Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2024 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
JANUARI 27–FEBRUARI 2
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 140-143
Hazina za Kiroho
it-2 1151
Sumu ya Nyoka
Lugha ya Mfano. Uwongo na maneno ya uchongezi ya waovu yanafananishwa na sumu hatari sana ya nyoka kwa sababu yanaweza kumharibia mtu sifa yake sana. (Zb 58:3, 4) Kuhusu wachongezi inasema, “sumu ya nyoka vipiri iko nyuma ya midomo yao,” kama tu ambavyo tezi ya mate yenye sumu ya nyoka kipiri inavyopatikana nyuma ya mdomo na meno yake yaliyo kwenye utaya wa juu. (Zb 140:3; Ro 3:13) Ulimi wa mwanadamu unapotumiwa vibaya kwa uchongezi, porojo, mafundisho ya uwongo, au maneno kama hayo yenye kudhuru, unaweza kusemwa ‘umejaa sumu yenye kuua.’—Yak 3:8.
FEBRUARI 3-9
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 144-146
Hazina za Kiroho
it-1 111 ¶9
Wanyama
Biblia inakazia sana kwamba viumbe wa hali ya chini wanapaswa kutendewa kwa haki na rehema. Biblia inaonyesha kwamba Yehova ni Mwandaaji Mwenye Upendo anayejali uhai wao na hali yao nzuri. (Met 12:10; Zb 145:15, 16) Sheria ya Musa iliamuru watu wawatunze vizuri wanyama wa kufugwa. Ikiwa mnyama angeonekana akitangatanga, alipaswa kurudishwa akiwa salama kwa mwenyewe; ikiwa angelemewa na mzigo na kuanguka, alipaswa kusaidiwa kutua mzigo huo. (Kut 23:4, 5) Hawakupaswa kutendewa vibaya. (Kum 22:10; 25:4) Kama ilivyo kwa wanadamu, wanyama pia walipaswa kunufaika na pumziko la Sabato. (Kut 20:10; 23:12; Kum 5:14) Wanyama waliohatarisha uhai wa mwanadamu walipaswa kudhibitiwa au kuuawa. (Mwa 9:5; Kut 21:28, 29) Wanyama wa aina tofauti hawakupaswa kuzaliana.—Law 19:19.
FEBRUARI 10-16
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 147-150
Hazina za Kiroho
it-1 316
Ndege
Mtunga-zaburi aliwaelekezea fikira “ndege wenye mabawa” wamsifu Yehova. (Zb 148:1, 10) Ndege humsifu Yehova kupitia jinsi walivyoumbwa kwa njia tata. Ndege mmoja anaweza kuwa na manyoya kati ya 1,000 na zaidi ya 20,000. Kila unyoya una kikonyo ambacho hugawanyika katika ndaka nyingi, kila ndaka huwa na mamia ya vijindaka vidogo na kila kijindaka huwa na viunganishi. Unyoya mmoja wa bawa la njiwa wenye urefu wa inchi sita unakadiriwa kuwa na mamia ya maelfu ya vijindaka na mamilioni ya viunganishi vya vijindaka. Mabawa ya ndege yamebuniwa kwa ufanisi wa hali ya juu zaidi hivi kwamba anaweza kupaa angani kwa urahisi zaidi kuliko ndege za kisasa zinazobeba abiria. Pia, mifupa ya ndege ina uwazi fulani kwa ndani unaomfanya awe mwepesi. Kwa mfano, mifupa ya ndege aina ya frigate ina uzito mdogo tu wa gramu 110 hivi, ingawa bawa lake lina upana wa mita 2. Isitoshe, ndani ya sehemu hizo zenye uwazi za baadhi ya ndege wakubwa wanaopaa juu sana, kuna vitu kama mihimili inayosaidia kutegemeza mabawa yao makubwa. Vitu vya aina hiyo hutumiwa pia kutegemeza mabawa ya ndege zilizotengenezwa na wanadamu.
FEBRUARI 24–MACHI 2
HAZINA ZA NENO LA MUNGU METHALI 2
Hazina za Kiroho
it-1 1211 ¶4
Utimilifu
Mtu hawezi kuwa mtimilifu katika njia hiyo kwa sababu ya jitihada zake binafsi za kudumisha maadili, bali ni kupitia imani yenye nguvu na kumtumaini Yehova na uwezo wake wa kuokoa. (Zb 25:21) Mungu anaahidi kwamba atakuwa “ngao” na “ngome,” akiilinda njia ya wale wanaotembea kwa ushikamanifu. (Met 2:6-8; 10:29; Zb 41:12) Hangaiko lao kuu la kupata kibali cha Yehova huwafanya wawe imara maishani na hilo litawawezesha kunyoosha vijia vyao ili kufikia malengo yao. (Zb 26:1-3; Met 11:5; 28:18) Ayubu alisema kwamba ingawa huenda watu wasio na lawama wakateseka kwa sababu ya watawala waovu na hata kufa pamoja na watu waovu, Yehova anatuhakikishia anajua mambo ambayo mtu asiye na lawama anapitia maishani na anamhakikishia kwamba urithi wa mtu huyo utadumu milele, atakuwa na wakati ujao wenye amani, na atarithi kilicho chema. (Ayu 9:20-22; Zb 37:18, 19, 37; 84:11; Met 28:10) Kama tu ilivyokuwa kwa Ayubu, kudumisha utimilifu ndiko humfanya mtu awe na thamani kubwa na astahili heshima, si utajiri. (Met 19:1; 28:6) Watoto wenye pendeleo la kuwa na mzazi mtimilifu huhesabiwa kuwa wenye furaha. (Met 20:7) Wanapokea urithi wa pekee kutoka kwa baba yao, yaani, kielelezo alichoweka. Kwa kuwa baba huyo ameishi maisha ya utimilifu anawapitisha jina zuri na pia heshima aliyopata miongoni mwa watu.