Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb08 kur. 43-64
  • Kuhuburi na Kufundisha Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhuburi na Kufundisha Ulimwenguni Pote
  • 2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb08 kur. 43-64

Kuhuburi na Kufundisha Ulimwenguni Pote

AFRIKA

IDADI YA NCHI 57

IDADI YA WATU 827,387,930

IDADI YA WAHUBIRI 1,086,653

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 2,027,124

Côte d’Ivoire

Wakaaji wa kijiji cha Bianouan, kilichoko upande wa mashariki, wana kiu ya kweli. Baadhi ya wakaaji hao huwaamsha wahubiri saa 12 alfajiri ili wajifunze Biblia kabla ya kwenda kufanya kazi kwenye mashamba. Wengine wanataka kujifunza Biblia jioni baada ya mikutano ya kutaniko. Siku moja, mwanamke ambaye hakujua kusoma alimwomba ndugu mmoja kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mwanamke huyo alisema kwamba mume wake atamsomea kitabu hicho. Ndugu huyo alimpa kitabu hicho na akamtembelea siku iliyofuata. Mwanamke huyo na mume wake walikuwa wakimsubiri kwa hamu. Mume huyo hakwenda shambani siku hiyo kwa sababu walikuwa wamesoma kitabu hicho usiku mzima. Sasa alitaka kuzungumzia mambo aliyosoma na ndugu huyo. Ndugu huyo alianza kujifunza na wenzi hao.

Benin

Familia moja kubwa inayoishi katika eneo la mbali walianza kujifunza. Baba alikuwa kasisi wa dini ya kienyeji. Majuma mawili tu baada ya kuanza kujifunza, familia yote ilikubali kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Jumamosi jioni, binti mkubwa aliugua ghafula na kufa. Licha ya msiba huo, baba alihudhuria kipindi cha Jumapili (Siku ya Yenga). Jumatatu alisema hivi kuhusu kifo hicho, “Shetani amefanya hivi ili kutuvunja moyo, lakini familia yetu haitamruhusu.” Baba huyo alitoa vifaa vyake vyote vya kanisa kama vile nguo, kofia, mshipi, mafuta ya kuweka rasmi, na fimbo ya mchungaji. Mke wake, aliyekuwa na cheo kanisani, alifanya vivyo hivyo. Kasisi huyo alisema: “Tumevunja ushirika wetu na kanisa hili.” Kisha kama tunavyosoma kwenye Matendo 19:19, alichoma kila kitu hadharani. Familia hiyo inafanya maendeleo mazuri.

Madagaska

Mwaka uliopita katika kijiji chenye wakaaji 500, kasisi mmoja alipewa kitabu Biblia Inafundisha na Shahidi mmoja katika kijiji kingine. Baada ya kukisoma kwa uangalifu, kasisi huyo alisadiki kwamba alikuwa amepata kweli, na aliwaambia washiriki wa kanisa lake mambo aliyokuwa amejifunza. Muda si muda, yeye pamoja na familia yake na watu wengine 20 walijitenga na kanisa hilo na wakaanza kufanya mikutano, kama Mashahidi wa Yehova wanavyofanya kila mahali. Mapainia wa pekee walikuja kuwasaidia. Walijifunza Biblia na watu wengi waliopendezwa na wakapanga mikutano ya Funzo la Kitabu la Kutaniko na Mnara wa Mlinzi ifanywe kwa kawaida. Mnamo Oktoba, watu watano wakawa wahubiri ambao hawajabatizwa, na sasa mapainia hao wamefanya mipango ili kuwe na Mkutano wa Watu Wote na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wastani wa watu 40 hivi wanahudhuria mikutano, na mafunzo ya Biblia zaidi ya 20 yanaongozwa.

Afrika Kusini

Hennie na mke wake walikuwa wanahubiri nyumba kwa nyumba. Walipokuwa wakitembea karibu na ua wa nyumba moja, mbwa mkali alipitisha kichwa chake kwenye seng’enge na kumuuma Hennie mkononi. Alitokwa na damu nyingi sana, kwa hiyo walirudi nyumbani, na mke wake akamwosha na kumfunga bendeji. Hennie alipanga kumwona daktari baadaye. Alimwambia mke wake kwamba hakutaka mbwa amzuie kuhubiri, kwa hiyo walirudi tena kwenye eneo baada ya saa moja hivi. Walianza kuhubiri nyumba iliyokuwa karibu na nyumba yenye mbwa mkali. Baada ya kuhubiri nyumba chache, mwanamume mmoja aliwakaribisha nyumbani kwake. Aliwasikiliza kwa makini na akawaomba wamtembelee tena. Alianza kujifunza Biblia, na baada ya muda mfupi akaanza kuhudhuria mikutano kwa kawaida. Alipojitenga na Kanisa Dutch Reformed, mwanamume fulani mwenye cheo kanisani alimtembelea na akataka kumpa cheo cha shemasi. Hata hivyo, alishikilia uamuzi wake wa kujitenga na kanisa. Anaendelea kufanya maendeleo na amejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

Tanzania

Wakati wa kampeni ya kuhubiri maeneo ya mbali mnamo Oktoba 2005, ndugu tisa kutoka Kutaniko la Iringa walienda eneo la Pawaga, lililo umbali wa kilomita 75 hivi. Walikuwa wamepata habari kwamba kulikuwa na mhubiri aliyeishi sehemu hiyo ya mbali, na hivyo wakaenda kumtafuta. Baada ya kuuliza watu kadhaa, walimpata ndugu huyo ambaye alisema kwamba amekuwa akiishi katika eneo hilo kwa zaidi ya miaka 20 akidhani kwamba kazi ya Ufalme ilikuwa bado imepigwa marufuku nchini Tanzania. Kwa muda huo wote alikuwa akiwahubiria watu na alisema kwamba baadhi yao walipendezwa kikweli na ujumbe wa Biblia. Kila walipotembelea Pawaga, ndugu wa Kutaniko la Iringa walijitolea kukaa kwa muda wa majuma mawili ili kufuatilia upendezi. Mnamo 2006, mapainia wa kawaida wawili walihamia eneo hilo lenye upendezi mwingi. Ndugu aliyeishi mahali hapo alisaidiwa kiroho, na kikundi hicho sasa kina wahubiri tisa. Kwa sasa wanafanya mikutano chini ya mti, lakini kuna mipango ya kujenga mahali padogo pa kukutania wakitumia vifaa vinavyopatikana katika eneo hilo.

Rwanda

Msichana anayeitwa Gentille alijulikana sana kwa sababu ya kufunga mabao alipocheza mpira. Watu walimwita Manayibitego, jina linalomaanisha “Mungu wa Mabao” katika Kinyarwanda. Waitaliano fulani walitambua kwamba ana kipaji na wakamzoeza zaidi. Kisha wakamwalika acheze mpira nchini Italia. Alivutiwa sana na wazo la kuhamia Ulaya na kupata nafasi ya kuwa mchezaji wa mpira anayejulikana sana. Hata hivyo, Gentille alijua kwamba ikiwa angekubali angelazimika kuacha familia yake. Mama yake ni Shahidi, na ingawa Gentille alijifunza Biblia, hakuchukua mambo aliyojifunza kwa uzito. Kucheza mpira ndilo lililokuwa jambo kuu maishani mwake. Gentille alizungumzia jambo hilo na mama yake na akatambua hatari za kiroho zilizohusika. Aliamua kukataa mwaliko huo na badala yake akatanguliza mambo ya Ufalme. Alibatizwa katika kusanyiko la hivi karibuni.

AMERIKA

IDADI YA NCHI 55

IDADI YA WATU 893,357,181

IDADI YA WAHUBIRI 3,367,544

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 3,236,692

Kurasao

Siku moja ndugu fulani alipoenda kuongoza funzo la Biblia, mwenye nyumba alimpa risasi na kumuuliza ikiwa alijua hiyo ni nini. Mwanamume huyo alieleza kwamba kabla ya ndugu huyo kumtembelea kwa mara ya kwanza, kwa miezi kadhaa alikuwa amefikiria kujiua kwa sababu alikuwa amepoteza kazi na familia yake. Akiwa na mawazo ya kulipiza kisasi, alikuwa ameamua kuua watu wanne ambao alifikiri walisababisha matatizo yake. Aliweka bunduki risasi nne na akaweka moja kando ili aitumie ikiwa angehitaji kujiua. Hata hivyo, kabla ya kuondoka nyumbani aliamua kumwomba Mungu msaada. Alifungua televisheni na kutafuta stesheni ya kidini. Wakati huo, Mashahidi wawili walimtembelea na hatimaye wakaanza kujifunza Biblia pamoja naye. Alitupa zile risasi nne, lakini akasahau ya tano. Alipoipata katika mfuko wake, alimwonyesha ndugu huyo, akamsimulia hadithi yote, na akamweleza jinsi ambavyo maisha yake yamebadilika tangu alipoanza kujifunza Biblia. Anasema kwamba watu watano wako hai kwa sababu ya Mashahidi wa Yehova. Sasa anahudhuria mikutano ya kutaniko.

Uruguai

Mashahidi wawili walikaribishwa nyumbani kwa mwanamke fulani. Huku akitokwa na machozi, mwanamke huyo aliwaambia kwamba alikuwa amesali usiku mzima akimwomba Mungu amfunulie mapenzi yake. Makasisi wa kanisa lake walikuwa wamemtembelea ili tu kukusanya fungu la kumi la kiasi kikubwa cha pesa alichokuwa amepokea. Alikuwa amevunjika moyo sana kwa sababu hawakuwa wamemtembelea tena, hata wakati alipokuwa amewaomba msaada akiwa na matatizo. Kwa zaidi ya mwezi mmoja hakuwa ameenda kanisani. Mwishowe, alimwambia kasisi mmoja kwamba alihisi amedanganywa na mafundisho yao yanayopingana. Hata hivyo, badala ya kumfafanulia zaidi mafundisho hayo, kasisi huyo alimwambia kwamba atapokea laana saba kwa kuliacha kanisa. Ndugu hao walimweleza kwamba Mungu wa kweli hutumia malaika wake kuwapata watu wanaotafuta kweli. Aliuliza maswali mengi na mara moja funzo likaanzishwa kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Baadaye, mume wake alianza kushiriki katika funzo hilo, na wote walihudhuria Ukumbusho na hotuba ya pekee. Walipendezwa sana na mafundisho waliyosikia katika Jumba la Ufalme na wakashangaa kwamba hakuna sadaka zinazoombwa. Wote wawili wanafanya maendeleo na wamepata marafiki wengi katika kutaniko.

Chile

Katika eneo lililo huko Cape Horn, kuna mwanamke ambaye anajifunza Biblia. Huenda hilo ndilo funzo la Biblia lililo eneo la kusini kabisa duniani. Yeye ni mke wa mtunzaji wa mnara wa taa katika eneo hilo la mbali. Mwanamke huyo alipokuwa Punta Arenas, dada mmoja aliyekuwa painia msaidizi alijifunza naye Biblia kwa majuma manne mpaka mwanamke huyo alipohamia Cape Horn. Tangu wakati huo, funzo hilo limeongozwa kupitia simu. Anafanya maendeleo mazuri.

Kosta Rika

Katika nchi hiyo, kuna Wahindi wa Guaymi 10,000 hivi, ambao wanaishi hasa katika mji mdogo wa Sixaola ulio karibu na mpaka wa Panama. Wenyeji wengi wamependezwa na kujifunza Biblia. Ili kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu hao, wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee walitumwa kwenye eneo hilo. Wameanza kujifunza lugha ya huko. Mambo mengi yametimizwa kwa msaada wa ndugu na dada 26 Waguaymi. Kwa mara ya kwanza, Ukumbusho ulifanywa katika lugha ya Guaymi, na kulikuwa na hudhurio la watu 264. Tangu wakati huo, kumekuwa na ongezeko kubwa. Kwa mfano, watu 20 hivi walikuwa wakihudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko lenye wahubiri 13. Sasa idadi hiyo imeongezeka na kuwa watu 40. Kwa sababu hiyo, vikundi viwili zaidi vya Funzo la Kitabu la Kutaniko vimeanzishwa.

Panama

Mwalimu wa mazoezi ya mwili anayeitwa Ramiro alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova mnamo 2004. Wakati huo, wanafunzi ambao alipaswa kuzoeza walihitaji saa 12 tu za mazoezi kwa juma ilhali alipaswa kufanya kazi kwa saa 24 kwa juma. Kwa hiyo, msimamizi wa shule alimwambia kwamba atahitaji kutumia muda uliobaki kufundisha wanafunzi hao mambo ya kidini. Msimamizi huyo alimwambia: “Waeleze tu kuhusu Mungu, Yesu, na Biblia.” Ramiro aliwafundisha mambo ambayo alikuwa akijifunza. Mwaka huo, akitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, aliwafundisha wanafunzi 150, waliokuwa katika darasa la sita mpaka nane. Mwaka uliofuata, kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilipotolewa, Ramiro alikuwa amefanya maendeleo na kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Aliendelea kufundisha na wakati huu alitumia kitabu Biblia Inafundisha. Wanafunzi walikuwa wameongezeka kufikia 160 wakiwa wamegawanywa katika vikundi sita tofauti. Matokeo yamekuwa nini? Ramiro pamoja na wahubiri wengine katika kutaniko sasa wanajifunza Biblia na wanafunzi kadhaa. Baadhi ya wazazi wao wamethamini kazi ya Ramiro kwa sababu ya mwenendo mzuri wa watoto wao. Wazazi fulani hata wamehudhuria mikutano ya kutaniko na makusanyiko fulani. Ramiro alibatizwa mnamo Novemba 2006 na anatumia kila nafasi anayopata kufundisha kweli za Biblia.

Guatemala

Huko Guatemala City, mhubiri anayeitwa Jeremy alienda kwenye nyumba ya kijana mmoja aliyejifunza naye Biblia. Nyumba hiyo ilikuwa kwenye kichochoro. Jeremy alibisha mlango, na dada ya kijana yule akafungua mlango na kumwambia kwamba ndugu yake hayupo. Jeremy alipokuwa mlangoni, vijana wawili walimkaribia. Mmoja wao alitoa bunduki na kuielekeza kwenye kichwa cha Jeremy na kumwambia, “Nimelipwa nikuue.” (Baadaye Jeremy aliambiwa kwamba majambazi hufanya hivyo ili kuwaogopesha watu.) Jeremy anasema hivi: “Msichana huyo alifunga mlango, nami nikawauliza wanaume hao, ‘Mnataka nini?’ Mmoja wao akajibu, ‘Unafanya nini hapa?’ Niliwaambia kwamba nilikuwa ninahubiri Neno la Yehova. Akaniambia kwa sauti kali, ‘Nipe ujumbe huo!’ Nilikuwa na wasiwasi na nisijue la kufanya. Nilifungua mkoba wangu na kutoa Biblia. Hilo lilimfanya kijana mwenye bunduki aanze kulia kwa sababu alijua kwamba alikuwa akifanya mambo mabaya. Alinisihi nimsaidie. Alipekua mkoba wangu na kutoa gazeti la Amkeni! lililokuwa likizungumza kuhusu pesa. Kisha kijana huyo mwingine akaanza kupekua mifuko yangu akitafuta kibeti, lakini yule aliyekuwa na bunduki akamwambia: ‘Mwache. Usimpekue.’ Kisha akanishukuru, akanikumbatia, na wakaondoka. Baada ya tukio hilo, nilihisi nikiwa mtulivu na nikamshukuru Yehova kwa kuniokoa.”

Jamhuri ya Dominika

Dada mmoja ambaye ni daktari wa meno alihudhuria semina ya siku moja kuhusu matibabu fulani ya meno. Madaktari wa meno zaidi ya 250 waliohudhuria walipewa nafasi ya kupata masomo ya ziada ya bei ghali huko Ulaya. Ni madaktari wanane tu ambao wangealikwa. Mwishoni mwa semina hiyo, dada yetu aliambiwa kwamba amechaguliwa kuhudhuria masomo hayo bila malipo yoyote. Akiwa ameshangaa, dada yetu alijibu: “Asanteni kwa kunifikiria, lakini sikujaza fomu, na sitaweza kukubali mwaliko huo. Nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, siwezi kutanguliza chochote isipokuwa hali ya kiroho ya familia yangu. Nikikubali masomo hayo, itanibidi kuyakazia uangalifu sana, lakini nina mikutano mitano ya Biblia kila juma ambayo ninapaswa kuikazia uangalifu. Je, unafikiri ningepata shangwe kutokana na masomo hayo na digrii ambayo ningepata ikiwa ningerudi nyumbani na kukuta vijana wangu wawili wakitumia dawa za kulevya au wakiwa na tabia mbaya kwa sababu sikuwapo?”

ASIA NA MASHARIKI YA KATI

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 3,993,686,009

IDADI YA WAHUBIRI 607,112

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 496,577

Israeli

Ella, msichana ambaye ni painia msaidizi, alimwona mwanamke mzee aking’ang’ana kubeba mfuko wa takataka. Ella alimsaidia na kumhubiria kwa ufupi. Mwanamke huyo alimweleza Ella mahali alipoishi, lakini Ella hakumpata ingawa alimtembelea mara nyingi. Mwishowe, mwanamke huyo alifungua mlango. Kwa kuwa mwanamke huyo ana tatizo la kusikia, hakuwa amemsikia Ella alipobisha mara hizo nyingine. Ella alianza kujifunza Biblia pamoja naye. Ingawa mwanzoni hakuwa anaamini kwamba kuna Mungu, alianza kumpenda Mungu na Neno lake. Baada ya miaka miwili, alijiweka wakfu kwa Yehova na akabatizwa hivi karibuni akiwa na umri wa miaka 92.

Mongolia

Mwanamke mmoja mzee anayeitwa Terbish alifanya kazi katika duka la vitabu maisha yake yote. Munkhzaya, dada painia mwenye umri wa miaka 18 alimtembelea. Terbish alimwambia kwamba kwa sababu alikuwa amesoma vitabu vingi angeweza kuelewa haraka kitabu chochote iwe atakisoma kuanzia mwanzo, katikati, au mwisho. Lakini Biblia ilikuwa tofauti. Ingawa aliisoma sana, hakuielewa. Kwenda kanisani hakukumsaidia kuielewa. Kwa hiyo, alijifunza peke yake, akiandika maelezo kuhusu kila andiko. Terbish alitaka hasa kuelewa Waebrania 11:6. Munkhzaya alimfafanulia mstari huo, akaanzisha funzo la Biblia, na kumkaribisha kwenye Jumba la Ufalme. Aliposikia mahali lilipokuwa, Terbish aliuliza: “Je, hilo ndilo jengo lenye maua maridadi nje? Kila mara ninapopita hapo, mimi husimama kuyaangalia. Je, utanionyesha mtu anayeyatunza?” Munkhzaya alifanya hivyo kwa shangwe. Sasa Terbish anajifunza kumhusu Muumba na anahudhuria mikutano. Munkhzaya anasema, “Maua yalimhubiria mwanamke huyo muda mrefu kabla ya mimi kufanya hivyo.”

Japani

Kwa sababu ya kuumwa na miguu, Hiroko mwenye umri wa miaka 78, hawezi kuhubiri kama zamani. Alisali ili apate mwongozo wa Mungu, na akapata kituo cha basi ambacho huwa na watu wengi ambapo anaweza kuketi kwa dakika 30. Yeye hutabasamu na kuwaonyesha watu urafiki. Kuna hospitali karibu, kwa hiyo akiwaona watu wamebeba dawa yeye huwauliza kuhusu afya yao. Ikiwa watu wanajaribu kusoma ratiba ya basi, yeye huwasaidia, na wale ambao hawafahamu eneo hilo, yeye huwaeleza sehemu zinazovutia. Yeye huwasikiliza wanapozungumza na kisha kuwapa magazeti. Yeye hukutana na baadhi ya watu hao kwa kawaida na hivyo anaweza kufanya ziara za kurudia.

Myanmar

Lazaru alikuwa mlanguzi wa dawa za kulevya. Maisha yake yalihusisha dawa za kulevya, uuaji, na mambo mengine maovu. Hata hivyo, dada mmoja painia alipomwonyesha jina la Mungu ni Yehova katika Biblia, mara moja Lazaru alitambua kweli na akakubali kujifunza Biblia. Alijifunza kwa muda mrefu, lakini pole kwa pole alifanya maendeleo ya kiroho. Lakini ilikuwa vigumu kwake kuacha mazoea mabaya. Alipowaambia wenzake kwamba anawaacha, walipatwa na wasiwasi kwani alijua mengi kuhusu kazi yao ya ulanguzi wa dawa za kulevya. Ingawa watu kadhaa walitumwa kumuua, Lazaru alifaulu kuwahepa. Mwishowe alihamia sehemu nyingine ambapo yeye na mke wake walibatizwa.

Taiwan

Wahubiri fulani walisimama kwa muda mfupi nje ya mkahawa mmoja ambao ulikuwa na jina la ajabu—Mkahawa wa Kitabu cha Ezra. Mhubiri mmoja alimuuliza mwenye mkahawa kwa nini alitumia jina Ezra. Alijibu kwamba sikuzote amevutiwa na bidii ya Ezra kwa ajili ya ibada ya kweli. Kwa miaka mingi, mwenye mkahawa huo alikuwa akienda kanisani, lakini alikuwa ameacha hivi karibuni kwa sababu mke wake ambaye ametoka Vietnam hangeweza kuelewa mahubiri yao. Mhubiri huyo alisema kwamba angemletea Biblia ya Kivietnamu na walifurahi sana alipowapelekea alasiri hiyo. Familia yote ilianza kujifunza.

India

Katika mji mmoja ambapo kazi ya kuhubiri inapingwa sana, dada watano walifungwa kwa siku nne kwa sababu ya kuhubiri. Mwanzoni, mlinzi wa jela alikuwa mkali na akawaonya wasihubiri Ukristo ndani ya jela. Hata hivyo, kadiri siku zilivyopita, alibadili mtazamo wake alipoona kwamba dada hao walikuwa wapole na wenye upendo. Dada hao waliwapa wafungwa wengine na mlinzi huyo vyakula na matunda waliyoletewa na akina ndugu. Usiku mmoja, mlinzi huyo aliwasikia dada hao wakizungumzia mambo katika kitabu Mkaribie Yehova. Muda si muda akaanza kushiriki katika mazungumzo yao akiwa ameketi kwenye mlango wa seli yao. Siku ambayo dada hao waliachiliwa, mlinzi huyo alifiwa na mtu wa ukoo. Dada hao walimfariji kwa kumwambia kuhusu tumaini la ufufuo.

Hapo awali, mlinzi mwingine aliwauliza walikuwa wamefanya makosa gani. Dada mmoja alimweleza kwamba kazi ya kuhubiri ilieleweka vibaya kuwa kugeuza imani ya watu kwa njia isiyo halali. Mlinzi huyo alivutiwa na mambo aliyosikia na akasema: “Ingawa mko jela, mnazungumza kwa utulivu sana. Mimi hukasirika haraka na mwenendo wenu unanifanya niaibike. Tafadhali nielezeni ninapozungumza kwa ukali na mnifundishe kuzungumza kama ninyi. Sielewi kwa nini watu wazuri kama ninyi mnafungwa.” Wakati wowote ambao angekuwa na nafasi angewaendea akina dada hao na kuwaambia: “Hebu nielezeni mengi kuhusu Biblia. Hilo hutuliza moyo wangu.” Pia wafungwa wawili wanaokabili mashtaka ya mauaji walivutiwa sana na ujumbe wa Biblia. Akina dada hao waliwahubiria wafungwa hao pamoja na wengine kwa busara. Kwa kuwa sasa wameachiliwa, dada hao wanatafuta njia za kufuatia upendezi waliopata walipokuwa jela.

Indonesia

Painia wa pekee anayeitwa Resmawati alikuwa amemaliza utumishi wa shambani na alipotaka kurudi nyumbani, mwanamke mmoja alimkaribisha nyumbani kwake ili wazungumzie Biblia. Siku tatu baadaye, Resmawati alirudi kumwona. Mwanamke huyo alianza kulia na akamwambia kuhusu mume wake ambaye alikuwa akimtendea vibaya. Resmawati alisoma Waebrania 4:12 na kumwambia kwamba kujifunza Biblia kunaweza kubadili mambo mengi. Alimsimulia kisa cha Tony kilichotajwa katika Kalenda ya Mashahidi wa Yehova ya 2003. Mwanamke huyo alipendezwa na akamwomba nakala ya kalenda hiyo. Alipomtembelea tena, Resmawati alimpelekea kalenda hiyo. Walianza kujifunza kitabu Biblia Inafundisha. Dada huyo alipomtembelea tena, mume wa mwanamke huyo aliomba kushiriki funzo hilo. Alikuwa amesoma kumhusu Tony katika kalenda na akaguswa sana. Jambo la kushangaza ni kwamba mume huyo ambaye pia anaitwa Tony alikuwa na mtazamo na tabia kama za Tony aliyetajwa katika kalenda. Aliposoma kisa cha Tony kwenye kalenda, alimwambia hivi mke na watoto wake: “Ni jina langu, sivyo? Mhubiri huyo alijuaje jina langu na kuandika kunihusu?” Mke wake alimjibu: “Mashahidi hawajui jina lako. Na hata kama wangejua, hawangeweza kuliweka mara moja kwenye kalenda, iwe kalenda ya 2003 au ya 2007!” Alipoona upendezi wa mume wake, alimwuliza kwa busara, “Je, ungependa kuwa kama Tony aliyetajwa kwenye kalenda?” Kwa kushangaza, mume wake akajibu: “Ningependa kujaribu.” Kama Tony aliyetajwa katika kalenda, Tony wa Indonesia ameacha tabia zake mbovu, akakata nywele zake ndefu na kuwa nadhifu. Familia yote inaendelea kujifunza Biblia.

Malasia

Katika sehemu fulani za Borneo, akina ndugu wanatumia picha za setilaiti kwenye Intaneti kutafuta nyumba. Ripoti yao inasema: “Hilo hutusaidia kuona nyumba katika misitu ya mvua. Baadhi ya paa ambazo sisi huona ni mazizi ya mbuzi na nyakati nyingine sisi hucheka sana kuhusu kuwahubiria ‘mbuzi.’ Lakini nyakati nyingine paa hizo huwa nyumba za watu. Hatujawahi kuhubiri eneo hilo la mlimani. Kwa kuwa msitu wa mvua una miti mingi, na si rahisi kufuata vijia vyake, picha za setilaiti hutusaidia.”

ULAYA

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 732,610,687

IDADI YA WAHUBIRI 1,533,790

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 749,911

Hungaria

Dada mwenye umri wa miaka 12 anasema: “Nilibatizwa miezi tisa iliyopita, na nimekuwa nikitumika kama painia msaidizi kwa miezi mitatu sasa. Mama yangu hunisaidia sana. Watu wengi wameniuliza jinsi nimefaulu kufanya upainia msaidizi huku nikiwa shuleni, lakini nafikiri kwamba ingekuwa vigumu kutimiza huduma yangu bila kuwa shuleni. Mimi huhubiri wakati wa mapumziko shuleni. Ninazungumza kuhusu Biblia kwa kawaida na wanafunzi watano. Najifunza Biblia na wawili kati yao. Hivyo, ninaona baraka za Yehova. Kufanya upainia si mzigo bali ni jambo linaloniletea shangwe. Mama yangu ni painia wa kawaida nami pia ningependa kuwa kama yeye. Ningependa kumtumikia Yehova wakati wote.”

Uingereza

Susan alianza kujifunza Biblia mnamo 2001 na akaendelea kufanya hivyo kwa miaka miwili. Wakati huo, ilikuwa vigumu sana kwake kuacha kuvuta sigara. Alijaribu mara nyingi lakini hakufaulu. Kwa sababu hiyo, aliacha kujifunza lakini akaendelea kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Miaka minne baadaye, Susan alihisi kwamba alihitaji kufanya maendeleo ya kiroho, kwa hiyo akaomba msaada kutanikoni. Alianza tena kujifunza, na akaona kwamba habari inayopatikana katika kitabu Mkaribie Yehova inaweza kumsaidia. Kuchunguza kwa undani jinsi Yehova anavyotupenda na jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunampenda kuligusa sana maisha yake. Kwa majuma nane tu aliacha kabisa kuvuta sigara. Susan anahisi kwamba kujifunza kitabu hicho kulimsaidia ajifunze kumtegemea Yehova. Alifanya maendeleo, akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa katika Kusanyiko la Wilaya la “Mfuateni Kristo!”

Estonia

Helgi, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 17 ambaye hakuwa akiishi na wazazi wake waliotalikiana, alipendezwa na kweli na akaanza kujifunza Biblia. Mwanzoni hakuhudhuria mikutano mingi kwa sababu alikuwa akitumia wakati wake mwingi akiimba katika bendi fulani. Alipozidi kuthamini kweli, alianza kufanya mabadiliko maishani. Aliwaeleza washiriki wengine wa bendi yao kwa nini hangeweza kuwatumbuiza watu siku za mikutano. Alijiandikisha kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na akafanya maendeleo na kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Alishiriki katika mashindano ya kitaifa ya uimbaji ambapo mshindi angepewa mkataba na kampuni maarufu ya kurekodi. Ingawa wasanii wengi walikataliwa katika majaribio ya kwanza, Helgi alipendwa na waamuzi na akasonga hadi kwenye hatua iliyofuata ya mashindano hayo. Hata hivyo, mashindano yaliyofuata yangefanywa wakati ambapo alipaswa kutoa hotuba yake ya kwanza kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Angefanya nini? Mama yake ambaye si Shahidi wa Yehova alipendekeza kwamba akose kuitoa hotuba yake au aiahirishe. Helgi alisema kwamba suala halikuwa kutoa hotuba tu bali lilikuwa kuhusu kile alichotanguliza maishani, mambo ya kiroho au ya kimwili. Alifikiria jambo hilo kwa uzito na akaamua kutoa hotuba yake badala ya kwenda kwenye mashindano ya uimbaji. Helgi alitoa hotuba hiyo na mama yake akaheshimu uamuzi wake.

Baadaye ripota mmoja wa televisheni alihudhuria Kusanyiko la Wilaya la “Mfuateni Kristo!” ili kuripoti kuhusu kusanyiko hilo na ubatizo. Alipomwona Helgi akiingia kwenye kidimbwi cha ubatizo, alichukua video ya ubatizo wake na baadaye akamhoji. Jioni hiyo, ripoti hiyo ilikuwa katika habari na ilitia ndani video yake akishiriki kwenye hatua ya mapema ya mashindano ya uimbaji na ikamalizia kwa ubatizo wake huku akisema hivi kwa tabasamu changamfu, “Huu ndio uamuzi bora zaidi nimewahi kufanya.”

Bulgaria

Ivelin ni mfungwa katika gereza la Belene. Aliiandikia hivi ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya nchi hiyo: “Nikiwa huku gerezani, nilipata gazeti Mnara wa Mlinzi na nina maswali mengi. Nimetubu dhambi zangu na ningependa kubadili moyo na tabia yangu. Nawaomba mfanye jambo fulani ngumu ambalo sidhani mnaweza kufanya. Je, mnaweza kuniandikia barua ili nijifunze kumhusu Yehova Mungu? Sijui kama mtanijibu lakini kujifunza tu kumhusu Yehova hunifurahisha. Ningependa kujifunza mengi kuhusu mambo haya si ili nijinufaishe mwenyewe tu bali pia ili niwasaidie wafungwa wengine. Kumbukeni kwamba msiponiandikia, siku moja nitatoka hapa na nitawasiliana nanyi!” Ndugu walifuatilia haraka upendezi huo na sasa wanajifunza na wafungwa kumi katika gereza hilo kutia ndani Ivelin.

Ureno

Painia wa pekee anayeitwa Jana anasimulia hivi: “Siku moja niliposhuka kutoka kwa gari-moshi, nilimwona mwanamume Mchina na nikaamua kumweleza habari njema. Alishangaa kwamba ninaweza kuzungumza Kichina na akaniambia kwamba alikuwa akienda hospitalini kwa sababu mke wake alikuwa karibu kujifungua kupitia upasuaji. Yeye na mke wake hawakujua Kireno, na hospitali ilikuwa imewaomba watafute mtu wa kuwatafsiria. Alikuwa amekata tamaa na akaniomba nimsaidie. Siku iliyofuata, madaktari waliniomba nivae nguo za madaktari ili niambatane na mwanamke huyo alipokuwa akipasuliwa. Wakati wa upasuaji, nilimshika mwanamke huyo mkono naye aliniuliza maswali mengi kuhusu Biblia na kazi yetu. Alijifungua msichana mrembo sana, na kwa kuwa mama huyo alithamini sana msaada wangu, aliniomba nimpe binti yake jina. Nilifikiri kidogo kisha nikachagua jina Sara. Alipenda jina hilo na akataka sana kujifunza kuhusu Sara anayetajwa katika Biblia na Mungu wake. Tulipotoka hospitalini, nilipendekeza kwamba ajifunze Biblia. Hapo awali, yeye na mume wake walikuwa wamekataa kuwasikiliza Mashahidi, lakini kwa sababu niliwasaidia wakati wa upasuaji, walibadili maoni yao mabaya. Walikubali mara moja funzo la Biblia na sasa wanahudhuria mikutano.”

Slovakia

Wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee walikutana na vijana wawili kutoka Afghanistan. Katika muda mfupi walioishi Slovakia, vijana hao walipendezwa na Biblia. Mapainia hao walikutana nao mara kadhaa na kuwapa Biblia na kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mapainia hao waliwaonyesha jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa ili wao wenyewe wajifunze Biblia na wawafunze wengine.

OCEANIA

IDADI YA NCHI 30

IDADI YA WATU 36,829,259

IDADI YA WAHUBIRI 96,691

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 51,122

New Zealand

Ndugu anayeitwa Paul alikutana na mwanamke mmoja alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba alasiri moja. Alipomtolea broshua, mwanamke huyo alimwambia kwamba hivi karibuni mtu fulani wa ukoo alikuwa amemwambia kwamba alihitaji kweli. Asubuhi hiyo alikuwa amesali kwa Yehova akitumia jina lake na akamwomba amtumie mtu fulani. “Saa tatu baadaye,” anasema Paul, “niliwasili mlangoni pake. Isitoshe, nilimtembelea wakati ambapo kwa kawaida hangekuwa nyumbani.” Alikubali kwa furaha kujifunza Biblia na anafanya maendeleo mazuri.

Australia

Armando na mke wake, Elvira, wanaishi Timor Mashariki, nchi iliyo chini ya ofisi ya tawi ya Australia. Mnamo 2006, eneo lao lilivamiwa mara nyingi na kabila lingine, nao walilazimika kukimbia kwa sababu maisha yao yalikuwa hatarini. Walikimbilia kambi ya wakimbizi wakiwa na vitu viwili tu, Biblia ya Armando na broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Walipokutana tena na akina ndugu, Armando na Elvira walianza kujifunza mara mbili kwa juma na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Pia Armando aliwahubiria watu wake wa ukoo ambao wanaishi katika kijiji kidogo kilicho mwendo wa saa nne na nusu kutoka Dili. Familia yake ilipopendezwa na ujumbe wa Ufalme, alifanya mipango mapainia kutoka Baucau wasafiri mwendo wa saa moja na nusu ili kuwafundisha Biblia. Zaidi ya watu 20 walikusanyika ili kuwasikiliza mapainia hao. Baba ya Armando ambaye alikuwa msemaji wa kikundi hicho alisema kwamba walikuwa tayari kutupilia mbali sanamu zao lakini wakauliza ikiwa wangeendelea kulindwa dhidi ya roho waovu. Mapainia hao waliwahakikishia kwamba Yehova angewasaidia kabisa. Kikundi hicho kilitupilia mbali sanamu zao. Sasa zaidi ya watu 25 kutoka kijiji hicho wanajifunza Biblia. Armando anatarajia kubatizwa hivi karibuni na Elvira anafanya maendeleo mazuri.

Guam

Katika kisiwa cha Saipan, ambacho kiko chini ya ofisi ya tawi ya Guam, dada mmoja alifurahi kugundua kwamba mume wake ambaye hapo awali alikuwa mpinzani, alikuwa akisoma kwa siri vichapo vingi alivyoweka nyumbani. Mbali na kusoma Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, alikuwa pia amesoma Vitabu vya Mwaka na kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Siku moja alimwita mkewe na watoto watano kwa ajili ya kile alichokiita “mkutano muhimu wa familia.” Hilo halikuwa jambo la kawaida. Kumbe baba huyo alitaka kuwapa binti zake watatu mashauri kuhusu ndoa. Alikuwa ameandika orodha ya sifa wanazopaswa kuangalia wanapotafuta waume. Baba huyo ambaye si mwamini alikuwa amependezwa sana na simulizi la maisha la Sheila Winfield da Conceição katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2006, hivi kwamba kama Sheila, aliandika orodha ya sifa za mume anayefaa. Aliwashauri binti zake waolewe tu na Shahidi wa Yehova na watafute waume ambao wanampenda Yehova na wanajua Biblia zaidi kuliko wao. Aliwaambia binti zake watatu kwamba ilikuwa tamaa yake wapate furaha ileile aliyokuwa amesoma katika gazeti hilo. Hilo liligusa mioyo yao na kuwapa tumaini kwamba siku moja baba yao atamtumikia Yehova pamoja nao.

Samoa

Hivi karibuni, ndugu mmoja na mke wake kutoka ofisi ya tawi nyingine walitumwa Samoa. Katika nyumba ya kwanza waliyohubiri, ndugu huyo alimwonyesha mwenye nyumba kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Alishangaa alipokaribishwa ndani. Hata hivyo, mwanamke huyo ambaye ni mfanyabiashara aliyestaafu alinyamaza kidogo, kisha akasema, “Nina dakika 45 tu asubuhi ya leo.” Ndugu huyo hajawahi kuambiwa hivyo na mwenye nyumba. Funzo lilianzishwa mara moja. Na ndugu huyo na mke wake waliporudi juma lililofuata, mwanamke huyo aliwakaribisha akiwa ameshika Biblia na kitabu Biblia Inafundisha mkononi. Kuna matumaini kwamba funzo hilo litaendelea.

Visiwa vya Solomon

Painia wa kawaida anayeitwa Emily ndiye Shahidi pekee katika eneo la kisiwa cha San Cristobal. Anaongoza mafunzo ya Biblia 20, na watatu kati yao wamekuwa wahubiri ambao hawajabatizwa kutia ndani wazazi wake. Lance na Diane, ambao ni watumishi wa kimataifa walichukua likizo na wakasafiri kwa muda wa saa 14 kwenye meli iliyosongamana ili kwenda kumsaidia Emily wakati wa Ukumbusho. Lance anasema: “Tulipofika, tulitaka tu kulala, lakini tukaona ni vizuri tumtembelee chifu wa kijiji hicho kwanza. Baada ya kumweleza kusudi la kutembelea eneo hilo, chifu huyo aliuliza: ‘Watu wengi hawajapata mwaliko wa Ukumbusho. Je, wao pia wanaweza kuhudhuria?’ Tukiwa na tabasamu changamfu, tulimwambia kwamba kila mtu amekaribishwa.

“Wakati wa kuanza Ukumbusho ulipokaribia, ni wanawake wawili tu na watoto kadhaa waliokuwa wameketi. Hata hivyo, tuliona watu wengi wakiwa karibu na miti, kwa hiyo tuliwakaribisha. Giza lilipoingia, tuliwasha taa kwa kutumia jenereta. Hotuba ya Ukumbusho iliendelea na kila mtu alisikiliza kwa makini.” Watu 130 hivi walisikiliza hotuba hiyo, kutia ndani mhudumu wa kanisa la Seventh Day Adventist ambaye alitaka Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa sababu ilieleweka kwa urahisi kuliko Biblia aliyotumia. Katika tukio hilo la pekee, mafunzo ya Biblia matano yalianzishwa.

Papua New Guinea

Vijiji viwili vilivyo karibu na mji mdogo vilikuwa chini ya uvutano wa Kanisa Katoliki, na hivyo ilikuwa vigumu kuhubiri huko. Hivi karibuni akina ndugu walitembelea wawakilishi wa vijiji hivyo na wakawaeleza kuhusu kazi yetu ya kuhubiri na kwa nini sisi hupenda kuzungumza na kila mtu. Kwa kupendeza, watu kijiji kimoja walikuwa wametoka tu kuzungumzia jinsi wanavyoweza kuwasaidia vijana kuwa na tabia nzuri. Akina ndugu waliwaambia wawakilishi wa vijiji hivyo kwamba kujifunza Biblia kunaweza kuwasaidia.

Akina ndugu walipewa ruhusa ya kuhubiri huko, na vijana kadhaa wakaanza kujifunza. Watu wa kijiji hicho waliona kwamba vijana hao walianza kuwa na tabia nzuri kwa sababu ya kushirikiana na Mashahidi wa Yehova na kwa hiyo wakaacha kupinga kazi yetu. Polepole, marafiki na wazazi wao wakaanza kujifunza pia, miongoni mwao kulikuwa na binti ya mwalimu wa dini ambaye alikuwa amewatisha akina ndugu. Alimwambia hivi binti yake: “Nilikosea sana wakati ule. Natumaini kwamba Mungu na Mashahidi wa Yehova watanisamehe.” Sasa katika vijiji hivyo viwili, kuna watu 27 wanaohudhuria mikutano kwa kawaida. Angalau wanne wamebatizwa na wanafanya upainia msaidizi. Wanajitahidi kufikia mradi wa kuwa mapainia wa kawaida.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 48]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

[Picha]

Mnara wa taa huko Cape Horn

[Ramani katika ukurasa wa 63]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

San Cristobal

[Picha katika ukurasa wa 44]

Funzo la “Mnara wa Mlinzi” katika kijiji cha Antanandava, Madagaska

[Picha katika ukurasa wa 46]

Kujifunza kitabu “Biblia Inafundisha” pamoja na kikundi cha watu huko Pawaga, Tanzania

[Picha katika ukurasa wa 49]

Funzo la Kitabu la Kutaniko huko Sixaola, Kosta Rika

[Picha katika ukurasa wa 50]

Ramiro akiwa na kitabu “Biblia Inafundisha”

[Picha katika ukurasa wa 53]

Hiroko akihubiri kwenye kituo cha basi

[Picha katika ukurasa wa 58]

Helgi (kulia) akitoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

[Picha katika ukurasa wa 64]

Lance, Diane, na Emily

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki