Jamhuri Ya Kongo (Brazzaville)
Kichwa, ‘Kweli Itawaweka Huru’ (The Truth Shall Make You Free) kilimeremeta kwenye jalada la kitabu cha zambarau katika kifurushi kilichofunguliwa. Etienne alitatanika. Bila shaka kifurushi hicho kilikuwa chake. Kilikuwa na anwani na jina lake, Etienne Nkounkou, mchora-ramani mkuu katika idara ya serikali, Bangui, Muungano wa Nchi za Afrika Magharibi na ya Kati. Lakini hakuagiza kitabu hicho wala hakufahamu shirika la Watch Tower la Uswisi lililokuwa limemtumia kitabu hicho. Hakujua kwamba kweli ya Biblia ambayo inaelezwa katika kitabu hicho ingebadili maisha yake. Kweli hiyo pia ingewaweka huru maelfu ya Waafrika wenzake na dini isiyo ya kweli, ukabila, na wangejua kusoma na kuandika. Ingewalinda watu wengi wasitegemee ahadi nyingi za kisiasa na hivyo kukatishwa tamaa baadaye. Ingewaimarisha na kuwapa tumaini wakati wa magumu. Pia ingewachochea watu wanaomwogopa Mungu wahatarishe uhai wao ili kuwasaidia wengine. Masimulizi hayo yatakugusa moyo na kukutia nguvu. Hata hivyo, kabla ya kujua Etienne alifanya nini, hebu tuchunguze kifupi nchi ya Afrika alikozaliwa.
Miaka kumi kabla ya Christopher Columbus kufunga safari yake maarufu ya kwenda Amerika mwaka wa 1492, mabaharia Wareno walioongozwa na Diogo Cão walifika kwenye mlango wa Mto Kongo huko Afrika ya kati. Hawakujua kwamba mto huo ulitiririka kwa maelfu ya kilometa kabla ya kufika baharini.
Wareno walikutana na wenyeji wa ufalme wa Kongo wenye ufanisi. Kwa mamia ya miaka, Wareno na wafanyabiashara wengine kutoka Ulaya walinunua pembe za tembo na watumwa kutoka kwa Waafrika walioishi pwani. Wazungu walianza kuingia barani mwishoni mwa miaka ya 1800. Pierre Savorgnan de Brazza, afisa wa jeshi la wanamaji la Ufaransa, alikuwa mmoja wa watu mashuhuri waliovumbua eneo hilo. Mnamo mwaka wa 1880, Brazza alitia sahihi mkataba na mfalme mmoja na eneo lililo kaskazini mwa Mto Kongo likawa koloni ya Ufaransa. Baadaye eneo hilo likawa Muungano wa Nchi za Afrika Magharibi na ya Kati. Jiji kuu lilikuwa Brazzaville.
Leo, Brazzaville ndilo jiji kubwa zaidi katika Jamhuri ya Kongo. Jiji hilo liko kwenye kingo za Mto Kongo. Sehemu kubwa ya mto huo wenye urefu wa kilometa 400 hutiririka kwa kishindo kwenye majabali na miamba kuelekea baharini, ambako meli ya Cão ilitia nanga wakati wa safari yake ya uvumbuzi. Ukiwa Brazzaville unaweza kuona kwa mbali Kinshasa, jiji kuu la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ng’ambo ya mto huo. Kwa kuwa nchi zote mbili zinaitwa kwa jina la mto huo, kwa kawaida nchi moja huitwa Kongo (Brazzaville) na nyingine Kongo (Kinshasa).
Maporomoko yanafanya isiwezekane kusafiri kwenye mto huo kutoka Brazzaville kuelekea Bahari ya Atlantiki. Hata hivyo, kuna reli kati ya Brazzaville na jiji la pwani la Pointe-Noire. Wakazi wengi wa Kongo huishi katika majiji hayo mawili na viunga vyake. Ijapokuwa kuna miji mingine ya pwani upande wa kaskazini, sehemu kubwa ya nchi hiyo yenye joto na misitu mingi ina watu wachache.
Kweli Yaanza Kuwaweka Watu Huru
Hebu sasa tuendelee na simulizi la Etienne. Alipokea kile kitabu mwaka wa 1947. Mara tu alipokipokea, Etienne alisoma sura kadhaa za kwanza na kuzizungumzia na jirani yake. Wote walitambua kwamba kinafundisha kweli na hivyo wakaamua kuwaalika rafiki zao Jumapili iliyofuata ili wakisome pamoja na kuchunguza maandiko yaliyomo. Wale waliofika walifurahia mambo waliyojifunza, wakaamua kukutana tena Jumapili iliyofuata. Afisa mmoja wa forodha anayeitwa Augustin Bayonne alihudhuria mkutano wa pili. Yeye pia alizaliwa Brazzaville kama Etienne, naye pia akawa mhubiri mwenye bidii wa kweli inayowaweka watu huru.
Juma lililofuata, Etienne alipokea barua mbili. Moja ilitoka kwa mtu ambaye alimfahamu huko Kamerun, aliyejua kwamba Etienne alipendezwa na mambo ya dini. Alimweleza kwamba alikuwa ametuma jina la Etienne kwenye ofisi ya Watch Tower Society huko Uswisi. Barua ya pili ilitoka Uswisi na ilimwarifu Etienne kwamba alikuwa ametumiwa kitabu fulani na ilimtia moyo akisome na kuwaeleza familia na rafiki zake mambo aliyojifunza. Pia barua hiyo ilikuwa na anwani ya ofisi ya Ufaransa ambako angeweza kupata habari zaidi. Sasa Etienne alielewa ni kwa nini alitumiwa kitabu hicho. Baada ya muda alianza kuwasiliana kwa ukawaida na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa.
Baada ya miaka michache, Etienne na Augustin walirudi Brazzaville. Lakini kabla ya kurudi, Etienne alimwandikia Timothée Miemounoua, rafiki yake aliyekuwa msimamizi wa chuo cha ufundi huko Brazzaville. Alianza barua yake kwa kusema hivi: “Ninafurahi kukufahamisha kwamba tumekuwa tukifuata njia isiyo ya kweli. Mashahidi wa Yehova wana kweli.” Kisha Etienne akamweleza yale ambayo alikuwa amejifunza. Alimtumia pia kitabu ‘Kweli Itawaweka Huru.’ Timothée alikubali ujumbe wa Biblia kama Etienne na Augustin. Ndugu hao watatu ndio waliokuwa Wakongomani wa kwanza kukubali kweli ya Biblia, na kila mmoja wao aliwasaidia wengine wengi kukubali kweli hiyo.
Timothée aliwaalika wanafunzi walioishi kwenye chuo cha ufundi washiriki katika mazungumzo ya Biblia saa za jioni. Aliomba pia atumiwe vichapo vingine vya Biblia. Kikundi hicho kidogo kilianza kufanya mikutano na kujitahidi sana kuhubiri. Baadaye, baadhi ya wanafunzi kama vile Noé Mikouiza na Simon Mampouya, walipata mapendeleo ya kuwa waangalizi katika tengenezo la Yehova.
Katika mwaka wa 1950, Eric Cooke, mishonari aliyeishi Rhodesia ya Kusini (sasa ni Zimbabwe), alitembelea vikundi vidogo vya watu waliopendezwa huko Bangui na Brazzaville ili kuwatia moyo. Hata hivyo, Ndugu Cooke hakujua Kifaransa. Etienne anasema hivi: “Akitumia kamusi yake ndogo ya Kiingereza na Kifaransa, ndugu huyo mnyenyekevu na mwenye fadhili alijitahidi sana kutueleza kuhusu tengenezo la Mungu na kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme. Nyakati nyingine hatukumwelewa hata kidogo.”
Kazi Yazuiwa
Ndugu Cooke alikuja kwa wakati unaofaa kwa kuwa Julai 24, 1950, afisa mkuu wa serikali ya kikoloni alizuia vichapo vya Mashahidi wa Yehova visiingizwe na kusambazwa nchini. Mwaka uliofuata, wahubiri katika ule uliokuwa Muungano wa Nchi za Afrika Magharibi na ya Kati waligawa vitabu sita tu ingawa walifanya mikutano 468 ya watu wote. Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1952 kilieleza hali ya ndugu hao kwa njia ya huruma na fadhili. Kilisema hivi: “Wazia ukiwa katika eneo kubwa lenye wahubiri 37 tu wa ujumbe wa Ufalme waliotawanyika kotekote nchini. Labda hujawahi kukutana na Mashahidi wengine isipokuwa wale wachache walio katika mji wenu. Ulijifunza kweli na jinsi ya kuhubiri kwa kusoma vichapo na barua chache ulizopokea kutoka kwenye ofisi ya tawi. Ndugu wanaoishi katika nchi za Afrika zinazotawaliwa na Ufaransa wanakabili [hali hizo].”
Baadaye Jacques Michel kutoka Ufaransa alikuja kuwatia moyo na kuwazoeza ndugu hao. Noé Mikouiza, mmoja wa wanafunzi kutoka kile chuo cha ufundi anakumbuka swali ambalo liliwatatanisha. Waliuliza: “Je, ni vibaya kunywa divai?” Wote walimkazia macho Ndugu Michel alipokuwa akifungua Zaburi 104:15. Baada ya kusoma mstari huo, Jacques aliwaeleza kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Mungu, lakini Wakristo hawapaswi kunywa kupita kiasi.
Ndugu waliokuwa wamebatizwa karibuni huko Brazzaville waliwahubiria wengine kwa bidii. Kwa kawaida, walivuka mto kwa feri ili kuhubiri Kinshasa, miisho ya juma. Mwaka wa 1952, Wakongomani wa kwanza kutoka upande wa kusini wa mto walibatizwa. Miaka hiyo ya mapema, ndugu wa Brazzaville walijitahidi sana kuwasaidia ndugu wa Kinshasa. Lakini mambo yangebadilika baadaye.
Mnamo Desemba 1954, akina ndugu walipanga kusanyiko jijini Brazzaville. Watu 650 walihudhuria na 70 wakabatizwa. Kweli ilikuwa ikiendelea kuwaweka watu wengi huru na dini isiyo ya kweli. Bila shaka viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo hawakufurahia jambo hilo na walijitahidi sana kuchochea serikali iwapinge Mashahidi wa Yehova. Polisi walifikiri kwamba Timothée Miemounoua ndiye kiongozi wa Mashahidi, hivyo mara nyingi walimwita kwenye kituo cha polisi. Walimtisha na kumpiga. Jambo hilo halikumvunja moyo wala halikuwaogopesha watu wa Yehova huko Brazzaville. Watu walizidi kupendezwa na kweli ya Biblia.
Serikali ilichukua hatua nyingine. Timothée Miemounoua pamoja na Aaron Diamonika, mmojawapo wa wanafunzi wa chuo cha ufundi waliokubali kweli, walikuwa wafanyakazi wa serikali. Katika mwaka wa 1955 serikali iliwahamisha hadi majiji ya mbali ya mashambani. Timothée alipelekwa Djambala na Aaron alipelekwa Impfondo. Jitihada hizo za kukomesha kazi ya kuhubiri hazikufua dafu. Ndugu wa Brazzaville waliendelea kuhubiri kwa bidii huku Timothée na Aaron wakihubiri na kuanzisha makutaniko katika maeneo yao mapya. Ingawa ndugu hao walikuwa na bidii, walitamani sana kupata msaada kutoka nchi nyingine. Msaada huo ulifika baada ya muda mfupi.
Mnamo Machi 1956, mishonari wa kwanza wanne waliwasili kutoka Ufaransa: Jean na Ida Seignobos pamoja na Claude na Simone Dupont. Mnamo Januari 1957, ofisi ya tawi ilifunguliwa Brazzaville ili kusimamia kazi ya kuhubiri katika Muungano wa Nchi za Afrika Magharibi na ya Kati. Ndugu Seignobos aliwekwa kuwa mwangalizi wa tawi. Muda mfupi baadaye, msiba ulitokea ghafula wakati Ida, mke wa Jean, alipokufa katika aksidenti ya gari walipokuwa wakitembelea makutaniko katika ile inayoitwa sasa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Jean aliendelea na kazi ya mzunguko.
Kuhubiri Mashambani
Wakati huo, Augustin Bayonne alikuwa mwangalizi wa mzunguko. Augustin alitembelea vijiji vilivyokuwa ndani sana msituni na pia kambi za Mbilikimo upande wa kaskazini na magharibi mwa nchi. Kwa sababu alizoea kutembea mbali sana, alijulikana kotekote kama Yule Anayetembea. Mara kwa mara, Jean Seignobos aliambatana na Ndugu Bayonne. Jean alishangaa kwamba watu walioishi ndani ya msitu walijua kwamba wanakuja. Ngoma zilitumiwa kuwasilisha ujumbe huu: “Yule Anayetembea anakuja na mzungu.”
Safari hizo zilikuwa na matokeo mengi mazuri. Hapo awali, watu walidai kwamba Mashahidi wa Yehova wanapatikana Kongo (Brazzaville) tu. Madai hayo yalithibitishwa kuwa ya uwongo wakati Ndugu Seignobos na mishonari wengine walipokuja, na sinema Utendaji wa Jamii ya Ulimwengu Mpya (The New World Society in Action) ilipoonyeshwa.
Kweli ya Biblia iliendelea kupenya katika vijiji vya mashambani na kuwaweka watu huru na mazoea ya kuwasiliana na pepo na migogoro ya kikabila. Ndugu wengi katika maeneo hayo hawakujua kusoma na kuandika. Hawakuwa na saa, hivyo walitazama jua ili kujua wakati wa kwenda mkutanoni. Walitumia vijiti vidogo kuhesabu wakati waliotumia katika huduma. Kila mara walipomhubiria mtu, waliweka kijiti kimoja kwenye kitambaa. Vijiti vinne viliwakilisha muda wa saa moja. Kwa njia hiyo waliweza kuandika ripoti zao za utumishi wa shambani mwishoni mwa kila mwezi. Kwa kweli, ndugu hawakuripoti saa zote walizohubiri kwani walimhubiria kila mtu ambaye waliongea naye.
Mabadiliko ya Kisheria na ya Kisiasa
Kumbuka kwamba katika mwaka wa 1950, vichapo vya Mashahidi wa Yehova havikuruhusiwa nchini. Kama tulivyoona, jambo hilo halikuzuia kazi ya kufanya wanafunzi. Wakiwa wamefadhaika, viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walipeleka malalamiko kwa wenye mamlaka, wakidai kwa uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa Wakomunisti. Kwa hiyo, ndugu kumi walikamatwa Alhamisi moja mwaka wa 1956, saa 11 alfajiri. Habari za kukamatwa kwao zilienea haraka; wapinzani wa kidini walishangilia. Kesi ilifanywa siku hiyohiyo katika mahakama iliyojaa ndugu waliokuja kusikiliza.
Noé Mikouiza asimulia hivi: “Wakati wa kesi, tulithibitisha kwamba sisi si Wakomunisti bali Wakristo, watumishi wa Mungu wanaotimiza maneno ya Mathayo 24:14. Wakili wetu aliyekuwa amesoma vichapo vyetu aliiambia mahakama kwamba ikiwa kila mtu angekuwa kama Mashahidi wa Yehova, basi hakungekuwa na wahalifu. Alasiri hiyohiyo uamuzi ulifanywa: ‘Hamna hatia.’ Kwa furaha, sote tulienda nyumbani haraka kubadili mavazi yetu kwa kuwa tulikuwa na mkutano jioni hiyo. Habari za kukamatwa kwetu zilikuwa zimeenea jijini kote, na tulitaka kila mtu ajue kwamba tulikuwa huru. Tulipokuwa mkutanoni, tuliimba nyimbo za Ufalme kwa sauti ya juu sana. Watu wengi waliotusikia tukiimba walishtuka. Walifikiri kwamba tulikuwa tumefungwa gerezani.”
Jamhuri ya Kongo ilipata uhuru Agosti 15, 1960. Migogoro ya kisiasa ilianza. Viongozi wa Jumuiya ya Wakristo walijihusisha sana katika migogoro hiyo, huku Mashahidi wa Yehova wakiendelea na kazi yao ya kuhubiri. Katika mwaka wa 1960, watu 3,716 walihudhuria kusanyiko la mzunguko Brazzaville. Vilevile, katika sehemu ya kaskazini, watu walikuwa wakimiminika katika makutaniko. Kwa mfano, katika eneo moja lenye wahubiri 70, watu elfu moja hivi walihudhuria mikutano ya kutaniko.
Mnamo Desemba 1961, shirika la Mashahidi linaloitwa Les Témoins de Jéhovah liliandikishwa kisheria. Kuandikishwa kisheria kulileta faida nyingi, lakini akina ndugu walijua kwamba halikuwa jambo la hekima kutegemea mambo kama hayo. Ndugu Seignobos anasimulia kilichotukia muda mfupi baadaye: “Siku moja niliitwa na afisa mmoja mkuu katika idara ya usalama ambaye alishtumu msimamo wetu wa Kikristo wa kutounga mkono siasa. Alitisha kunifukuza kutoka nchini. Niliogopa kwamba angenifukuza kwa kuwa alikuwa na mamlaka ya kufanya hivyo. Hata hivyo, siku iliyofuata alikufa kutokana na mshtuko wa moyo.”
Maisha ya Mishonari Katika Miaka ya 1960
Katika Februari 1963, Fred Lukuc na Max Danyleyko waliwasili kutoka Haiti. Baada ya kuoa, Fred alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko. Mwanzoni, alipotembelea makutaniko, ilikuwa vigumu kwake kutofautisha kila familia. Anasema hivi: “Sikuwajua wake wa wazee wala watoto wao. Bado akina ndugu walikuwa wakifuata desturi ya Afrika ya kati ya wake kuendelea kuitwa kwa majina ya baba zao hata baada ya kuolewa na watoto kuitwa majina ya watu wa ukoo au rafiki za familia.
“Siku ya kwanza ya ziara yetu, ndugu walikuwa wenye haya na walisita kuzungumza nasi kwenye Jumba la Ufalme. Mkutano ulipoanza, tuliona jambo lisilo la kawaida. Ndugu na wavulana wakubwa waliketi upande mmoja wa jumba; watoto na akina dada waliketi upande mwingine. Upande wa akina ndugu ulikuwa umejaa mkutano ulipoanza, lakini kulikuwa na dada wachache upande wa pili. Mkutano ulipokuwa ukiendelea, dada wengine waliwasili wakiwa wamebeba Biblia na vitabu kwa ustadi sana vichwani, huku wakiambatana na watoto wao wachanga.
“Nilisimama jukwaani kulisalimu kutaniko na kuwajulisha jina langu na la mke wangu. Baada ya kuwakaribisha kwa uchangamfu, nilitua, nikatazama upande wa wanaume, kisha nikasema: ‘Tafadhali akina ndugu, nawapa dakika kumi ili kila mmoja aketi na mke na watoto wake. Kuanzia sasa, tafadhali ketini na familia zenu kama wanavyofanya watu wa Yehova ulimwenguni pote.’ Walitii maagizo hayo kwa furaha.”
Haikuwa rahisi kusafiri kwa magari ya umma. Leah, mke wa Ndugu Lukuc akumbuka: “Tulibeba vitanda vidogo vya kukunjwa, neti ya mbu, ndoo, vichujio vidogo vya maji, nguo, vitabu, magazeti, na sinema za Biblia. Ili kuonyesha sinema hizo, ilitubidi kubeba nyaya za umeme, balbu, kanda na hati za sinema, jenereta ndogo, na mtungi wa petroli. Tulibeba vitu hivyo vyote tuliposafiri kwa malori ya umma. Ili kuketi sehemu ya mbele pamoja na dereva, ilitulazimu kufika kwenye kituo cha malori saa nane usiku, la sivyo, tungeketi sehemu ya nyuma ya lori pamoja na wanyama, mizigo, na abiria wengine wengi huku tukichomwa na jua.
“Pindi moja, baada ya kutembea kwa saa nyingi jua likituchoma, tulikuta chungu wamevamia nyumba ndogo ya udongo ambamo tulikaa. Walipanda ndoo ya maji, wakatengeneza daraja kwa miili yao hadi kwenye mkebe mdogo wenye siagi, na kula siagi yote. Usiku huo, tulikula mkate mkavu na dagaa mkebe mmoja. Ingawa tulikuwa tumechoka na tulijisikitikia, tulienda kulala na kuwaacha ndugu wakiimba nyimbo za Ufalme kwa sauti nyororo, wakiota moto nje. Ilipendeza na kutuliza sana kusikia nyimbo hizo tulipokuwa tukisinzia!”
Mishonari Waaminifu na Wazee Wenyeji
Kuanzia mwaka wa 1956 hadi 1977, zaidi ya mishonari 20 walitumikia nchini Kongo (Brazzaville). Ingawa nyakati nyingine maisha yalikuwa magumu kwao, kila mmoja wao alitimiza mengi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa mfano, wote waliotumikia kama waangalizi wa tawi walikuwa mishonari. Ndugu Seignobos aliporudi Ufaransa mwaka wa 1962, Larry Holmes aliwekwa kusimamia kazi ya kuhubiri. Baada ya Larry na mkewe Audrey kuacha utumishi wa mishonari mwaka wa 1965, Ndugu Lukuc akawa mwangalizi wa tawi.
Ndugu wengi wenyeji walikuwa waangalizi bora. Mpango wa Halmashauri ya Tawi ulipoanzishwa mwaka wa 1976, Baraza Linaloongoza liliwaweka ndugu watatu: Ndugu mwenyeji, Marcellin Ngolo, na mishonari, Jack Johansson na Palle Bjerre.
Augustin Bayonne—Yule Anayetembea—alihudhuria darasa la 37 la Gileadi mwaka wa 1962. Baada ya kuhitimu, alitumwa Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambako karibu miaka 15 awali alikuwa amesoma kitabu ‘Kweli Itawaweka Huru.’ Baada ya muda, Augustin alioa na kupata watoto. Alirudi Brazzaville, akakubali mikutano ya Kikristo ifanywe nyumbani kwake. Baadaye alitoa kiwanja kwa ajili ya Jumba la Ufalme ambalo lilijengwa baadaye.
Augustin Bayonne na Timothée Miemounoua tayari wamekufa. Kabla ya kifo chake, Timothée aliandika simulizi fupi la maisha yake. Alimalizia simulizi hilo kwa kunukuu Waebrania 10:39: “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.” Etienne Nkounkou, mmoja wa wale watu watatu wa kwanza kukubali kweli nchini Kongo, sasa anakaribia umri wa miaka 90. Lo, jinsi ndugu hao walivyokuwa kielelezo kizuri sana katika utumishi mwaminifu!
Wakati wa Majaribu
Katika Agosti 1970, Jamhuri ya Kongo ilikubali serikali ya Kikomunisti. Kumbuka kwamba katika miaka iliyopita, wenye mamlaka waliwanyanyasa akina ndugu kwa madai ya kwamba walikuwa Wakomunisti. Lakini sasa serikali ya Kikomunisti iliyokuwa ikitawala iliwashutumu kwa sababu hawakuwa Wakomunisti!
Hata hivyo, kwa kipindi fulani serikali hiyo mpya haikuingilia kazi ya Mashahidi wa Yehova. Makusanyiko na mikutano ilifanywa hadharani, na mishonari wapya waliruhusiwa nchini. Hata hivyo hatimaye akina ndugu walianza kusumbuliwa na serikali ya Kikomunisti. Kwanza, maafisa fulani waliwashutumu mishonari kuwa wapelelezi. Kisha kazi ya Mashahidi wa Yehova ikapigwa marufuku Januari 3, 1977. Mishonari wote walifukuzwa nchini isipokuwa Jack na Linda Johansson. Jack anasema hivi kuhusu kipindi hicho: “Katika utumishi wetu wote wa mishonari, imani yetu haijawahi kujaribiwa na kuimarishwa kama katika hiyo miezi michache tuliyokuwa peke yetu katika ofisi ya tawi. Tulidhaniwa kuwa wapelelezi wa Shirika la Upelelezi la Marekani. Maadui wa serikali, kutia ndani viongozi wa dini walikamatwa na kuuawa. Kwa hiyo, tulijua kwamba tulikuwa hatarini. Hata hivyo, tuliona jinsi Yehova alivyotulinda na hilo liliimarisha imani yetu.”
Noé Mikouiza alimsihi waziri mkuu awaruhusu Jack na Linda wakae nchini. Ombi lake lilikataliwa; iliwabidi kuondoka. Majengo ya ofisi ya tawi na Majumba ya Ufalme yalichukuliwa, na ofisi ya tawi ikafungwa. Kwa kipindi kifupi, ofisi ya tawi ya Ufaransa ilisimamia kazi ya kuhubiri, lakini baadaye ofisi ya tawi ya Kinshasa ilikabidhiwa daraka hilo.
Ingawa akina ndugu waliwekewa vizuizi, hawakuteswa vikali kama Mashahidi katika nchi nyingine. Hata hivyo, ndugu fulani waliogopa na wakawatia wengine woga. Bado ndugu walifanya mikutano kwa ukawaida, lakini kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba karibu ikome. Ili kutatua tatizo hilo, ofisi ya tawi ya Kinshasa iliwatuma wazee kuwatia moyo na kuwaimarisha ndugu walioishi ng’ambo ya mto.
André Kitula alikuwa mmoja wa wazee hao. Katika Juni 1981 alianza kutembelea yale makutaniko 12 jijini Brazzaville akiwa mwangalizi wa mzunguko. Alipotembelea kutaniko la kwanza, aliona kwamba akina ndugu walihudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi siku ya Jumanne. Hata hivyo, hakuna mhubiri aliyekuja kwenye mkutano wa utumishi wa shambani Jumatano. André alipokuwa akihubiri peke yake, mwenye nyumba mmoja alimwambia hivi: “Mashahidi wa Yehova ndio waliokuwa wakitufariji, lakini sasa hawaji!”
André alipokuwa akihubiri asubuhi hiyo, aliambiwa hivi na ndugu mmoja aliyekutana naye: “Sote tumeacha kuhubiri nyumba kwa nyumba.” Ndugu huyo aliwaambia wahubiri wengine kuhusu utendaji wa André. Alasiri hiyo dada kadhaa walikuja kwenye mkutano wa utumishi wa shambani. Punde si punde, wahubiri kotekote Brazzaville walianza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Katika muda wa miaka mitatu ambayo André na mke wake Clémentine walitumikia huko, hakuna ndugu hata mmoja aliyekamatwa. Ndugu walioishi nje ya jiji kuu walipata habari hizo. Walikata kauli kwamba ikiwa ndugu jijini Brazzaville hawakuogopa kwenda nyumba kwa nyumba basi wao pia hawakuwa na sababu ya kuogopa.
David Nawej, aliyekuwa akifanya kazi katika ofisi ya tawi ya Kinshasa, anaeleza kwa nini ofisi ya tawi ilifurahi kuwasaidia hasa ndugu walioishi ng’ambo ya mto. Anasema: “Ndugu wa Brazzaville ndio walioleta kweli Kinshasa. Baadaye, wakati serikali ya Kikomunisti ilipofanya ndugu wapunguze bidii yao ya kuhubiri, Mashahidi kutoka Kinshasa walikwenda kuwasaidia. Maneno ya Mhubiri 4:9, 10 yalithibitika kuwa kweli: ‘Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.’ Kwa habari yetu, ndugu walisema: ‘Kongo mbili ni bora kuliko Kongo moja.’”
Kusonga Mbele Licha ya Mabadiliko ya Kisiasa
Kulikuwa na msukosuko na mabadiliko ya kisiasa mwaka wa 1991. Kongo (Brazzaville) iliacha mfumo wa chama kimoja na kufuata mfumo wa vyama vingi. Ingawa kulikuwa na shangwe na vigelegele mitaani, akina ndugu walikumbuka onyo la Zaburi 146:3: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.” Muda mfupi baadaye maneno hayo yalithibitika kuwa kweli.
Hata hivyo, mabadiliko ya kisiasa yaliwafaidi watu wa Yehova. Katika Novemba 12, 1991, waziri wa mambo ya ndani alitoa amri ya kuondoa marufuku juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova. Majumba ya Ufalme yaliyokuwa yamechukuliwa yalirudishwa isipokuwa majengo ya zamani ya ofisi ya tawi, ambayo bado yanakaliwa na Walinzi wa Rais. Mnamo Agosti 1992, makusanyiko ya wilaya ya kwanza baada ya miaka 15 yalifanywa Brazzaville na Pointe-Noire. Mwaka huo, idadi ya mafunzo ya Biblia iliongezeka hadi 5,675, karibu mara nne ya idadi ya wahubiri!
Kuondolewa kwa marufuku kuliwawezesha mishonari kuja nchini tena. Mapainia wa pekee wapya walitumwa maeneo ya kaskazini ambako watu wengi waliohudhuria mikutano hawakujua kusoma na kuandika. Makutaniko katika majiji yalikuwa yamewafundisha watu wengi kusoma na kuandika. Sasa ulikuwa wakati wa kujitahidi kuwafundisha watu kote nchini kusoma na kuandika.
Serikali ilibadilika tena baada ya uchaguzi wa mwaka wa 1993. Chama cha upinzani hakikuridhika na matokeo ya uchaguzi huo, kwa hiyo hali ya hatari ilitangazwa kwa majuma kadhaa. Vita, migomo, amri za kutotembea nje usiku, vizuizi barabarani, na uporaji yakawa mambo ya kawaida. Watu walishtuka na kukata tamaa. Matatizo ya kiuchumi yaliongezeka. Msisimuko wa mwaka wa 1991 ulikuwa umetoweka.
Mbali na msukosuko wa kisiasa, kulikuwa pia na matatizo ya kikabila. Baadhi ya ndugu walilazimika kuhamia maeneo yenye usalama kwa sababu ya migogoro ya kikabila. Kwa sababu hiyo, makutaniko machache yalivunjwa. Wakati huohuo, ndugu waliendelea kuonyesha kwamba kweli iliwaweka huru na chuki ya kikabila. Wakati wa msukosuko huo, ndugu waliwasaidia na kuwalinda ndugu wenzao bila kujali kabila lao. Watu wengi walianza kutambua kwamba ni Yehova peke yake anayeweza kuwapa usalama wa kweli.
Ofisi ya tawi ya Kinshasa ilitoa mwongozo na kitia moyo. Mwishoni mwa mwaka wa 1996, hali ya usalama ilikuwa imerudi katika eneo hilo, na idadi ya wahubiri ilifikia 3,935. Wakati huo, kulikuwa na mishonari watano ambao waliishi katika nyumba moja ya mishonari huko Brazzaville. Mnamo Aprili 1997, mishonari wengine wanne walipowasili makao mengine ya mishonari yalifunguliwa huko Pointe-Noire.
Upande wa kaskazini wa mto, huko Kongo (Brazzaville) kulikuwa na amani na kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme iliendelea bila matatizo. Wakati huohuo, vita vilikuwa vimepamba moto katika nchi jirani ya Kongo (Kinshasa). Vita vilipokaribia jiji la Kinshasa, mishonari walilazimika kuhama. Kwa hiyo, mwishoni mwa Mei, mishonari waliotoka Kinshasa walikuwa wakitumikia kwa bidii pamoja na mishonari wenzao huko Brazzaville na Pointe-Noire. Hakuna yeyote aliyetarajia kwamba hali ingekuwa mbaya sana baada ya siku chache.
Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe Vyazuka
Vita vilizuka ghafula huko Brazzaville Juni 5, 1997. Vita hivyo vilikuwa kati ya majeshi ya rais aliyekuwa akitawala na majeshi ya rais wa zamani. Mizinga mikubwa ililipua na kuharibu jiji na viunga vyake. Maelfu walikufa. Maiti zilitapakaa kila mahali. Kulikuwa na hali ya taharuki jijini. Haikuwa rahisi kutofautisha makundi yaliyokuwa yakipigana. Utulivu wa Brazzaville ulitoweka kabisa. Huduma za feri kuelekea Kinshasa zilikatizwa. Watu wengi walikimbilia msituni, huku wengine wakikimbilia kwenye visiwa vidogo mtoni kwa kutumia mitumbwi yao. Wengine walijaribu kuvuka Mto Kongo kwenda Kinshasa. Kulikuwa na vita karibu na Kinshasa pia, lakini havikuwa vya kikatili kama vita vya Brazzaville.
Sawa na watu wengine, ndugu walipatwa pia na matatizo kwa sababu ya vita, lakini watumishi hao wa Mungu walikuwa na mtazamo tofauti kwa sababu ya kujua kweli. Waliamini kabisa maneno ya Zaburi 46:1, 2: “Kwetu Mungu ni kimbilio na nguvu, msaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu. Ndiyo sababu hatutaogopa, hata dunia ikibadilika na hata milima ikitikisika na kuingia katika moyo wa bahari kuu.”
Ndugu wengi walifika Kinshasa na Halmashauri ya Tawi ikafanya mipango ili wapate chakula, makao, na matibabu. Familia huko Kinshasa zilifurahia kuonyesha upendo na ukarimu kwa waamini wenzao kutoka Brazzaville.
Ndugu kadhaa walibaki Brazzaville ili kuwasaidia wale ambao walishindwa kukimbia. Jean Théodore Otheni na mkewe, Jeanne ambaye ni painia wa kawaida, walikuwa miongoni mwa wale waliobaki. Mnamo Agosti, kombora lilirushwa ndani ya nyumba yao na kumjeruhi vibaya Jeanne. Jean alimkimbiza Kinshasa lakini ilikuwa kuchelewa mno. Jean anakumbuka: “Jeanne alipenda sana huduma hadi kifo chake. Alinipa kitabu chake cha anwani na kusema: ‘Usikose kuwatembelea wanafunzi wangu wote wa Biblia, kwa sababu ninawathamini sana.’ Nilimkumbatia, na nilipoangalia uso wake tena, alikuwa tayari amekufa.” Kama ndugu wengine wengi, Jean ameendelea kumtumikia Yehova kwa bidii, akiwa na uhakika kamili katika ahadi ya ufufuo.
Kwa sababu huduma za feri kati ya majiji hayo mawili zilikuwa zimekatizwa, wale waliokuwa na mashua ndogo zenye injini waliwasaidia watu waliotaka kukimbia Brazzaville. Ndugu jasiri wa Brazzaville, kutia ndani Louis-Noël Motoula, Jean-Marie Lubaki, na Symphorien Bakeba, walijitolea kuwatafuta ndugu waliopotea na kuwasaidia wale waliobaki Brazzaville. Ndugu hao waliendesha mashua zao ndogo katika mikondo yenye nguvu ya Mto Kongo ili wawatafute akina ndugu katika visiwa vidogo na kwenye kingo za mto huo. Walilazimika kuingia katika eneo lenye vita huko Brazzaville ambako watu walikuwa wakiuawa kikatili. Walihatarisha uhai wao kwa ajili ya ndugu zao.
Symphorien, aliyekuwa stadi katika kuvuka mto huo, aliuvuka mara nyingi sana wakati wa vita. Nyakati nyingine alivuka ili kuwasaidia wale waliobaki Brazzaville. Kwa mfano, pindi moja, alivuka akiwa na magunia kumi ya mchele aliyokuwa akiwapelekea ndugu walioishi katika eneo lenye usalama wa kadiri huko Brazzaville. Bila shaka ilikuwa vigumu kuvuka mto huo, lakini ilikuwa vigumu hata zaidi kufikisha magunia hayo bila kunyang’anywa na waporaji. Katika safari hiyo, kulikuwa na abiria mmoja ambaye alionekana kuwa mtu mwenye cheo. Mtu huyo alimuuliza Symphorien alikokuwa akipeleka mchele. Symphorien alimweleza kwamba alikuwa akiwapelekea ndugu zake Wakristo mchele huo, kisha akatumia nafasi hiyo kumweleza kuhusu tumaini lake linalotegemea Biblia. Mashua ilipofika ukingoni, mtu huyo alijitambulisha kuwa afisa wa cheo cha juu. Aliwaita askari kadhaa na kuwaagiza walinde mchele huo hadi Symphorien apate gari la kuusafirisha kwa akina ndugu.
Kwa kawaida, Symphorien alivuka mto ili kuwasaidia ndugu wakimbie Brazzaville. Kuna safari moja ambayo hatasahau kamwe. Anasema: “Mikondo ya Mto Kongo ni yenye nguvu sana, lakini watu wengi wenye mashua wanajua kuvuka bila kupelekwa kwenye maporomoko hatari. Tulipoondoka Brazzaville, mashua yetu ilikuwa na ndugu saba na watu wengine watano. Petroli iliisha tulipokuwa katikati ya mto. Tulifaulu kuiendesha mashua hadi kwenye kisiwa kidogo ambako tulitia nanga. Tulifurahi wakati mashua nyingine ndogo ilipopitia hapo, na nahodha akaahidi kutununulia petroli huko Kinshasa. Tulingojea tukiwa na wasiwasi kwa muda wa saa moja na nusu, mpaka alipoleta petroli.”
Baada ya muda, ofisi ya tawi ya Kinshasa ilikuwa ikiwatunza ndugu na dada 1,000 hivi pamoja na familia zao na watu waliopendezwa. Oktoba 1997, vita vilikuwa vimekwisha na wakimbizi wakaanza kurudi Brazzaville.
Mishonari wote waliokuwa Brazzaville na Pointe-Noire walikuwa wamehamishwa kwa sababu ya vita. Baadhi yao walirudi makwao huko Uingereza na Ujerumani, na wengine walienda Benin na Côte d’Ivoire. Hali ilipotulia kidogo, baadhi yao walirudia migawo yao huko Kongo (Brazzaville). Isitoshe, mishonari saba walitarajiwa kuwasili kutoka Ufaransa mnamo Desemba 1998. Eddy na Pamela May, mishonari wenye uzoefu, waliokuwa wakitumikia katika ofisi ya tawi ya Kinshasa, walitumwa Brazzaville, na makao mapya ya mishonari yakafunguliwa.
Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe Vyazuka Tena
Mwaka uliofuata, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilizuka tena Brazzaville. Kwa mara nyingine tena, maelfu waliuawa kutia ndani Mashahidi kadhaa. Mishonari waliokuwa wamefika majuzi nchini, walipelekwa hadi makao ya mishonari katika nchi jirani ya Kamerun. Ingawa kulikuwa na uvumi kwamba vita vingefika jiji la pwani la Pointe-Noire, mishonari watatu walibaki huko. Hatimaye, vita hivyo viliisha mnamo Mei 1999.
Kwa sababu Mashahidi wengi walilazimika kukimbia, idadi ya makutaniko ilipungua kutoka 108 hadi 89. Sasa jiji la Brazzaville lina wahubiri 1,903 katika makutaniko 23 na Pointe-Noire lina wahubiri 1,949 katika makutaniko 24. Wakati wa vita viwili vya wenyewe kwa wenyewe, Mashahidi wa Yehova kutoka sehemu nyingine waliwasaidia kimwili ndugu na dada zao wa kiroho. Kama kawaida, watu ambao si Mashahidi wa Yehova walifaidika pia na msaada huo.
Kujapokuwa na vita, njaa, magonjwa, na magumu mengine mengi, Mashahidi wa Kongo (Brazzaville) walihubiri kwa wastani saa 16.2 kila mwezi. Mnamo Aprili 1999, vita vya pili vya wenyewe kwa wenyewe vilipoelekea kwisha, asilimia 21 ya wahubiri walikuwa katika utumishi wa wakati wote.
Kushangilia Katika Kweli
Vita vimeleta uharibifu mkubwa katika nchi hiyo, nusura iangamie. Jiji la Brazzaville linajengwa upya, lakini bado kuna mengi ya kufanya. Baadhi ya miradi iliyo muhimu zaidi ni ujenzi wa Majumba ya Ufalme, ambamo watu hujifunza kweli ya Biblia. Katika Februari 2002, Majumba manne ya Ufalme yaliwekwa wakfu, mawili huko Pointe-Noire na mawili Brazzaville.
Jumba moja lilipokuwa likiwekwa wakfu huko Brazzaville, ndugu mmoja mzee alisimulia yaliyotukia wakati wa marufuku miaka 15 iliyopita. Ndugu walikuwa wamepanga kufanya kusanyiko la siku moja katika uwanja fulani mnamo Januari 1. Walifikiri kwamba kusanyiko halingevurugwa kwa kuwa watu wangekuwa wakisherehekea mwaka mpya. Hata hivyo, baada ya kipindi cha asubuhi, polisi walikuja na kuvunja kusanyiko hilo. Ndugu huyo alisema: “Tuliondoka kwenye uwanja wa kusanyiko machozi yakitutiririka. Leo tumekusanyika kwenye uwanja huohuo macho yetu yakitiririka machozi. Lakini sasa tunatiririkwa na machozi ya furaha kwa sababu tumekuja kuweka wakfu Jumba la Ufalme.” Naam, jumba hilo maridadi limejengwa kwenye uwanja huohuo!
Zaidi ya miaka 50 imepita tangu Etienne Nkounkou, Augustin Bayonne, na Timothée Miemounoua walipojifunza kweli kwa kutumia kitabu ‘Kweli Itawaweka Huru.’ Katika kipindi hicho, maelfu ya watu nchini Kongo (Brazzaville) wameiga imani yao na wengine wengi wanaendelea kufanya hivyo, kukiwa na matarajio ya ongezeko kubwa zaidi wakati ujao. Zaidi ya mafunzo ya Biblia 15,000 yanaongozwa, mara tatu na nusu ya idadi ya wahubiri! Idadi ya waliohudhuria Ukumbusho iliongezeka hadi 21,987 mwaka wa 2003. Mwishoni mwa mwaka wa utumishi wa 2003, wahubiri 4,536 kutia ndani mishonari 15, walikuwa wakijitahidi kwa bidii kuwasaidia wengi kujifunza kweli itakayowaweka huru.—Yoh. 8:31, 32.
[Blabu katika ukurasa wa 143]
Ngoma zilitumiwa kuwasilisha ujumbe huu: “Yule Anayetembea anakuja na Mzungu”
[Blabu katika ukurasa wa 144]
Ndugu hawakuwa na saa, hivyo walitazama jua ili kujua wakati wa kwenda mkutanoni
[Blabu katika ukurasa wa 151]
“Tulienda kulala na kuwaacha ndugu wakiimba nyimbo za Ufalme kwa sauti nyororo wakiota moto nje. Ilipendeza na kutuliza sana kusikia nyimbo hizo tulipokuwa tukisinzia!”
[Sanduku katika ukurasa wa 140]
Maelezo Mafupi Kuhusu Kongo (Brazzaville)
Nchi: Jamhuri ya Kongo inapakana na Gabon, Kamerun, Jamhuri ya Afrika ya Kati, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Nchi hiyo ni kubwa kuliko Finland au Italia. Eneo la pwani linafika umbali wa kilometa 60 barani, kisha kuna nyanda zinazoinuka kufikia meta 800. Sehemu nyingine za nchi hiyo zina misitu na mito mikubwa.
Watu: Kuna watu zaidi ya milioni tatu wa makabila mbalimbali. Mbilikimo wanaishi katika maeneo yenye misitu mikubwa.
Lugha: Ingawa lugha rasmi ni Kifaransa, Kilingala huzungumzwa sana katika sehemu za kaskazini. Kimonokutuba huzungumzwa katika sehemu za kusini.
Kazi: Watu hujiruzuku kwa kulima mashamba madogo na kuvua samaki katika mito, maziwa, na bahari. Wawindaji stadi hujiruzuku kwa kuwinda wanyama wengi wa pori walio msituni.
Chakula: Watu hupenda kula muhogo au wali kwa mchuzi uliotiwa pilipili wa samaki au kuku. Kuna matunda mengi kama vile maembe, mananasi, mapapai, machungwa, na maparachichi.
Hali ya hewa: Kongo ni nchi yenye joto jingi na unyevu mwaka mzima. Kuna majira mawili: majira ya mvua kutoka Machi hadi Juni, na majira ya kiangazi kutoka Juni hadi Oktoba.
[Chati/Grafu katika ukurasa wa 148, 149]
Mfuatano Wa Matukio Nchini Kongo (BRAZZAVILLE)
1940
1947: Kitabu ‘Kweli Itawaweka Huru’ chaamsha upendezi.
1950: Mishonari Eric Cooke atembelea Brazzaville. Serikali yazuia vichapo vya Mashahidi wa Yehova visiingizwe nchini.
1956: Mishonari wa kwanza kutoka Ufaransa wawasili mwezi wa Machi.
1957: Ofisi ya tawi yafunguliwa mwezi wa Januari.
1960
1961: Shirika la Mashahidi wa Yehova laandikishwa kisheria Desemba 9 ingawa bado vichapo vyao haviruhusiwi nchini kwa mwaka mwingine mmoja.
1977: Mashahidi wa Yehova wapigwa marufuku. Majengo ya ofisi ya tawi yatwaliwa, na mishonari wafukuzwa.
1980
1981: André Kitula aanzisha tena kazi ya kuhubiri jijini Brazzaville.
1991: Waziri wa mambo ya ndani aondoa marufuku. Baadaye, makusanyiko ya wilaya yafanywa kwa mara ya kwanza baada ya miaka 15.
1993: Hali ya hatari yatangazwa kwa sababu ya misukosuko ya kijamii na ya kisiasa.
1997: Vita vya wenyewe kwa wenyewe vyazuka Juni 5. Mishonari wahamishwa. Ofisi ya tawi ya Kinshasa yafanya mipango ya kuwapa wakimbizi 1,000 chakula, makao, na matibabu.
1999: Vita vingine vya wenyewe kwa wenyewe vyazuka. Mishonari wahamishwa tena.
2000
2002: Majumba manne mapya ya Ufalme yawekwa wakfu mwezi wa Februari. Hayo ndiyo majumba ya kwanza kuwekwa wakfu.
2003: Wahubiri watendaji wafikia 4,536 nchini Kongo (Brazzaville).
[Grafu]
(See publication)
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
5,000
2,500
1940 1960 1980 2000
[Ramani katika ukurasa wa 141]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
JAMHURI YA AFRIKA YA KATI
KAMERUN
GUINEA YA IKWETA
GABON
JAMHURI YA KONGO
Impfondo
Djambala
BRAZZAVILLE
Pointe-Noire
Mto Kongo
JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA KONGO
KINSHASA
ANGOLA
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 134]
[Picha katika ukurasa wa 138]
Kikundi cha awali cha wanafunzi wa Biblia mwaka wa 1949, kuanzia kushoto hadi kulia: Jean-Seth Mountsamboté, Timothée na Odile Miemounoua, na Noé Mikouiza
[Picha katika ukurasa wa 139]
Etienne Nkounkou
[Picha katika ukurasa wa 142]
Jean Seignobos alivuka mito kwa feri ili kutembelea makutaniko ya mashambani nchini Kongo
[Picha katika ukurasa wa 147]
Fred na Leah Lukuc (katikati) pamoja na kutaniko lililokutana katika nyumba ya Augustin Bayonne
[Picha katika ukurasa wa 150]
Ubatizo katika Bahari ya Atlantiki huko Pointe-Noire
[Picha katika ukurasa wa 152]
Augustin Bayonne, Yule Anayetembea, alihudhuria darasa la 37 la Gileadi mwaka wa 1962
[Picha katika ukurasa wa 153]
Jengo hili lilitumiwa kama ofisi ya tawi kuanzia 1967 hadi 1977
[Picha katika ukurasa wa 155]
Noé Mikouiza
[Picha katika ukurasa wa 158]
Louis-Noël Motoula, Jean-Marie Lubaki, na Symphorien Bakeba