Picha inayoonyesha jukwaa na bango lililokuwa juu yake
1922—Miaka Mia Moja Iliyopita
“MUNGU . . . hutupatia ushindi kupitia . . . Yesu Kristo.” (1 Kor. 15:57) Maneno hayo, ambayo yalichaguliwa kuwa andiko la mwaka wa 1922, yaliwahakikishia Wanafunzi wa Biblia kwamba uaminifu wao ungethawabishwa. Na kwa kweli mwaka huo, Yehova aliwathawabisha wahubiri hao wenye bidii. Aliwabariki walipoanza kuchapisha na kujalidi vitabu vyao wenyewe na kutumia redio ili kueneza kweli za Ufalme. Kisha baadaye katika mwaka wa 1922, ilikuwa wazi tena kwamba Yehova alikuwa akiwabariki watu wake. Wanafunzi wa Biblia walifaulu kukusanyika katika kusanyiko la kihistoria lililofanywa huko Cedar Point, Ohio, Marekani. Kusanyiko hilo lilibadili jinsi mambo yalivyofanywa katika tengenezo la Yehova kuanzia wakati huo hadi leo.
“WAZO LENYE KUSISIMUA”
Uhitaji wa machapisho uliongezeka kadiri kazi ya kuhubiri ilivyopanuka. Akina ndugu katika Betheli ya Brooklyn walikuwa wakitokeza magazeti, lakini bado walitegemea makampuni ya kibiashara ili kutengeneza vitabu vyenye jalada gumu. Baada ya vitabu kutopatikana katika kipindi cha miezi kadhaa na kuathiri kazi ya kuhubiri, Ndugu Rutherford alimuuliza Robert Martin, msimamizi wa kiwanda, kuhusu uwezekano wa kutokeza vitabu.
Kiwanda cha Concord Street huko Brooklyn, New York
Ndugu Martin anakumbuka hivi: “Lilikuwa wazo lenye kusisimua, kwa sababu lilimaanisha kufunguliwa kwa kiwanda kamili cha kupanga chapa, kupakaza kwa kutumia umeme, kuchapa, na kujalidi.” Akina ndugu walikodi jengo kwenye barabara ya 18 Concord Street huko Brooklyn na wakanunua vifaa walivyohitaji.
Si kila mtu aliyefurahishwa na maendeleo hayo. Mkurugenzi mkuu wa kiwanda ambacho kilikuwa kikichapisha vitabu vyetu alipotembelea kiwanda hicho kipya alisema hivi: “Mna kiwanda cha uchapishaji chenye mashine za hali ya juu, na hamna mtu anayejua jinsi ya kuzitumia. Baada ya miezi sita mashine zote hizi zitakuwa zimeharibika.”
Ndugu Martin alisema hivi: “Maneno hayo yalionekana kuwa ya kweli, lakini aliyeyasema alimpuuza Bwana; na sikuzote Bwana amekuwa pamoja nasi.” Ndugu Martin alikuwa sahihi. Baada ya muda mfupi, kiwanda hicho kipya kilikuwa kikitokeza vitabu 2,000 kwa siku.
Wafanyakazi wakiwa wamesimama kando ya mashine za kuchapa kiwandani
KUWAFIKIA MAELFU KUPITIA REDIO
Zaidi ya kuchapisha vitabu vyao wenyewe, watu wa Yehova walianza kutumia njia mpya ya kueneza habari njema, yaani, matangazo ya redio. Jumapili alasiri, Februari 26, 1922, Ndugu Rutherford alizungumza kwenye redio kwa mara ya kwanza. Alitoa hotuba yenye kichwa, “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe” kwenye kituo cha redio cha KOG huko Los Angeles, California, Marekani.
Inakadiriwa kwamba watu 25,000 walisikiliza programu hiyo. Baadhi yao walituma barua za shukrani kwa ajili ya programu hiyo. Mojawapo ya barua hizo ilitoka kwa Willard Ashford, mkaaji wa Santa Ana, California. Alimpongeza Ndugu Rutherford kwa kutoa hotuba yenye “kusisimua na yenye kupendeza.” Kisha aliongezea hivi: “Kulikuwa na wagonjwa watatu katika nyumba yetu na hakuna yeyote kati yetu ambaye angeweza kukusikiliza isipokuwa kupitia njia hii, hata kama ungetoa hotuba karibu na eneo tunaloishi.”
Vipindi zaidi vilipeperushwa katika majuma yaliyofuata. Kufikia mwisho wa mwaka huo, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilikadiria kwamba “angalau watu 300,000 [walikuwa] wamepokea ujumbe kupitia [redio].”
Wanafunzi wa Biblia walitiwa moyo na maelezo hayo, nao wakaamua kujenga kituo cha redio huko Staten Island, eneo lililo karibu na Betheli ya Brooklyn. Katika miaka iliyofuata, Wanafunzi wa Biblia walitumia kituo hicho cha WBBR, kueneza ujumbe wa Ufalme kwa watu wengi zaidi.
“ADV”
Toleo la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1922, lilitangaza kwamba kusanyiko la watu wote lingefanywa huko Cedar Point, Ohio, kuanzia Septemba 5 hadi 13, 1922. Wanafunzi wa Biblia walisisimka sana walipowasili huko Cedar Point.
Katika hotuba yake ya kwanza, Ndugu Rutherford aliwaambia hivi wasikilizaji: “Nina hakika kabisa kwamba, Bwana . . . [atabariki] kusanyiko hili na kuhakikisha kwamba ushahidi mkubwa zaidi utatolewa kuliko wakati mwingine wowote hapa duniani.” Wasemaji katika kusanyiko hilo waliwatia moyo tena na tena akina ndugu washiriki katika kazi ya kuhubiri.
Umati uliohudhuria kusanyiko la mwaka wa 1922, huko Cedar Point, Ohio
Kisha Ijumaa, Septemba 8, wahudhuriaji 8,000 hivi waliingia kwenye ukumbi wakiwa wamesisimka kusikiliza hotuba ya Ndugu Rutherford. Walitarajia kwamba angeeleza maana ya herufi “ADV,” zilizokuwa zimechapishwa kwenye mwaliko. Wasikilizaji walipoketi kwenye viti vyao, bila shaka baadhi yao walitambua bango kubwa lililokuwa limekunjwa juu ya jukwaa. Arthur Claus, ambaye alikuwa amesafiri kuja kwenye kusanyiko kutoka huko Tulsa, Oklahoma, Marekani, alipata mahali pa kuketi ambapo angeweza kusikia vizuri, na hilo lilikuwa jambo la pekee kwa sababu siku hizo hakukuwa na vipaza sauti.
“Tulikuwa tunasikiliza kila neno kwa makini”
Ili kuhakikisha kwamba hotuba hiyo haingevurugwa, mwenyekiti alitangaza kwamba mtu yeyote aliyechelewa hangeruhusiwa kuingia kwenye ukumbi wakati wa hotuba ya Ndugu Rutherford. Saa tatu na nusu asubuhi, Ndugu Rutherford alianza kwa kunukuu maneno haya ya Yesu kwenye Mathayo 4:17: “Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Alipokuwa akizungumzia jinsi wanadamu wangesikia kuhusu Ufalme huo alisema hivi: “Yesu mwenyewe alisema kwamba katika wakati wa kuwapo kwake angeongoza kazi ya kuwavuna watu wake, wakati ambapo angewakusanya upande wake wafuasi washikamanifu na wa kweli.”
Ndugu Claus, ambaye alikuwa ameketi kwenye ukumbi mkuu anakumbuka hivi: “Tulikuwa tunasikiliza kila neno kwa makini.” Lakini ghafla alianza kujisikia vibaya na akalazimika kuondoka kwenye ukumbi. Arthur aliondoka shingo upande, akijua kwamba hangeruhusiwa kuingia tena.
Baada ya dakika chache, alianza kujihisi vizuri. Alisimulia kwamba alipokuwa akitembea kuelekea kwenye ukumbi alisikia watu wakipiga makofi kwa sauti kubwa. Jambo hilo lilimfanya asisimke sana! Aliamua kwamba angesikiliza sehemu iliyobaki ya hotuba hiyo yenye kusisimua hata ikiwa angelazimika kupanda kwenye paa. Ndugu Claus ambaye wakati huo alikuwa kijana mwenye umri wa miaka 23, alipata sehemu ambayo angeweza kupanda kwenye paa! Madirisha kwenye paa yalikuwa yamefunguliwa, na alipokaribia alitambua kwamba angeweza “kusikia sauti vizuri sana.”
Lakini Arthur hakuwa peke yake. Baadhi ya rafiki zake walikuwa pia kwenye paa. Mmoja wao, Frank Johnson, alikuja mbio na kumuuliza, “Una kisu cha mfukoni chenye makali?”
Arthur akamjibu, “Ndiyo ninacho.”
“Wewe ndiye jibu la sala zetu,” akasema Frank. “Unaona kitambaa hiki kikubwa kilichokunjwa? Ni bango lililofungwa kwenye misumari hii. Msikilize kwa makini Jaji.a Na atakaposema, “nanyi mnapaswa kutangaza, kutangaza,’ kata kamba hizi nne.”
Basi Arthur, akiwa na kisu mkononi alisubiri pamoja na wenzake ili kusikia maneno hayo. Baada ya muda mfupi, Ndugu Rutherford akafikia kilele cha hotuba yake. Akichochewa na hisia na shauku, inaelekea Ndugu Rutherford alisema hivi kwa sauti kubwa: “Iweni mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila kisehemu cha Babiloni kiwe ukiwa. Utangazeni ujumbe kotekote. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme anatawala! Ninyi ndio mawakala wa kumtangaza. Kwa hiyo, mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na Ufalme wake!”
Arthur alisimulia kwamba yeye na wale ndugu wengine walikata kamba na lile bango likafunguka kwa utaratibu mzuri. Kupatana na zile herufi “ADV,”b lile bango lilisomeka hivi: “Mtangazeni Mfalme na Ufalme.”
KAZI MUHIMU
Kusanyiko la huko Cedar Point liliwasaidia akina ndugu wakazie fikira kazi muhimu ya kuhubiri kuhusu Ufalme, na wale walio na roho ya utayari walifurahia kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Kolpota mmoja (ambao sasa wanajulikana kama painia) kutoka Oklahoma, Marekani aliandika hivi: “Wilaya ambayo tulihubiri iko katika eneo lenye makaa ya mawe, na kuna umaskini mkubwa.” Alisema kwamba mara nyingi watu waliposikia ujumbe uliokuwa katika gazeti la Golden Age, “[wangeanza] kulia.” Aliongezea hivi: “Ni baraka kubwa sana kuwafariji.”
Wanafunzi hao wa Biblia walihisi uharaka wa maneno haya ya Yesu yanayopatikana kwenye Luka 10:2: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” Mwaka huo ulipokaribia kwisha, walikuwa wameazimia hata zaidi kuutangaza ujumbe wa Ufalme kila mahali.
a Wakati mwingine Ndugu Rutherford aliitwa “Jaji” kwa sababu pindi fulani alitumikia akiwa jaji wa pekee huko Missouri, Marekani.
b ADV ni ufupisho wa neno la Kiingereza “Advertise” ambalo linamaanisha “Kutangaza.”