Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb92 kur. 42-64
  • Ripoti ya Ulimwengu Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ripoti ya Ulimwengu Pote
  • 1992 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Afrika
  • Esia
  • Ulaya
  • Amerika ya Kilatini
  • Amerika Kaskazini na Visiwa vya Karibea
  • Visiwa vya Pasifiki
  • Nchi Zilizo Chini ya Marufuku
1992 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb92 kur. 42-64

Ripoti ya Ulimwengu Pote

Afrika

Mtunga zaburi aliandika kwamba mwovu “hukaa katika maoteo ya vijiji” na kutoka “mahali pa siri humwua asiye na hatia.” (Zab. 10:8) Muda wa karne zote, waabudu wa Yehova wasio na hatia wamekuwa wakionewa na waovu wasio na huruma. Ndivyo ilivyo leo katika sehemu fulani za Afrika.

Vita vya wenyewe kwa wenyewe katika Liberia viliua ndugu zetu 33 na vimefanya wengine wengi wakimbie nchi hiyo na kutafuta usalama katika Côte d’Ivoire na Sierra Leone, wakitoroka na nguo zile tu walizovaa. Halmashauri za msaada, zilizoanzishwa katika miji miwili kwenye mipaka ya Liberia na Côte d’Ivoire, hazikutunza tu wakimbizi hawa maskini bali pia zilipeleka misaada kwa Mashahidi wenye kuteseka waliobakia Liberia. Mashahidi katika Côte d’Ivoire, Sierra Leone, na Ghana walipakia tani nyingi za nguo, pamoja na dawa, vyakula, na pesa, kuingiza katika Liberia. Akina ndugu katika Abidjan pia wametoa msaada wa haraka na kwa wororo wanashughulikia kikundi kikubwa cha wakimbizi ambacho pia kina uhitaji mkubwa.

Wengi wa ndugu hawa wameona mambo ya kushtusha na yenye kusikitisha. Kwa mfano, mzee mmoja anayetumikia katika Monrovia, jiji kuu la Liberia, akumbuka: “Katika Julai 27, 1990, familia yangu nami tuliondolewa nyumbani mwetu kwa nguvu kama saa nane hivi usiku. Waasi hao walitutoa nje, ambapo tuliungana na mamia ya majirani zetu. Tulihakikishiwa kwamba baada ya upekuzi mfupi wa sehemu hiyo, tungerudi nyumbani. Hatukuona nyumba zetu tena. Badala yake, tuliongozwa hadi kwenye kambi kuu ya wakimbizi umbali wa kilometa 50. Mgongoni nilimbeba shangazi ya mke wangu ambaye hajiwezi, kwa mwendo huo wote. Tulimwomba Yehova nguvu wakati wote, tulipoona miili mifu imetapakaa kila mahali.

“Baada ya muda wa saa moja hivi wa kuyumbayumba kwa hofu huku tukisindikizwa na waasi waliokuwa nyuma yetu, tuliingia kwenye mtego wa ushambulizi wa askari wa serikali. Risasi zilirushwa kutoka kila upande huku tukijitupa chini. Watu wengi waliuawa; wengine walitoroka. Kwa ghafula, niling’amua kwamba mwana wangu mwenye miaka 14 alikuwa hayupo! Upesi, tukiwa watu 45 wa mji tulikamatwa na kupelekwa kwenye stesheni ya petroli iliyoachwa ukiwa. Halafu ikaamuliwa kwamba sisi sote tungeuawa. Askari mmoja akachukua bunduki yake ili anipige risasi, lakini alishindwa kutia kibano cha risasi katika bunduki yake. Wakati huo huo, kamanda wa kikundi hicho aliwasili na kuamuru tuchukuliwe hadi kwenye makao ya wanajeshi. Usiku huo, watu tisa waliuawa. Tulimwomba Yehova atusaidie tuendelee kuwa waaminifu.

“Asubuhi iliyofuata kamanda aliamua kwamba sisi sote tungeweza kuondoka. Hata alijitoa kutupeleka kwenye moja la malori yake. Tulikataa na badala yake tukauliza tupewe wilibaro ambayo tungebebea shangazi ya mke wangu, halafu tukaondoka peke yetu. Tukiwa katikati ya safari yetu, malori ya kijeshi yalitupita. Yalipofikia makutano ya barabara mbele yetu, mlipuko mkuu ulitokea. Kutupwa kwa risasi kwa bunduki ya kumimina risasi kulifuata kwa muda wa dakika 30 hivi. Risasi zilizokosa shabaha zilipita kasi kila upande huku tukikimbilia majificho. Kikosi cha askari kilichokuwa kimejitoa kutusafirisha kiliangamizwa chote. Jinsi tulivyoshukuru kwamba hatukukubali toleo la kamanda kusafiri kwa gari!

“Ingawa mke wangu alikuwa mjamzito wa miezi mitano, alijikakamua kijasiri kutembea kilometa 58 katika siku moja tu. Bado tulikabiliwa na tatizo la kutoroka. Ndugu mmoja Mlebanoni alipojua juu ya tatizo letu alipanga kulipia nauli zetu za basi zee lililokuwa tu ndiyo njia ya usafiri ya kuondoka nchi hiyo.

“Hatimaye tulifika salama ng’ambo ya mpaka kuingia Côte d’Ivoire. Hata hivyo, tulihuzunika sana kwa sababu hatukujua alikoenda mwana wetu wa miaka 14 wakati wa ushambulizi uliotajwa mapema. Tulifikiri kwamba alikuwa amekufa, kwa kuuawa. Hata hivyo, kwa shangwe yetu kuu, tulifahamishwa miezi sita baadaye kwamba aliokoka. Mipango ilifanywa ili aweze kuungana nasi hapa katika Côte d’Ivoire.”

Mashahidi wengine waliona maono ya kuogofya. Clement kutoka Naijeria alikuwa ameishi kwa miaka 17 katika Monrovia, lakini alilazimika kukimbia. Majeshi ya waasi yalikuwa yanatafuta Wanaijeria na Waghana wote waliokuwa nchini. Ikiwa waasi wangemkamata, angepigwa risasi. Vituo vingi vya ukaguzi kufikia mia moja, kutoka Monrovia hadi Danané katika Côte d’Ivoire, vilikuwa kati ya Clement na usalama. Yeye aliweza kupita vingi vya vituo hivyo kwa kusema kwamba alikuwa mgeni aliyetaka kuondoka nchini. Kwenye kimoja cha vituo hivyo, elezo lake halikufanikiwa. Ilikuwa kwamba atauawa. Clement aliamua kutoa ushahidi mzuri kabla ya kuuawa. Alimhubiria kamanda kuhusu Ufalme wa Mungu na kumwonyesha magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa kupigwa butaa, kamanda alivuma akisema: “Sikiliza, sisi tuna kazi ya kutimiza kwa wakati huu. Tutakapomaliza, tutaangalia unayosema. Sasa, ebu ondoka!”

Baadaye, Clement alipopata utulivu wa akili kuweza kuwazia tukio hilo, alisema kwamba ajua kile Mithali 18:10 inachomaanisha inaposema kwamba jina la Yehova ni ngome imara. Ilikuwa tu ni kwa kutumia jina la Yehova na kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu kwamba aliweza kupita vituo vile vingine vilivyobakia. Hatimaye, alivuka mpaka na kuingia Côte d’Ivoire. Alikuwa amefikia usalama! Wengine wa wafanyakazi wa ofisi ya tawi hivi majuzi waliweza kurudi Liberia.

Si nchi zote zilizo na hadithi ya kuhuzunisha. Msumbiji inatupa sababu nzuri ya kushangilia. Katika Februari 11, 1991, serikali ya Maputo ilikubali kutambuliwa kisheria kwa shirika liitwalo Mashahidi wa Yehova wa Msumbiji. Tuna shukrani nyingi sana kwa tokeo hilo kwa sababu lamaanisha kwamba wamisionari waweza sasa kupewa makao katika Msumbiji. Vichapo na magazeti yanaweza sasa kuingizwa nchini bila kizuizi. Makao ya wamisionari yameanzishwa katika majiji matatu, yakiwa na nafasi ya kutosha jumla ya wamisionari 18. Depo ya Sosaiti imo katika kila moja la makao hayo.

Hata hivyo, vijana wahitaji wadumishe kutokuwamo kwao na kuonyesha ushikamanifu wao kwa Yehova wakati wa vita vya kuvizia vinavyoendelea katika nchi hiyo. Msichana mmoja wa miaka 12 ambaye ni kiziwi na bubu alitekwa nyara na majeshi ya waasi kwa makusudi ya kingono. Lakini wazazi wake walikuwa wamemzoeza vema kwa kanuni za Biblia. Wale waliomkamata walipotaka kumnajisi, alikataa katakata. Dada huyo mchanga angeelekeza kidole mbinguni kuonyesha kwamba ukosefu wa adili ni kinyume cha sheria za Mungu. Kwa sababu ya kuazimia kwake imara, siku moja wale waliomkamata walimpiga kikatili na kumwacha wakidhani kwamba amekufa. Miezi miwili ilipita kabla hajarudi kwa wazazi wake, akiandamana na mwanamke aliyekuwa naye wakati wa kutekwa kwake. “Sijui yale mliyofundisha msichana huyu mchanga,” mwanamke huyo akasema, “lakini ninavutiwa na mwenendo wake wa adili. Yeye hakukubali kushindwa na mbano wa askari-jeshi. Alikuwa wa kutokeza sana! Dini yenu ni ipi?” Kwa sababu ya msimamo thabiti wa dada huyo kiziwi, mwanamke huyo sasa anajifunza na Mashahidi na anafanya maendeleo mazuri katika kujifunza kweli.

Esia

“Baraka yako na iwe juu ya watu wako,” Mfalme Daudi wa kale akaimba. (Zab. 3:8) Leo, baraka ya Yehova i juu ya watu wake pia. Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika nchi zilizoko katika Esia wanaweza kutoa ushuhuda wa jambo hilo hakika.

Katika Korea uhai wa dada mmoja uliokolewa kwa njia isiyo ya kawaida kwa kutembea akiwa na Hati ya Kitiba. Alipokuwa akitoka kwenye gari lake alilokuwa ameegesha, kwa ghafula alishambuliwa na watu wanne, waliomwingiza kwa nguvu nyuma ya gari lake na kumlaza kwenye sakafu. Alitoa pete yake na kibeti chake ili wamwachilie huru, lakini hawakuridhika. Fikira yenye kuhofisha kwamba huenda wakamshambulia kingono ikaja akilini mwake. Akaanza kupiga mayowe kwa kadiri alivyoweza. “Tutalazimika kumuua,” mmoja wa wanaume hao akafoka. Akadungwa kisu mguuni na pajani. Kisha wakafunga macho yake kwa ugwe na wakafunga miguu yake pamoja. Kwa kukata tamaa, alianza kusali na kulia kwa sauti, akitumia jina la Yehova.

Kwa ghafula, wanaume hao wakanyamaa kimya kabisa. Mwishowe, mmoja wao akauliza: “Bibi, je! wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Walikuwa wamepata Hati ya Kitiba yake walipopekuapekua ndani ya kibeti chake. Wakaamua kwamba hawatamuua lakini wakampeleka kwa gari hadi karibu na nyumbani kwa dada huyo, wakamwacha ndani ya gari, na upesi wakatoweka. Dada huyo asali kwamba wanaume hao wote watatubu tendo lao la ukosefu wa sheria wawe waabudu wa Yehova.

Kama ilivyo katika nchi nyingi, wake wa nyumbani zaidi na zaidi katika Japani wanajiunga na jamii ya wafanyakazi, jambo ambalo linafanya iwe vigumu kuwafikia nyumbani na habari njema. Hivyo dada mmoja painia katika Jiji la Niigata aliamua kupeleka ujumbe wa Ufalme katikati ya jiji—ambapo watu walikuwa. Alipata eneo la kibiashara kutoka kundi lake akaanza kuhubiri, akiwatolea kifupi watu wa biashara ambao alikutana nao funzo la Biblia nyumbani. Yeye alitumia broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” na akafuatia waliopendezwa kwa kufanya ziara za kurudia kwa wote walioonyesha kupendezwa hata kwa kiasi kidogo. Alidokezea wenye kupendezwa kwamba wangeweza kujifunza kwa dakika 30 katika mkahawa, sebule ya duka kubwa, au katika bustani wakati wa chakula cha mchana. Katika kila kipindi cha somo, yeye huelekezea fikira kwenye jambo moja tu na amekuwa akiongoza mafunzo manane kwa pindi moja katika eneo hilo la kibiashara.

Wafilipino zaidi ya 60,000 wamekuja kutoka Ufilipino ili kufanya kazi za nyumbani katika nyumba za Wachina kwenye kisiwa cha Hong Kong. Wengi wa wafanyakazi hawa ni Wakatoliki wa Roma. Dada mmoja alikutana na mtu kama huyo kwenye mtambo wa kupandisha watu orofani na akamwuliza tu kama angependezwa kujifunza mengi juu ya Biblia. Jibu lilikuwa: “Nimekuwa nikisali ili nijifunze mengi juu ya Biblia.” Funzo la Biblia lilianzishwa upesi jinsi hiyo.

Katika Saiprasi mhubiri mchanga kutoka Nikosia aandika hivi: “Jina langu ni Marcos; nina umri wa miaka 12. Katika somo la mafunzo ya kidini, mwalimu alipangia kuwe na masomo matatu kuhusu dini. Nilihakikisha kwamba nimeleta darasani kitabu Mankind’s Search for God. Kabla ya somo la kwanza kuanza, nilimwonyesha mwalimu kitabu hicho. Aligeuzageuza kurasa zacho halafu akakiweka juu ya dawati lake. Baadaye kidogo akaambia darasa: ‘Nitatumia kitabu cha Marcos kwa mafunzo, kwa sababu kina habari nyingi zaidi kuliko kitabu kilichoandaliwa na shule.’” Kijana Marcos amalizia: “Ninatia moyo vijana wote walio wahubiri kuwa na vichapo vya Sosaiti kila wakati shuleni.”

Lucas, ambaye alizaliwa akiwa Mkatoliki wa Roma, alianza kujifunza Biblia katika Sri Lanka. Alikuwa mmoja wa wanaume wanne waliofanya kazi kwenye mashua ya uvuvi iliyokuwa ya Mbuddha. Mwajiri wake alitaka kupata baraka za miungu wa baharini katika biashara yake ya uvuvi, hivyo akauliza wanabaharia hao kufunga safari ya hija kwenye kitovu maarufu cha ibada cha waamini wa Uhindu na Ubuddha. Lucas akaeleza kwamba hangeweza kushiriki, kwa sababu aliamini kwamba Yehova ndiye Mungu pekee wa kweli. “Utajiunga nasi au ufutwe kazi!” mwajiri akasema kwa ukali. Lucas akajiuzulu mara moja. Akarudi kwenye kijiji chake na kwa muda wa siku chache tu akapata kazi kwenye mashua nyingine. Sasa anaweza kujifunza kwa ukawaida.

Wakati Bangnam, mwanamke kijana aliyeolewa anayeishi katika Thailandi alipoanza kujifunza Biblia, wazazi wake wakawa wagonjwa. Wazazi hao walimwendea mganga aliyesema kwamba roho za watu wa ukoo wao waliokufa hazikutoa idhini ya binti kubadili dini yao, na ikiwa wazazi wake wangetaka wapone, ingewalazimu wasimamishe masomo ya Biblia ya binti yao. Wazazi hao walimwomba binti yao aache kujifunza. Painia wa pekee aliyekuwa anajifunza na Bangnam aliwaonyesha wazazi hao katika Biblia kwamba haingeweza kuwa ni roho za waliokufa ndizo zinazoleta tatizo hilo, bali ni roho waovu. (Mhu. 9:5, 6) Ndipo wazazi hao walipoamua kwamba wanapaswa kupeleka binti yao mbali sana. Hata hivyo, dada huyo akawaonyesha jinsi Biblia inavyofunza watoto kupenda wazazi wao na jinsi Bangnam alivyotaka kuishi nao na kuwatunza kwa sababu aliwapenda. Mama yake aliposikia hayo, alitulia akakubali kwenda pamoja na dada huyo kumwona daktari wa kitiba kwenye mji. Daktari hakupata ugonjwa wowote. Walipokuwa wanarudi nyumbani, kulikuwa na mvua kubwa, na kwa kuwa usiku ulikuwa ukikaribia, huyo painia wa pekee akadokeza kwamba mama huyo alale nyumbani kwake. Asubuhi iliyofuata mama ya Bangnam aliamka akiwa ameburudika na alikuwa na msisimuko mwingi, kwa sababu alikuwa amelala vema usiku wote bila tatizo lolote la kupumua. Baba alipojua juu ya maendeleo ya afya ya mke wake, alikubali kuondoa vitu vyote vya uwasiliani-roho. Upesi afya yake ikawa nzuri pia. Bangnam amebatizwa, na mume wake anafanya maendeleo kuelekea wakfu.

Than huishi Myanmar. Yeye alikuwa askari-jeshi, lakini kazi-maisha yake ilikwisha na akakata tamaa sana. Maisha yake ya kukata tamaa yalianza hivi: Wakati wa mapigano makali na majeshi ya waasi, kombora lililipuka karibu na kificho cha chini ya ardhi ambapo alikuwa amejificha. Kificho hicho kiliporomoka, kikizika nusu ya mwili wake. Baada ya kufukuliwa kutoka chini ya bomoko hilo, kwa kushangaa kwake aligundua kwamba hangeweza kusogeza miguu yake—alikuwa amepooza. Upesi akaondolewa jeshini. Akiwa katika hali hiyo ya kukosa tumaini, akaanza kutafakari juu ya mabaya yaliyompata, akapoteza imani yote katika Mungu, akafikiria kujiua. Wakati uo huo, ndugu mmoja painia wa pekee alikuwa akimtembelea jirani ya Than akiongoza funzo la Biblia kwa ukawaida. Than alipojua ni nani yule aliyekuwa akizuru kwa ukawaida, alimkaribisha nyumbani mwake pia. Painia huyo alimtia moyo Than kwa Maandiko. Funzo la Biblia lilianzishwa. Haikuchukua muda mrefu kwake kutambua kwamba hiyo ndiyo kweli, naye kwa msisimuko akaanza kutoa ushahidi kwa wengine. Pia alitaka kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, ambalo liko kilometa 8 hivi kwa umbali. Alipata magurudumu mawili ya baiskeli yaliyokuwa yametumiwa na kujijengea kigari cha kusukuma. Akiwa na azimio kubwa, yeye hujivuta na kujisukuma mwenyewe akipanda na kushuka miteremko hadi kwenye Jumba la Ufalme na huhudhuria mikutano kwa ukawaida. Sasa yuna tumaini jangavu la wakati ujao ulio bora badala ya kuwa mwenye kukata tamaa sana.

Ulaya

“Nafsi yetu imeokoka kama ndege katika mtego wa wawindaji, mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la BWANA [Yehova, NW].” (Zab. 124:7, 8) Jinsi Zaburi hii ielezavyo vema ndugu zetu katika Ulaya ya Mashariki!

Mwaka uliopita wa utumishi ulikuwa wa kutokeza kwa historia ya Mashahidi wa Yehova katika Urusi. Mbali na vilele vya kutokeza katika hesabu za wahubiri na mapainia, vilele saba vya maangusho ya vitabu na vilele kumi vya maangusho ya magazeti vilitoa sababu nyingine kwa ndugu zetu kushangilia katika uhuru wao mpya waliopata. Vilele hivyo vilipatikana kwa sababu, kwa mara ya kwanza kabisa, safirisho la vichapo lingeweza kupokewa.

Jumatatu, Machi 18, 1991, tawi la Ujerumani lilipeleka lori la kwanza, likiwa na karibu tani 20 za vichapo, hadi Urusi. Kabla ya hilo, akina ndugu walipokea vichapo vyao katika vifurushi vidogo kwa posta. Ilikuwaje wakati lori la kwanza lenye vichapo lilipowasili?

Ilikuwa usiku wa manane katika mji wa Lvov, wakati mzee mwenyeji alipojibu simu isiyotazamiwa. Ni tawi la Ujerumani lililokuwa likipiga simu kumjulisha kwamba lori kubwa lenye kichwa cha manjano na kiwiliwili cha buluu lilikuwa likipakiwa vichapo ambavyo vingeelekea Urusi. Walikubaliana juu ya mahali pa kukutana—mpaka wa Polandi-Urusi. Kufikia wakati ambapo Mashahidi wa Urusi walipofika kwenye mpaka Jumatano, hali ya hewa ilikuwa imegeuka kuwa baridi sana. Bila kutishwa na baridi kali na mvua iliyochanganyikana na theluji, akina ndugu walichukua zamu ya kuchunguza kila lori lililokuwa linakaribia mpaka. Mmoja wao alisema: “Tumekuwa tukingoja wakati huu wa maana kwa muda wa miongo ya miaka. Hivyo, tunaliona kuwa pendeleo kungoja kwa saa kadhaa au labda hata siku kadhaa.”

Hatimaye, Ijumaa Machi 22, saa mbili kamili asubuhi, lori la kichwa cha manjano na kiwiliwili cha buluu lingeweza kuonwa likielekea kwenye mpaka. Kutoka kwenye vina vya mioyo ya akina ndugu sala zilipanda kuelekea mbinguni. Lori hilo lilipita mpaka likaingia kwenye udongo wa Urusi. Wakati maofisa wawili wa forodha waliotatanishwa walipoona kiasi cha vichapo hivyo, walishindwa jinsi ya kushughulika na hali hiyo wakaanza kuzungumzia jambo hilo. Baada ya ukaguzi wa hati na mizigo, maofisa walitikisa vichwa vyao kwa ukubali na wakaruhusu lori hilo lipite kwa kuashiria haraka kwa mikono yao. “Shangwe yetu ilizidi sana!” akina ndugu wakasema walipokumbuka mambo ya nyuma. “Baada ya miongo mingi ya miaka ya mateso makali, ndugu zetu hatimaye wanapata chakula kingi cha kiroho.”

Ruhusa ya kupakua mizigo kwenye lori ilitolewa. Ndugu zaidi ya 70 walingojea kwa hamu kusaidia katika kazi hiyo. Walifanyiza mistari miwili ya kupitisha mizigo, vifurushi vya fasihi vikipitishwa kama kwamba kwa upatano wa kimuziki, kutoka mkono hadi mkono. Jumamosi, siku iliyofuata, akina ndugu walikuja kutoka maeneo ya mbali kotekote katika bara hilo kubwa ili wachukue vichapo. Ndugu wawili waliokuwa wamesafiri kilometa 3,520 walikuwa wa kwanza kufika. “Yehova Mungu alifanya yale ambayo hakuna mtu awezaye kuyafanya, nasi tulikuwa mashahidi wa matukio hayo,” akasema mmoja wao.

Kutoka mji wa Dresden katika ile iliyoitwa hapo kwanza Ujerumani Mashariki laja ono hili: “Kwa muda mrefu, mke wangu nami tulikuwa tumejaribu kuwasadikisha wazazi wangu wakubali kweli, lakini yote tuliyopata ni upinzani. Hata hivyo, katika Novemba 1988 mke wangu alilazimika kwenda hospitali kwa majuma matatu. Tulilazimika kumwacha binti yetu Sara, mwenye miezi 18 katika utunzaji wa nyanya na babu.

“Mambo yalianza kutendeka siku hiyo ya kwanza. Walipokuwa kwenye meza ili kula kiamshakinywa, Sara alishangaa ni kwa nini nyanya na babu waliketi tu na kuanza kula. Hivyo akamdukua nyanya yake, akakunja mikono yake, na kusema: ‘Nyanya, sali!’ Akainamisha kichwa chake na kufunga macho yake kabisa. Nyanya hakuitikia; Sara akarudia ombi lake. Hatimaye, mama yangu akang’amua kile Sara alichotaka, kwa hiyo akasema sala ya bwana kama vile Walutheri wafanyavyo. Jioni hiyo mama yangu aliniuliza sisi ni wa dini gani. Yeye alijua tu kwamba tulikuwa tumejiuzulu kutoka kanisani. Yeye hakuwa ameturuhusu tueleze lolote jingine. Nikamweleza mambo mengi. Nyanya akakubali kumtendea Sara kwa njia ile aliyozoea kutendewa nasi, hivyo nikampa Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, kwa sababu Sara alizoea kusikia hadithi kila jioni.

“Sara alimfanya nyanya amsomee hadithi tatu au nne kila usiku. Wazazi wangu walishangazwa kuona maarifa ya Biblia ambayo Sara alikuwa nayo, kwa sababu wakati mwingine angeweza kukatiza hadithi na kuimalizia yeye mwenyewe. Mama yangu akaanza kuwa mdadisi wa yale aliyokuwa akimsomea Sara usiku baada ya usiku. Katika Mei 1990 tulianza funzo la Biblia nyumbani pamoja na wazazi wangu. Upesi wakajiuzulu kutoka ushirika wa kanisa wakaja kwenye mikutano pamoja nasi. Mwaka mmoja baadaye, katika Mei 1991, mama yangu akawa mhubiri asiyebatizwa na sasa anajitayarisha kubatizwa. Baba yangu pia anafanya maendeleo mazuri. Tunamshukuru Yehova kwa kumtumia msichana wetu mchanga na kitabu Hadithi za Biblia ili kutimiza jambo tulilokuwa tumejaribu kufanya kwa muda mrefu bila kufanikiwa.”

Katika Austria vijana wengi wanachukua msimamo thabiti kwa ajili ya ibada ya kweli. Mfano mmoja ni Melanie, msichana wa miaka 11. Kwa sababu ya hali za familia, dada wa kambo alipewa daraka la kutunza Melanie likitwaliwa kutoka kwa mama yake. Dada huyo wa kambo pamoja na mume wake wakaanza kujifunza Biblia kwa msaada wa Mashahidi wa Yehova, na Melanie akajiunga pia. Wote wakafanya maendeleo mazuri. Melanie alitaka kuacha Kanisa la Katoliki. Hata hivyo, kulingana na sheria ya Austria, hilo laweza kufanywa tu baada ya kufikia umri wa miaka 14. Je! hilo lilimzuia Melanie? La! alienda kwa mkurugenzi wa Ofisi ya Masilahi ya Vijana akajulisha tamaa yake. Baada ya mahoji mkurugenzi huyo alisema hivi katika barua kwa Melanie: “Baada ya kufikiri kwa uzito, ningependa kukujulisha kwamba ninatoa ruhusa uache Kanisa la Katoliki. Hata hivyo, kwa sababu ya sheria iliyopo, itakuwa lazima pia kwa mahakama kukubaliana na uamuzi ambao nimefanya.” Kwa hiyo ilimlazimu Melanie kuwa mbele ya hakimu akiwa peke yake na kutoa sababu za kwa nini alitaka kuliacha kanisa. Septemba 21, 1990, alipata uamuzi mzuri wa mahakama fulani ya kwao. Ulikuwa ushindi bora kama nini kwa msichana wa miaka 11! Melanie sasa anashiriki kwa shangwe katika kazi ya kuhubiri akiwa mhubiri asiyebatizwa.

