Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w20 Machi kur. 2-7
  • Upendo na Uthamini Wetu kwa Yehova Hutuchochea Kubatizwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upendo na Uthamini Wetu kwa Yehova Hutuchochea Kubatizwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UPENDO ULIO MUHIMU ZAIDI
  • Kwa Nini Ubatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Unawezaje Kujitayarisha kwa Ajili ya Ubatizo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Mjengwe na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Je, Ninapaswa Kujiweka Wakfu kwa Mungu na Kubatizwa?
    Biblia Inatufundisha Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
w20 Machi kur. 2-7

MAKALA YA 10

Upendo na Uthamini Wetu kwa Yehova Hutuchochea Kubatizwa

“Ni nini kinachonizuia kubatizwa?”—MDO. 8:36.

WIMBO 37 Kumtumikia Yehova kwa Nafsi Yote

MUHTASARIa

1-2. Kama inavyoonyeshwa kwenye andiko la Matendo 8:27-31, 35-38, ni nini kilichomchochea towashi Mwethiopia kubatizwa?

JE, UNATAMANI kubatizwa na kuwa mwanafunzi wa Kristo? Watu wengi wamechochewa kuchukua uamuzi huo kwa sababu ya upendo na uthamini wao kwa Yehova. Fikiria mfano wa ofisa mmoja aliyetumikia chini ya malkia wa Ethiopia.

2 Mwethiopia huyo alichukua hatua mara moja na kutenda kulingana na mambo aliyojifunza katika Maandiko. (Soma Matendo 8:27-31, 35-38.) Ni nini kilichomchochea? Ni wazi kwamba alithamini Neno la Mungu; alikuwa akisoma mistari fulani ya kitabu cha Isaya akiwa kwenye gari lake. Na Filipo alipozungumza naye, alianza kuthamini mambo ambayo Yesu alikuwa amemtendea. Lakini kwa nini ofisa huyo alikuwa amesafiri kwenda Yerusalemu? Kwa sababu tayari alikuwa amesitawisha upendo kwa Yehova. Tunajuaje? Alikuwa ametoka tu kumwabudu Yehova huko Yerusalemu. Inaonekana mwanamume huyo alikuwa ameacha dini ya wazazi wake na kujiunga na taifa pekee lililokuwa wakfu kwa Mungu wa kweli. Upendo huo kwa Yehova ndio uliomchochea achukue hatua nyingine muhimu, yaani, kubatizwa na kuwa mwanafunzi wa Kristo.—Mt. 28:19.

3. Ni nini kinachoweza kumzuia mtu kubatizwa? (Tazama sanduku “Ni Nini Kilicho Moyoni Mwako?”)

3 Kumpenda Yehova kunaweza kukuchochea ubatizwe. Lakini upendo unaweza pia kukuzuia kufanya hivyo. Jinsi gani? Fikiria mifano ifuatayo. Huenda unawapenda sana watu wa familia yako na marafiki na una wasiwasi kwamba ikiwa utabatizwa watakuchukia. (Mt. 10:37) Au huenda umezoea kufanya mambo fulani ambayo unajua Mungu anachukia, na unaona kuwa ni vigumu kuyaacha. (Zab. 97:10) Au huenda tangu utotoni umekuwa ukisherehekea sikukuu zinazohusiana na dini ya uwongo. Na labda unakumbuka mambo mazuri yanayohusiana na sikukuu hizo. Hivyo, huenda ukaona kuwa vigumu kuacha kusherehekea sikukuu zinazomchukiza Yehova. (1 Kor. 10:20, 21) Swali unalopaswa kujiuliza ni, “Ni nini au ni nani ninayempenda zaidi?”

Ni Nini Kilicho Moyoni Mwako?

Yesu alilinganisha ujumbe ulio katika Biblia na mbegu, na akalinganisha moyo wa mwanadamu na aina mbalimbali za udongo. (Luka 8:4-8) Huenda umekuwa ukijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa kipindi fulani. Kwa nini usisome andiko la Luka 8:11-15 na kujiuliza, ‘Moyo wangu unalingana na aina gani ya udongo?’

  • Ndege akitua kwenye udongo uliokanyagwa-kanyagwa.

    Udongo uliokanyagwa-kanyagwa: Mtu wa aina hii hatafuti wakati wa kujitayarisha kabla ya kujifunza Biblia na mwalimu wake. Ana kawaida ya kuahirisha funzo lake la Biblia au kukosa mikutano kwa sababu ya kujishughulisha na mambo mengine.

  • Udongo ulio kwenye mwamba.

    Udongo ulio kwenye mwamba: Mtu wa aina hii anaruhusu upinzani au shinikizo kutoka kwa marafiki au watu wa familia yake limzuie kumtii Yehova na kuishi kulingana na viwango Vyake.

  • Udongo ulio kwenye miiba.

    Udongo ulio kwenye miiba: Mtu wa aina hii anapenda mambo anayojifunza kumhusu Yehova, lakini anahisi kwamba kuwa na pesa na mali kutamfanya awe na furaha na kujihisi akiwa salama. Ana kawaida ya kukosa funzo lake la Biblia kwa sababu yuko kazini au anafurahia burudani fulani.

  • Udongo ambao ngano imesitawi kwa wingi.

    Udongo mzuri: Mtu wa aina hii anajifunza Biblia kwa ukawaida na anajitahidi kutumia mambo anayojifunza. Jambo kuu maishani mwake ni kumpendeza Yehova. Licha ya majaribu na upinzani, yeye huendelea kuwaambia wengine mambo anayojua kumhusu Yehova.

Wewe ndiye unayeamua jinsi moyo wako utakavyokuwa. Kama aina hizo mbalimbali za udongo katika mfano wa Yesu, moyo wako wa mfano unaweza kulainishwa, kutolewa magugu, na kuboreshwa. Kumbuka, wewe ndiye unayechagua aina ya udongo ambao ungependa kuwa.

UPENDO ULIO MUHIMU ZAIDI

4. Ni jambo gani kuu litakalokuchochea ubatizwe?

4 Kuna mambo mengi unayoweza kupenda na kuthamini. Kwa mfano, hata kabla ya kuanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova, huenda ulikuwa unalithamini sana Neno la Mungu. Na huenda tayari ulikuwa unampenda Yesu. Sasa, baada ya kufahamiana na Mashahidi wa Yehova, huenda unafurahia kuwa pamoja nao. Lakini kupenda mambo hayo mazuri huenda kusikufanye uwe na tamaa ya kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Jambo kuu litakalokuchochea uchukue hatua ya kubatizwa ni kumpenda Yehova Mungu kibinafsi. Ukimpenda Yehova zaidi kuliko kitu au mtu mwingine yeyote, hutaruhusu kitu chochote au mtu yeyote akuzuie kumtumikia yeye. Upendo wako kwa Yehova utakuwa kama lango linaloongoza kwenye ubatizo na pia kama kingo za chuma zitazokusaidia uendelee kubaki kwenye njia ya kumtumikia Mungu.

5. Tutazungumzia maswali gani?

5 Yesu alisema kwamba lazima tumpende Yehova kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zetu zote. (Marko 12:30) Unaweza kujifunza jinsi gani kumpenda na kumheshimu sana Yehova? Kutafakari jinsi Yehova anavyotupenda kutatuchochea tumpende pia. (1 Yoh. 4:19) Ni matendo au hisia gani nyingine utakazokuwa nazo mara tu utakapositawisha upendo huo muhimu zaidi?b

6. Kulingana na andiko la Waroma 1:20, tunaweza kujifunza kumhusu Yehova jinsi gani?

6 Jifunze kumhusu Yehova kupitia uumbaji. (Soma Waroma 1:20; Ufu. 4:11) Tafakari kuhusu hekima inayoonekana waziwazi kupitia jinsi mimea na wanyama walivyoumbwa. Jifunze kuhusu jinsi mwili wako ulivyoumbwa kwa njia ya kustaajabisha. (Zab. 139:14) Na ufikirie kuhusu nguvu ambazo Yehova aliweka katika jua letu, ukizingatia kwamba jua ni nyota moja tu kati ya mabilioni ya nyota.c (Isa. 40:26) Kadiri unavyotafakari mambo hayo, ndivyo utakavyozidi kumheshimu Yehova. Hata hivyo, kujua kwamba Yehova ni mwenye hekima na mwenye nguvu, ni sehemu tu ya msingi wa uhusiano wako pamoja naye. Ili ujenge upendo wenye nguvu kwa Yehova, unahitaji kujua mengi zaidi kumhusu.

7. Ili upendo wako kwa Yehova uzidi kuongezeka, unahitaji kusadiki nini?

7 Unahitaji kusadiki kwamba Yehova anakujali wewe binafsi. Je, wewe huona kuwa vigumu kuamini kwamba Muumba wa mbingu na dunia anakuona na anakujali? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba Yehova “hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Mdo. 17:26-28) Yeye “huichunguza kabisa mioyo yote,” na kama Daudi alivyomwambia Sulemani, Mungu anakuahidi kwamba “ukimtafuta, atakuruhusu umpate.” (1 Nya. 28:9) Isitoshe, sababu inayokufanya ujifunze Biblia sasa ni ile ambayo Yehova aliitaja aliposema, “Nimekuvuta kwangu.” (Yer. 31:3) Kadiri unavyozidi kuthamini mambo yote ambayo Yehova amekufanyia, ndivyo utakavyompenda zaidi.

8. Unaweza kuonyeshaje kwamba unathamini upendo wa Yehova?

8 Njia moja ya kuonyesha kwamba tunathamini upendo wa Yehova ni kwa kuzungumza naye katika sala. Upendo wako kwake utazidi kuongezeka kadiri unavyomweleza kuhusu mambo yanayokuhangaisha na kumshukuru kwa mambo yote ambayo anakutendea. Pia, urafiki wako pamoja naye utazidi kuimarika kadiri unavyojionea jinsi anavyojibu sala zako. (Zab. 116:1) Utasadiki kwamba anakuelewa vizuri. Lakini ili umkaribie Yehova, unahitaji kuelewa njia yake ya kufikiri. Na unahitaji kujua mambo anayotaka ufanye. Njia pekee itakayokusaidia upate ujuzi huo ni kujifunza Neno lake, Biblia.

Dada akinunua bidhaa kwenye soko la nje, anampatia trakti mwanamke aliyesimama kwenye kibanda cha mboga-mboga.

Njia bora zaidi ya kumkaribia Mungu na kujua mambo anayotaka tufanye ni kujifunza Biblia (Tazama fungu la 9)d

9. Unaweza kuonyeshaje kwamba unaithamini Biblia?

9 Jifunze kulithamini Neno la Mungu, Biblia. Ni Biblia tu inayoeleza ukweli kumhusu Yehova na kusudi lake kukuelekea. Unaonyesha kwamba unaithamini Biblia kwa kuisoma kila siku, kwa kujitayarisha kabla ya kujifunza na mwalimu wako wa Biblia, na kwa kutumia mambo unayojifunza. (Zab. 119:97, 99; Yoh. 17:17) Je, una ratiba ya kibinafsi ya kusoma Biblia? Je, unaifuata ratiba hiyo, kwa kuhakikisha kwamba unasoma Biblia kila siku?

10. Taja mojawapo ya mambo ya pekee kuhusu Biblia.

10 Jambo moja la pekee kuhusu Biblia ni kwamba ina masimulizi ya watu waliojionea kwa macho yao wenyewe mambo ambayo Yesu alifanya. Ndicho kitabu pekee kinachoeleza kwa usahihi mambo ambayo Yesu amekufanyia. Kadiri unavyojifunza mambo ambayo Yesu alisema na kutenda, ndivyo utakavyochochewa kusitawisha urafiki pamoja naye.

11. Unaweza kujifunzaje kumpenda Yehova?

11 Jifunze kumpenda Yesu, na upendo wako kwa Yehova utaongezeka. Kwa nini? Kwa sababu Yesu aliiga kikamilifu sifa za Baba yake. (Yoh. 14:9) Hivyo, kadiri unavyojifunza mengi zaidi kumhusu Yesu, ndivyo utakavyomwelewa na kumthamini zaidi Yehova. Fikiria jinsi Yesu alivyowahurumia watu waliodharauliwa na wengine, kama vile maskini, wagonjwa, na walio dhaifu. Fikiria pia kuhusu ushauri mzuri anaokupatia na jinsi maisha yako yanavyokuwa mazuri zaidi unapomsikiliza.—Mt. 5:1-11; 7:24-27.

12. Huenda ukachochewa kufanya nini kadiri unavyojifunza kumhusu Yesu?

12 Upendo wako kwa Yesu utazidi kuimarika unapotafakari kwa kina kuhusu dhabihu aliyotoa ili dhambi zetu zisamehewe. (Mt. 20:28) Unapoelewa kwamba Yesu alikuwa tayari kufa kwa ajili yako, huenda ukachochewa kutubu na kumwomba Yehova akusamehe. (Mdo. 3:19, 20; 1 Yoh. 1:9) Na kadiri unavyompenda Yesu na Yehova, ndivyo utakavyotamani kuwa karibu na watu wanaowapenda pia.

13. Yehova amekuandalia nini?

13 Jifunze kuipenda familia ya Yehova. Huenda watu wako wa familia ambao si waamini na marafiki wako wa awali wasielewe kwa nini unataka kujiweka wakfu kwa Yehova. Huenda hata wakakupinga. Yehova atakusaidia kwa kukupatia familia ya kiroho. Ikiwa utaendelea kuwa karibu na familia hiyo ya kiroho, utajionea upendo na kupata utegemezo unaohitaji. (Marko 10:29, 30; Ebr. 10:24, 25) Baada ya muda, huenda watu wako wa familia wakajiunga pamoja nawe kumtumikia Yehova na kuishi kulingana na viwango vyake.—1 Pet. 2:12.

14. Kama inavyotajwa kwenye 1 Yohana 5:3, umegundua nini kuhusu viwango vya Yehova?

14 Jifunze kuthamini na kufuata viwango vya Yehova. Kabla ya kumjua Yehova, huenda ulijiwekea viwango vyako mwenyewe, lakini sasa unatambua kwamba viwango vya Yehova ni bora zaidi. (Zab. 1:1-3; soma 1 Yohana 5:3.) Fikiria kuhusu shauri la Biblia kwa waume, wake, wazazi, na watoto. (Efe. 5:22–6:4) Je, umejionea maisha ya familia yako yakizidi kuwa mazuri kwa sababu ya kufuata mashauri hayo? Je, mazoea yako ya kibinafsi yamekuwa mazuri zaidi kwa sababu ya kutii mwongozo wa Yehova kuhusu kuchagua marafiki kwa hekima? Je, furaha yako imeongezeka? (Met. 13:20; 1 Kor. 15:33) Bila shaka jibu lako kwa maswali hayo ni ndiyo.

15. Unaweza kufanya nini ikiwa unahitaji msaada wa kutambua jinsi ya kutumia kanuni za Biblia?

15 Nyakati nyingine, huenda ukaona kuwa vigumu kutambua jinsi unavyoweza kutumia kanuni za Biblia unazojifunza. Hiyo ndiyo sababu Yehova anatumia tengenezo lake kukuandalia habari zinazotegemea Biblia, zinazoweza kukusaidia utambue tofauti kati ya lililo sawa na lisilo sawa. (Ebr. 5:13, 14) Unaposoma na kujifunza habari hizo, utaona jinsi zinavyokufaa kihususa, nawe utatamani kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova.

16. Yehova amewapanga watu wake jinsi gani?

16 Jifunze kulipenda na kuliunga mkono tengenezo la Yehova. Yehova amewapanga watu wake katika makutaniko; Yesu, Mwanawe, ndiye kichwa cha makutaniko yote. (Efe. 1:22; 5:23) Yesu amekiweka rasmi kikundi kidogo cha wanaume waliotiwa mafuta ili waongoze na kupanga kazi anayotaka itimizwe leo. Yesu alikiita kikundi hicho cha wanaume “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” nao huchukulia kwa uzito jukumu lao la kukulisha na kukulinda wewe kiroho. (Mt. 24:45-47) Mojawapo ya njia ambazo mtumwa mwaminifu anakutunza ni kwa kuhakikisha kwamba wazee wa kutaniko wanaostahili wanawekwa rasmi ili kukuchunga. (Isa. 32:1, 2; Ebr. 13:17; 1 Pet. 5:2, 3) Wazee wako tayari kujimimina wenyewe kwa ajili yako, kukufariji, na kukusaidia uzidi kumkaribia Yehova zaidi na zaidi. Lakini mojawapo ya mambo muhimu zaidi wanayoweza kukufanyia, ni kukusaidia uwafundishe wengine kumhusu Yehova.—Efe. 4:11-13.

17. Kulingana na andiko la Waroma 10:10, 13, 14, kwa nini sisi huzungumza na wengine kumhusu Yehova?

17 Wasaidie wengine wajifunze kumpenda Yehova. Yesu aliwaambia wafuasi wake wawafundishe wengine kumhusu Yehova. (Mt. 28:19, 20) Inawezekana mtu akatii amri hiyo ili tu kutimiza wajibu. Lakini kadiri upendo wako kwa Yehova unavyozidi kukua, ndivyo utakavyohisi kama mtume Petro na Yohana waliosema: “Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:20) Kumsaidia mtu kumpenda Yehova, ni kati ya mambo machache sana ambayo hutuletea furaha nyingi. Wazia shangwe nyingi ambayo mweneza-injili Filipo alipata alipomsaidia yule Mwethiopia kujifunza kweli iliyo katika Maandiko na kubatizwa! Unapomwiga Filipo kwa kutii amri ya Yesu ya kuhubiri, unathibitisha kwamba unataka kuwa Shahidi wa Yehova. (Soma Waroma 10:10, 13, 14.) Utakapofikia hatua hiyo, inaelekea utauliza swali ambalo yule Mwethiopia aliuliza: “Ni nini kinachonizuia kubatizwa?”—Mdo. 8:36.

18. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

18 Utakapoamua kubatizwa, utakuwa umechukua hatua muhimu zaidi maishani mwako. Kwa kuwa hiyo ni hatua nzito sana, unahitaji kufikiria kwa makini mambo yanayohusika. Unahitaji kujua nini kuhusu ubatizo? Unahitaji kufanya nini kabla na baada ya ubatizo? Tutajibu maswali hayo katika makala inayofuata.

UNGEJIBUJE?

  • Nia yetu kuu ya kumtumikia Yehova inapaswa kuwa nini, na kwa nini unajibu hivyo?

  • Tunaweza kujifunzaje kumpenda Yehova?

  • Tunaweza kunufaikaje kwa kutafakari mfano ulio kwenye Luka 8:11-15?

WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova

a Baadhi ya watu wanaompenda Yehova, hawana uhakika ikiwa wako tayari kubatizwa na kuwa Mashahidi wake. Ikiwa unahisi hivyo, makala hii itakusaidia uchunguze baadhi ya mambo hususa unayoweza kufanya yatakayokusaidia kufikia hatua ya ubatizo.

b Watu hutofautiana, hivyo huenda wengine wakafuata mapendekezo yaliyotajwa katika makala hii kwa mpangilio tofauti.

c Kwa mifano zaidi, tazama broshua Uhai​—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai.

d MAELEZO YA PICHA: Dada akimpa trakti mwanamke kijana aliyekutana naye akinunua bidhaa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki