Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 3/15 kur. 141-144
  • Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa —CHINA

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa —CHINA
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • WAMISIONARI WA KWANZA WAFIKA
  • HODARI IJAPOKUWA HATARI INAYOKARIBIA
  • MAGUMU YAONGEZEKA KATIKA BARA
  • MWANZO WA MWISHO
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 3/15 kur. 141-144

Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa

—CHINA

CHINA ndilo taifa la dunia lenye idadi ya watu wengi zaidi. Likiwa katika pembe ya mashariki ya kusini ya Asia na kupakana na Japan na Korea, lina eneo la karibu maili milioni tatu na nusu ya mraba.

Wachina walio wengi ni wakulima, wenye kukuza mifugo, kuku, na mabata, mpunga na mboga kulisha watu milioni 800 wa nchi hiyo. Karne zilizopita Wachina wamesitawisha sifa ya kuwa wenye bidii sana, na ya kushinda taabu kwa uthabiti wa kusifika. Kwa mapokeo wao ni Wabuddha, wenye maoni ya kwamba mambo yatokea kwa ajali tu na kwamba mambo yote yatokeayo yaliandikwa tangu zamani. Dini yao ya Buddha ni mchanganyiko wa dini ya kale ya Tao wa China ikiongozwa na filosofia ya Confucius, ibada ya mababu ikiwa na sehemu kubwa katika maisha ya jamaa.

Kwa mapokeo jamaa ya Wachina imeungana sana. Jamaa za jimbo moja wasemao lugha moja wanafanyiza ukoo usioweza kuvunjwa vyepesi. Biashara ya mtu mwenyewe inakuwa biashara ya ukoo. Kwa Wachina hawa, fedha yafananisha uwezo nayo yaabudiwa kama mungu, lakini kuwaza kwao juu ya mwanzo na kusudi la uzima kwaelekea kutokuwapo.

Je! watu wa China wamepata nafasi ya kuzisikia habari njema za ufalme wa Mungu? Hata katika miaka ya kwanza ya tengenezo la kisasa la mashahidi wa Yehova wa Kikristo habari njema zilifika China. Ingawa Zion’s Watch Tower lilichapwa kwanza na kugawa Julai 1879, katika mwaka wa 1883 lilikuwa limekwisha penya China. Katika mwaka wa 1883, Binti Downing, mmisionari wa Presbyterian Board in Chefoo, China, alikuta nakala ya The Watch Tower. Makala iliyozungumza ukombozi ilimvuta; aliandikisha awe akipata gazeti hilo, akaiacha dini yake na kuwa shahidi wa Yehova. Alizungumza na wamisionari wengine akawa njia ya kusaidia wengine waache dini ya uongo.

Msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society alipendezwa sana na kuhubiri habari njema za ufalme wa Mungu kama ilivyoamriwa katika Mathayo 24:14. Kwa hiyo, mapema katika mwaka wa 1912, C. T. Russell alisafiri baharini akaingia katika mji wa bandari ya Shanghai kama mwenyekiti wa halmashauri ya wanaume saba, akitoa hotuba na ujumbe wa kuonya juu ya mwisho unaokaribia wa “Majira ya Mataifa.” Hotuba hizi zilisaidia kuzieneza mbegu za kweli kwenye maeneo ya mbali zaidi.

Miaka ya kuanza na wa 1930 mapainia hodari kutoka Australia walipanda pia mbegu za kweli katika Mashariki. Afisi ya kutoa mahitaji ya utumishi ya mapainia hawa iliwekwa Shanghai.

WAMISIONARI WA KWANZA WAFIKA

Katika siku yenye joto kali wakati wa hari, Juni 17, 1947, Harold King na Stanley Jones walifika Shanghai, wakiwa wanafunzi wenye kuhitimu wa darasa la nane la Gileadi. Mapainia Wajeremani watatu walikuwako kuwalaki. Ndugu Jones na King walipokuwa wakila chakula chao cha jioni walipashwa habari za hali zilivyokuwa, kiroho na nchini pia, katika Shanghai.

Shanghai ulikuwa katika hali yenye hatari, kidini, kibiashara na kisiasa. Chama kilichoitwa Nationalist Kuo Ming Tang Party kilikuwa vitani na Wakomunisti wa Mao Tse-tung katika majimbo ya kaskazini nayo vita ikakaribia-karibia Shanghai kila siku. Watoro waliongezea hesabu ya watu katika mji uliokuwa umesongamana tayari. Yalikuwako maelfu ya waombaji kweli kweli, ambao wengi wao walikaushwa na baridi na kufa wakati wa siku za masika zenye baridi. Kufikia sehemu ya kwanza ya mwaka wa 1948, Waingereza walikuwa hawaheshimiwi sana. Maelfu ya watu, zaidi wanafunzi, waliteketeza majengo ya Waingereza katika Canton. Miito ya kutiana shime vitani ilibandikwa katika majengo kukawa na maonyesho ya kupinga Waingereza. Kukamatwa kwa sababu za kisiasa, fujo zilizohusu mchele, biashara za magendo, anasa na uchafu yote yalikuwa mambo ya kawaida katika maisha Shanghai.

Ilikuwa kazi ngumu kwanza; wote walipaswa wategemee kadi za ushuhuda zilizoandikwa Kichina kuutoa ujumbe. Vitabu vilipatikana katika Kiingereza na Kichina. Wakati huo kitabu Salvation na vijitabu vitano vilitafsiriwa Kichina. Kwa wamisionari ilielekea kwamba walikuwa wanagongesha vichwa vyao ukutani. Lugha ya Shanghai ilikuwa kizuizi kikubwa kilichopaswa kushindwa. Watu walio wengi walikuwa Wabuddha nao hawakusikiliza Biblia vyepesi. Karibu milango yote ilikuwa na madhabahu ya vitu vitakatifu pamoja na mishumaa ya sanamu yenye kuwaka. Ndani, nyumba pia zilikuwa na vitu vitakatifu na madhabahu. Vioo vilipigiliwa dirishani na katika milango mikubwa ya kuingilia ili kutisha pepo wabaya wasije. Juu ya malango vilikuwako vipande vya karatasi vyekundu vyenye semi za bahati njema na picha za kutisha za miungu ya Wabuddha.

Baraka ya Yehova ilikuwa juu ya kikundi hiki kidogo cha mashahidi wake Yeye, nayo mambo yalianza kutokea. Ndugu Jones alikutana na mfanya kazi wa kanisa la mahali pake aliyekuwa mke mwenye shughuli za nyumbani, Nancy Yuen, katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Mumewe hakupendezwa na Biblia hata chembe, lakini Bibi Yuen aliona mara hiyo tofauti kati ya Kristendomu na Ukristo wa kweli. Alianza kuja mikutanoni kwa kawaida na kuliacha kanisa lake. Alisema Kiingereza vizuri na akawa rafiki mkubwa wa Dada Groezinger. Dada hawa wawili wakiwa pamoja waliwatia moyo walio wadogo waliokuwa wameanza kushirikiana mikutanoni, kwa sababu ya roho yao yenye furaha na ya kirafiki. Sasa alikuwako mhubiri Mchina, Nancy Yuen, akihubiri nyumba kwa nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia, yote kwa Kichina.

Tawi la Shanghai lilipanga kuwe na ubatizo Julai mwaka wa 1948. Akina ndugu walishukuru sana kuona watu tisa wakibatizwa; wote isipokuwa mmoja walikuwa Wachina.

HODARI IJAPOKUWA HATARI INAYOKARIBIA

Wakati huu, hali ya kisiasa katika China ilikuwa inaharibika sana na hii ingekuwa na matokeo yenye mfiko wa mbali juu ya kazi ya Ufalme. Kwanza majeshi ya Wakomunisti yalipokuwa katika majimbo ya kaskazini, kikundi kidogo cha Mashahidi kilikuwa kimeweza kufanya kazi yao waliyogawiwa na Mungu ya kufanya wanafunzi bila magumu yo yote makubwa. Maisha katika Shanghai yaliendelea kuwa yenye mwendo wa kawaida wa ghasia na kelele. Halafu habari zikaja kwamba majeshi Mekundu yalikuwa yamefika katika kingo za kaskazini za Mto Yangtze yakiutisha mji mkuu Nanking wa chama kiitwacho Nationalist Kuo Ming Tang. Sasa watu katika Shanghai walipatwa na wasiwasi na hangaiko, wakaanza kutoka kwa wingi. Wote waliokuwa na fedha ya kuondoka mjini walianza kufanya hivyo, kutia na mwenye Jumba la Ufalme. Je! wangepoteza Jumba la Ufalme lao? Walipewa sakafu yote ya chini ya duka kwa dola 1,000, ambazo ndugu wenyewe waliweza kuchanga wakiwa na zawadi zaidi kutoka kwa wenye kupendezwa.

Kila siku ilipozidi kupita maisha katika Shanghai yakawa yenye wasiwasi zaidi. Kufikia Machi na Aprili mwaka wa 1949 majeshi Mekundu yalishambulia nao Wanationalist walikuwa wakiondoka bara na kutorokea Taiwan. Manowari za Waingereza na Waamerika zilizoonekana kwa kawaida zimetia nanga katika Mto Hwang Pu, sasa zilikuwa zimeondoka. Wamisionari walipokuwa wamelala vitandani mwao usiku waliweza kusikia mifyatuo ya bunduki kwa mbali majeshi ya Wakomunisti yalipokuwa yakiukaribia Shanghai.

Sasa Ndugu Jones na King wenyewe walikabiliwa na uamuzi mzito. Je! wangeondoka Shanghai kabla mji haujaanguka kwa Wakomunisti au wangebaki pamoja na ndugu zao na kuwapa msaada na tegemezo lililohitajiwa? Baada ya mazungumzo marefu na baada ya kuomba uongozi wa Yehova juu ya shauri hili, iliamuliwa kwamba wote wawili wangekaa na kuangalia “kondoo” wa Yehova.

Halafu usiku mmoja mifyatuo ya bunduki ilikuwa mikubwa na yenye nguvu zaidi kuliko kawaida. Ikatangazwa asubuhi na mapema katika radio kwamba mji ulikuwa umeanguka! Ndugu Jones na King walitoka wakanunue chakula wakaona vikosi vya Wakomunisti vimejipanga barabarani, wamekaa kitako, wamelala kingoni wakionekana wachovu sana. Matangazo ya radio yaliwaeleza watu kwamba hawakuwa na haja ya kuliogopa Jeshi Jekundu kwa maana walikuwa rafiki za watu, na kwamba waendelee na mambo kama kawaida. Walisema uhuru ulihakikishwa kabisa.

Siku ya kwanza ya mapinduzi, Ndugu Jones na King walifanya ziara za haraka kwa wahubiri na kuwakuta wote wako salama. Mipango ilikuwa kwamba wangeendesha huduma yao kama kawaida. Kwa kuwa uhakikisho mwingi sana ulikuwa umetolewa kwamba walio wachache na vikundi vya kidini wangelindwa, ilionekana hakukuwa na sababu ya kufanya vingine. Mikutano ya kundi iliendelea kama kawaida, na, kwa kweli, hudhurio liliongezeka. Kwanza ukaribishaji milangoni ulikuwa wa kawaida, lakini ukawa mgumu zaidi na zaidi watu wengi zaidi walipoanza kufuata maenezi ya serikali mpya. Dola ya Kichina (sarafu yao) ikawa sawa na dola milioni 100 kwa dola moja ya United States. Vitabu viliangushwa milangoni kwa dola milioni 10 kila kimoja! Hata mwombaji alikuwa milionea.

Zijapokuwa hali, watu wengi wema sana walishika kweli na kusimama imara mashahidi wa Yehova walipokamatwa na kufungwa, baada ya mapinduzi ya Wakomunisti. Mmoja alikuwa William Koo, ambaye, baada ya kujifunza na Ndugu King na kufanya maendeleo mazuri, mwishowe alipata kuwa mwangalizi wa kundi Shanghai. M. P. Liu aliipata kweli kupitia kwa Ndugu Lew naye akawa mwenye bidii sana katika kazi. Wengine walikuwa jamaa ya Liang, ambao ingawa ilikuwa lazima waadhibiwe na tengenezo walitubu nao waendelea kusimama imara. Basi hawa ni wengine wa watu wabakio katika kumbukumbu ya ndugu zao. Lakini, la maana zaidi Yehova ajua habari zao naye atawathawabisha kulingana na kazi yao.

Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Wakomunisti, Ndugu King alimfikia C. C. Chen. Kijana huyu mwanamume alionyesha kupendezwa isivyo kawaida. Haukupita muda mrefu kabla hajabatizwa na kuchukua kazi za pekee za kuaminiwa kundini. Serikali ya Wakomunisti ilimpa kazi katika kituo cha umeme cha Shanghai chini ya Ndugu Vong ili akapate mazoezi katika ufundi wa umeme. Akina ndugu kundini hawakuwa na habari kwamba C. C. Chen huyu alikuwa amedanganywa na mawazo ya Wakomunisti naye alikuwa akitumiwa nao kama mpelelezi kundini. Baadaye, katika kesi ya Ndugu Jones na King, yeye ndiye aliyekuwa shahidi mkubwa wa mashtaka. Ilikuwa wazi kwamba alikuwa amekuwa akiwapasha Wakomunisti habari kwa muda mrefu.

Miaka ya kwanza mitatu, kazi, kutia na huduma ya nyumba kwa nyumba, iliendelea bila kuzuiliwa. Akina ndugu waliendesha huduma yao wazi kabisa, kwa maana Wakomunisti walikuwa na shughuli nyingi wakianzisha kazi zao wenyewe na usimamizi. Katika mwaka wa 1950 kumi na mmoja walibatizwa. Katika mwaka wa 1951, watu 105 walihudhuria Ukumbusho, na leseni ya kuingiza vitabu nchini kutoka Hong Kong ikapatikana hata ndugu wakaweza kupata vitabu vyote vya Kiingereza vya karibuni.

Ulizo lililoulizwa mara nyingi lilikuwa: Mtu wa maisha ya asili ya Kichina au ya Kibuddha asiye na ujuzi wa Biblia hapo kwanza angeweza kusaidiwa aikubali kweli? Jibu lilikuja wakati Paul Lam alipomshuhudia Helen Lau akiwa katika kazi yake ya kilimwengu, mwenye duka la Kichina la majani ya chai. Ndugu Lam alimwagushia kitabu Salvation cha Kichina na kujitolea amsaidie kuielewa Biblia. Ingawa hakujua Kiigereza kingi, mwanamke huyu alihudhuria mikutano na kuchukua kitabu cha Kiingereza “Let God Be True.” Alianza kushiriki katika hudumu ya shambani, akabatizwa na kuanza kufanya upainia mwaka wa 1954. Karibuni alifanya dada zake wawili wadogo wapendezwe, waliovutwa na urafiki na subira ya Mashahidi, nao pia wakawa watumishi wa Yehova. Ndiyo, ilihakikishwa kwamba kweli ya Biblia ingeweza kushinda mapokeo yenye nguvu ya Kichina.

Funzo jingine lilianzwa na kijana mwanamume ambaye ‘alitaka kujifunza Kiingereza,’ lakini aliyejifunza mengi zaidi ya hilo. Lam Yan Yue na wanashule wengine walianza kujifunza na Ndugu Carnie. Mwishowe wanashule waliacha, lakini urafiki na unyofu wa wamisionari ulimvuta Yan Yue. Yeye hakuogopa kwamba ataacha kumheshimiwa, bali alimshukuru mmisionari ambaye “hakuwa mwoga asisahihishe maoni yangu yenye makosa,” kama alivyosema. Baadaye alibatizwa kisha akaanza kutumikia kama mwangalizi wa kundi.

MAGUMU YAONGEZEKA KATIKA BARA

Kwa kuwa jamii ya Wakomunisti yenye kusimamia mambo ya kisiasa ilikuwa ikitenda kwa ukamili zaidi, ilikuwa lazima wafanya kazi wahudhurie mikutano ya Wakomunisti kabla na baada ya kazi. Kila kibarabara kilikuwa na “halmashauri” yake na mikutano ya kisiasa nao walikuwa wakishtaki watu wo wote ‘wenye kupinga Wakomunisti.’ Usimamizi wa Wakomunisti ulipanuliwa na kusimamia dini pia. Dini zote zilipaswa ziwe na wahubiri Wachina, zipewe fedha na Wachina na kutengenezwa na Wachina. Wo wote wasiopatana na hili walipaswa wajiandikishe. Kwa hiyo ilikuwa lazima mashahidi wa Yehova wajiandikishe.

Mwaka wa 1952 walikuwako wahubiri 22 na kumi na saba wakabatizwa. Sasa maisha yalikuwa yanapata kuwa magumu zaidi kwa ndugu wa nchini. Walitakiwa wajifunze “mawazo ya Mao.” Wakati wa saa za kazi na baada ya hapo walikuwa wakikuta milango imefungwa kufuli mtu ye yote asiweze kuondoka. Ilikuwa lazima wasikilize Ukomunisti ukielezwa kwa saa nne wakati mmoja. Si ajabu kwamba walipata burudisho jingi penye Jumba la Ufalme. Kama alivyoeleza ndugu mmoja, “Jumba la Ufalme dogo katika Shanghai lilikuwa kama chemchemi katikati ya jangwa kavu la uonezi wenye chuki wa kisiasa.” Ndugu zetu wapendwa waliweza kuliokoka jangwa la kiroho la China ya Wakomunisti kwa sababu ya roho ya Yehova na kujilisha Neno lake kwa kawaida. Hawakuvunjika moyo nao walifurahi sana kuona watu 85 wakihudhuria Ukumbusho wa mwaka wa 1953 na watu kumi waliobatizwa mwaka huo.

MWANZO WA MWISHO

Siku moja Ndugu King alipokuwa anahubiri, mlinzi mshupavu wa kibarabara alifanyiza tamasha ya kuchukiza. Bila ya kuwa na habari, Ndugu King alikuwa akielekeana na kundi la watu wenye ukatili. Polisi alikuja na kumwambia Ndugu King alikuwa mwenye kosa kwa sababu alikuwa akifundisha watu na kuchafua amani yao. Siku mbili baadaye wamisionari waliitwa kwenye kituo cha polisi. Amri zilitolewa kwa wazi: “Hakuna kuhubiri nje ya Jumba la Ufalme.” Kutembelea watu ambao mafunzo ya Biblia yalikuwa yanaongozwa nao ndiko kulikoruhusiwa peke yake, nayo majina yao yalipaswa yapelekwe kwa polisi. Lakini, funzo la Biblia halikupotea hata moja.

Sasa akina ndugu waliweza kuona kwamba kazi ingepaswa kuendeshwa kwa busara zaidi. Wazungu walionekana vyepesi, kwa hiyo ikakubaliwa kwamba ndugu Wachina wangeendesha huduma ya shambani nyumba kwa nyumba huku wamisionari wakitoa ushuhuda madukani na kwa wengine waliokutana nao njiani.

Mwanzoni mwa mwaka wa 1954, mmoja wa wamisionari, Lew Ti Himm, alikufa. Alikuwa amekuwa mfanya kazi mwenye bidii na asiyechoka. Mwaka uo huo, ingawa wahubiri kumi walipotea mume mmoja na mkewe walipoadhibiwa, hata hivyo kulikuwa na kilele kipya cha wahubiri wa Ufalme Machi wa mwaka wa 1955, nao akina ndugu wakatumia wastani ya saa 10.6 katika huduma. Jambo kuu la mwaka lilikuwa hudhurio la watu 175 penye Ukumbusho.

Kufikia wakati huu vitabu vingi vilikuwa vimekwisha zuiwa, ingawa magazeti yaliendelea kuja kwa muda. Lakini hivi viliacha kuja mwaka wa 1956. Kwa kweli, hakukuwa na marufuku ya waziwazi juu ya vitabu. Ni kwamba tu havikufika huku. Ndugu King akumbuka hivi: “Hata nakala moja haikupenya. Jama! walikuwa na uchunguzi mkali sana.” Walakini, dada mwaminifu katika Uingereza alisaidia kwa kuandika mambo ya maana ya makala za mafunzo za Watchtower kwa barua za ndege na kuzituma Shanghai.

Katikati ya mwaka wa 1956, matata yalitokea tena. Wahubiri watano walifungiwa na polisi na kuhojiwa kwa saa tano. Nancy Yuen alifungiwa kwa siku nne. Hili lilikuwa onyo ‘kuendesha dini yenu katika kanisa lenu wenyewe tu.’ Ndugu zetu walizidi kuhubiri, lakini kwa busara nyingi. Miezi minne tu baadaye, Nancy Yuen alikamatwa kwa mara ya pili. Alikuwa amekwenda kwenye funzo la Biblia naye hakurudi nyumbani tena. Wamisionari walipouliza juu ya hali yake na mahali alikokuwa walijibiwa vikali: “Hili ni shauri la Kichina. Shikeni lenu wenyewe.” Tangu wakati huo na kuendelea, mama yake aliwaangalia watoto wake wadogo. Aliweza kumtembelea Nancy miaka miwili baadaye katika kituo cha uzuizi. Miaka hiyo Nancy alikuwa amekuwa akihojiwa sikuzote katika jitihada ya kumfanya ashtaki ndugu zake, lakini yeye alibaki mwaminifu kwa Yehova na ndugu zake. Mwishowe alihukumiwa kufungwa. Wakati mmoja Ndugu Jones alimwona kwa mbali katika ua wa jela ya Shanghai ambako yeye alifungwa baadaye.

International Refugee Organization (Tengenezo la Mataifa Yote la Watoro) liliacha kutenda sasa na wale waliokuwa chini ya mamlaka yake walikaa tena katika nchi nyingine. Hivyo Ndugu Mobius, Guettler na Poethko walipaswa waondoke. Mashirika ya biashara ya kigeni yalifungwa na jamaa ya Groezinger ikaondoka. Sasa Ndugu Jones na King walipaswa wafanye kazi nyingi wajiruzuku. Yehova alizibariki jitihada zao, nao wakafurahi kuona watu 107 wakihudhuria Ukumbusho wa mwaka wa 1958.

Baada ya kusanyiko la mataifa yote la mashahidi wa Yehova katika New York mwaka wa 1958, ilipangwa Ndugu Charles, mwangalizi wa tawi katika Hong Kong, arudie Shanghai kwa meli kutembelea ndugu zetu huko. (Ndugu Jones alikuwa ametuma ombi la cheti cha kutoka China alihudhurie kusanyiko hilo akakataliwa, na kwa njia hiyo wakajulishwa hawakuruhusiwa kutoka nchini.) Meli ilipofika bandarini hakuna aliyeruhusiwa kufika ufuoni. Lakini Ndugu Jones na King walisafiri kwa kivukio mtoni wakijaribu kumwona Ndugu Charles. Walimwona kwa mbali na kumpungia mikono, nao ujumbe ukapita. Kwa sauti yake kubwa yenye kuvuma, Ndugu King aliita, “Tafadhali kamwambie Mama sote tu wenye furaha na wazima!” Ndugu Charles akajibu, “watu 250,000 wawatumieni upendo wao.” Bila shaka alikuwa akimaanisha hesabu ya waliohudhuria “Divine Will” International Assembly katika mji wa New York, Julai 27 mpaka Agosti 3.

Hali njema iliyochukuliwa na mashahidi wa Yehova ilikasirisha sana vikundi vingine vya kidini vilivyokuwa vimekubali mara nyingi kufanya vilivyoagizwa. Sasa vilichochea polisi na kulalamika kwamba mashahidi wa Yehova walikuwa wanaruhusiwa waendelee bila kukatizwa na serikali. Hili lilitokeza mambo.

Oktoba 14, 1958, Ndugu Jones na King walikuwa wameamka saa 12:30 asubuhi na mapema, wakatayarisha kiamsha-kinywa chao na walikuwa karibu kuketi Ndugu King alipoona polisi wakikimbia katika kibarabara chao. “Sijui wanamfuata nani sasa,” kasema yeye. Jibu lilikuja mlango wao ulipogongwa kwa nguvu sana. Walikamatwa kama “wataka maasi” nayo nyumba ikapekuliwa-pekuliwa sana. Saa tano baadaye walipelekwa kwenye kituo cha uzuizi, ambako waliendelea kuhojiwa sikuzote kwa miaka miwili.

Penye kesi yao mwaka wa 1960, majina ya ndugu na dada Wachina yalisomwa ikasemekana kwamba hawa wangejaribiwa baadaye. Mwangalizi wa kundi, Ndugu Koo, Ndugu Liu na Nancy Yuen pia walikuwamo katika orodha ndefu ya majina. Hivyo katika Oktoba wa mwaka wa 1958 kazi ya mashahidi wa Yehova ilikomeshwa kwa nguvu katika China.

Mashahidi wa Yehova wako hai sana nao watendaji sana katika shamba hili lenye magumu. Wanajitahidi kutoa ushuhuda na kufanya wanafunzi. Wanaweza kuona kwamba Yehova anaiharakisha kazi nao wana hakika kabisa kwamba ataifungua mioyo ya watu wengi zaidi wenye mfano wa kondoo wajifunze kweli. Ongezeko zaidi lawezekana sana kati ya wapya wengi wanaoshirikiana sasa. Kwa habari ya ndugu zetu wapendwa walioko nyuma ya “Pazia la Mianzi,” twaweza kuwakumbuka katika sala zetu mbele za Yehova. Mara kwa mara, sisi twapata habari wanaendeleza ukamilifu wao katika nchi hiyo. Kama ushuhuda zaidi utatolewa China au sivyo kabla ya “dhiki kubwa” kutokea lazima tuache mikononi mwa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki