Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2023 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
JANUARI 1-7
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 32-33
Faraja kwa Wanaokabiliana na Mahangaiko
it-1 710
Elihu
Elihu hakuonyesha upendeleo, wala hakumsifusifu yeyote. Alitambua kwamba yeye, kama tu Ayubu, alikuwa ameumbwa kwa udongo na kwamba Mweza-Yote alikuwa Muumba wake. Lengo la Elihu halikuwa kumwogopesha Ayubu bali alizungumza naye kama rafiki wa kweli, akimwita Ayubu kwa jina lake, jambo ambalo Elifazi, Bildadi, na Sofari hawakufanya.—Ayu 32:21, 22; 33:1, 6.
JANUARI 15-21
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 36-37
Hazina za Kiroho
it-1 492
Mawasiliano
Zamani katika maeneo ambako Biblia iliandikwa, habari na mawazo yaliwasilishwa katika njia mbalimbali kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine. Kwa kadiri kubwa, habari za kawaida katika eneo fulani na pia zilizotoka mbali ziliwasilishwa kwa mdomo. (2Sa 3:17, 19; Ayu 37:20) Wasafiri, ambao mara nyingi walisafiri katika misafara, walisimulia habari kutoka maeneo ya mbali waliposimama ili kupata chakula, maji, na bidhaa nyingine katika majiji au vituo mbalimbali vilivyokuwa kwenye barabara ambako misafara yao ilipita. Misafara mingi sana ilipitia Palestina ikitoka na kwenda maeneo ya mbali kwa sababu nchi hiyo iko eneo linalofaa kabisa kati ya Asia, Afrika, na Ulaya. Kwa sababu hiyo wakaaji wa nchi hiyo wangepata habari nyingi kuhusu matukio muhimu katika nchi za mbali. Mara nyingi, habari za kitaifa na pia kutoka nchi za mbali, zingepatikana kwenye soko la jiji.
JANUARI 22-28
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 38-39
Hazina za Kiroho
it-2 222
Mpaji-sheria
Yehova akiwa Mpaji-sheria. Yehova, ndiye Mpaji Sheria wa kweli katika ulimwengu mzima. Ametunga sheria zinazoongoza uumbaji usio na uhai (Ayu 38:4-38; Zb 104:5-19), na wanyama. (Ayu 39:1-30) Mwanadamu pia, kwa kuwa ameumbwa na Yehova, anapaswa kutii sheria za Yehova za asili, na kwa kuwa mwanadamu ni kiumbe mwenye uwezo wa kufuata maadili, kufikiri, na kusitawisha hali ya kiroho, anapaswa pia kutii sheria za Mungu za maadili. (Ro 12:1; 1Ko 2:14-16) Pia, sheria za Yehova huwaongoza viumbe wa roho, malaika.—Zb 103:20; 2Pe 2:4, 11.
Sheria za Yehova za asili haziwezi kuvunjwa. (Yer 33:20, 21) Sheria zake zinaonekana katika ulimwengu mzima na ni thabiti na zinategemeka sana hivi kwamba wanasayansi wanaweza kutumia sheria wanazojua kukadiria mwendo wa mwezi, sayari, na vitu vingine vilivyo angani kwa usahihi wa nukta ya sekunde. Yeyote anayepuuza sheria za asili anapatwa na madhara mara moja. Vivyo hivyo, sheria za Mungu za maadili hazibadiliki na mtu hawezi kuzikwepa au kuzivunja na bila kupata madhara. Zinapaswa kufuatwa kama sheria zake za asili, ingawa huenda mtu anayezikiuka asipatwe na madhara papo hapo. “Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”—Gal 6:7; 1Ti 5:24.
JANUARI 29–FEBRUARI 4
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 40-42
Hazina za Kiroho
it-2 808
Dhihaka
Ayubu alikuwa mwanamume aliyedumisha utimilifu wake licha ya kudhihakiwa sana. Lakini alisitawisha mtazamo usiofaa na akafanya kosa, naye alirekebishwa. Elihu alimwambia hivi: “Ni nani aliye kama Ayubu, anayekunywa dharau kama maji?” (Ayu 34:7) Ayubu alizingatia sana kujitetea badala ya kumtetea Mungu, na akaanza kukuza uadilifu wake zaidi ya ule wa Mungu. (Ayu 35:2; 36:24) Alipodhihakiwa vikali na “marafiki” wake watatu, Ayubu alionyesha kwamba dhihaka hizo zilielekezwa dhidi yake badala ya dhidi ya Mungu. Kwa njia hiyo alikuwa kama mtu anayejitoa ili afanyiwe kejeli na kudhihakiwa na ambaye alishangilia alipotendewa hivyo, hivi kwamba ikawa kana kwamba anakunywa dhihaka hizo kwa shangwe kama maji. Baadaye Mungu alimweleza Ayubu kwamba kikweli wadhihaki hao (baada ya kila kitu kuchunguzwa) walikuwa wakisema uwongo dhidi ya Mungu. (Ayu 42:7) Vivyo hivyo, Yehova alimwambia nabii Samweli hivi Waisraeli walipodai wanataka mfalme: “Hawajakukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme wao” (1Sa 8:7) Naye Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtachukiwa na mataifa yote [si kwa sababu yenu wenyewe, bali] kwa sababu ya jina langu.” (Mt 24:9) Kukumbuka mambo hayo kutamsaidia Mkristo kuvumilia dhihaka akiwa na mtazamo unaofaa na kumstahilisha kupokea thawabu kwa sababu ya uvumilivu wake.—Lu 6:22, 23.
FEBRUARI 5-11
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | ZABURI 1-4
Hazina za Kiroho
it-1 425
Makapi
Kifuniko chembamba cha nje au gamba la punje za nafaka kama vile mtama na ngano ambazo pia zinaitwa pumba. Ingawa Biblia inazungumzia makapi kwa njia ya mfano, inataja mazoea ya kupura yaliyokuwa ya kawaida katika nyakati za kale. Baada ya kuvuna, kifuniko hicho cha nje kisichoweza kuliwa hakikuwa na kazi yoyote, na hivyo kilifaa kuwakilisha kitu chepesi, kisicho na thamani, na kisichotamaniwa, kitu kilichopaswa kutenganishwa na vitu vizuri na kutupwa.
Kwanza, shughuli ya kupura ilitenganisha makapi na punje. Kisha kwa kupepeta, pumba zingepeperushwa na upepo kama vumbi. (Ona KUPEPETA.) Hilo linaonyesha vizuri jinsi Yehova Mungu anavyowaondoa waasi-imani kutoka miongoni mwa watu wake na pia jinsi anavyowaangamiza watu waovu na mataifa yanayompinga. (Ayu 21:18; Zb 1:4; 35:5; Isa 17:13; 29:5; 41:15; Ho 13:3) Ufalme wa Mungu utapondaponda maadui wake katika vipande vidogovidogo hivi kwamba watapeperushwa kwa urahisi kama makapi.—Da 2:35.
Mara nyingi, makapi ambayo hayakuwa na umuhimu wowote yangekusanywa na kuchomwa ili yasipeperushwe tena na kuchafua marundo ya nafaka. Vivyo hivyo, Yohana Mbatizaji alitabiri uharibifu uliokuwa ukija dhidi ya watu wa dini ya uwongo—Yesu Kristo akiwa Mpuraji, atakusanya ngano, “lakini atayateketeza makapi kwa moto usioweza kuzimwa.”—Mt 3:7-12; Lu 3:17; ona KUPURA.
FEBRUARI 12-18
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | ZABURI 5-7
Hazina za Kiroho
it-1 995
Kaburi
Kwenye Waroma 3:13 mtume Paulo ananukuu Zaburi 5:9, na kulinganisha koo za watu waovu na “kaburi lililo wazi.” Kama tu kaburi lililo wazi linavyoingizwa miili iliyokufa na vitu vilivyoharibika, koo zao hufunguka ili kutokeza maneno yanayoweza kusababisha kifo na uharibifu.—Linganisha Mt 15:18-20.
FEBRUARI 19-25
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | ZABURI 8-10
Hazina za Kiroho
it-1 832
Kidole
Kwa njia ya mfano, Mungu anasemwa kuwa anatimiza kazi zake kwa “kidole (au vidole)” chake, kama vile alipoandika zile Amri Kumi kwenye mabamba ya mawe (Kut 31:18; Kum 9:10), alipofanya miujiza (Kut 8:18, 19), na alipoumba mbingu (Zb 8:3). Simulizi la uumbaji lililo kwenye Mwanzo linatusaidia kutambua kwamba “vidole” vya Mungu vilivyotumiwa katika uumbaji vinarejelea roho yake takatifu, au nguvu ya utendaji, kwa kuwa nguvu ya utendaji ya Mungu (ruʹach, “roho”) inasemekana kuwa ilikuwa ikienda huku na huku juu ya maji. (Mwa 1:2) Hata hivyo, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatupa njia muhimu ya kuelewa matumizi haya ya mfano. Simulizi la Mathayo linaeleza kwamba Yesu alifukuza roho waovu ‘kupitia roho takatifu ya Mungu’ naye Luka anatuambia alifanya hivyo “kupitia kidole cha Mungu.”—Mt 12:28; Lu 11:20.