Guyana
“Guyana,” ni jina linalomaanisha “Nchi ya Maji Mengi.” Nchi hiyo iko Amerika Kusini na mpaka wake wa kusini uko umbali wa kilometa 130 tu kaskazini ya ikweta. Jina hilo linafaa sana kwa kuwa nchi ya Guyana ina mito zaidi ya 40 na vijito vingi sana ambavyo huondoa maji kwenye misitu ya mvua ambayo imefunika sehemu kubwa ya nchi hiyo yenye ukubwa wa kilometa 215,000 za mraba! Baadhi ya mito hiyo ndiyo mipaka kati ya Guyana na nchi jirani za Brazili, Suriname, na Venezuela. Watu wanaoishi mbali na pwani hutegemea sana mito, na kuna vijiji na mashamba mengi kando-kando ya mito hiyo. Naam, mito imehusika sana katika biashara na historia ya Guyana, kutia ndani historia ya watu wa Yehova.
Nchi ya Guyana ina mito minne mikubwa ambayo ni Essequibo, Demerara, Berbice, na Courantyne. Mto Essequibo, ambao ndio mrefu zaidi, una urefu wa kilometa 1,000, upana wa kilometa 30 kwenye mlango wake, na visiwa 365. Kimoja cha visiwa hivyo ni Kisiwa cha Fort, kilichokuwa makao makuu ya serikali ya ukoloni ya Uholanzi. Mito hiyo mikubwa inayoanzia kwenye milima iliyo barani, inatiririka kaskazini na baadaye inajipinda kupitia uwanda mwembamba wa pwani hadi Bahari ya Atlantiki. Mito hiyo ina baadhi ya maporomoko yenye kuvutia zaidi ulimwenguni. Kwa mfano Maporomoko ya Kaieteur, kwenye Mto Potaro wenye upana wa meta 120, ambao hutiririka na kuingia katika Mto Essequibo, yana urefu wa meta 226.
Guyana huwavutia watu wanaopenda maumbile kwa kuwa ina sehemu nyingi zenye kupendeza. Katika mito yake kuna fisi-maji, mamba weusi, chewa, au Arapaima, ambaye ni kati ya samaki wakubwa zaidi wa maji yasiyo ya chumvi ambao wamewahi kugunduliwa. Samaki hao wenye mapafu hula nyama, nao wanaweza kufikia urefu wa meta 3, na uzito wa kilogramu 220. Wanyama aina ya chui huwinda kimya-kimya katika misitu yenye giza-giza, nao tumbili wenye mlio mkali hupiga kelele wakiwa kwenye miti, ambayo pia ni makao ya aina za ndege zaidi ya 700. Ndege hao wanatia ndani tai mkendege, kasuku wenye rangi zenye kuvutia, na kwembe.
Guyana ina watu wapatao 770,000. Watu hao wanatia ndani Wahindi wa Mashariki, ambao mababu wao walikuja kutoka India chini ya mapatano ya kuwa watumishi au wanafunzi wa ufundi kwa muda fulani; watu weusi, ambao ni wazao wa watumwa Waafrika; Wahindi wenyeji kama vile Waarawaki, Wakaribu, Wawapisiana, Wawarau; na machotara. Ingawa lugha ya Kikrioli huzungumzwa kotekote nchini, Kiingereza ndiyo lugha rasmi. Guyana ndiyo nchi pekee ya Amerika Kusini ambako Kiingereza huzungumzwa.
Maji ya ile Kweli Yafika Guyana
“Maji” ya uzima ambayo hutuliza kiu ya kiroho yalianza kutiririka nchini Guyana yapata mwaka wa 1900. (Yoh. 4:14) Mtu fulani aitwaye Peter Johassen, aliyefanya kazi katika kambi ya wakataji miti karibu na Mto Courantyne, alipata nakala ya gazeti ambalo sasa ni Mnara wa Mlinzi (Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence). Alimpa Bw. Elgin gazeti hilo asome naye Elgin akaandikia Watch Tower Society barua akiomba vichapo zaidi vya Biblia, kutia ndani kitabu fulani kuhusu kusudi la Mungu (The Divine Plan of the Ages). Ingawa Elgin hakushikilia kweli aliyojifunza, aliwafanya wengine wavutiwe nayo. Hivyo, kikundi kidogo kilianzishwa huko New Amsterdam, mji ulio kwenye mlango wa Mto Berbice.
Wakati huohuo, huko Georgetown, mji mkuu wa Guyana, Edward Phillips alipata vichapo vya Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Kwa kuwa Phillips alitaka sana kuwaeleza wengine mambo aliyokuwa akijifunza, aliwakusanya jamaa na marafiki nyumbani kwake kwa mazungumzo ya ukawaida na ya kirafiki kuhusu Biblia. Mnamo mwaka wa 1908 aliandika barua na kuomba mwakilishi wa Watch Tower Society atumwe Guyana, ambayo wakati huo iliitwa Guiana ya Uingereza.a Miaka minne baadaye, Evander J. Coward alifika Guyana na kutoa hotuba za Biblia kwa maelfu ya watu waliokusanyika kwenye kumbi za mji wa Georgetown na New Amsterdam.
Frederick, mwana wa Phillip, anakumbuka ziara ya Coward. Anaandika: “Baada ya muda mfupi, Ndugu Coward alijulikana sana mjini Georgetown, na kwa sababu ya mahubiri yake, watu wenye kupendezwa walianza kujiunga na kikundi chetu cha Wanafunzi wa Biblia. Wakati huo tulijifunza kitabu kuhusu kusudi la Mungu (The Divine Plan of the Ages), kitabu kuhusu uumbaji mpya (The New Creation), na vitabu vinginevyo. Baada ya muda mfupi hakukuwa na nafasi ya kutosha katika nyumba yetu, hivyo mnamo mwaka wa 1913, tukakodi chumba fulani cha juu kwenye jengo la Somerset House mjini Georgetown. Mikutano ya kutaniko ilifanywa katika chumba hicho hadi mwaka wa 1958.” Mnamo mwaka wa 1914, Edward Phillips alikubali nyumba yake itumiwe kama ofisi ya tawi ya kwanza nchini Guyana. Aliwekwa kuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi, naye alifanya kazi hiyo hadi alipokufa mwaka wa 1924.
Katika mwaka wa 1916, “Drama ya Uumbaji” (Kiingereza), iliyokuwa onyesho la picha na sinema, ilichochea sana kazi ya kuhubiri. “Wakati huo, tulifurahia amani na maendeleo ya kiroho,” anaandika Frederick. “Magazeti nchini Guyana hata yalichapisha mfululizo wa hotuba za Charles T. Russell, Mwanafunzi mashuhuri wa Biblia.”
Mwaka wa 1917, hali ilikuwa imebadilika nchini Guyana. Kulikuwa na wasiwasi mwingi kwa sababu ya vita, naye kasisi mmoja maarufu akawahimiza watu waiombee Uingereza na nchi zilizoiunga mkono. Katika barua aliyoandikia vyombo vya habari, Coward alieleza hali ya ulimwengu kwa kuilinganisha na unabii wa Biblia. Na kwenye ukumbi wa mji wa Georgetown, alitoa hotuba yenye kuchochea sana yenye kichwa “Kubomoa Kuta za Babiloni.”
Ripoti moja katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1983 inasema: “Makasisi walikasirika sana hivi kwamba waliwashawishi wenye mamlaka wamfukuze Ndugu Coward na kupiga marufuku vichapo kadhaa. Marufuku hiyo haikuondolewa hadi mwaka wa 1922.” Hata hivyo, watu wengi walimheshimu Coward kwa kuwa alihubiri kwa ujasiri. Hata alipokuwa akiondoka, walisimama gatini na kupaaza sauti: “Yeye tu ndiye aliyehubiri kweli.” Wafanyakazi wa bandari hata walitisha kugoma ili kupinga kufukuzwa kwa Coward, lakini ndugu wakawashauri wasifanye hivyo.
Baada ya vita vya kwanza vya ulimwengu, Wanafunzi wa Biblia walikabili jaribu lisilo wazi, ambalo kwa muda fulani lilizuia kazi ya kueneza kweli ya Ufalme. Mwasi imani mmoja ambaye zamani alifanya kazi kwenye makao makuu huko Brooklyn, alitembelea Guyana mara kadhaa akiwa na nia ya kuwapotosha Wanafunzi wa Biblia ili waache tengenezo.
Gazeti la Mnara wa Mlinzi ambalo limetajwa linasema: “Kwa muda fulani, Wanafunzi wa Biblia katika nchi hiyo waligawanyika katika vikundi vitatu, yaani, ndugu waliokuwa washikamanifu kwa tengenezo, wapinzani, na wale ambao hawakujua la kufanya. Hata hivyo, Yehova aliwabariki ndugu wale tu waliokuwa washikamanifu, na hatimaye idadi yao ikaongezeka.” Malcolm Hall, aliyebatizwa mwaka wa 1915, na Felix Powlett, aliyebatizwa mwaka wa 1916, walikuwa kati ya ndugu hao washikamanifu. Wote wawili walimtumikia Yehova kwa bidii na waliishi kwa zaidi ya miaka 90.
Ili kuwatia moyo ndugu waliokuwa waaminifu, George Young kutoka makao makuu, alikuja Guyana mwaka wa 1922 na kukaa kwa muda wa miezi mitatu hivi. “Alikuwa mfanyakazi asiyechoka,” akasema Felix Powlett. Young aliwachochea wengi walichunguze Neno la Mungu kwa makini zaidi kwa sababu ya ujuzi wake wa Biblia, sauti yake yenye nguvu, ishara zake za mwili, na mifano aliyotumia alipotoa hotuba. Habari hii kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1923 inategemea ripoti za Young: “Idadi ya watu wanaopendezwa na kweli katika nchi hii imeongezeka. Hudhurio limeongezeka kwenye mikutano yote ya watu wote, majumba ya mikutano yanafurika watu, nao ndugu wameongeza bidii yao.” Kwa mfano, kwenye jengo la Somerset House wastani wa watu 100 walikuwa wakihudhuria mikutano, hata ingawa wahubiri wa Ufalme walikuwa 25 tu wakati huo.
Mwaka wa 1923, ndugu walikuwa wakijitahidi pia kuwafikia watu walioishi mbali na pwani. Mara nyingi walibeba nyavu za kulalia na vichapo tu, wakitumaini kwamba watu wakarimu wangewapa chakula. Mtu alipowakaribisha, walilala kwake. Lakini walipokosa kukaribishwa walining’iniza nyavu zao za kulalia chini ya mti na kulala huko. Mara nyingi walivumilia mbu wengi sana. Asubuhi iliyofuata walichunguza andiko katika kitabu cha andiko la siku (Daily Heavenly Manna), ambacho kilichapishwa na tengenezo la Yehova, kisha kuomba lifti kwenye mashua au kutembea kwa miguu hadi kijiji kingine.
Ndugu waliendelea kujitahidi kuwafikia watu walioishi kwenye maeneo ya mbali hadi Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza. Wakati huo petroli iliuzwa kwa kipimo, na watu hawakuweza kusafiri sana. Kabla ya hapo, katika mwaka wa 1931, Wanafunzi wa Biblia walikubali jina Mashahidi wa Yehova. Vikundi vidogo vya Wanafunzi wa Biblia walioishi pwani walikubali kwa furaha jina hilo jipya na kuonyesha bidii yao kwa kuongeza utumishi wao. Mwishoni mwa miaka ya 1930, wahubiri walianza kutumia vinanda katika huduma ili kutoa hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Frederick Phillips, aliyekuwa msimamizi wa ofisi ya tawi wakati huo, anasema: “Siku hizo hakukuwa na redio vijijini, na watu walijua tumefika kijijini mwao waliposikia sauti ya muziki ikivuma kutoka kwenye vikuza sauti vyetu. Muziki huo ulifuatwa na hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Karibu kila mtu kijijini alikuja, baadhi yao wakiwa wamevaa nguo za kulala.”
Vituo vya redio pia vilisaidia kueneza habari njema. Kituo kimoja nchini Guyana kilitangaza ujumbe wa Ufalme kila Jumatano na Jumapili. Bila shaka, Shetani aliona utendaji huo wote, naye alijaribu kuzuia kazi ya kuhubiri kwa kutumia hisia za uzalendo zilizochochewa na Vita vya Pili vya Ulimwengu.
Vita vya Pili vya Ulimwengu na Utendaji Baada ya Vita
Katika mwaka wa 1941, wakati wa vita vya pili vya ulimwengu, Guyana ilikuwa na wahubiri wa Ufalme 52. Mwaka huohuo, gazeti la Mnara wa Mlinzi na la Amkeni! (lililoitwa Consolation) yalipigwa marufuku. Mnamo mwaka wa 1944 vichapo vyote vya watu wa Yehova vilipigwa marufuku. Ripoti moja katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1946 inasema: “Mashahidi wa Yehova hawakuruhusiwa kuwa na Biblia yoyote, hata kama haikuwa na maelezo ya Watch Tower na hata kama ilikuwa imechapishwa na vyama vingine vya Biblia.”
Katika Aprili mwaka wa 1946, Nathan Knorr kutoka makao makuu alitembelea Guyana. Aliandamana na William Tracy, aliyekuwa amehitimu Shule ya Gileadi muda mfupi kabla ya hapo. Walikuja ili kuwatia ndugu moyo na kuiomba serikali iondoe marufuku. Katika mkutano uliofanywa huko Georgetown, Ndugu Knorr aliwaeleza ndugu na watu wenye kupendezwa 180 waliokuwa wamekusanyika kwamba, wanafunzi wa zamani wa Yesu hawakuwa na Biblia wala vitabu vya kuwasaidia katika huduma. Hata hivyo, Yehova aliwabariki kwa ongezeko kubwa. Kwa nini? Kwa sababu waliendelea kuhubiri. Kwa hiyo, hapana shaka kwamba Mungu angewabariki watumishi wake wa siku hizi kama wangeendelea kuhubiri bila kuacha.
Wakati huohuo, ndugu waliendelea kutafuta njia za kisheria ili marafuku hiyo iondolewe. Kwa mfano, mwaka mmoja hivi baada ya vita kwisha, ndugu hao walipata sahihi za watu 31,370 kwenye waraka wa kupinga marufuku hiyo. Waraka huo ulipelekewa serikali. Isitoshe, ili watu wa Guyana wajue yaliyokuwa yakiendelea, tengenezo la Yehova lilichapisha trakti iliyoeleza mambo kinaganaga. Kichwa cha trakti hiyo kilisema: “BIBLIA TAKATIFU YAPIGWA MARUFUKU HUKU GUIANA YA UINGEREZA—WATU 31,000 WATIA SAHIHI WARAKA NA KUTAKA GAVANA awarudishie uhuru wa ibada wakaaji wote wa koloni hii, hata wawe wa dini gani.”
Ndugu Knorr pia alimtembelea W. L. Heape, aliyekuwa waziri wa koloni hiyo na kuomba marufuku iondolewe. Baada ya mazungumzo yao ya dakika 30, Ndugu Knorr alimpa Bw. Heape nakala ya kitabu kimoja cha funzo (“The Truth Shall Make You Free”), naye akamwomba akisome kwa makini. Bw. Heape alisema kwamba atakisoma. Isitoshe, alimwambia Ndugu Knorr kwamba marufuku juu ya vichapo vyetu ilikuwa ikizungumziwa na wanachama tisa wa kamati ya usimamizi wakati huohuo! Bw. Heape alisema kweli, kwa kuwa mnamo Juni 1946, gavana alitangaza kuondolewa kwa marufuku hiyo.
Muda mfupi baadaye, ndugu walipokea katoni 130 zenye vumbi zilizokuwa zimezuiliwa, ambazo zilikuwa na vitabu na vijitabu 11,798. Wahubiri wa Ufalme, ambao wakati huo walikuwa 70, walifurahi sana kuweza kuwatolea watu vichapo tena, nao wakavigawa vyote kwa muda wa majuma kumi tu. Mwezi wa Agosti, ndugu walianza pia kuhubiri barabarani, na walipata matokeo mazuri. “Magazeti yetu yalikuwa rahisi kugawa, karibu sawa na magazeti ya kila siku,” yasema ofisi ya tawi.
Hata wakati wa marufuku, ndugu waliendelea kupata chakula muhimu cha kiroho, kwa sababu ya jitihada za ndugu fulani aliyefanya kazi kwenye posta kuu huko Georgetown. Ndugu huyo anaandika: “Nilihisi kwamba nilikuwa na wajibu wa kuhakikisha kwamba nakala za Mnara wa Mlinzi zimefika kwenye ofisi ya tawi. Dada walisaidia kupiga chapa au kurudufisha nakala za funzo kwa kutumia mashine ya kunakili, kisha familia mbalimbali zikapewa nakala hizo kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.”
Wamishonari Wapya Wachochea Kazi ya Kuhubiri
Kazi ya kuhubiri ilipamba moto wakati wamishonari waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi walipofika Guyana katika miaka ya 1940. Wamishonari hao walikuwa William Tracy, mhitimu wa darasa la tatu, na pia John na Daisy Hemmaway, na Ruth na Alice Miller, wahitimu wa darasa la tano. Mashahidi hao wenye bidii waliwaeleza ndugu wenyeji mambo muhimu waliyojifunza Gileadi, nao waliweka mfano mzuri katika kazi ya kuhubiri.
Ndugu Tracy aliwahangaikia watu walioishi katika maeneo ya mbali. Aliandika: “Ili kuwasiliana na watu waliopendezwa ambao waliishi mbali, na pia kutafuta wengine wenye kupendezwa, nilisafiri kokote nchini, kutia ndani eneo lote la pwani na kando-kando ya mito. Nilisafiri kwa gari-moshi la pwani, basi, baiskeli, mashua kubwa na ndogo, na hata mitumbwi.”
Wamishonari pia waliwasaidia mapainia wenyeji kuwa na mpango mzuri ili waweze kuhubiri kwenye eneo kwa utaratibu, na ikiwezekana kujitahidi kuhubiri katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa. Kumbuka kwamba mnamo mwaka wa 1946, Guyana ilikuwa na makutaniko matano tu na kilele cha wahubiri 91 wa Ufalme. Lakini hakuna jambo linaloweza kuwashinda watu ambao wametiwa nguvu na roho ya Mungu.—Zek. 4:6.
Mwanzoni, mapainia wengi waliohubiri pamoja na wamishonari walikuwa wazee. Hata hivyo, licha ya umri wao, walikuwa wenye bidii. Mapainia hao walikuwa Isaac Graves, George Headley, Leslie Mayers, Rockliffe Pollard, na George Yearwood. Akina dada walikuwa Margaret Dooknie, Ivy Hinds, Frances Jordan, Florence Thom, Atalanta Williams, na Princess Williams (si wa ukoo mmoja). Mapainia hao walihubiri ujumbe wa Ufalme katika maeneo mbalimbali wakiwa wamebeba vitabu, vijitabu, na magazeti.
Ivy Hinds (sasa anaitwa Wyatt) na Florence Thom (sasa anaitwa Brissett) walitumwa katika mji wa Bartica ulio kilometa 80 hivi kutoka pwani, karibu na Mto Essequibo. Watu hupita katika mji huo wanapoelekea barani ambako kuna migodi ya dhahabu na almasi. Kulikuwa na ndugu mmoja tu huko. John Ponting, ambaye wakati huo alikuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi na wa mzunguko, anaandika: “Katika muda wa miezi miwili, watu 20 walikuwa wakihudhuria mikutano, na 50 walihudhuria Ukumbusho.” Jerome Flavius, aliyekuwa kipofu ni kati ya wale waliokubali kweli. John anasema, “Muda si muda, Flavius alikuwa akitoa hotuba bila msaada, baada ya Ivy Hinds kumsomea habari kuhusu hotuba hiyo mara kadhaa.”
Ingawa umri wa Esther Richmond na Frances Jordan ulikuwa unakaribia miaka 70, walijifunza kuendesha pikipiki ili waweze kuhubiri kwenye eneo kubwa zaidi. Ndugu Ponting anasema: “Margaret Dooknie, ambaye hakukumbuka miaka ambayo alikuwa amefanya utumishi wa upainia, alikuwa akitembea na kuchoka sana hivi kwamba nyakati nyingine tulimkuta amelalia benchi kwenye bustani. Hatutawasahau kamwe watu kama hao.”
Mfano wa wamishonari na mapainia wazee uliwachochea vijana wengi kuanza utumishi wa upainia. Kwa sababu hiyo, watu wengi walijifunza kweli, na vikundi na makutaniko yakaanzishwa sehemu mbalimbali nchini. Katika mwaka wa 1948, Guyana ilikuwa na wahubiri 220. Katika mwaka wa 1954 idadi hiyo ilifikia 434. Wakati huohuo, ndugu wa Kitty-Newtown waliofanya mikutano yao katika jengo la Somerset House waliongezeka wakawa wengi sana hivi kwamba waliweza kuanzisha kutaniko la Newtown, lililokuwa la pili katika mji mkuu wa Georgetown. Leo mji huo una makutaniko tisa.
Baiskeli, Punda, na Mikokoteni Yenye Vikuza-Sauti
Mwanzoni mwa miaka ya 1950, ndugu walifuata mwongozo wa ofisi ya tawi na kutoa hotuba za hadharani kotekote mjini Georgetown. Kwa kawaida hotuba hizo zilitolewa Jumamosi jioni na Jumapili alasiri. Walitumia mkokoteni waliokuwa wamejitengenezea kubeba kikuza sauti fulani chenye nguvu, vikuza-sauti vidogo viwili, nguzo za kuwekelea vikuza-sauti, na nyaya. Albert Small aliyebatizwa mwaka wa 1949 anasema, “Mchana, tuliweka ubao mahali pa mikutano. Ubao huo ulisema: ‘Maswali Yako ya Biblia Yajibiwa,’ na ulionyesha saa za mikutano. Wengi walikuja kusikiliza hotuba hizo, na baadaye baadhi yao wakawa Mashahidi.”
Hotuba ambazo Nathan Knorr na mwandishi wake, Milton Henschel, walitoa kwenye ukumbi wa sinema wa mji wa Georgetown mapema mwaka wa 1954, zilionyesha kwamba kungekuwa na ongezeko. John Ponting alikuwapo naye anasema hivi: “Watu 1,400 waliketi ndani, nao wengine 700 wakasikiliza wakiwa nje hadi mvua kubwa ilipowalazimisha wengi wao kuingia ndani. Hotuba hizo zilitangazwa na waendesha baiskeli waliobeba mabango. Jioni, tulitumia ubao wenye mwangaza uliovutwa na punda, na ndugu alitoa matangazo kupitia kikuza-sauti.”
Twatembelea Maeneo Mengi Barani
Alipokuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi, William Tracy aliwatia ndugu moyo wawatembelee watu walioishi kwenye maeneo ya mbali. Yeye mwenyewe alitembelea maeneo ya Mto Essequibo na Berbice na kupanga makusanyiko ya mzunguko kwa ajili ya vikundi vidogo na makutaniko katika maeneo hayo. Kwa kawaida, makusanyiko hayo yalifanywa katika kumbi za sinema na shule za umma. Mara nyingi kumbi za sinema tu ndizo zilizokuwa na nafasi ya kutosha. Kwenye kusanyiko lililofanywa mwaka wa 1949 katika ukumbi wa sinema kijijini Suddie, karibu na mlango wa Mto Essequibo, hotuba ya watu wote yenye kichwa “Fundisho la Moto wa Mateso Latumiwa Kuwatisha Watu” iliwavutia watu sana. Baadhi yao walianza kuwaita Mashahidi wa Yehova lile kanisa ambalo halifundishi kuhusu moto wa mateso.
Katika mwaka wa 1950, William Tracy aliyekuwa ameoa karibuni, alitumwa tena Marekani. John Ponting ndiye aliyewekwa kuwa mwangalizi mpya wa ofisi ya tawi na mwangalizi anayesafiri. John pia alisaidia kuhubiri katika maeneo fulani kando-kando ya mito. Ndugu walisafiri kwa meli za kawaida. Wanavijiji walioishi kando-kando ya mito walipokuja kwa mitumbwi yao kupokea na kutuma barua, ndugu waliwaomba wawapeleke kwenye ufuo, wakitumaini kwamba mtu fulani angewapa chakula na mahali pa kulala. Kwa kawaida, baada ya kuwahubiria watu kijijini, familia fulani iliwakaribisha ndugu hao nyumbani kwao jioni. Siku iliyofuata, mtu fulani aliwasafirisha kwa mtumbwi ili wahubiri kwenye kijiji kingine. Alasiri moja walitembelea kiwanda cha kupasulia mbao. Meneja wa kiwanda hicho alisimamisha kazi, akawakusanya wafanyakazi, na kuwaruhusu ndugu hao wawatolee hotuba ya dakika 15. Wote walichukua vichapo.
Mnamo Julai 1952, Thomas Markevich, aliyehitimu darasa la 19 la Shule ya Gileadi, alitumwa Guyana. Yeye pia alienda kuhubiri katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa. Tom anasema: “Unapata furaha ya pekee unapomweleza ujumbe wa Ufalme mtu ambaye hajawahi kuhubiriwa. Lakini wakati mwingine unaona mambo yenye kushangaza sana. Nilisafiri kwa mashua kwenye Mto Demerara, kisha nikaingia msituni kwa miguu, ambako nilipata nyumba moja ndogo. Baada ya kunisalimu, mwenye nyumba hiyo alinikaribisha ndani, akanipa kiti, na kunisikiliza. Nilipotazama huku na huku katika nyumba yake, nilishangaa kuona kwamba kuta zilikuwa zimefunikwa kwa karatasi za magazeti ya Mnara wa Mlinzi ya miaka ya 1940! Yaonekana mtu huyo tayari alikuwa amehubiriwa ujumbe wa Ufalme, labda kwenye mashua, mjini Georgetown, au huko Mackenzie.”
Donald Bolinger, ndiye mmishonari wa kwanza kufunga safari ngumu ya kwenda kwenye Maporomoko ya Kaieteur, kwa kupitia nchi kavu. Alipokuwa akiwahubiria Wahindi wenyeji alikutana na ofisa wa serikali aliyekuwa akifanya kazi huko. Hatimaye ofisa huyo alijiweka wakfu kwa Yehova naye alisaidia kikundi kilichoanzishwa huko baadaye. Wahubiri kadhaa walihamia maeneo ya mbali, kama vile maeneo yenye migodi ya almasi au dhahabu, kwa sababu ya kazi yao. Ingawa waliishi mbali na Mashahidi wengine, mara nyingi walihubiri nyumba kwa nyumba kambini. Ni nini kilichowasaidia kuendelea kuwa na nguvu kiroho? Walikuwa na ratiba nzuri ya kujifunza na kuhubiri.
Utumishi ‘Wenye Kufurahisha na Kuridhisha’
Wamishonari John na Daisy Hemmaway walitumikia nchini Guyana kuanzia mwaka wa 1946 hadi 1961. Nyakati nyingine walipokuwa likizoni, wamishonari hao walikaa kwa majuma mawili katika wilaya ya kaskazini-magharibi, karibu na Venezuela, ambako makabila ya Wakaribu, Waarawaki, na makabila mengine ya Wahindi wenyeji waliishi. Pindi moja waliwaachia Waarawaki vichapo vingi sana. Jambo hilo halikuwafurahisha watawa Wakatoliki waliosimamia shule ya eneo hilo. Watawa hao waliwauliza watoto kama wazazi wao walikuwa wamepokea vichapo vyovyote. Wazazi waliposikia hayo walikasirika sana na kumwambia kasisi kwamba wao wenyewe wangejichagulia vitabu vya kusoma. Maneno hayo hayakumvunja moyo kasisi huyo badala yake, wakati wa ibada ya Jumapili, alishutumu kijitabu kuhusu tumaini la kuishi duniani milele (Can You Live Forever in Happiness on Earth?) ambacho watu wengi walikuwa wamekubali. Lakini mbinu hiyo ilishindwa pia, kwa kuwa siku ambayo ndugu na dada Hemmaway waliondoka, wanakijiji wengi walienda kuwaomba nakala ya kijitabu hicho.
Ili kufika kwenye eneo hilo, lililo kilometa 300 hivi kutoka pwani, John na Daisy walisafiri kwa feri, gari-moshi, na lori. Walibeba vitu vya lazima tu pamoja na vichapo na baiskeli, ambayo waliihitaji ili kusafiri kwenye barabara za udongo na kufikia vijia vidogo vya Wahindi. John anaeleza, “Vijia hivyo vinaelekea huku na huku, na ni lazima mtu atumie akili au akate vitawi na kuviweka mahali ambapo vinakutana ili asipotee anaporudi. Mtu anapokutana na mnyama aina ya chui kwenye vijia hivyo, kwa kawaida yeye husimama tuli na kumtazama. Hatimaye, mnyama huyo huondoka njiani polepole. Tumbili huruka huku na huku kwenye miti huku wakitoa mlio mkali kupinga kuingiliwa kwa makao yao, naye mnyama aina ya sloth, ambaye huning’inia juu chini, humtazama tu mpita njia bila kufanya lolote. Mara kwa mara mtu anaweza kumwona ndege aina ya kwembe mwenye rangi za kuvutia akila papai mahali pasipo na miti.”
Baada ya kutumikia akiwa mmishonari kwa miaka 15 nchini Guyana, Ndugu Hemmaway alieleza hisia zake hivi: “Huo ulikuwa utumishi wenye kufurahisha na kuridhisha sana. Unapata furaha isiyo na kifani unapoketi kwenye sakafu ya udongo katika nyumba ya makuti, na kuwaeleza Wahindi wenyeji kuhusu Ufalme wa Mungu na kuwafundisha njia mpya ya maisha. Hatutawasahau kamwe watu hao wanyenyekevu waliokubali mafundisho ya Biblia na kujiweka wakfu kwa Mungu.”
Mapainia Wenyeji Wahudhuria Shule ya Gileadi
Mapainia kadhaa wenyeji walipata pia pendeleo la kuhudhuria Shule ya Gileadi, na baadhi yao wakarudi Guyana. Baadhi ya mapainia hao ni Florence Thom (sasa anaitwa Brissett), darasa la 21, 1953; Albert na Sheila Small, darasa la 31, 1958; na Frederick McAlman, darasa la 48, 1970.
Florence Brissett anasema: “Nilitarajia kutumwa katika nchi za kigeni, lakini niliiona kuwa baraka kutoka kwa Yehova nilipotumwa katika kijiji cha Skeldon, nchini Guyana. Wengi kati ya wanashule wenzangu wa zamani, walimu, marafiki, na watu niliofahamiana nao walikubali kujifunza Biblia pamoja nami kwa sababu walinijua. Hata wengine, kama vile Edward King ambaye mke wake alikuwa akijifunza pamoja nami, waliniomba nijifunze Biblia pamoja nao! Kasisi wa Kanisa la Anglikana aliposikia kwamba mke wa Edward alikuwa akijifunza, alimwita Edward na kumwamuru asimamishe funzo hilo mara moja. Lakini badala ya kufanya hivyo, Edward mwenyewe alianza kujifunza.”
Baada ya Ndugu na Dada Small kurudi kutoka Shule ya Gileadi, Albert alitumikia kwa miaka mingi katika Halmashauri ya Tawi na pia akiwa mwangalizi wa mzunguko. Licha ya matatizo ya afya, leo Albert na Sheila wanatumikia wakiwa mapainia wa pekee katika kutaniko moja nchini Guyana, naye Albert ni mzee kutanikoni. Si mapainia wote waliotoka Guyana ambao walirudi huko. Kwa mfano, Lynette Peters, mhitimu wa darasa la 48, alitumwa Sierra Leone. Bado anatumikia katika nchi hiyo.
Sinema Yaamsha Upendezi
Sinema kuhusu jamii ya ulimwengu mpya (The New World Society in Action), ilitumiwa sana na Mashahidi wa Yehova katika miaka ya 1950. Ilihusu makao makuu huko Brooklyn na kusanyiko kubwa lililofanywa huko Yankee Stadium, New York City, mwaka wa 1953. Sinema hiyo iliwasaidia Mashahidi na watu wengine kuelewa vizuri zaidi tengenezo la Yehova na ukubwa wake. Bila shaka, sinema hiyo iliwavutia sana watu walioishi ndani ya msitu wa mvua na ambao hawakuwa wamewahi kuona sinema yoyote!
Mara nyingi, sinema hiyo ilionyeshwa nje kwenye ua mkubwa. Watu walikuwa wakitembea kilometa nyingi kuja kuiona. Huenda ukauliza, ‘Lakini, ndugu waliwezaje kuionyesha katika maeneo yasiyokuwa na umeme?’ Alan Johnstone, mhitimu wa Shule ya Gileadi aliyekuja Guyana mwaka wa 1957 na kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko, alionyesha sinema hiyo pindi kadhaa. Anaandika: “Mahali ambapo hapakuwa na umeme, kwa fadhili wenyeji walituazima jenereta zao ambazo walitumia kuangazia maduka yao usiku. Ili kuonyesha sinema hiyo tulitandaza shuka kubwa kati ya miti miwili.”
Baada ya onyesho moja kama hilo, John na Daisy Hemmaway walirudi nyumbani kwa meli. Abiria wengi walikuwa wamesikia kuhusu sinema hiyo, wao nao walitaka kuiona. Hivyo, nahodha alipokubali sinema hiyo ionyeshwe, ndugu na dada Hemmaway walitandaza shuka yao kwenye sitaha na kukiweka kifaa cha kuonyeshea sinema katika chumba kimoja chenye dirisha lililoelekeana na sitaha hiyo. John anaandika: “Makasisi wa Kanisa Katoliki na Kanisa la Anglikana walikuwa katika meli hiyo.” “Ingawa hawakunyenyekea kutazama sinema hiyo ilipoonyeshwa kwenye nchi kavu, sasa waliitazama wakiwa melini, labda bila kutaka. Hata kifaa cha kuonyeshea sinema kilikuwa kimewekwa katika chumba chao. Baadaye abiria waliwauliza maswali mengi ambayo ni Mashahidi wa Yehova tu wanaoweza kuyajibu.”
John Ponting anaandika hivi kuhusu uvutano wa sinema hiyo: “Wakati huo, sinema hiyo ilikuwa na matokeo mazuri katika maeneo ambayo Mashahidi walikuwa wachache, na ambako walionwa kuwa watu wasio wa maana. Watu wenye kutilia shaka walipata nafasi ya kuona tengenezo kubwa lenye watu wa jamii mbalimbali, nao wakaanza kutuheshimu. Sinema hiyo ilibadili mtazamo wa wengi, nao wakakubali kujifunza Biblia. Baadaye, baadhi yao wakawa wazee wa kutaniko. Katika muda wa majuma mawili tu, mwangalizi mmoja wa mzunguko alionyesha sinema hiyo mara 17. Mara nyingi aliionyesha nje, na watu 5,000 waliitazama.
“Pindi nyingine, mwangalizi mmoja wa mzunguko alisafiri kwa muda wa siku mbili kwenye mto wenye maporomoko, kisha akatembea kwa miguu kwenye kijia cha msitu kwenda kuonyesha sinema hiyo. Jitihada zake hazikuwa za bure kwa kuwa Wahindi wenyeji wengi, ambao hawakuwa wamewahi kuona sinema, waliifurahia. Siku iliyofuata, wanakijiji wengi ambao walikuwa wafuasi wa kanisa la Presbiteri, walichukua magazeti. Baada ya ziara hiyo, watu wote wa kijiji hicho walikuwa na maoni mazuri kuwahusu watu wa Yehova.”
Kuanzia mwaka wa 1953 hadi 1966, Guyana ilikumbwa na msukosuko wa kisiasa na wa kijamii. Msukosuko huo ulipamba moto kati ya mwaka wa 1961 hadi 1964, na kulikuwa na fujo, uporaji, mauaji, na mgomo wa nchi nzima. Hakukuwa na usafiri wa aina yoyote, na watu wengi walikuwa na woga. Ndugu hawakunyanyaswa moja kwa moja, lakini baadhi yao waliteseka kwa sababu ya hali hizo. Kwa mfano, ndugu wawili walipigwa, na wengine wawili, kutia ndani Albert Small, wakapigwa marisau kwa bunduki. Iliwabidi kwenda hospitalini ili marisau hizo ziondolewe. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba vikosi vya Uingereza viliingilia kati.
Sinema kuhusu jamii ya ulimwengu mpya ilifaa sana wakati huo wa msukosuko kwa kuwa ilionyesha watu kutoka mataifa yote ambao wana amani na umoja wa kweli! Isitoshe, ndugu hawakuacha kuhudhuria mikutano na kuhubiri kwa sababu ya ukosefu wa usafiri. Iliwabidi watembee mbali kidogo isivyo kawaida, au kutumia baiskeli. Zaidi ya yote, walionyeshana upendo wa kweli wa Kikristo. Albert Small anasema, “Walijali wenzao na waligawana vitu walivyokuwa navyo.”
Dada Wahubiri Katika Maeneo ya Mbali
Dada pia walipeleka ujumbe wa Ufalme katika maeneo ya mbali. Kwa mfano, Ivy Hinds na Florence Thom waliwekwa kuwa mapainia wa pekee huko Bartica, karibu na msitu. Mahadeo, aliyekuwa mhubiri pekee katika eneo hilo, aliishi huko pamoja na mkewe Jamela. Jamela hakujua kusoma wala kuandika kwa kuwa wakati huo wasichana wengi wa jamii ya Wahindi wa Mashariki hawakupelekwa shuleni. Hata hivyo, alitaka kujisomea Biblia na kusaidia kuwafundisha wana wao wawili. Florence alisema, “Kwa baraka za Yehova na msaada wangu, upesi Jamela alijifunza kusoma, kuandika, na kuwahubiria wengine.”
Ingawa Florence na Ivy walikuwa wamekaa Bartica kwa miezi miwili, bado hawakuwa wamepata nyumba nzuri ya kuishi. Walihitaji pia mahali pa kufanyia mikutano, kwa kuwa walikuwa wanaongoza mafunzo kumi ya Biblia. Hali hiyo ilikatisha tamaa hata zaidi wakati walipojulishwa kwamba mwangalizi wa mzunguko angekuja kuwatembelea. Isitoshe, mwangalizi huyo angekuja juma ambalo wafanyakazi wa mashambani na malaya kutoka Georgetown walimiminika Bartica na kufanya idadi ya watu katika mji huo iongezeke mara tatu!
Lakini mkono wa Yehova si mfupi. Florence anasema: “Wakati wa jioni-jioni, siku moja kabla ya mwangalizi wa mzunguko kufika, tulikutana na mtu mmoja mwenye nyumba za kukodisha, ambaye alikubali kukodisha nyumba moja ndogo yenye vyumba viwili vya kulala, katikati ya mji. Tulifanya kazi kwa bidii sana kusafisha kuta na kuzipaka rangi, kisha tukang’arisha sakafu. Tuliweka pazia na kuingiza vyombo vya nyumbani, na kumaliza kazi hiyo alfajiri. Huo ulikuwa usiku wenye hekaheka kwelikweli! John Ponting, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko, hakuweza kuamini masikio yake tulipomweleza yote tuliyofanya. Mkutano wa kwanza wakati wa ziara yake, ambao ulifanywa jioni, ulihudhuriwa na watu 22, jambo lililotupa tumaini kwamba karibuni kungekuwa na kutaniko mjini Bartica.”
Kusafiri kwa Mashua Zinazoitwa Kingdom Proclaimers
Zamani, ndugu walisafiri kwa mashua na mitumbwi yoyote iliyopatikana ili kufika kwenye vijiji vilivyokuwa kando-kando ya mito. Baadaye walinunua mashua ambazo waliziita Kingdom Proclaimer 1, Kingdom Proclaimer 2, hadi Kindom Proclaimer 5. (Mashua mbili za kwanza hazitumiki sasa.)
Frederick McAlman anasema: “Tulikuwa tukisafiri kwa mashua tukifuata mkondo wa maji ili kuhubiri kuanzia ukingo wa mashariki wa Mto Pomeroon hadi kijiji cha Hackney, umbali wa kilometa 11 kutoka mlango wa mto huo. Huko tulilala vizuri nyumbani kwa Dada DeCambra, ambaye wakati huo alikuwa mkunga katika eneo hilo. Asubuhi na mapema siku iliyofuata, tulisafiri hadi mlango wa mto huo kabla ya kuuvuka na kwenda kwenye ukingo wa magharibi. Kisha tulisafiri kwa mashua umbali wa kilometa 34 hadi Charity.” Kwa miaka mitano, ndugu walipiga makasia kwenda upande wa juu na wa chini wa Mto Pomeroon, kabla ya kununua mashua fulani ya zamani iliyokuwa na injini.
Kwa kawaida haikuwa hatari kusafiri kwenye mito hiyo, lakini ndugu walihitaji kuwa waangalifu kwa kuwa kulikuwa na mashua nyingine kwenye mito. Mashua ya kwanza na ya pili, hazikusafiri kwa kasi kwa kuwa ziliendeshwa kwa kuvuta makasia. Frederick anasema: “Jumamosi moja alasiri, nilipokuwa nikirudi nyumbani baada ya kuhubiri kwenye eneo la Mto Pomeroon, mashua kubwa ya kubeba mizigo iliyokuwa ikisafiri kwa kasi sana iligongana na mashua yangu. Nahodha na wafanyakazi wa mashua hiyo hawakuwa macho kwa sababu walikuwa wamelewa. Nilirushwa kutoka katika mashua yangu Kingdom Proclaimer 1, na kutumbukia mtoni, chini ya mashua yao. Nilizama majini, lakini nikaendelea kupambana ili kujiokoa. Kichwa changu kilikuwa kikigonga sehemu ya chini ya mashua yao, nami nilikuwa sentimeta chache tu kutoka kwenye rafadha yake iliyokuwa ikizunguka kwa nguvu. Kijana mmoja kwenye meli hiyo aliponiona, alijitosa mtoni na kuniokoa. Nilikuwa na maumivu kwa majuma kadhaa kwa sababu ya majeraha, lakini nilishukuru kwamba nilikuwa hai!”
Frederick hakuvunjwa moyo na mkasa huo. Anaeleza: “Niliazimia kuendelea kuhubiri, kwa sababu watu walioishi kando-kando ya mto huo walipendezwa na Biblia. Katika kijiji cha Sirikie, umbali wa kilometa 11 kutoka Charity, kulikuwa na Funzo la Kitabu la Kutaniko ambalo niliongoza.”
Nahubiri kwa Juma Moja Pamoja na Mwangalizi wa Mzunguko
Mwangalizi wa mzunguko anahitaji kuwa mvumilivu ili kutumikia katika sehemu za mashambani za Guyana. Mbali na kusafiri kwenye mito, barabara za vumbi, na vijia vya msitu, nyakati nyingine waangalizi wa mzunguko pamoja na wake zao hukabiliana na mbu na wadudu wengine, wanyama aina ya chui, mvua nyingi na, katika maeneo mengine, wanyang’anyi. Wao pia hukabili hatari ya kushikwa na malaria, homa ya matumbo, na magonjwa mengine ya kawaida katika maeneo yenye joto.
Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliwatembelea wahubiri walioishi kando ya Mto Demerara, mbali na kutaniko, naye anaandika hivi: “Baada ya kutembelea Kutaniko la Mackenzie, tulisafiri kwa mashua siku ya Jumatatu ili kumtembelea ndugu fulani katika kijiji cha Yaruni, kilicho kando ya mto huo, umbali wa kilometa 40 hivi kutoka Mackenzie. Tulipofika huko, tulihubiri kwenye pande zote mbili za mto kwa kutumia mtumbwi, huku tukifuata mkondo wa maji kurudi Mackenzie.
“Watu walikuwa wakarimu sana, nao walitupa matunda na hata wakatukaribisha kula pamoja nao. Siku ya Ijumaa, tulisafiri kwa mashua ili kupanda meli iliyotupeleka hadi Soesdyke, ambako tulishuka na kupanda mtumbwi kwenda ufuoni. Ndugu fulani alitulaki, kisha tukavuka Mto Demerara kwenda nyumbani kwake huko Georgia. Jioni hiyohiyo, tulifanya mkutano pamoja na familia yake.
“Siku iliyofuata, sote tulivuka Mto Demerara kwenda Soesdyke. Tulihubiri katika eneo la Soesdyke na pia katika eneo lenye watu wengi, karibu na uwanja wa ndege wa Timehri. Pia tulitembelea eneo lenye marundo ya mchanga, ambako watu waliupakia kwenye malori yaliyoupeleka Georgetown. Jumamosi usiku, tulifanya mkutano mwingine pamoja na familia hiyo huko Georgia. Siku iliyofuata, sote tulivuka mto tena na kwenda Soesdyke ambako tulihubiri asubuhi, kisha hotuba ya watu wote ikatolewa alasiri nje ya jengo moja la posta. Ziara yetu iliisha hivyo.” Bidii ya waangalizi wa mzunguko wenye kujitolea kama hao na wake zao, ilikuwa na matokeo kwa kuwa sasa kuna kutaniko lenye maendeleo huko Soesdyke. Ndugu wana Jumba lao la Ufalme lililojengwa mwaka 1997.
Waangalizi wa mzunguko pia walipatwa na mikasa. Jerry na Delma Murray, waliokuwa wakisafiri kwa pikipiki, walifika kwenye mtaro fulani ambao daraja lake lilikuwa limetengenezwa kwa mbao chache zilizounganishwa pamoja. Delma alingoja huku Jerry akivuka daraja hilo kwa pikipiki. Lakini wakati wa kuvuka mambo yalienda mrama, na Jerry akatumbukia kwenye maji yenye matope pamoja na pikipiki na sanduku. Delma alipiga mayowe na wanakijiji wakaja mbio kusaidia. Muda mfupi baadaye, wasiwasi uligeuka kuwa kicheko kwa kuwa, kama vile ndugu mmoja alivyoandika, “mzungu huyo alipanda ufuoni akiwa amefunikwa na magugu, na viatu vikiwa vimejaa matope.”
Wahindi Wenyeji Wakubali Habari Njema
Alipokuwa akihubiri sokoni huko Charity, mapema miaka ya 1970, Frederick McAlman alimwachia Monica Fitzallen, Mhindi mwenyeji, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 176.) Monica, ambaye aliishi katika eneo lililotengewa Wahindi wenyeji, alirudi nyumbani na magazeti hayo. Pindi fulani alipokuwa mgonjwa, Monica aliyasoma na kutambua kwamba mambo yaliyosema ni ya kweli. Muda si muda, akawa ndiye mhubiri pekee wa habari njema katika eneo hilo, naye akabatizwa mwaka wa 1974.
Monica anasema: “Nilihubiri nyumba kwa nyumba kwa bidii, na nilifurahia kuwaeleza watu wa eneo letu mambo mapya niliyokuwa nimejifunza. Hata hivyo, ili kufika nyumbani kwao, ilinibidi kusafiri kwa mashua kwenye mito na vijito. Idadi ya watu wenye kupendezwa ilipoongezeka, nilianza kufanya mikutano pamoja nao, na tulisoma na kuzungumzia habari kwenye kitabu cha kujifunzia Biblia, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele.”
Je, bidii ya Monica ilikuwa na matokeo? Ndiyo, kwa kuwa sasa kuna wahubiri wengine 13 katika eneo hilo, kutia ndani mumewe, mwanaye na mke wake, na mjukuu wake msichana. Zamani, ndugu katika kikundi hicho kidogo walikuwa wakisafiri kwa muda wa saa 12 kwa mtumbwi hadi Kutaniko la Charity, lililokuwa karibu zaidi. Lakini sasa wanafanya mikutano katika eneo lao, na hudhurio huwa mara tatu zaidi ya wahubiri!
Kutaniko la Charity limekuwa na ongezeko pia. Sasa lina wahubiri 50, na wengi wao husafiri kwenye Mto Pomeroon ili kufika mikutanoni. Wastani wa watu wanaohudhuria mikutano ni zaidi ya 60, na watu 301 walihudhuria Ukumbusho mwaka wa 2004. Kutaniko la Charity pia lina Jumba jipya la Ufalme.
Ongezeko Kubwa Huko Baramita
Baramita ni eneo lingine nchini Guyana ambako wenyeji wengi wamekubali ujumbe wa Ufalme. Eneo la Baramita ambalo liko kaskazini-magharibi mwa Guyana, ni makao ya Wahindi wa kabila la Wakaribu. Wakaribu ni baadhi ya wakaaji wa kwanza kabisa wa eneo la Karibea, na jina hilo linalotokana na jina la kabila hilo. Lugha yao inaitwa Kikaribu.
Ruby Smith ambaye ni Mkaribu, alianza kupendezwa na kweli mwaka wa 1975 alipopewa trakti na nyanya yake. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 181.) Ruby alikuwa na umri wa miaka 16 wakati huo. Alifanya maendeleo ya kiroho na kubatizwa mwaka wa 1978 kwenye Kusanyiko la “Imani Ishindayo.” Muda mfupi baadaye, familia yao ilihamia Georgetown kwa sababu za kibiashara. Huko, Ruby aliolewa na Eustace Smith. Eustace hakuongea Kikaribu, hata hivyo, yeye na Ruby walitaka sana kuhamia Baramita ili kuwaeleza jamaa za Ruby na watu wengine ujumbe wa Ufalme. Ruby anasema: “Yehova aliona yaliyokuwa mioyoni mwetu naye alijibu sala zetu kwa sababu mwaka wa 1992, tulienda Baramita.”
Ruby anaongeza: “Tulipofika Baramita, nilianza kuhubiri mara moja. Tulifanyia mikutano yetu chini ya nyumba yetu ndogo, ambayo ilikuwa meta 1.5 hivi juu ya ardhi. Muda si muda, watu wakawa wengi sana wasiweze kutoshea katika nyumba hiyo, hivyo tukaazima mahema. Habari kuhusu mikutano hiyo zilipoenea, hudhurio liliongezeka na kufikia watu 300! Kwa kuwa nilisoma Kikaribu kwa ufasaha, nilipewa mgawo wa kufasiri Mnara wa Mlinzi. Watu hao wote waliwezaje kusikia? Tulitumia maikrofoni ya bei rahisi inayotumia mawimbi ya FM, na wengi kati ya wasikilizaji walibeba redio zao ambazo zilinasa mawimbi hayo ya sauti.
“Wakati huo, mimi na Eustace tuliona kwamba kikundi hicho kilihitaji Jumba la Ufalme. Kwa hiyo, baada ya kukadiria gharama na kuzungumzia mradi huo pamoja na wengine, tulianza kujenga. Ndugu yangu Cecil Baird alitoa vifaa vingi vilivyotumiwa katika ujenzi, nao wengine wakasaidia kwa kufanya kazi. Ujenzi ulianza Juni 1992 na kuisha mapema mwaka uliofuata, kabla tu ya Ukumbusho. Tulishangaa kuwaona watu 800 waliokuja kusikiliza hotuba ambayo ilitolewa na Gordon Daniels, mwangalizi anayesafiri.
“Kikundi cha Baramita kimekuwa kutaniko tangu Aprili 1, 1996, na Jumba la Ufalme liliwekwa wakfu Mei 25, mwaka huohuo. Tangu wakati huo jumba hilo limepanuliwa na sasa linatoshea watu zaidi ya 500, na ndugu wanaweza kulitumia kwa makusanyiko ya mzunguko na ya pekee. Naam, sasa kutaniko hilo ambalo mwanzoni lilikuwa kikundi kidogo tu, lina wahubiri wapatao 100, nayo Mikutano ya Watu Wote huhudhuriwa na wastani wa watu 300. Watu 1,416 wamehudhuria Ukumbusho!”
Arusi Kubwa Sana!
Katika wilaya ya Baramita, wanaume na wanawake wengi waliokuwa wakiishi pamoja bila kufunga ndoa walihalalisha ndoa zao kupatana na kanuni za Biblia. Lakini ilikuwa vigumu kwa baadhi yao kupata vyeti muhimu, kama vile vyeti vya kuzaliwa. Hata hivyo, baada ya juhudi nyingi na pia kusaidiwa na akina ndugu kujua tarehe zao za kuzaliwa na habari nyingine, watu hao waliweza kufunga ndoa.
Pindi moja, wenzi 79 walifunga ndoa kwenye sherehe ileile. Hotuba ya arusi ilitolewa na Adin Sills, wa Halmashauri ya Tawi. Siku tatu baadaye, watu 41, wengi wao wakiwa baadhi ya wale waliofunga ndoa, waliomba kuwa wahubiri.
Hali katika eneo lote la Baramita imekuwa bora sana kwa kuwa watu wengi wanapendezwa na Neno la Mungu. Jumba la Ufalme lilipokuwa likiwekwa wakfu, mzee mmoja alisema: “Sasa Baramita ni eneo lenye utulivu na amani. Hiyo ni kwa sababu zaidi ya asilimia 90 ya watu wa eneo hilo huhudhuria mikutano kwa ukawaida.”
Katika mwaka wa 1995, wilaya ya Baramita ilikumbwa na ukame mbaya. Watu wa Yehova walifanyaje? Wakati huo Gillian Persaud alikuwa mwalimu huko Baramita. Aliposikia kwamba ndege ndogo imetua kwenye uwanja mdogo uliokuwa karibu, dada huyo alitimua mbio ili kuzungumza na rubani kabla ndege hiyo haijaondoka. Alimwomba rubani huyo ampeleke Georgetown, ambako alienda moja kwa moja hadi kwenye ofisi ya tawi ili kueleza hali ya akina ndugu.
James Thompson, ambaye wakati huo alikuwa katika Halmashauri ya Tawi, anasema: “Baraza Linaloongoza lilituruhusu kupeleka chakula na bidhaa nyingine kwa ndege huko Baramita. Pia tulipanga wahubiri 36 wapelekwe kwa ndege hadi Georgetown kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Kwa wengi wao, hiyo ilikuwa mara yao ya kwanza kuhudhuria kusanyiko.”
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma
Tangu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ianzishwe mwaka wa 1987, nchi nyingi, kutia ndani Guyana, zimefaidika na kazi ya wazee na watumishi wa huduma waseja ambao wamehudhuria shule hiyo. Baada ya kuhudhuria shule hiyo iliyofanywa katika kisiwa jirani cha Trinidad, ndugu wengi wenyeji wamesaidia sana katika kazi ya Ufalme nchini Guyana. Sasa baadhi yao ni mapainia wa kawaida, mapainia wa pekee, na wazee wa kutaniko. Wale waliorudi katika makutaniko ya kwao wanajitahidi sana kutunza kondoo za Yehova.
Wahitimu kadhaa wa shule hiyo wameweza kukubali majukumu zaidi. Kwa mfano, Floyd na Lawani Daniels, ambao ni ndugu wa kimwili, walitumwa kama mapainia wa pekee katika makutaniko yaliyohitaji wazee haraka. David Persaud alipata pendeleo la kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko. Mwanafunzi mwenzake, Edsel Hazel, aliwekwa katika Halmashauri ya Tawi ya Guyana. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi kuhusu ndugu fulani waliohudhuria shule hiyo: “Nimewaona ndugu hao wote wakifanya maendeleo kiroho, hasa baada ya kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma.”
Kutumikia Katika Eneo Lenye Uhitaji Mkubwa
Mwishoni mwa miaka ya 1970, Pwani ya Atlantiki, iliyo magharibi ya Mto Essequibo, ilikuwa na wakaaji 30,000 hivi na wahubiri 30 tu. Kwa hiyo, pindi kwa pindi ofisi ya tawi ilikuwa ikiwatuma mapainia wa pekee ili wahubiri katika sehemu mbalimbali za eneo hilo na walikaa katika kila eneo kwa muda wa mwezi mmoja. Ndugu aliyesimamia kikundi kimoja cha mapainia hao alisema: “Ndugu hao walihubiri katika eneo hilo lote na kuwaachia watu vitabu 1,835. Walifanya ziara nyingi za kurudia na kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.”
Ndugu mwingine alisema: “Tulisafiri kwa mashua zetu ndogo umbali wa kilometa 27, kwa muda wa saa mbili. Nyakati nyingine, tulilazimika kuburuta au kusukuma mashua katika matope yaliyofika kwenye magoti, lakini jitihada zetu hazikuwa za bure kwa kuwa wenye nyumba walikuwa wakarimu. Mwalimu mmoja wa muziki aliyekuwa akitumia kitabu chetu cha nyimbo kufundisha muziki alisema: ‘Ninapenda sana mpangilio wa muziki wenu.’ Kisha akatuchezea nyimbo mbili na kukubali vitabu sita.”
Ndugu na dada wengine walijitolea kusaidia katika maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa. Fikiria kisa cha Sherlock na Juliet Pahalan. Sherlock anaandika: “Katika mwaka wa 1970, mimi na Juliet tulialikwa kwenda kusaidia Kutaniko la Eccles, lililokuwa karibu na Mto Demerara, kilometa 13 kusini ya Georgetown. Kutaniko hilo lilikuwa na matatizo na ikabidi wengine watengwe. Kutaniko liliachwa na wahubiri 12 hivi, na watoto wao ambao hawakuwa wamebatizwa. Kwa muda fulani, mimi tu ndiye niliyekuwa mzee. Isitoshe, kutaniko hilo lilishughulikia kikundi kidogo katika kijiji cha Mocha, kilichokuwa mbali. Kila Jumatatu jioni, niliongoza Funzo la Kitabu la Kutaniko huko Mocha, kisha lingine huko Eccles.
“Pia, niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi. Kwa kuwa hatukuwa na magazeti ya kutosha kwa ajili ya kila mmoja, tulisoma fungu kwanza, kisha tukauliza swali, kinyume na ilivyofanywa wakati huo. Tulibeba mishumaa kwenye mikutano kwa sababu umeme ulikuwa ukipotea-potea; wakati wa majira ya mvua tulishambuliwa na mbu wengi sana. Wakati huo ndugu wengi walisafiri kwa miguu au kwa baiskeli kwenda kwenye mikutano au eneo la kuhubiri. Wahubiri wa Mocha walisafiri vivyo hivyo kuja Eccles. Baada ya mikutano, nilikuwa nikiwabeba watu wengi iwezekanavyo kwa gari langu dogo na kuwapeleka makwao Mocha.”
Je, jitihada hizo zote zilikuwa na matokeo? Ndugu Pahalan anaandika hivi kuhusu wakati huo: “Nilipokuwa Eccles, mimi na mke wangu tulijifunza Biblia na watu kadhaa, na wengi wao, kutia ndani familia zao, bado ni Mashahidi. Sasa baadhi yao ni wazee wa kutaniko. Hizo ni baraka zisizo na kifani!”
Kutumikia Katika “Paradiso ya Mapainia”!
Katika miaka michache iliyopita, ndugu na dada wapatao 50, hasa mapainia kutoka Ireland, Kanada, Marekani, Ufaransa, na Uingereza wameenda katika Nchi ya Maji Mengi ili kujiunga na wenyeji kusema: “Njoo! . . . Yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” (Ufu. 22:17) Baadhi yao wameweza kukaa nchini humo kwa miezi michache na wengine kwa miaka mingi. Wanapopungukiwa na pesa, wengi hurudi nyumbani kufanya kazi kwa muda, kisha wao hurudi tena Guyana. Wengi wanaona kwamba hali yao ya kiroho imekuwa bora kwa sababu ya utumishi wao nchini Guyana. Wanathamini sana kuzungumzia mambo ya kiroho pamoja na watu ambao, kwa ujumla, wanaiheshimu sana Biblia. Hata wengi ambao si Wakristo hufurahia kuzungumza na Mashahidi wa Yehova. Isitoshe, nyakati nyingine wenye nyumba huwakaribisha ndugu kwa chakula. “Kwa hiyo, hatutii chumvi tunaposema kwamba Guyana ni paradiso ya mapainia,” asema Ricardo Hinds, ambaye sasa ni mratibu wa Halmashauri ya Tawi.
Arlene Hazel, ambaye sasa anatumikia kwenye ofisi ya tawi pamoja na mumewe Edsel, anakumbuka mambo fulani yaliyowapata katika maeneo ya mashambani ya Guyana: “Mnamo 1997, baada ya kuwasiliana na ofisi ya tawi, tulitumwa Lethem, mji ulio mbali mashambani, karibu na mpaka wa Brazili. Tulitumikia huko pamoja na Wakanada wenzetu, Robert na Joanna Welch, na dada Mmarekani, Sarah Dionne, ambaye alikuwa amefika Lethem miezi michache kabla yetu. Richard Achee, ndugu aliyekuwa amebatizwa na ambaye alikuwa daktari wa mifugo, aliishi huko wakati huo. Ofisi ya tawi ilitupa majina 20 ya watu waliokuwa wakijifunza zamani, lakini tukapata kwamba wengi wao hawakuwa wenye kupendezwa. Hata hivyo, wawili kati yao, walitaka kuwa wahubiri.
“Tulifanya mkutano wetu wa kwanza chini ya mwembe, na watu 12 walihudhuria, kutia ndani sisi mapainia 6. Miezi michache baadaye, watu 60 walihudhuria Ukumbusho wa kwanza tuliofanya huko. Wakati huo, mapainia walikuwa watatu tu. Hata hivyo, tulikuwa tukijitahidi kuongoza mafunzo 40 ya Biblia! Mwangalizi wa mzunguko alipokuja, alitushauri tuache kujifunza na yeyote ambaye hakuhudhuria mikutano. Huo ulikuwa ushauri mzuri, kwa kuwa watu tulioendelea kujifunza nao walifanya maendeleo.”
Miaka minne baadaye, kikundi cha Lethem kikawa kutaniko lenye wahubiri 14. Hudhurio kwenye makusanyiko ya pekee huko Lethem limeongezeka hadi watu 100. Huo ni uthibitisho ulio wazi kwamba Yehova anabariki jitihada za watumishi wake, na jambo hilo hufanya wavumilie shida zozote ambazo huenda zikawapata.
Mikutano Katika “Nyumba za Chini” na Katika Majumba ya Kukodiwa
Tangu kazi ya kuhubiri ianze nchini Guyana, imekuwa vigumu kupata Majumba ya Ufalme yanayofaa. Katika mwaka wa 1913, ndugu kadhaa waliokuwa Georgetown walikodi chumba kwenye jengo la Somerset House, ambacho walikitumia kwa miaka 45. Kufikia mwaka wa 1970, ni makutaniko mawili tu, la Charlestown huko Georgetown na la Palmyra huko Berbice, ambayo yalikuwa na Jumba la Ufalme. Hata hivyo, miaka mitatu kabla ya hapo, idadi ya wahubiri nchini Guyana ilikuwa imepita 1,000! Kwa hiyo, makutaniko mengi yalikutanika katika majengo ya kukodiwa, ambayo mara nyingi hayakuwa yenye kupendeza.
Kwa mfano, mwishoni mwa miaka ya 1950, Kutaniko la Wismar, karibu na Mto Demerara, liliongezeka sana hivi kwamba ndugu walilazimika kutafuta jumba linalofaa. Waliruhusiwa kutumia jengo lililoitwa Islander Hall. Walifanya mkutano wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi katikati ya juma, na Mkutano wa Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi Jumapili jioni. Lakini haikuwa rahisi kutayarisha jumba hilo kwa ajili ya mikutano. Kwanza ndugu walivuka Mto Demerara kutoka Mackenzie hadi Wismar kwa mashua ndogo. Ndugu mmoja alibeba katoni la magazeti, mwingine katoni la vitabu, na wa tatu akabeba fomu mbalimbali na masanduku ya michango. Kila kitu kilipaswa kuwa tayari kabla ya mikutano kuanza. Baada ya mikutano, vitu hivyo vilirudishwa.
Mikutano pia ilifanywa katika zile zilizoitwa nyumba za chini. Kwa kuwa Guyana ni nchi ambayo hukumbwa na mafuriko mara kwa mara, nyumba nyingi hujengwa juu ya nguzo za mbao au saruji. Nyumba hizo huwa na nafasi chini ambayo inaweza kutumiwa kwa shughuli nyingine, kama vile mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, nchini Guyana, watu wengi wanaamini kwamba ikiwa dini haina jengo linalofaa la mikutano, basi haina baraka za Mungu.
Isitoshe, mikutano iliyofanywa katika nyumba za chini ilivurugwa mara kwa mara na kuifanya ikose heshima inayostahili. Wakati mmoja, kuku aliyeshtuliwa na mbwa aliruka na kuingia mahali tulipokuwa tukifanyia mikutano na kutua juu ya kichwa cha msichana wa miaka sita. Msichana huyo alipiga mayowe yaliyomshtua kila mtu. Jambo hilo lilifanya ndugu wacheke baada ya mikutano, hata hivyo, liliwakumbusha kwamba walihitaji mahali pazuri pa ibada. Isitoshe, wapya hawakuchochewa kuhudhuria mikutano hiyo ambayo ilifanywa katika Majumba ya Ufalme yaliyokuwa chini ya nyumba.
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme
“Kwa miaka 32 niliyokuwa katika Kutaniko la Charity, tulikodi majumba matano mbalimbali yaliyokuwa chini ya nyumba,” asema Frederick McAlman. “Kwa kuwa tulikuwa chini ya nyumba, tulihitaji kuwa waangalifu nyakati zote ili tuzigongwe vichwa na mbao zilizokuwa juu. Mtoto wa dada mmoja aligongwa kichwa, kwa kuwa dada huyo, ambaye alikuwa amembeba, hakukadiria vizuri urefu wa mbao hiyo. Baadaye alimweleza babake, ambaye hakuwa Shahidi, yale yaliyotokea. Wazazi wake walikata kauli kwamba kutaniko hilo lilihitaji kuwa na mahali pao pa ibada. Mamake alisema atatoa kiwanja, naye babake akasema kwamba atagharimia ujenzi wa jumba hilo, nao wakafanya hivyo. Jumba hilo la Ufalme ambalo limefanyiwa ukarabati mara kadhaa, bado hutumiwa kama kituo cha ibada ya kweli katika eneo hilo. Pia, hutumiwa kama Jumba la Makusanyiko katika mzunguko huo.”
Zamani, ilichukua miezi mingi kujenga Jumba la Ufalme. Hivyo ndivyo ilivyokuwa huko Eccles. Sherlock Pahalan, ambaye wakati huo alikuwa mzee huko Eccles anaeleza: “Tulifanya mikutano yetu katika shule. Tulijua kwamba watu wangeongezeka kama tungekuwa na Jumba la Ufalme. Lakini wahubiri wa Eccles walikuwa wachache na maskini. Hata hivyo, waliazimia kujenga Jumba la Ufalme. Nilitafuta kiwanja kinachofaa katika eneo hilo, lakini sikufanikiwa.
“Wakati huohuo, ndugu wa Georgetown walituazima visanduku viwili vya kutengenezea matofali, nao wakatufundisha jinsi ya kutengeneza matofali ya saruji. Mwanzoni, ilichukua muda wa saa kadhaa kutengeneza matofali 12 tu, lakini baada ya kuzoea tukawa stadi, hasa akina dada. Tatizo lingine lilikuwa kupata saruji kwa kuwa iliuzwa kwa kipimo. Ilinibidi kutuma maombi ili kupata kibali cha kuuziwa saruji ya kiasi fulani. Nilikuwa nikienda kwenye gati asubuhi na mapema na kupiga foleni ili kuhakikisha kwamba tulipata saruji hiyo. Kisha ilinibidi kutafuta lori lililokuwa likienda Eccles, ambalo lilikuwa na nafasi ya kutosha kubebea saruji hiyo. Yehova alitusaidia sikuzote. Lakini bado tulihitaji kiwanja.”
Sherlock anaongeza: “Katika mwaka wa 1972, mimi na Juliet tulienda likizo Kanada. Huko tulimtembelea binamu yangu ambaye si Shahidi. Alitueleza kwamba ana viwanja viwili huko Eccles lakini watu wa jamaa yake hawakuwa wakivitunza vizuri. Hivyo akaniomba nimsaidie. Nilimwambia kwamba ningefurahi kumsaidia, na kwamba nilikuwa nikitafuta kiwanja huko Eccles ili kujenga Jumba la Ufalme. Bila kusita, aliniambia nichague kimoja kati ya viwanja hivyo viwili.
“Wakati wa ujenzi, tuliona uthibitisho zaidi kwamba Mungu alikuwa akitusaidia. Vifaa vingi vya ujenzi havikupatikana kwa urahisi, isipokuwa saruji, kwa hiyo tulitumia vifaa vingine tofauti na vile vilivyokusudiwa mwanzoni na kazi ikasonga mbele. Isitoshe, ni ndugu wachache tu waliokuwa na ustadi uliohitajiwa, na ilitubidi kufanya mipango mingi ili wafanyakazi wa kujitolea waweze kufika mahali pa ujenzi. Nilisafiri mamia ya kilometa kwa gari langu dogo nikiwapeleka na kuwarudisha akina ndugu. Hatimaye, ujenzi wa Jumba letu la Ufalme ulimalizika. Karl Klein wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuliweka wakfu, jambo ambalo tulifurahia sana.”
Majumba ya Ufalme Yaliyojengwa Haraka
Mpaka mwaka wa 1995, zaidi ya nusu ya makutaniko ya Guyana yalikuwa yakikutana katika majengo yaliyokodiwa, kutia ndani nyumba za chini. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ikaanzisha halmashauri ya ujenzi ya kitaifa ili kushughulikia uhitaji huo. Mnamo Oktoba mwaka huohuo, ndugu walimaliza ujenzi wa jumba lao la kwanza ambalo lilijengwa kwa muda mfupi. Jumba hilo lilijengwa katika kijiji cha Mahaicony, karibu na Mto Mahaicony, kilometa 50 hivi mashariki ya Georgetown. Majirani waliposikia kwamba Mashahidi wa Yehova watajenga Jumba la Ufalme katika miisho-juma minne tu, mmoja wao alisema: “Ikiwa mtajenga kibanda cha kuku, ni sawa, lakini hamwezi kujenga nyumba ya mawe kwa muda mfupi kama huo.” Muda si muda mtu huyo alibadili maoni yake.
Katika nchi hiyo ambamo chuki mbaya ya ubaguzi hutokea mara kwa mara, ujenzi wa Majumba ya Ufalme umeonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hufanya kazi kwa umoja wa kweli wa Kikristo, bila kubaguana kijamii au kitaifa. Mwanamke mmoja mzee aliyetazama Jumba la Ufalme likijengwa huko Mahaicony alimwambia mwangalizi mmoja wa mzunguko hivi: “Niliwaona watu kutoka jamii sita wakifanya kazi pamoja!”
Ofisi ya Tawi Yajengwa
Katika mwaka wa 1914, ofisi ya kwanza ya tawi nchini Guyana ilifunguliwa nyumbani kwa Phillips, na haikuhamishwa hadi mwaka 1946. Mwaka huo kulikuwa na wahubiri 91 nchini humo. Mwaka wa 1959, wahubiri walikuwa wameongezeka na kufikia 685, na kazi ikaendelea kupanuka. Kwa hiyo, mnamo Juni 1960, ndugu walinunua kiwanja kwenye barabara ya Brickdam namba 50, Georgetown. Nyumba zilizokuwa kwenye kiwanja hicho zilifanyiwa marekebisho madogo na kutumiwa kama ofisi ya tawi na makao ya wamishonari. Lakini kufikia mwaka wa 1986, majengo hayo yakawa hayatoshi. Kwa hiyo, baada ya kupata kibali cha Baraza Linaloongoza, ofisi mpya ilijengwa kwenye kiwanja hicho. Watumishi wa kimataifa, wakisaidiwa na ndugu wenyeji, walimaliza ujenzi huo mwaka wa 1987.
Kama vile binti za Shalumu, ambao walimsaidia baba yao kujenga upya sehemu fulani ya kuta za Yerusalemu, dada walisaidia sana katika ujenzi huo. (Neh. 3:12) Kwa mfano, dada 120 waliokuwa katika vikundi kumi hivi, walitengeneza matofali 12,000 ya saruji ambayo yalihitajiwa katika ujenzi huo. Walitumia visanduku 16 vya kutengenezea matofali, nao wakamaliza kazi hiyo kwa siku 55. Hiyo haikuwa kazi rahisi hata kidogo! Walihitaji kutumia vipimo sahihi walipochanganya saruji na mchanga ili mchanganyiko ushikamane vizuri na pia usiwe na maji mengi, la sivyo matofali yangebomoka yalipoinuliwa kutoka kwenye visanduku.
Ndugu wenyeji ndio waliokuwa walinzi usiku na mara nyingi walikuja moja kwa moja kutoka kazini. Wengine walifanya kazi pamoja na watumishi wa kimataifa ambao waliwafundisha mbinu mbalimbali za ujenzi. Harrinarine (Indaal) Persaud, mmoja wa ndugu hao, anasema: “Nilipewa kazi ya kuweka mapambo fulani kwenye vizingiti vya dirisha, nami sikuwa nimewahi kufanya kazi hiyo. Nilijitahidi na hatimaye nikafaulu kuyaweka vizuri. Baada ya kuchunguza kazi yangu na kupendezwa nayo, ndugu aliyesimamia ujenzi alisema: ‘Sasa utafanya vivyo hivyo kwenye madirisha yote.’” Leo, ndugu huyo kijana huwafundisha wengine ustadi huo wanapojenga Majumba ya Ufalme.
Kwa kuwa iliwabidi ndugu kuagiza vitu fulani kutoka nje ya nchi, walihitaji msaada wa wakuu wa serikali. Kwa sababu hiyo, maofisa wengi walikuja mahali tulipokuwa tukijenga, kutia ndani Rais Forbes L. Burnham na msafara wake. Wote, akiwemo seremala fulani mwenyeji, walivutiwa na jinsi jengo hilo lilivyojengwa kwa ustadi. Seremala huyo alisema: “Ninyi mnajenga majengo ya hali ya juu sana.” Mnamo Januari 14, 1988, Don Adams, mwakilishi wa Brooklyn ambaye wakati huo alikuwa mwangalizi wa eneo la dunia, alitoa hotuba ya kuweka jengo hilo wakfu.
Mnamo Februari 12, 2001, ujenzi mwingine ulianza, lakini katika eneo lingine. Kwa mara nyingine, kazi hiyo ilifanywa na watumishi wa kimataifa wakisaidiwa na ndugu wenyeji. Ofisi hiyo mpya ya tawi iliwekwa wakfu mnamo Jumamosi, Februari 15, 2003. Hotuba ya kuweka jengo hilo wakfu, ambayo ilitolewa na Richard Kelsey kutoka ofisi ya tawi ya Ujerumani, ilisikilizwa na watu 332.
Wamishonari wengi waliotumikia nchini Guyana zamani walirudi kwa ajili ya tukio hilo, baadhi yao kwa mara ya kwanza tangu waondoke miaka mingi iliyopita! Watu 4,752 kutoka nchi 12, ambao ni zaidi ya mara mbili ya idadi ya wahubiri wa Guyana, walihudhuria mkutano wa pekee Jumapili.
Mipango ya Makusanyiko Yahitaji Hekima
Mara nyingi ndugu hukodi mahali pa kufanyia makusanyiko ya mzunguko na ya makusanyiko ya pekee. Huko mashambani, huenda hata wakajenga mahali pa kukutania. Thomas Markevich, aliyetumikia nchini Guyana kuanzia mwaka wa 1952 hadi mwaka wa 1956 anasema: “Tulifanya kusanyiko letu karibu na Mto Demerara, kilometa 60 kutoka Georgetown. Mashahidi mia mbili hivi kutoka mji huo walitaka kuhudhuria ili kuwaunga mkono ndugu wa eneo hilo. Kwa hiyo tukaamua kujenga Jumba la Kusanyiko la muda kwa kutumia vifaa vilivyopatikana huko. Kwa mfano tulitumia mianzi kutengeneza viti na nguzo, na majani ya migomba kuezeka paa.
“Tulikusanya vifaa hivyo, tukaviweka kwenye behewa dogo la reli, kisha tukalielekeza kwenye mteremko. Lakini behewa hilo lilituponyoka mahali ambapo reli ilijipinda, likapinduka, na kutumbukiza mizigo yote mtoni. Hata hivyo, mkasa huo ulitusaidia, kwa kuwa mizigo ilielea bila shida hadi mahali pa ujenzi! Kusanyiko lilipoanza, ndugu waliotutembelea walifurahi kuungana na mamia ya wanakijiji kwenye kusanyiko hilo la siku tatu.”
Thomas anaongeza: “Baada ya kusanyiko, sote tulihubiri katika eneo fulani la karibu ambalo halikuwa limegawiwa kutaniko lolote. Katika kijiji kimoja tulipanga hotuba ya watu wote itolewe. Wanakijiji wote walikuja kusikiliza hotuba hiyo, kutia ndani tumbili fulani wa kufugwa. Tumbili huyo alisikiliza kwa muda, kisha akaamua kuhama alipokuwa. Aliruka-ruka kidogo na kutua kwenye bega langu. Alitazama huku na huku, kisha akaruka na kurudi kwa mwenyewe. Hakuondoka hapo hadi mwisho wa hotuba, jambo ambalo liliniondolea wasiwasi!”
Makusanyiko
Mapema katika miaka ya 1900, makusanyiko makubwa yalifanywa wakati wa ziara ya wawakilishi wa pekee wa makao makuu ya ulimwengu, kama vile Ndugu Coward na Young. Katika mwaka wa 1954, Nathan Knorr na Milton Henschel, walikuja Guyana kuhudhuria kusanyiko kuhusu jamii mpya (New World Society), ambalo lilihudhuriwa na watu 2,737.
Miaka mingi baadaye, katika mwaka wa 1999, wajumbe 7,100 walihudhuria makusanyiko mawili nchini Guyana katika mji wa Georgetown na wa Berbice. Ndugu walilazimika kufanya mabadiliko fulani makubwa ya dakika za mwisho kuhusiana na kusanyiko la Georgetown, jambo lililowatatiza sana. Ofisi ya tawi inaandika: “Mchezaji maarufu wa sinema alifika kutoka India, akiandamana na kikundi chake cha wacheza-dansi. Wasimamizi wa uwanja walikataa kuahirisha onyesha hilo, ingawa sisi ndio tuliokuwa wa kwanza kuomba kutumia uwanja huo.”
“Bila kukawia, tuliamua kutumia uwanja wa kriketi na kuyajulisha makutaniko mara moja. Kusanyiko lilipaswa kuanza baada ya siku nane tu! Lakini bado kulikuwa na matatizo mengine. Katika eneo la Karibea, mchezo wa kriketi unaheshimiwa sana na uwanja wa kriketi huonwa kuwa eneo takatifu. Kwa hiyo, wasimamizi hawakuturuhusu kukanyaga nyasi za uwanja huo. Lakini drama ingefanywaje? Na tungejenga jukwaa letu wapi?
“Licha ya hayo, tuliendelea na mipango yetu, tukiwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia. Naye alitusaidia! Tuliruhusiwa kutumia sehemu iliyokuwa na nyasi, mradi tu tujenge jukwaa na kijia cha juu ili tusikanyage nyasi. Ili kumaliza ujenzi huo, sote tulifanya kazi kwa bidii usiku kucha. Hali ya hewa nayo haikuwa nzuri, kwa kuwa mvua ilinyesha karibu wakati wote. Licha ya matatizo hayo yote, kusanyiko lilichelewa kuanza kwa dakika chache tu.
“Kusanyiko liliendelea vizuri na hali ya hewa haikutusumbua isipokuwa siku ya mwisho, Jumapili. Mvua ilikuwa inanyesha tulipoamka. Muda si muda, maji yalijaa uwanjani, yakafika sentimeta tano chini ya kile kijia na jukwaa. Mvua hiyo iliacha kunyesha muda mfupi tu kabla ya programu kuanza. Pia, nyaya za umeme hazikuwa zimewekwa chini, bali zilikuwa zimeunganishwa upande wa chini wa mbao. Hivyo, lilikuwa jambo zuri sana kwamba tulilazimika kujenga jukwaa na kijia cha juu!”
Wahudhuriaji wote 6,088 waliifurahia drama kwa kuwa ilipoanza, jua lilikuwa likiangaza. Majuma mawili baadaye, watu 1,038 walihudhuria kusanyiko la pili huko Berbice. Watu 7,126 walihudhuria makusanyiko mwaka huo. Hilo lilikuwa hudhurio kubwa zaidi likilinganishwa na hudhurio la miaka iliyotangulia. Hivi karibuni, hudhurio limekaribia watu 10,000.
Matarajio Mazuri ya Wakati Ujao
Katika unabii wake, Ezekieli aliona hekalu la Yehova lililorudishwa katika hali ya utukufu. Mto ulitiririka kutoka kwenye hekalu hilo, nao uliendelea kupanuka na kuongezeka kina hadi ‘ukubwa wake ukawa mara mbili.’ Mto huo ulileta uhai kwenye Bahari ya Chumvi isiyo na uhai.—Eze. 47:1-12.
Ibada safi imesonga mbele tangu mwaka wa 1919 na watu wa Mungu wameona unabii huo ukitimizwa. Siku hizi, maandalizi mengi ya kiroho yaliyo kama mto, yaani, Biblia, vifaa vya kujifunzia Biblia, mikutano, na makusanyiko, huzima kiu ya kiroho ya mamilioni ulimwenguni.
Mashahidi wa Yehova nchini Guyana huliona kuwa pendeleo kushiriki katika utimizo wa unabii huo. Isitoshe, wataendelea kutumia mito kwa njia halisi kabisa, wanapowapelekea chakula cha kiroho wote walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele,” hata wawe wanaishi wapi katika Nchi hii ya Maji Mengi.—Mdo. 13:48.
[Maelezo ya Chini]
a Guiana ya Uingereza ilipopata uhuru Mei 1966, jina lake lilibadilishwa kuwa Guyana. Tutatumia jina hilo inapofaa kulingana na muktadha.
[Sanduku katika ukurasa wa 140]
Maelezo Mafupi Kuhusu Guyana
Nchi: Eneo la pwani, ambalo sehemu yake kubwa iko chini ya usawa wa bahari, lina udongo wa kitope ulioletwa na mito. Eneo hilo limekingwa kwa kuta kubwa zenye urefu wa kilometa 230. Asilimia 80 hivi ya nchi hii ni misitu, kutia ndani nyanda za juu za bara ambapo mito mingi ya Guyana inaanzia.
Watu: Karibu nusu ya watu wa nchi hii ni Wahindi wa Mashariki, zaidi ya asilimia 40 ni Waafrika weusi au machotara, na asilimia 5 hivi ni Wahindi wenyeji. Asilimia 40 hivi hujidai kuwa Wakristo, asilimia 34 ni Wahindu, na asilimia 9 ni Waislamu.
Lugha: Kiingereza ndiyo lugha rasmi, lakini lugha ya Kikrioli inatumiwa kotekote nchini.
Kazi: Asilimia 30 hivi ya watu ni wakulima. Wengine hufanya kazi ya uvuvi, utunzaji wa misitu, na uchimbaji wa migodi.
Chakula: Mazao yanayopandwa sana ni mchele, kakao, matunda ya jamii ya machungwa, nazi, kahawa, mahindi, mhogo, miwa, na matunda na mboga nyinginezo za nchi zenye joto. Wanyama wanaofugwa kwa ajili ya chakula ni ng’ombe, nguruwe, kuku, na kondoo. Vyakula vikuu vinavyotoka baharini ni samaki na uduvi.
Hali ya hewa: Hali ya hewa ya Guyana ni yenye joto na haibadiliki sana. Eneo la pwani hupata sentimeta 150-200 za mvua kila mwaka. Ingawa Guyana iko karibu na ikweta, hakuna joto kali kwa sababu ya pepo ambazo huvuma daima kutoka Bahari ya Atlantiki.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 143-145]
Hakuna Mtu Aliyeweza “Kufunga” Kinywa Chake
Malcolm Hall
Alizaliwa: 1890
Alibatizwa: 1915
Maisha yake: Alikuwa mwenyeji wa kisiwa cha Leguan na alikuwa kati ya wahubiri wa kwanza wa habari njema katika eneo hilo, na alishughulikia kikundi kilichoanzishwa huko.
Imesimuliwa na Yvonne Hall, mjukuu wa kaka yake.
Siku moja ofisa wa uchaguzi alimwuliza ndugu ya babu yangu hivi: “Je, ni kweli kwamba hupigi kura? Ikiwa ndivyo, tutakufunga na kuchukua Biblia yako.” Yeye alimjibu hivi, huku akimkazia macho: “Lakini utakifanyaje kinywa changu? Je, unaweza kukifunga kisiseme kweli ambazo viongozi wenu wa dini wameficha kwa muda mrefu?” Ofisa huyo aliweza tu kusema hivi: “Nitashughulikia mambo yako baadaye.”
Ndugu huyo wa babu alibatizwa mwaka wa 1915, na alikuwa mmoja wa wahubiri wa Ufalme wa kwanza kabisa nchini Guyana. Ndugu mmoja alisema kwamba “aliipigania kweli kabisa.” Alisikia kuhusu kweli ya Ufalme alipokuwa akiishi na kufanya kazi mjini Georgetown. Yeye aliitambua kweli baada ya kusikia hotuba moja tu kwenye jengo la Somerset House. Alienda nyumbani na kuchunguza katika Biblia yake maandiko yote aliyosikia.
Baadaye, alirudi nyumbani huko Leguan na kuanza kuwahubiria wengine. Miongoni mwa watu wa kwanza kukubali ujumbe wa Ufalme walikuwa dada zake wawili na baadhi ya wapwa wake wakubwa. Hao ndio waliokuwa watu wa kwanza kufanya mikutano katika nyumba ya ndugu ya Babu.
Mwanzoni, makasisi walikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya wenyeji, na ilikuwa vigumu sana kuwashawishi watu hao wakubali habari njema. Makasisi walikuwa wakisema kwamba ndugu ya babu yangu alikuwa “mwenda-wazimu, mwenye kichaa cha Biblia.” Lakini hiyo haikupunguza bidii yake. Kwa mfano, kila Jumapili asubuhi Babu aliweka kinanda chake nje ya nyumba yake ili kutoa hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Mara nyingi watu walisimama barabarani na kusikiliza.
Baada ya muda, watu kadhaa walianza kuthamini hotuba hizo. Jambo hilo lilidhihirika wakati wa Ukumbusho, ambapo chumba cha juu cha ndugu ya babu yangu kilijaa watu. Yeye ndiye aliyekuwa mwenye-kiti, msemaji, na ndiye tu aliyekula mkate na kunywa divai kwenye Ukumbusho. Mmoja wa wanafunzi wake wa Biblia, Leroy Denbow, alianza utumishi wa upainia na hata alikuwa mwangalizi wa mzunguko kwa muda fulani.
Baada ya kustaafu kazi ya ofisa wa hesabu katika meli iliyosafiri kwenye Mto Essequibo, ndugu ya babu yangu alianza utumishi wa upainia, naye alihubiri kwenye kisiwa cha Leguan na kisiwa jirani cha Wakenaam. Kwa kawaida aliamka saa 10:30 alfajiri ili kukamua ng’ombe na kushughulikia nguruwe wake. Ilipofika saa 1:30 asubuhi, alioga, akasoma andiko la siku na sehemu fulani katika Biblia, kisha akala kiamsha-kinywa na kujitayarisha kwenda kuhubiri. Bado ninakumbuka jinsi alivyokuwa akiijaza baiskeli yake pumzi kabla ya kwenda. Alikuwa akisafiri angalau umbali wa kilometa 20 kila siku.
Ndugu ya babu yangu aliyekuwa na tumaini la kwenda mbinguni alikufa Novemba 2, 1985, baada ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka ipatayo 70. Na wakati huo wote, hakuna aliyeweza “kufunga” kinywa chake. Leo kuna kutaniko katika kisiwa cha Leguan na Wakenaam.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 155-158]
Maisha Yangu Yalibadilika Nilipojibiwa Maswali Niliyokuwa Nayo Tangu Utotoni
Albert Small
Alizaliwa: 1921
Alibatizwa: 1949
Maisha yake: Alianza utumishi wa upainia mwaka wa 1953. Alihudhuria Shule ya Gileadi pamoja na mkewe Sheila mwaka wa 1958, nao wakatumwa Guyana.
“Mungu ndiye aliyekuumba.” Hivyo ndivyo nilivyoambiwa sikuzote nilipokuwa mvulana. Kwa hiyo Mama aliponiambia kwamba mimi ndiye niliyekuwa mbaya kati ya watoto wake wanne, niliwaza kwamba Mungu alikuwa amewaumba watoto watatu wazuri na mmoja mbaya.
Nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, nilimwuliza mwalimu wa shule ya Jumapili, “Ni nani aliyemwumba Mungu?” Hakunijibu. Hata hivyo, nilipokuwa mtu mzima nilijiunga na Kanisa la Kipresibiteri kama vile watu wengi walivyozoea kufanya nyakati hizo. Hata hivyo, mengi ya maswali yangu hayakujibiwa. Kwa mfano, tulipokuwa kanisani tuliimba wimbo uliosema, kwa sehemu: ‘Mtu tajiri katika jumba la kifahari, naye maskini kwenye lango lake. Mungu alimwumba mmoja wa hali ya juu na mwingine wa hali ya chini; alipanga hali yao.’ Nilijiuliza, ‘Je, kweli Mungu “alipanga hali yao”?’ Pindi moja nilimwuliza kasisi, “Ikiwa Mungu alimwumba Adamu na Hawa, jamii mbalimbali zilitoka wapi?” Alinijibu kwa ufupi kwamba masimulizi ya Mwanzo ni hadithi tu.
Kisha, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, tulitiwa moyo tuwaombee askari wa Uingereza. Hatimaye, jambo hilo lilinisadikisha kwamba mafundisho ya kanisa langu yalipingana na mambo niliyosoma katika Biblia. Lakini, nilijiuliza, ‘Niende wapi?’ Hivyo nikabaki katika kanisa hilo. Nilimwoa Sheila nilipokuwa na umri wa miaka 24.
Siku moja nilikuwa nimerudi tu nyumbani kutoka kanisani wakati ambapo Shahidi wa Yehova alitutembelea. Tulikuwa tukiwaita Mashahidi lile kanisa ambalo halifundishi kuhusu moto wa mateso, nami sikutaka kuwasikiliza. Walifanya mikutano yao kwenye nyumba za watu na hawakuvalia mavazi yoyote ya makasisi. Isitoshe, mambo fulani yaliyokuwa yametukia maishani mwangu, kutia ndani kumwoa mwanamke mzuri, yalinifanya nikate kauli kwamba Mungu ananijali.
Wakati Shahidi huyo aliyeitwa Nesib Robinson alipojitambulisha, nilikuwa nikitengeneza gurudumu la baiskeli yangu. Nilimwambia: “Gurudumu hili limetoboka. Ikiwa wewe ni Mkristo, nisaidie kulitengeneza.” Kisha kwa ghafula nikaingia ndani ya nyumba. Juma lililofuata, nilipokuwa nikitoka kwenda kanisani nikiwa na Biblia yangu mkononi, nilimwona Nesib akipanda ngazi kuelekea kwenye nyumba yetu. Nilimwambia: “Sipendezwi na dini yako, mke wangu yuko ndani. Ongea naye.” Kisha nikaenda zangu.
Nilijuta kwamba nilisema hivyo, kwa kuwa nilipokuwa kanisani, badala ya kumsikiliza pasta, nilikuwa nikiwaza, ‘Bw. Robinson akiendelea kuongea na mke wangu, huenda asiwe na wakati wa kutayarisha supu yetu ya pekee ya Jumapili.’ Kumbe, sikuhitaji kuwa na wasiwasi kwa kuwa nilipofika nyumbani, supu ilikuwa tayari. Nilitaka kujua yaliyotokea, kwa hiyo nikamwuliza Sheila hivi: “Je, uliongea na yule jamaa?” Akajibu: “Ndiyo. Aliketi na kuhubiri, huku nikipika.”
Muda mfupi baadaye, Sheila alikubali funzo la Biblia. Pia alijifungua mtoto wetu wa kwanza ambaye alikuwa amekufa. Nilimwuliza Bw. Robinson kwa nini mambo kama hayo hutokea. Alinijibu kwamba halikuwa kosa la Mungu bali ni matokeo ya kutotii kwa Adamu na Hawa na hali ya kutokamilika tuliyorithi kutoka kwao. Jibu hilo liliniridhisha.
Mara nyingi Nesib alinitembelea kwenye karakana yangu ya kutengenezea vitu vya mbao. Mazungumzo yetu yalihusu kazi yangu, lakini kila mara alitaja jambo fulani kutoka katika Biblia kabla hajaondoka. Baada ya muda, tulikuwa tukizungumzia Neno la Mungu zaidi kuliko useremala. Siku moja niliamua kumwuliza swali moja au mawili ambayo yalikuwa yamenisumbua katika maisha yangu yote. Kwa kuwa wahudumu “rasmi” wa kanisa walikuwa wameshindwa kunijibu maswali hayo nilifikiri hata yeye atashindwa.
Nilimwuliza Nesib swali la kwanza, “Ni nani aliyemwumba Mungu?” na kusisitiza anijibu kwa kutumia Biblia. Nesib alisoma Zaburi 90:2 ambayo inasema hivi kulingana na Union Version: “Kabla haijazaliwa milima, wala hujaiumba dunia, na tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” Alinitazama na kuniuliza: “Unaona vile Biblia inavyosema? Hakuna yeyote aliyemwumba Mungu, amekuwapo sikuzote.” Jibu hilo lililo wazi lilinistaajabisha na kufanya nimwulize maswali yote niliyokuwa nimeyafungia moyoni kwa miaka mingi. Majibu ya Kimaandiko ya Nesib, hasa kuhusu kusudi la Mungu la kuifanya dunia iwe paradiso, yaliniletea shangwe kubwa sana.
Nilivutiwa sana nilipoenda kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza. Kwa nini? Kwa sababu nilishangaa kuwaona wasikilizaji wakitoa maelezo kwenye mkutano, jambo ambalo sikuona kamwe kanisani. Mke wangu, ambaye hakuwa ameanza kuhudhuria mikutano, hakuwako wakati huo. Nilipomweleza kuhusu mkutano huo, alisema: “Twende pamoja.” Na tumeendelea kwenda kwa miaka 55 sasa!
Mimi na Sheila tulibatizwa katika Bahari ya Atlantiki mwaka wa 1949. Katika mwaka wa 1953, nilianza utumishi wa upainia. Miaka miwili baadaye, Sheila alijiunga nami katika kazi hiyo ya upainia ambayo nimeifanya kwa miaka 50. Katika mwaka wa 1958 tulialikwa kuhudhuria darasa la 31 la Shule ya Gileadi na kutumwa Guyana. Nilifanya kazi ya mwangalizi anayesafiri kwa miaka 23 nikiwa na mke wangu, kisha tukawa mapainia wa pekee, na bado tunaendelea na utumishi huo. Naam, ninamshukuru Yehova kwa kunijibu maswali niliyokuwa nayo tangu utotoni na pia kwa kuniruhusu mimi na mke wangu kumtumikia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 163-166]
“Mimi Hapa! Nitume Mimi”
Joycelyn Ramalho (zamani aliitwa Roach)
Kuzaliwa: 1927
Kubatizwa: 1944
Maisha yake: Sasa yeye ni mjane. Utumishi wake wa wakati wote wa miaka 54 unatia ndani muda alioandamana na mume wake alipokuwa mwangalizi anayesafiri.
Nilizaliwa katika kisiwa cha Nevis huko Karibea. Mama yangu alikuwa mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, mfuasi wa kanisa la Methodisti, na mwuguzi. Alinifundisha kumwamini Mungu. Kwa sababu ya kazi yake, tulihamia kijiji kidogo kisiwani. Jumapili iliyofuata, tulienda kwenye kanisa la Methodisti na kuketi kwenye benchi moja. Lakini baada ya dakika chache, tuliambiwa kwamba “wenye” benchi hiyo walikuwa wamefika, kwa hiyo tulipaswa tuketi kwingine. Hata ingawa kwa fadhili mtu mmoja alituruhusu tuketi kwenye benchi “yake,” Mama aliamua kwamba hatutarudi kamwe kwenye kanisa hilo. Badala yake tulijiunga na Kanisa la Anglikana.
Mapema katika miaka ya 1940, Mama alipokuwa akimtembelea rafiki yake, alikutana na Shahidi kutoka St. Kitts ambaye alimpa vichapo kadhaa. Kwa kuwa Mama alipenda kusoma, alisoma vichapo hivyo kwa hamu na kuitambua kweli. Aliolewa muda mfupi baadaye, na sote tukahamia Trinidad. Wakati huo vichapo vyetu vilikuwa vimepigwa marufuku huko, lakini tuliweza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Muda si muda, Mama, na vilevile baba yangu wa kambo, James Hanley, waliacha Kanisa la Anglikana nao wakaanza kumtumikia Yehova.
Nilipokuwa Trinidad, nilikutana na dada kijana aitwaye Rose Cuffie. Sikujua kwamba miaka 11 baadaye, Rose angekuwa mmoja kati ya wamishonari ambao ningeshirikiana nao katika utumishi. Wakati huo, tamaa yangu ya kumtumikia Yehova iliendelea kuongezeka. Ningali ninakumbuka mara ya kwanza nilipoenda kuhubiri peke yangu. Kwenye nyumba ya kwanza, mwenye nyumba alitoka nje, na ghafula nikashindwa kuongea. Sijui nilisimama hapo kwa muda gani, lakini nilifungua Biblia, nikasoma Danieli 2:44, na kuondoka mara moja!
Nilianza utumishi wa upainia mwaka wa 1950, na baada ya miaka miwili hivi, nilifurahi sana kupokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 21 la Shule ya Gileadi. Wanafunzi watatu katika darasa letu walitumwa Guyana: mimi, Florence Thom, aliyetoka Guyana, na Lindor Loreilhe, ambaye niliishi naye katika chumba kimoja. Tulifika Novemba 1953 na tukatumwa Skeldon, mji ulio umbali wa kilometa 180 hivi kutoka Georgetown, karibu na mlango wa Mto Courantyne. Ndugu katika kikundi hicho cha mbali walikuwa wametungoja kwa hamu.
Watu wengi katika eneo la Skeldon walikuwa Wahindi wa Mashariki, nao walikuwa ama Wahindu ama Waislamu. Wengi hawakuwa na elimu, kwa hiyo tulipowahubiria, mara nyingi walisema: “Dada, eleza mambo kwa njia rahisi.” Mwanzoni, watu 20 hadi 30 walikuwa wakihudhuria mikutano, lakini idadi hiyo ikapungua wakati wale ambao hawakupendezwa kikweli walipoacha kuja.
Mwanamke mmoja alifanya maendeleo naye akataka kuwa mhubiri. Lakini nilipofika nyumbani kwake wakati tuliokuwa tumepanga, mwanaye mwenye umri wa miaka 14 ndiye aliyekuwa tayari na mwenye hamu ya kwenda pamoja nami. Mama yake alisema: “Bi. Roach, unaweza kwenda na Frederick badala yangu.” Baadaye tuligundua kwamba baba ya mwanamke huyo, ambaye ni Mwanglikana sugu, alimpinga vikali. Hata hivyo, mwanaye, Frederick McAlman, alifanya maendeleo makubwa ya kiroho na baadaye akahudhuria Shule ya Gileadi.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 170.
Baadaye nilitumwa tena Henrietta, ambako kulikuwa na ndugu mmoja tu. Eneo hilo lilishughulikiwa na Kutaniko la Charity. Painia mwenzangu mpya alikuwa Rose Cuffie, niliyetangulia kumtaja. Mimi na Rose tulihubiri kwa siku nne kila juma huko Henrietta, na kila Ijumaa tuliondoka mapema na kusafiri kwa baiskeli kilometa zaidi ya 30 kwenye barabara za vumbi hadi Charity, ambako tulihudhuria mikutano. Tulibeba vyakula, shuka, mablanketi, na vyandalua vya mbu.
Tuliwahubiria watu walioishi karibu na njia, kisha tukaenda kumtia moyo dada mmoja asiyetenda, na wahubiri kadhaa walioishi mbali na kutaniko. Tulikuwa tukijifunza gazeti la Mnara wa Mlinzi pamoja nao. Siku ya Jumapili, baada ya kurudi Henrietta, tulikuwa tukijifunza Mnara wa Mlinzi pamoja na wanafunzi wetu wa Biblia. Hatukuwa na matatizo yoyote makubwa, ila tu mambo madogo kama vile kulowa maji wakati wa mvua au gurudumu kutoboka.
Shangwe yetu haikupungua. Hata mwanamke mmoja alituambia hivi siku moja: “Sikuzote nyinyi ni wenye furaha; ni kama hamsumbuliwi na chochote.” Yehova aliongeza furaha yetu kwa kutupa huduma yenye matokeo. Hata yule dada asiyetenda ambaye tulimtembelea alianza kumtumikia Yehova tena. Sasa miaka 50 hivi imepita na angali mwaminifu.
Mnamo Novemba 10, 1959, niliolewa na painia aitwaye Immanuel Ramalho. Tulitumikia pamoja huko Suddie, kilometa 23 kusini ya Henrietta. Nikiwa huko, nilipata mimba lakini ikaharibika. Kuwa na shughuli nyingi katika huduma kulinisaidia kupambana na hali hiyo. Baadaye tulipata watoto wawili. Hata hivyo, tuliendelea na utumishi wa upainia.
Mnamo mwaka wa 1995, Immanuel alikufa. Tulimtumikia Yehova pamoja katika maeneo mbalimbali. Tulikuwa tumeona vikundi vidogo-vidogo vikikua na kuwa makutaniko yenye maendeleo, yenye wazee, watumishi wa huduma, na hata Majumba ya Ufalme! Pia, kwa miaka kumi, nilifurahia kuandamana na mume wangu alipokuwa mwangalizi anayesafiri. Ijapokuwa ninamkosa Immanuel sana, ninafarijiwa sana na utegemezo wenye upendo ninaopata kutoka kwa Yehova na kutaniko.
Nabii Isaya alijibu mwaliko wa kumtumikia Yehova kwa maneno haya: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Mimi na mume wangu tulijaribu sana kuiga mtazamo mzuri wa nabii huyo. Ni kweli kwamba, kama vile Isaya, tulivumilia magumu na hata nyakati zenye kuvunja moyo. Lakini shangwe tuliyopata ilipita magumu hayo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 170-173]
Nilitumwa Nchi ya Nyumbani Baada ya Shule ya Gileadi
Frederick McAlman
Alizaliwa: 1942
Alibatizwa: 1958
Maisha yake: Baada ya kuhudhuria shule ya Gileadi, alitumwa kwao Guyana. Sasa yeye na mkewe, Marshalind, wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida.
Nilipokuwa na umri wa miaka 12, mmishonari anayeitwa Joycelyn Roach (sasa anaitwa Ramalho) alianza kujifunza Biblia pamoja na mama yangu. Nilikuwa nikijiunga na mazungumzo yao. Mama aliacha kujifunza, lakini mimi niliendelea na kuanza kuhudhuria -mikutano. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, Dada Roach na wamishonari wenzake, Rose Cuffie na Lindor Loreilhe, walinibeba kwa baiskeli zao kwenda kuhubiri. Roho yao ya umishonari ilinichochea zaidi kuliko nilivyotambua wakati huo.
Nilipoanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova, nilikuwa Mwanglikana na nilikuwa nikijitayarisha kupokea kipaimara. Pindi moja, kasisi alijaribu kufafanua Utatu “mtakatifu.” Baada ya kumsikiliza kwa muda, nilieleza maoni yangu, nikisema kwamba sikuamini kwamba fundisho hilo liko katika Biblia. Alinijibu kwa hasira: “Ninajua kwamba unasoma vitabu fulani, na vitabu hivyo ni hatari. Usivisome. Unapaswa kuamini Utatu.” Tangu wakati huo, sikurudi tena katika kanisa la Anglikana lakini niliendelea kujifunza na Mashahidi. Nilibatizwa mwaka wa 1958.
Mnamo Septemba 1963, nilipokea barua kutoka kwenye ofisi ya tawi iliyonialika kuwa painia wa pekee. Nilikubali mwaliko huo. Mgawo wangu mpya ulikuwa katika Kutaniko la Fyrish karibu na Mto Courantyne, na painia mwenzangu alikuwa Walter McBean. Tulitumikia pamoja kwa mwaka mmoja na kuhubiri pande zote za mto huo. Hiyo ilitutayarisha kwa ajili ya mgawo wetu uliofuata—Kutaniko la Paradise, lililokuwa na wahubiri kumi tulipofika mwaka wa 1964. Tulifanya upainia huko kwa miaka minne na idadi ya wahubiri iliongezeka kufikia 25.
Katika mwaka wa 1969, nilialikwa kuhudhuria darasa la 48 la Gileadi. Mwaka huohuo nilifurahi sana kuwa mgeni wa familia ya Betheli ya Brooklyn ili niweze kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” la mwaka wa 1969. Tulifurahi kama nini kukutana na ndugu na dada waaminifu! Sitasahau kamwe wakati Frederick W. Franz, ndugu wa Baraza Linaloongoza, alipotualika chumbani mwake. Alikuwa na vitabu vingi sana hivi kwamba sikujua kitanda chake kilikuwa wapi! Mwingine aliyependa kujifunza Neno la Mungu ni Ulysses Glass, mmoja wa walimu wetu wa Gileadi. Bado nakumbuka maneno yake: “Usahihi, ufupi, na uwazi ni muhimu ili uandishi na ufundishaji wetu uwe mzuri.”
Bila shaka nilivunjika moyo niliposikia kwamba nitatumwa Guyana. Niliiona Guyana kuwa nyumbani, bali si mgawo wa kigeni. Hata hivyo, Ndugu Glass aliniita kando na kwa fadhili akanisaidia kubadili maoni yangu. Alinikumbusha kwamba kuhudhuria shule ya Gileadi ni pendeleo kubwa sana na kwamba labda ningetumwa sehemu ya Guyana ambayo ni mpya kwangu. Ndivyo ilivyokuwa, kwa kuwa nilitumwa Kutaniko la Charity karibu na Mto Pomeroon. Wakati huo kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri watano tu.
Mimi na mwenzangu Albert Talbot hatukuwa na uzoefu wa kusafiri kwenye mito, kwa hiyo ilitubidi kujifunza jinsi ya kuendesha mashua yetu. Huenda ukaona jambo hilo kuwa rahisi, lakini nakuhakikishia kuwa sivyo ilivyo. Ukiyapuuza mawimbi na upepo, utakaa mahali palepale tu au uzunguke-zunguke bila kwenda popote. Tunashukuru kwamba tulipata msaada kutoka kwa dada mmoja mwenyeji ambaye alikuwa mwalimu stadi.
Kwa miaka kumi tulisafiri kwa mashua tukitumia nguvu ya mikono yetu kupiga makasia. Kisha mwenyeji mmoja akataka kuuzia kutaniko injini ya kuendesha mashua, lakini hatukuwa na pesa za kutosha. Kwa hiyo, unaweza kuwazia jinsi tulivyofurahi tulipopokea hundi kutoka katika ofisi ya tawi ili kununua injini hiyo. Yaonekana kwamba makutaniko kadhaa yalikuwa yamesikia kuhusu uhitaji wetu, nayo yakataka kutusaidia. Baada ya muda fulani, tulinunua mashua nyingine ambazo ziliitwa Kingdom Proclaimer. Jina hilo lilifuatwa na nambari ya kutambulisha kila mashua.
Baada ya kuhubiri pamoja na mapainia tofauti-tofauti, nilikutana na yule ambaye angekuwa mwenzi wangu wa maisha, Marshalind Johnson, painia wa pekee aliyetumwa katika Kutaniko la Mackenzie. Babake Eustace Johnson, ambaye alikuwa amekufa, alijulikana sana Guyana, naye alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko kwa miaka kumi hivi kabla ya kifo chake. Sasa mimi na Marshalind ni mapainia wa kawaida na tuna jumla ya miaka 72 ya utumishi wa wakati wote, kutia ndani miaka 55 tuliyotumikia tukiwa mapainia wa pekee. Katika kipindi hicho, tulilea watoto sita.
Yehova pia amebariki jitihada zetu katika huduma. Kwa mfano, mapema miaka ya 1970 tulipokuwa tukihubiri karibu na Mto Pomeroon, tulikutana na fundi wa nguo ambaye alikubali kujifunza Biblia. Alikuwa mwanafunzi mzuri. Tulimtia moyo ajifunze majina ya vitabu vya Biblia. Fundi huyo aliyakariri yote kwa juma moja na pia aliweza kutaja kurasa zake! Yeye, mke wake, na watoto saba kati ya tisa ni Mashahidi. Mimi na yeye tunatumikia tukiwa wazee katika kutaniko la Charity. Kwa kweli singepata baraka kama hizi iwapo wale wamishonari wa mapema wenye bidii hawangeniwekea mfano mzuri.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 176-177]
Nilijifunza Neno la Mungu Kupitia Barua
Monica Fitzallen
Alizaliwa: 1931
Alibatizwa: 1974
Maisha Yake: Kwa kuwa aliishi mbali, Monica alijifunza Biblia kupitia barua kwa miaka miwili na aliwahubiria sana Wahindi wenyeji. Yeye hukariri maandiko anayotumia katika huduma kwa kuwa sasa yeye ni kipofu.
Ninaishi katika eneo lililotengewa Wahindi wenyeji linaloitwa Waramuri, ambalo liko karibu na Mto Moruka, katika wilaya ya kaskazini-magharibi mwa Guyana. Nilipopata kweli mapema katika miaka ya 1970, kutaniko la karibu lilikuwa Charity, karibu na Mto Pomeroon. Ili kufika huko, nilisafiri kwa muda wa saa 12 kwa mtumbwi.
Nilikutana na Mashahidi wa Yehova nilipokuwa nikinunua vitu huko Charity. Frederick McAlman alinipa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Niliyakubali, nikayapeleka nyumbani, na kuyaweka kwenye sanduku, ambamo yalikaa kwa miaka miwili. Kisha nikawa mgonjwa na sikuweza kutoka kitandani kwa muda fulani, nami nikashuka moyo sana. Ndipo nilipoyakumbuka magazeti hayo. Niliyasoma na mara moja nikatambua kweli.
Wakati huo, mume wangu Eugene, alianza kutafuta kazi naye akaamua kusafiri kuelekea upande wa chini wa mto hadi Charity. Nilikuwa nimeanza kupata nafuu, hivyo nikaenda naye. Hata hivyo, sababu yangu kuu ya kwenda huko ilikuwa kuwatafuta Mashahidi wa Yehova. Sikuhitaji kuwatafuta sana, kwa kuwa mwanamke mmoja Shahidi alikuja nyumbani kwetu. Nilimwuliza, “Je, wewe ni mmoja wa watu wa Mnara wa Mlinzi?” Alipojibu ndiyo, nilimwuliza kumhusu mtu niliyekuwa nimekutana naye sokoni miaka miwili iliyopita. Alienda kumtafuta Frederick McAlman mara moja, ambaye alikuwa akihubiri na wahubiri fulani katika eneo lililokuwa karibu.
Wote wawili waliporudi, Ndugu McAlman alinionyesha jinsi ya kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Nilikubali kujifunza. Kwa kuwa mimi na Eugene tulihitaji kurudi nyumbani, nilijifunza kupitia barua. Nilijifunza vitabu viwili kwa njia hiyo—kitabu Kweli na “Mambo Mawili Yasiyobadilika Asiyoweza Mungu Kusema Uongo.” Nilipokuwa nikijifunza kitabu Kweli, niliacha Kanisa la Anglikana na kuwa mhubiri. Kasisi aliniandikia hivi: “Usiwasikilize Mashahidi wa Yehova. Wao huielewa Biblia kijuujuu tu. Nitakuja kuzungumzia jambo hilo nawe.” Lakini hakuja kamwe.
Kwa kuwa hakukuwa na wahubiri wengine katika eneo hilo, niliwaeleza majirani wangu mambo mapya niliyojifunza. Pia nilimhubiria mume wangu, ambaye ninafurahi kusema kwamba alibatizwa mwaka mmoja baada yangu. Leo Eugene ni mmoja kati ya wahubiri wetu 14.
Katika miaka ya karibuni, magonjwa ya macho yamenifanya niwe kipofu, kwa hiyo sasa mimi hukariri maandiko ninayotumia katika huduma. Hata hivyo, namshukuru Yehova kwa kuwa bado ninaweza kumtumikia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 181-183]
Yehova Amenipa ‘Maombi ya Moyo Wangu’
Ruby Smith
Alizaliwa: 1959
Alibatizwa: 1978
Maisha yake: Yeye ni Mkaribu na alikuwa mstari wa mbele katika kuhubiri habari njema huko Baramita, eneo la Wahindi wenyeji nchini Guyana.
Niliwasiliana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza mwaka wa 1975. Nilikuwa na umri wa miaka 16. Nyanya yangu alipokea trakti kutoka kwa mwanaye wa kambo na kuniomba nimtafsirie, kwa kuwa hakuweza kusoma Kiingereza. Nilishangazwa na ahadi za Biblia zilizozungumziwa katika trakti hiyo, hivyo nikajaza sehemu ya nyuma na kuituma kwenye ofisi ya tawi. Vichapo nilivyoomba vilipofika, nilivisoma na kuanza kuwaeleza wengine juu ya kweli za Kimaandiko nilizojifunza. Nilianza na nyanya yangu na shangazi yangu. Kwa kusikitisha, baba yangu hakupenda utendaji wangu.
Muda si muda, nyanya yangu na shangazi yangu wakaanza kuhubiri. Baadhi ya wanakijiji walikuja nyumbani kwetu ili kujifunza Biblia. Kadiri nilivyosoma, ndivyo nilivyotambua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko maishani ili kumpendeza Yehova. Hiyo ilitia ndani kukiri kwa baba yangu kwamba nilikuwa nimeiba kitu fulani katika karakana yake na kupatana na ndugu yangu. Baada ya kusali sana, nilifaulu kufanya yote hayo.
Wakati huohuo, ofisi ya tawi ilipanga ili painia wa pekee, Sheik Bakhsh, atembelee eneo letu. Hata hivyo, Ndugu Bakhsh hakuweza kukaa kwa muda mrefu, kwa hiyo yeye na ndugu mwingine, Eustace Smith, ambaye baadaye alikuja kuwa mume wangu, walijifunza nami kupitia barua.
Katika mwaka wa 1978, nilienda Georgetown kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Imani Ishindayo.” Nilipofika katika mji huo mkuu, nilienda moja kwa moja hadi kwenye ofisi ya tawi kuwaeleza kwamba ninataka kubatizwa. Walipanga ili Albert Small azungumzie pamoja nami maswali ambayo wazee huzungumzia pamoja na wale wanaotaka kubatizwa. Nilifurahi kama nini kurudi Baramita nikiwa mtumishi wa Yehova aliyebatizwa!
Nilianza kuhubiri mara moja kwa bidii nyingi sana. Wengi walipendezwa, kwa hiyo nikawaomba baadhi yao wajenge mahali pa ibada. Huko, nilifasiri gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza kila Jumapili katika Kikaribu. Hata hivyo, baba yangu alipinga utendaji wangu naye akasisitiza nisiwe nikitoka nyumbani Jumapili. Kwa hiyo nilikuwa nikirekodi makala hizo kwenye kanda kwa siri na kumpa mmoja wa ndugu zangu azipeleke kwenye mikutano. Kufikia wakati huu, karibu watu 100 walikuwa wakihudhuria kwa ukawaida.
Muda mfupi baadaye, familia yetu ilihamia Georgetown kwa sababu za kibiashara, naye nyanya yangu akahamia kwenye kijiji cha Matthews Ridge. Shangazi yangu alibaki Baramita lakini akaacha kuwahubiria wengine habari njema. Kwa hiyo utendaji wa Ufalme ukakoma kwa muda.
Nikiwa huko Georgetown, nilikutana na Eustace Smith, na muda mfupi baadaye tukaoana. Hata ingawa Eustace hakuweza kuongea Kikaribu, sisi wawili tulitaka kwenda Baramita ili kuwasaidia watu wenye kupendezwa. Katika mwaka wa 1992 tamaa yetu ilitimia. Mara tu tulipofika, tulianza kuhubiri na kupanga mikutano. Muda si muda, hudhurio liliongezeka na kufikia 300 hivi!
Pia tulipanga kuwe na darasa la kujifunza kusoma na kuandika baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi. Yolande, mtoto wetu wa kwanza, alisaidia kufundisha darasa hilo. Alipoanza kusaidia, alikuwa na umri wa miaka 11 na alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Leo, yeye na binti yetu wa pili, Melissa, ni mapainia wa kawaida.
Katika mwaka wa 1993, Yehova alibariki kutaniko la Baramita likapata Jumba la Ufalme. Pia alitupa “zawadi katika wanadamu” ambao waliongea Kikaribu na walioweza kuliongoza kutaniko. (Efe. 4:8) Kuanzia Aprili 1, 1996, Baramita likawa kutaniko rasmi. Pia ninafurahi kusema kwamba mama yangu, nyanya yangu, na karibu ndugu na dada zangu wote wako katika kutaniko hilo. Kwa kweli, Yehova amenipa ‘maombi ya moyo wangu.’—Zab. 37:4.
[Picha]
Mimi na Eustace leo
[Chati/Picha katika ukurasa wa 148-149]
GUYANA MFUATANO WA MATUKIO
1900: Watu waanza kusoma na kuzungumzia gazeti ambalo sasa linaitwa Mnara wa Mlinzi (Zion’s Watch Tower) na vitabu vingine vinavyozungumzia Biblia.
1910
1912: E. J. Coward ahutubia mamia ya watu huko Georgetown na New Amsterdam.
1913: Chumba cha kufanyia mikutano chakodiwa kwenye jengo la Somerset House. Chatumiwa hadi mwaka wa 1958.
1914: Ofisi ya tawi ya kwanza yaanzishwa huko Georgetown.
1917: Serikali yapiga marufuku vichapo fulani baada ya kukazwa na makasisi.
1922: Marufuku yaondolewa. George Young atembelea Guyana.
1940
1941: Gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! (lililoitwa Consolation) yapigwa marufuku.
1944: Vichapo vyote vya Mashahidi wa Yehova vyapigwa marufuku.
1946: Marufuku yaondolewa mwezi wa Juni. Wamishonari wa kwanza kutoka Shule ya Gileadi wafika.
Miaka ya 1950: Sinema kuhusu jamii ya ulimwengu mpya (The New World Society in Action) yaonyeshwa kotekote Guyana.
1960: Ofisi ya tawi yanunua uwanja Georgetown. Majengo yaliyopo yatumiwa kama ofisi ya tawi na makao ya Wamishonari.
1967: Idadi ya wahubiri yapita 1,000.
1970
1988: Ofisi mpya ya tawi kwenye uwanja wa zamani yawekwa wakfu.
1995: Jumba la Ufalme lililojengwa kwa muda mfupi lakamilishwa.
2000
2003: Ofisi ya tawi ya sasa kwenye uwanja mpya yawekwa wakfu.
2004: Kuna wahubiri 2,163 nchini Guyana.
[Grafu]
(See publication)
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
2,000
1,000
1910 1940 1970 2000
[Ramani katika ukurasa wa 141]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
GUYANA
Baramita
Hackney
Charity
Henrietta
Suddie
GEORGETOWN
Mahaicony
Soesdyke
Bartica
Yaruni
New Amsterdam
Mackenzie
Wismar
Skeldon
Berbice
Orealla
Lethem
Essequibo
Demerara
Berbice
Courantyne
VENEZUELA
BRAZILI
SURINAME
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 134]
[Picha katika ukurasa wa 137]
Evander J. Coward
[Picha katika ukurasa wa 138]
Jengo la Somerset House mjini Georgetown, Guyana, ambamo mikutano ilifanyiwa kuanzia mwaka wa 1913 hadi 1958
[Picha katika ukurasa wa 139]
George Young
[Picha katika ukurasa wa 146]
Frederick Phillips, Nathan Knorr, na William Tracy, mwaka wa 1946
[Picha katika ukurasa wa 147]
Mnamo Juni 1946, tangazo hili lilitolewa, na hivyo marufuku juu ya vichapo vyetu ikaondolewa nchini Guyana
[Picha katika ukurasa wa 152]
Nathan Knorr, Ruth Miller, Milton Henschel, Alice Tracy (aliitwa Miller kabla ya kuolewa), na Daisy na John Hemmaway
[Picha katika ukurasa wa 153]
John Ponting
[Picha katika ukurasa wa 154]
Geraldine na James Thompson walitumika nchini Guyana kwa miaka 26
[Picha katika ukurasa wa 168]
Kikundi cha wahubiri wanaotumia mashua
[Picha katika ukurasa wa 169]
Kuhubiri kando-kando ya Mto Moruka katika “Kingdom Proclaimer 3”
[Picha katika ukurasa wa 175]
Jerry na Delma Murray
[Picha katika ukurasa wa 178]
Frederick McAlman na Eugene na Monica Fitzallen wakihubiria Mhindi mwenyeji huku akitengeneza mtumbwi wake
[Picha katika ukurasa wa 184]
Kusanyiko la mzunguko huko Baramita, mwaka wa 2003
[Picha katika ukurasa wa 185]
Watu wengi wilayani Baramita wamekubali kweli ya Biblia
[Picha katika ukurasa wa 186]
Kuhubiri kwa kutumia mtumbwi
[Picha katika ukurasa wa 188]
Sherlock na Juliet Pahalan
[Picha katika ukurasa wa 191]
Guyana ni “paradiso ya mapainia”
[Picha katika ukurasa wa 194]
Jumba la Ufalme huko Orealla, Guyana
[Picha katika ukurasa wa 197]
Ofisi ya tawi ya zamani kwenye barabara ya Brickdam namba 50, Georgetown, iliyojengwa mwaka wa 1987
[Picha katika ukurasa wa 199]
Halmashauri ya Tawi, kuanzia kushoto kuelekea kulia: Edsel Hazel, Ricardo Hinds, na Adin Sills
[Picha katika ukurasa wa 201]
Ofisi ya tawi ya Guyana iliyojengwa hivi majuzi