Mwanamke mmoja katika Finlandi, baada ya kujeruhiwa vibaya katika aksidenti ya gari, alikuwa amelala hospitalini, akifikiri: ‘Ikiwa uhai wangu ungalikoma, je! uzima ungalikuwa ndio uo huo tu?’ Aliporudi nyumbani, alitafuta jibu katika Biblia lakini hakupata lolote. Akatweta hivi: “Mungu mbinguni, tafadhali, acha nijue kusudi la maisha. Ninajua lapasa kuwa katika Biblia. Ninakuomba kwa moyo, unisaidie nilielewe.” Dakika kumi hazikuwa zimepita wakati kengele ilipolia, na ni nani aliyekuwa amesimama kwenye mlango? Mmoja wa Mashahidi wa Yehova mwenye tabasamu changamfu. “Nilishtuka,” akasema. “Fikira yangu ya kwanza ilikuwa: ‘Ooh, la! Mbona awe tu ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?’ Lakini nilijizuia na nikamwambia aingie ndani. Tangu wakati huo uelewevu wangu wa Biblia umeendelea kuwa bora.”

Amerika ya Kilatini

“Nitamshukuru BWANA [Yehova, NW] kwa kadiri ya haki yake; nitaliimbia jina la BWANA [Yehova, NW] Aliye juu.” (Zab. 7:17) Kwa mwaka wa utumishi uliopita, zaburi hiyo ya Daudi imekuwa kichwa kikuu kwa wahubiri wanaoishi katika Amerika ya Kilatini.

Je! muda wa kujifunza mageuzi unapasa usawazishwe na wa kujifunza uumbaji pia? Hilo ni swali linaloulizwa mara nyingi katika Ekwedori. Katika mji wa bandari wa Guayaquil, mwalimu mmoja aliamua kufikiria habari iliyo katika kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? pamoja na wanafunzi wake 104. Mwishoni mwa muhula wake wa shule Januari iliyopita, aliwauliza wanafunzi wake mfululizo wa maswali. Moja lilikuwa: “Kwa kufikiria ithibati yote ya kisayansi na Kibiblia iliyotolewa katika darasa hili, mmefikia uamuzi gani kuhusiana na asili ya uhai?” Majibu mengi yalipendelea uumbaji wa kimungu. Mwanafunzi mmoja alijibu: “Nimefikia uamuzi wa kwamba dunia na vyote vilivyomo ndani yayo lazima viwe vilifanyizwa na mtu ambaye alifanya mambo kikamilifu. Ni lazima kuwe kulikuwa na mtu ambaye alikuwa mwenye upendo sana na ambaye alikuwa na kusudi kwa watu wanaoishi hapa. Ni jambo lisilo la akili kufikiri kwamba kitu tata kama vile watu walio hai kingeweza kuumbwa kwa nasibu. Ni jambo lisilowezekana kwa mwanadamu kuumba kitu tata kama uhai.”

Kweli ya Biblia imekuwa na tokeo kubwa kwa mwalimu huyu hivi kwamba yeye mwenyewe alibatizwa katika Desemba, 1990. Wanafunzi wake 42 walikuwako ili kushuhudia ubatizo wake katika kusanyiko la mzunguko la kwao. Ikasadifu kwamba, kumbe wanafunzi 31 kati yao walikuwa nao wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova katika Guayaquil!

Mwanafunzi wa Biblia anayeishi katika sehemu ya ndani ya Guyana karibu na Mto Moruka hujifunza kwa njia ya barua. Mwanamke huyu alitamani sana kuwako katika ibada safi pamoja na Mashahidi wa Yehova kwenye usiku wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kwa gharama kubwa alikodi mtumbwi na akiwa na mwana wake wa miaka 13 na binti mwenye miaka 12 akauendesha mtumbwi kwa saa 21 hadi kwenye kundi la karibu zaidi katika Charity. Safari hiyo ilimlazimu kusafiri katika Mto Moruka hadi kwenye Bahari ya Atlantiki na kuuendesha kurudi tena kwenye bara katika Mto Pomeroon. Aliondoka saa 3:30 ya usiku na kufika saa 12:20 ya jioni siku iliyofuata, akisimama kwa muda wa saa moja tu kupumzika. Baada ya Ukumbusho ilimlazimu kurudi mara moja, kwani mtumbwi huo ulikuwa ukikodiwa kwa siku moja tu. Yeye ni mhubiri asiyebatizwa na katika wakati huo wa Ukumbusho alikuwa mjamzito miezi minne!

Machi iliyopita katika Venezuela, padri mmoja wa Katoliki ya Roma alikuja kwenye ofisi ya tawi akitaka fasihi. Halafu akaomba aweze kuzungumza na mtu kuhusu mambo fulani ya mafundisho fulani. Alijieleza kuwa ana umri zaidi ya miaka 65 na kwamba ametumika akiwa padri kwa miaka 37. Alisomea upadri katika Roma, Italia. Kwa miaka minne iliyopita, alikuwa akisoma habari zinazohusu mabaraza ya Kanisa la Katoliki na aligutushwa na yale aliyopata. “Kanisa liko mbali na kweli,” akasema.

“Siku hizi nimekuwa nikisoma zaidi Biblia kuliko katika maisha yangu yote,” akasema. “Nimevurugika. Mafundisho ya kanisa hayapatani na Biblia. Ninalazimika kufundisha, lakini dhamiri yangu hainiruhusu kufundisha uwongo. Ninatafuta njia ya kutoka katika mateso hayo. Nimeweka maisha yangu yote kuwa wakfu kwa kanisa; sasa mimi ni mzee, na ninaweza kufanya nini katika umri wangu? Ningepata kazi wapi? Ninaishi katika makao mazuri, nina gari la anasa, nina pesa katika benki, lakini nikiacha kanisa, nitapoteza yote haya. Sijui nifanyeje.”

Ndugu huyo akamwonyesha maandiko kadhaa yanayothibitisha kwamba Yehova haachi wale wanaomtumikia Yeye. Akijua kwamba huyo padri alikuwa amejifunza Kigiriki, ndugu huyo akamwonyesha Biblia The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures, akimfungulia katika Mathayo 10:28. Kwa kusisimuka, padri huyo akasema, “Lakini hilo ni wazi kabisa kabisa—nafsi hufa! Kwa hiyo huo umekuwa uwongo mwingine!”

Baada ya kuzungumza kwa muda fulani, ndugu huyo akamuuliza padri huyo kwa nini alikuwa amekuja kwenye ofisi ya tawi. Jibu lake lilikuwa la kupendeza sana. Mhubiri mwenye umri wa miaka 14 aliingia katika kanisa lake katika Karakas, akamkuta bibi mmoja akiomba, na kumwuliza alikokuwa padri. “Huko nyuma,” ndilo lilikuwa jibu. Hivyo ndugu huyo kijana akaenda nyuma ya kanisa na kupata ofisi ya padri. “Wataka nini?” padri akamuuliza mvulana huyo. Mhubiri wetu kijana akasema kwamba alikuwa amekuja kuzungumza juu ya Biblia; akamwambia padri kwamba Babuloni Mkubwa ataharibiwa, na ikiwa padri hangetoka katika dini bandia, yeye pia angeharibiwa. Padri huyo alishangaa sana kuona kwamba mvulana wa miaka 14 angeweza kueleza mambo mengi hivyo kwa ujasiri kwa mtu wa umri wake hivi kwamba hangeweza kusema. Mhubiri huyo mchanga akamweleza mahali ofisi ya tawi ilipo. Hiyo ndiyo sababu padri huyo alikuja kwenye ofisi.

Baada ya mazungumzo ya saa mbili, padri huyo akaondoka. Tunatumaini kwamba atakuwa na ujasiri kukabiliana na wakubwa wake na kuikubali kweli.

Amerika Kaskazini na Visiwa vya Karibea

Mashahidi katika Amerika Kaskazini na visiwa vya Karibea hurudisha mwangwi wa maneno haya ya mtunga zaburi Daudi: “Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA [Yehova, NW]. Naam, vyote vilivyo ndani yangu vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA [Yehova, NW], wala usizisahau fadhili zake zote.”—Zab. 103:1, 2.

Nyakati fulani, watu mmoja mmoja wanaopendezwa huenda wakawa na maoni kwamba wao ni wazee zaidi kuweza kubadili dini. Hata hivyo, mwanamke mmoja mzee katika British Columbia, Kanada, hana maoni kama hayo. Alijulikana sana katika jumuiya yake ndogo, kwa sababu alikuwa mwalimu wa sanaa na mmoja wa wategemezaji wakuu wa Kanisa la Anglikana. Yeye mwenyewe alikuwa amelipia altare katika kanisa na alikuwa msomaji asiyehitimu katika mahubiri ya kidini. Kwa kuwa alipendezwa na Biblia, alikuwa anapelekewa magazeti kwa ukawaida na Mashahidi wenyeji kwa miaka kadhaa lakini hakuwa amefanya maendeleo zaidi ya hapo. Miaka mitano hivi iliyopita, binti yake na mume wa binti yake walihamia nyumba yake, kwa kusingizia eti walitaka kumsaidia katika miaka yake ya uzee. Hata hivyo, wao waliwapinga Mashahidi wa Yehova wakamsumbua-sumbua mama yao ahamie makao ya kutunzia walio wazee-wazee. Bila shaka yeye hakuwa tayari kwa hilo! Wakati binti yake na mkwe wake walipokuwa wameenda safari ya likizo, yeye alihamia nyumba ya kufungashwa kwa gari.

Hatimaye, dada mmoja alitumia mfikio wa moja kwa moja, akaonyesha njia yetu ya kujifunza Biblia, kisha akamwuliza kama angependezwa na kujifunza Biblia. Itikio lake lilikuwa: “Nilikuwa nikiwaza ungeniuliza lini!” Kwa vile alivyokuwa anaamini Biblia kwa moyo mweupe, alielewa upesi kweli za msingi za Biblia, akisema: “Ikiwa limo katika Biblia, basi lazima liwe kweli.” Hata hivyo, aliendelea kuhudhuria kanisa lake, akihisi kwamba kwa njia hiyo angeweza kusaidia washiriki wenzake wa kanisa.

Baada ya kujifunza kwa muda wa mwaka mmoja na nusu, akapata habari kwamba askofu mkuu wa Kanisa la Kianglikana, aliye kwenye makao makuu alikuwa ametumia vibaya fedha za kanisa na alikuwa ameenda katika safari ya likizo Karibea pamoja na karani wake, hata ingawa alikuwa mwanamume aliyeoa. Pia alipata kujua kwamba askofu mkuu huyo alikuwa amejaribu kulaumu shemasi wa kanisa kwa utumizi huo mbaya wa fedha. Kisa hiki chote kilifichuliwa wakati wa mazungumzo ya wote yaliyopamba moto katika kanisa. Wakati wa mazungumzo hayo, alimwita askofu huyo “mnafiki mzee,” kisha akatoka kanisani na kufunga mlango kwa nguvu nyuma yake, asirudi tena kamwe.

Alipohudhuria mikutano kwa mara ya kwanza katika Jumba la Ufalme, mwanamke huyo alisema: “Siamini jinsi mlivyo na wanaume wengi na jinsi wanavyohusika na kuwa watendaji katika mambo ya kundi. Katika kanisa nilimokuwamo, wanaume wachache waliokuja waliketi tu na kulala usingizi.” Alibatizwa siku ya Septemba 29, 1990, akiwa na umri wa miaka 87.

Baada ya ziara yake ya hivi karibuni katika Greenland, mwangalizi wa mzunguko mmoja alishangilia hivi: “Mwujiza unaendelea! Na huu ndio mwanzo tu.” Wapya wengi wanahudhuria mikutano, mafunzo yanaanzishwa, na wapya wanajiunga katika utumishi wa shambani na wanabatizwa.

Watu kadhaa kati ya hao wapya wamelazimika kupiga vita vya muda mrefu ili kupata uhusiano wenye kukubalika na Yehova. Kwa mfano, Andy (silo jina lake halisi) alikuwa katika miaka yake ya kati ya 30. Alikuwa anaishi na Eunice (silo jina lake halisi); Andy alikuwa mlevi na mwenye mashirika mabaya. Hilo lilitatiza uhusiano wao, na dhamiri yake yenye kusumbuka ilijionyesha katika njia zisizopendeza nyakati nyingine. Lakini ndipo Eunice alipoanza kujifunza Biblia. Polepole akaelewa kwamba ikiwa angetaka kukubalika machoni pa Yehova, ni lazima atakase maisha yake, na hivyo akahama kutoka kwa Andy.

Hilo lilifanya Andy aelewe ile hali aliyokuwamo: Alikuwa amechagua kileo—Eunice alikuwa amechagua njia ya maisha ya Kikristo. Eunice alifanya maendeleo zaidi akabatizwa, na yeye ni dada mwenye bidii katika kundi.

Ndipo Andy alipoomba funzo. Akafanya maendeleo ya kiroho, akashangilia katika mambo aliyokuwa akijifunza, lakini bado akawa anarudia-rudia udhaifu wake wa zamani. Alihudhuria mikutano mara chache sana na hangeweza kujitenga na ushirika mbaya. Katika 1989, Andy alihudhuria mkusanyiko wa wilaya—na hapo ndipo alipofanya uamuzi mkuu. Sasa akaamini kuwa angeweza kushinda tatizo hilo, akamwendea daktari apate msaada. Alilazwa hospitalini, na aliporudi nyumbani, kundi lilikuwa tayari kumsaidia. Anasema: “Nilihisi kuwa mwenye msingi mzuri zaidi wa kuanza mambo ya kiroho. Nilikuwa sinywi pombe tena, na maisha yangu yaliimarishwa. Katika kundi nikapata washiriki wapya badala ya wale wa zamani. Uhusiano wangu na Yehova ukawa halisi zaidi, na hapo tu ndipo nilipohisi ningeweza kumwendea kwa sala. Tangu wakati huo, sala imekuwa yenye msaada mkubwa kwangu. Nimesali mara nyingi sana kwa Yehova, naye amenisikia. Wakati kishawishi kilipokuwa kikubwa mno na tamaa yangu ya kufanya mabaya ikawa karibu inishinde, ilikuwa ni kama wakati wote nilikutana na baadhi ya rafiki zangu wa kutoka Jumba la Ufalme, ambao walinitia moyo niendelee na kuishi katika maisha yangu mapya.”

Huu ndio mwaka wa tatu ambao Andy amekuwa hanywi pombe. Neno la Mungu, roho Yake, na tengenezo Lake limemsaidia Andy. Alianza kuhubiri na alibatizwa kwenye Mkusanyiko wa “Wapendao Uhuru” katika Godthaab (Nuuk) Agosti uliopita.

Mtu anapoazimia kushiriki katika ibada ya Yehova, kutojiweza kwa kimwili huwa si kizuizi. Kwa mfano, Kenwyn, ambaye sasa ana umri wa miaka 17, huishi katika kisiwa cha Grenada. Alipokuwa mwenye umri wa miaka 4 alianguka, na uwezo wake wa kutembea uliathiriwa sana. Alipokuwa mkubwa zaidi, kutembea kukawa kugumu zaidi na zaidi. Kufikia umri wa miaka 15, alilazimika kutembea kwa msaada wa mikongojo. Alipofikia umri wa miaka 17, upasuaji uliokusudiwa kurekebisha tatizo lake la kutembea haukufanikiwa.

Ilikuwa wakati huu kwamba Kenwyn alianza kujifunza na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliyekuwa misionari. Alifanya maendeleo mazuri katika kukubali maarifa ya Biblia lakini akasita alipoalikwa ashiriki maarifa yake na wengine katika utumishi wa nyumba kwa nyumba. Alikuwa mwoga kwa sababu ya hali yake ya kimwili na angejibu: “Nitakuambia nitakapokuwa tayari.” Alitiwa moyo aweze kujisomea mambo yaliyoonwa katika Amkeni! na Mnara wa Mlinzi juu ya Mashahidi waliokuwa na udhaifu wa kimwili na bado walihubiri kwa ukawaida kutoka mlango hadi mlango. Baada ya kusoma mambo hayo yaliyoonwa, akamjulisha misionari huyo hivi: “Niko tayari sasa.”

Na alikuwa tayari kweli. Alitumia saa 19 akitolea wengine ushuhuda katika mwezi wake wa kwanza katika utumishi wa shambani. Mwezi uliofuata, aliripoti saa 63. Akabatizwa katika Machi mwaka huu na akajiandikisha kuwa painia msaidizi mwezi uliofuata. Kenwyn aweza kuonwa akitembea kwa mikongojo akipanda na kushuka sehemu yenye vilima-vilima ya eneo lake la kutolea ushahidi. Ni mfano wenye kutokeza kama nini na chanzo cha kitia-moyo katika kundi lake! Kwa sababu vilima si kizuizi kwa kazi yake ya kuhubiri, akina ndugu kwa shauku humwita “Gari-Magurudumu-Manne.”

Visiwa vya Pasifiki

“Na yeye atakuwa na raia kutoka bahari hadi bahari na kutoka mto hadi miisho ya dunia,” Zaburi 72:8, NW, ikatabiri. Kupatana na maneno hayo, Solomoni mkuu, Kristo Yesu, ana raia kotekote duniani, kutia na visiwa vya Pasifiki.

Wakaaji wa visiwa vidogo na visiwa vya matumbawe katika sehemu ya magharibi mwa Pasifiki vilivyo chini ya tawi la Guamu wanaendelea kupokea ushahidi katika lugha nyingi. Kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kinapatikana katika nyumba nyingi. Kutoka kisiwa kimoja kuna ono hili: Mwanamke mmoja aliyekubali nakala ya kitabu hiki aliona kwamba baba yake, ambaye ndiye pasta wa kanisa lao, alikuwa anatumia kitabu chekundu katika mahubiri yake akiwa kwenye mimbari. Baada ya mahubiri alimwona akikiweka kwa usiri ndani ya kasha lake ili kwamba wengine wasikione. Lakini alikiona, na baada ya mahubiri akamwuliza: “Baba, kwa nini unatumia kitabu hicho chekundu?” Akajibu: “Yale kinachosema ni ya kweli.” Akamwuliza ni wapi alikokipata. “Ni kitabu chako,” akasema. Baada ya ono hilo yeye na mume wake waliazimia kujifunza Biblia kwa msaada wa Mashahidi wenyeji. Siku moja majirani zake walianza kumdhihaki kwa sababu ya kuruhusu Mashahidi wajifunze naye, na hali baba yake ni pasta. Lakini pasta aliposikia hayo, aliwakemea na kuwaambia: “Msiseme lolote dhidi yao [Mashahidi] kwa sababu wao ni watu wa Mungu wanaotuletea habari njema.”

Tawi katika Papua New Guinea lilipokea barua ifuatayo kutoka Mkoa wa Morobe: “Sisi hapa katika Lengbati huishi katika sehemu ya nchi yenye vichaka vingi ambapo kuna milima mikubwa na hakuna barabara za magari. Kuna kiwanja kidogo cha ndege, lakini ndege huwa haiji mara nyingi. Katika 1987 kulikuwako na Shahidi mmoja tu aliyefanya utumishi wa shambani na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mwangalizi wa mzunguko pamoja na mke wake wakaja na kututunza, na katika wakati huo upinzani ukazuka. Maadui wa Ufalme wakajaribu kusimamisha kazi yetu, wakachoma Jumba la Ufalme mbele ya macho ya mwangalizi wa mzunguko. Tokeo la upinzani huu lilikuwa nini? Sasa tuna wahubiri saba na tunakutana katika Jumba la Ufalme jipya tulilojenga. Tunapofanya kazi ya Ufalme, tunajihisi tukiwa wenye furaha sana, kama vile ambavyo ndugu na dada zetu wote kwingineko wanavyohisi wanapofanya kazi hiyo hiyo.”

Vijana wanaweza kufanya mengi kusaidia vijana wengine wajifunze kweli. Katika Australia, Linda mwenye miaka tisa aliulizwa na mwalimu wake aketi kando ya msichana mwingine, Rebecca, aliyekuwa ameketi peke yake. Linda alifanya urafiki na Rebecca akazungumza naye kuhusu Ufalme. Hatimaye akaanzisha funzo na Rebecca wakati wa chakula cha mchana shuleni, akitumia kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. Halafu wakazungumza na mwanafunzi mwingine, aitwaye Ebony, naye akajiunga na funzo. Halafu akaja Sarah, mwanafunzi mwingine bado, na kuuliza kama angeweza kujiunga katika mchezo waliokuwa wanacheza. Linda akaeleza kuwa haukuwa mchezo—walikuwa wakijifunza Biblia. Hivyo, Sarah akajiunga pia. Msichana mwingine akauliza kama angeweza kujiunga, na sasa nyakati nyingine kuna vikundi viwili vya watoto wakijifunza kitabu Mwalimu Mkuu, kikundi kimoja kikiongozwa na Linda na kile kingine na Rebecca. Halafu mwalimu akawa mwenye udadisi na alitaka kujua yale waliyokuwa wakifanya, hivyo Linda akamwonyesha kitabu Mwalimu Mkuu, na mwalimu akawaruhusu waendelee.

Nchi Zilizo Chini ya Marufuku

“Uniponye nao wanaonifuatia [wanyanyasi wangu, NW], kwa maana wao ni hodari kuliko mimi,” Daudi akamlilia Yehova, mwokozi wake. (Zab. 142:6) Leo, katika nchi ambazo zimezuia kazi ya kutoa ushahidi, watu wa Yehova wanamtegemea kwa wokovu wao. Na Yehova husikia maombi yao na kuwafariji.

Mwaka wa utumishi uliopita, mwaka wao wa 15 kuwa chini ya marufuku mfululizo, umethibitika kuwa wenye shughuli sana, pamoja na kuwa wenye baraka, kwa Mashahidi wa Yehova walioko katika nchi moja Esia. Kilele kipya cha wahubiri wa Ufalme kilifikiwa—ongezeko la asilimia 9! Hata hivyo, bado hadhari yahitajiwa. Kwa mfano, kundi moja hukutana katika nyumba ya mzee. Kwa sababu isiyo wazi, majirani hawakupendezwa na hiyo mikutano wakaanza kutupa matofali na mawe juu ya paa ya mabati ya nyumba hiyo. Huku hasira zikipanda, baadhi ya akina ndugu walitaka kukabiliana na washambulizi hao. Hata hivyo, mzee huyo kwa utulivu aliwasadikisha kuitegemea roho ya Yehova hivyo wasitumie nguvu. Majirani wa karibu zaidi walichimba mtaro kando ya upande wa nje wa ukuta wa makao ya ndugu huyo, uliokuwa na kina cha meta moja na upana wa nusu meta, wakitumaini kwamba ukuta huo ungeporomoka, na hivyo mikutano ingesimamishwa. Mzee huyo alimngojea Yehova kwa subira. Mwezi mmoja baadaye, jirani aliyekuwa mchochezi akawa mgonjwa. Alipoondoka aende hospitali, bila uangalifu aliendesha gari lake kinyumenyume hadi ndani ya mtaro uliochimbwa kando ya ukuta wa ndugu huyo. Majirani walimsaidia atoke kwenye shida yake, lakini hakuna mtu ambaye angeweza kumsaidia kiafya. Aliendelea kuwa dhaifu zaidi kisha muda mfupi baada ya hapo akafa. Badala ya kulipiza kisasi, akina ndugu walisubiri wakajifunza kwamba kuondokewa na watesi huja kwa njia zisizotazamiwa na zisizo za kawaida.

Shirika moja la vijana la chama cha kisiasa kinachotawala katika nchi moja ya Afrika laendelea kuwaonea Mashahidi kwa ukatili kwa sababu wao wakataa kubeba kadi za chama cha kisiasa. Mnyanyaso umeendelea bila kukoma kwa miaka 24 iliyopita. Wakati huu wote, watu wa Yehova wameendelea kunyenyekea mamlaka zilizo kuu, bila kuzitukana au kutafuta kulipiza kisasi.—Rum. 13:1.

Uthabiti wao kwa kanuni za Biblia umefanya baadhi ya wapinzani wao wawaheshimu. Kwa mfano, ndugu mmoja alikamatwa na kupelekwa gerezani zaidi tu ya mwaka mmoja uliopita. Ofisa mkuu wa polisi akasema: “Hatimaye sasa tumekushika.” Hata hivyo, muda huo wote polisi walikuwa wamejua kuhusu kawaida yake ya shughuli za kitheokrasi lakini walikuwa hawajachukua hatua yoyote hadi gari alilokuwa akiendesha, ambalo lilikuwa limebeba mzigo wa fasihi za Biblia, lilipogongana na gari la polisi. Ingawa ndugu huyo alihukumiwa, alitendewa vema akiwa gerezani.

Ndugu ambaye gari hilo lilisajiliwa kwa jina lake, aliletwa mbele ya polisi pia. Ilikuwa lazima aeleze kwa nini gari lake lilikuwa limebeba fasihi zisizo halali eti. Alipokuwa akihojiwa aliulizwa: “Je! wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Yeye akajibu: “Kabla ya marufuku nilikuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Tangu marufuku yaanze mimi sijabadili dini yangu. Familia yangu nami huomba nyumbani, na huwa hatuingilii mambo ya mtu mwingine. Kwa hiyo, wewe waonaje Ofisa?” Kwa kustaajabisha, mashtaka yote dhidi yake yalisimamishwa, naye akaruhusiwa kuendesha gari hilo nyumbani. Hivyo, Mashahidi wameendelea kuwa waaminifu kwa Mungu wao muda huu wote wa miaka, na Yehova amewapa ongezeko na nguvu ili wasikate tamaa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki