolewa kama dhabihu ya hatia, pamoja na kiasi fulani cha mafuta yaliyotolewa, kwenye sikio la kulia la mtu huyo aliyekuwa na ukoma. (Law 14:14, 17, 25, 28) Utaratibu kama huo unatajwa kuhusu mwanamume aliyetaka kuendelea kuwa mtumwa kwa bwana wake maisha yake yote. Katika kisa hicho, mtumwa huyo aliletwa kwenye mwimo wa mlango, kisha bwana wake alitoboa sikio la mtumwa huyo kwa kutumia sindano. Alama hiyo ya kudumu katika kiungo cha kusikia, iliwakilisha tamaa ya mtumwa huyo ya kuendelea kumtumikia bwana wake kwa utii.—Kut 21:5, 6.
DESEMBA 28–JANUARI 3
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 16-17
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 226 ¶3
Azazeli
Kama mtume Paulo alivyoeleza, Yesu alipotoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi za wanadamu, alitimiza mengi zaidi ya yaliyotimizwa na “damu ya ng’ombe dume na ya mbuzi.” (Ebr 10:4, 11, 12) Kwa njia hiyo akawa yule “anayesingiziwa makosa ya wengine,” na ‘aliyebeba magonjwa yetu,’ yule ambaye “alichomwa kwa sababu ya makosa yetu.” (Isa 53: 4, 5; Mt 8:17; 1Pe 2:24) ‘Alichukua’ dhambi za wote wanaoonyesha imani katika thamani ya dhabihu yake. Alionyesha uandalizi wa Mungu wa kuondoa dhambi kabisa. Kwa njia hizo, mbuzi “wa Azazeli” anafananisha dhabihu ya Yesu Kristo.