Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
JULAI 5-11
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 11-12
“Jinsi Yehova Anavyotaka Kuabudiwa”
it-2 1007 ¶4
Nafsi
Kutumikia kwa Nafsi Yote. Kama iliyoonyeshwa tayari, “nafsi” inarejelea mtu mwenyewe. Hata hivyo maandiko fulani yanatuambia tumtafute, tumpende, na kumtumikia Mungu ‘kwa moyo wetu wote na kwa nafsi yetu yote’ (Kum 4:29; 11:13, 18), na Kumbukumbu la Torati 6:5 inasema hivi: “Ni lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” Yesu alisema ni lazima tumtumikie Yehova kwa nafsi yote na nguvu na akaongezea kusema, “kwa akili yako yote.” (Mk 12:30; Lu 10:27) Basi swali linajitokeza kwa nini mambo hayo mengine yanatajwa pamoja na nafsi, ikiwa nafsi inatia ndani vitu hivyo vyote. Tutoe mfano ili kufafanua hilo: Mtu anaweza kununuliwa na mtu mwingine kuwa mtumwa (nafsi yake), kwa njia hiyo anakuwa mali ya mmiliki wake ambaye pia ni bwana wake. Lakini huenda asimtumikie bwana wake kwa moyo wote, akichochewa kabisa na tamaa ya kumpendeza, na hivyo huenda asitumie nguvu zake zote au akili yake yote kuendeleza faida za bwana wake. (Linganisha Efe 6:5; Kol 3:22.) Hivyo, mambo hayo mengine yanatajwa ili tuyakazie uangalifu na tusiyasahau au kukosa kuyatumia katika utumishi wetu kwa Mungu, kwa kuwa sisi ni mali yake, na kwa Mwana wake, ambaye alitoa uhai wake kama fidia ili kutununua. Kumtumikia Mungu kwa “nafsi yote” kunahusisha kila sehemu ya mtu, hakuna sehemu ya mwili, utendaji, uwezo, au tamaa ambayo haipaswi kuhusishwa.—Linganisha Mt 5:28-30; Lu 21:34-36; Efe 6:6-9; Flp 3:19; Kol 3:23, 24.
it-1 84 ¶3
Madhabahu
Waisraeli waliagizwa wabomoe madhabahu zote za kipagani na kuharibu nguzo na miti mitakatifu ambayo kwa kawaida ilijengwa kando yake. (Kut 34:13; Kum 7:5, 6; 12:1-3) Hawakupaswa kujenga vitu kama hivyo wala kuwateketeza motoni watoto wao kuwa dhabihu kama Wakanaani walivyofanya. (Kum 12:30, 31; 16:21) Badala ya kuwa na madhabahu nyingi, taifa la Israeli lilipaswa kuwa na madhabahu moja tu kwa ajili ya kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli, na madhabahu hiyo ingekuwa mahali ambapo Yehova angechagua. (Kum 12:2-6, 13, 14, 27; linganisha hilo na Babiloni, ambalo lilikuwa na madhabahu 180 kwa ajili ya mungu wa kike Ishta pekee.) Mwanzoni waliagizwa kujenga madhabahu ya mawe ambayo hayajachongwa baada ya kuvuka Mto Yordani (Kum 27:4-8), na Yoshua alijenga madhabahu hiyo juu ya Mlima Ebali. (Yos 8:30-32) Baada ya kushinda na kugawanya nchi ya ahadi, makabila ya Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase yalijenga madhabahu kubwa kando ya Mto Yordani, ambayo kwa muda ilisababisha vurugu kati ya makabila yale mengine hadi ilipoamuliwa kwamba madhabahu hiyo si ishara ya kwamba walikuwa wameasi imani, bali ilikuwa ukumbusho wa uaminifu wao kwa Yehova akiwa Mungu wa kweli.—Yos 22:10-34.
Hazina za Kiroho
it-1 925-926
Gerizimu, Mlima
Kupatana na maagizo yaliyotolewa na Musa, makabila ya Israeli yalikusanyika kwenye Mlima Gerizimu na Mlima Ebali chini ya uongozi wa Yoshua muda mfupi baada ya kushinda jiji la Ai. Wakiwa hapo, watu walisikiliza waliposomewa baraka ambazo wangepata ikiwa wangemtii Yehova na laana ambazo wangepata ikiwa wangekosa kumtii. Makabila ya Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, Yosefu, na Benjamini yalisimama mbele ya Mlima Gerizimu. Walawi wakiwa pamoja na sanduku la agano walikuwa bondeni, na makabila yale mengine sita yalikuwa mbele ya Mlima Ebali. (Kum 11:29, 30; 27:11-13; Yos 8:28-35) Inaonekana kwamba makabila yaliyokuwa mbele ya Mlima Gerizimu yalijibu baada ya baraka kusomwa kuelekea upande wao, kisha yale makabila mengine yalijibu baada ya laana kusomwa kuelekea upande wa Mlima Ebali. Ingawa imesemwa kwamba baraka zilisomwa kuelekea Mlima Gerizimu kwa sababu mlima huo ni maridadi zaidi na wenye rutuba, tofauti na Mlima Ebali ambao kwa sehemu kubwa una miamba isiyo na rutuba, Biblia haitoi habari zozote kuhusu jambo hilo. Sheria ilisomwa kwa sauti “mbele ya kutaniko lote la Israeli, lililotia ndani wanawake, watoto, na wakaaji wageni walioishi miongoni mwao.” (Yos 8:35) Wakiwa mbele ya milima yote miwili umati huo mkubwa ungeweza kusikia maneno yaliyosomwa popote walipokuwa wamesimama. Huenda hilo liliwezekana kwa sababu eneo hilo lina uwezo mzuri wa kusambaza sauti.—Ona EBALI, MLIMA.
JULAI 12-18
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 13-15
“Jinsi Sheria Ilivyothibitisha Yehova Anawajali Maskini”
it-2 1110 ¶3
Sehemu ya Kumi
Inaonekana kwamba kulikuwa na sehemu nyingine ya kumi, ambayo ilitolewa kila mwaka kwa makusudi ambayo hayakuhusisha kutegemeza ukuhani wa Walawi, ingawa Walawi walishiriki. Kwa kawaida ilitolewa na kufurahiwa kwa njia kubwa na familia za Waisraeli walipokutana kwa ajili ya sherehe zao za kitaifa. Katika visa ambavyo ilikuwa mbali sana kusafirisha sehemu hiyo ya kumi hadi Yerusalemu, mazao yalibadilishwa kuwa pesa ambazo zingetumiwa Yerusalemu ili kuiandalia familia hiyo chakula na kujifurahisha wakati wa makusanyiko matakatifu. (Kum 12:4-7, 11, 17, 18; 14:22-27) Mwishoni mwa kila mwaka wa tatu na mwaka wa sita wa mzunguko wa sabato wa miaka saba, badala ya sehemu hiyo ya kumi kutumiwa kulipia gharama wakati wa makusanyiko ya kitaifa, ilitengwa kwa ajili ya Walawi, wakaaji wageni, wajane, na mayatima walioishi miongoni mwao.—Kum 14:28, 29; 26:12.
it-2 833
Mwaka wa Sabato
Mwaka wa Sabato uliitwa “mwaka wa kufuta madeni [hash·shemit·tahʹ].” (Kum 15:9; 31:10) Mwaka huo nchi ilipumzika kabisa bila kulimwa. (Kut 23:11) Watu walipaswa pia kufuta madeni ya wenzao. Madeni hayo ‘yalifutwa kwa agizo la Yehova,’ ili kumtukuza. Ingawa wengine wana maoni tofauti, wasomi fulani wanasema kwamba madeni hayakufutwa kabisa, bali mtu aliyekuwa akidai hangeweza kumshinikiza Mwebrania mwenzake alipe deni, kwa kuwa wakulima hawakupata mapato yoyote katika mwaka huo; hata hivyo mkopeshaji angeweza kumshinikiza mgeni alipe deni. (Kum 15:1-3) Marabi fulani wanasema kwamba mtu alipokopa ili kumsaidia ndugu aliyekuwa maskini angefutiwa deni lake, lakini madeni kwa sababu ya shughuli za kibiashara yalionwa kwa njia tofauti. Inasemekana kwamba katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, Hillel alianzisha utaratibu wa mkopeshaji kwenda mahakamani ili kuhakikisha kwamba deni lingelipwa kwa kufanya mkataba fulani.—The Pentateuch and Haftorahs, kilichohaririwa na J. Hertz, London, 1972, uku. 811, 812.
it-2 978 ¶6
Mtumwa
Sheria zilizoongoza uhusiano kati ya mtumwa na bwana wake. Kwa Waisraeli, hali ya mtumwa Mwebrania ilitofautiana na mtumwa aliyekuwa mgeni. Ingawa mtumwa ambaye hakuwa Mwebrania aliendelea kuwa mali ya mmiliki wake, na mwana angeweza kurithi mtumwa huyo kutoka kwa baba yake (Law 25:44-46), mtumwa Mwebrania alipaswa kuachiliwa katika mwaka wa saba wa utumwa wake au wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50, ikitegemea ni mwaka upi uliokuja kwanza. Mtumwa Mwebrania alipaswa kutendewa kama mfanyakazi wa kuajiriwa wakati wa kipindi chote ambacho angekuwa mtumwa. (Kut 21:2; Law 25:10; Kum 15:12) Mwebrania aliyemilikiwa kama mtumwa na mkaaji mgeni, na familia ya mkaaji huyo mgeni, au na mgeni mwingine, angeweza kukombolewa wakati wowote. Angeweza kujikomboa au akombolewe na mtu mwenye haki ya kumkomboa. Bei ya ukombozi ilitegemea idadi ya miaka iliyobaki kabla ya Mwadhimisho wa Miaka 50 au hadi mwaka wa saba wa utumwa wake. (Law 25:47-52; Kum 15:12) Alipokuwa akimweka huru mtumwa Mwebrania, bwana wake alipaswa kumpa zawadi ya kumsaidia kuanza maisha yake akiwa mtu huru. (Kum 15:13-15) Ikiwa mtumwa alikuja akiwa na mke, aliondoka pamoja na mke wake. Hata hivyo, ikiwa bwana wake alimpa mke (ni wazi alikuwa mke ambaye si Mwebrania naye hakuwa na haki ya kuwekwa huru katika mwaka wa saba wa utumwa wake), mke huyo na watoto wake waliendelea kuwa mali ya bwana wake. Katika hali kama hiyo, mtumwa Mwebrania angeweza kuchagua kubaki na bwana wake. Sikio lake lingetobolewa kwa sindano ili kuonyesha kwamba angeendelea kuwa mtumwa milele.—Kut 21:2-6; Kum 15:16, 17.
JULAI 19-25
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 16-18
“Kanuni za Kuhukumu kwa Uadilifu”
it-1 343 ¶5
Upofu
Upofu ulitumiwa kuwa mfano wa ukosefu wa haki kwa kupotosha hukumu, na Sheria ilisema mambo mengi ya kukataza kutoa rushwa, zawadi, au upendeleo, kwa kuwa vitu kama hivyo vingempofusha hakimu na kumzuia kutekeleza haki bila upendeleo. “Rushwa huwapofusha watu wanaoona vizuri.” (Kut 23:8) “Rushwa hupofusha macho ya wenye hekima.” (Kum 16:19) Hakimu, hata awe mnyoofu au mwenye utambuzi kadiri gani, anaweza kuathiriwa na zawadi kutoka kwa wahusika wa kesi, iwe anajua au kwa kutojua. Inafaa kwamba sheria ya Mungu haikazii tu kwamba zawadi ina uwezo wa kupofusha, bali pia hisia za huruma zina uwezo huo, inaposema: “Usiwabague maskini au kuwapendelea matajiri. Unapaswa kumhukumu mwenzako kwa haki.” (Law 19:15) Kwa hiyo, hakimu hakupaswa kutoa uamuzi dhidi ya matajiri kwa sababu tu walikuwa matajiri au kwa kuchochewa na hisia za huruma au ili tu apendwe na watu.—Kut 23:2, 3.
it-2 511 ¶7
Namba, Tarakimu
Mbili. Mara nyingi namba mbili huonekana katika hali za kisheria. Masimulizi yanayopatana ya mashahidi wawili huongezea uzito wa ushahidi unaotolewa. Mashahidi wawili, au hata watatu, walihitajika ili kuthibitisha jambo mbele ya mahakimu. Kanuni hiyo inatumika pia katika kutaniko la Kikristo. (Kum 17:6; 19:15; Mt 18:16; 2Ko 13:1; 1Ti 5:19; Ebr 10:28) Mungu alifuata kanuni hiyo alipomtambulisha Mwana wake mbele ya watu kuwa Mkombozi wa wanadamu. Yesu alisema hivi: “Katika Sheria yenu imeandikwa: ‘Ushahidi wa watu wawili ni wa kweli.’ Mimi ninatoa ushahidi juu yangu mwenyewe, na Baba aliyenituma hutoa ushahidi kunihusu.”—Yoh 8:17, 18.
it-2 685 ¶6
Kuhani
Makuhani hasa ndio waliopewa pendeleo la kufafanua sheria ya Mungu, na walitimiza fungu muhimu wakiwa mahakimu katika Israeli. Katika majiji ambayo waligawiwa makuhani waliwasaidia mahakimu, nao pia walitumika wakiwa mahakimu katika kesi ngumu kupita kiasi ambazo mahakama za chini zilishindwa kufanya maamuzi. (Kum 17:8, 9) Ikiwa mtu angeuawa na isijulikane aliuawa na nani, makuhani walipaswa kuwepo wanaume wazee wa jiji waliposhughulikia kesi hiyo, ili kuhakikisha utaratibu unaofaa ulifuatwa na hivyo kuondoa hatia ya damu katika jiji hilo. (Kum 21:1, 2, 5) Mume mwenye wivu alipomshtaki mke wake kwa kufanya uzinzi kwa siri, mke alipaswa kuletwa kwenye hema la ibada, ambapo kuhani angefuata utaratibu ulioonyeshwa katika sheria uliokusudia kumwomba Yehova ahukumu moja kwa moja kwa kuwa Yeye alijua ikiwa mwanamke huyo alikuwa na hatia au la. (Hes 5:11-31) Katika visa vyote, hukumu iliyotolewa na makuhani au mahakimu waliowekwa rasmi ilipaswa kuheshimiwa; kukataa kimakusudi kuiheshimu au kuitii kungeleta adhabu ya kifo.—Hes 15:30; Kum 17:10-13.
Hazina za Kiroho
it-1 787
Kufukuza
Kulingana na sheria, ili hukumu ya kifo itekelezwe, kosa lilipaswa kuthibitishwa na angalau mashahidi wawili. (Kum 19:15) Mashahidi hao walipaswa kuwa wa kwanza kumpiga kwa mawe yule mtu mwenye hatia. (Kum 17:7) Kufanya hivyo kungeonyesha bidii yao kwa ajili ya kutekeleza sheria ya Mungu na kudumisha usafi wa kutaniko la Israeli na pia kungewazuia watu wasitoe ushahidi wa uwongo, ovyoovyo, au bila kufikiri.
BORESHA HUDUMA YAKO
it-1 519
Mahakama, Hukumu
Kutaniko la Kikristo. Ingawa kutaniko la Kikristo halina mamlaka ya kisheria kutenda kama mahakama, linaweza kuchukua hatua dhidi ya washiriki wanaohitaji nidhamu ya kiroho, na hata linaweza kuwaondoa kutanikoni. Hivyo, mtume Paulo aliliambia kutaniko, yaani, wale wanaoongoza na ambao wanaliwakilisha, kwamba wanapaswa kuwahukumu wale walio ndani ya tengenezo. (1Ko 5:12, 13) Paulo na Petro walipokuwa wakiyaandikia makutaniko na pia waangalizi, walisema kwamba wazee wanapaswa kuangalia kwa uangalifu hali ya kiroho ya kutaniko na kumsaidia au kumhimiza yeyote ambaye angechukua hatua isiyofaa au isiyo ya hekima. (2Ti 4:2; 1Pe 5:1, 2; linganisha Gal 6:1.) Wowote ambao wangesababisha migawanyiko au madhehebu walipaswa kuonywa mara ya kwanza na ya pili kabla ya kutaniko kuwachukulia hatua. (Tit 3:10, 11) Lakini watu waliozoea kutenda dhambi walipaswa kuondolewa, kufukuzwa kutoka kutanikoni. Kufanya hivyo ni ishara ya kutiwa nidhamu, kuwaonyesha wakosaji kwamba zoea lao la dhambi haliwezi kuvumiliwa kutanikoni. (1Ti 1:20) Paulo anawaagiza wanaume walio na jukumu la kutenda kama mahakimu kutanikoni kwamba wanapaswa kukutana ili kusikiliza jambo hilo. (1Ko 5:1-5; 6:1-5) Wanapaswa kukubali shtaka kuwa la kweli ikiwa tu kuna mashahidi wawili au watatu, wakipima ushahidi bila kuhukumu kimbele, na bila kufanya jambo lolote kwa upendeleo.—1Ti 5:19, 21.
JULAI 26–AGOSTI 1
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 19-21
“Uhai wa Mwanadamu Ni Wenye Thamani kwa Yehova”
it-1 344
Damu
Mwanadamu ana haki ya kufurahia uhai ambao Mungu alimpa, na yeyote aliyemnyang’anya uhai huo aliwajibika mbele za Mungu. Hilo lilionekana Mungu alipomwambia Kaini hivi: “Damu ya ndugu yako inanililia kwa sauti kutoka ardhini.” (Mwa 4:10) Mtu anayemchukia ndugu yake, na hivyo kutamani afe, au kumchongea au kutoa ushahidi wa uwongo dhidi yake, na hivyo kuhatarisha uhai wake, angejiletea hatia kuhusiana na damu ya ndugu yake.—Law 19:16; Kum 19:18-21; 1Yo 3:15.
Hazina za Kiroho
it-1 518 ¶1
Mahakama, Hukumu
Mahakama za chini zilikuwa kwenye lango la jiji. (Kum 16:18; 21:19; 22:15, 24; 25:7; Ru 4:1) Neno “lango” linamaanisha eneo la wazi ndani ya jiji lililokuwa karibu na lango. Malango yalikuwa maeneo ambapo Sheria ilisomwa mbele ya watu waliokusanyika na ambapo maagizo kutoka kwa wenye mamlaka yalitangazwa. (Ne 8:1-3) Kwa kuwa watu wengi wangeingia na kutoka kupitia lango hilo siku nzima, ilikuwa rahisi kupata mashahidi wa kushughulikia mambo yaliyowahusu raia, kama vile uuzaji wa mali, na kadhalika. Pia, mahakimu wangechochewa kushughulikia kesi kwa uangalifu na kwa haki kwa sababu zilifanyiwa langoni ambapo watu wote wangeweza kuwaona walipozishughulikia na walipotoa maamuzi. Inaonekana kwamba kulikuwa na sehemu iliyotengwa kando ya lango ambapo mahakimu wangeweza kushughulikia kesi wakiwa wameketi. (Ayu 29:7) Samweli alisafiri na kuzunguka Betheli, Gilgali, na Mispa “naye alikuwa mwamuzi wa Israeli katika maeneo hayo yote,” kutia ndani Rama, ambapo nyumba yake ilikuwa.—1Sa 7:16, 17.
AGOSTI 2-8
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 22-23
“Jinsi Sheria Ilivyoonyesha Yehova Anawajali Wanyama”
it-1 375-376
Mzigo
Katika nyakati za kale, wanyama walitumiwa mara nyingi kubeba mizigo, na Waisraeli waliambiwa ikiwa wangemwona punda wa mtu waliyemchukia akiwa amelemewa na mzigo na kuanguka, badala ya kumwacha, ‘walipaswa kumsaidia kufungua mnyama huyo.’ (Kut 23:5) Kiasi cha vitu ambavyo mnyama anaweza kubeba vinaitwa mzigo, kama vile “muzigo . . . kadiri nyumbu wawili wanavyoweza kubeba.”—2Fa 5:17, Zaire Swahili Bible.
it-1 621 ¶1
Kumbukumbu la Torati
Kitabu cha Kumbukumbu la Torati kinaonyesha kwamba wanyama hawakupaswa kutendewa kwa ukatili. Waisraeli hawakupaswa kumchukua ndege aliyeketi kwenye kiota chake, kwa kuwa ni hisia yake ya kutaka kuwalinda makinda yake iliyomfanya awe katika hali hiyo ya hatari. Alipaswa kuachiliwa huru, lakini Waisraeli wangeweza kujichukulia makinda yake. Hivyo, ndege huyo angeweza kupata makinda wengine. (Kum 22:6, 7) Mkulima hakupaswa kuwafunga ng’ombe dume na punda katika nira moja, ili ng’ombe dume asimuumize punda aliyekuwa dhaifu zaidi. (22:10) Ng’ombe dume hakupaswa kufungwa kinywa alipokuwa akipura nafaka ili asiteseke kwa njaa huku nafaka ikiwa karibu sana, naye alikuwa akitumia nguvu zake kuipura.—25:4.
Hazina za Kiroho
it-1 600
Deni, Mtu Anayedaiwa
Deni linarejelea kitu ambacho mtu anadaiwa, wajibu wa kulipa pesa au kutoa kitu. Katika Israeli la kale, watu walipata madeni kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi. Lilikuwa jambo lenye kusikitisha kwa Mwisraeli kuwa na madeni; kwa kuwa mkopaji alikuwa mtumwa wa mkopeshaji. (Met 22:7) Hivyo, watu wa Mungu waliamriwa wawe wakarimu na wasiwe na ubinafsi wanapowakopesha Waisraeli wenzao waliokuwa na uhitaji, na wasijipatie faida kutokana na hali mbaya ya wenzao kwa kuwatoza riba. (Kut 22:25; Kum 15:7, 8; Zb 37:26; 112:5) Lakini wageni wangeweza kudaiwa riba. (Kum 23:20) Wasomi Wayahudi wanasema uandalizi huo ulihusu mikopo ya kibiashara, si mikopo ya kushughulikia matatizo. Kwa kawaida, wageni walikuwa nchini Israeli kwa muda tu, mara nyingi wakiwa wafanyabiashara, na wangeweza kutarajiwa kulipa riba, hasa kwa kuwa wao pia walikuwa wakiwakopesha wengine kwa riba.
AGOSTI 9-15
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 24-26
“Jinsi Sheria Ilivyoonyesha Yehova Anawajali Wanawake”
it-2 1196 ¶4
Mwanamke
Hata sheria za vita ziliwalinda wote wawili, mke na mume, kwa kumruhusu mwanamume aliyefunga ndoa asiende vitani katika mwaka wa kwanza wa ndoa. Hilo liliwapa wenzi hao wa ndoa nafasi ya kutumia haki yao ya kupata mtoto, kwa kuwa kupata mtoto kungempa mke faraja mume wake alipokuwa mbali, na hasa ikiwa angekufa vitani.—Kum 20:7; 24:5.
it-1 963 ¶2
Kuokota Masalio
Ni wazi kwamba mpango huo muhimu kwa ajili ya waliokuwa maskini nchini, haukuendekeza uvivu, bali uliwachochea watu wawe wakarimu, wasiwe na ubinafsi, na wategemee baraka za Yehova. Unatusaidia kuelewa maneno haya ya Daudi: “Sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa, wala watoto wake wakitafuta mkate.” (Zb 37:25) Kwa kukubali uandalizi huo uliotolewa na Sheria, hata maskini, kwa kufanya kazi ngumu, hawangekosa chakula, na wao na watoto wao hawangehitaji kuombaomba mkate.
Hazina za Kiroho
it-1 640 ¶5
Talaka
Cheti cha Talaka. Kwa sababu tu baadaye watu walitenda kwa njia isiyofaa, haipaswi kueleweka kwamba mpango wa awali wa talaka uliokuwa kwenye Sheria ya Musa ulifanya iwe rahisi kwa mume Mwisraeli kumtaliki mke wake. Ili afanye hivyo, alipaswa kuchukua hatua rasmi. Alipaswa kuandika hati fulani, “amwandikie mwanamke huyo cheti cha talaka.” Kisha mume huyo alipaswa kumpa cheti hicho “na kumruhusu aondoke nyumbani mwake.” (Kum 24:1) Ingawa Maandiko hayatoi habari za ziada kuhusu mchakato wote, inaonekana kwamba hatua hii ya kisheria ilihusisha kushauriana na wanaume waliowekwa rasmi, ambao kwanza walijitahidi kuwapatanisha wenzi hao. Muda uliohusika katika kutayarisha cheti na kukamilisha talaka kisheria ungempa mume aliyekuwa akitoa talaka nafasi ya kufikiria upya uamuzi wake. Kulipaswa kuwa na msingi wa talaka, na inapatana na akili kuamini kwamba sheria hiyo ilipotumiwa vizuri, ingewazuia watu wasitafute talaka upesi. Mbali na hilo, haki za mke na masilahi yake zililindwa. Maandiko hayatuelezi ni habari zipi zilizokuwa katika “cheti cha talaka.”
AGOSTI 16-22
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 27-28
Hazina za Kiroho
it-1 360
Alama ya Mpaka
Sheria ya Mungu ilikataza kurudisha nyuma alama za mipaka. (Kum 19:14; ona pia Met 22:28.) Kwa kweli, mtu aliyesogeza “alama ya mpaka wa jirani yake” alilaaniwa. (Kum 27:17) Kwa kuwa watu waliomiliki ardhi walitegemea mazao kutoka kwenye mashamba yao, kurudisha nyuma mpaka kungemaanisha kumnyima mtu mwingine sehemu ya anachotumia kupata mahitaji ya lazima. Kufanya hiyo kulikuwa sawa na wizi na hayo ndiyo maoni ambayo watu walikuwa nayo zamani. (Ayu 24:2) Lakini kulikuwa na watu fulani ambao hawakuwa wanyoofu waliofanya mambo hayo, na wakuu wa Yuda katika siku za Hosea walilinganishwa na watu wanaosogeza nyuma mpaka.
AGOSTI 23-29
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 29-30
Hazina za Kiroho
it-1 665 ¶3
Sikio
Kupitia watumishi wake, Yehova alisema kwamba Waisraeli wakaidi na wasio watiifu hawakuwa na ‘masikio yaliyotahiriwa.’ (Yer 6:10; Mdo 7:51) Ni kana kwamba masikio yao yalikuwa yamezibwa. Walikuwa na masikio ambayo hayakuwa yamefunguliwa na Yehova, anayewapa wale wanaomtafuta masikio ya uelewaji na utii, lakini anaruhusu uwezo wa kusikia wa wasio watiifu upotee. (Kum 29:4; Ro 11:8) Mtume Paulo alitabiri kuhusu wakati ambapo wale wanaodai kuwa Wakristo wangeondoka kwenye imani ya kweli, wakiwa hawataki kusikia kweli ya Neno la Mungu, lakini wakitamani masikio yao “yafurahishwe” na mambo yanayowapendeza, na hivyo wangewasikiliza walimu wa uwongo. (2Ti 4:3, 4; 1Ti 4:1) Pia, masikio ya mtu yanaweza ‘kuwashwa’ kwa sababu ya kusikia habari zinazoshtua, hasa habari kuhusu msiba.—1Sa 3:11; 2Fa 21:12; Yer 19:3.