Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb94 kur. 42-64
  • Ripoti ya Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ripoti ya Ulimwenguni Pote
  • 1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Afrika na Visiwa Jirani
  • Asia
  • Ulaya
  • Amerika ya Kati na ya Kusini
  • Amerika Kaskazini na Visiwa vya Karibea
  • Visiwa vya Pasifiki
  • Nchi Ambako Hali Zimekuwa Zenye Kufaa Zaidi
1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb94 kur. 42-64

Ripoti ya Ulimwenguni Pote

Afrika na Visiwa Jirani

Afrika ni kontinenti iliyogawanyika kwa sababu ya vita vya kikabila na vya kitaifa. Lakini Ufunuo 7:9-14 (NW), latabiri kwamba “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” utaunganika katika ibada ya Yehova, ukiwa na taraja la kuokoka kuingia katika ulimwengu wake mpya wenye amani. Maelfu mengi ya watu kotekote Afrika wanatoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba wao ni sehemu ya umati huo wenye furaha.

Katika Cape Town, Afrika Kusini, mmoja wa dada zetu alishtuka wakati mwenye nyumba alipomkatiza, akimuuliza: “Kusudi lako ni nini?” Yeye alijibu moja kwa moja: “Ni kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja na watu.” Kwa kushangaza, mtu huyo akajibu: “Basi karibu ndani na tuanze sasa.” Kulikuwa na mazungumzo mazuri pamoja na Myahudi huyo, na dada yetu akapanga kurudi na mume wake. Mtu huyo amefanya maendeleo mazuri. Kuongezea funzo lake, yeye amesoma Biblia kuanzia mwanzo hadi mwisho mara nne, na amesoma kitabu chote cha Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi mara tatu. Yeye pia ni mwenye shughuli akishiriki kweli pamoja na watu wake wa ukoo. Yeye ni mwenye shukrani sana kwamba Yehova alifungua macho yake aone kweli. Ile siku ambayo dada yetu alimzuru mara ya kwanza, yeye aliiambia familia yake hivi: “Njoni mwasalimu watu hawa, kwani Mungu amewatuma kwetu.” Alikuwa amekuwa akifikiria kujiua.

Mahusiano ya familia yaweza kuwa na sehemu ya maana katika kueneza kweli. Painia msaidizi mmoja alianzisha funzo katika kijiji kimoja katika Maurishasi. Darmen, mvulana mdogo jirani mwenye udadisi, alisikiliza kwa upendezi. Aliwaambia wazazi wake, na hasa mama yake aliye Mhindu, juu ya yale aliyosikia. Mama yake alisadiki kwamba yale aliyokuwa akijifunza sasa yalikuwa kweli, kwa hiyo akabomoa mahali maalumu pa ibada pa Uhindu shambani mwake. Darmen alisema na watu wote wa ukoo katika kijiji hicho—ndugu, dada, ndugu-wakwe, wajomba, shangazi, na binamu zake. Alipojua juu ya andiko la siku, alizungumzia hilo pamoja nao. Jioni fulani, watu zaidi ya 30 walishiriki katika mazungumzo hayo hadi jioni sana. Baada ya majuma machache, mume na mke walio mapainia wa pekee walipanga kujifunza nao. Sasa watu 13 kutoka familia hiyo wamebatizwa; wengine 4 ni wahubiri wasiobatizwa. Vipi juu ya Darmen? Sasa yeye ameoa, na yeye na pia mke wake hutumikia wakiwa mapainia wa pekee.

Vita vya wenyewe kwa wenyewe vimevuruga sana maisha za watu katika Liberia. Wahubiri kutoka Mto Mano walipokuwa wakihudhuria mkusanyiko katika Monrovia, eneo lao la nyumbani lilishambuliwa na hawakuweza kurudi huko muda wa mwaka wote. Lakini mhubiri mmoja asiyebatizwa aliyekuwa ameachwa nyuma aliendelea kuhubiri. Ingawa hakuhisi mwenye sifa ya kustahili kutumia Jumba la Ufalme, kwani hakuwa amebatizwa bado, yeye alililinda lisiporwe. Alieleza kwamba alikuwa pia amejitahidi kufanya “ziara za uchungaji” kwa wale ambao hapo mbeleni walikuwa wakijifunza, ili kufanya upendezi wao katika kweli uendelee, na alikuwa ameongoza mikutano katika nyumba yake mwenyewe. Alikuwa miongoni mwa wale waliobatizwa kwenye Mkusanyiko wa “Ufundishaji wa Kimungu” mwaka huu.

Jambo kuu la mwaka katika Jamhuri ya Afrika ya Kati lilikuwa ile amri ya serikali mnamo Januari 20, 1993, ambayo iliondoa kabisa marufuku juu ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Ingawa akina ndugu walikuwa wamefurahia kiasi fulani cha uhuru kwa miaka kadhaa, sasa wao wana utambulisho wa kisheria. Hilo limefanya waweze kufungua tena Majumba ya Ufalme yao. Shule, hospitali, na ofisi nyingi za serikali nchini hazifanyi kazi kwa sababu ya ukosefu wa fedha za mishahara. Lakini, wajapokuwa na matatizo yao wenyewe ya kifedha, Mashahidi wa Yehova wamerekebisha na kupaka rangi Majumba ya Ufalme yote matano katika Bangui na wanayatumia tena yakiwa vitovu vya ibada safi.

Tofauti iliyo kati ya Mashahidi wa Yehova na vikundi vinginevyo vya kidini iko wazi kwa wachunguzi fulani Waafrika. Kwa sababu ya msukosuko wa kikabila kusini mwa Zaire, kikundi cha Wakasai waliokuwa wamefukuzwa na Wakatanga walikimbilia usalama kwenye nyumba ya chifu katika kijiji kimoja karibu na Kamina. Baada ya kuuliza ni nini kilitukia, chifu huyo aliuliza: ‘Je! kuna Mashahidi wa Yehova wowote miongoni mwenu?’ Wakafanya uchunguzi, halafu wakajibu: ‘La.’ Chifu huyo akauliza: ‘Kwa nini? Hakuna wowote kijijini?’ ‘Kunao wachache,’ wakajibu. ‘Basi kwa nini baadhi yao hawapo hapa?’ chifu huyo akasisitiza. Hatimaye, yeye alisema: ‘Sasa mwaona sababu inayofanya Mashahidi wa Yehova waseme kwamba dini zenu ni za uwongo. Wale waliowafukuza ni washiriki wa makanisa yenu, lakini Mashahidi wa Yehova hawajafukuza ndugu zao. Kinyume cha hilo, wamewakaribisha na kuwalinda.’

Mahali ambapo kutojua kusoma na kuandika ni tatizo, huenda wahubiri wakapata kwamba hawahitaji kufundisha tu kweli ya Biblia, bali pia kufundisha kusoma na kuandika. Dada mmoja painia aliyekuwa akifanya hivyo kwa ajili ya wanafunzi wake katika Zimbabwe alishangaa walipotaka kulipa kwa ajili ya utumishi wake akiwa mwalimu. Baadaye yeye aliandika hivi: “Nilimkumbuka Gehazi, mtumishi wa Elisha, na jinsi alivyopigwa kwa ukoma. Kwa hiyo nikawaambia, ‘Thawabu yangu ni kuwaona mkifanya maendeleo kujifunza kweli na kutenda yale mnayojifunza. Sitaki fedha zenu.’”—2 Fal. 5:20-27.

Asia

Ni katika Mashariki ambako Yehova aliiweka paradiso ya awali na kuwaweka wanadamu wawili wa kwanza. Walishindwa kuthamini yale ambayo Yehova alikuwa amewafanyia. Lakini katika siku yetu, kuna mamia ya maelfu ya watu wa Mashariki wanaotoa uthibitisho kwamba wanathamini kikweli njia za Yehova zenye uadilifu, na wanashiriki na wengine kwa bidii habari juu ya kusudi la Mungu la kufanya dunia yote kuwa paradiso.

Dada mmoja katika Japani ambaye analazimika kufanya kazi wakati wote ili kutegemeza familia yake hufurahia utumishi wa painia. Yeye huwezaje hilo? Kwa kutumia vizuri wakati anaotumia katika gari-moshi kila siku. Safari hiyo huchukua saa moja unusu kwenda. Inambidi awe mwenye busara, lakini kwa kuwa abiria husafiri kwa gari-moshi lilelile kila siku, yeye hata hufanya ziara za kuwarudia watu wanaomsikiliza. Kwa wastani, yeye huangusha magazeti 167 kila mwezi na ameanzisha mafunzo saba ya Biblia humo ndani ya gari-moshi.

Ingawa dada painia katika Malaysia alizuru mara kadhaa nyumbani kwa mwanamke mmoja ambaye walikuwa wakijifunza naye, hakumpata yeyote nyumbani. Hata hivyo, jirani mwenye sura ya ukali alikuwa akimtazama sikuzote kwa kumshuku. “Mbona nisiseme na mtu huyu?” yule dada akasababu. “Kila mara nijapo, yeye huwa hapo, na labda anaweza kuniambia mahali mwanamke huyo alipo.” Mwanamume huyo alimsalimu kwa dharau: “Wataka nini? Kusudi lako ni nini?” Lakini, kwa kushangaza, baada ya kumwambia kwamba mwanamke huyo alikuwa amehama, mtu huyo alisikiliza ujumbe wa Biblia na hata akakubali kujifunza, naye alifanya hivyo akiwa na idili. Funzo lilipofanywa mara ya kwanza, mke wake alikuwako pia, pamoja na rafiki yake aliyekuwa mshiriki mshupavu wa madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo na aliyejaribu kukomesha funzo hilo la Biblia. Lakini baada ya kusikia majibu ya dada huyo yenye utulivu na yenye kusababu dhidi ya mashambulizi hayo ya maneno, mtu huyo alimwambia rafikiye ashike lake na amwache ajifunze kama alivyotaka. Maendeleo yalikuwa ya haraka. Kazi yake ya maisha ilikuwa ni ya uwasiliani-roho, lakini alipojifunza kwamba Biblia hushutumu uwasiliani-roho, yeye alitupa vifaa vyote vya uwasiliani-roho bila kukawia. Yeye na mke wake sasa wanahudhuria mikutano ya kutaniko kwa kawaida kila juma.

Alipokuwa akishiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba, dada mmoja painia katika India alikutana na wasichana watatu waliokuwa wanafunzi wa chuo. Ingawa wao ni Wahindu, walikubali toleo la kujifunza Biblia kwa sababu walikuwa wakitafuta majibu ya maswali mengi. Baadaye, walipokea na kusoma kile kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu. Kitabu hicho ndicho kilichowasadikisha kabisa juu ya kutofaa kwa ibada ya sanamu. Walimweleza mama yao juu ya yale waliyokuwa wamejifunza, naye akatupa miungu yake yote ya sanamu. Wasichana hao walitupa ubao wao wa Ouija. Baadaye walisema: “Hatuwezi kusahau mwaka 1992. Katika Januari tulitoka nje ya ‘Babuloni Mkubwa’ kwa kuondolea mbali sanamu. Katika Aprili tulianza kuhudhuria mikutano kwa kawaida. Katika Agosti tukawa wahubiri wasiobatizwa. Katika Oktoba sisi sote wanne tukabatizwa. Katika Novemba wawili kati yetu tukawa mapainia wasaidizi wenye kuendelea, na katika Desemba tulikuwa tukiongoza mafunzo kumi ya Biblia, kutia na lile la nyanya yetu mwenye miaka 71.”

Wahubiri katika Thailandi wapata kwamba idadi yenye kuongezeka ya watu katika eneo lao wanasumbuliwa na mashetani. Mume na mke mmoja katika Nakhon Sawan waliishi katika nyumba iliyojaa sanamu. Walipoendelea katika funzo lao la Biblia, mume huyo alitaja kwamba mambo ya kiajabu-ajabu yalikuwa yakitendeka nyumbani mwao nayo yalikuwa yakiwazuia wasilale. Yeye alisema pia kwamba mkewe alipojaribu kwenda kwenye Jumba la Ufalme, alihisi kana kwamba mtu fulani alikuwa akishika mgongo wake, akimzuia asiondoke nyumbani. Mhubiri huyo alielekeza fikira zao kwenye habari katika broshua Roho za Wafu. Mtu huyo aliungama kwamba yale iliyoeleza ni yaleyale yaliyokuwa yakiwapata. Yeye alionyeshwa kutoka kwa Maandiko mambo aliyohitaji kufanya ili kupata baraka za Yehova. (Kum. 7:25, 26; 1 Yoh. 5:21) Siku iliyofuata aliomba akina ndugu wamsaidie kuondoa nyumbani mwake sanamu zote kutia na vitu vinginevyo vya kidini—vya kutosha kujaza kilori kidogo—na kuvichoma mbele yake nje ya jiji. Imani yake iliimarishwa sana alipoona kwamba sanamu hizo zilizokuwa vitu vyake vya kutolea ibada, havikuweza kujiokoa. Kuanzia wakati huo na kuendelea, watu wa nyumba hiyo hawakushambuliwa tena na mashetani na walifanya maendeleo mazuri ya kiroho.

Kwa sababu ya kukosa uhakika juu ya mambo yatakayowapata wakati ujao, vijana wengi wanatafuta majibu. Baadhi yao wanasaidiwa na ile broshua Furahia Milele Maisha Duniani! na kile kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Mama mmoja Mbuddha katika Sri Lanka aliandika hivi: “Nachukua fursa hii kuwashukuru kwa moyo wangu wote kwa kusaidia binti yangu kupata njia ifaayo. Nilifurahi sana wakati nilipoona kile kitabu mlichompa binti yangu. Nafikiri ni zawadi bora zaidi aliyowahi kupata maishani mwake. Yeye anakisoma tena na tena na hata mimi mwenyewe nimekisoma. Kwa hiyo, kwa mara nyingine tena, ningependa kuwashukuru kwa moyo wangu wote kwa zawadi hiyo nzuri sana.”

Ulaya

Katika nchi nyingi, hali za kiuchumi ni ngumu. Lakini watumishi wa Yehova wana “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58, NW) Badala ya kuomboleza kwa sababu ya hali ya ukosefu wa kazi, Mashahidi katika Finlandi wamekuwa wakitwaa kila fursa kutumia wakati mwingi zaidi wakisaidia watu kuona kwa nini nyakati ni ngumu sana na kwa nini twahitaji Ufalme wa Mungu.

Wahubiri wachanga wana sehemu gani katika hilo? Hapa kuna kielelezo: Dada mmoja katika Finlandi alikuwa katika utumishi wa shambani pamoja na binti yake wa miaka mitano. Walikutana na mwanamume ambaye, kwa sababu ya chuki isiyo na sababu, hakutaka kusema na dada yule. Lakini binti yake alipompa trakti moja, yeye hangeweza kuikataa. Baadaye, mke wake alipopata trakti hiyo juu ya meza ya jikoni, aliisoma. Alipenda yale ambayo trakti hiyo ilisema juu ya tumaini la paradiso. Aliagiza kile kitabu Kuishi Milele kutoka kwa Sosaiti na akaanza kukisoma. Wahubiri walipokuja tena mlangoni pake, funzo la Biblia lilianzishwa. Mume wake alipinga. Lakini, baada ya kuona jinsi Jumba la Ufalme lilivyojengwa kwa siku chache, yeye alisema: “Ikiwa Mashahidi wa Yehova waweza kufanya mambo kama hayo, ni lazima kuwe kuna nguvu kubwa zaidi inayosukuma tengenezo hilo.” Yeye pia alianza kujifunza, na wote wawili walibatizwa baada ya mwaka mmoja.

Makutaniko mengi katika Ureno hueneza eneo lao kila juma, na bado wanawapata watu wa mfano wa kondoo. Dada mmoja asimulia hivi: “Kabla ya kwenda kwenye utumishi kila asubuhi, mimi husali kwa Yehova anisaidie kupata mtu anayependezwa kujifunza Biblia.” Siku moja alipanga kujifunza na wale wanaofanya kazi katika duka la kinyozi. Baadaye, funzo hilo lilipohamishwa kwenye nyumba ya dada huyo, ni mwanamke mmoja tu aliyekuja. Yeye alisema: ‘Wale wengine hawapendezwi, mimi napendezwa.’ Kwa muda wa mwezi mmoja yeye mwenyewe alikuwa akiongoza mafunzo mawili. Upesi akabatizwa na kuingia katika kazi ya painia.

Ingawa mume na mke mmoja katika Swedeni walikuwa wameoana kulingana na desturi ya Wajipsi (Waromani), wao walioana kulingana na sheria ya Swedeni, na wakajitoa kwa ajili ya ubatizo wakiwa Mashahidi wa Yehova katika 1992. Kwa sababu ya staha ambayo yeye hupewa na Wajipsi wengineo, mume huyo ameweza kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Katika Januari 1993 yeye alikuwa akiongoza mafunzo 21. Aliongoza funzo moja pamoja na kikundi kikubwa sana kiasi cha kwamba aliomba aweze kutumia Jumba la Ufalme. Mwangalizi wa mzunguko alipoenda pamoja naye kwa ajili ya funzo hilo, Wajipsi 26 walio watu wazima walikuwa katika nyumba hiyo, wakingoja kwa ajili ya funzo hilo. Lakini ndugu huyo mpya alisema: “Sielewi watu wako wapi jioni hii. Kwa kawaida tunakuwa watu kati ya 40 na 50 hapa.” Funzo hilo liliongozwa katika lugha tatu—Kiswedeni, Kikroatia, na Kiromani. Jambo linalovutia watu hawa zaidi ya baraka ya ulimwengu mpya ni upendo wa Mungu pamoja na mtazamo usio wa kupendelea na usio wa chuki unaoonekana miongoni mwa watu wa Yehova.

Ili kuepuka kurudufisha kazi na kutumia nyenzo kwa njia iliyo bora zaidi, mabadiliko makubwa yamefanywa katika kazi kwenye ofisi za matawi kadhaa. Uholanzi na Uswisi zilitiwa ndani. Ofisi ya tawi la Uholanzi hushughulikia tafsiri ya Kiholanzi; hiyo pia huratibu utokezaji na ugawanyaji wa kaseti za vidio kwa ajili ya Ulaya. Lakini uchapaji wa magazeti ya Kiholanzi, pamoja na uhifadhi na usafirishaji wa fasihi kwa ajili ya Uholanzi, sasa unashughulikiwa na tawi katika Ujerumani. Vivyo hivyo, uchapaji na usafirishaji uliofanywa katika Uswisi hapo mwanzoni, sasa unashughulikiwa katika Ujerumani. Baadhi ya familia ya Betheli waliokuwa wakitumikia katika Emmen, Uholanzi, walijitolea kusaidia katika matawi mengineyo, kwa hiyo wawili waligawiwa kwenda Uingereza, wanne kwenda Ujerumani, na saba kwenda Naijeria, ambako matbaa ya rangi nne kutoka Uholanzi inawekwa. Vifaa kutoka Uswisi vitatumiwa kuboresha uchapaji katika Ufilipino, na mume na mke mmoja kutoka Uswisi wataenda huko ili kusaidia kwa muda. Ndugu mwingine kutoka Uswisi anahamishwa hadi Naijeria. Wengine watatumikia tena wakiwa mapainia.

Kwa zaidi ya miaka mia moja, ndugu zetu wamekuwa wakitoa ushahidi katika Ailandi, na udumifu wao wenye subira waendelea kupata matokeo. Mhubiri mmoja katika Tipperary alianza funzo la Biblia na mtu mmoja wa mahali hapo, aitwaye Michael. Hata hivyo, baadaye, yeye alijaribu kumwepuka mhubiri huyo. Mhubiri huyo alipong’amua yale yaliyokuwa yakitukia, yeye an dada mwingine walienda kumtafuta kwenye baa kwa sababu walihisi kwamba yeye alipendezwa kikweli. Walipoingia katika baa hiyo, kila mtu alinyamaza humo; kila mtu alijua dada hao. Wahubiri hao walimkumbusha tu Michael juu ya mipango ya kujifunza. Baada ya wao kuondoka, yeye alijaribu kuficha yale yaliyotukia akiwaambia hivi wale wanaume wengine: “Ni kweli, nilipaswa kutengeneza jiko lake, lakini nikasahau!” Lakini yeye aling’amua kwamba hangeweza kuwaepa wale dada tena.

Baada ya hayo, Michael alifanya maendeleo mazuri. Yeye alimwoa May, ambaye alikubali kujifunza, ingawa hapo mwanzoni alishuku upendezi mchangamfu wa wale dada. Halafu Michael na May wakaanza kumweleza dada ya May aitwaye Breda mambo waliyokuwa wakijifunza. Wakati wa 1993, wote watatu walibatizwa. Wakati uo huo, ndugu ya May na rafikiye msichana, pia ndugu mdogo wa Michael pamoja na mkewe, walianza kujifunza na kuhudhuria mikutano. Kwa hiyo, kwa sababu dada yetu alikuwa mdumifu, watu saba wananufaika kutokana na kweli.

Sara mwenye miaka mitano, katika Austria, ni mtoto mwenye urafiki sana na mara nyingi husema na wapita-njia kando ya nyumba yao. Pindi moja, yeye alimuuliza hivi mwanamke mmoja mchanga kwa njia ya moja kwa moja: “Je! wewe huvuta sigareti?” Mwanamke huyo alipojibu la, Sara alikuwa tayari na swali lake lililofuata: “Je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Akitatanika kidogo, mwanamke huyo alijibu, “Ndiyo!” Hilo lilimfanya aongee na mamake Sara. Yeye alieleza kwamba ingawa alikuwa amelelewa akiwa Shahidi, yeye hakuwa amewasiliana nao hata kidogo. Alimwomba mamake Sara amzuru. Maneno ya Mathayo 21:16 ni ya kweli kama nini: “Kwa vinywa vya watoto wachanga na wanyonyao umekamilisha sifa”!

Mashahidi wa Yehova katika Slovakia walikuwa na furaha kubwa sana mnamo Machi 24, 1993, wakati shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova liliposajiliwa kihalali, hilo likikomesha rasmi marufuku iliyokuwa imewekwa miaka 43 iliyopita. Hiyo ilifuatiwa mnamo Septemba 1, na jambo ilo hilo katika Jamhuri ya Cheki. Kuna watu wengi katika nchi hizo ambao wametamaushwa na dini na siasa. Baadhi yao wanatafuta kweli. Ilikuwa hivyo kuhusu mume na mke walio wazee-wazee katika Bobron na Orave, katika Slovakia. Mwanamke huyo alikuwa ameuliza kasisi juu ya Biblia, lakini yeye alikuwa amejibu hivi: “Hanka, chagua kitabu bora zaidi cha kusoma.” Lakini, yeye na mumewe waliendelea kusoma Biblia. Walikuwa wakifanya mabadiliko maishani mwao kupatana na yale waliyokuwa wakijifunza. Ili kutosheleza njaa yao ya kiroho, walikuwa wameandikisha magazeti kadhaa ya kidini. Sasa walikubali kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Kama vile mwanamke huyo alivyosema baadaye, tangu mwanzoni mwa mazungumzo yake pamoja na mapainia hao, alihisi kwamba Mungu mwenyewe alikuwa amewatuma.

Amerika ya Kati na ya Kusini

“Tazama! Watumishi wangu wenyewe wataimba kwa shangwe kwa sababu ya hali njema ya moyo.” (Isa. 65:14, NW) Hali hiyo njema ya moyo ya kiroho ni dhahiri miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika Meksiko. Kujapokuwa upinzani mwingi kutoka kwa Kanisa Katoliki, mnamo Mei 7, 1993, serikali ya Meksiko ilisajili mashirika yetu mawili ya kidini: La Torre del Vigía, A.R., na Los Testigos de Jehová en México, A.R. Kuanzia siku hiyo Mashahidi wa Yehova wakawa dini iliyotambuliwa rasmi. Sasa wanatazamia kuweka vibao vya kutambulisha waziwazi Majumba ya Ufalme yao kwa mara ya kwanza.

Mwaka uliopita, makutaniko mapya 445 yalifanyizwa. Katika Juni, wahubiri walijumlika kuwa 375,351. Idadi ya waliohudhuria Ukumbusho ilikuwa 1,349,998. Wahubiri waongezekapo, eneo hufanyiwa kazi mara nyingi zaidi. Katika eneo moja linalofanyiwa kazi mara nyingi, dada wawili walizuru nyumba moja ambapo mwenye nyumba aliyekuwa na hasira alipaza sauti: “Tayari nimewaambia kwamba sitaki mje nyumbani kwangu na ujumbe wenu. Kwa nini hamwezi kusikia?” Mmoja wa dada hao alijibu: “Waona, sisi ni wahubiri wengi. Bila shaka uliwaambia baadhi ya wahubiri wenzetu. Hata hivyo, twaweza kufanya mipango ili mtu yeyote asikuzuru. Tafadhali tupe jina lako na nambari kamili ya nyumba yako na tutapitisha habari hii kwa Mashahidi wote katika eneo hili halafu hakuna mtu atakayekuzuru tena.” Kisha mwenye nyumba akasema: “La, si lazima mtende kwa kupita kiasi hivyo. Bado mwaweza kunizuru, lakini tafadhali si mara nyingi hivyo.” Muda mfupi baadaye, dada hao walikutana na mwanamke uyo huyo kwenye Jumba la Ufalme. Ni nini kilikuwa kimetokea? Mhubiri mwingine alipomzuru, yeye alikubali funzo la Biblia!

Ingawa Guiana ya Kifaransa ina idadi ndogo zaidi ya watu katika nchi za Amerika Kusini, masilahi ya kiroho yanasitawi huko. Katika Aprili, tawi liliripoti kilele chalo cha 21 mfululizo cha wahubiri, na wanafikia wastani wa saa 14.5 kwa kila mhubiri katika utumishi wa shambani kila mwezi. Katika nchi hiyo pia, ‘mdogo amekuwa elfu,’ na ni wenye furaha kuwa sehemu ya “taifa hodari” linalomsifu Yehova ulimwenguni pote.—Isa. 60:22.

Tofauti iliyo kati ya Mashahidi na watu wengine huvutia wapendao uadilifu. Dada mmoja mzee-mzee katika Caracas, Venezuela, alienda kwenye benki kuchukua fedha. Bila kuzihesabu, alizitia ndani ya mfuko wake. Lakini alipofika nyumbani, alipata kwamba mhesabu-fedha alikuwa amempa bolívares 1,200 (dola 13 za US) zaidi. Alipigia benki simu na kumwambia mhesabu-fedha kwamba ikiwa kufikia mwisho wa siku angegundua kwamba fedha fulani zilikosekana, yeye alipaswa amjulishe. Saa 11:00 jioni yeye alikuja kwenye nyumba ya dada huyo na kumwambia kwamba alikuwa akikosa bolívares 1,200. Dada huyo alipompa fedha hizo, yeye alipaza sauti: “Hii ndiyo mara ya kwanza mtu yeyote kufanya hivi! Ningalipoteza kazi yangu.” Dada huyo alitumia fursa ya wakati huo na kwenye ziara za baadaye kwenye benki kutoa ushahidi. Upesi funzo la Biblia likaanzishwa na mwanamume huyo mchanga, naye anahudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme.

Wanapotoa ushahidi, mapainia katika Chile wajua vema kwamba Yehova anaelekeza kazi. (1 Kor. 3:9) Mume na mke mmoja katika Chile kusini walikuwa tayari kwenda nyumbani baada ya kuhubiri muda wa saa tisa katika eneo la mbali. Kwenye barabara kuu, basi la mwisho la kwenda Antuco liliwapita. Walikuwa wamechoka na wenye njaa, na mbele yao kulikuwa na mwendo wa kupanda kilima wa kilometa 40. Giza na baridi ilikuwa ikiingia. Magari mengine pia yaliwapita kana kwamba hawakuwapo. Walipokuwa wakitembea, walijiuliza Yehova alikuwa amewapangia nini. Halafu, bila ya wao kulisimamisha, basi lililokuwa likielekea upande waliotoka lilisimama kuwachukua; kwa hiyo wakalipanda. Walipofika kwenye mji mmoja na kushuka, walikumbuka mume na mke fulani waliokuwa wamejuana nao miezi kadhaa iliyopita. Je! labda wao walijua mtu fulani ambaye ana gari na ambaye angewapeleka Antuco? Mume huyo alikuwa na wazo bora zaidi: “Mbona msilale kwetu leo?”

Mapainia hao walipokubali, mke wa nyumba hiyo alisisimka na kupaza sauti: ‘Sasa mtakuwa nasi kujibu maswali yetu!’ Na kwa kweli waliuliza maswali mengi—juu ya Yehova, wapakwa, mtumwa mwaminifu, umati mkubwa, hayawani-mwitu, na kadhalika! Mume na mke hao walikuwa wamechukua kitabu Kuishi Milele na kukisoma mpaka wakakijua sana. Lo, jinsi walivyokuwa wamesali kwamba mtu fulani aweze kuwasaidia kuelewa zaidi! “Na ndiyo nyinyi hapa!” Baada ya mazungumzo marefu yenye kuridhisha, familia hiyo yenye ukaribishaji-wageni iliwaandalia mlo mzuri halafu wakapewa kitanda kizuri. Mapainia hao walishukuru kama nini kwamba Yehova alikuwa amewatumia kwa njia hiyo!

Nyakati nyingine, fadhili ndiyo inayopenya mtazamo usio wa kirafiki wa wapinzani, wala si kutoa hoja. Kama vile Mithali 25:15 isemavyo, “Ulimi laini [“mpole,” NW] huvunja mifupa.” Brumilda Castillo, Shahidi ambaye hapo mwanzoni alikuwa mtawa wa kike, alizuru familia moja ambayo ni ya Wakatoliki wenye kujitoa katika Ekwedori. Mke wa familia hiyo alipomwona Shahidi huyo, alimtukana. Dada yetu hakujaribu kukanusha mashtaka hayo; yeye alitabasamu tu, akamshukuru mwanamke huyo, na kusema kwamba kwa kweli angeweza kuzungumza naye wakati mwingine. Dada yetu alipokuwa akiondoka, alikutana na mume wa yule mke, naye hakuitikia tu kama mke wake, bali pia alimwamuru Dada Castillo aondoke kwenye uwanja wake. Kwa mara nyingine tena, yeye alitabasamu, akamshukuru, na kusema kwamba alitumaini kuzungumza naye wakati mwingine. Mume na mke hao walipozungumzia juu ya yale yaliyotokea, walishangaa. Yeye angewezaje kutabasamu na kuwashukuru na hali wao walikuwa wamekuwa wafidhuli kwake? Walivutiwa sana, hivi kwamba mume huyo alimkaribisha Shahidi aliyefuata kumzuru. Shahidi huyo aliwaalika kwenye mkutano, nao wakaja. Ni nani aliyekuwa wa kwanza kuwasalimu? Yule dada waliyemtenda vibaya. Walimwomba msamaha sana, naye akatwaa fursa hiyo kuanza kuwazuru.

Siku moja mtu huyo alitaka kujua Shahidi huyo alikionaje kikanisa kidogo alichokuwa amejenga katika uwanja wake na kukijaza sanamu. Shahidi huyo aliuliza kama yeye angemkasirikia ikiwa angemwambia kweli. “Bila shaka sivyo,” yeye akajibu. “Je! utafanya yale ambayo Biblia husema wapaswa kufanya?” yeye akauliza. “Nitayafanya siku ii hii,” yeye akaahidi. Kwa hiyo alimwonyesha yale ambayo Biblia yake ya Katoliki ilisema juu ya utumizi wa sanamu. Baada ya hayo, yeye akasema: “Nataka unisaidie niondolee mbali sanamu hizi zote.” Ilichukua siku nne kuziondolea mbali zote na kuzichoma.

Wote wanaokuwa watumishi wa Yehova wahitaji kuvaa utu mpya. Hata hivyo, huenda hilo likaonekana kuwa jambo gumu sana kwa watu wengine. Katika kaskazini-mashariki mwa Brazili, kijana mmoja aliyekubali kujifunza Biblia alikuwa na sifa mbaya sana. Familia yake ilisema kwamba karibu kila siku mtu fulani alikuja nyumbani mwao kulipwa madeni ambayo yeye alikuwa amepata alipokuwa akinywa. Kila mara wazazi wake walihofia kwamba angeuawa. Kila mtu aliwaambia wale mapainia waliokuwa wakiongoza funzo hilo: “Mnapoteza wakati wenu kujifunza naye. Yeye hatabadilika kamwe.” Lakini “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu.” (Ebr. 4:12) Mtu huyo alipoacha unywaji na ukosefu wa adili, mji wote ulivutiwa. Wazazi wake walipaza sauti: “Amani imetujia tena nyumbani mwetu!” Kwa sababu ya mabadiliko ambayo amefanya, watu wengine watatu katika familia yao wanajifunza pia na kuhudhuria mikutano.

Amerika Kaskazini na Visiwa vya Karibea

Kwenye pindi zaidi ya moja, Yesu alikazia umaana wa mtu kupenda jirani yake kama yeye mwenyewe. Kuna njia nyingi ambazo upendo huo waweza kuonyeshwa. Dada mmoja katika Martiniki aandika hivi: ‘Asubuhi moja nilipokuwa nikiendesha gari kwenda kazini, nilimchukua mwanamke mmoja mchanga aliyeonekana kuwa mgonjwa. Tulipokuwa tukielekea mjini, nilisema naye juu ya kusudi la Mungu na baraka za ulimwengu mpya. Yeye alisema kwamba mama yake alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova lakini maisha yake mwenyewe yalijaa magumu na hakuamini kwamba Mungu angeweza kuboresha hali yake. Nilipendekeza kwamba ajifunze Biblia pamoja nami kwa mwezi mmoja, naye akakubali. Baada ya mwezi huo mmoja, nilimuuliza kama alitaka kuendelea. “Ndiyo, nataka kuliko wakati mwingine wowote,” yeye akasema.

‘Hali ya familia yake ilikuwa mbaya. Baadaye, mume wake aliyekuwa na mwanamke mwingine alipomwamuru aondoke nyumbani, nilimsaidia yeye na watoto wake. Baadaye, aliondoka Martiniki na kwenda Ufaransa, alikokuwa amepata kazi.

‘Muda fulani baadaye, mume wake alikuja mlangoni pangu. Mwanzoni niliogopa. Lakini yeye alikuwa amevutiwa sana na mabadiliko ya mkewe na mwenendo wangu mwenyewe. Alikuwa amekuja kuomba funzo la Biblia.’

Dada mmoja painia ambaye pia ni mwalimu wa shule katika Jameika asema kwamba kwa kupendezwa na watu na kuwa mwenye fadhili kwao, mara nyingi yeye huweza pia kuwasaidia kiroho. Aliona kwamba baadhi ya wanafunzi katika shule aliyoajiriwa walikuwa wakipata ugumu katika somo fulani hususa, kwa hiyo aliwapa kwa fadhili msaada wa ziada. Ili kuwasaidia wafahamu thamani ya elimu, yeye alitumia pia habari katika kitabu Vijana Huuliza. Yale aliyokuwa akifanya yalibadili mtazamo wa wale walioyaona. Kama tokeo, aliweza kuanzisha mafunzo manne ya Biblia na kuangusha kiasi kikubwa cha fasihi.

Ili kuharakisha kazi ya kutoa ushahidi katika vijiji vya mbali, tawi la Alaska linatumia ndege iliyonunuliwa hivi karibuni, inayofaa zaidi kazi yetu kuliko ile tuliyokuwa nayo hapo mwanzoni. Mwendo wa utendaji huu ni karibu mara mbili ya ule wa miaka iliyopita.

Walipokuwa wakizuru nyumba moja katika Jamhuri ya Dominika, wahubiri wawili waliona mle ndani mume na mke waliokuwa wamepiga magoti wakisali. Walingoja hadi mume na mke hao walipomaliza kusali, halafu wakabisha tena. Watu hao walipokuja mlangoni, wahubiri hao walisalimiwa kwa maneno: “Asante, Mungu, kwa kusikiliza sala yetu.” Wao walikubali kwa hamu toleo la msaada wa kujifunza Biblia. Siku mbili baadaye, wakati maandiko yanayoshutumu utumizi wa sanamu yalipozungumzwa, bila kukawia wao walituomba radhi na kukusanya sanamu zote zilizokuwako nyumbani mwao. (Kum. 7:25) Akimgeukia mke wake, mume huyo aliuliza: “Je! tuko pamoja na Yehova au pamoja na Ibilisi?” “Yehova,” yeye akajibu. Kwa hayo, walichoma sanamu zote—nao walikuwa na nyingi. Kiroho, mashamba ni meupe tayari kwa mavuno katika Jamhuri ya Dominika, na katika miaka ya hivi karibuni Mashahidi wenyeji wamefurahi kukaribisha zaidi ya Mashahidi 150 wengineo ambao wamekuja kutoka ng’ambo ili kusaidia katika kazi ya kukusanya.

Visiwa vya Pasifiki

Machi 1, 1993, ilikuwa siku ya maana kwa ndugu zetu katika Ufilipino. Siku hiyo Mahakama Kuu Zaidi ilibatilisha kwa umoja uamuzi uliofanywa na mahakama hiyo katika 1959. Ilitetea haki ya Mashahidi wa Yehova “kukataa kusalimu bendera ya Ufilipino kwa sababu ya itikadi zao za kidini.” Hivyo wanafunzi hawakupaswa kuzuiwa wasiende shule, ziwe za umma au za watu binafsi, kwa sababu kupatana na itikadi za kidini, wao hawakuisalimu bendera, hawakuimba wimbo wa taifa, wala hawakukariri kiapo cha uzalendo kilichoagizwa.

Dada mmoja kwenye kisiwa cha Guam anayefanya kazi ya kimwili wakati wote alitaka kupanua huduma yake. Alitamani kushiriki furaha ya wahubiri waliosimulia mambo waliyoona juu ya mafunzo ya Biblia yenye matokeo. Mara nyingi alisali kwa Yehova juu ya jambo hilo. Alipochunguza hali zake, alikuja kung’amua kwamba kuna uwezekano wa kuwa na mafunzo ya Biblia palepale alipofanyia kazi kila siku. Baada ya kumwomba Yehova ujasiri na utegemezo, alianza kusema na wafanyakazi wenzake. Mwanzoni ilikuwa vigumu; wale walioonyesha kupendezwa walidhihakiwa na wengine. Ili kufikia watu mbalimbali na habari njema, yeye alijitayarisha vizuri na alipata sala kuwa sehemu ya maana ya matayarisho yake. Sherehe za kilimwengu zilipofika, alieleza msingi wa Kimaandiko wa kutoshiriki kwake. Alitafuta fasihi ambayo ingemfaa zaidi kila mmoja. Katika kisa kimoja, alisoma tu Biblia yake kwa ukimya akiwa mahali ambapo mfanyakazi mwenzake angeweza kumwona. Na kwa kweli, mwanamke huyo akawa mdadisi, na funzo likaanzishwa. Hatua kwa hatua dada huyo alianza kusitawisha mafunzo ya Biblia yenye maendeleo. Alipohamishwa kwenye idara nyingine, fursa mpya zilijitokeza. Mwanafunzi mmoja alimjulisha kwa rafiki yake mpendwa aliyeonyesha pia kupendezwa, ambaye naye alisema na mama yake, ndugu yake, na dada-mkwe wake. Wote walijifunza kwa ukawaida. Wengi sana walionyesha kupendezwa hivi kwamba ilimbidi dada yetu aombe wahubiri wengine wamsaidie kuwatunza. Ndiyo, dada yetu amejifunza kwamba matokeo yafaayo na furaha nyingi hupatikana kwa kutoa ushahidi wa vivi-hivi.

Alipokuwa kwenye makaburi, mhubiri mmoja tineja katika Australia alimwona mwanamke Mfilipino akilia kwenye kaburi moja. Alizungumza naye na akaelekeza kwenye maandishi kwenye jiwe la kaburi la babu yake yaliyoandikwa: “Alala akingojea ufufuo.” Hiyo ilifungua njia ya kutoa ushahidi zaidi. Mipango ilifanywa ya kukutana naye mahali hapohapo juma lililofuata, lakini yeye hakuja. Yule mhubiri mchanga aliendelea kumtafuta. Yeye na mama yake walitafuta katika matangazo ya mazishi katika gazeti la mahali hapo hadi walipopata jina lililoonekana kuwa la Mfilipino. Kwa msaada wa kitabu cha simu, waliwasiliana naye. Mwanamke huyo alieleza kwamba alikosa kufika kwa sababu ya matatizo ya usafiri. Lakini alipendezwa kikweli, na mipango ilifanywa kwa ajili ya funzo la Biblia. Kuwafikiria watu pamoja na kuendelea bila kuvunjika moyo huleta matokeo mazuri.

Nchi Ambako Hali Zimekuwa Zenye Kufaa Zaidi

Wakati wa miaka mitano iliyopita, mabadiliko yenye kushangaza yametokea. Katika angalau nchi 35, vizuizi vimeondolewa ili kazi ya kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme iwe huru zaidi. Katika nchi nyingi kati ya hizo, marufuku yameondolewa au shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova limeandikishwa kisheria. Hilo limefungua shamba kubwa kama nini! Ni nini linalofanywa ili kulilima?

Wamishonari 12 pamoja na mapainia wa pekee 20 kutoka Finlandi, wametumwa Estonia. Wahubiri wengine angalau 200 wamehamia Estonia ili kutumikia katika maeneo ambako uhitaji ni mkubwa zaidi. Akina ndugu waripoti: “Watu wa Estonia wana hamu kubwa ya kuzungumzia Biblia. Karibu kila mtu huukaribisha ujumbe.”

Katika Maardu, Estonia, ndugu walipewa uwanja bure ili wajenge Jumba la Ufalme lao, lakini wao walipewa na meya masharti fulani: (1) Ni lazima watengeneze ile bustani ndogo iliyo kando ya jumba hilo; (2) ni lazima Jumba la Ufalme hilo likamilishwe kufikia Oktoba 15, 1993; (3) ni lazima kila mkazi wa jiji hilo awe huru kuhudhuria mikutano, na; (4) ni lazima Mashahidi wawaambie wakazi wa Maardu juu ya ujumbe wa Biblia na kuwafundisha njia bora ya maisha. Akina ndugu walikubali kwa moyo wote masharti hayo yote manne ya meya!

Kwa kuwa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Cape Verde iliandikishwa kisheria katika 1991, wamishonari kumi wamepewa mgawo kwenye eneo hilo. Wao wanapata matokeo ya aina gani? Mume na mke mmoja wamishonari wanaripoti kwamba wanaongoza mafunzo na watu 70, ambao baadhi yao walianza kuongoza mafunzo na wengine baada ya miezi miwili au mitatu tu. Kikundi kilicho mbali cha wahubiri sita kilifurahi wakati watu 150 walipokuja kusikiliza hotuba ya mwangalizi wa mzunguko. Na televisheni ya taifa ilionyesha ujenzi wa Jumba la Ufalme la kwanza katika nchi hii.

Mnamo Januari 8, 1993, Mahakama Kuu Zaidi katika Zaire ilitangaza kwamba ile marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova kuwa si halali. Mwaka huu, wahubiri 75,944 walishiriki katika huduma ya shambani huko. Waliongoza mafunzo yapatayo 163,454 ya Biblia. Zaidi ya hayo, watu 310,088 walihudhuria Ukumbusho.

Zaidi ya miaka 25 iliyopita, serikali ya Kambodia ilikataa kufanyiza upya viza za George na Carolyn Crawford, kwa hiyo walilazimika kuacha mgawo huo wa mishonari. Tangu wakati huo, mara nyingi kumekuwa hakuna Mashahidi katika Kambodia. Hata hivyo, mwaka jana Ndugu Crawford alipokelewa kwa fadhili na mkurugenzi katika Wizara ya Dini ya Kambodia. Mkurugenzi huyo alitaka kujua ni jinsi gani Wakambodia wangenufaika ikiwa wamishonari wetu wangeruhusiwa tena nchini. Vikundi vingine vya kidini viliahidi manufaa za kimwili. Lakini Ndugu Crawford alieleza kwamba Mashahidi wa Yehova hufundisha watu kuishi kupatana na sheria na kanuni za Biblia na kwamba hilo hutokeza manufaa za kiroho, kiadili, na zile halisi, pia jinsi wale wafanyavyo hivyo huja kuwa raia bora zaidi. Waziri huyo alifurahi. Kibali kilitolewa ili wamishonari wawili waingie humo nchini mara hiyo, wengine wakifuata baadaye. Mnamo Januari 20, 1993, barua ilipokewa ambayo ilitoa idhini kwa Watch Tower Society kufungua ofisi katika jiji kuu, Phnom Penh, kwa ajili ya kazi ya kuhubiri ya dini ya Kikristo ya “Yehova.”

Baada ya marufuku ya miaka 40 juu ya Mashahidi wa Yehova katika Romania, wao walipewa utambulisho wa kisheria katika 1990. Wametumia vizuri hali zao zilizobadilika. Mwaka uliopita, kulikuwa na ongezeko la asilimia 15 katika wapiga mbiu ya Ufalme. Tayari, Majumba ya Ufalme 130 yamejengwa au yanajengwa. Baadhi ya wahubiri wanachukua hatua ya kwanza kufikia sehemu ambako hakuna Mashahidi. Katika Septemba 1991, dada mapainia wawili walihamia kwenye mji mdogo wa Urziceni, kilometa 57 kutoka Bucharest. Wakati huo hakukuwa Mashahidi wowote katika jiji hilo; sasa 10 wamebatizwa, na 66 walihudhuria Ukumbusho. Ni nani anayeongoza mikutano? Mwanzoni, akina dada waliipanga na kuiongoza. Sasa ndugu mwenye umri wa karibu miaka 80 ambaye ni mtumishi wa huduma, husafiri umbali wa kilometa 30, mara tatu kwa juma, ili kuongoza mikutano hiyo. Mara moja kwa mwezi, wazee kutoka Bucharest hutoa hotuba ya watu wote na kuongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya kikundi hicho.

Hata katika nchi fulani ambako Mashahidi wa Yehova bado wako chini ya marufuku, wao wameweza kuendelea na huduma yao bila kuzuiwa sana. Katika mojayapo nchi hizo, wahubiri sasa wanafanyia kazi eneo lao kwa ukamili zaidi, wakizuru kila nyumba badala ya kuzuru moja katika mtaa mmoja halafu kwenda kwa nyingine katika mtaa mwingine ili kuepuka kutambuliwa. Katika mji mmoja, wenye mamlaka walisimamisha kikundi cha wahubiri, wakachunguza vitambulisho vyao, na kuwahoji. Akina ndugu walieleza kwamba wao walikuwa wanafunzi wa Biblia na kwamba walitaka kushiriki na wengine yale waliyokuwa wakijifunza. Wenye mamlaka waliwaomba msamaha kwa sababu ya kuwasumbua na wakawaacha waende. Ilikuwa siku yenye furaha ya utumishi wa kitheokrasi.

Katika nchi nyingine ambamo Mashahidi wa Yehova hutendwa kwa ukatili, hivi karibuni wao wamekuwa wakikutana na kuhubiri kwa uhuru zaidi. Huko ni Malawi. Hapo mwanzoni, walipokuwa na kusanyiko dogo, wao walikuwa wakiweka ua wa nyasi kuzunguka nyumba ili mwangaza wa taa usionekane nje. Lakini katika mzunguko mmoja waling’amua kwamba maofisa wa mahali hapo ambao walijua juu ya mikutano yao hawakuwa wakichukua hatua dhidi yao tena; kwa hiyo, wakati wa kusanyiko la hivi karibuni, hawakujenga ua, na hata waliimba nyimbo. Katika eneo jingine, ndugu mmoja alipokuwa akihubiri sokoni, ofisa wa mahali hapo aliyemwona alisema hivi: “Msituogope tena. Tunataka ninyi mhubiri, na hata sisi twapaswa kuwa miongoni mwenu.” Katika eneo jingine tena, mtu mmoja, ambaye kama Sauli wa Tarso, alikuwa kiongozi wa wale waliowanyanyasa Mashahidi alikubali funzo la Biblia. Upesi wengine walihudhuria funzo hilo, na idadi ya wale waliojifunza ilipanda hadi 26. Baada ya yule mtu wa kwanza kubatizwa, idadi ya wale waliojifunza kwa sababu ya mwendo wake uliobadilika ilipanda hadi 66. Halafu, mwishowe, mnamo Agosti 12, 1993, marufuku ya miaka 26 juu ya Mashahidi wa Yehova katika Malawi iliondolewa. Hiyo ni sababu ya kushangilia kama nini!

Matukio katika Albania yamekuwa yenye kutia moyo kwelikweli. Mwishoni mwa Oktoba, mapainia wa pekee 16 kutoka Italia na 4 kutoka Ugiriki walitumwa Albania. Baada ya juma moja katika Albania, ingawa wao walikuwa tu ndio wanaanza kujifunza lugha hiyo, walikuwa wameanzisha mafunzo ya Biblia 90! Katika Gjirokastër, mtangazaji mmoja wa redio alivutiwa sana na yale aliyokuwa akijifunza kutoka kwa mmoja wa mapainia hao wa pekee hivi kwamba akatangaza hivi kwenye redio: “Mashahidi wa Yehova watakuzuru nyumbani. Watazungumzia jinsi ya kuwa na maisha ya familia yenye furaha na kukufunza juu ya yale ambayo Biblia husema. Fungua milango yako. Wasikilize.”

Tangu marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova katika Benin ilipoondolewa katika 1990, misongamano ya watu imemiminika kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Mwaka uliopita, watu 15,951 walihudhuria Ukumbusho—wakiwa karibu mara tano idadi ya wahubiri. Kutaniko moja lenye wahubiri 37 lilikuwa na 698 waliohudhuria!

Katika 1992, hatua za mwisho zilichukuliwa ili kuwapa Mashahidi wa Yehova utambulisho wa kisheria katika Togo, hilo likileta mwisho wa marufuku iliyokuwa imewekwa katika 1978. Maelfu ya watu walikuwa na hamu ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Katika 1993, wale wahubiri 7,125 waliongoza mafunzo ya Biblia nyumbani yapatayo 19,014. Katika Lomé, jiji kuu, kuna wahubiri 4,200, katika makutaniko 33, wanaokutana katika Majumba ya Ufalme sita. Wao wahitaji kwa haraka mahali pengi zaidi pa kukutania. Hata ingawa kulikuwa na msukosuko wa kisiasa, uliofanya wakimbizi wapatao 300,000 kutoroka kutoka Lomé kwenda nchi jirani, Baraza Linaloongoza lilipanga ofisi mpya ya tawi ianze kutenda kazi huko mnamo Juni 1, 1993. Jinsi hilo lilivyowatia moyo akina ndugu katika Togo!

Katika Februari 1993, ile marufuku ya miaka 23 juu ya Mashahidi wa Yehova katika Kameruni iliondolewa. Lilipokuwa likitoa maelezo juu ya uamuzi huo wa serikali, gazeti moja la Kameruni liliandika hivi juu ya watu wa Yehova: “Kijamii, wao huonyesha tabia iliyo tofauti sana na unafiki wa wale walio karibu nao, . . . wao huhubiri kwa kielelezo.” Gazeti hilo liliongeza kwamba, baada ya uhuru wa ibada kupewa Mashahidi, “makanisa yote ya zamani ya Jumuiya ya Wakristo yakabili ushindani mkubwa sana.” Kujapokuwa marufuku hiyo ya muda mrefu, kuna Mashahidi 19,268 katika Kameruni, na watu 67,671 walihudhuria Ukumbusho huko mwaka uliopita.

Vipi juu ya nchi zilizokuwa sehemu ya ile iliyokuwa Muungano wa Sovieti? Kama ilivyosemwa mapema, baadhi ya mikusanyiko yenye kusisimua zaidi katika 1993 ilifanywa katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Katika nchi 12 kati ya hizo, wakati wa mwaka uliopita ndugu zetu walitoa jumla ya muda wa saa 14,180,165 katika kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme, wanafunzi wapya 14,973 wakabatizwa, na wakati wa Ukumbusho, watu 256,242 walikusanyika ili kuadhimisha kifo cha Yesu Kristo. Ndiyo, ni dhahiri kwamba nchi hizi pia, zitawakilishwa vizuri katika ule ‘umati mkubwa kutoka kila taifa na kabila na watu na lugha’ utakaookoka dhiki kubwa inayokuja, ukiwa na taraja la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova, wenye uadilifu.—Ufu. 7:9, 14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki