Rumania
Biblia ilitabiri kwamba Wakristo wa kweli wangeteswa vikali katika siku za mwisho. (Mwa. 3:15; Ufu. 12:13, 17) Nchini Rumania unabii huo umetimizwa kwa kadiri kubwa. Hata hivyo, masimulizi haya yanaonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova nchini Rumania hawajaruhusu chochote kuzima moto wa kweli unaowaka katika mioyo ya watu wa Mungu. (Yer. 20:9) Badala yake wamejipendekeza “kuwa wahudumu wa Mungu, kwa kuvumilia mengi, kwa dhiki, kwa hali za uhitaji, kwa magumu, kwa mapigo, [na] kwa vifungo vya gerezani.” (2 Kor. 6:4, 5) Masimulizi haya kuhusu jinsi walivyodumisha utimilifu wao na yawatie moyo wote wanaotaka kutembea na Mungu katika nyakati hizi ngumu.
Kipindi hatari kuliko vyote katika historia ya wanadamu kilianza mwaka wa 1914. Katika nchi nyingi za Ulaya kulikuwa na itikadi kali za kisiasa, mauaji yenye kuogofya, na serikali katili za kimabavu. Rumania iliathiriwa sana na mambo hayo yote, na Warumania waliteseka sana. Wale ambao kwa kumtii Yesu Kristo waliazimia kumpa “Mungu vitu vya Mungu” na kukataa kuabudu serikali, waliteseka pia.—Mt. 22:21.
Kabla ya mwaka wa 1945, makasisi wa Kanisa Othodoksi na Kanisa Katoliki walichochea mashambulizi dhidi ya watu wa Yehova. Walifanya hivyo katika mahubiri yao makanisani, na kwa kupanga njama na wanasiasa na polisi ili kuwachochea wachukue hatua dhidi ya watu wa Yehova. Baadaye Wakomunisti ndio waliowatesa kikatili kwa miaka 40 hivi.
Habari njema iliwezaje kuenea licha ya hali hizo ngumu? Jambo hilo liliwezekana kwa sababu Yesu alitimiza ahadi hii: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Hebu tuzungumzie jinsi mbegu za Ufalme zilivyopandwa kwa mara ya kwanza miaka mia moja iliyopita katika eneo ambalo leo linaitwa Ulaya Mashariki.
Warumania Warudi Nchini Kwao
Mwanafunzi wa Biblia Charles Taze Russell alitembelea sehemu mbalimbali za Ulaya Mashariki mwaka wa 1891, alipokuwa katika safari ya kuhubiri. Lakini alisikitika kidogo kwa sababu hakupata matokeo mazuri. Alisema hivi: “Watu hawakuwa tayari kuikubali kweli.” Lakini mambo yangebadilika nchini Rumania baada ya muda mfupi. Ndugu Russell mwenyewe angesaidia sana kuanzisha kazi nchini humo, lakini si kwa njia ya moja kwa moja. Vipi?
Mwishoni mwa miaka ya 1800, Warumania wengi walihamia nchi nyingine ili watafute kazi kwa sababu ya hali ngumu za kijamii na za kiuchumi nchini kwao, na baadhi yao walienda Marekani. Mbali na faida za kimwili, wengine kati yao walipata ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia. Károly Szabó na József Kiss ni baadhi yao. Wanaume hao walipendezwa na mambo ya kiroho na walisikiliza hotuba kadhaa za Biblia zilizotolewa na Ndugu Russell.
Ndugu Russell alitambua kwamba wanaume hao wawili walipendezwa kikweli na Biblia naye akajitambulisha na kuongea nao. Walipokuwa wakizungumza aliwapendekezea Károly na József warudi Rumania wakawaeleze watu wao wa ukoo na marafiki wao kuhusu Ufalme. Wote wawili walikubali na wakasafiri kwa meli hadi Rumania mwaka wa 1911. Waliamua kwenda kuishi mjini Tirgu-Mures huko Transylvania.
Alipokuwa safarini kwenda nchini kwao, Ndugu Szabó alisali kwamba angalau mtu mmoja katika jamaa yao angekubali kweli. Alipofika nyumbani alitenda kupatana na sala yake na kuwahubiria watu wake wa ukoo, akiwemo Zsuzsanna Enyedi, ambaye alimkaribisha kukaa nao. Mume wa Zsuzsanna alikuwa mtunza-bustani, naye Zsuzsanna aliuza maua sokoni.
Zsuzsanna aliyekuwa Mkatoliki alihudhuria Misa kila asubuhi kabla ya kwenda kazini, na kila usiku baada ya familia yake kulala alienda bustanini kusali. Károly aliona mambo hayo na usiku mmoja alimwendea bustanini, akaweka mkono begani mwake, na kusema: “Zsuzsanna, wewe una moyo mweupe. Utaipata kweli.” Na kama Ndugu Szabó alivyosema, mwanamke huyo mwenye sifa nzuri alikubali ujumbe wa Ufalme na akawa mtu wa kwanza mjini Tirgu-Mures kujiweka wakfu kwa Yehova. Alikuwa mwaminifu hadi alipokufa akiwa na umri wa miaka 87.
Ndugu Szabó alimhubiria pia Sándor Józsa, mwanamume kijana aliyekuwa mfanyakazi wa familia ya Enyedi. Sándor alihudhuria mikutano yote ambayo ndugu hao wawili waliongoza, na alifanya maendeleo haraka. Punde si punde, kijana huyo mwenye umri wa miaka 18 alianza kuhubiri na kutoa hotuba nzuri za Biblia katika kijiji chao cha Sărăţeni, katika Mkoa wa Mureş. Hatimaye wanaume sita pamoja na wake zao, na watoto wao 24, yaani, wavulana 11, na wasichana 13, wakawa ‘barua zake za kumpendekeza.’—2 Kor. 3:1, 2.
Ndugu Kiss na Szabó walianza kuhubiri mjini Tirgu-Mures na hatimaye wakahubiri katika sehemu zote za Transylvania. Walipokuwa katika kijiji cha Dumbrava, umbali wa kilometa 30 kutoka Cluj-Napoca, walimkuta Mbaptisti Vasile Costea. Vasile alikuwa mtu mfupi na thabiti, na alikuwa mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii. Fundisho la Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo lilimtatanisha, kwa hiyo alitega sikio József na Károly walipomfafanulia Maandiko. Baada ya kubatizwa, Vasile aliyejua Kihungaria, aliwahubiria kikamili Warumania na Wahungaria walioishi katika mkoa wao. Baadaye, akawa mtumishi wa wakati wote naye akaendelea na utumishi huo hadi alipokufa.
Ndugu Szabó alihubiri habari njema pia katika mji wa Satu-Mare kaskazini-magharibi mwa Rumania. Alipokuwa huko alimkuta Paraschiva Kalmár, mwanamke mwenye kumcha Mungu aliyekubali kweli kwa moyo wote. Paraschiva aliwafundisha watoto wake tisa kumpenda Yehova. Leo, kuna vizazi vitano vya Mashahidi katika familia yake.
Alexa Romocea ni Mrumania mwingine aliyejifunza kweli huko Marekani na kurudi Rumania kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Alexa alirudi kwenye kijiji chao cha Benesat, kaskazini-magharibi mwa Transylvania. Baada ya muda mfupi kikundi chao cha Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, kilianza kufanya mikutano katika eneo hilo. Wana wa ndugu ya Alexa, Elek na Gavrilă Romocea, walikuwa katika kikundi hicho. Leo, kuna vizazi vitano vya Mashahidi katika familia kubwa ya Alexa pia.
Elek aliteswa vikali kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi. Kwa hiyo, alihamia Marekani ambako alihudhuria kusanyiko la pekee la Wanafunzi wa Biblia huko Cedar Point, Ohio, mwaka wa 1922. Alikuwa na pendeleo la kuwafasiria wasikilizaji walioongea Kirumania kwenye kusanyiko hilo. Gavrilă alibaki Rumania na aliandamana na Ndugu Szabó na Kiss walipohubiri na kutembelea makutaniko na vikundi vipya huko Transylvania. Baadaye alifanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya kwanza nchini humo.
Mrumania anayeitwa Emanoil Chinţa alikamatwa wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu na akapelekwa kwenye gereza la jeshi nchini Italia, mbali na nyumbani kwake. Alipokuwa huko aliwapata Wanafunzi wa Biblia ambao walikuwa wamefungwa kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Emanoil alikubali kwa moyo ujumbe wao wa Kimaandiko. Baada ya kuachiliwa mwaka wa 1919, alirudi nyumbani huko Baia-Mare katika Mkoa wa Maramureş. Alihubiri habari njema kwa bidii na akasaidia kuanzisha kikundi cha Wanafunzi wa Biblia.
Kwa sababu ya bidii na roho ya kujitolea ya wahubiri wa kwanza wa habari njema na ya wale waliosikiliza ujumbe wao, idadi ya wanafunzi iliongezeka na vikundi vingi vya Wanafunzi wa Biblia vikaanzishwa. Miaka minane tu baada ya Károly Szabó na József Kiss kurudi Rumania, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme na watu waliopendezwa 1,700 katika madarasa 150 ya kujifunzia Biblia. Leo madarasa hayo yanaitwa vikundi au makutaniko. Ndugu Kiss alikuwa painia katika nchi ya kwao hadi alipokufa akiwa na umri wa miaka 86. Ndugu Szabó alirudi Marekani mwaka wa 1924, ili kupanga kazi ya kuwahubiria Wahungaria walioishi nchini humo.
Kuandaa Chakula cha Kiroho
Vichapo vilisaidia sana kueneza ujumbe wa Ufalme na kuwalisha wale waliokuwa na njaa ya kiroho. Ili kuandaa chakula cha kiroho, ndugu walipanga magazeti, trakti, na vitabu vichapwe katika makampuni ya uchapaji. Kuanzia mwaka wa 1914, toleo la kila mwezi la Mnara wa Mlinzi lenye kurasa 16, trakti, na vilevile vitabu vya Kihungaria vilichapwa katika kiwanda cha mtu fulani huko TirguMures. Kiwanda hicho kiliitwa Oglinda, jina linalomaanisha “Kioo.”
Kuanzia mwaka wa 1916, viwanda vya kibiashara nchini humo vilichapa magazeti, vitabu, na vijitabu katika Kirumania kama vile kijitabu kuhusu maskani (Tabernacle Shadows of the “Better Sacrifices”), gazeti la kurasa nane lenye makala zilizoteuliwa kutoka katika Mnara wa Mlinzi, kijitabu ambacho leo kinaitwa Kuyachunguza Maandiko Kila Siku (Daily Heavenly Manna for the Household of Faith), na kitabu cha nyimbo (Hymns of the Millennial Dawn). Kuanzia mwaka wa 1918, kiwanda fulani huko Detroit, Michigan, Marekani, kilichapa na kusafirisha hadi Rumania gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kirumania na trakti ya kila mwezi (People’s Pulpit) iliyofunua kwa ujasiri dini za uwongo.
Kwa kuwa habari njema ilikuwa ikienea sana, Jacob B. Sima, Mwanafunzi wa Biblia mwenye asili ya Kirumania, alitumwa Rumania kusaidia kupanga kazi ya kuhubiri na kuiandikisha kisheria. Punde baada ya kufika Cluj-Napoca mnamo mwaka wa 1920, Ndugu Sima alifanya mkutano na Károly Szabó, na baadaye József Kiss. Hangaiko lao kuu lilikuwa kupata nyumba inayofaa jijini Cluj-Napoca ambayo ingetumiwa kama ofisi ya tawi. Hata hivyo, kwa sababu ya upungufu wa nyumba, ndugu hao waliamua kufungua ofisi nyumbani kwa ndugu fulani. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ya kwanza ilifunguliwa Aprili 1920 na shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova likaandikishwa. Ofisi ya tawi ya Rumania ilisimamia kazi kwa muda pia katika nchi ya Albania, Bulgaria, Hungaria, na ile iliyokuwa Yugoslavia.
Wakati huo roho ya mapinduzi iliyoenea katika nchi za Balkani ilianza kuathiri Rumania pia. Mbali na msukosuko wa kisiasa, chuki dhidi ya Wayahudi ilienea haraka sana, hasa katika vyuo vikuu, na wanafunzi katika majiji kadhaa wakafanya ghasia. Kwa hiyo, serikali ikapiga marufuku mikutano ya hadharani. Ijapokuwa watumishi wa wakati wote hawakuhusika katika ghasia hizo, zaidi ya 20 kati yao walikamatwa na kutendwa vibaya, na wakanyang’anywa vichapo vyao.
Ingawa hivyo, ndugu waliendelea kuhubiri kwa bidii na walihitaji vichapo vingi zaidi. Kwa kuwa gharama ya uchapaji katika viwanda vya kibiashara ilizidi kupanda, ndugu kwenye ofisi ya tawi walitafuta njia nyingine za kuchapa. Wakati huohuo, kiwanda cha uchapaji ambacho ndugu walikuwa wakitumia kwenye Barabara ya Regina Maria, Na. 36, huko Cluj-Napoca, kilikuwa kikiuzwa. Baada ya kupata kibali kutoka makao makuu, ofisi ya tawi ilinunua kiwanda hicho kilichokuwa kwenye kiwanja chenye jengo moja lenye orofa nne na lingine lenye orofa mbili.
Marekebisho ya majengo hayo yalianza mnamo Machi 1924, na ndugu kutoka sehemu za mbali kama vile Baia-Mare, Bistriţa, na Rodna walijitolea kufanya kazi. Ili kutoa michango kwa ajili ya mradi huo, ndugu kadhaa waliuza baadhi ya vitu vyao, na wengine walichanga chakula na vifaa vya ujenzi. Walisafirisha vifaa vingi kwa kutumia mifuko ya pekee inayoitwa desagi, iliyobebwa kwa mikanda begani au na farasi.
Ili kuboresha uchapaji, ofisi ya tawi ilinunua mashine tatu za kupanga herufi, mashine tatu za kuchapa, mashine ya kukunja karatasi, mashine ya kupamba kwa dhahabu, na vifaa vingine. Kwa hiyo, vitabu vilivyochapwa katika kiwanda hicho vilikuwa bora kuliko vitabu vyote nchini Rumania.
Kulikuwa na Wanabetheli 8 na mmoja wao aliwasimamia watu 40 wasiokuwa Mashahidi ambao waliajiriwa kufanya kazi kwa zamu tatu katika kiwanda hicho. Ripoti ya mwaka wa kwanza wa uchapaji, yaani mwaka wa 1924, inaonyesha kwamba walifanya kazi kwa bidii. Magazeti 175,000, vitabu 226,075, na vijitabu 100,000, vilichapwa katika Kirumania na Kihungaria! Kitabu The Harp of God kilichapwa, na pia The Divine Plan of the Ages ambacho ni cha kwanza kati ya vitabu saba vya Studies in the Scriptures.
Baada ya matayarisho ya miaka miwili, ofisi ya tawi ilichapa pia katika Kirumania kitabu (Scenario of the Photo-Drama of Creation) kinachotegemea hotuba kuhusu uumbaji (“Photo-Drama of Creation”). Hotuba hiyo ina sinema na picha zenye rangi zilizoambatanishwa na sauti. Wahudhuriaji walionyeshwa matukio kuanzia uumbaji wa dunia hadi mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Kitabu hicho, hakikuvutia sana kama ile hotuba, lakini kilikuwa na picha 400, na masomo mafupi kuhusu mafundisho ya Biblia, historia, na sayansi, yaliyowachochea wasomaji wengi waichunguze Biblia zaidi.
Madarasa ya Kujifunzia Biblia Yaongezeka
Joseph Rutherford aliwahimiza wasikilizaji hivi kwenye kusanyiko la mwaka wa 1922, huko Cedar Point, Ohio: “Tangazeni, tangazeni, tangazeni, Mfalme na Ufalme wake!” Mwito huo wenye kusisimua uliwachochea watu wa Mungu ulimwenguni pote wahubiri kwa bidii zaidi. Nchini Rumania ndugu walihubiri habari njema katika maeneo mapya na wakawasaidia wengi wawe wanafunzi.
Wapya walijifunzaje Biblia siku hizo? Walijiunga na madarasa yaliyoitwa Mafunzo ya Biblia ya Kiberoya. Maswali yaliandaliwa, na masomo yalitegemea vichapo vilivyotumwa kwa njia ya posta. Ratiba ya mafunzo ilipatikana katika Mnara wa Mlinzi. Wanafunzi waliokuwa wamefanya maendeleo walinufaika pia kwa Masomo ya Shule ya Jumapili ya Kimataifa, yaliyowasaidia kuwa walimu stadi wa Neno la Mungu.
Wawakilishi wa ofisi ya tawi walikuwa wakitembelea madarasa hayo ili kutoa hotuba na misaada mingineyo ya kiroho. Hata hivyo, kwa kawaida, waangalizi wanaosafiri ndio waliofanya ziara za uchungaji na kufundisha. Mwaka wa 1921, kulikuwa na waangalizi sita wanaosafiri, na miaka miwili tu baadaye kulikuwa na waangalizi wanane. Wahubiri hao wenye bidii walipanga mikutano katika mamia ya majiji, miji, na vijiji, nao waliwahutubia maelfu waliokuwa na njaa ya kiroho.
Emanoil Chinţa, aliyetajwa mapema, na Onisim Filipoiu walikuwa kati ya waangalizi hao wanaosafiri. Wasabato na Wabaptisti wengi walisikiliza hotuba fulani ya Ndugu Chinţa huko Bukovina katika eneo la kaskazini, na baadhi yao wakakubali kweli. Baadaye ndugu hao wawili walitumwa Bucharest, ambako waliwasaidia wengi kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu. Mtu mmoja aliyethamini msaada huo aliandika hivi: “Ninamshukuru Mungu kwa kuwatuma Ndugu Emanoil na Onisim, ambao walijitahidi sana kunisadikisha na kunifundisha Neno la Mungu. Bwana atafanya kazi kubwa katika mji huu, lakini uvumilivu unahitajika.”
Ndugu walifanya makusanyiko yao ya kwanza mwaka wa 1920. Moja lilifanywa huko Brebi, Mkoa wa Sălaj, na lingine mjini Ocna Dejului, Mkoa wa Cluj. Wahudhuriaji waliweza kusafiri kwa gari-moshi na ndugu na watu waliopendezwa ambao waliishi katika miji hiyo wakawakaribisha kulala nyumbani kwao. Watu 500 hivi kutoka sehemu zote za Rumania walihudhuria, na wakatoa ushahidi mzuri kwa mwenendo wao bora.
Hata hivyo, ongezeko la haraka la idadi ya wahubiri wa Ufalme lilichochea upinzani. Wanadini na wanasiasa waliwatesa ndugu tangu mwanzo wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.
Kichaa cha Vita Chawapa Maadui Nafasi
Wenye mamlaka walichochewa na makasisi na hisia za uzalendo, na hawakuwavumilia wale wasiokuwa wazalendo, wala wale wasiokuwa tayari kwenda vitani kutetea nchi yao. Kwa hiyo, Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipoanza, ndugu wengi walikamatwa na kuhukumiwa. Baadhi yao, kama vile Ioan Rus aliyekuwa ameoa majuzi, waliuawa. Ndugu huyo alitoka katika kijiji cha Petreştii de Mijloc, kusini ya Cluj-Napoca.
Daniel, ambaye ni mtu wa ukoo wa Ioan anasema hivi: “Ioan Rus aliitwa jeshini mwaka wa 1914. Kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi alipelekwa Bucharest na kuhukumiwa kifo. Alilazimishwa kuchimba kaburi lake mwenyewe na kusimama kando yake huku akikabili kikosi cha wauaji. Ofisa mkuu alimruhusu Ioan kusema maneno yake ya mwisho. Ioan akaamua kutoa sala kwa sauti. Wanajeshi hao waliguswa sana na sala ya Ioan hivi kwamba walikataa kumuua. Ndipo, ofisa mkuu akampeleka mwanajeshi mmoja kando na kumwahidi likizo na mshahara wa miezi mitatu kwa kumpiga mfungwa huyo risasi. Mtu huyo alikubali, na akapata likizo kwa kumuua Ioan.”
Ndugu Kiss na Szabó walikamatwa mwaka wa 1916, na wakahukumiwa kifungo cha miaka mitano. Walionwa kuwa “hatari,” kwa hiyo, kila mmoja wao alifungwa akiwa peke yake kwa miezi 18 katika gereza lenye ulinzi mkali huko Aiud. József na Károly walikuwa “hatari” kwa njia gani? Hakimu alisema kwamba “walieneza mafundisho yaliyo tofauti na yale yaliyokubaliwa na wengi.” Kwa hiyo, walifungwa si kwa sababu ya kukataa kuua, bali kwa sababu walifundisha kweli za Biblia zilizopinga mafundisho ya makanisa.
Walipokuwa gerezani ndugu hao waliwaandikia ndugu katika makutaniko na vikundi ili kuwatia moyo. Barua moja ilisema hivi: “Tunafurahi sana kwamba Baba yetu wa mbinguni, ambaye anastahili shukrani, sifa, na heshima, ameruhusu nuru ya Mnara wa Mlinzi ing’ae. Tunajua kwamba ndugu zetu wanathamini Mnara wa Mlinzi nao wanalilinda katika ulimwengu huu wenye msukosuko.” Wote wawili waliachiliwa mwaka wa 1919 nao wakasaidia kufungua ofisi ya tawi mwaka uliofuata.
Upinzani wa Makasisi Wazidi
Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipokwisha mwaka wa 1918, makasisi waliendelea kuwapinga watu wa Mungu. Kasisi mmoja alichambua hadharani maoni ya Wanafunzi wa Biblia kuhusu fundisho la kutokufa kwa nafsi na la bikira Maria. Aliandika hivi: “Tamaa ya maisha bora hapa duniani inawafanya [Wanafunzi wa Biblia] warukwe na akili. Wanasema kwamba sisi sote ni ndugu na dada na kwamba watu wa mataifa yote ni sawa.” Kisha akasema kwamba ni vigumu kuchukua hatua ya kisheria dhidi ya Wanafunzi wa Biblia, kwa sababu “wanajifanya kuwa eti wenye kupenda kweli, watakatifu, wenye amani, na wanyenyekevu.”
Mnamo mwaka wa 1921, makasisi huko Bukovina waliandikia Wizara ya Mambo ya Ndani na ya Sheria ili kuomba kazi ya Wanafunzi wa Biblia ipigwe marufuku. Katika sehemu zote ambazo kweli ilikuwa imeenea, makasisi waliwakasirikia watu wa Mungu. Kanisa Othodoksi, Kanisa Katoliki, na makanisa mengine yalimchochea mtu mmoja-mmoja na wafanya ghasia wawachukie na kuwashambulia akina ndugu. Ofisi ya tawi iliandikia makao makuu hivi: “Katika nchi hii makasisi wengi ni maofisa wa serikali, na hilo huathiri kazi yetu kwa kadiri fulani. Hakungekuwa na matatizo kama wangeshika sheria, lakini wao hutumia vibaya mamlaka yao.”
Kwa sababu ya malalamiko mengi ya makasisi, Wizara ya Dini iliwaruhusu polisi kuwazuia watu wa Yehova wasihubiri wala wasifanye mikutano. Kwa hiyo, polisi wakawa chombo cha makanisa, nao wakawakamata ndugu na kuwashtaki kwa uwongo kwamba wanasababisha mchafuko. Hata hivyo, sheria haikuwa wazi, kwa hiyo adhabu zilitofautiana. Mwenendo mzuri wa akina ndugu ulitatanisha pia. Hakimu mmoja alisema: “Haiwezekani kuwahukumu Wanafunzi wa Biblia kwa sababu wao wanapenda amani kuliko watu wengine wote.”
Hata hivyo, upinzani ulizidi, na gazeti la Mnara wa Mlinzi likapigwa marufuku mwishoni mwa mwaka wa 1926. Lakini hilo halikuzuia chakula cha kiroho kisiingizwe nchini, kwani ndugu walibadili tu jina la gazeti hilo! Kuanzia toleo la Januari 1, 1927, chapa ya Kirumania iliitwa Mavuno, na baadaye Nuru ya Biblia, na hatimaye Pambazuko. Chapa ya Kihungaria iliitwa Hujaji Mkristo, kisha Injili, na mwishowe, Gazeti la Wale Wanaoamini Damu ya Kristo.
Inasikitisha kwamba katika kipindi hicho Jacob B. Sima aliasi imani. Kwa sababu ya matendo yake, majengo yote ya ofisi ya tawi na vifaa vyote vilipotezwa mwaka wa 1928! Ripoti katika Kitabu cha Mwaka cha 1930 inasema kwamba ndugu “wametawanyika na kuwa na shaka sana.” Kwa sababu ya matukio hayo yenye kufadhaisha, kazi ilisimamiwa na ofisi ya tawi ya Ujerumani kuanzia mwaka wa 1929, na baadaye ikasimamiwa na Ofisi ya Tawi ya Ulaya ya Kati, huko Bern, Uswisi. Ofisi hizo mbili zilisimamia kazi kupitia ofisi ambayo ndugu walifungua baadaye huko Bucharest.
‘Tafadhali, Usikiteketeze Kitabu Changu!’
Licha ya majaribu hayo, ndugu waaminifu walijipanga upya na kuendelea kuhubiri, nao walihubiri hata kwenye maeneo mapya. Agosti 24, 1933, ofisi ya Rumania iliandika hivi: “Watu wana njaa ya kiroho. Ndugu wanatuandikia kwamba wanapohubiri, wanakijiji wengi huandamana nao nyumba kwa nyumba ili wapate nafasi zaidi ya kusikia kweli.”
Mwanamke mmoja maskini aliomba kitabu kilichokuwa kikitolewa, naye akatoa mchango mdogo kwa ajili ya kazi ya Ufalme. Kasisi wa kijiji hicho aliposikia jambo hilo alienda mara moja nyumbani kwa mwanamke huyo na kumwambia: “Nipe kile kitabu, ili nikitupe motoni!”
Mwanamke huyo akamsihi kasisi: “Tafadhali, Baba, usikiteketeze, kimetufariji, na kitatusaidia kuvumilia umaskini wetu!” Alikataa katakata kumpa kasisi kitabu hicho.
Mwanamke mwingine aliyethamini vitabu vyetu alikuwa amewaajiri Mashahidi wa Yehova. Siku moja mwanamke huyo mwenye cheo aliwaambia wafanyakazi wake hivi: “Sasa ninyi si watumishi wangu tena bali ndugu zangu!” Katika kijiji kingine ndugu aliwaambia watoto kadhaa kwamba alikuwa akihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Watoto nao wakawatia wapita-njia moyo wakubali vitabu hivyo. Watoto hao walitangaza: “Vitabu hivi vinazungumza kumhusu Mungu.” Ndugu huyo alishangaa na akakosa la kusema kwa sababu watoto hao walisema kwa shauku kwa niaba yake, na punde akagawa vitabu vyake vyote!
Nicu Palius, painia mpole kutoka Ugiriki, alikuja kuhubiri nchini Rumania. Baada ya kuhubiri jijini Bucharest alihamia Galaţi, bandari kubwa kwenye Mto Danube. Nicu aliandika hivi mwishoni mwa mwaka wa 1933: “Niliwahubiria Warumania kwa miezi miwili na nusu hivi, na Yehova Mungu akanibariki sana ijapokuwa sikujua lugha yao. Baadaye niliwahubiria Wagiriki na Waarmenia, na Bwana akanisaidia kuhubiri katika miji 20. Wagiriki hasa walifurahia ujumbe wa Ufalme.”
Naam, licha ya uchochezi wa makasisi, watu wengi wenye mioyo myeupe walitaka kusikia habari njema. Kwa mfano, meya wa mji fulani alisoma kwa hamu vijitabu kadhaa na baadaye akasema kwamba anatamani sana ulimwengu mpya uje. Katika mji mwingine mtu fulani aliomba vitabu kadhaa, na akaahidi kuwagawia wote waliotaka kuvisoma.
Kazi Yapangwa Upya
Mwaka wa 1930, miaka miwili baada ya Sima kuasi imani, Martin Magyarosi aliwekwa kusimamia kazi. Magyarosi alikuwa raia wa Rumania mwenye asili ya Kihungaria aliyetoka Bistriţa, Transylvania. Baada ya kuzoezwa kwa majuma sita kwenye ofisi ya tawi ya Ujerumani, Ndugu Magyarosi alifungua ofisi huko Bucharest. Punde si punde, Mnara wa Mlinzi katika Kirumania, lililokuwa likichapwa kwa muda nchini Austria na Ujerumani, lilianza kuchapwa tena nchini Rumania na kampuni ya uchapishaji iliyoitwa Kitabu cha Dhahabu.
Baada ya kujitahidi sana ndugu walifaulu kuandikisha shirika jipya la kisheria mwaka wa 1933, yaani, shirika la Mashahidi wa Yehova la The Bible and Tract Society. Barua za shirika hilo zilipelekwa katika sanduku kwenye Barabara ya Crişana, Na. 33, Bucharest. Hata hivyo, kwa sababu ya upinzani wa kidini na wa kisiasa, ndugu waliweza tu kuliandikisha kama shirika la kibiashara.
Hata hivyo, jitihada hizo ziliwasaidia ndugu wasiwashuku tena ndugu wenye madaraka, na kazi ya kuhubiri ikasonga mbele. Hata wahubiri wengi wakawa mapainia, na wengine wakafanya mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri, hasa wakati wa majira ya baridi kali, wakati ambapo watu wa mashambani hawana kazi nyingi. Ndugu walisikiliza pia hotuba za Biblia kutoka ng’ambo zilizosambazwa kwenye redio. Hotuba hizo ziliwasaidia hasa watu ambao hawakuhudhuria mikutano kwa sababu ya kuwaogopa majirani au makasisi. Mnara wa Mlinzi lilionyesha saa za vipindi, vichwa vya hotuba, na mitabendi za redio.
Kazi ya kuhubiri habari njema ilisonga mbele pia kwa sababu ya santuri za kubebwa zilizotengenezwa na Mashahidi wa Yehova. Katika miaka ya 1930, makutaniko na watu waliweza kuagiza santuri hizo na hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Tangazo moja katika toleo fulani la Huduma Yetu ya Ufalme (ambayo iliitwa Bulletin wakati huo) lilisema kwamba hotuba hizo ziliwatia moyo “ndugu na vilevile watu waliopenda kweli ambao walikuwa na santuri.”
Kujaribiwa na Ndugu Wasio Waaminifu
Katika miaka ya 1920 na 1930, Neno la Mungu lilieleweka vizuri zaidi, na pia daraka la kila Mkristo la kutoa ushahidi kuhusu kweli. Hivyo, mwaka wa 1931, Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba watu wa Mungu wanapaswa kuitwa Mashahidi wa Yehova. Jina hilo la Kimaandiko si kibandiko tu, bali wote wanaoitwa Mashahidi wa Yehova wanatetea na kutangaza kwamba Yehova ndiye Mungu. (Isa. 43:10-12) Wanafunzi wa Biblia waliopinga kazi ya kuhubiri walikwazwa na jambo hilo nao wakaacha tengenezo. Baadhi yao wakawa waasi-imani na kujiita Wamilenia. Je, imani ya waaminifu ingestahimili jaribu hilo? Je, wangeendelea kuhubiri licha ya upinzani kutoka kwa makasisi na waasi-imani?
Ingawa baadhi ya ndugu waliacha kweli kwa sababu ya upinzani huo, wengi waliendelea kumtumikia Yehova kwa bidii. Ripoti moja ya mwaka wa 1931, inasema: “Kuna ndugu 2,000 hivi nchini Rumania, nao wamegawa vitabu 5,549 na vijitabu 39,811, licha ya matatizo hayo makubwa.” Mwaka uliofuata ndugu walifanikiwa hata zaidi, waligawa vitabu na vijitabu 55,632.
Isitoshe, nyakati nyingine upinzani uliwasaidia ndugu badala ya kuwazuia. Kwa mfano, Mashahidi wote katika eneo fulani waliamua kuonyesha wazi kwamba wamejitenga na “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:2, 4) Kwa siku tano mfululizo, ndugu na dada hao wajasiri walimiminika kwenye ofisi ya baraza la mji ili waandike hati za kujiuzulu kutoka katika makanisa yao ya zamani.
Viongozi wa mji walishtuka, na kasisi wa eneo hilo akashikwa na bumbuazi. Kwanza alikimbilia kituo cha polisi ili apate msaada, lakini wapi. Kwa hiyo, akarudi haraka kwenye ofisi ya baraza la mji na kumshtaki kwa uwongo mthibitishaji wa hati za kisheria kuwa Mkomunisti, kwa sababu aliwasaidia watu hao kuandika hati zao. Mthibitishaji huyo aliudhika na kumwambia kwamba hata kama watu wote mjini wangekuja kwake, angewasaidia kuandika hati za kujiuzulu. Kwa hiyo, kasisi akashindwa na ndugu wakafaulu kuandika hati zao.
“Je, Unataka Kunipiga Risasi?”
Makasisi waliwachambua Mashahidi wa Yehova kwa hasira katika mahubiri yao. Waliendelea pia kuichochea serikali ipige marufuku kazi ya Mashahidi. Bila shaka makasisi walitumia Wizara ya Dini, chombo chao cha kisiasa, kuwachochea polisi wawanyanyase ndugu. Kwa mfano, siku moja mkuu wa polisi na ofisa mwenzake waliingia katika nyumba ambamo ndugu walikuwa wakifanyia mkutano.
Yule mkuu alimwambia hivi mwenye nyumba, ndugu ambaye tutamwita George: “Ninataka kuona kibali chako cha kuendesha ibada nyumbani kwako.”
Kwa sababu George alijua kwamba yamkini polisi huyo hakuwa na ruhusa ya kupekua nyumba yake, alimuuliza hivi: “Ni nani aliyekupa ruhusa ya kuingia nyumbani kwangu?”
Jamaa huyo alishindwa kujibu, kwa hiyo, George akamwomba aende zake. Alielekea mlangoni shingo upande. Lakini alipokuwa akitoka alimwamuru ofisa mwenzake alinde lango la mbele na kumkamata George ikiwa angejaribu kuondoka. Baadaye, George alipotoka nje, ofisa huyo alimkamata “kwa mamlaka ya sheria.”
“Kwa mamlaka ya sheria gani?” George akamuuliza.
“Nina hati ya kukukamata,” akasisitiza.
George alijua sheria kwa sababu alikuwa polisi hapo awali, basi, akamwomba amwonyeshe hati hiyo. Na kama George alivyofikiri, polisi huyo hakuwa na hati ya kumkamata. Kwa sababu alishindwa kumkamata George kisheria, alijaribu kumtisha kwa kutia risasi katika bunduki yake.
George akamuuliza: “Je, unataka kunipiga risasi?”
“La, mimi si mjinga,” ofisa huyo akajibu.
George akamuuliza: “Kwa nini basi, unatia risasi katika bunduki yako?”
Ndipo polisi huyo alipotambua kwamba ametenda kwa ujinga, na akaondoka. George hakutaka nyumba yake ipekuliwe isivyo haki tena, kwa hiyo akamshtaki yule mkuu wa polisi kwa kuingia nyumbani kwake bila ruhusa. Inashangaza kwamba mkuu huyo wa polisi alihukumiwa kifungo cha siku 15 gerezani.
Katika kisa kingine, ndugu mzee alitoa ushahidi mzuri mahakamani. Hakimu alishika mkononi vitabu viwili vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Alivitikisa mbele ya ndugu, huku akimshtaki kwa kusambaza vitabu vya kidini.
Ndugu huyo akajibu: “Ukiniadhibu kwa sababu ninatangaza kweli ya Neno la Mungu, nitaliona jambo hilo kuwa alama ya heshima. Bwana Yesu aliwaambia wafuasi wake wafurahi wanapoteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ndivyo manabii wa kale walivyotendwa. Yesu mwenyewe aliteswa na kutundikwa mtini, si kwa sababu alifanya makosa, bali kwa sababu alihubiri kweli kutoka kwa Mungu.”
Ndugu huyo akaongeza: “Basi, ikiwa mahakama hii itaniadhibu kwa sababu ninatangaza ujumbe wa Yesu kuhusu Ufalme kwa kutumia vile vitabu viwili, itakuwa ikimwadhibu mtu asiye na hatia.” Hakimu akafuta mashtaka.
“Ndugu Nchini Rumania Wateswa Vikali Kuliko Kwingineko”
Baada ya mwaka wa 1929, mambo kama vile kushuka kwa bei za mazao, ukosefu wa kazi, na msukosuko wa kisiasa yalifanya Wafashisti na vikundi vingine vya siasa kali vienee. Isitoshe, katika miaka ya 1930, uvutano wa utawala wa Nazi wa Ujerumani ulianza kuenea nchini Rumania. Hayo yalikuwa dalili ya mambo mabaya kwa Mashahidi wa Yehova. Kitabu cha Mwaka cha 1936 kilisema hivi: “Ndugu nchini Rumania wateswa vikali kuliko kwingineko.” Kuanzia 1933 hadi 1939, kesi 530 zilifunguliwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Waendesha mashtaka walisisitiza daima kazi ipigwe marufuku na ofisi huko Bucharest ifungwe.
Hatimaye, saa 2:00 usiku Juni 19, 1935, polisi walifika kwenye ofisi wakiwa na hati bandia, wakachukua faili na zaidi ya vijitabu 12,000, na kumweka mlinzi. Hata hivyo, ndugu mmoja alifaulu kutoroka kupitia mlango wa nyuma naye akawasiliana na wakili fulani aliyewapenda Mashahidi. Mtu huyo aliyekuwa seneta, aliwapigia simu watu fulani wenye mamlaka na ofisi ikafunguliwa tena na faili zikarudishwa. Lakini kwa muda mfupi tu.
Aprili 21, 1937, Wizara ya Dini ilitoa amri iliyochapishwa katika gazeti rasmi la serikali na katika magazeti mengine. Amri hiyo ilisema kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova imepigwa marufuku kabisa nchini Rumania na kwamba wale wanaosambaza au hata kusoma vitabu vyao wangekamatwa na kuadhibiwa, na pia kunyang’anywa vitabu hivyo.
Ndugu walikata rufani. Lakini waziri aliyehusika aliahirisha kesi hiyo mara tatu kwa sababu alijua haikuwa na msingi mzuri. Kabla kesi hiyo haijasikizwa, Mfalme Carol wa Pili, akajitangaza kuwa mtawala wa kimabavu wa Rumania. Amri mpya dhidi ya Mashahidi wa Yehova ilitolewa mnamo Juni 1938. Ndugu wakawasilisha kesi tena. Pia, waliandikia mfalme barua rasmi, na kumweleza kwamba vitabu vya Mashahidi vinaelimisha, havipingi serikali, wala havichochei mchafuko. Barua hiyo ilinukuu uamuzi uliokuwa umetolewa na mahakama kuu kuhusu jambo hilo. Mfalme aliituma barua hiyo kwenye Wizara ya Dini. Matokeo yalikuwa nini? Wizara hiyo ilifunga kirasmi ofisi ya Bucharest Agosti 2, 1938.
Katika kipindi hicho kigumu, ndugu mmoja-mmoja, na hata familia nzimanzima, walikamatwa na kuhukumiwa vifungo vya gerezani. Baadhi yao walikamatwa kwa sababu tu waliimba nyimbo za Ufalme nyumbani kwao. Walihukumiwa vifungo vya miezi mitatu hadi miaka miwili. Ndugu waliokamatwa walitambuliwaje? Wengi wao walipelelezwa na watu walioshawishiwa na makasisi, ambao walijifanya kuwa mafundi, wachuuzi, na kadhalika.
Yeyote aliyepatikana na vitabu vyetu alikamatwa. Ndugu mmoja aliyefanya kazi ya kukata miti, alienda msituni akiwa na Biblia yake na Kitabu cha Mwaka. Siku moja polisi walipekua vitu vya kila mtu na wakapata vitabu vya huyo ndugu. Walimkamata na kumlazimisha kutembea umbali wa kilometa 200 hadi mahakamani, ambako alihukumiwa kifungo cha miezi sita. Magereza yalikuwa machafu, yalijaa watu, na kulikuwa na chawa wengi. Wafungwa hawakupewa chakula kingine isipokuwa supu zenye maji mengi.
Majaribu Yazidi Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu
Vita vya Pili vya Ulimwengu, ambavyo vingeathiri Rumania kwa muda mrefu, vilianza wakati jeshi la Ujerumani lilipovamia Poland alfajiri na mapema Septemba 1, 1939. Katika jitihada zao za kutwaa maeneo, watawala wa Muungano wa Sovieti na Ujerumani waliokuwa wametia sahihi mapatano ya kutoshambuliana, waligawanya Ulaya Mashariki. Rumania iligawanywa kama keki tu. Hungaria ilichukua Transylvania kaskazini; Muungano wa Sovieti ukachukua Bessarabia na Bukovina Kaskazini; nayo Bulgaria ikapata Dobruja kusini. Rumania ilipoteza thuluthi moja ya eneo lake na watu wake. Serikali ya kimabavu ya Kifashisti ilianza kutawala Rumania mwaka wa 1940.
Serikali hiyo mpya ilisimamisha katiba kwa muda na kuamua kwamba dini tisa tu zingekubaliwa. Dini kuu kati ya hizo zilikuwa Kanisa Othodoksi, Kanisa Katoliki, na makanisa ya Lutheri. Marufuku dhidi ya Mashahidi wa Yehova ilibaki. Matendo ya jeuri yalikuwa ya kawaida, na jeshi la Ujerumani lilivamia nchi hiyo mnamo Oktoba 1940. Katika hali hizo ngumu mawasiliano yalikatishwa kati ya Rumania na Ofisi ya Tawi ya Ulaya ya Kati huko Uswisi.
Martin Magyarosi alitoka Bucharest na kuhamia TirguMures, Transylvania, kwa sababu Mashahidi wengi wa Yehova waliishi katika mkoa huo. Mke wake Maria tayari alikuwa amehamia Tirgu-Mures kwa sababu ya matatizo ya afya. Pamfil na Elena Albu, ambao pia walikuwa wamefanya kazi kwenye ofisi huko Bucharest, wakahamia Baia-Mare, sehemu ya kaskazini. Walipokuwa katika miji hiyo miwili, Ndugu Magyarosi na Albu walipanga upya kazi ya kuhubiri na ya kuchapa Mnara wa Mlinzi kisiri. Mfanyakazi mwenzao Teodor Morăraş, alibaki Bucharest, naye alisimamia kazi katika sehemu iliyobaki ya Rumania hadi alipokamatwa mwaka wa 1941.
Ndugu waliendelea kuhubiri kwa bidii, na waligawa vitabu vinavyozungumzia Biblia kila walipopata nafasi, lakini kwa tahadhari sana. Kwa mfano, waliacha vijitabu kwenye sehemu za umma kama vile mikahawa, vituo vya gari-moshi, na sehemu nyinginezo, wakitumaini kwamba mtu fulani angevutiwa navyo. Waliendelea pia kutii agizo la Maandiko la kukutanika pamoja ili kutiana moyo kiroho, huku wakijihadhari wasitambuliwe. (Ebr. 10:24, 25) Kwa mfano, katika sehemu za mashambani, wakulima walikuwa na desturi ya kusaidiana kuvuna na kusherehekea mavuno kwa kusimulia hadithi za vichekesho. Ndugu walifanya mikutano ya Kikristo badala ya karamu hizo za kitamaduni.
‘Walikazwa Katika Kila Njia’
Ndugu Magyarosi alikamatwa mnamo Septemba 1942 lakini akaendelea kupanga kazi ya kuhubiri akiwa gerezani. Ndugu na Dada Albu walikamatwa pia, pamoja na ndugu na dada wengine 1,000 hivi. Wengi wao waliachiliwa baada ya kupigwa na kufungwa kwa karibu majuma sita. Mashahidi 100, wakiwemo akina dada, walihukumiwa vifungo vya miaka 2 hadi 15 kwa sababu hawakuunga mkono jeshi. Ndugu watano walihukumiwa kifo, lakini adhabu hiyo ikabadilishwa kuwa vifungo vya maisha. Polisi wenye silaha waliwakamata hata mama na watoto wadogo usiku, na kuacha mifugo na nyumba zao bila ulinzi, ili wezi wapore.
Walipofika gerezani ndugu “walikaribishwa” na kikundi cha walinzi ambao walimfunga kila mmoja miguu na kumlaza sakafuni na kumshikilia kwa nguvu huku mmoja wao akimpiga nyayo kwa rungu gumu la mpira. Mifupa ilivunjika, kucha za vidole zikatoka, na ngozi ikawa nyeusi na kubambuka kama tu maganda ya mti. Makasisi waliotembelea magereza hayo waliwadhihaki kwa kusema: “Yehova wenu yuko wapi sasa awaokoe?”
Ndugu ‘walikazwa katika kila njia lakini hawakuachwa bila msaada.’ (2 Kor. 4:8, 9) Waliwafariji wafungwa wengine kwa kuwaeleza ujumbe wa Ufalme, na baadhi yao wakaukubali. Fikiria kisa cha Teodor Miron kutoka kijiji cha Topliţa, kaskazini-mashariki mwa Transylvania. Kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, Teodor alielewa kwamba Mungu anakataza mauaji, kwa hiyo akakataa kujiunga na jeshi. Hivyo, mnamo Mei 1943, alihukumiwa kifungo cha miaka mitano. Muda mfupi baadaye, alimkuta Martin Magyarosi, Pamfil Albu, na Mashahidi wengine gerezani naye akakubali kujifunza Biblia. Teodor alifanya maendeleo kwa haraka na baada ya majuma machache akajiweka wakfu kwa Yehova. Lakini alibatizwaje?
Nafasi ilitokea wakati Teodor na Mashahidi wengine 50 Warumania hivi walipokuwa wakipelekwa kwenye kambi ya Wanazi huko Bor, Serbia. Walipokuwa safarini kuelekea Bor, walikaa kwa muda mfupi huko Jászberény, Hungaria, ambako ndugu Wahungaria zaidi ya mia moja walijiunga nao. Walipokuwa huko walinzi waliwatuma ndugu kadhaa waende mtoni wakajaze pipa la maji. Walinzi hawakwenda nao kwa sababu waliwaamini. Teodor alijiunga nao na akabatizwa mtoni. Kutoka Jászberény wafungwa walipelekwa hadi Bor kwa gari-moshi na mashua.
Katika kambi ya Bor kulikuwa na Wayahudi 6,000; Wasabato 14; na Mashahidi 152. Ndugu Miron anasema hivi: “Hali zilikuwa mbaya, lakini Yehova alitusaidia. Mlinzi fulani aliyetupenda alitumwa Hungaria mara kwa mara, naye alituletea vitabu. Baadhi ya Mashahidi ambao aliwajua na kuwaamini walitunza familia yake alipokuwa safarini, kwa hiyo akawa kama ndugu yao. Mtu huyo aliyekuwa luteni alituonya kulipokuwa na hatari. Kambini kulikuwa na wazee 15 wa kutaniko, kama wanavyoitwa leo, nao walipanga mikutano mitatu kila juma. Watu 80 waliihudhuria mikutano zamu zao za kazi zilipowaruhusu. Pia tuliadhimisha Ukumbusho.”
Wenye mamlaka katika kambi fulani waliwaruhusu Mashahidi wasiofungwa wawaletee ndugu zao waliokuwa wamefungwa chakula na vitu vingine. Kati ya mwaka wa 1941 na 1945, Mashahidi 40 hivi kutoka Bessarabia, Moldova, na Transylvania walipelekwa kwenye kambi ya mateso huko Şibot, Transylvania. Kila siku walifanya kazi katika kiwanda cha mbao kilichokuwa nje ya kambi. Kwa sababu chakula kilikuwa haba kambini, Mashahidi walioishi karibu na kiwanda hicho waliwaletea chakula na nguo kila juma. Ndugu waligawa vitu hivyo kulingana na uhitaji.
Ndugu hao waliwatolea wafungwa wenzao na walinzi ushahidi mzuri kwa matendo yao. Walinzi walitambua pia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wenye kutegemeka na kuaminika. Kwa hiyo, walipewa uhuru fulani ambao wafungwa wengine hawakuwa nao. Hata mlinzi mmoja huko Şibot akawa Shahidi.
Baraka Baada ya Vita
Vita vilipokwisha huko Ulaya mnamo Mei 1945, Mashahidi wote wa Yehova waliachiliwa kutoka katika magereza na kambi za kazi ngumu. Martin Magyarosi aliyekuwa na miaka 62 wakati huo alirudi Bucharest. Alipofika, alikuta kwamba ofisi ya zamani ilikuwa imeporwa kabisa. Hakuna kitu kilichobaki hata taipureta! Ripoti moja ilisema hivi: “Kazi ya Bwana ilianzishwa upya bila vifaa vyovyote vile.” Ndugu walipanga upya kazi na kutoa ombi la kuliandikisha kisheria shirika la Mashahidi wa Yehova la Rumania. Muda si muda walifanikiwa, na shirika hilo likaandikishwa kisheria Julai 11, 1945.
Jambo hilo liliwawezesha kupanga mikutano ya watu wote, makusanyiko, na uchapaji wa magazeti na vitabu. Mipango hiyo ilifanya kazi isonge mbele, na ilisaidia kumaliza migawanyiko na vurugu zilizokuwapo wakati wa marufuku. Katika mwaka wa kwanza baada ya vita, ndugu walichapa vijitabu 870,000 hivi, na zaidi ya nakala 85,500 za gazeti la Mnara wa Mlinzi, licha ya upungufu wa karatasi nchini humo! Watu 1,630 walibatizwa.
Ndugu walianza kuhubiri waziwazi hata kabla kazi haijaandikishwa kisheria. Walipanga mikutano na hotuba za pekee za watu wote. Ndugu mmoja anasema hivi kuwahusu Mashahidi katika Mkoa wa Maramureş: “Ndugu walifanya mikutano hata kabla wanajeshi hawajaondoka kabisa. Walitoka katika vijiji vyote vya eneo hilo na hawakuogopa hata kidogo. Ilikuwa pindi yenye kusisimua sana. Baadhi yao walitembea umbali wa kilometa 80 huku wakiimba na kuwahubiria watu njiani. Kila Jumapili mwenyekiti alitangaza mahali ambapo mkutano ungefanywa Jumapili iliyofuata.”
Hotuba za watu wote zilitangazwa na kutolewa katika maeneo yaliyokuwa na Mashahidi wachache na yale yasiyokuwa na Mashahidi wowote. Ndugu walitoka usiku wa manane na kutembea kilometa 100 hivi hadi kwenye maeneo hayo. Mara nyingi walitembea bila viatu kwa sababu viatu vilikuwa ghali, lakini walivibeba begani na kuvivaa kulipokuwa na baridi kali sana au hali nyingine mbaya. Kwa kawaida siku moja kabla ya mkutano, ndugu waliwatolea watu vitabu na magazeti, wakatangaza kichwa cha hotuba, na kuwaalika watu. Baada ya hotuba walirudi nyumbani kwao.
Ndugu walifanya makusanyiko mengi huko Baia-Mare, Cluj-Napoca, Tirgu-Mures, na Ocna Mureş, na mamia ya Mashahidi na watu waliopendezwa wakahudhuria. Ubatizo ndilo jambo lililovutia hasa kwenye kusanyiko lililofanywa Baia-Mare, mnamo Juni 1945, nao ulifanywa kwenye mto uliokuwa umbali wa kilometa kumi kutoka mji huo. Baada ya hotuba kutolewa katika bustani ya ndugu fulani, watu 118 walibatizwa katika Mto Lăpuşul, karibu na bustani hiyo. Ubatizo huo katika mazingira hayo mazuri ulikuwa wa pekee sana.
Mjini Tirgu-Mures, ndugu walikodi jumba la maonyesho lililotoshea watu 3,000. Baadhi ya ndugu walitembea kwa miguu na wengine wakasafiri kwa gari-moshi, magari yanayokokotwa na farasi, na baiskeli. Walifika siku iliyotangulia kusanyiko na wengine kati yao wakaanza kuhubiri mara moja na kuwaalika watu kwenye hotuba ya watu wote iliyozungumzia safina ya Noa. Ndugu wengi walitokwa na machozi walipoona kotekote mjini mabango yenye maandishi maridadi yaliyotangaza hotuba. Hawakufikiri kamwe kwamba wangekuwa na uhuru huo wa kuhubiri habari njema!
Jitihada za ndugu zilibarikiwa sana. Watu wengi sana walihudhuria hivi kwamba iliwabidi kuweka vipazasauti viwili nje kwa ajili ya wale ambao hawakupata nafasi ndani ya jumba. Jambo hilo liliwawezesha majirani wengi kusikia hotuba wakiwa kwenye madirisha yao. Wakuu wa mji na watu wengi mashuhuri walialikwa ili wajionee mwenendo wa Mashahidi wa Yehova na kusikiliza mafundisho yao. Jambo la ajabu ni kwamba sehemu iliyotengwa kwa ajili yao ilijaa, na wakajiunga na ndugu kuimba.
Kusanyiko la Kwanza la Kitaifa
Mnamo Septemba 28 na 29, 1946, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko lao la kwanza la kitaifa nchini Rumania. Lilifanywa kwenye Uwanja wa Waroma jijini Bucharest. Kampuni ya reli ilikubali kupanga gari-moshi la pekee na hata kupunguza nauli kwa nusu! Gari-moshi hilo liliwasafirisha wahudhuriaji zaidi ya 1,000 kutoka sehemu za mbali zaidi za nchi hadi Bucharest. Wengi walibeba mabango yaliyowavutia watu njiani. Hata hivyo, safari hiyo haikuwa shwari kabisa.
Makasisi walisikia kuhusu kusanyiko hilo nao wakajaribu kusimamisha gari-moshi hilo. Mashahidi walioishi Bucharest walianza kumiminika kwenye kituo cha gari-moshi mwendo wa saa 3.00 asubuhi ya Ijumaa iliyotangulia kusanyiko, wakitarajia kuwakaribisha ndugu zao kati ya saa 3:00 na saa 4:00 asubuhi hiyo. Walisubiri hadi mwendo wa saa 12:00 jioni, ndipo gari-moshi lilipofika hatimaye. Ni vigumu kueleza jinsi wageni na wale waliowakaribisha walivyosisimka walipokumbatiana. Polisi wenye silaha walikuwapo ili kudumisha amani, lakini hawakuwa na kazi.
Haikuwa rahisi kupata mahali pa kulala kwa sababu sehemu kubwa ya Bucharest pamoja na nyumba 12,000 zilikuwa zimeharibiwa wakati wa vita. Lakini ndugu hawakushindwa la kufanya. Walinunua mabua mengi sana na kuyatandaza chini kwenye bustani ya ndugu aliyeishi katika kiunga kinachoitwa Berceni. Kwa sababu kulikuwa na joto isivyo kawaida katika mwezi wa Septemba, ndugu, dada, na watoto waliohudhuria kusanyiko walilala kwa starehe kwenye godoro la mabua, nyota zikimetameta angani. Leo kuna Jumba la Ufalme maridadi mahali hapo.
Wale 3,400 waliohudhuria kusanyiko Jumamosi asubuhi walifurahi sana kusikia kwamba Mnara wa Mlinzi lilikuwa limeanza kuchapishwa tena mara mbili kwa mwezi katika Kirumania na Kihungaria. Asubuhi hiyo ndugu waligawiwa nakala 1,000 za toleo la kwanza la gazeti hilo. Kwa kipindi fulani, kila toleo lilikuwa na makala nne za funzo, ili wote wanufaike na habari walizokosa wakati wa vita.
Jumapili asubuhi ilitengwa kwa ajili ya kazi ya kuhubiri. Wahubiri walitangaza hotuba ya watu wote kotekote. Mabango yao yalikuwa na picha ya nyundo, upanga, na chuma cha kufulia. Maandishi yalisema: “‘Panga Zinafuliwa Kuwa Majembe’—Mungu Aliongoza Maneno Hayo Yaandikwe. Manabii Wawili Waliyaandika. Lakini Ni Nani Watakaotenda Kupatana Nayo?” Wahubiri waliwapa watu karatasi za mwaliko na kuwatolea magazeti waliyoyabeba katika mifuko myeupe yenye maneno, “Mashahidi wa Yehova,” “Wahubiri wa Ufalme wa Mungu,” au “Wahubiri wa Utawala wa Mungu.”
Martin Magyarosi alianza hotuba yake alasiri hiyo kwa kusema: “Leo, viongozi wa ulimwengu wanajadiliana kuhusu amani huko Paris. Hapa, kwenye kusanyiko letu kuna wahudhuriaji 15,000. Kama ungewapekua Mashahidi wa Yehova wote waliopo, hungepata upanga wala hata bunduki moja. Kwa nini? Kwa sababu sisi tumekwisha fua panga zetu kuwa majembe!” Hotuba hiyo ilikuwa yenye kuvutia na ya wakati unaofaa kwa sababu athari za vita zilionekana kila mahali.
Mkuu wa sheria, katibu mmoja wa Wizara ya Mambo ya Ndani, polisi kadhaa, na kikundi cha makasisi wa Kanisa Othodoksi walihudhuria Jumapili. Ndugu na wale wenye mamlaka walifikiri kwamba makasisi wangesababisha mchafuko kama walivyotisha kufanya. Lakini mtu mmoja tu ndiye aliyejaribu kuvuruga mkutano huo. Ndugu walimzuia walipomwona akielekea kwenye jukwaa wakati wa hotuba ya watu wote, wakashika mikono yake kwa nguvu, na kumrudisha kitini. Walimnong’onezea hivi: “Hakuna haja kwa kasisi wa Kanisa Othodoksi kuwahutubia watu hawa, lakini umekaribishwa kwa moyo wote kuketi na kusikiliza.” Hakujaribu kusababisha mchafuko tena. Baadaye, yule mkuu wa sheria alisema kwamba alifurahia hotuba zilizotolewa na kwamba alivutiwa na utaratibu wa Mashahidi wa Yehova.
Baadaye, ndugu mmoja aliandika hivi kuhusu kusanyiko hilo: “Njama ya maadui ilishindwa kabisa, na ndugu walirudi nyumbani wakiwa na shangwe nyingi.” Ndugu walikuwa na roho mpya ya amani na umoja, na hilo lilitia moyo sana kwa sababu wengi walikuja kusanyikoni wakiwa wamechanganyikiwa kwa sababu ya migawanyiko iliyotokea wakati wa vita.
Lakini mambo yaliwaendea mrama makasisi kwa sababu katika maeneo mengi watu wenye mamlaka hawakuwaunga mkono tena kuwapinga Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, bado waliendelea kuwachambua ndugu katika mahubiri yao. Baadhi yao hata waliwalipa wahuni ili wawapige wahubiri wa Ufalme, wanaume kwa wanawake, walipowaona wakihubiri. Siku moja mke wa kasisi mmoja wa Kanisa Othodoksi alimpiga dada painia kwa fimbo hadi ilipovunjika! Ripoti moja ya kipindi hicho inasema: “Tumewasilisha kesi dhidi ya makasisi wengi kama hao.”
Jitihada Nyingine za Kurudisha Umoja
Alfred Rütimann, kutoka ofisi ya tawi ya Uswisi, alitembelea Rumania kwa miezi miwili katika mwaka wa 1947. Kulikuwa na mpango wa kufanya kusanyiko, na Ndugu Hayden C. Covington kutoka makao makuu alikuwa aandamane na Ndugu Rütimann katika safari zake. Hata hivyo, wenye mamlaka hawakuwaruhusu ndugu kufanya kusanyiko, wala hawakumpa Ndugu Covington kibali cha kuingia nchini. Lakini Alfred Rütimann alipata kibali cha miezi miwili, naye akatembelea Rumania mwezi wa Agosti na Septemba.
Kwanza alienda Bucharest, ambako ndugu na dada wenye furaha walimkaribisha kwenye uwanja wa ndege kwa kumpa shada maridadi la maua. Walimpeleka kwenye ofisi ya Bucharest iliyokuwa nyumbani kwa mtu aliyependezwa kwenye Barabara ya Alion, Na. 38. Ofisi ilihamishiwa huko mnamo Januari 1947. Hata hivyo, kwa sababu ya uhasama wa Wakomunisti, anwani rasmi ya ofisi ilibaki kuwa Barabara ya Basarabia, Na. 38. Ofisi hiyo ilikodiwa mnamo Julai 1945, na ilikuwa na meza kuukuu, kiti, taipureta ambayo haikufanya kazi, na kabati iliyojaa magazeti na vijitabu vilivyokuwa vimechakaa. Kazi haingezuiwa hata kama vitu hivyo vingechukuliwa. Dada fulani alifanya kazi katika ofisi hiyo mara mojamoja.
Ndugu Rütimann alifanya mkutano pamoja na Pamfil Albu, msimamizi wa shirika la kisheria, na Martin Magyarosi, aliyesimamia kazi wakati huo. Ndugu hao wawili walikuwa pia waangalizi wa wilaya. Mawasiliano yalikuwa yamezuiwa kwa miaka kadhaa, na ndugu Warumania walisisimka sana kusikia kuhusu maendeleo katika tengenezo la Yehova, kama vile kuanzishwa kwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Shule ya Gileadi ya kuwazoeza wamishonari. Bila shaka wote walitaka Shule ya Kitheokrasi ianzishwe nchini Rumania. Ndugu walipanga mara moja yale masomo 90 ya kitabu cha shule (Theocratic Aid to Kingdom Publishers) yachapwe hatua kwa hatua katika Kirumania na Kihungaria.
Hata hivyo, kusudi kuu la ziara ya Ndugu Rütimann lilikuwa kutembelea makutaniko na vikundi vingi iwezekanavyo ili awatolee ndugu hotuba muhimu za kusanyiko walilokosa. Kwa hiyo, yeye na Ndugu Magyarosi aliyekuwa mfasiri wake, walifunga safari ya kwenda kwenye maeneo mawili ambako kulikuwa na ndugu wengi zaidi. Walianzia Transylvania.
Transylvania na Maeneo ya Mbali Zaidi
Wahubiri huko Transylvania, kama katika karibu sehemu nyingine zote, walijitahidi sana kuhudhuria hiyo mikutano ya pekee. Kwa sababu wageni hao wawili walikuwa na mengi ya kufanya, akina ndugu walikuwa tayari kukesha hadi usiku sana. Kwa mfano, ijapokuwa hotuba zilianza saa 4:00 usiku na kuendelea hadi saa 8:00 katika kijiji cha Vama Buzăului, hakuna hata mmoja kati ya wale wasikilizaji 75 aliyelalamika.
Alfred Rütimann aliandika hivi baadaye: “Maoni ya watu hao juu ya wakati yanatofautiana sana na maoni ya Waswisi. Wako tayari kuamka saa 8:00 usiku au hata saa 9:00 ili wawakaribishe wageni, nao hawazingatii sana wakati! Ijapokuwa nyakati nyingine wao hutembea mbali sana bila viatu, ni kana kwamba wana wakati mwingi kuliko sisi na hawana haraka. Kwanza nilifikiri si jambo la hekima kupanga mkutano usiku sana, lakini Ndugu Magyarosi akanihakikishia kwamba ni sawa.”
Mkutano uliofuata ulifanyiwa mjini Tirgu-Mures, nao ulikuwa na watu 31,000. Mji huo pia uliathiriwa sana na vita na karibu madaraja yote yalikuwa yameharibika. Hata hivyo, ndugu 700 kutoka makutaniko 25 walisafiri umbali wa kilometa 50 hivi hadi sehemu ya msitu isiyo na miti karibu na mji ambako mkutano ulifanyiwa.
Ndugu hao walienda pia Cluj-Napoca, ambako watu 300 kutoka makutaniko 48 walikuwa wamekusanyika. Walipokuwa mjini humo, Ndugu Magyarosi alimwonyesha Ndugu Rütimann kiwanda cha uchapaji kilichopotezwa mwaka wa 1928 kwa sababu ya Jacob Sima. Ni nini kilichompata? Ndugu Rütimann alisema hivi katika ripoti yake: “Alikufa mwaka uliopita. Alikuwa mlevi.”
Baadaye walienda Satu-Mare na Sighet Marmaţiei, karibu na Ukrainia. Kulikuwa na zaidi ya makutaniko 40 ya Kirumania, Kihungaria, na Kiukrainia katika eneo hilo. Wakulima na watu wengine katika vijiji vya eneo hilo walijitegemea, kwa kuwa walikula mazao ya mashamba yao, nao walifuga wanyama, hasa kondoo. Walipanda vilevile mimea inayotumiwa kutengeneza nyuzi za kitani na katani. Walijitengenezea mavazi na mablanketi, na kulainisha ngozi walizotumia. Fundi fulani kijijini aliwashonea viatu. Ndugu na dada wengi walihudhuria mikutano hiyo ya pekee wakiwa wamevalia mavazi yao ya kitamaduni ya kitani na katani yenye mapambo.
Baadaye, Ndugu Rütimann na Ndugu Magyarosi walienda Moldavia, kaskazini-mashariki mwa Rumania. Kwanza walienda kijijini Frătăuţii, ambako ndugu walikuwa wakarimu sana licha ya umaskini. Waliwasha taa za mafuta na kuwapa wageni wao maziwa, mkate, sima, na mayai yaliyochemshwa na kutumbukizwa katika siagi. Wote walitumia mabakuli madogo. Ndugu Rütimann aliandika: “Chakula hicho kilikuwa kitamu sana.” Ili wasisikie baridi usiku huo, wageni walilala jikoni katika vitanda vilivyowekwa karibu na joko. Wenye nyumba walilala jikoni pia kwenye magunia yenye mabua.
Mashahidi kwenye eneo hilo walihubiri kwa bidii na Yehova aliwabariki sana kama ripoti zinavyoonyesha. Mapema mwaka wa 1945 kulikuwa na wahubiri 33 katika eneo hilo. Katika miaka miwili iliyofuata idadi yao iliongezeka mara kumi hadi 350!
Ndugu hao walihisi kwamba kwa kweli walikuwa mashambani waliposafiri umbali wa kilometa 120 hadi Bălcăuţi na Ivăncăuţi kwa gari lililokokotwa na farasi wawili. Ndugu mmoja aliandika: “Farasi wadogo wa Rumania ni wazuri sana na wanaweza kutembea hata kwenye barabara mbovu kabisa, mchana au usiku.” Kutaniko la Bălcăuţi lilianzishwa mwaka wa 1945. Hapo awali wahubiri wote wa kutaniko hilo walikuwa wafuasi wa kanisa fulani la kiinjili, na mtumishi wa kutaniko alikuwa mhubiri wa kanisa hilo. Kwa sababu ya mvua, mkutano ulifanywa katika nyumba ya ndugu huko Ivăncăuţi. Lakini hilo halikuwasumbua wale wasikilizaji 170, ambao baadhi yao walikuwa wametembea bila viatu umbali wa kilometa 30 ili wafike.
Ndugu hao wawili walitoa hotuba katika miji 19, na wahubiri na watu waliopendezwa 4,504 kutoka makutaniko 259 walihudhuria. Kabla ya kurudi Uswisi, Alfred Rütimann alitoa hotuba pia huko Orăştie na Arad, na ndugu kadhaa walitembea umbali wa kilometa 60 hadi 80 ili kusikiliza hotuba hizo. Mkulima mmoja mwenye umri wa miaka 60 alithamini mpango huo sana hivi kwamba alitembea bila viatu umbali wa kilometa 100 ili ahudhurie!
Mikutano hiyo ya pekee ilikuwa muhimu sana na ya wakati unaofaa nchini Rumania kwa sababu ndugu walihitaji kutiwa moyo na mashamba ya kiroho yalikuwa tayari kuvunwa. Warumania walikuwa wamechoshwa na watawala wakandamizaji na taabu za vita, na wengi walikuwa wameacha kuzitumaini dini. Isitoshe, thamani ya pesa iliposhuka sana mnamo Agosti 1947, wengi wakawa maskini ghafula. Kwa hiyo, wengi waliopinga ujumbe wa Ufalme awali, walikuwa tayari kusikiliza.
Mikutano hiyo ilifaa pia kwa sababu muda usio mrefu, mateso makali zaidi yangeanza. Mateso hayo yalichochewa na itikadi ya kwamba hakuna Mungu na pia na viongozi wakatili wasiokubali uhuru wa dini, nayo yangeendelea kwa miaka 40 hivi!
Wakomunisti Waanza Kutawala Rumania
Wakomunisti walianza kutawala Rumania mnamo Novemba 1946, mwaka mmoja kabla ya ziara ya Alfred Rütimann. Chama hicho kilimaliza upinzani wote katika miaka michache iliyofuata, na kuharakisha mabadiliko ili utamaduni na siasa nchini Rumania zipatane na sera za Sovieti.
Katika kipindi hicho cha amani ndugu walichapa mamia ya maelfu ya magazeti, vijitabu, na vitabu vinginevyo, na kuvipeleka kwenye vituo 20 kotekote nchini. Wakati huohuo, wengi waliongeza utumishi wao na baadhi yao kama vile Mihai Nistor na Vasile Sabadâş wakawa mapainia.
Mihai alitumwa kaskazini-magharibi na katikati ya Transylvania, naye aliendelea kuwa painia hata baada ya marufuku ya Wakomunisti kuondolewa. Alisakwa na maadui kwa miaka mingi wakati wa marufuku. Aliepukaje kukamatwa? Anasema: “Nilitengeneza mfuko uliofanana na ile iliyotumiwa na watu waliouza madirisha. Nilizunguka katikati ya vijiji na miji katika maeneo niliyohubiri nikiwa nimevaa mavazi ya kazi na kubeba viunzi vya madirisha na vyombo vya kazi. Kila nilipomwona polisi au mtu niliyemshuku, nilitangaza madirisha yangu kwa sauti kubwa. Ndugu wengine walitumia mbinu tofauti ili wawaepuke wapinzani. Kazi hiyo ilikuwa yenye kusisimua, lakini ilikuwa hatari kwetu na kwa watu waliotukaribisha tukae nyumbani kwao. Hata hivyo, tulifurahi sana kuwaona wanafunzi wa Biblia wakifanya maendeleo na idadi ya wahubiri ikiongezeka.”
Vasile Sabadâş pia aliendelea kuwa painia ijapokuwa alilazimika kuhama mara nyingi. Alisaidia hasa kuwatafuta na kuwasaidia ndugu waliotawanywa na Idara ya Usalama ya serikali mpya ya Kikomunisti. Vasile alisema: “Ili nisikamatwe ilinibidi kujihadhari na kubuni mbinu mpya. Kwa mfano, nilipotaka kusafiri hadi sehemu nyingine ya nchi, nilitafuta sababu hususa za kusafiri, kama vile pendekezo la daktari la kwenda mahali fulani kutibiwa.
“Kwa sababu sikushukiwa, nilifaulu kupata njia za kuwasiliana na ndugu ili wapate chakula cha kiroho kwa ukawaida. Andiko lililonichochea ni Isaya 6:8: ‘Mimi hapa! Nitume mimi,’ na pia Mathayo 6:33: ‘Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme.’ Maandiko hayo yalinipa shangwe na kunitia nguvu kuvumilia.” Vasile alihitaji sifa hizo, kwa sababu licha ya kujihadhari, hatimaye angekamatwa kama wengine wengi.
Mashambulizi ya Kijeuri Dhidi ya Tengenezo la Mungu
Kufikia mwaka wa 1948, ilikuwa vigumu zaidi kuwasiliana na makao makuu, kwa hiyo, ndugu waliwasiliana kwa kuandika ujumbe wa lugha ya siri kwenye kadi za posta. Kwa mfano, mnamo Mei 1949, Martin Magyarosi alituma ujumbe ulioandikwa na Petre Ranca, mfanyakazi mwenzake katika ofisi ya Bucharest. Alisema: “Watu wote wa familia ni wazima. Kulikuwa na upepo na baridi kali, nasi hatukuweza kufanya kazi shambani.” Baadaye ndugu mwingine aliandika kwamba “jamaa haiwezi kupata vyakula vitamu” na kwamba “wengi ni wagonjwa.” Alimaanisha kwamba haikuwezekana kuingiza chakula cha kiroho nchini Rumania, na ndugu wengi walikuwa wamefungwa.
Baada ya agizo la Wizara ya Sheria kutolewa Agosti 8, 1949, ofisi na makao ya Bucharest yalifungwa na vifaa vyote vikachukuliwa, hata vitu vya kibinafsi. Mamia ya ndugu walikamatwa na kuadhibiwa katika miaka iliyofuata. Wafashisti walipotawala, Mashahidi wa Yehova walishtakiwa kwa uwongo kuwa Wakomunisti, lakini Wakomunisti walipoanza kutawala, ndugu walibandikwa jina “mabeberu” na kushtakiwa isivyofaa kwa kueneza propaganda ya Marekani.”
Wapelelezi na watoa-habari walikuwa kila mahali. Kitabu cha Mwaka cha 1953 kilisema kwamba Wakomunisti wamechukua hatua “kali sana hivi kwamba mtu yeyote huku Rumania anayepokea barua kutoka nchi za Magharibi hutiwa kwenye orodha ya watu wasiotakiwa na kupelelezwa sana.” Ripoti hiyo inasema pia: “Ni vigumu kuwazia woga uliopo. Hata watu katika familia hawatumainiani. Uhuru umetoweka kabisa.”
Pamfil na Elena Albu, Petre Ranca, Martin Magyarosi, na wengine wengi walikamatwa mapema mwaka wa 1950 na kushtakiwa kwa uwongo kuwa wapelelezi wa Marekani na nchi za Ulaya zisizo za Kikomunisti. Baadhi yao walitendwa kikatili ili wafunue mambo ya siri na wakiri kwamba wao ni “wapelelezi.” Hata hivyo, hawakukiri chochote ila kwamba wanamwabudu Yehova na kufanya kazi ya Ufalme wake. Baada ya kutendwa kwa jeuri, baadhi ya ndugu walifungwa gerezani, na wengine wakapelekwa kwenye kambi za kazi ngumu. Je, mateso hayo yaliathiri kazi ya kuhubiri? Mwaka huo, yaani 1950, idadi ya wahubiri iliongezeka kwa asilimia 8. Bila shaka hilo linaonyesha nguvu za roho ya Mungu!
Ndugu Magyarosi alipokuwa anakaribia miaka 70, alipelekwa kwenye gereza la Gherla huko Transylvania, ambako alifia mwishoni mwa mwaka wa 1951. Ripoti moja ilisema: “Alivumilia mateso mengi makali kwa ajili ya kweli, hasa tangu akamatwe mnamo Januari 1950. Sasa hateseki tena.” Naam, kwa miaka 20 hivi, Martin alivumilia mashambulizi ya ukatili ya makasisi, Wafashisti, na Wakomunisti. Utimilifu wake unatukumbusha maneno haya ya mtume Paulo: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.” (2 Tim. 4:7) Mkewe Maria, hakukamatwa kamwe, hata hivyo, alikuwa mfano mzuri kwa kuvumilia mateso mengi. Ndugu mmoja anasema kwamba Maria “alikuwa dada mwenye akili, aliyejitoa kabisa katika kazi ya Bwana.” Baada ya Martin kukamatwa, Maria alitunzwa na watu wa ukoo. Mmoja aliyemtunza ni binti yake, Mărioara, ambaye pia alifungwa na kuachiliwa mwaka wa 1955.
“Mashahidi wa Yehova Ni Watu Wazuri”
Serikali ilitoa msamaha mwaka wa 1955, na karibu ndugu wote wakaachiliwa. Lakini uhuru wao haukudumu kwa muda mrefu. Tangu mwaka wa 1957 hadi 1964, Mashahidi wa Yehova walisakwa na kukamatwa tena, na baadhi yao wakahukumiwa kifungo cha maisha. Hata hivyo, ndugu waliofungwa hawakukata tamaa bali walitiana moyo ili wasimame imara. Walijulikana kwa maadili yao na uaminifu wao. Mtu fulani aliyefungwa kwa sababu za kisiasa, alisema: “Mashahidi wa Yehova ni watu wazuri, ambao hawakusalimu amri wala kukana dini yao.” Aliongeza kwamba katika gereza alimofungwa, Mashahidi walikuwa “wafungwa waliopendwa kuliko wengine wote.”
Msamaha mwingine ulitangazwa mwaka wa 1964. Lakini uhuru haukudumu hata wakati huo. Wengi walikamatwa tena kati ya mwaka wa 1968 na 1974. Ndugu mmoja aliandika: “Tunateseka na kudhihakiwa kwa sababu tunahubiri Injili. Tafadhali waombeeni ndugu zetu waliofungwa. Tunajua kwamba ni lazima tuvumilie majaribu hayo. Hata hivyo, tutaendelea kuhubiri habari njema kwa ujasiri kama Mathayo 24:14 linavyotabiri. Tunawasihi kwa moyo wote, msitusahau!” Kama tutakavyoona, Yehova alisikia sala ambazo washikamanifu walitoa kwa moyo wote na kwa machozi, naye akawafariji kwa njia tofauti-tofauti.
Shetani Apanda Mbegu za Shaka
Ibilisi huwatumia watu wa nje na pia ndugu wasio waaminifu kuwashambulia watumishi wa Mungu. Kwa mfano, ndugu fulani waliokuwa na madaraka ya usimamizi kabla ya kufungwa, hawakupewa tena madaraka hayo walipoachiliwa mwaka wa 1955. Waliudhika nao wakajaribu kupanda mbegu za fitina. Inahuzunisha kwamba ingawa walisimama imara gerezani, walipoachiliwa walishindwa kuendelea kusimama imara kwa sababu ya kiburi! Ndugu mmoja mashuhuri alishirikiana na maofisa wa Idara ya Usalama ili aepuke kuadhibiwa. Tendo hilo liliwadhuru sana ndugu waaminifu na kazi ya kuhubiri.—Mt. 24:10.
Watu wa Mungu walihitaji kushughulikia pia matatizo yaliyosababishwa na maoni yaliyotofautiana juu ya mambo ambayo kila mmoja alipaswa kujiamulia kupatana na dhamiri. Kwa mfano, walipokamatwa, mara nyingi ndugu waliambiwa wachague kati ya kwenda gerezani au kufanya kazi katika migodi ya chumvi. Baadhi yao walihisi kwamba wale waliochagua kufanya kazi katika migodi walivunja kanuni za Biblia. Wengine walisisitiza kwamba dada hawapaswi kutumia vipodozi na ni kosa kutazama sinema au michezo ya kuigiza, au hata kuwa na redio.
Lakini ndugu wengi hawakusahau kamwe kwamba jambo muhimu ni kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu. Jambo hilo linaonekana wazi katika ripoti ya mwaka wa 1958 inayoonyesha kwamba wahubiri 5,288 walishiriki katika kazi ya kuhubiri. Hilo ni ongezeko la wahubiri 1,000 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia! Pia, watu 8,549 walihudhuria Ukumbusho, na 395 wakabatizwa.
Walikabili jaribu lingine kuanzia mwaka wa 1962, wakati Mnara wa Mlinzi lilipoonyesha kwamba “mamlaka zilizo kubwa” zinazotajwa katika Waroma 13:1 ni mamlaka za kiserikali za wanadamu, na si Yehova Mungu wala Yesu Kristo kama ilivyoaminiwa hapo awali. Ilikuwa vigumu kwa ndugu wengi huko Rumania kukubali maoni hayo mapya kwa sababu walikuwa wameteswa sana na watawala wakatili. Hata wengine kati yao waliamini kwamba hiyo ilikuwa mbinu ya Wakomunisti ya kuwadanganya ili watii kabisa Serikali, kinyume cha kanuni inayoonyeshwa katika Mathayo 22:21.
Ndugu mmoja aliongea na Shahidi mwenzake aliyekuwa ametembelea Berlin, Roma, na majiji mengineyo. Anasema: “Msafiri huyo alithibitisha kwamba maoni hayo mapya hayakuwa mbinu ya Wakomunisti, bali chakula cha kiroho kutoka kwa jamii ya mtumwa. Hata hivyo, bado nilikuwa na shaka, kwa hiyo, nikamuuliza mwangalizi wa wilaya tufanye nini.”
Alinijibu hivi: “Tusonge mbele katika utumishi, hilo ndilo tunalopaswa kufanya!”
“Huo ulikuwa ushauri mzuri, na ninafurahi kusema kwamba bado ‘ninasonga mbele.’”
Licha ya matatizo makubwa ya mawasiliano, ndugu kwenye makao makuu na kwenye ofisi ya tawi iliyosimamia kazi nchini Rumania, walijitahidi sana kuwajulisha ndugu kweli zilizofunuliwa na kuwasaidia kufanya kazi pamoja kama familia ya kiroho yenye umoja. Kwa kusudi hilo, waliandika barua na makala za Huduma Yetu ya Ufalme zilizofaa hali hizo.
Watu wa Yehova walipataje chakula hicho cha kiroho? Kila ndugu katika Halmashauri ya Nchi aliwasiliana kisiri na waangalizi wanaosafiri na wazee wa makutaniko kupitia ndugu na dada waaminifu waliopeleka barua na ripoti kwenye ofisi nchini Uswisi. Kwa hiyo, ndugu walipata kwa kadiri fulani chakula cha kiroho na mwongozo kutoka kwa tengenezo la Yehova.
Ndugu na dada waaminifu walijitahidi pia kuendeleza umoja katika makutaniko na vikundi vyao. Mmoja wao ni Iosif Jucan, ambaye alizoea kusema hivi: “Hatuwezi kuokoka Har–Magedoni tusipoendelea kujilisha chakula cha kiroho na kukaa karibu na ‘Mama.’” Alimaanisha kwamba ni muhimu kubaki karibu na sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Ndugu wengi kama yeye waliwasaidia sana watu wa Mungu nao walikuwa ulinzi dhidi ya wale waliojaribu kuharibu umoja.
Mbinu za Maadui
Ili kujaribu kudhoofisha imani ya watumishi wa Yehova au kuwatiisha, Wakomunisti walitumia wapelelezi, ndugu wa uwongo, mateso, habari zisizo za kweli, tishio la kuuawa, na waasi-imani. Wapelelezi na wale waliowapasha wenye mamlaka habari walikuwa watu kama vile majirani, wafanyakazi wenzi, waasi-imani, watu wa familia, na maofisa wa Idara ya Usalama. Maofisa hao hata walijiingiza makutanikoni kwa kujifanya kuwa watu wanaopendezwa na kweli na wakajifunza maneno yanayotumiwa na watu wa Mungu kuhusiana na mambo ya kiroho. ‘Ndugu hao wa uwongo’ walisababisha madhara mengi na pia wakasababisha ndugu wengi wakamatwe. Mmoja wa ndugu hao wa uwongo ni Savu Gabor. Alikuwa na madaraka kutanikoni, naye alifichuliwa mwaka wa 1969.—Gal. 2:4.
Maofisa wa serikali walipeleleza pia familia na mtu mmoja-mmoja kwa kutumia vifaa vya kunasa sauti. Timotei Lazăr anasema: “Nilipokuwa gerezani kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi, mara kwa mara maofisa wa Idara ya Usalama waliwaita wazazi wangu na ndugu yangu mdogo kwenye makao yao makuu na kuwahoji kwa muda wa saa sita hivi. Siku moja waliweka vifaa vya kunasa sauti nyumbani kwetu. Jioni hiyo ndugu yangu ambaye ni fundi wa umeme aliona kwamba kifaa cha kupimia umeme kilizunguka haraka isivyo kawaida. Alitafuta-tafuta na akagundua vifaa viwili vya kunasa sauti ambavyo alivipiga picha na kuviondoa. Kesho yake maofisa wa Idara ya Usalama walikuja kuitisha vitu vyao vya kuchezea, kama walivyoviita.”
Mara nyingi, makala zilizokuwa zimechapishwa katika nchi nyingine za Kikomunisti zilichapishwa upya Rumania ili kueneza habari za uwongo nchini humo. Kwa mfano, makala “Madhehebu ya Mashahidi wa Yehova Yenye Kupinga Maendeleo” ilikuwa imechapishwa kwanza katika gazeti fulani la Urusi. Katika makala hiyo, Mashahidi wa Yehova walishtakiwa kwa uwongo kuwa “shirika la siasa” ambalo “linachochea maasi katika nchi za Kisoshialisti.” Iliwasihi wasomaji wafichue majina ya wote wanaounga mkono mafundisho ya Mashahidi. Hata hivyo, watu wenye akili waliona kuwa habari hizo za kisiasa zilionyesha kwamba wapinzani walikuwa wameshindwa, kwani bado Mashahidi wa Yehova walikuwapo na bila shaka waliendelea kuhubiri.
Wakati maofisa wa Idara ya Usalama walipomkamata ndugu au dada walimtesa kwa ukatili mno. Ili kuwalazimisha waliokamatwa waongee hata walitumia dawa zilizoathiri akili na mfumo wa neva. Ndugu Samoilă Bărăian aliyepewa dawa hizo anasema: “Baada ya kuanza kunihoji, walinilazimisha kunywa dawa zilizonidhuru zaidi kuliko kupigwa. Punde nilitambua kwamba nimeathiriwa sana. Sikuweza kutembea vizuri wala kupanda ngazi. Halafu nikaanza kukosa usingizi. Sikuweza kukaza fikira wala kuongea sawasawa.
“Afya yangu iliendelea kuzorota. Baada ya mwezi mmoja hivi nilipoteza uwezo wa kunusa. Tumbo langu liliharibika, na nilihisi kana kwamba viungo vyangu vyote vilikuwa vimeteguka. Nilikuwa na maumivu makali. Miguu yangu ilitokwa na jasho sana hivi kwamba viatu vyangu viliharibika baada ya miezi miwili tu na nikalazimika kuvitupa. Mara kwa mara yule aliyenihoji alipaaza sauti hivi: ‘Kwa nini unasema uwongo? Huoni hali yako?’ Nilikuwa karibu kufoka kwa hasira na ilinibidi kujizuia sana.” Ndugu Bărăian alipona kabisa hatimaye.
Maofisa wa Idara ya Usalama waliwatesa pia kiakili na kihisia. Alexa Boiciuc anasema: “Usiku mmoja niliamshwa na kupelekwa kwenye jumba ambako nilisikia ndugu akipigwa. Baadaye nilisikia dada akilia, kisha nikasikia sauti ya mama yangu. Huo ulikuwa usiku mbaya zaidi kwangu. Ingalikuwa afadhali wanipige mimi.”
Ndugu waliambiwa watasamehewa wakifunua majina ya Mashahidi wengine na pia wakati na mahali pa mikutano. Wake walichochewa kuwaacha waume wao waliofungwa ili watoto wao wawe na maisha bora.
Kwa sababu Serikali ilikuwa imewanyang’anya mali zao, iliwabidi ndugu wengi kufanya kazi kwenye mashamba ya umma. Kazi haikuwa ngumu sana, lakini wanaume walipaswa kuhudhuria mikutano ya kisiasa, iliyofanywa mara kwa mara. Wale ambao hawakuhudhuria walidhihakiwa na mishahara yao ikapunguzwa kabisa. Ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova waliteseka, kwa kuwa hawakuhudhuria mikutano hiyo wala kushiriki katika mambo mengine ya kisiasa.
Maofisa wa serikali walipopekua nyumba za Mashahidi, walipora mali zao, hasa vitu ambavyo wangeweza kuviuza. Na mara nyingi katika majira ya baridi kali waliharibu majiko yaliyotumiwa kupasha nyumba joto. Kwa nini waliyaharibu majiko hayo? Walisema kwamba waliyaharibu kwa sababu yalikuwa maficho mazuri ya vitabu. Hata hivyo ndugu hawakuacha kuhubiri, na kama tutakavyoona, hata wale walioteseka katika kambi za kazi ngumu na magereza waliendelea kufarijiana na kutoa ushahidi kumhusu Yehova.
Kumsifu Yehova Katika Kambi na Magereza
Mbali na magereza, Rumania ilikuwa na kambi tatu kubwa za kazi ngumu. Moja ilikuwa karibu na mlango wa Mto Danube, nyingine kwenye Kisiwa Kikubwa cha Braila, na ile ya tatu ilikuwa karibu na mfereji unaounganisha Mto Danube na Bahari Nyeusi. Mwanzoni mwa utawala wa Wakomunisti, Mashahidi waliofungwa walijikuta mara nyingi pamoja na watu waliowatesa hapo awali, ambao walikamatwa kwa sababu waliunga mkono serikali ya zamani. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alijikuta pamoja na makasisi 20! Haikosi walikuwa na mazungumzo yenye kusisimua.
Kwa mfano, ndugu katika gereza moja aliongea kwa undani na profesa wa dini ambaye hapo awali aliwahoji watu waliotaka kusomea ukasisi. Ndugu alitambua mara moja kwamba profesa huyo hakujua chochote kuhusu Biblia. Mkuu wa jeshi wa ile serikali iliyoanguka alikuwa miongoni mwa wafungwa waliosikiliza.
Mkuu huyo wa jeshi alimuuliza yule profesa: “Inakuwaje kwamba mafundi wanajua Biblia vizuri kuliko wewe?”
Yule profesa akajibu: “Kwenye vyuo vikuu vya dini tunafundishwa desturi za kanisa na mambo mengineyo, lakini si Biblia.”
Huyo mkuu wa jeshi hakuvutiwa, kwa hiyo akasema: “Tulitegemea ujuzi wako, lakini sasa ninaona kwamba tumedanganyika vibaya sana.”
Hatimaye, wafungwa kadhaa walikubali kweli na wakajiweka wakfu kwa Yehova, akiwemo mtu mmoja aliyekuwa amehukumiwa kifungo cha miaka 75 kwa wizi. Utu wa mtu huyo ulibadilika sana hivi kwamba wenye mamlaka gerezani walitambua mabadiliko hayo, nao wakampa kazi mpya ambayo kwa kawaida mtu ambaye amefungwa kwa wizi hangepewa. Alipewa kazi ya kwenda mjini bila mlinzi kununua vitu vilivyohitajika gerezani!
Hata hivyo, maisha yalikuwa magumu gerezani na chakula kilikuwa haba. Wafungwa hata waliomba viazi vyao visitolewe maganda. Walikula pia viazi-sukari, nyasi, majani, na mimea mingineyo ili tu kujaza tumbo. Wafungwa kadhaa walikufa hatimaye kwa sababu ya kukosa chakula kizuri na wote waliugua ugonjwa wa kuhara damu.
Katika majira ya kiangazi ndugu walioishi karibu na mlango wa Mto Danube walichimba na kuhamisha udongo kwa ajili ya ujenzi wa bwawa fulani. Katika majira ya baridi kali walifanya kazi ya kukata matete wakisimama juu ya barafu mtoni. Walilala katika meli kuukuu ya chuma nao wakavumilia baridi, uchafu, chawa, na walinzi wasio na huruma ambao hawakujali hata mfungwa alipokufa. Lakini katika hali yoyote ile, ndugu walitiana moyo na kusaidiana kudumisha nguvu za kiroho. Fikiria kilichompata Dionisie Vârciu.
Kabla tu ya kuachiliwa, ofisa mmoja alimuuliza Dionisie: “Je, kifungo chako kimebadili imani yako, Vârciu?”
Dionisie akajibu: “Samahani! Je, wewe ungebadili suti bora kwa suti duni?”
Ofisa huyo akajibu: “La.”
Dionisie akasema: “Vivyo hivyo, gerezani humu hakuna mtu hata mmoja aliyenipa chochote kilicho bora kuliko imani yangu. Kwa nini basi niibadili?”
Ndipo ofisa huyo akampa Dionisie mkono na kusema: “U huru Vârciu. Usiache imani yako.”
Ndugu na dada kama Dionisie ni wanadamu tu. Ujasiri na nguvu zao za kiroho zilitokana na imani katika Yehova, waliyoidumisha kwa njia za ajabu.—Met. 3:5, 6; Flp. 4:13.
Kujifunza kwa Kutegemea Kumbukumbu
András Molnos anasema hivi: “Nilipata mazoea mazuri ya kiroho gerezani.” Vipi? Aliona umuhimu wa kukusanyika pamoja na ndugu kila juma ili kujifunza Neno la Mungu. András anasema: “Mara nyingi, hatukuwa na vitabu wala magazeti, kwa hiyo tulitegemea kumbukumbu. Ndugu walijitahidi kukumbuka makala za Mnara wa Mlinzi walizojifunza kabla ya kufungwa. Ndugu wachache walikumbuka kila kitu katika gazeti, hata maswali ya makala za funzo!” Baadhi yao walikumbuka vizuri makala hizo kwa sababu walikuwa wamezinakili kwa mkono kabla ya kukamatwa.—Ona sanduku, “Njia za Kufanya Nakala,” kwenye ukurasa wa 132-133.
Walipopanga mikutano ya Kikristo ndugu wenye madaraka walitangaza habari ambayo ingezungumziwa, na kila mfungwa alijitahidi kukumbuka yote aliyojua kuhusu habari hiyo kama vile maandiko na mambo aliyokuwa amesoma katika vitabu vya Kikristo vya kujifunzia Biblia. Hatimaye, wote walikutana ili kuzungumzia habari hizo. Kiongozi aliyeteuliwa kwenye mkutano alifungua kwa sala na kuongoza mazungumzo kwa kuuliza maswali. Baada ya wengine wote kutoa maelezo, ndugu huyo alitoa maelezo yake, kisha akauliza swali lingine.
Majadiliano kama hayo hayakuruhusiwa katika magereza fulani. Lakini ndugu hawakushindwa kujifunza. Ndugu mmoja anasema hivi: “Tulikuwa tukitoa kioo cha dirisha la bafu, na kukipaka mchanganyiko wa maji, sabuni, na chokaa tuliyokuwa tumetoa ukutani. Kilipokauka, tuliandika somo la siku hiyo kwenye kioo hicho. Ndugu mmoja alinong’ona maneno, huku mwingine akiyaandika.
“Tulikaa katika seli kadhaa za gereza, na vikundi vya funzo vilipangwa katika seli hizo. Kila somo lilipitishwa kutoka ndugu mmoja hadi mwingine katika ile seli yenye kioo. Ndugu katika zile seli nyingine walipataje habari hizo? Mmoja wetu aliziwasilisha kwa mfumo wa mawasiliano wa Morse kwa kugongagonga polepole ukuta au mabomba ya kupasha joto. Wakati huohuo, kila ndugu katika zile seli nyingine alitumia kikombe chake kama kifaa cha kukuza sauti kwa kukiweka ukutani au kwenye mabomba na kuweka sikio kwenye kikombe hicho. Wale ambao hawakujua mfumo wa Morse hawakuwa na budi kujifunza mfumo huo.”
Ndugu katika magereza fulani waliletewa chakula cha kiroho na dada wenye akili waliobuni mbinu mbalimbali. Kwa mfano, walipooka mikate dada hao walificha magazeti au vijitabu ndani ya donge. Ndugu waliita chakula hicho mkate kutoka mbinguni. Akina dada waliingiza hata sehemu za Biblia magerezani kwa kukunja-kunja kurasa za Biblia na kuziweka ndani ya mipira midogo ya plastiki kisha kuipaka rojo ya chokoleti na kakao.
Hata hivyo, ndugu waliweza kusoma tu walipoenda chooni. Hakuna mahali pengine ambapo askari waliwaruhusu kuwa peke yao hata kwa dakika chache. Baada ya kusoma, walificha kile walichosoma nyuma ya tangi la maji la choo. Hata wafungwa wasiokuwa Mashahidi walijua maficho hayo, na wengi wao walifurahia kusoma kwa utulivu pia.
Wanawake na Watoto Wadumisha Utimilifu
Viorica na Aurica Filip walinyanyaswa na watu wa familia yao, sawa na Mashahidi wengine wengi. Wasichana hao walikuwa na ndugu saba na dada mmoja. Viorica anasema hivi: “Kwa sababu Aurica alitamani kumtumikia Yehova, alilazimika kuacha chuo kikuu cha Cluj-Napoca mwaka wa 1973, naye akabatizwa muda mfupi baadaye. Nilipendezwa nilipoona bidii yake isiyo na unafiki, nami nikaanza kujifunza Neno la Mungu. Nilipojifunza juu ya ahadi ya Mungu ya uzima wa milele katika paradiso duniani, nilijiuliza, ‘Kweli kuna jambo bora kuliko hili?’ Nilipoendelea kujifunza, nilianza kufuata kanuni za Biblia kuhusu kutounga mkono siasa, na nikakataa kujiunga na Chama cha Kikomunisti.”
Viorica anaongeza: “Nilijiweka wakfu kwa Yehova mwaka wa 1975. Nilikuwa nimehama nyumbani na niliishi na mtu wa ukoo katika mji wa Sighet Marmaţiei, ambako nilifanya kazi ya ualimu. Kwa sababu sikuunga mkono siasa, wakuu wa shule waliniambia kwamba ningeachishwa kazi mwishoni mwa mwaka huo wa masomo. Watu wa familia yetu hawakutaka nifutwe kazi, kwa hiyo walianza kuninyanyasa mimi na dada yangu.”
Hata watoto wa shule walitishwa, nyakati nyingine na maofisa wa Idara ya Usalama. Mbali na kuteswa kimwili na kutukanwa, wengi walifukuzwa shuleni na kulazimishwa kutafuta shule nyingine. Wengine nao walizuiwa kabisa wasipate elimu zaidi. Maofisa wa Idara ya Usalama hata walijaribu kuwashawishi watoto wawe wapelelezi!
Daniela Măluţan, ambaye sasa ni painia, anasema: “Mara nyingi niliaibishwa mbele ya wanadarasa wenzangu kwa sababu nilikataa kujiunga na Shirika la Vijana Wakomunisti, lililotumiwa kuwashawishi vijana wakubali Ukomunisti. Nilipoanza darasa la tisa, maofisa wa Idara ya Usalama walininyanyasa sana. Hali kadhalika walimu na wafanyakazi wengine shuleni waliokuwa wakiwapasha wenye mamlaka habari. Kuanzia mwaka wa 1980 hadi 1982, nilihojiwa baada ya kila majuma mawili katika ofisi ya mwalimu mkuu siku ya Jumatano. Hata hivyo, mwalimu mkuu hakuruhusiwa kusikiliza mahojiano hayo. Akina ndugu katika Mkoa wa Bistriţa-Năsăud walimfahamu vizuri ofisa mkuu wa Idara ya Usalama aliyenihoji kwa sababu alituchukia sana na kutusaka kwa bidii. Ofisa huyo hata alinionyesha barua zilizokuwa na habari mbaya kuwahusu ndugu wenye madaraka. Lengo lake lilikuwa kunifanya nisiwaamini tena ndugu hao, nikane imani yangu, na kunishawishi niwe mpelelezi wa Idara ya Usalama, ijapokuwa nilikuwa mtoto wa shule tu. Alishindwa kabisa.
“Hata hivyo, sikupatwa na mabaya tu. Kwa mfano, mwalimu wangu wa historia aliyekuwa mwanachama wa Chama cha Kikomunisti, alitaka kujua kwa nini nilihojiwa mara nyingi sana. Siku moja aliahirisha somo la historia na kwa muda wa saa mbili akaniuliza maswali mengi juu ya dini yangu. Alivutiwa na majibu yangu na hakuelewa kwa nini nilitendwa vibaya. Baada ya mazungumzo hayo aliheshimu maoni yetu na hata akakubali vitabu vyetu.
“Lakini wakuu wa shule waliendelea kunipinga na wakanilazimisha kuacha shule baada ya darasa la kumi. Hata hivyo, nilipata kazi mara moja na sijajuta kamwe kwamba niliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova. Ninamshukuru Yehova kwamba nililelewa na wazazi Wakristo walioshikilia utimilifu wao ijapokuwa waliteseka sana wakati wa utawala wa Wakomunisti. Bado ninakumbuka mfano wao mzuri.”
Wanaume Vijana Wajaribiwa
Katika harakati zao dhidi ya Mashahidi wa Yehova, maofisa wa Idara ya Usalama waliwalenga hasa wanaume vijana waliokataa kujiunga na jeshi. Kusudi wakate tamaa, vijana hao walikamatwa, wakafungwa, na kuachiliwa tena na tena. Ndugu mmoja kijana, József Szabó alihukumiwa kifungo cha miaka minne baada tu ya kubatizwa.
Baada ya kufungwa kwa miaka miwili, József aliachiliwa mwaka wa 1976, na muda si muda akafahamiana na msichana ambaye angemwoa baadaye. József anasema: “Tuliamua kuoana na tukaweka tarehe ya arusi yetu. Ndipo nilipoitwa tena na Mahakama ya Jeshi ya Cluj. Kesi yangu ingesikilizwa siku tuliyokuwa tumepanga kufunga ndoa! Hata hivyo, mimi na mchumba wangu tulifunga ndoa, na baadaye nikaenda mahakamani. Ijapokuwa nilitoka tu kuoa, nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu, na nikakaa gerezani miaka yote mitatu. Ni vigumu kueleza jinsi nilivyoumia moyoni kwa sababu ya kutenganishwa na mke wangu.”
Shahidi mwingine kijana anayeitwa Timotei Lazăr, anasema hivi: “Mnamo mwaka wa 1977, mimi na ndugu yangu mdogo tuliachiliwa. Kaka yetu aliyeachiliwa mwaka mmoja mapema alikuja nyumbani ili tusherehekee uhuru wetu pamoja. Lakini alinaswa katika mtego, kwani maofisa wa Idara ya Usalama walikuwa wakimngojea. Tulikuwa tumetengana kwa miaka miwili, miezi saba, na siku 15, na sasa ndugu yetu anakamatwa tena na kupelekwa gerezani kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Mimi na ndugu yangu mdogo tuliwatazama tu kwa huzuni.”
Maadhimisho ya Ukumbusho
Wapinzani waliongeza bidii yao ya kuwasaka Mashahidi wa Yehova katika siku ya Ukumbusho kila mwaka. Walipekua nyumba za akina ndugu, wakawatoza faini, na kuwakamata. Ili wasitambuliwe, ndugu waliadhimisha kifo cha Yesu katika vikundi vidogo, hata nyakati nyingine familia mojamoja tu.
Teodor Pamfilie anaeleza hivi: “Jioni, katika siku moja ya Ukumbusho, mkuu wa polisi alikunywa pombe pamoja na marafiki wake hadi usiku sana. Alipoondoka ili akasake nyumba za ndugu, alimwomba mtu ambaye hakumfahamu ampeleke kwa gari lake. Lakini, gari halikuwaka mara moja. Hatimaye, liliwaka na wakaja nyumbani kwetu, ambako sisi na Mashahidi wengine wachache tulikuwa tukiadhimisha Ukumbusho. Hata hivyo, kwa sababu tulikuwa tumefunga mapazia ya madirisha vizuri ilionekana kama nyumba ina giza na walifikiri hakuna mtu nyumbani. Hivyo, wakaenda kwenye nyumba nyingine. Lakini, akina ndugu walikuwa wamemaliza kuadhimisha Ukumbusho na wote walikuwa wameenda nyumbani kwao.
“Sisi nasi tulimaliza maadhimisho nyumbani mwetu, na ndugu wakatoka haraka. Mimi na ndugu yangu wa kimwili tu ndio tuliokuwapo wakati polisi wawili walipoingia ghafula. Walisimama katikati ya chumba na kuuliza hivi kwa ukali: ‘Ni nini kinachoendelea hapa?’
“‘Hakuna,’ nikamjibu. ‘Mimi na ndugu yangu tunapiga gumzo tu.’
“Mmoja wao akasema: ‘Tunajua kwamba kulikuwa na mkutano hapa. Wale wengine wako wapi?’ Kisha akamtazama ndugu yangu na kuongeza: ‘Na wewe unafanya nini hapa?’
“‘Nilikuja kumtembelea huyu,’ akasema akinielekezea mkono. Maofisa hao walitoka wakiwa wameudhika. Siku iliyofuata tulijua kwamba ijapokuwa polisi walijaribu sana hawakufaulu kumkamata hata mtu mmoja!”
Makao Makuu Yawasihi Wakuu wa Rumania
Kwa sababu Mashahidi wa Yehova walitendwa kikatili sana, ndugu kwenye makao makuu walituma barua yenye kurasa nne kwa balozi wa Marekani mnamo Machi 1970 na barua yenye kurasa sita kwa rais wa Rumania, Nicolae Ceauşescu, mnamo Juni 1971. Ndugu walisema hivi katika barua waliyomwandikia balozi: “Tunawaandikia kwa sababu ya upendo wetu wa Kikristo na kwa sababu tunawajali ndugu zetu huko Rumania.” Baada ya kutaja majina ya watu saba waliofungwa kwa sababu ya imani yao, barua hiyo inasema hivi: “Tumejulishwa kwamba baadhi ya watu tuliowataja hapa juu wametendwa kikatili sana gerezani. . . . Mashahidi wa Yehova si wahalifu. Hawajiingizi katika mambo ya siasa wala maasi popote ulimwenguni, bali wao hujishughulisha hasa na ibada yao.” Walimalizia barua kwa kuwaomba wenye mamlaka “wapunguze dhiki ya Mashahidi wa Yehova wanaoteseka.”
Barua kwa Rais Ceauşescu ilisema hivi: “Mashahidi wa Yehova nchini Rumania hawana uhuru wa dini ambao katiba ya Rumania inaruhusu,” bali wanakabili hatari ya kukamatwa na kutendwa kwa ukatili wanapowaeleza wengine kuhusu imani yao na wanapokusanyika ili kujifunza Biblia. Barua hiyo ilitaja pia msamaha uliokuwa umetangazwa kitambo kidogo wakati ndugu wengi walipoachiliwa. “Tulitarajia kwamba hali ingebadilika kwa . . . Mashahidi wa Yehova. Lakini tunasikitika kwamba tarajio hilo halikutimizwa. Habari tunazopokea kutoka sehemu zote za Rumania zinaonyesha hali yenye kuhuzunisha kwamba Mashahidi wa Yehova bado wanateswa na Serikali. Nyumba zao hupekuliwa, wao hunyang’anywa vitabu vyao, wanaume na wanawake hukamatwa na kufikishwa mahakamani, baadhi yao huhukumiwa vifungo vya miaka mingi, na wengine hutendwa kikatili. Wanatendwa hivyo kwa sababu ya kusoma na kuhubiri Neno la Yehova Mungu. Mambo hayo yanaharibu sifa ya nchi yenu, na tunawahangaikia sana Mashahidi wa Yehova nchini Rumania.”
Vitabu viwili vilitiwa ndani ya barua hiyo, yaani, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele katika Kirumania na Uzima wa Milele Katika Uhuru wa Wana wa Mungu katika Kijerumani.
Rumania ilipotia sahihi Mwafaka wa Helsinki mwaka wa 1975, hali ilibadilika kidogo kwa Mashahidi wa Yehova. Mwafaka huo uliunga mkono haki za binadamu, na uhuru mbalimbali wa msingi, kama vile uhuru wa dini. Baada ya Rumania kutia sahihi mwafaka huo, wale waliokataa kujiunga na jeshi ndio tu waliokamatwa na kufungwa.
Kisha mwaka wa 1986, katiba mpya ikaamuru kwamba hakuna mtu, hata wenye mamlaka, anayeweza kuingia nyumbani kwa mtu bila kibali cha mwenye nyumba, isipokuwa katika hali fulani zinazokubalika kisheria. Hatimaye ndugu waliweza kujihisi salama walipofanya mikutano ya Kikristo, hata kuadhimisha Ukumbusho, katika nyumba zao.
Uchapaji wa Kisiri
Wakati wa marufuku, chakula cha kiroho kiliingizwa nchini Rumania kwa njia ya magazeti, vitabu, stensili, na kwa njia nyinginezo, kisha nakala zikafanywa nchini humo. Nyakati nyingine habari ilikuwa imetafsiriwa tayari katika Kirumania na Kihungaria, lakini kwa kawaida ndugu walitafsiri kutoka Kiingereza, Kifaransa, Kijerumani, au Kiitaliano. Chakula hicho cha kiroho kililetwa na watu kama vile watalii kutoka nchi za kigeni, wanafunzi waliokuja kusoma, na Warumania waliorudi nyumbani baada ya kusafiri.
Maofisa wa Idara ya Usalama walijaribu sana kuwakamata wale waliopeleka vifaa, na pia kujua mahali ambapo kazi ya uchapaji na kutoa nakala ilifanyiwa nchini Rumania. Kwa busara, ndugu walifanya kazi hiyo katika nyumba kadhaa za akina ndugu zisizopenya sauti katika miji na majiji kadhaa. Katika nyumba hizo walitengeneza vyumba vidogo vya siri kwa ajili ya mashine za kufanya nakala. Baadhi ya vyumba hivyo vilikuwa nyuma ya majoko, ambayo kwa kawaida yanashikamana na ukuta. Hata hivyo, ndugu waliyarekebisha majoko hayo ili yaweze kusogezwa na wakatengeneza mlango uliofichika nyuma yake.
Sándor Parajdi alifanya kazi ya uchapaji wa kisiri mjini Tirgu-Mures, ambako alichapa andiko la siku, Huduma Yetu ya Ufalme, Mnara wa Mlinzi, na Amkeni! Ndugu Sándor anasema: “Tulifanya kazi kwa muda wa saa 40 hivi mwishoni mwa kila juma, na kulala kwa zamu kwa muda wa saa moja. Harufu ya kemikali ilipenya mavazi na ngozi zetu. Siku moja niliporudi nyumbani, mwana wangu aliyekuwa na miaka mitatu alisema hivi: ‘Baba, unanuka kama andiko la siku!’”
Traian Chira, aliyekuwa na mke na watoto, alifanya nakala na kusafirisha vichapo katika Mkoa wa Cluj. Traian alipewa mashine kuukuu ya kufanya nakala iliyoendeshwa kwa mkono ambayo iliitwa Kinu. Ilifanya kazi, lakini vitabu vilivyochapwa kwa mashine hiyo havikuvutia hata kidogo. Kwa hiyo, Traian akamwomba ndugu aliyekuwa fundi airekebishe. Ndugu huyo alichunguza mashine hiyo, lakini Traian alipomtazama usoni alijua kwamba mashine hiyo kuukuu haingerekebika. Ndipo ndugu huyo akasema kwa furaha: “Ninaweza kukutengenezea mashine mpya!” Na alifanya mengi zaidi. Alitumia chumba cha chini ya ardhi cha dada fulani kama karakana na akatengeneza mashine ya kukata chuma. Hakutengeneza mashine moja tu ya kufanya nakala bali mashine zaidi ya kumi! Mashine hizo mpya zilipelekwa kwenye sehemu nyingine za nchi na zikafanya kazi vizuri.
Katika miaka ya 1980 ndugu kadhaa walifundishwa kuendesha mashine bora za kufanya nakala zenye mabamba duara ya kuchapia. Ndugu Nicolae Bentaru alizoezwa kwanza, naye akawazoeza wengine. Watu wote wa familia ya Bentaru walisaidiana kufanya kazi hiyo, na kila mtu alikuwa na kazi fulani. Ndivyo zilivyofanya familia nyingi. Ilikuwa vigumu kufanya kazi hiyo kisiri, hasa katika kipindi ambapo maofisa wa Idara ya Usalama walipekua nyumba na kuwapeleleza watu. Kwa hiyo, iliwabidi ndugu kufanya kazi haraka, na walitumia saa nyingi Jumamosi na Jumapili ili kufanya kazi ya kuchapa na kusafirisha vitabu. Kwa nini walifanya kazi hiyo Jumamosi na Jumapili? Kwa sababu katikati ya juma walikuwa wakifanya kazi ili kuruzuku familia.
Iliwabidi ndugu kuwa waangalifu pia waliponunua karatasi. Mteja aliulizwa sababu ya kununua karatasi hata aliponunua furushi moja tu la karatasi 500 tu, na ndugu walitumia karatasi 40,000 hivi kila mwezi! Kwa hiyo, ndugu walihitaji kuwa waangalifu waliposhughulika na wafanyakazi madukani. Na kwa kuwa magari yalichunguzwa kwa ukawaida, ilikuwa lazima wajihadhari pia waliposafirisha vifaa.
Matatizo ya Kutafsiri
Ndugu na dada wachache walioishi katika sehemu mbalimbali za Rumania walitafsiri vitabu katika lugha za kienyeji, kama vile Kiukrainia, ambayo ni lugha ya watu wachache wanaoishi kaskazini nchini humo. Baadhi ya watafsiri walikuwa walimu wa lugha ambao walikuwa wamekubali kweli. Wengine walikuwa wamejifunza lugha mpya.
Zamani, watafsiri waliandika tafsiri zao kwa mkono katika vitabu, ambavyo vilipelekwa Bistriţa, jiji la kaskazini, ili tafsiri isahihishwe. Watafsiri na wale waliosahihisha tafsiri walikutana mara moja au mbili kwa mwaka ili kuzungumzia matatizo yaliyohusu kazi yao. Ndugu na dada hao walipotambuliwa, wengi wao walipekuliwa, wakahojiwa, wakapigwa, na kutiwa mbaroni. Baadhi yao walizuiliwa kwenye kituo cha polisi kwa muda wa saa chache au siku chache, kisha wakaachiliwa na kukamatwa tena. Hiyo ilikuwa njia ya kuwatisha. Wengine walizuiliwa nyumbani au kuamriwa wapige ripoti kwenye kituo cha polisi kila siku. Na wengi kama vile Dumitru na Doina Cepănaru na Petre Ranca walifungwa gerezani.
Dumitru Cepănaru alikuwa mwalimu wa lugha na historia ya Rumania katika shule ya upili, na mke wake Doina alikuwa daktari. Hatimaye maofisa wa Idara ya Usalama waliwapata, wakawakamata, na kuwafunga katika magereza tofauti kwa miaka saba na nusu. Doina alifungwa akiwa peke yake kwa miaka mitano. Majina yao yalitajwa katika ile barua ambayo ndugu kwenye makao makuu walimwandikia balozi wa Rumania huko Marekani. Doina alimwandikia mume wake na dada waliofungwa barua 500 ili awatie moyo.
Mwaka mmoja baada ya Dumitru na Doina kukamatwa, mama ya Dumitru, Sabina Cepănaru alikamatwa pia, naye akafungwa kwa miaka mitano na miezi kumi. Mtu mmoja tu katika familia yao, yaani mume wa Sabina, hakufungwa ingawa alipelelezwa sana na Idara ya Usalama. Yeye pia alikuwa Shahidi wa Yehova, na alijihatarisha sana kwa kuwatembelea kwa ukawaida wale watu watatu wa jamaa yao waliokuwa wamefungwa.
Petre Ranca aliwekwa kuwa katibu wa ofisi ya Mashahidi wa Yehova nchini Rumania mwaka wa 1938. Kwa sababu ya wadhifa huo na kazi yake ya kutafsiri, alikuwa mmojawapo wa watu waliosakwa sana na maofisa wa Idara ya Usalama. Hatimaye alikamatwa mwaka wa 1948, na baada ya kuachiliwa na kukamatwa mara kadhaa akafikishwa mahakamani pamoja na Martin Magyarosi na Pamfil Albu mwaka wa 1950. Alishtakiwa kwa uwongo kuwa mwanachama wa kikundi cha wapelelezi cha Marekani, na alivumilia kifungo cha miaka 17 katika magereza mabaya zaidi nchini humo, yaani, Aiud, Gherla, na Jilava. Pia alizuiliwa nyumbani kwa miaka mitatu katika Mkoa wa Galaţi. Ndugu huyo mwaminifu, aliyekuwa na tumaini la kimbingu, alimtumikia Yehova kwa moyo wote hadi alipokufa mnamo Agosti 11, 1991.
Kazi ambayo ndugu hao walioshika utimilifu walifanya kwa upendo, inatukumbusha maneno haya: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.”—Ebr. 6:10.
Makusanyiko Yafanywa Mashambani
Katika miaka ya 1980, ndugu walifanya makusanyiko makubwa kila walipopata nafasi, kama vile wakati wa arusi au mazishi. Kwenye arusi walipiga hema kubwa mahali palipofaa mashambani na kulipamba kwa mazulia maridadi yaliyokuwa na maandiko na picha za matukio yanayosimuliwa katika Biblia. Meza na viti vilipangwa kwa ajili ya “wageni” wengi, na maandishi makubwa ya Mnara wa Mlinzi na andiko la mwaka lilining’inizwa jukwaani. Kwa kawaida wahubiri wa eneo hilo walileta chakula kulingana na uwezo wao. Hivyo, wote walifurahia karamu ya kimwili na ya kiroho.
Kwanza hotuba ya arusi au mazishi ilitolewa, kisha hotuba nyingine kuhusu habari mbalimbali za Biblia zikatolewa. Nyakati nyingine wasemaji walizuiwa kufika kwa wakati, kwa hiyo, ndugu wengine waliostahili walikuwa tayari kutoa hotuba. Kwa kawaida walitumia Biblia tu, kwani hakukuwa na mihtasari.
Katika majira ya kiangazi watu wengi walioishi mijini walimiminika mashambani ili wajiburudishe. Mashahidi wa Yehova walifanya vivyo hivyo, nao walitumia nafasi hiyo kufanya makusanyiko madogo milimani na misituni. Walifanya hata drama za Biblia.
Watu walipenda pia kwenda kwenye pwani ya Bahari Nyeusi wakati wa likizo, na sehemu hiyo ilifaa sana kwa ubatizo. Wapya walibatizwaje bila watu wengine kutambua? Nyakati nyingine walicheza “mchezo” fulani. Wale waliotaka kubatizwa na wahubiri kadhaa waliobatizwa walisimama katika duara majini wakitupiana mpira. Msemaji alitoa hotuba akisimama katikati yao, kisha wale wapya wakabatizwa kwa njia isiyotambulika.
Jumba la Wafugaji wa Nyuki
Mnamo mwaka wa 1980, ndugu katika mji wa Negreşti-Oaş, kaskazini-magharibi mwa Rumania, waligundua njia nzuri ya kupata kibali cha kujenga Jumba la Ufalme. Siku hizo Serikali iliwatia watu moyo wafuge nyuki. Kwa hiyo ndugu kadhaa waliofuga nyuki waliamua kuanzisha shirika lao la wafugaji wa nyuki, na hivyo kupata sababu mwafaka ya kujenga jumba la mikutano.
Baada ya kuongea na wazee wa mzunguko wao, ndugu waliandikisha shirika lao katika Shirika la Wafugaji wa Nyuki la Rumania na wakaenda kwenye ofisi ya baraza la mji ili kutoa ombi la kujenga jumba la mikutano. Wenye mamlaka waliidhinisha mara moja ujenzi wa jengo la mbao lenye urefu wa meta 34 na upana wa meta 14. Wale wafugaji wa nyuki na wasaidizi wao walifurahi sana nao wakamaliza ujenzi kwa miezi mitatu. Wakuu wa mji hata waliwashukuru!
Kwa sababu wengi wangehudhuria mkutano wa kwanza katika jumba hilo ambao ungeendelea kwa saa kadhaa, ndugu waliomba na kupata kibali cha kulitumia kwa ajili ya karamu ya mavuno ya nafaka. Zaidi ya Mashahidi 3,000 kutoka sehemu zote za nchi walihudhuria mkutano huo. Wakuu wa mji walishangaa kwamba watu wengi sana walikuja kusaidia kuvuna na “kusherehekea” baadaye.
Bila shaka, sherehe hiyo ilikuwa kusanyiko lenye kunufaisha sana kiroho. Kwa sababu ya kusudi rasmi la jumba hilo, nyuki walitajwa mara nyingi katika hotuba mbalimbali kama vielelezo. Kwa mfano, wasemaji walikazia bidii ya nyuki, uwezo wake wa kujielekeza, utaratibu wake, ujasiri wake anapolinda mzinga, na sifa nyinginezo nyingi.
Baada ya mkutano huo wa kwanza, jumba hilo lililoitwa Jumba la Nyuki, lilitumiwa na ndugu hadi marufuku ilipoondolewa na likaendelea kutumiwa kwa miaka mitatu baadaye.
Waangalizi wa Eneo la Dunia Waendeleza Umoja
Kwa miaka mingi Wakomunisti walijaribu juu chini kupanda mbegu za shaka miongoni mwa watu wa Mungu, kuvunja umoja wao, na kuzuia mawasiliano. Kama ambavyo tumetaja, walifaulu kwa kadiri fulani. Bado kulikuwa na migawanyiko katika miaka ya 1980. Ziara za waangalizi wa eneo la dunia na mabadiliko ya kisiasa yalisaidia kusuluhisha tatizo hilo.
Ndugu Gerrit Lösch, aliyetumikia katika Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Austria wakati huo, alitembelea Rumania mara kadhaa katikati ya miaka ya 1970. Sasa Ndugu Lösch ni mmojawapo wa ndugu wa Baraza Linaloongoza. Mwaka wa 1988, wawakilishi wa Baraza Linaloongoza Theodore Jaracz na Milton Henschel walitembelea Rumania mara mbili wakiandamana na Ndugu Lösch na mfasiri Jon Brenca, aliyekuwa Mwanabetheli huko Marekani wakati huo. Baada ya ziara hizo zenye kutia moyo, maelfu ya ndugu waliokuwa wamejitenga na watu wa Yehova walirudi zizini bila wasiwasi.
Mabadiliko ya kisiasa yaliathiri sana nchi za Kikomunisti huko Ulaya, na kuzidhoofisha sana hivi kwamba hatimaye serikali nyingi za Kikomunisti zilianguka mwishoni mwa miaka ya 1980. Mambo yalipamba moto nchini Rumania mwaka wa 1989, serikali ya Kikomunisti ilipopinduliwa. Kiongozi wa Chama cha Kikomunisti, Nicolae Ceauşescu, na mke wake waliuawa mnamo Desemba 25. Serikali mpya ilianza kutawala mwaka uliofuata.
Uhuru Hatimaye!
Mashahidi wa Yehova hawakuunga mkono upande wowote wakati huo wa mabadiliko ya kisiasa nchini Rumania. Hata hivyo, mabadiliko hayo yaliwaletea wale Mashahidi 17,000 nchini Rumania uhuru ambao hawakuutarajia. Halmashauri ya Nchi iliandika: “Baada ya miaka 42 ya mateso, tunatuma kwa shangwe ripoti kuhusu kazi ya kuhubiri huku Rumania. Tunamshukuru Baba yetu mwenye upendo, Yehova Mungu, aliyesikiliza sala za mamilioni ya ndugu na kukomesha yale mateso makali.”
Shirika la Dini la Mashahidi wa Yehova liliandikishwa kisheria Aprili 9, 1990, na mara moja ndugu wakapanga makusanyiko ya mzunguko kotekote nchini. Watu zaidi ya 44,000 walihudhuria makusanyiko hayo. Idadi hiyo inazidi kwa mara mbili idadi ya wahubiri, ambayo ilikuwa 19,000 hivi. Ripoti ya utumishi wa shambani ilionyesha kwamba kuanzia Septemba 1989 hadi Septemba 1990, idadi ya Mashahidi wa Yehova iliongezeka kwa asilimia 15!
Wakati huo Halmashauri ya Nchi ilisimamia kazi chini ya mwongozo wa ofisi ya tawi ya Austria. Baada ya kipindi cha miaka 66, ofisi ya tawi ilifunguliwa tena nchini Rumania mwaka wa 1995.
Ndugu Wasaidiwa Wakati wa Matatizo ya Uchumi
Uchumi wa Rumania ulizorota sana katika miaka ya 1980, na bidhaa zilikuwa haba nchini. Kisha serikali ya Kikomunisti ilipopinduliwa, uchumi uliharibika kabisa na watu wakaumia sana. Mashahidi wa Yehova nchini Austria, Hungaria, na ile iliyokuwa Chekoslovakia na Yugoslavia, waliwapelekea ndugu zao nchini Rumania kilo 70,000 za chakula na mavazi. Bidhaa hizo zilikuwa nyingi sana hivi kwamba ndugu waliweza kuwagawia majirani wao wasio Mashahidi baadhi ya vitu hivyo. Ripoti moja inasema: “Kila mara msaada ulipotolewa, ndugu walitumia nafasi hiyo kutoa ushahidi kikamili.”
Mbali na msaada wa kimwili ndugu walipata pia chakula kingi cha kiroho. Wengi walitokwa na machozi malori yaliyojaa vichapo yalipofika, kwani walikuwa wamezoea kuwa na nakala moja tu ya Mnara wa Mlinzi kwa wote katika kikundi. Isitoshe, kuanzia Januari 1, 1991, Mnara wa Mlinzi katika Kirumania lilichapishwa sawia na chapa ya Kiingereza, na lilikuwa lenye picha za rangi! Kwa sababu ya mabadiliko hayo watu wengi kwenye eneo walikubali kulisoma.
Vikundi vya Majadiliano Vyaachwa na Mikutano ya Kawaida Yaanzishwa
Wakati wa mateso, ndugu hawakuweza kufanya mikutano fulani kama vile Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwa njia ya kawaida. Badala yake ndugu wachache walikutanika, wakasoma habari, kisha wakaijadili. Kwa kawaida walikuwa na kitabu kimoja tu au vitabu vichache.
Jon Brenca, ambaye sasa anatumika katika Halmashauri ya Ofisi ya Tawi nchini Rumania, anasema hivi: “Kitabu Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kilichapwa katika Kirumania mwaka wa 1992. Kabla ya hapo ndugu wachache tu ndio waliokuwa na nakala za kitabu hicho zilizochapwa nchini humu. Tulianza kuwazoeza wazee kuongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na kuwashauri wanafunzi mwaka wa 1991. Hata hivyo, mara nyingi wazee walisita kutoa ushauri, kwa kuwa siku hizo ushauri ulitolewa na ndugu akiwa jukwaani. Baadhi yao walisema: ‘Ndugu wataudhika tukiwashauri mbele ya wengine.’”
Nyakati nyingine ndugu walielewa mambo vibaya. Kwa mfano, wakati ndugu mmoja aliyehitimu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma alipotembelea kutaniko fulani mwaka wa 1993, mzee mmoja alimwendea akiwa na ile ratiba ya shule inayotaja kwamba makutaniko makubwa yanapaswa kuwa na shule ya pili. Mzee huyo aliuliza hivi akifikiri kwamba shule ya pili ilikuwa ya wanafunzi waliokuwa wamefanya maendeleo: “Ningependa kujua ni lini tutakapostahili kuwa na shule ya pili? Tuna ndugu ambao wangestahili kupandishwa ngazi.” Kwa fadhili mgeni huyo alifafanua jambo hilo.
Ndugu Brenca anaeleza: “Makusanyiko ya mzunguko yaliwaelimisha sana ndugu, kwa kuwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huongozwa na mwangalizi wa wilaya kwenye makusanyiko hayo. Hata hivyo, baada ya miaka michache wote walikuwa wamezoea mpango huo.”
Shule ya Utumishi wa Upainia ilianzishwa nchini Rumania mwaka wa 1993 na imewasaidia maelfu ya mapainia kufanya maendeleo ya kiroho na kuhubiri na kufundisha kwa ustadi zaidi. Si rahisi kuwa painia nchini Rumania kwa kuwa ni vigumu kupata kazi inayomruhusu mtu kufanya utumishi wa wakati wote. Hata hivyo, ndugu na dada zaidi ya 3,500 walishiriki katika utumishi wa upainia mwaka wa 2004.
Waangalizi Wanaosafiri Wazoezwa
Roberto Franceschetti na Andrea Fabbi kutoka ofisi ya tawi ya Italia walitumwa Rumania mwaka wa 1990 kwa kusudi la kusaidia kupanga upya kazi. Ndugu Franceschetti anasema: “Nilikuwa na miaka 57, na hali ya uchumi haikuwa nzuri nchini Rumania wakati huo, kwa hiyo, ilikuwa vigumu kwangu na kwa mke wangu Imelda kuzoea maisha nchini humo.
“Tulipofika Bucharest saa 1:00 jioni, Desemba 7, 1990, halijoto ilikuwa nyuzi 12 Selsiasi chini ya kiwango cha kuganda na theluji ilitanda kotekote jijini. Tulikutana na ndugu fulani katikati ya jiji na tukawauliza kuhusu mahali pa kulala. Walisema: ‘Hatujui bado.’ Lakini mwanamke kijana ambaye mama na nyanya yake ni Mashahidi alisikia mazungumzo yetu na akatukaribisha mara moja nyumbani kwake. Tulikaa kwake kwa majuma kadhaa hadi tulipopata makao yanayofaa jijini. Ndugu wenyeji walitutia moyo, na hilo lilitusaidia kuzoea hali hizo mpya.”
Roberto, aliyehitimu darasa la 43 la Shule ya Gileadi mwaka wa 1967, alikaa Rumania pamoja na mke wake kwa miaka tisa hivi, na ndugu walinufaika sana kutokana na uzoefu wao katika utumishi wa Yehova. Roberto anasema: “Mnamo Januari 1991, Halmashauri ya Nchi ilipanga mkutano pamoja na waangalizi wote 42 wanaosafiri. Mizunguko mingi ilikuwa na makutaniko sita au saba tu. Waangalizi walikuwa wakitumia siku nne kwa ajili ya kila ziara katika makutaniko, yaani, miisho ya juma miwili. Kwa kawaida hawakuandamana na wake zao. Nyakati hizo waangalizi wa mzunguko walikuwa wakifanya kazi ya kujiruzuku ili wasishukiwe na wenye mamlaka. Lakini sasa ndugu hao wangeweza kufuata ratiba ileile ya waangalizi katika nchi nyingine na kutembelea makutaniko kuanzia Jumanne hadi Jumapili.
“Baada ya kueleza mpango huo niliwaambia wale ndugu 42 hivi: ‘Ikiwa mnataka kuendelea kuwa waangalizi wa mzunguko, tafadhali inueni mikono.’ Hakuna hata mmoja aliyeinua mkono! Papo hapo tukapoteza waangalizi wote wanaosafiri nchini mwetu! Hata hivyo, baada ya kusali na kutafakari kuhusu jambo hilo, baadhi yao walikubali kuendelea. Ndugu ambao walikuwa wamehitimu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma kutoka Austria, Italia, Marekani, Ufaransa, na Ujerumani, walikuja kusaidia pia.”
Jon Brenca, mtu mwenye asili ya Kirumania, alitoka Betheli huko Brooklyn na kuhamia Rumania, ambako alitumikia kwa miaka kumi. Kwanza Jon alikuwa mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya. Anasema hivi: “Mnamo Juni 1991, nikiwa mwangalizi wa wilaya nilianza kufanya kazi pamoja na wale waangalizi wa mzunguko waliokubali ule mpango mpya. Mara niliona kwamba si waangalizi tu waliokuwa na tatizo la kuzoea mpango huo mpya, bali pia akina ndugu katika makutaniko. Baadhi ya wazee walisema hivi: ‘Haitawezekana kwa wahubiri kuunga mkono mpango wa kuhubiri kila siku.’ Lakini hatimaye wote waliunga mkono mpango huo mpya.”
Shule ya Huduma ya Ufalme na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma pia zilisaidia kuwaelimisha ndugu. Wakati wa Shule ya Huduma ya Ufalme huko Baia-Mare, mzee mmoja alitokwa na machozi alipomwendea mmojawapo wa walimu na kusema: “Nimekuwa mzee kwa miaka mingi, lakini hadi sasa sikuwa nimeelewa jinsi ya kufanya ziara za uchungaji. Ninashukuru Baraza Linaloongoza kwa elimu hiyo bora.”
Ndugu walikuwa wamesikia kuhusu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, lakini hawakufikiri kamwe kwamba ingefanyiwa nchini mwao. Hebu wazia furaha yao wakati darasa la kwanza la shule hiyo lilipofanywa mwaka wa 1999! Tangu wakati huo madarasa manane mengine yamefanywa, na ndugu kutoka Moldova na Ukrainia wanaoongea Kirumania wameihudhuria.
“Nimepata Kweli!”
Watu wengi sasa huhubiriwa kwa ukawaida, lakini watu milioni saba, yaani, thuluthi moja ya wakaaji wote, wanaishi katika maeneo ambayo hayajagawiwa yeyote. Watu katika maeneo fulani hawajahubiriwa habari njema kamwe, kwa hiyo mavuno bado ni mengi! (Mt. 9:37) Mapainia wa kawaida na wa pekee na wazee wa makutaniko wametambua uhitaji huo na kuhamia maeneo hayo. Vikundi vingi na makutaniko mengi yameanzishwa kwa njia hiyo. Isitoshe, ofisi ya tawi imewaomba ndugu katika makutaniko waende wakahubiri katika maeneo ambayo hayahubiriwi kwa ukawaida. Kama katika nchi nyingine, mipango hiyo imefanikiwa sana.
Katika kijiji kimoja cha mbali, mwanamke mwenye umri wa miaka 83 alipata gazeti la Mnara wa Mlinzi kutoka kwa mmojawapo wa binti zake, aliyeliokota katika pipa la takataka jijini Bucharest. Mwanamke huyo alisoma hilo gazeti na pia maandiko yote yaliyoonyeshwa. Alisoma maandiko hayo katika Biblia yake iliyokuwa na jina la Mungu. Alipozungumza na binti yake tena, alisema kwa shauku: “Mpendwa wangu, nimepata kweli!”
Aliongea pia na kasisi wa kijiji chao na kumuuliza kwa nini hajawaeleza watu kuhusu jina la Mungu. Kasisi hakumjibu lakini alimwomba Biblia yake na gazeti hilo ili avichunguze. Mwanamke huyo alikubali kwa heshima, lakini huyo kasisi hakumrudishia kamwe Biblia yake wala gazeti hilo la Mnara wa Mlinzi. Baadaye, Mashahidi wa Yehova walipokuja kuhubiri kijijini kwao, aliwakaribisha, akaanza kujifunza Neno la Mungu kwa kutumia kitabu Ujuzi, na kufanya maendeleo haraka. Leo, yeye na binti zake wote ni Mashahidi.
Uhuru wa Kukusanyika Hatimaye!
Mashahidi wa Yehova nchini Rumania walifurahi sana kuhudhuria Makusanyiko ya Wilaya ya “Lugha Iliyo Safi” ya mwaka wa 1990. Kwa wengi wao, hiyo ilikuwa mara ya kwanza kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Makusanyiko yalifanywa katika jiji la Brasov na Cluj-Napoca. Majuma mawili mapema ndugu 2,000 walihudhuria kusanyiko la Kirumania huko Budapest, Hungaria. Ijapokuwa makusanyiko yaliyofanywa nchini Rumania yalikuwa ya siku moja tu, ndugu walifurahi sana kusikiliza hotuba za wawakilishi wa Baraza Linaloongoza Milton Henschel na Theodore Jaracz. Zaidi ya watu 36,000 walihudhuria na watu 1,445 wakabatizwa. Hiyo ni asilimia 8 ya wahubiri wote nchini humo!
Kusanyiko la Kimataifa lenye kichwa “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” lilikuwa lifanywe jijini Bucharest mwaka wa 1996. Lakini makasisi wa Kanisa Othodoksi walijaribu juu chini kulizuia kusanyiko hilo lisifanywe. Wao na wafuasi wao walibandika karatasi zenye maneno yaliyochochea chuki kotekote jijini, kwenye kuta za makanisa na za majengo, na kwingineko. Karatasi moja iliandikwa: “Uwe mfuasi wa Kanisa Othodoksi au ufe.” Nyingine ilisema: “Tutawaomba wenye mamlaka wazuie kusanyiko hilo lisifanywe. NJOONI TUTETEE IMANI YA MABABU ZETU. Mungu na atujalie!”
Kwa sababu ya mambo hayo, wakuu wa jiji hawakuwapa ndugu kibali cha kufanya kusanyiko hilo jijini Bucharest. Hata hivyo, ndugu walifaulu kupata mahali pa kufanyia makusanyiko jijini Brasov na Cluj-Napoca kuanzia Julai 19 hadi 21, na wakafaulu pia kupanga makusanyiko madogo huko Bucharest na Baia-Mare kwa ajili ya wale wasioweza kuhudhuria yale makusanyiko mengine.
Waandishi wa habari walivutiwa kuona kwamba ndugu hawakuvurugika na kwamba waliweza kupanga mambo upya kwa muda mfupi sana. Kwa hiyo, licha ya uchambuzi wa makasisi, habari nzuri kuhusu tukio hilo zilisambazwa na vyombo vya habari siku iliyotangulia kusanyiko. Lakini hata habari mbaya zilizosambazwa mapema zilileta manufaa fulani kwa kuwa zilifanya jina la Yehova lijulikane. Ndugu mmoja huko Bucharest alisema hivi: “Ushahidi uliotolewa kwa majuma hayo matatu unalingana na kazi ya kuhubiri ya miaka mitatu kotekote nchini. Badala ya kutuzuia, mbinu za Kanisa Othodoksi la Rumania zimetusaidia kueneza habari njema.” Watu 40,206 walihudhuria makusanyiko hayo, na 1,679 wakabatizwa.
Kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya “Watekelezaji wa Neno la Mungu,” ya mwaka wa 2000, ndugu walifurahi sana kupata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kirumania. Ndugu mmoja kijana aliyeithamini Biblia hiyo alisema hivi: “Nilimkaribia Yehova hata zaidi niliposoma jina lake katika tafsiri hiyo. Ninamshukuru Yehova na tengenezo lake kwa moyo wangu wote.”
Jumba la Kusanyiko Badala ya Jumba la Nyuki
Hakuna Majumba ya Ufalme yaliyojengwa wakati wa utawala wa Kikomunisti ila tu lile Jumba la Nyuki lililotajwa mapema. Kwa hiyo, marufuku ilipofutwa kulikuwa na uhitaji mkubwa sana wa Majumba ya Ufalme. Katika miaka ya majuzi, mpango wa Hazina ya Majumba ya Ufalme umewawezesha ndugu kujenga kwa wastani Jumba moja la Ufalme kila siku kumi! Majumba hayo yote yasiyo na madoido yanafanana, nayo yamejengwa kwa vifaa vinavyopatikana kwa urahisi. Kama ilivyo katika nchi nyingine, majirani, wafanyabiashara, na wakuu wa miji hutolewa ushahidi kwa mipango mizuri ya ujenzi na roho ya kujitolea ya wajenzi, hasa wakati majumba yanapojengwa kwa muda mfupi.
Katika Mkoa wa Mureş, ndugu waliwaendea wenye mamlaka ili kupata kibali cha kuweka umeme katika Jumba la Ufalme lililokuwa likijengwa. Ofisa mmoja aliwauliza: “Mna haraka gani? Itachukua angalau mwezi mmoja kushughulikia kibali chenu, na hamtakuwa mmeendelea sana.” Kwa hiyo, ndugu wakamwendea mkurugenzi.
Yeye pia aliuliza: “Kwani mna haraka gani? Mmetoka tu kuweka msingi, sivyo?”
Ndugu wakajibu: “Naam, lakini tuliweka msingi juma lililopita, sasa tunaweka paa!” Mkurugenzi alielewa, naye akatoa kibali kesho yake.
Jumba la kwanza la Kusanyiko nchini Rumania lililojengwa mjini Negreşti-Oaş, lina jumba kuu linalotoshea watu 2,000, na uwanja unaowatoshea watu 6,000. Ndugu Lösch alifurahi sana alipoalikwa kutoa hotuba ya kuweka wakfu jumba hilo na akaitoa katika Kirumania. Ndugu kutoka zaidi ya makutaniko 90 katika mizunguko mitano, walikuwa wamesaidia kujenga. Hata kabla jumba hilo halijawekwa wakfu, kusanyiko la wilaya lilifanywa humo mnamo Julai 2003, na watu 8,572 wakahudhuria. Jumba hilo la Kusanyiko lilizungumziwa sana na wafuasi wa Kanisa Othodoksi. Lakini si wote waliolichambua. Baadhi ya makasisi hata waliwapongeza ndugu kwa roho yao ya kujitolea.
Hakuna Silaha Itakayofanikiwa Dhidi ya Watumishi wa Mungu
Wakati Károly Szabó na József Kiss waliporudi nchini kwao mwaka wa 1911, hawakujua Yehova angebariki kwa kadiri gani kazi waliyoanzisha. Fikiria: Katika miaka kumi iliyopita watu 18,500 wamebatizwa nchini Rumania. Sasa kuna wahubiri 38,423 nchini humo. Watu 79,370 walihudhuria Ukumbusho mwaka wa 2005! Kwa sababu ya ongezeko hilo, makao mapya ya Betheli yaliwekwa wakfu mwaka wa 1998 na kupanuliwa mwaka wa 2000. Jengo lenye Majumba matatu ya Ufalme lilijengwa pia kwenye kiwanja cha Betheli.
Hata hivyo, msingi wa ongezeko hilo uliwekwa katika pindi za mateso makali sana hivi kwamba mambo mengine kuyahusu hayawezi kutajwa. Sifa zote na zimwendee Yehova aliyewalinda Mashahidi wake washikamanifu. (Zab. 91:1, 2) Yehova ametoa ahadi hii kuwahusu watumishi wake waaminifu: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu. Hilo ndilo fungu la urithi la watumishi wa Yehova.”—Isa. 54:17.
Ili wasipoteze hilo “fungu la urithi” lenye thamani, Mashahidi wa Yehova nchini Rumania wameazimia kuyakumbuka machozi ya wale wote walioteseka kwa ajili ya uadilifu kwa kuiga imani yao.—Isa. 43:10; Ebr. 13:7.
[Sanduku katika ukurasa wa 72]
Maelezo Mafupi Kuhusu Rumania
Nchi: Rumania iliyo na ukubwa wa kilometa 238,000 za mraba ina umbo kama duara na upana wa kilometa 720 kutoka mashariki hadi magharibi. Nchi hiyo inapakana na Ukrania, Moldova, Bulgaria, Serbia na Montenegro, na Hungaria.
Watu: Rumania ina watu milioni 22 wa jamii mbalimbali kama vile Warumania, Wahungaria, Wajerumani, Wayahudi, Waukrainia, jamii fulani ya wahamaji, na nyinginezo. Robo tatu hivi ya wakaaji ni wafuasi wa Kanisa Othodoksi la Rumania.
Lugha: Lugha rasmi ni Kirumania. Lugha hiyo ilitokana na Kilatini kilichozungumzwa na Waroma wa kale.
Kazi: Asilimia 40 hivi ya wafanyakazi nchini Rumania hufanya kazi ya ukulima, ukuzaji wa misitu, au uvuvi; asilimia 25 hufanya kazi kwenye viwanda, migodi, au hufanya kazi ya ujenzi; na asilimia 30 hufanya kazi za kuwahudumia wengine.
Chakula: Mazao yanatia ndani mahindi, viazi, miwa, viazi-sukari, ngano, na zabibu. Wanyama wanaofugwa hasa ni kondoo. Wanyama wengine wa kufugwa ni ng’ombe, nguruwe, na kuku.
Hali ya hewa: Kiwango cha joto na mvua hutofautiana kulingana na eneo. Kwa ujumla, halijoto ni ya wastani na kuna majira manne.
[Sanduku katika ukurasa wa 74]
Maeneo Mbalimbali ya Rumania
Sehemu kubwa ya nchi ya Rumania ni mashamba. Nchi hiyo ina mandhari mbalimbali na maeneo ya kihistoria kama vile Maramureş, Moldavia, Transylvania, na Dobruja. Eneo la kaskazini la Maramureş ndilo eneo pekee ambalo halikuvamiwa na Waroma. Watu huishi katika vijiji vya milimani mbali na miji, nao hufuata utamaduni wa mababu zao Wadashia. Eneo la mashariki la Moldavia linajulikana sana kwa chemchemi zake za maji yenye madini, viwanda vya kutengeneza divai, na nyumba za watawa zilizojengwa katika karne ya 15. Bucharest, ambalo ndilo jiji kubwa zaidi na pia makao makuu ya serikali ya Rumania, liko katika eneo la kusini linaloitwa Walachia.
Eneo la Transylvania lililo katikati ya Rumania ni tambarare na limezungukwa upande mmoja na Milima ya Carpathia. Eneo hilo lina majumba ya kale ya kifalme, miji na mabomoko. Hekaya kumhusu Dracula anayesemekana kuwa alifyonza damu ya wanadamu ilianzia huko. Hekaya hiyo ilitokana na Wakuu Vlad Dracul, au Vlad Ibilisi, na Vlad Tepes, ambaye aliitwa Vlad Mtundikaji kwa sababu ya njia yake ya kuwaua adui zake. Wakuu hao waliishi katika karne ya 15. Watalii hutembelea maeneo mengi yanayosemekana kuwa makao ya wakuu hao.
Eneo la Dobruja, linalopakana na Bahari Nyeusi lina pwani yenye urefu wa kilometa 250 hivi na delta yenye kuvutia ya Mto Danube. Mto huo ambao ni wa pili kwa urefu barani Ulaya ndio mpaka wa kusini wa nchi ya Rumania na maji yake hutoka katika sehemu nyingi za nchi hiyo. Mto Danube una delta yenye ukubwa wa kilometa 4,300 za mraba. Delta hiyo ndiyo eneo kubwa zaidi lenye umajimaji barani Ulaya ambalo ni hifadhi ya mimea na viumbe wa aina mbalimbali. Kuna zaidi ya aina 300 za ndege; aina 150 za samaki; na zaidi ya aina 1,200 za mimea inayotia ndani mivinje na mayungiyungi.
[Sanduku katika ukurasa wa 87]
Wafuasi wa Madhehebu ya Zamolxis Wajiunga na Kanisa Othodoksi la Rumania
Karne kadhaa kabla ya Wakati wa Kawaida, Wagetae na Wadashia, ambao ni wa ukoo mmoja, waliishi katika eneo ambalo sasa linaitwa Rumania. Mungu wao Zamolxis, alikuwa mungu wa anga na wa wafu. Leo, karibu Warumania wote hudai kwamba wao ni Wakristo. Badiliko hilo lilitokeaje?
Muungano wa jamii hizo za Wagetae na Wadashia ulikuwa tisho kubwa wakati Milki ya Roma ilipokuwa ikitwaa Rasi ya Balkani. Ama kweli, Mfalme Decebalus aliyetawala jamii hizo, aliyashinda majeshi ya Roma mara mbili vitani. Hata hivyo, mapema katika karne ya pili W.K., Roma ilitwaa eneo hilo na kulifanya kuwa jimbo lake. Jimbo hilo liliitwa Dashia, nalo lilikuwa na ufanisi mkubwa na liliwavutia walowezi wengi Waroma. Walowezi hao walioana na Wadashia, wakawafundisha Kilatini, na wazao wao ndio mababu za Warumania.
Walowezi na pia wafanya biashara walieneza dini zinazojidai kwamba ni za Kikristo katika eneo hilo. Dini hizo ziliimarika zaidi katika mwaka wa 332 W.K., wakati Maliki Konstantino alipofanya mapatano ya amani na Wagothi, ambao ni Wajerumani walioishi kaskazini ya Mto Danube.
Baada ya Kanisa la Mashariki kutengana na Kanisa la Roma mnamo 1054, watu wengi katika eneo hilo walijiunga na Kanisa Othodoksi la Mashariki. Kanisa Othodoksi la Rumania lilitokana na Kanisa Othodoksi la Mashariki. Mwishoni mwa karne ya 20, Kanisa Othodoksi la Rumania lilikuwa na zaidi ya waumini milioni 16, na hivyo likawa kanisa la Othodoksi la pili kwa ukubwa katika nchi za Balkani.
[Sanduku/picha katika ukurasa wa 98-100]
Tuliimba Huku Mabomu Yakianguka
Teodor Miron
Alizaliwa: 1909
Alibatizwa: 1943
Maelezo mafupi kumhusu: Alijifunza kweli gerezani. Alikuwa katika kambi za mateso za Nazi na kambi za kazi ngumu za Kikomunisti kwa miaka 14.
Mnamo Septemba 1, 1944, vikosi vya Ujerumani vilipoanza kurudi nyuma, mimi, nilikuwa kati ya ndugu 152 na wafungwa wengine walioondolewa kwenye kambi ya mateso ya Bor, huko Serbia, ili wapelekwe Ujerumani. Hatukula kwa siku kadhaa. Tulipopata chakula kidogo, kama vile viazi-sukari vilivyoachwa kando ya barabara karibu na mashamba, tulikila pamoja. Iwapo mmoja alikuwa dhaifu sana asiweze kutembea, wale waliokuwa na nguvu walimbeba kwenye mkokoteni.
Hatimaye, tulifika kwenye kituo cha gari-moshi, tukapumzika kwa saa nne hivi, kisha ili tupate nafasi ya kusafiria tuliondoa mizigo kutoka kwenye mabehewa mawili ya gari-moshi ambayo hayakuwa na paa. Kulikuwa na nafasi ya kusimama tu, nasi hatukuwa na nguo nzito za kujikinga na baridi, bali kila mmoja alikuwa na blanketi alilolitumia kujifunika mvua ilipoanza kunyesha. Tulisafiri katika hali hiyo usiku kucha. Tulipofika kwenye kijiji fulani saa 4:00 asubuhi siku iliyofuata, ndege mbili zilipiga kichwa cha gari-moshi letu kwa mabomu nasi tukalazimika kusimama. Ijapokuwa mabehewa yetu yalikuwa nyuma tu ya kichwa hicho, hakuna aliyeuawa. Kichwa kingine cha gari-moshi kiliunganishwa na behewa letu nasi tukaendelea na safari.
Baada ya kusafiri kilometa 100 hivi, tulisimama kwa saa mbili katika kituo fulani. Tukiwa hapo, tuliwaona wanaume na wanawake fulani waliobeba viazi kwa vikapu. Tulidhani wao ni wachuuzi wa viazi. Lakini tulikosea. Walikuwa ndugu na dada zetu wa kiroho waliokuwa wamesikia kutuhusu na kujua kwamba tulikuwa na njaa. Walimpa kila mmoja wetu viazi vitatu vikubwa vilivyochemshwa, kipande cha mkate, na chumvi kidogo. Hiyo ‘mana kutoka mbinguni’ ilitutegemeza kwa siku nyingine mbili hadi tulipofika Szombathely, Hungaria, mwanzoni mwa mwezi wa Desemba.
Tulikaa Szombathely wakati wa baridi kali, na tulikula hasa mahindi yaliyokuwa yamefunikwa kwa theluji. Katika mwezi wa Machi na Aprili mwaka wa 1945, mji huo maridadi ulipigwa kwa mabomu, na maiti zilizokatwakatwa zikatapakaa barabarani. Watu wengi waliangukiwa na vifusi, na mara kwa mara tuliwasikia wakililia msaada. Tulitumia vijiko na vifaa vingine kuokoa baadhi yao.
Majengo yaliyokuwa karibu na makao yetu yalipigwa kwa mabomu, lakini jengo letu halikupigwa. Kila mara king’ora kilipolia kutahadharisha kwamba mabomu yangeangushwa, watu wote waliogopa sana na kukimbilia usalama. Mwanzoni, sisi pia tulikuwa tukikimbia, lakini baada ya muda hatukuona tena uhitaji wa kufanya hivyo kwa kuwa hakukuwa na mahali salama pa kujificha. Hivyo, tulikaa tu na kujitahidi kutulia. Muda si muda, walinzi wakawa wakibaki nasi. Walisema kwamba Mungu wetu angeweza kuwaokoa wao pia! Mnamo Aprili 1, usiku wetu wa mwisho katika mji wa Szombathely, mabomu mengi sana yaliangushwa katika mji huo kuliko wakati mwingine wowote. Licha ya hilo, tulikaa katika jengo letu huku tukimsifu Yehova kwa nyimbo na kumshukuru kwa sababu ya kuwa na amani ya moyoni.—Flp. 4:6, 7.
Siku iliyofuata tuliamriwa tuanze safari ya kwenda Ujerumani. Tulikuwa na magari mawili yanayokokotwa na farasi, hivyo, tulisafiri kwa magari hayo na pia kwa miguu kwa kilometa 100 hivi hadi tulipofika kwenye msitu fulani uliokuwa kilometa 13 kutoka mahali ambapo majeshi ya Urusi yalikuwa. Tulikaa katika shamba la tajiri fulani usiku kucha, na siku iliyofuata walinzi wetu wakatuachilia. Tulimshukuru Yehova kwa sababu alikuwa ametutunza kimwili na kiroho, kisha tukitokwa na machozi tukaagana na wenzetu na kwenda makwetu. Baadhi yetu tulitembea kwa miguu na wengine wakasafiri kwa gari-moshi.
[Sanduku katika ukurasa wa 107]
Upendo wa Kikristo Waonyeshwa
Katika mwaka wa 1946, eneo la mashariki mwa Rumania lilikumbwa na njaa. Ingawa walikuwa maskini, Mashahidi wa Yehova walioishi katika maeneo ya Rumania ambayo hayakuathiriwa sana na Vita vya Pili vya Ulimwengu walichanga chakula, nguo, na pesa kwa ajili ya ndugu zao wenye uhitaji. Kwa mfano, Mashahidi waliofanya kazi kwenye migodi ya chumvi katika mji wa Sighet Marmaţiei, karibu na mpaka wa Ukrainia, walinunua chumvi kutoka kwenye migodi hiyo, na kuiuza katika majiji na miji iliyokuwa karibu, kisha wakatumia pesa walizopata kununua mahindi. Wakati huohuo, Mashahidi wa Yehova nchini Marekani, Sweden, Uswisi, na nchi nyingine pia walichanga tani tano za chakula.
[Sanduku/picha katika ukurasa wa 124, 125]
Tulikumbuka Mistari 1,600 ya Biblia
Dionisie Vârciu
Alizaliwa: 1926
Alibatizwa: 1948
Maelezo mafupi kumhusu: Kuanzia mwaka wa 1959, alikaa katika magereza mbalimbali na kambi za kazi ngumu kwa zaidi ya miaka mitano. Alikufa mwaka wa 2002.
Tulipokuwa gerezani, tuliruhusiwa kuwasiliana na familia zetu, na kila mwezi waliruhusiwa kutuletea kifurushi cha zawadi chenye uzani wa kilo tano. Wale tu waliomaliza kazi zao ndio waliopewa vifurushi vyao. Tulikuwa tukigawanya chakula katika sehemu 30 hivi ili kila mmoja wetu apate kiasi sawa na mwenzake. Pindi moja tuligawanya matofaa mawili katika sehemu 30 hivi. Ni kweli kwamba kila sehemu ilikuwa ndogo, hata hivyo ilipunguza njaa yetu.
Hata ingawa hatukuwa na Biblia au vichapo vya kujifunzia Biblia, tulidumisha hali yetu ya kiroho kwa kujikumbusha mambo tuliyokuwa tumejifunza kabla ya kutiwa gerezani na kwa kuyazungumzia pamoja na wengine. Tulipanga kwamba kila asubuhi ndugu mmoja akumbuke na kukariri mstari fulani wa Biblia. Kisha tukaurudia-rudia kwa sauti ya chini na kuutafakari asubuhi tulipokuwa katika matembezi ya kulazimishwa yaliyochukua dakika 15 hadi 20. Tuliporudi kwenye seli yetu yenye upana wa meta mbili na urefu wa meta nne ambapo 20 kati yetu tulikuwa tukikaa, tulitumia dakika 30 hivi kutoa maelezo kuhusu mstari huo. Tulikumbuka jumla ya mistari 1,600 ya Biblia. Alasiri, tulizungumzia habari mbalimbali kutia ndani maandiko 20 hadi 30 yanayohusiana na habari hizo. Sote tuliziweka habari hizo akilini.
Mwanzoni ndugu fulani alifikiri kwamba alikuwa mzee sana asiweze kukariri maandiko mengi ya Biblia. Lakini alikuwa tu akipuuza uwezo wake. Baada ya kutusikia tukikariri maandiko mara 20 hivi, yeye pia aliweza kukumbuka na kukariri maandiko mengi, na jambo hilo likamfurahisha sana!
Naam, tulikuwa wenye njaa na dhaifu kimwili, lakini Yehova aliendelea kutulisha na kutuimarisha kiroho. Hata baada ya kuachiliwa, tulihitaji kudumisha hali yetu ya kiroho kwa kuwa maofisa wa Idara ya Upelelezi waliendelea kutunyanyasa wakitarajia kwamba tutakana imani yetu.
[Sanduku katika ukurasa wa 132, 133]
Njia za Kufanya Nakala
Katika miaka ya 1950 habari zilinakiliwa kwa mkono, mara nyingi kwa kutumia karatasi za kaboni. Hiyo ndiyo iliyokuwa njia rahisi zaidi na ifaayo ya kufanya nakala za vichapo vya kujifunzia Biblia. Ingawa njia hiyo ilikuwa ya polepole na yenye kuchosha, ilileta manufaa kwa sababu wale walionakili walikumbuka karibu habari zote. Kwa hiyo, walipofungwa gerezani, waliwatia wengine moyo sana kiroho. Ndugu pia walitumia mashine za kuchapa, lakini ilikuwa lazima kuwajulisha polisi kuzihusu na ilikuwa vigumu kuzipata.
Mashine za kufanya nakala zilizotumia stensili zilianza kutumiwa mwishoni mwa miaka ya 1950. Ili kutengeneza stensili, ndugu walichanganya gundi, jelatini, na nta, kisha wakatandaza mchanganyiko huo juu ya kifaa chenye umbo la mstatili, hasa kioo. Wakitumia wino maalumu walioutengeneza wenyewe, ndugu hao waliandika herufi zilizoinuka kwenye karatasi. Wino ulipokauka, waliweka karatasi hiyo vizuri juu ya ule mchanganyiko na kuibana ili kutengeneza stensili. Hata hivyo, stensili hizo hazikudumu, kwa hiyo walilazimika kutengeneza stensili mpya daima. Na sawa na zile habari zilizonakiliwa kwa mkono, stensili hizo ziliwahatarisha akina ndugu kwa sababu mtu aliyenakili angeweza kujulikana kupitia mwandiko wake.
Kuanzia miaka ya 1970 hadi miaka ya mwisho-mwisho ya marufuku, ndugu walitengeneza na kutumia zaidi ya mashine kumi ndogo za kuchapa ambazo ziliendeshwa kwa mkono. Zilitengenezwa kwa kuiga muundo wa mashine fulani kutoka Austria, nazo zilitumia mabamba ya kuchapia ambayo yalitengenezwa kwa karatasi iliyofunikwa kwa plastiki. Ndugu waliiita mashine hiyo Kinu. Mwishoni mwa miaka ya 1970, mashine chache za kuchapa zenye mabamba ya duara zilinunuliwa, lakini ndugu hawakuweza kuzitumia kwa kuwa walishindwa kutengeneza mabamba ya kuchapia. Hata hivyo, kuanzia mwaka wa 1985, ndugu kutoka nchi iliyoitwa Chekoslovakia, ambaye alikuwa mtaalamu, aliwafundisha akina ndugu jinsi ya kutengeneza mabamba hayo. Baadaye, ndugu waliweza kuchapa vichapo vingi na bora zaidi.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 136, 137]
Yehova Alinizoeza
Nicolae Bentaru
Alizaliwa: 1957
Alibatizwa: 1976
Maelezo mafupi kumhusu: Alifanya kazi ya uchapaji wakati wa utawala wa Wakomunisti na sasa yeye na mke wake Veronica ni mapainia wa pekee.
Nilianza kujifunza Biblia mwaka wa 1972 mjini Săcele na nikabatizwa miaka minne baadaye nikiwa na umri wa miaka 18. Kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku wakati huo, na mikutano ilifanywa katika vikundi vya Funzo la Kitabu la Kutaniko. Hata hivyo, tulipata chakula cha kiroho kwa ukawaida na hata tulionyeshwa picha za slaidi za drama za Biblia zilizoambatanishwa na sauti iliyorekodiwa.
Baada ya kubatizwa, kazi niliyopewa kwanza ilikuwa kuendesha mashine ya slaidi. Miaka miwili baadaye, nilipata pendeleo la kufanya kazi ya kununua karatasi kwa ajili ya uchapaji ulioendeshwa kwa siri. Katika mwaka wa 1980, nilijifunza jinsi ya kuchapa na nilisaidia kuchapa Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na vichapo vingine. Tulitumia mashine ya kufanya nakala na mashine nyingine ndogo ya kuchapa iliyoendeshwa kwa mkono.
Wakati huo, nilifahamiana na Veronica, dada mzuri na mwaminifu kwa Yehova, na tukaoana. Veronica alinisaidia sana katika kazi yangu. Katika mwaka wa 1981, Otto Kuglitsch kutoka ofisi ya tawi ya Austria alinifundisha kuendesha mashine yetu ya kwanza ya kuchapa yenye bamba duara la kuchapia. Tuliweka mashine nyingine ya kuchapa huko Cluj-Napoca mwaka wa 1987, nami nikapewa kazi ya kuwazoeza ndugu kuiendesha.
Baada ya marufuku kuondolewa mnamo 1990, mimi, Veronica, na mwana wetu, Florin, tuliendelea na kazi ya kuchapa na kusambaza vichapo kwa miezi minane. Florin alisaidia kupanga kurasa ambazo baadaye zilibanwa, kukatwa, kuunganishwa, kupakiwa, na kusafirishwa. Katika mwaka wa 2002, sote watatu tulitumwa kufanya utumishi wa upainia katika mji wa Mizil ulio na watu 15,000 na ambao uko umbali wa kilometa 80 kaskazini ya Bucharest. Mimi na Veronica ni mapainia wa pekee, naye Florin ni painia wa kawaida.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 139, 140]
Yehova Aliwapofusha Maadui
Ana Viusencu
Alizaliwa: 1951
Alibatizwa: 1965
Maelezo mafupi kumhusu: Tangu alipokuwa na miaka kumi na kitu, aliwasaidia wazazi wake kunakili vichapo. Baadaye, alisaidia kutafsiri vichapo katika Kiukrainia.
Siku moja mwaka wa 1968, nilikuwa nikinakili Mnara wa Mlinzi kwenye stensili za karatasi ili lichapwe. Si kuwa mwangalifu, na hivyo sikuficha stensili hizo kabla ya kwenda kwenye mkutano wa Kikristo. Mara niliporudi nyumbani usiku wa manane nilisikia gari likisimama. Kwa ghafula, maofisa watano wa Idara ya Usalama wakaingia wakiwa na kibali cha kupekua nyumba yetu. Nilijawa na hofu lakini nikaweza kutulia. Pia, nilimwomba Yehova anisamehe kwa kutokuwa mwangalifu, na nikaahidi kutosahau tena kuficha vifaa vya kazi.
Ofisa aliyewasimamia aliketi mezani karibu na karatasi nilizokuwa nimezifunika upesi kwa kitambaa niliposikia gari likisimama. Aliketi hapo hadi uchunguzi ulipokamilika saa kadhaa baadaye. Ofisa huyo alikivuta-vuta kitambaa hicho mara kadhaa alipokuwa akiandika ripoti yake kando kidogo na karatasi hizo. Ripoti yake ilisema kwamba hawakupata vichapo vyovyote vilivyopigwa marufuku nyumbani kwetu wala yeyote aliyekuwa na vichapo vya aina hiyo.
Hata hivyo, walimpeleka Baba huko Baia-Mare. Mimi na Mama tulisali kwa bidii kwa ajili yake, na pia tukamshukuru Yehova kwa kutulinda usiku huo. Tulifurahi sana Baba aliporudi siku chache baadaye.
Baada ya siku kadhaa, nilipokuwa nikinakili kichapo fulani kwa mkono, nilisikia tena gari likisimama nje ya nyumba yetu. Nilizima taa na kuchungulia kupitia dirisha lililofunikwa. Niliwaona wanaume kadhaa wenye mavazi rasmi na beji zinazong’aa mabegani mwao wakishuka na kuingia kwenye nyumba iliyokuwa ng’ambo ya barabara. Usiku uliofuata kikundi kingine kilishika zamu na hivyo tukajua kuwa walikuwa maofisa wa Idara ya Usalama. Licha ya hilo tuliendelea kunakili vichapo, lakini ili tusigunduliwe, tulivisafirisha kupitia shamba lililokuwa nyuma ya nyumba yetu.
Baba alizoea kusema: “Barabara iliyo kati yetu na adui zetu ni kama ile nguzo ya wingu kati ya Waisraeli na Wamisri.” (Kut. 14:19, 20) Mambo niliyojionea yalithibitisha kwamba Baba hakukosea kusema hivyo!
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 143, 144]
Tuliokolewa na Bomba la Moshi
Traian Chira
Alizaliwa: 1946
Alibatizwa: 1965
Maelezo mafupi kumhusu: Mmoja kati ya ndugu waliochapa na kusafirisha vichapo wakati wa marufuku.
Jumapili moja asubuhi, nilipakia mifuko minane ya vichapo garini mwangu. Haikutoshea kwenye buti ya gari, hivyo niliondoa kiti cha nyuma na kuweka mifuko kadhaa mahali hapo, kisha nikaifunika kwa blanketi na kuweka mto juu yake. Yeyote aliyetazama angefikiri mimi na familia yangu tulikuwa tunaenda ufuoni. Pia, ili kuificha kabisa, niliifunika ile mifuko iliyokuwa kwenye buti kwa blanketi.
Tulimwomba Yehova atubariki, kisha sote watano, yaani, mimi, mke wangu, wavulana wetu wawili na binti yetu, tukaanza safari ya kupeleka vichapo Tirgu-Mures na Brasov. Tuliimba nyimbo za Ufalme tulipokuwa tukisafiri. Baada ya kilometa 100 hivi, tulifika kwenye sehemu ya barabara yenye mashimo mengi. Kwa kuwa gari lilikuwa zito, bomba la moshi liligonga kitu fulani barabarani na kuvunjika. Tulisimama nami nikaweka kipande hicho kilichovunjika kwenye buti juu ya lile blanketi, karibu na gurudumu la ziada, kisha tukaendelea na safari yetu huku gari likipiga makelele wee!
Mjini Luduş, polisi fulani alitusimamisha ili akague gari letu. Baada ya kuangalia namba ya injini na kukagua honi, kifaa cha kufuta kioo, taa, na kadhalika, akataka kuona gurudumu la ziada. Alipokuwa akielekea nyuma ya gari niliinama dirishani na kumwambia mke na watoto wetu: “Salini. Yehova tu ndiye anayeweza kutuokoa sasa.”
Nilipofungua buti, polisi huyo alikiona mara moja kile kipande cha bomba la moshi. “Hiki ni kitu gani?” akauliza. “Utalipa faini!” Alifurahi kupata kasoro fulani na akaacha kulikagua gari. Nilifunga buti, nikatulia na kulipa faini kwa shangwe! Hilo tu ndilo jambo lenye kuogopesha lililotupata, na hivyo ndugu wakapata vichapo vyao.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 147-149]
Kukabiliana na Maofisa wa Idara ya Usalama
Viorica Filip
Alizaliwa: 1953
Alibatizwa: 1975
Maelezo mafupi kumhusu: Alianza utumishi wa wakati wote mwaka wa 1986 naye ni Mwanabetheli.
Wakati mimi na dada yangu Aurica tulipojifunza Biblia na kuwa Mashahidi wa Yehova, watu wa familia yetu walianza kututenda kikatili. Jambo hili lilituumiza lakini pia lilituimarisha kukabiliana na maofisa wa Idara ya Usalama baadaye. Nilikabiliana nao jioni moja mnamo Desemba 1988. Wakati huo nilikuwa nikiishi na Aurica na familia yake katika jiji la Oradea, karibu na mpaka wa Hungaria.
Nilipoenda nyumbani kwa ndugu aliyesimamia kazi ya kutafsiri, nilibeba mkobani gazeti lililokuwa limetafsiriwa ambalo nilikuwa nikilisahihisha. Sikujua kwamba maofisa wa Idara ya Usalama walikuwa wakipekua nyumba hiyo na kuwahoji wenyeji na wageni wote. Nilipoona hilo, nilifaulu kuteketeza gazeti lililokuwa mkobani mwangu bila kugunduliwa. Kisha maofisa hao wakanipeleka pamoja na Mashahidi wengine kituoni kwao ili watuhoji zaidi.
Walinihoji usiku kucha, na siku iliyofuata walipekua nyumba yangu ndogo iliyokuwa katika kijiji jirani cha Uileacu de Munte. Sikuwa nikiishi huko, lakini akina ndugu walitumia nyumba hiyo kuhifadhi vifaa vya kazi ya siri. Walipopata vifaa hivyo, maofisa hao walinirudisha kituoni na kunipiga kwa rungu ya mpira ili niwasaliti wenye vifaa hivyo au wale waliokuwa wakivitumia. Nilimsihi Yehova aniwezeshe kuvumilia kipigo hicho. Nilihisi utulivu, na maumivu yalikuwa yanaisha muda mfupi baada ya kila pigo. Hata hivyo, punde baadaye mikono yangu ilivimba na sikudhani ningeweza tena kuandika. Niliachiliwa jioni hiyo nikiwa mchovu na mwenye njaa sana, na sikuwa na pesa.
Nilitembea hadi kwenye kituo kikuu cha basi huku ofisa fulani akinifuata. Sikuwa nimewaambia wenye kunihoji mahali ninapoishi, hivyo sikuenda moja kwa moja kwa Aurica kwa kuwa nilihofu kwamba ningemhatarisha yeye na familia yake. Sikujua nifanyeje au niende wapi, hivyo nilisali kwa Yehova na kumwambia kuwa nina njaa kali na ninatamani kulala kitandani mwangu. Nilijiuliza, ‘Je, ninaomba jambo lisilowezekana?’
Nilifika kwenye kituo wakati basi lilipokuwa linataka kuondoka. Ijapokuwa sikuwa na nauli nilikimbia na kulipanda. Nilipolipanda niligundua kwamba lilikuwa likielekea kwenye kijiji ambako nyumba yangu ilikuwa. Yule ofisa alifaulu kulipanda, akaniuliza lilikuwa likienda wapi, kisha akashuka. Nilikata kauli kwamba ofisa mwingine angekuwa akiningojea Uileacu de Munte. Nilifurahi kwa kuwa dereva aliniruhusu kusafiri kwa basi hilo. Lakini nilijiuliza, ‘Mbona naenda Uileacu de Munte?’ Sikutaka kwenda kwangu kwa kuwa sikuwa na chakula chochote huko wala hata kitanda.
Bado nilikuwa nikimweleza Yehova mahangaiko yangu tulipofika viungani mwa Oradea, ambapo dereva alisimamisha basi ili rafiki yake ashuke. Mimi pia nikashuka. Basi lilipoondoka, nilifurahi sana, na kwa kujitahadhari sana nikaenda kwa ndugu fulani niliyemjua. Nilipofika mke wake alikuwa akimalizia kupika kimojawapo cha vyakula nivipendavyo sana, yaani, mchuzi wa nyama, mboga, na pilipili. Walinikaribisha kwenye mlo huo.
Baadaye usiku huo, wakati nilipoona kwamba hali ilikuwa salama nilienda kwa Aurica na kulala kitandani mwangu. Naam, Yehova alinipa mambo mawili niliyomwomba, yaani, mlo mzuri na kitanda changu. Tuna Baba mzuri sana!
[Sanduku katika ukurasa wa 155]
Vijana Wanaoendelea Kuzingatia Mambo ya Kiroho
Wakati wa mateso, vijana Wakristo walidumisha utimilifu, na wengi wao walihatarisha uhuru wao kwa ajili ya habari njema. Sasa vijana wanakabili majaribu tofauti na inasikitisha kwamba baadhi yao wameacha kukesha. Lakini wengine wameendelea kukesha. Kwa mfano, kikundi cha vijana katika shule ya sekondari huko Câmpia Turzii huzungumzia andiko la siku wakati wa pumziko la asubuhi. Wanalizungumzia kwenye ua wa shule au kwenye uwanja wa michezo, na mara kwa mara wanafunzi wengine hujiunga nao.
Dada mmoja kijana alisema: “Kusoma andiko la siku pamoja na rafiki zangu hunilinda na kunitenga kwa muda na wanafunzi ambao hawamtumikii Yehova. Pia, ninatiwa moyo kuwa na Mashahidi wengine wa Yehova shuleni.” Mwalimu mkuu na walimu wengine wamewapongeza vijana hao wenye sifa nzuri.
[Sanduku katika ukurasa wa 160]
Kuthibitisha Kisheria Habari Njema
Alhamisi, Mei 22, 2003, Wizara ya Utamaduni na Dini ya Rumania ilitoa taarifa iliyothibitisha kwamba Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova, lililoandikishwa mnamo Aprili 9, 1990, ni shirika la kisheria linalotambuliwa na Serikali. Hivyo, kama dini nyingine zilizoandikishwa, Mashahidi wa Yehova wana haki zote za kisheria zinazohusu dini zilizoandikishwa kisheria kutia ndani haki ya kuhubiri na kujenga Majumba ya Ufalme. Hatua hiyo ya kutambuliwa ndiyo ya mwisho katika mapambano ya kisheria ya miaka mingi.
[Chati/Grafu katika ukurasa wa 80, 81]
RUMANIA—MFUATANO WA MATUKIO
1910
1911: Károly Szabó na József Kiss warudi kutoka Marekani.
1920: Ofisi ya tawi yafunguliwa huko Cluj-Napoca. Ofisi hiyo yasimamia kazi nchini Albania, Bulgaria, Hungaria, Rumania, na nchi iliyoitwa Yugoslavia.
1924: Kiwanda cha uchapaji na majengo kwa ajili ya ofisi ya tawi yanunuliwa huko Cluj-Napoca.
1929: Kazi yasimamiwa na ofisi ya tawi ya Ujerumani na baadaye na Ofisi ya Tawi ya Ulaya ya Kati huko Uswisi.
1938: Serikali yafunga kabisa ofisi ya tawi ya Rumania, huko Bucharest.
1940
1945: Shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova nchini Rumania laandikishwa.
1946: Watu wapatao 15,000 wahudhuria kusanyiko la kwanza nchini humo linalofanyiwa Bucharest.
1947: Alfred Rütimann na Martin Magyarosi watembelea Rumania mwezi wa Agosti na Septemba.
1949: Serikali ya kikomunisti yawapiga marufuku Mashahidi wa Yehova na kutwaa mali zote za ofisi ya tawi.
1970
1973: Ofisi ya tawi ya Uswisi yaacha kusimamia kazi na daraka hilo lakabidhiwa ofisi ya tawi ya Austria.
1988: Wawakilishi wa Baraza Linaloongoza watembelea Rumania.
1989: Serikali ya kikomunisti yaanguka.
1990: Mashahidi wa Yehova waandikishwa kisheria. Makusanyiko yafanywa.
1991: Gazeti Mnara wa Mlinzi la Kirumania lachapishwa sawia na la Kiingereza likiwa na picha zenye rangi.
1995: Ofisi ya tawi ya Rumania yafunguliwa upya huko Bucharest.
1999: Shule ya Mazoezi ya Kihuduma yafanywa kwa mara ya kwanza nchini Rumania.
2000
2000: Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kirumania yatolewa.
2004: Jumba la Kusanyiko la kwanza nchini Rumania lawekwa wakfu huko Negreşti-Oaş.
2005: Kuna wahubiri watendaji 38,423 nchini Rumania.
[Grafu]
(See publication)
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
40,000
20,000
1910 1940 1970 2000
[Ramani katika ukurasa wa 73]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
POLAND
SLOVAKIA
HUNGARIA
UKRAINIA
MOLDOVA
RUMANIA
Satu-Mare
Oradea
Arad
Negreşti-Oaş
Baia-Mare
MARAMUREŞ
Brebi
Bistriţa
Topliţa
Cluj-Napoca
Tirgu-Mures
Ocna Mureş
TRANSYLVANIA
Mil. ya Carpathia
Frătăutii
Bălcăuţi
Ivăncăuţi
Prut
MOLDAVIA
Brasov
Săcele
Mizil
BUCHAREST
WALACHIA
Galaţi
Braila
Mto Danube
DOBRUJA
SERBIA NA MONTENEGRO
BULGARIA
MAKEDONIA
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 66]
[Picha katika ukurasa wa 69]
Károly Szabó na József Kiss walirudi nchini kwao mwaka wa 1911, ili wahubiri ujumbe wa Ufalme
[Picha katika ukurasa wa 70]
Paraschiva Kalmár anayeketi, mume wake, na wanane kati ya watoto wao
[Picha katika ukurasa wa 71]
Gavrilă Romocea
[Picha katika ukurasa wa 71]
Elek na Elisabeth Romocea
[Picha katika ukurasa wa 77]
Ujenzi wa ofisi mpya jijini Cluj-Napoca, mwaka wa 1924
[Picha katika ukurasa wa 84]
Upinzani ulipozidi, majina ya vichapo yalibadilishwa
[Picha katika ukurasa wa 86]
Nicu Palius alitoka Ugiriki ili asaidie kuhubiri
[Picha katika ukurasa wa 89]
Watu wasikiliza hotuba ya Biblia iliyorekodiwa, mwaka wa 1937
[Picha katika ukurasa wa 95]
Martin na Maria Magyarosi (mbele) na Elena na Pamfil Albu
[Picha katika ukurasa wa 102]
Kusanyiko la mzunguko huko Baia-Mare mwaka wa 1945
[Picha katika ukurasa wa 105]
Bango linalotangaza kusanyiko la kitaifa la mwaka wa 1946
[Picha katika ukurasa wa 111]
Mihai Nistor
[Picha katika ukurasa wa 112]
Vasile Sabadâş
[Picha katika ukurasa wa 117]
Kifaa cha kunasa sauti kilichotumiwa na Idara ya Usalama
[Picha katika ukurasa wa 120]
Kambi ya kazi ngumu ya Periprava, karibu na Mto Danube
[Picha katika ukurasa wa 133]
Kile Kinu
[Picha katika ukurasa wa 134]
Veronica na Nicolae Bentaru katika chumba cha siri chini ya nyumba yao
[Picha katika ukurasa wa 138]
Doina na Dumitru Cepănaru
[Picha katika ukurasa wa 138]
Petre Ranca
[Picha katika ukurasa wa 141]
Makusanyiko yaliyofanywa katika miaka ya 1980
[Picha katika ukurasa wa 150]
Shule ya Utumishi wa Upainia ya kwanza iliyofanywa nchini Rumania mwaka wa 1993
[Picha katika ukurasa wa 152]
Roberto na Imelda Franceschetti
[Picha katika ukurasa wa 157]
Licha ya upinzani wa makasisi, maelfu walihudhuria Makusanyiko ya Kimataifa ya mwaka wa 1996, yenye kichwa “Wajumbe wa Amani ya Kimungu”
[Picha katika ukurasa wa 158]
(1) Jengo lenye Majumba ya Ufalme matatu, Tirgu-Mures
(2) Ofisi ya tawi ya Rumania, Bucharest
(3) Jumba la Kusanyiko, Negreşti-Oaş
[Picha katika ukurasa wa 161]
Ndugu wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi, kuanzia kushoto juu kuelekea kulia: Daniele Di Nicola, Jon Brenca, Gabriel Negroiu, Dumitru Oul, na Ion Roman