Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb09 kur. 142-255
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
  • 2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • JINSI KAZI YAO ILIVYOANZA
  • SINEMA YA “PHOTO-DRAMA” ILIFUNGUA NJIA
  • MAPAINIA WATUMWA KWENYE ENEO
  • MATATIZO WALIYOKABILI WAKIFANYA UPAINIA
  • WAVUKA KUINGIA MAKEDONIA
  • KAZI YAPIGWA MARUFUKU
  • KUMCHAGUA AMA TOLSTOY AU YEHOVA
  • MATESO WAKATI WA VITA
  • ALIKUWA MWAMINIFU MPAKA MWISHO
  • WALIHUKUMIWA KIFO
  • MAJARIBU YA USHIKAMANIFU
  • KUTAMBULIWA KISHERIA KWA KADIRI FULANI
  • “WENYE KUJIHADHARI KAMA NYOKA”
  • MAJUMBA YA UFALME YA MAPEMA
  • MIPANGO BORA INACHOCHEA UKUZI WA KIROHO
  • MAENDELEO YENYE KUTIA MOYO HUKO MAKEDONIA
  • TULIKUSANYIKA KWA UMOJA HUKO UJERUMANI
  • MAPAINIA WA YUGOSLAVIA WASAIDIA
  • KUBATIZA WATU KWENYE MASHAMBA YA MPUNGA
  • KUTUMIA KWA BUSARA UHURU ULIOONGEZEKA
  • NDUGU VIJANA WANASIMAMA IMARA
  • KUSANYIKO LA KIMATAIFA LENYE KUSISIMUA
  • JIJI LAZINGIRWA
  • KUPATA MAANDALIZI YA KIMWILI NA YA KIROHO
  • WENYE BIDII LAKINI WAANGALIFU
  • FAMILIA YENYE UAMINIFU
  • MSIMAMO WA KIKRISTO WA KUTOUNGA MKONO UPANDE WOWOTE
  • MISAADA YAFIKA
  • SAFARI ISIYOSAHAULIKA!
  • BAADA YA VITA
  • UPENDO WA KINDUGU WAKATI WA VITA
  • UJUMBE WA TUMAINI WENYE KUTIA NGUVU
  • WAFANYAKAZI WALIOJIDHABIHU
  • “SIAMINI KWAMBA NIMEIONA SIKU HII!”
  • MAJENGO MAPYA YA OFISI YA TAWI NA MAJUMBA YA UFALME
  • KAZI YA UFALME INASONGA MBELE
  • VICHAPO VINAZUIWA
  • UJENZI WA MAJUMBA YA UFALME
  • TAFSIRI YA ULIMWENGU MPYA
  • KUVUKA KUINGIA MAKEDONIA
  • KUWAHUBIRIA WAROMANI
  • ‘MSAADA WENYE KUTIA NGUVU’
  • HALI MBAYA SANA YA KUONGEZEKA KWA BEI KUPITA KIASI
  • KUTAFSIRI BIBLIA
  • UPINZANI WA KIDINI UNAONGEZEKA
  • KUFINYANGWA NA MAONI YA YEHOVA
  • UMOJA KATIKA IBADA NA MAFUNDISHO
  • UKUZI WA KIROHO
  • MAJUMBA YA UFALME NA MAPAINIA
  • HALMASHAURI ZA UHUSIANO NA HOSPITALI
  • KUTOSHELEZA MAHITAJI YA HESABU INAYOONGEZEKA YA WAHUBIRI
  • WAKATI UJAO MZURI
2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb09 kur. 142-255

Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia

ENEO la nchi ambayo hapo zamani iliitwa Yugoslavia lina mambo mbalimbali yenye kuvutia sana. Ulaya ya Kati na Ulaya Mashariki ziko upande wa kaskazini, Ugiriki na Uturuki upande wa kusini, na Italia upande wa magharibi. Eneo hilo lina watu wa utamaduni, lugha, na dini mbalimbali. Hata hivyo, watu wengi wakisikia jina Yugoslavia wanafikiria vita na misukosuko. Tangu kiongozi aliyeitwa Francis Ferdinand alipouawa mwaka wa 1914 mpaka maangamizi ya hivi karibuni ya jamii nzima-nzima, eneo hilo la Rasi ya Balkani limekuwa na migogoro mingi. Watu wa eneo hilo walipopigana ili kupata uhuru walianzisha nchi mbalimbali. Mwishowe, nchi ya Yugoslavia iligawanyika, na sasa katika eneo hilo kuna nchi huru za Bosnia na Herzegovina, Kroatia, Makedonia, Montenegro, Serbia, na Slovenia.

Hata ingawa nchi hizo zimekabili matatizo ya kisiasa, kijamii, na ya kidini kuna mambo yenye kuvutia sana pia, masimulizi kuhusu upendo, umoja, na tumaini. Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo wameshinda ubaguzi na chuki ambayo imevuruga kabisa maeneo hayo ya Balkani. Ingawa wana utamaduni mbalimbali, wana umoja kwa sababu ni washikamanifu kwa serikali iliyo kuu zaidi, Ufalme wa Mungu.

JINSI KAZI YAO ILIVYOANZA

Kazi ya watu wa Yehova ilianza jinsi gani katika eneo hilo? Masimulizi yetu yanaanza na kijana fulani kinyozi anayeitwa Franz Brand, mwenyeji wa eneo la kaskazini la Yugoslavia linaloitwa Vojvodina. Alikuwa ameenda Austria kutafuta kazi. Akiwa huko, alijifunza kweli, kisha akarudi katika mji wao mwaka wa 1925 akiwa Shahidi. Alijiunga na kikundi kidogo ambacho kilikuwa kikisoma na kuzungumzia vitabu vya kujifunzia Biblia vinavyoitwa Studies in the Scriptures, ambavyo walikuwa wamepewa na watu wao wa ukoo walio nchini Marekani.

Kikundi hicho kilitambua kwamba kinapaswa kuhubiri, na vijitabu viwili vinavyoeleza mafundisho ya Biblia vikatafsiriwa katika Kiserbia. Inahuzunisha kwamba kabla ya vijitabu hivyo kugawanywa, kikundi hicho kilitembelewa na ndugu mwenye madaraka aliyeasi tengenezo na kuanzisha dhehebu lake. Alimshawishi kila mtu aachane na Wanafunzi wa Biblia, lakini alishindwa kumshawishi Franz.

Franz alihamia Maribor, Slovenia, ambako alipata kazi kwenye saluni ya kunyoa. Alimhubiria mwenye saluni hiyo ya kunyoa, Richard Tautz, akakubali kweli. Franz na Richard waliitwa vinyozi wanaoamini Biblia, na walitumia mahali pao pa kazi kama kituo cha kuhubiri. Watu waliokuja kunyolewa walisikiliza kwa makini sana hivi kwamba hawakutaka kusogea au kuongea walipokuwa wakinyolewa! Mmoja wao alikuwa mwanasiasa, aliyeitwa Ðuro Džamonja. Mwingine aliitwa Rudolf Kalle, na alikuwa na duka la kurekebisha taipureta. Ðuro na Rudolf walifanya maendeleo ya haraka nao wakabatizwa bila kukawia. Ðuro aliacha siasa na kusaidia kuanzisha shirika la The Lighthouse Society of Bible Students katika Ufalme wa Yugoslavia. Shirika hilo la kisheria liliwawezesha akina ndugu kuhubiri na kufanya mikutano kwa uhuru.

SINEMA YA “PHOTO-DRAMA” ILIFUNGUA NJIA

Mwaka wa 1931, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi ya Uswisi ilituma ndugu wawili ili waonyeshe sinema ya “The Photo-Drama of Creation” katika miji yote mikubwa huko Yugoslavia. Majumba yalijaa watu, nao walitazama kwa makini sana Ðuro alipokuwa akionyesha sinema hiyo. Sinema ya “Photo-Drama” iliwachochea wengi kupendezwa na kweli ya Biblia katika nchi yote. Wakati huo, akina ndugu walikuwa wakifanya mikutano ya Kislovenia na Kijerumani huko Maribor. Na huko Zagreb na maeneo ya karibu, vikundi vya akina ndugu vilikusanyika ili kuzungumzia vichapo ambavyo vilikuwa vimetafsiriwa katika Kikroatia.

Kisha, ndugu wakaamua kuanza kutafsiri Mnara wa Mlinzi katika Kislovenia na Kikroatia. Ilikuwa kazi ngumu sana nyakati hizo. Baada ya gazeti kutafsiriwa, dada alipiga chapa gazeti lote akitumia karatasi ya kaboni, lakini alitokeza nakala 20 tu kwa wakati mmoja. Baadaye, walipata mashini ya kunakili, wakaanza kutokeza nakala 200 za Mnara wa Mlinzi kwa wakati mmoja.

Ndugu na dada walibeba magazeti hayo na kusafiri kwa gari-moshi sehemu mbalimbali za Yugoslavia ili kuhubiri. Nyakati nyingine, ndugu wa Slovenia walikodi lori na kumwajiri dereva ambaye hakuwa Shahidi. Aliwapeleka kwenye eneo ambalo walipanga kuhubiri, kisha aliwangoja mchana kutwa mpaka walipomaliza. Siku hizo, wahubiri hao wa Ufalme hawakuwa wamezoezwa sana, na nyakati nyingine ujumbe wao ulikuwa wa moja kwa moja; hata hivyo, Yehova alibariki bidii yao kwa kuwasaidia kupata watu “waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Mdo. 13:48.

Franc Sagmeister anakumbuka hivi: “Nilisikia kuhusu kweli mwaka wa 1931 kutoka kwa shangazi yangu, Terezija Gradič, na mume wake Franc. Mume wa shangazi alikuwa kati ya wahubiri wa kwanza nchini Slovenia. Hata hivyo, Franc ambaye mwanzoni alipinga dini vikali, alianza kuisoma Biblia kwa bidii. Hilo lilinivutia sana, hivyo, nikajiunga naye katika kujifunza Maandiko. Hata ingawa nilipingwa na familia yangu, nilitaka kuwafundisha wengine mambo mapya niliyojifunza. Kasisi wa parokia alipojulishwa hilo, aliniita mara moja. Akaniambia kwamba sikuruhusiwa kuwa na Biblia kwa sababu singeweza kuielewa. Nilikataa kumpa Biblia yangu. Baadaye, baba yangu alipokufa, nilikutana na kasisi huyo barabarani, naye alikasirika sana kwa sababu sikuwa nimelipia Misa hata moja ya kumwombea baba yangu. Nikamwambia, ‘Niko tayari kulipia Misa 100, hata 1,000 ikiwa zitamsaidia baba.’

“‘Zinasaidia, zinasaidia!’ akasema kasisi.

“‘Ikiwa yuko mbinguni,’ nikasema, ‘hahitaji Misa yako, na ikiwa yuko motoni, hahitaji Misa yoyote.’

“Kasisi akauliza hivi: ‘Namna gani ikiwa yuko toharani?’

“Nilimjibu hivi: ‘Bwana kasisi, unajua vizuri kwamba nina mali nyingi sana. Niko tayari sasa hivi kukupa mali yote hiyo mbele ya wakili ikiwa unaweza kunithibitishia kwa kutumia Biblia kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo inaendelea kuishi anapokufa, kwamba kuna mahali pa moto wa mateso na toharani, na kwamba Mungu ni Utatu.’

“Alinikodolea macho, akawasha sigara, na kuondoka.”

MAPAINIA WATUMWA KWENYE ENEO

Katika miaka ya 1930, wanaume na wanawake wenye bidii walifungua njia ya kuangaza nuru ya kweli katika nchi ya Yugoslavia. Kwa mfano, huko Maribor, Slovenia, Grete Staudinger, Katarina Konečnik, na baadaye Karolina Stropnik walijiandikisha katika ule uliokuja kuitwa utumishi wa upainia wa wakati wa likizo. Upande wa kusini huko Mostar, mji mkuu wa Herzegovina, kiongozi wa kikundi cha wanamuziki anayeitwa Alfred Tuček alitambua kweli naye akawa painia. Dušan Mikić, mwenye umri wa miaka 23 kutoka Zagreb, Kroatia, alipata kijitabu kinachoitwa Wafu Wako Wapi? Yeye pia alifanya maendeleo ya haraka, akabatizwa, kisha akawa painia. Muda si muda, hesabu ya mapainia iliongezeka wakati ndugu na dada wenye bidii walipokuja kutoka Ujerumani.

Kweli ilikuwa ikitia mizizi nchini Yugoslavia, lakini ilipigwa marufuku huko Ujerumani. Ofisi ya tawi ya Uswisi ilipanga kuwatuma mapainia 20 hivi wenye uzoefu nchini Yugoslavia, kama vile Martin Poetzinger, Alfred Schmidt, Vinko na Josephine Platajs, na Willi na Elisabeth Wilke. Ingawa hawakuzungumza Kislovenia au Kiserbo-Kroatia, mapainia hao wenye kujidhabihu walihubiri kwa ujasiri wakitumia kadi za kutoa ushuhuda, wakaweka msingi wa maendeleo ya wakati ujao.

MATATIZO WALIYOKABILI WAKIFANYA UPAINIA

Bidii ya mapainia hao kwa ajili ya Yehova na upendo wao kwa watu uliwasaidia kushinda matatizo ya kujifunza lugha na kukosa pesa. Ilikuwa vigumu pia kusafiri kutoka eneo moja kwenda lingine. Kwa kawaida, walitembea umbali wa kilomita 40 katika milima na mabonde kukiwa na hali mbaya sana ya hewa ili kufika kwenye vijiji vilivyo mbali. Dada mmoja painia anakumbuka kwamba alivua viatu na kutembea miguu mitupu kutoka kijiji mpaka kijiji ili viatu vyake visiharibike. Martin Poetzinger, ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikumbuka sana jinsi alivyosafiri maeneo ya mashambani akiwa amebeba mgongoni mfuko uliojaa vitabu, na kuwahubiria wote waliotaka kusikiliza.

Tatizo la kusafiri lilikwisha wakati ndugu mmoja nchini Uswisi aliponunua baiskeli na kuwapa mapainia hao waaminifu. Baiskeli hizo zilitumiwa katika huduma kwa miaka mingi.

Ingawa watu wa Yugoslavia walijulikana kwa sababu ya ukarimu wao, kulikuwa na upinzani wa kidini na mapainia wetu walipingwa vikali. Makasisi walikuwa na mamlaka kubwa sana juu ya wafuasi wao, hasa katika vijiji vidogo. Nyakati nyingine, makasisi waliwachochea watoto wa shule wawafuate mapainia na kuwarushia mawe. Viongozi wa kidini pia waliwachochea wenye mamlaka ili wawashambulie mapainia, wachukue vitabu vyao, na kuwakamata.

Pindi moja, Willi Wilke alipokuwa akihubiri katika kijiji kimoja cha mashambani huko Kroatia, alisikia watu wengi wenye msisimuko katika uwanja wa kijiji hicho. Yeye na mke wake, pamoja na Grete Staudinger, ambaye pia alikuwa painia, walikuwa wakiwaachia watu kijitabu (kinachoitwa Righteous Ruler, yaani, Mtawala Mwadilifu), ambacho kilikuwa na picha ya Yesu Kristo kwenye jalada. Wilke anasema hivi: “Nilishtuka sana nilipofika na kuona umati wenye hasira wa watu 20 hivi, wakiwa wamebeba mapanga ya kuvuna huku wakiwa wamemzingira mke wangu. Hapo karibu, kikundi kingine cha watu kilikuwa kikiteketeza vijitabu vyetu.”

Mapainia hao hawakujua kwa nini wanakijiji hao wapole walikuwa wamekasirika sana hivyo, na Dada Wilke hangeweza kujua kwa nini walikasirika kwa sababu hakujua vizuri lugha yao. Hata hivyo, Grete aliongea vizuri sana Kijerumani na lugha za wenyeji hao. Alisonga karibu na kuwauliza, “Mabibi na mabwana, mnafanya nini?”

“Hatumtaki Mfalme Peter!” wakamjibu wote kwa pamoja.

“Hata sisi hatumtaki,” Grete akawaambia.

Kwa mshangao, watu hao walionyesha picha iliyo kwenye jalada la kijitabu hicho na kuuliza, “Basi kwa nini mnaeneza habari zake?”

Sasa Grete alielewa kilichowakasirisha. Mwaka uliotangulia wa 1934, Mfalme Alexander wa Kwanza wa Yugoslavia aliuawa, na mwanaye Peter alipaswa kurithi kiti chake cha ufalme. Hata hivyo, watu wa kijiji hicho walitaka kujitawala badala ya kutawaliwa na wafalme wa Serbia. Wanakijiji hao walifikiri kwamba picha ya Yesu Kristo ilikuwa ya Mfalme Peter!

Tatizo hilo lilisuluhishwa na ushahidi kamili ukatolewa kumhusu Mfalme, Yesu Kristo. Watu fulani walioteketeza vijitabu vyao sasa walitaka vingine. Mapainia hao waliondoka kwenye kijiji hicho wakiwa na furaha, nao walihisi kwamba Yehova alikuwa amewalinda.

Mapainia hao walihitaji pia kufikiria desturi za wenyeji. Walipokuwa wakihubiri katika vijiji vyenye Waislamu wengi huko Bosnia, walikuwa waangalifu sana ili wasiwaudhi wenyeji. Kwa mfano, kumtazama kwenye macho mwanamke Mwislamu aliyeolewa kungemkasirisha sana mume wake.

Wakati huo, kulikuwa na makutaniko na vikundi vichache sana nchini. Kwa hiyo, baada ya kuhubiri mchana kutwa katika kijiji kilicho mbali, nyakati nyingine ilikuwa vigumu kupata mahali pa kulala usiku. Mapainia hawangeweza kukodi chumba kizuri cha kulala kwa sababu hawakuwa na pesa za kutosha. Josephine Platajs anakumbuka hivi: “Katika kijiji kimoja kila mtu alikataa kutupa mahali pa kulala kwa sababu walimwogopa kasisi wao Mkatoliki. Usiku ulikuwa umeingia tulipokuwa tukiondoka katika kijiji hicho. Njiani, tuliona mti mkubwa na majani yake makavu yalikuwa yameanguka chini—tulilala kwenye majani hayo usiku huo! Tulitumia mifuko yetu ya kubeba nguo chafu kama mto wa kulalia, na mume wangu aliifunga baiskeli kwa kamba na kuifungilia kamba hiyo kwenye mguu wake. Tuliamka asubuhi na kugundua kwamba tulilala karibu na kisima, kwa hiyo tulipata maji ya kuoga. Yehova alitulinda na pia alitimiza mahitaji yetu ya kimwili.”

Mapainia hao waliona jinsi Yehova alivyowatunza hata katika mambo madogo. Walihangaikia kutangaza habari njema kuliko kuwa na maisha ya starehe.

WAVUKA KUINGIA MAKEDONIA

Alfred na Frida Tuček, ambao walikuwa mapainia, walieneza ujumbe wa Ufalme walipokuwa wakisafiri kutoka Slovenia kwenda Bulgaria. Katika mji wa Strumica, Makedonia, walimhubiria mwenye duka mmoja anayeitwa Dimitar Jovanovič, na kumwazima vitabu fulani. Mwezi mmoja baadaye, walipokuwa wakirudi kutoka Bulgaria, walimtembelea tena. Waliposikia kwamba hakusoma vitabu hivyo, walimwomba avirudishe ili wampe mtu mwingine ambaye angevithamini. Hilo lilimchochea Dimitar kuvisoma. Akawasihi wampe nafasi nyingine ya kusoma vitabu hivyo. Baada ya kuvisoma, aligundua kwamba alikuwa amepata kweli, naye akawa mtu wa kwanza kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova huko Makedonia.

Dimitar aliwafunza kweli ndugu wengine wawili, Aleksa na Kosta Arsov. Muda si muda, kukawa na Mashahidi watatu huko Makedonia. Wakiwa na magazeti, kinanda cha santuri, na santuri zenye hotuba, walianza kuhubiri. Kasisi mmoja wa dini ya Kiinjili ya Methodisti alipata gazeti letu, akampa kijana fulani mwerevu katika kanisa lake, anayeitwa Tušo Carčev. Tušo alifurahia mambo aliyosoma akamsihi kasisi huyo ampe magazeti zaidi. Punde si punde, Tušo alijifunza kwamba watu hawakupaswa kulipwa ili wahubiri habari njema. Kwa msisimuko, alimwambia hivyo yule kasisi, naye akaamua kutomletea magazeti zaidi. Tušo alipata anwani ya ofisi ya tawi ya Maribor katika magazeti hayo na akaandika barua akiomba atumiwe magazeti zaidi. Ofisi hiyo iliwasiliana na Dimitar, Aleksa, na Kosta na kuwaomba wamtembelee Tušo. Baada ya muda kikundi kilianzishwa.

Mwaka wa 1935, ofisi ya tawi ilihamishwa kutoka Maribor, Slovenia, hadi mji mkuu wa Yugoslavia, Belgrade, Serbia. Franz Brand pamoja na Rudolf Kalle walipewa mgawo wa kusimamia ofisi hiyo.

KAZI YAPIGWA MARUFUKU

Broshua iliyochapishwa na Kanisa Katoliki mwaka wa 1933 inathibitisha kwamba ndugu zetu walikuwa na bidii sana siku hizo. Broshua hiyo ilieleza kwa undani sana kuhusu kazi ya kuhubiri ya Mashahidi, na kanisa hilo lilitabiri kwamba kazi yetu ingekoma baada ya muda mfupi. Walikosea kama nini!

Makasisi walikasirishwa na bidii ya kikundi kidogo cha mapainia kaskazini mwa Yugoslavia. Walikasirika hata zaidi wakati mahakama zilipopinga jitihada zao za kukomesha kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Hata hivyo, mwishowe kasisi Myesuiti kutoka Slovenia akawa waziri wa mambo ya ndani. Alianza kwa kuvunjilia mbali shirika la Lighthouse Society; na katika Agosti 1936, kazi ya Mashahidi ikapigwa marufuku na serikali. Wenye mamlaka walifunga Majumba ya Ufalme na kuchukua vitabu vyote. Angalau makutaniko yalikuwa yamejulishwa mapema, na wenye mamlaka hawakupata vitabu vingi. Ili kazi iweze kuendelea, nyumba ndogo ya kuchapishia iliyoitwa Kula stražara (Mnara wa Mlinzi) ilifunguliwa huko Belgrade, na mikutano iliendelea kufanywa katika nyumba za watu.

Huku kazi yetu ikiwa imepigwa marufuku, serikali ilijitahidi hata zaidi kusimamisha kazi ya kuhubiri. Watumishi wa wakati wote walianza kuwindwa, na hali ya ndugu zetu Wajerumani ikawa ngumu zaidi. Wengi wa mapainia hao walikuja Yugoslavia baada ya kazi yetu kupigwa marufuku katika nchi nyingine za Ulaya, na sasa kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku Yugoslavia pia. Ingawa mapainia hao walishikwa na kufungwa gerezani, bidii yao haikufifia. Dada mmoja alisema hivi: “Nyakati nyingine ilikuwa vigumu kutembelewa gerezani, lakini Yehova hakutuacha kamwe. Siku moja ndugu fulani alipokuja kututembelea alinyimwa ruhusa. Alizungumza na askari wa gereza kwa sauti kubwa sana hivi kwamba tuliweza kumsikia. Tulitiwa moyo sana tuliposikia sauti yake tu.”

Wakati huo wa msukosuko, ujasiri ulihitajiwa ili kutafsiri na kusambaza kijitabu kimoja (kinachoitwa Judge Rutherford Uncovers Fifth Column, yaani, Judge Rutherford Afunua Wasaliti), ambacho kilieleza waziwazi jukumu la makanisa ya Katoliki katika kuunga mkono mipango ya kisiasa ya serikali ya Nazi. Kilitafsiriwa katika Kiserbia, Kikroatia, na Kislovenia, na nakala 20,000 zilichapishwa katika kila moja ya lugha hizo. Kijitabu hicho kilipigwa marufuku mara moja, kisha mapainia wa kigeni wakafukuzwa nchini na wakili wa serikali akaagiza wachapishaji wa kijitabu hicho wafungwe gerezani kwa miaka 10 mpaka 15. Ingawa kulikuwa na hatari, wahubiri wachache waliokuwa Yugoslavia walisambaza vijitabu 60,000 haraka-haraka.

Lina Babić, ambaye alijifunza kweli Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikikaribia kwisha na ambaye alishirikiana kwa ukaribu na ndugu na dada waaminifu anasema hivi: “Wakati huo watu walikuwa na hamu kubwa sana ya kujifunza Biblia na walifurahia kuisoma.” Anasimulia hivi: “Kwa kuwa sikuzote tulihitaji kuwa waangalifu, niliamua kunakili vitabu kwa mkono katika kijitabu changu cha kibinafsi. Kwa njia hiyo, ikiwa ningepekuliwa, ingeonekana ni kana kwamba yalikuwa maandishi yangu binafsi.”

KUMCHAGUA AMA TOLSTOY AU YEHOVA

Vita vya ulimwengu vilipokuwa karibu kuanza, mgawanyiko ulitokea katika moja ya makutaniko makubwa zaidi katika Yugoslavia. Watu fulani kutanikoni walikuwa wameanza kueneza maoni ya Leo Tolstoy, mwandikaji Mrusi na mwanafalsafa wa dini. Tolstoy, ambaye zamani alikuwa mshiriki wa Kanisa Othodoksi la Urusi, alisadiki kwamba makanisa yote ya Kikristo yalikuwa yamepotoka na yalikuwa yameharibu kabisa sifa ya Ukristo. Ndugu fulani walifuata maoni hayo ya kutoamini dini zote na hawakutosheka na tengenezo la Yehova. Ndugu aliyekuwa akiongoza Kutaniko la Zagreb alitumia vibaya madaraka yake kuwashawishi wahubiri wengi wakubali maoni ya Tolstoy. Ndugu huyo alikuwa na uvutano mkubwa sana hivi kwamba watu wengi kutanikoni, zaidi ya watu 60, walipitisha azimio la kuacha tengenezo la Yehova.

Rudolf Kalle aliposikia hivyo, alisafiri haraka kutoka Belgrade mpaka Zagreb ili kukutana na kutaniko lote. Alizungumzia kweli za msingi za Biblia ambazo Yehova alikuwa amefunua kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. (Mt. 24:45-47) Kisha akauliza: “Ni nani aliyewafundisha kweli hizo? Ni Tolstoy au ni tengenezo la Yehova?” Rudolf alinukuu Yoshua 24:15, akawaomba wale waliotaka kubaki ndani ya tengenezo la Yehova wainue mikono yao. Ni wawili tu walioinua mikono.

Rudolf anasema, “Lilikuwa jambo lenye kutia uchungu sana.”

Ilionekana kana kwamba mambo yote mazuri yaliyotimizwa katika kutaniko hilo yalikuwa karibu kupotea.

Halafu Rudolf akawaita wale wawili waliokuwa waaminifu waje kwenye jukwaa, kisha akasema: “Tumebaki watatu tu. Sisi ndio tunaowakilisha watu wa Yehova katika jiji hili. Ninawaomba wengine wote waondoke kwenye jumba hili na kwenda zao. Tafadhali, tuacheni peke yetu! Tunataka kumtumikia Mungu wetu, Yehova, nanyi mnaweza kwenda kumtumikia Tolstoy wenu. Hatutaki kushirikiana nanyi tena.”

Kwa sekunde chache, kukawa na kimya kabisa. Kisha, mtu mmoja baada ya mwingine akaanza kuinua mkono wake na kusema: “Mimi pia ninataka kumtumikia Yehova.” Mwishowe, ni yule mtumishi wa kutaniko aliyeasi imani na wafuasi wake wachache tu ndio waliotoka na kwenda. Jaribu hilo la ushikamanifu liliwatia nguvu watumishi waaminifu wa Yehova na kuwatayarisha kwa ajili ya majaribu makali zaidi ambayo wangekabili baada ya muda mfupi.

MATESO WAKATI WA VITA

Mnamo Aprili 6, 1941, jeshi la Ujerumani lilishambulia Yugoslavia. Ofisi ya tawi iliharibiwa na ndege za kivita zilizoshambulia sana Belgrade. Wanajeshi wa Ujerumani waliigawanya nchi ya Yugoslavia. Kwa muda fulani, vita vilikatiza mawasiliano kati ya ndugu wa Betheli ya Serbia na ndugu wa Slovenia, Kroatia, na Makedonia. Hali ilikuwa mbaya zaidi kwa ndugu waliokuwa upande wa kusini kabisa wa Makedonia, kwa kuwa hawangeweza tena kuwasiliana baada ya vita.

Kwa ghafula, akina ndugu walikabili matatizo mapya. Ndugu na dada zetu wapendwa walijaribiwa vikali na kupepetwa ulimwengu wote ulipotumbukia katika vita. Imani na upendo wao kwa Yehova na tengenezo lake vilijaribiwa.

Ofisi ya Belgrade ilifungwa, na kazi ya kuwagawia akina ndugu chakula cha kiroho ilipangiwa Zagreb, Kroatia. Walihitaji kuwa wenye busara zaidi na kufanya mambo kwa siri zaidi kwa sababu badala ya kutozwa faini na kufungwa gerezani walipelekwa katika kambi za mateso na kuhukumiwa kifo.

Majeshi ya Ujerumani yalipoteka na kuigawanya Yugoslavia, kambi za mateso zilijengwa. Huko Kroatia, kambi hizo zilitumiwa kuwatenga na kuwaua watu wa makabila fulani madogo, na watu wachache wasio Wakatoliki, vilevile wafuasi wa dini yoyote ambao walipinga serikali. Huko Serbia, majeshi ya Nazi yalijenga kambi za mateso na kambi za kazi ngumu. Kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote, ndugu zetu zaidi ya 150 kutoka Hungaria walifungwa katika kambi moja karibu na Bor, Serbia. Pia, katika nchi ya Yugoslavia, Mashahidi wa Yehova walitafutwa sana na serikali ya Nazi. Kwa hiyo, walihubiri hasa kwa njia isiyo rasmi. Wahubiri walishauriwa wabebe Biblia zao na kitabu kimoja tu, na waliambiwa mambo ya kusema wanaposhikwa. Walifanya mikutano yao katika vikundi vidogo na hawakujua mikutano mingine ilifanyiwa wapi.

Kwa kuwa vichapo havingeweza kuletwa nchini kwa njia salama, vilichapishwa kisiri-siri. Ndugu walichapisha na kuunganisha magazeti na vijitabu usiku kucha katika sehemu mbalimbali. Pia, walijitahidi sana kupata pesa za kuendesha kazi hiyo ya uchapishaji. Kupitia wafanyabiashara mbalimbali, sikuzote akina ndugu walifanikiwa kupata vitu walivyohitaji kwa kazi ya kuchapa. Chuki ya kitaifa na ya kidini ilipokuwa ikisitawi Yugoslavia, ndugu zetu walikuwa na umoja, na walichanga pesa zao ili kutayarisha chakula cha kiroho kinachookoa uhai. Wangesafirisha kwa njia gani chakula hicho kwa wahubiri walio mbali katika eneo lao?

Stevan Stanković, mfanyakazi wa reli, kutoka Serbia, alikuwa tayari kuwasaidia akina ndugu bila kujali malezi yao. Bila kujali hatari, Stevan alikubali kazi ya kupeleka vitabu kwa siri kutoka Kroatia mpaka nchi ya Serbia iliyokuwa chini ya ulinzi wa wanajeshi. Siku moja polisi waligundua vitabu katika sanduku alilobeba. Walitaka kujua vitabu hivyo vilitoka wapi. Hata hivyo, Stevan alikuwa mshikamanifu kwa ndugu zake, akakataa kuwapa habari hiyo. Polisi walimtia gerezani ili wamhoji halafu wakampeleka kwenye kambi ya mateso ya Jasenovac iliyo karibu. Ndugu yetu mwaminifu aliuawa katika kambi hiyo ambayo ilijulikana sana kwa sababu ya ukatili.

Mihovil Balković, ndugu mwenye busara na mwenye ubunifu, alikuwa fundi wa mabomba huko Kroatia katika nyakati hizo zenye taabu. Zaidi ya kufanya kazi yake, aliwatembelea akina ndugu ili kuwatia moyo na kuwapelekea vitabu. Mjukuu wake anasema hivi: “Pindi moja, alipata habari kwamba gari-moshi ambalo alikuwa amepanda lingekaguliwa katika mji unaofuata. Kwa hiyo, badala ya kushuka katika kituo alichotaka, alishuka katika kituo kilichotangulia. Mji wote ulizingirwa na seng’enge lakini alipata kijia katika shamba la mizabibu. Alibeba vitabu katika mfuko wake wa mgongoni, akaweka chupa mbili za pombe ya kienyeji (rakija) katika sehemu ya juu ya mfuko pamoja na mboga chache. Alipokuwa akitembea polepole katika shamba hilo la mizabibu, alipita handaki moja na kwa ghafula mwanajeshi mmoja akasema kwa sauti kubwa: ‘Simama! Wewe ni nani?’ Alipokaribia, mwanajeshi mmoja alimuuliza, ‘Umebeba nini?’

“‘Unga kidogo, maharagwe, na viazi vichache,’ akajibu.

“Alipoulizwa chupa alizobeba zilikuwa na nini, alisema, ‘Nusa na hata unaweza kuonja.’

“Mwanajeshi huyo alipoonja, Mihovil alisema, ‘Hii ni chupa yako, mwanangu, na iliyobaki ni yangu.’

“Kwa kuwa wanajeshi hao walitosheka na jibu lake na pombe ya rakija, wakasema, ‘Mzee, unaweza kwenda!’

Mjukuu wa Mihovil anamalizia hivi: “Kwa hiyo, vitabu vilifika bila tatizo.”

Bila shaka, Mihovil alikuwa jasiri. Alisafiri katika maeneo yaliyomilikiwa na wanajeshi wa pande mbili zilizopigana. Nyakati nyingine, Mihovil alikutana uso kwa uso na wanajeshi waliounga mkono Ukomunisti; na nyakati nyingine, alikutana na wanajeshi Wafashisti wa Ustašea au wanajeshi waasi wa Četnik. Badala ya kuogopa, alitumia nafasi hizo kutoa ushahidi na kuwaeleza kuhusu tumaini la wakati ujao ambalo linazungumziwa katika Biblia. Alihitaji ujasiri mkubwa sana kwa sababu sikuzote Mashahidi walikabili hatari ya kuuawa. Alikamatwa mara nyingi, akahojiwa, na kufungwa gerezani.

Vita vilipokaribia kwisha, usiku wa Novemba 9, 1944, wanajeshi Wakomunisti walivamia nyumba ya Mihovil, wakachukua vitabu, na kumkamata Mihovil. Inasikitisha kwamba Mihovil hakurudi tena. Baadaye iliripotiwa kwamba alikatwa kichwa.

Josip Sabo alikuwa mvulana tu alipokuwa akipeleka vitabu katika eneo la Slavonia huko Kroatia kwa baiskeli yake. Katika sehemu ya mizigo ya baiskeli yake, aliweka sanduku la kubebea vitabu, na alifunika vitabu kwa matunda ya pea. Wakati huo, kulikuwa na vizuizi na walinzi katika barabara za kuingia katika karibu kila kijiji.

Katika kila kizuizi wanajeshi walimuuliza hivi Josip: “Umebeba nini ndani ya sanduku hilo?”

“Nimebeba matunda ya pea ya mjomba wangu,” alijibu, na wanajeshi hao walichukua tunda moja au mawili. Alipokaribia mwisho wa safari, hakukuwa na matunda ya kutosha kufunika vitabu. Kwa hiyo, Josip alifuata njia isiyotumiwa ili matunda yaliyobaki yasichukuliwe na aweze kulinda vitabu vyenye thamani vilivyofichwa chini yake.

ALIKUWA MWAMINIFU MPAKA MWISHO

Lestan Fabijan, mjenzi wa nyumba kutoka Zagreb, aliwafundisha kweli Ivan Sever, Franjo Dreven, na Filip Huzek-Gumbazir. Wote walibatizwa katika muda wa miezi sita wakaanza kuhubiri na kufanya mikutano. Jioni ya Januari 15, 1943, wanajeshi waliokuwa wakilinda doria walifika kwenye nyumba ya Ivan Sever na kumkamata pamoja na Franjo Dreven na ndugu mwingine, Filip Ilić. Walipekua nyumba yake wakachukua vitabu vyote, na kuwakamata ndugu hao.

Lestan alipata habari kwamba walikuwa wamekamatwa, kwa hiyo akaenda pamoja na Filip Huzek-Gumbazir kumfariji mama na dada ya Franjo. Hata hivyo, wanajeshi Wakomunisti walisikia kuhusu ziara yao, wakawakamata Lestan na Filip. Ndugu hao watano walieleza wakitumia Biblia kwamba walimtumikia Yehova peke yake na kwamba wao ni askari-jeshi wa Kristo. Walihukumiwa kifo kwa sababu wote walikataa kuchukua silaha na kupigana katika vita. Basi, walishikwa mateka.

Usiku mmoja ndugu hao watano waliamshwa usingizini, wakavuliwa nguo zote, na kupelekwa msituni. Walipokuwa wakitembea, walipewa nafasi ya kubadili maoni yao. Wanajeshi walijaribu kuvunja azimio la ndugu hao kwa kuwashawishi wakitumia upendo wao kwa familia zao. Walizungumza kuhusu mke mjamzito wa Filip Huzek-Gumbazir na watoto wake wanne. Aliwajibu kwamba alikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova angewatunza. Franjo Dreven hakuwa na mke wala watoto, kwa hiyo, walimuuliza ni nani ambaye angemtunza mama yake na dada yake.

Walipofika, wanajeshi hao waliwaagiza ndugu hao wasimame katika baridi kali sana. Kisha wakaanza kuwaua. Kwanza, walimpiga risasi Filip Huzek-Gumbazir. Halafu wanajeshi walingoja na kuwauliza wale wengine ikiwa walitaka kubadili msimamo wao. Hata hivyo, ndugu hao walikuwa wameazimia kubaki thabiti. Kwa hiyo, wanajeshi hao walimuua Franjo, halafu Ivan, kisha Lestan. Mwishowe, Filip Ilić, aliyekuwa amebaki, alilegeza msimamo wake akakubali kujiunga na hao wanajeshi. Hata hivyo, miezi mitatu baadaye, alirudi nyumbani akiwa mgonjwa na kusimulia yaliyotendeka. Alijaribu kuokoa uhai wake kwa kulegeza msimamo wake lakini akafa ghafula kwa sababu ya ugonjwa.

Huko Slovenia, ndugu na dada zetu wengi waliteswa. Kwa mfano, Franc Drozg, fundi wa vifaa vya chuma mwenye umri wa miaka 38, alikataa kushiriki katika vita. Kwa hiyo, wanajeshi Wanazi walimuua huko Maribor mnamo Juni 8, 1942. Watu fulani walioshuhudia wanasema kwamba kabla hajapigwa risasi alivishwa shingoni ishara yenye maneno “Mimi si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yoh. 17:14) Imani yake yenye nguvu inathibitishwa na barua aliyoandika dakika chache kabla ya kuuawa, alisema hivi: “Rafiki mpendwa! Rupert, leo nilihukumiwa kifo. Usiomboleze kwa ajili yangu. Ninakutumia salamu zangu za upendo pamoja na wote walio nyumbani. Tutaonana katika Ufalme wa Mungu.”

Wenye mamlaka walifanya yote waliyoweza kukomesha kazi ya kuhubiri, hata hivyo, Yehova alithibitika kuwa Mungu wa wokovu. Kwa mfano, kwa kawaida polisi walikuja ghafula na kuwapanga kwenye foleni wakaaji wote wa eneo fulani na kuchunguza vitambulisho vyao. Watu wote ambao polisi waliwatilia shaka walipelekwa gerezani. Wakati huohuo, polisi wengine walipekua nyumba za watu. Mara nyingi ndugu waliona Yehova akiwalinda kwa kuwa polisi hawakuingia katika nyumba zao huku wakifikiri kwamba tayari walikuwa wamezipekua. Angalau katika pindi mbili, nyumba za akina ndugu zilikuwa na vitabu vingi, na pia mashini za kunakili. Wale walioshiriki katika kazi ya kuhubiri nyakati hizo zenye hatari waliona tena na tena uhakikisho huu wa Biblia ukitimia: “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.”—Yak. 5:11.

WALIHUKUMIWA KIFO

Vita vya Pili vya Ulimwengu viliisha mwaka wa 1945, na kipindi kibaya zaidi cha umwagaji wa damu katika historia ya wanadamu kikafikia mwisho. Ndugu walitumaini kwamba kushindwa kwa Hitler na washiriki wake kungefanya vizuizi viondolewe na kwamba wangepata tena uhuru wa kuhubiri. Kulikuwa na sababu nzuri ya matumaini hayo: Serikali mpya ya Kikomunisti iliyosimamishwa iliahidi kuleta uhuru wa vyombo vya habari, uhuru wa kusema, na uhuru wa ibada.

Hata hivyo, Septemba 1946, ndugu 15 na dada 3 walikamatwa. Kati yao ni Rudolf Kalle, Dušan Mikić, na Edmund Stropnik. Uchunguzi uliendelea kwa miezi mitano. Wenye mamlaka waliwashtaki Mashahidi kuwa wanawatendea vibaya watu na Serikali na kwamba wanahatarisha sana nchi ya Yugoslavia. Walidai kuwa kazi yetu iliongozwa kutoka Marekani na kwamba tulihubiri Ufalme wa Mungu kama kisingizio cha kuharibu usoshalisti na kurudisha ubepari. Kasisi mmoja Mkatoliki alikuwa mstari wa mbele kuwashtaki ndugu kwamba ni wapelelezi wa Marekani wanaojifanya kuwa watu wa dini.

Mahakamani, ndugu hao walioshtakiwa walijitetea wenyewe kwa ujasiri na wakatoa ushahidi mzuri kumhusu Yehova na Ufalme wake. Ndugu mmoja kijana anayeitwa Vjekoslav Kos, alisema hivi: “Enyi mahakimu wenye hekima, nilipata dini hii na mafundisho ya Biblia kutoka kwa mama yangu, na niliabudu Mungu. Wakati wa uvamizi wa Wajerumani, mama alifungwa gerezani. Dada zangu wawili na ndugu yangu walikuwa pia washiriki wa dini ya mama yangu. Walipelekwa pia kwenye kambi ya mateso ya Dachau, ambako walipigwa risasi kwa kuwa walionwa kuwa wakomunisti kwa sababu walimwabudu Mungu. Na ni kwa sababu ya dini hiyohiyo kwamba niko hapa leo mbele ya mahakama nikishtakiwa kuwa Mfashisti.” Mahakama ilimwachilia huru.

Hata hivyo, mahakama hiyo haikuwahurumia ndugu wengine. Watatu kati ya ndugu walioshtakiwa walihukumiwa kuuawa kwa kupigwa risasi, na waliobaki walihukumiwa kifungo cha jela kuanzia mwaka 1 mpaka miaka 15. Hata hivyo, ndugu zetu ulimwenguni pote walipinga vikali na kwa haraka sana ukosefu huo wa haki. Mashahidi wa Marekani, Kanada, Visiwa vya Uingereza, na Ulaya waliandikia serikali ya Yugoslavia maelfu ya barua za malalamiko. Walituma pia mamia ya telegramu. Hata maofisa fulani wa serikali waliandika ili kuwatetea akina ndugu. Kwa sababu ya kuungwa mkono sana hivyo, hukumu za vifo zilibadilishwa na kuwa vifungo vya miaka 20 gerezani.

Hata hivyo, upinzani haukukoma. Miaka miwili baadaye, wenye mamlaka wa Slovenia walimkamata Janez Robas na mke wake, Marija, pamoja na Mashahidi wenzake Jože Marolt na Frančiška Verbec, kwa sababu ya kuhubiri. Shtaka lilisema hivi kwa sehemu: “‘Madhehebu ya wayehova’ . . . yaliwaandikisha washiriki wapya na kuwachochea kupinga mfumo wetu wa kijamii [na] kuwakataza kuwa wanajeshi.” Wakidai kwamba akina ndugu walijaribu kudhoofisha ulinzi wa nchi, wenye mamlaka walitoa hukumu ya vifungo vya gereza pamoja na kazi ngumu kwa muda wa miaka mitatu mpaka miaka sita.

Mwaka wa 1952, kwa sababu ya mabadiliko ya kisiasa, wafungwa wote waliachiliwa huru; na ujumbe wa Ufalme ukaendelea kuhubiriwa. Ahadi hii ya Yehova ilithibitika kuwa ya kweli: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu.”—Isa. 54:17.

Hata hivyo, serikali iliendelea kujitahidi kudhoofisha azimio la akina ndugu la kusimama imara katika imani. Vyombo vya habari vilisema kwamba akina ndugu ni “wagonjwa wa akili” na “watu wenye msimamo mkali wa kiwazimu-wazimu hivi.” Ndugu fulani walianza kuvurugwa na ripoti mbaya zilizoendelea kuenezwa na pia woga wa kuchunguzwa kila mara. Mashahidi waaminifu walipoachiliwa huru kutoka gerezani, wengine katika makutaniko waliwaona kuwa wapelelezi. Hata hivyo, Yehova aliendelea kuyaimarisha makutaniko kupitia ndugu washikamanifu na wakomavu.

Josip Broz Tito alipochukua mamlaka mwishoni mwa Vita vya Pili vya Ulimwengu, ilikuwa wazi kwamba jeshi ndilo lingeongoza mambo nchini Yugoslavia. Wale waliokataa kufanya kazi katika jeshi, haidhuru sababu walizotoa, walionwa kuwa wapinzani wa serikali.

MAJARIBU YA USHIKAMANIFU

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Ladislav Foro, mwenye umri wa miaka 9, kutoka Kroatia, alikuwa kwenye mkutano wa lazima wa watu wa mji huo wakati kasisi mmoja Mkatoliki alipokuwa akihubiri. Baada ya mahubiri hayo, Ladislav alitazama kwa mshangao na kuona nyuma ya pazia la jukwaa kasisi huyo akivua kanzu yake ya kasisi. Ndani ya kanzu hiyo alikuwa amevalia vazi la chama cha Ustaša, na alikuwa amejifunga kiunoni mshipi ambao ulishikilia gruneti au bomu la mkononi. Akiwa ameshika upanga wake, kasisi huyo alipanda juu ya farasi na kupiga kelele: “Akina ndugu, acheni twende tuwageuze watu wawe Wakristo! Mtu yeyote akikataa, mnajua jambo la kufanya!”

Ladislav alijua kwamba mtu wa Mungu hakupaswa kutenda hivyo. Muda mfupi baadaye, akiwa pamoja na mjomba wake alianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi iliyofanywa kisiri-siri. Ingawa hilo liliwakasirisha wazazi wake, Ladislav aliendelea kuhudhuria mikutano na akafanya maendeleo mazuri ya kiroho.

Alipoitwa kujiunga na jeshi katika mwaka wa 1952, Ladislav alikataa waziwazi kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutokuwamo. Maofisa walimhoji tena na tena ili kujaribu kumlazimisha kula kiapo cha kujiunga na jeshi. Pindi moja, walimpeleka kwenye kambi ya jeshi ambamo makurutu au askari wanafunzi 12,000 walikusanyika ili kula kiapo. Walimsimamisha Ladislav mbele ya askari hao wote na wakamwekelea bunduki kwenye bega lake. Papo hapo, akaitupa bunduki hiyo chini. Wakitumia vipaza-sauti ili kila mtu asikie, askari-jeshi walisema kwamba ikiwa Ladislav angeitupa tena bunduki hiyo chini, wangempiga risasi. Alipokataa kwa mara ya pili, walimpeleka na kumsukuma ndani ya shimo lenye urefu wa mita kadhaa lililochimbwa na bomu. Amri ya kumuua ikatolewa, na askari-jeshi mmoja akapiga risasi mara mbili ndani ya shimo hilo, kisha wanajeshi hao wakarudi kambini. Hata hivyo, risasi zilimkosa ndugu huyo!

Usiku huo, maofisa wakamtoa Ladislav ndani ya shimo hilo na wakampeleka gerezani huko Sarajevo. Alipewa barua iliyosema kwamba waamini wengine wa dini yake walikuwa wakilegeza msimamo wao wakati yeye anaendelea kuteseka gerezani pamoja na wafungwa wahalifu. Maofisa hao waliendelea tena na tena kumshinikiza kupitia mazungumzo marefu kama hayo. Hata hivyo, Ladislav alifikiri hivi: ‘Je, nilikubali kumtumikia Yehova kwa sababu ya mtu fulani? Hapana! Je, niko hapa ili nimpendeze mwanadamu? Hapana! Je, uhai wangu unategemea yale ambayo wengine huenda wakasema, kufikiri, au kufanya? Hapana!’

Kufikiri kwa njia hiyo ya kiroho kulimsaidia Ladislav kubaki mwaminifu gerezani mpaka alipoachiliwa huru miaka minne na nusu baadaye. Baada ya muda alitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko na aliungwa mkono na mke wake mshikamanifu, Anica, ambaye alikuwa mwabudu mwenzake.

KUTAMBULIWA KISHERIA KWA KADIRI FULANI

Baada ya kuvunja uhusiano na Muungano wa Sovieti mwaka wa 1948, Tito alipunguza mamlaka ya serikali kuu na hatua kwa hatua akawapa watu uhuru zaidi. Hata ingawa serikali ilikuwa bado ni ya kisoshalisti, dini ilipewa uhuru zaidi.

Serikali iliomba kukutana na wawakilishi wa Mashahidi wa Yehova na ikapendekeza kwamba Mashahidi waandike mkataba mpya ambao ungewezesha kazi yao itambuliwe kisheria. Ndugu waliandika mkataba huo, na mnamo Septemba 9, 1953, Mashahidi wa Yehova wakatambuliwa tena kisheria nchini Yugoslavia.

Wakati nchi nyingine za Kikomunisti zilipokuwa zikiwafukuza ndugu zetu, Mashahidi nchini Yugoslavia walikuwa na uhuru wa kutosha wa kukusanyika katika majumba yaliyochaguliwa. Hilo pia lilitokeza nafasi kwa akina ndugu huko Makedonia kupokea vichapo na kuwasiliana na ofisi ya tawi huko Zagreb. Lakini ingawa Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kisheria kama dini mwaka wa 1953, waliruhusiwa kisheria kuhubiri nyumba kwa nyumba baada ya miaka 38 kupita.

Matatizo yaliendelea. Kwa sababu ya msimamo wa kutokuwamo wa akina ndugu, wenye mamlaka waliona kazi yao ya kuhubiri kuwa njia ya kueneza propaganda. Polisi wa siri wa taifa hilo pamoja na wapelelezi walifanya iwe vigumu sana kufanya kazi ya kuhubiri. Ndugu waliopatikana wakihubiri walikamatwa na kutozwa faini. Ripoti moja ilisema hivi: “Ndugu bado wanakamatwa na kushtakiwa. Hayo ndiyo mambo yanayotendeka hasa huko Slovenia, ambako Kanisa Katoliki lina uvutano mkubwa zaidi na ambako watu wengi wa Yehova wanachunguzwa na polisi na maofisa wao, ambao wanakusudia kuwashika wakijifunza Neno la Mungu. Lakini ndugu wanaonyesha kwamba wameazimia kushinda kusudi la mateso hayo, kwa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”

“WENYE KUJIHADHARI KAMA NYOKA”

Walipokuwa wakihubiri katika maeneo ya mashambani ya Slovenia, ndugu waliwauliza kwanza wenye nyumba ikiwa walikuwa na mayai ya kuuza. Ikiwa bei ilikuwa nzuri, wahubiri walinunua mayai ili kuepuka kutokeza shaka. Baada ya kupata mayai ya kutosha, waliwauliza wenye nyumba zinazofuata ikiwa walikuwa na kuni. Wakati wa majadiliano kuhusu bei, wangeweza kubadili mazungumzo na kuingia katika Biblia ikiwa hilo lilionekana kuwa jambo la busara.—Mt. 10:16.

Katika eneo linalozunguka Zagreb, Kroatia, ndugu walihubiri eneo kwa utaratibu lakini kwa uangalifu sana ili wasigunduliwe. Mbinu moja ilikuwa kuhubiri kila nyumba ya kumi. Kwa mfano, ikiwa walipewa mgawo wa kuhubiri nyumba ya kwanza, wahubiri hao walihubiri nyumba ya 1, 11, 21, 31, na kadhalika. Kupitia jitihada hizo, watu wengi walimjua Yehova. Hata hivyo, kwa sababu ya magumu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, mahubiri yasiyo rasmi yalitumiwa mara nyingi.

Huko Serbia ndugu walikutana katika nyumba za watu binafsi. Damir Porobić anaeleza jinsi mikutano ilivyofanywa katika nyumba ya nyanya yake baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Anasema: “Watu watano hadi kumi walihudhuria. Nyumba ya nyanya yangu ilifaa kwa sababu ilifikika kwa urahisi kutoka kwenye barabara mbili. Hilo liliwawezesha wote kuja na kuondoka kisiri-siri bila kutokeza shaka.”

Veronika Babić alizaliwa huko Kroatia, na familia yake ilianza kujifunza Biblia katikati ya miaka ya 1950. Baada ya kubatizwa mwaka wa 1957, Veronika alihamia Sarajevo, Bosnia, pamoja na mume wake. Milica Radišić, ambaye alitoka katika eneo la Slavonia, huko Kroatia, alibatizwa mwaka wa 1950. Familia yake pia ilihamia Bosnia. Zikishirikiana, familia hizo zilianza kueneza kweli ya Ufalme huko Bosnia. Kama katika sehemu nyingine za Yugoslavia, walipaswa kuhubiri kwa uangalifu. Veronika anaeleza: “Tulishtakiwa kwa polisi, na vichapo vyetu vikachukuliwa. Tulikamatwa, tukahojiwa, tukatishwa kwamba tutatiwa gerezani, na tukatozwa faini. Hata hivyo, hakuna jambo lolote lililoweza kutuvunja moyo au kutuogopesha. Badala yake, yote hayo yaliimarisha imani yetu katika Yehova.”

Milica anakumbuka: “Siku moja, mwanamume mmoja alikuja kwenye Jumba la Ufalme na akaonyesha kupendezwa na Biblia. Alikaribishwa vizuri na hata akakaa kwa muda katika nyumba za akina ndugu. Alitoa maelezo kwa bidii kwenye mikutano. Lakini baadaye binti yetu, akiwa mahali pake pa kazi, alimwona mwanamume huyo akihudhuria mkutano wa polisi wa siri. Kisha, tukatambua kwamba alikuwa ametumwa na polisi ili kutupeleleza. Kwa kuwa uhusiano wake na polisi haukuwa tena jambo la siri, aliacha kuja.”

MAJUMBA YA UFALME YA MAPEMA

Kabla ya kuandikishwa kisheria na serikali, ilikuwa kinyume cha sheria kwa Mashahidi wa Yehova kukusanyika katika nyumba za watu binafsi, na akina ndugu walikabili hatari ya kukamatwa walipokusanyika. Hata hivyo, hata baada ya kuruhusiwa kukusanyika hadharani, ilikuwa vigumu kupata mahali pa kukusanyikia, kwa kuwa watu wengi hawakuwapenda Mashahidi wa Yehova na hivyo walikataa wakodi nyumba zao. Kwa hiyo, Mashahidi waliamua kununua majengo ambamo wangekutania.

Punde si punde, ndugu walipata jengo la kiwanda katikati ya mji wa Zagreb, Kroatia. Waliligeuza jengo hilo kuwa Jumba la Ufalme maridadi lenye viti 160 hivi na wakaongeza ofisi ndogo ya kuchapishia vichapo. Jumba hilo la Ufalme lilitumiwa pia kwa ajili ya makusanyiko na lilianza kutumiwa mwaka wa 1957 wakati kusanyiko la kwanza la wilaya lilipofanywa kwa ajili ya Mashahidi kutoka sehemu zote za Yugoslavia. Miaka michache baadaye, ndugu walinunua nyumba moja katikati ya mji wa Zagreb kwenye Barabara ya Kamaufova, ambayo ilitumiwa na familia ya Betheli mpaka mwaka wa 1998.

Katika mwaka wa 1957, ndugu walinunua jengo huko Belgrade, Serbia, ambalo lilitumiwa kama Jumba la Ufalme na pia kama ofisi ya kufanyia kazi ya Betheli. Baadaye, walipata nyumba ya farasi huko Ljubljana, Slovenia, na wakaigeuza kuwa Jumba la Ufalme. Katika mwaka wa 1963, waligeuza kibanda kimoja cha kurekebishia magari huko Sarajevo kuwa jumba, ambalo lilitumiwa na kutaniko la kwanza huko Bosnia na Herzegovina. Baadhi ya majengo hayo yalihitaji kurekebishwa kabisa; lakini ndugu walijitoa kwa ukarimu na kutoa mali zao, na Yehova alibariki jitihada zao.

MIPANGO BORA INACHOCHEA UKUZI WA KIROHO

Katika mwaka wa 1960, waangalizi wanaosafiri walipewa migawo ya kuyasaidia na kuyatia moyo makutaniko. Ndugu wengine waliombwa watumike wakiwa waangalizi wa mizunguko wa “miisho-juma.” Ndugu hao walikubali kutumia siku zao za likizo ili kusafiri na kuwatia moyo akina ndugu na kuwasaidia kuwa na umoja katika siku hizo za mapema.

Henrik Kovačić, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Kroatia, anakumbuka: “Kwa karibu mwaka mmoja, nilitumika pamoja na mke wangu nikiwa mwangalizi wa mzunguko mwishoni mwa juma, na baadaye nikawa mwangalizi anayesafiri wa wakati wote. Ndugu walikuwa maskini sana, na mara nyingi tulikaa mahali ambapo hapakuwa na mabomba ya maji wala vyoo vinavyotumia maji. Lakini ndugu walithamini sana ziara zetu na walituonyesha upendo na ukarimu wa pekee sana. Mara nyingi, walituachia vitanda vyao na walitupa chakula, ingawa wao wenyewe walikuwa na mapato kidogo sana. Katika makutaniko fulani, ili tusiwe mzigo kwao, tulikaa katika nyumba tofauti kila usiku.”

Šandor Palfi, ambaye sasa anatumika katika Halmashauri ya Nchi huko Serbia, anasema: “Kutumika nikiwa mwangalizi mwishoni mwa juma lilikuwa jambo lenye kusisimua sana, ingawa haikuwa rahisi. Ndugu walitungojea kwa hamu sana. Walikuwa maskini, lakini walifanya yote waliyoweza ili kutupa kile kilichokuwa bora zaidi. Kwao, ziara ya mwangalizi wa mzunguko ilikuwa pindi ya pekee sana.”

Huku akitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko, Miloš Knežević alisimamia pia kazi ya ofisi ya tawi huko Yugoslavia. Kwa makumi ya miaka ya utawala wa Ukomunisti, Ndugu Knežević alikuwa mstari wa mbele katika kushughulikia kesi nyingi za kisheria zilizowakabili ndugu zetu.

MAENDELEO YENYE KUTIA MOYO HUKO MAKEDONIA

Katika mwaka wa 1968, kijana mmoja kutoka Kočani, Makedonia, alikuwa akisoma kwenye chuo kimoja huko Zagreb, ambako alipata kweli. Aliporudi nyumbani, aliwahubiria habari njema watu wake wa ukoo na marafiki.

Stojan Bogatinov, ambaye alikuwa mtu wa kwanza kubatizwa kutoka Kočani, anakumbuka: “Kijana huyo alikuwa binamu yangu. Nilikuwa mhudumu wa hoteli, na mara nyingi mimi na wafanyakazi wenzangu tulizungumza kuhusu dini. Pindi moja baada ya mazungumzo yetu, mshiriki wa Kanisa Othodoksi aliingia hotelini kula chakula. Nilipokuwa nikimhudumia, nilimuuliza ikiwa ningeweza kupata Biblia kutoka katika kanisa lao, kwa sababu nilitaka sana kujifunza kuhusu Mungu. Aliniambia kwamba angejaribu kuniletea nakala moja. Punde si punde, nilipata nakala yangu ya ‘Agano Jipya.’ Nilifurahi sana hivi kwamba baada ya kazi nilirudi nyumbani haraka ili nianze kuisoma.

“Nikiwa njiani, nilishangaa kumwona binamu yangu, aliyerudi kutoka Zagreb. Alinialika nyumbani kwake, lakini nikamwambia kwamba singeweza kwenda kwa sababu nilikuwa na msisimko mwingi wa kurudi nyumbani ili nisome Biblia yangu. ‘Nina kitu fulani ambacho kitakupendeza,’ binamu yangu akanijibu. ‘Nyumbani nina vitabu ambavyo vitakusaidia kuielewa Biblia.’ Tulienda nyumbani kwake, na nilifurahi kuona kwamba alikuwa na Biblia nzima, broshua kadhaa, na magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi ya Kikroatia. Alinipa vichapo hivyo, nikaanza kuvisoma mara moja. Papo hapo, nilitambua kwamba nilikuwa nikisoma kitu fulani cha pekee. Sikujua jambo lolote kuhusu Mashahidi wa Yehova, lakini nilitaka kuwajua.

“Binamu yangu aliporudi Zagreb, nilienda pamoja naye. Nikiwa huko, Shahidi mmoja mkarimu, Ivica Pavlaković, alinialika nyumbani kwake, ambako nilikaa kwa muda wa siku tatu. Wakati huo niliuliza maswali mengi, na nyakati zote alijibu maswali yangu kwa kutumia Biblia, jambo ambalo lilinivutia sana. Nilihudhuria mkutano wa kutaniko na nilitiwa moyo na ushirika mchangamfu wa kindugu.

“Ivica alinipeleka Betheli huko Zagreb, na nilitoka huko nikiwa mwenye furaha na nikiwa na vichapo vingi. Baada tu ya siku chache ambazo singeweza kusahau, nilirudi Kočani nikiwa na hazina ya kiroho niliyopata. Hakukuwa na Mashahidi walioishi karibu, hivyo tulianza kuandikiana kwa ukawaida na Ivica. Barua zangu zilijaa maswali mengi, na Ivica aliniandikia majibu ya maswali hayo. Kadiri nilivyojifunza zaidi, ndivyo nilivyowaambia wengine mambo niliyojifunza, na mke na watoto wangu wakaanza kupendezwa. Punde si punde, familia yetu iliungana katika kweli, na tukajifunza mengi kuhusu Biblia. Tulifurahi, na kwa bidii tulianza kuzungumza na watu wetu wa ukoo na marafiki kuhusu habari njema; na wengi walitusikiliza. Lakini pamoja na kuhubiri mateso pia yalifuata.”

TULIKUSANYIKA KWA UMOJA HUKO UJERUMANI

Ingawa ndugu zetu huko Yugoslavia hawakuwa wametenganishwa kama wale wa nchi nyingine za Kikomunisti, walikuwa wachache na walitamani kuona upendo wa ndugu zetu wa ulimwenguni pote. Kwa hiyo, walipopata habari kwamba Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” lilipangwa kufanyika mwaka wa 1969, waliomba serikali iwaruhusu kutoka nchini ili wahudhurie kusanyiko hilo. Wazia furaha waliyohisi walipokubaliwa kusafiri!

Kusanyiko lilifanywa katika uwanja mkubwa huko Nuremberg, Ujerumani, mahali ambapo Hitler, aliyetisha kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova, alihudhuria maonyesho ya wanajeshi wake makumi machache ya miaka mapema. Programu ilitolewa katika lugha nyingi, na wajumbe kutoka Yugoslavia walisisimuka kujua kwamba kungekuwa na programu mbalimbali katika lugha zao katika eneo lenye miti mingi karibu na uwanja mkuu. Jukwaa kubwa liligawanya uwanja huo wa michezo ili nusu ya wajumbe, walioketi upande mmoja, wasikilize programu katika Kiserbia na Kikroatia, huku ile nusu nyingine, upande wa pili wa jukwaa, wasikilize programu katika Kislovenia. Programu hiyo ya siku nane iliongeza sana ujuzi na imani ya akina ndugu.

Magari ya moshi na mabasi yalikodiwa kutoka sehemu zote za Yugoslavia ili kupeleka wajumbe Ujerumani. Ndugu mmoja kutoka Kroatia aliyesafiri kwenda Ujerumani anaeleza hivi: “Tukiwa wenye msisimko wa kuungana na ndugu na dada zetu, tulionyesha kwa fahari ishara zilizotangaza kusanyiko hilo kupitia madirisha ya gari-moshi letu.”

Ndugu walifurahi kuwaona na kuwasikiliza Nathan Knorr na Frederick Franz kutoka makao makuu ya ulimwenguni. Mjumbe mmoja anakumbuka: “Ilikuwa vigumu kwetu kuzuia furaha yetu walipokuja kwenye sehemu yetu ya uwanja ili kutusalimu.” Baraka ambazo ndugu wa Yugoslavia walipata zilipita kwa mbali jitihada nyingi walizofanya ili kuhudhuria kusanyiko hilo. Milosija Simić aliyesafiri kutoka Serbia anasema: “Ilinigharimu mishahara ya miezi miwili ili kusafiri kwenda kusanyikoni, na ilikuwa vigumu kupata siku kumi za likizo kazini. Sikuwa na uhakika ikiwa ningeendelea na kazi yangu baada ya kurudi kutoka kusanyikoni, lakini niliazimia kusafiri. Lilikuwa kusanyiko zuri ajabu! Mpaka leo hii, miaka 40 hivi baadaye, bado ninatokwa na machozi ya shangwe ninapokumbuka kusanyiko hilo.” Baada ya kujiunga na Mashahidi wenzao kutoka kila sehemu ya Yugoslavia ili kufurahia umoja wa undugu wetu wa ulimwenguni pote, akina ndugu walirudi nyumbani wakiwa wametiwa nguvu kukabiliana na matatizo yaliyokuwa mbele yao.

MAPAINIA WA YUGOSLAVIA WASAIDIA

Mapainia wa Ujerumani waliokuja mwanzoni mwa miaka ya 1930 walifanya kazi kubwa ya kueneza habari njema. Sasa kwa sababu ya kuongezeka kwa hesabu ya wahubiri, ndugu na dada wengi wa Yugoslavia walianza utumishi wa painia. Kwa mfano, Slovenia ilikuwa tayari kutuma mapainia wenye uzoefu kwenye sehemu za mbali zaidi za Yugoslavia ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa zaidi. Kwa ujasiri, mapainia hao walikabiliana na tatizo la kujifunza tamaduni na lugha mpya.

Jolanda Kocjančič anakumbuka: “Nilifika Priština, ambalo ndilo jiji kubwa zaidi huko Kosovo. Kialbania na Kiserbia zinazungumzwa huko. Ingawa mimi na Minka Karlovšek hatukuzungumza lugha hizo, tuliamua kuanza kuhubiri, na hivyo ndivyo tulivyojifunza lugha hizo. Kwenye nyumba ya kwanza, tulikutana na mtoto wa kiume wa kwanza wa mjane mmoja ambaye alikuwa wa asili ya Kicheki. Tulianza mazungumzo yetu katika Kislovenia tukichanganya na maneno fulani ya Kiserbia, kwa kusema, ‘Tungependa kuzungumza na familia yenu kuhusu habari njema kutoka katika Biblia.’

“‘Ingieni,’ akajibu, ‘mama yangu amekuwa akiwangojea.’

“Tulipoingia, mama huyo, Ružica, alikuja haraka kukutana nasi. Alisema kwamba siku 14 zilizopita alisali kwa Yehova akimwomba atume mtu fulani ili amfundishe kumhusu. Dada yake, ambaye ni Shahidi wa Yehova katika ile inayoitwa sasa Jamhuri ya Cheki, alimwambia tena na tena asali kwa Yehova na kumwomba msaada. Ružica aliamini kabisa kwamba ziara yetu ilikuwa jibu kwa sala yake. Hivyo, Ružica alitufundisha Kiserbia, na sisi tukamfundisha kweli kutoka katika Biblia. Wanafunzi ambao walikuwa wanakodi nyumba yake walijiunga nasi katika funzo la Biblia. Mmoja wa wanafunzi hao alitupa kamusi ya Kialbania, ambayo ilitusaidia kujifunza lugha hiyo.”

Huko Montenegro, Zoran Lalović, alikuwa mvulana mdogo alipopewa Biblia na painia mmoja kutoka Zagreb, Kroatia. Miaka mitano baadaye, mwaka wa 1980, painia mmoja wa pekee alikuja kutoka Serbia na akajifunza naye. Zoran anasema: “Ilikuwa vigumu kwangu kuachana na marafiki wangu wa disko, lakini nilipoachana nao, nilifanya maendeleo ya haraka na nikabatizwa miezi michache tu baadaye huko Belgrade, Serbia. Punde tu baadaye, kwa kuwa kulikuwa na ndugu wachache sana, nilipewa mgawo wa kutoa hotuba ya watu wote. Pia, tulianza kuongoza mikutano yote katika jiji la Podgorica.”

KUBATIZA WATU KWENYE MASHAMBA YA MPUNGA

Stojan Bogatinov kutoka Makedonia, alisema hivi: “Watu walipokuwa tayari kwa ajili ya ubatizo, niliwabatiza. Hatukuwa na kidimbwi cha kutumia, na mto wa eneo hilo ulikuwa mdogo sana. Hata hivyo, katika eneo letu kulikuwa na mashamba mengi ya mpunga yaliyokuwa na mifereji ya maji. Mifereji fulani ilikuwa yenye kina kirefu na safi vya kutosha ili kutumiwa kwa ajili ya ubatizo. Ninakumbuka ubatizo wa kwanza tuliofanya katika shamba moja la mpunga. Tulipokuwa tukipita katika shamba hilo kuelekea kwenye mfereji, mtu fulani aliniambia hivi kwa sauti, ‘Stojan, umepata wafanyakazi wapya!’

“‘Ndiyo, ndiyo,’ nilimjibu, ‘kuna kazi nyingi sana.’ Hawakujua kwamba tulikuwa wafanyakazi katika mavuno ya kiroho ambayo yalikuwa yanaendelea Makedonia.”

Akina ndugu huko Makedonia hawakuwa wakiwasiliana sana na ofisi ya tawi, hivyo bado walikuwa na mambo mengi ya kujifunza kuhusu utaratibu wa kitheokrasi. Stojan Stojmilov alianza kuhudhuria mikutano huko Ujerumani, na aliporudi Makedonia, alifurahi kuwapata Mashahidi huko Kočani. Anaeleza: “Nilipofika na kuwaambia akina ndugu jinsi mikutano inavyoongozwa huko Ujerumani, papo hapo waliniomba niongoze Funzo la Mnara wa Mlinzi na nitoe hotuba ya watu wote. Niliwaeleza kwamba sijabatizwa, lakini walisisitiza kwamba mimi ndiye ninayestahili zaidi. Hivyo basi, nikakubali kufanya yale waliyoomba. Mwishowe, mimi na mke wangu tulifanya maendeleo, nasi pia tukabatizwa katika mashamba ya mpunga.”

Veselin Iliev, ambaye kwa sasa anatumika akiwa mzee huko Kočani, anaeleza: “Tulikuwa na ujuzi mdogo kuhusu utaratibu wa kitheokrasi, lakini tulipenda sana kweli.” Baada ya muda, Yehova alihakikisha kwamba mambo yamerekebishwa. Kuchapishwa kwa vichapo zaidi vya Kimakedonia kulisaidia sana kuendeleza kweli ya Ufalme na kuimarisha makutaniko.

KUTUMIA KWA BUSARA UHURU ULIOONGEZEKA

Kwa kuwa Yugoslavia haikuwa chini ya mamlaka ya Urusi, watu walikuwa na uhuru mwingi ambao hawakuwa nao nyuma ya Pazia la Chuma. Mwishoni-mwishoni mwa miaka ya 1960, Yugoslavia ilikuwa nchi ya kwanza ya Kikomunisti kufuta viza na kulegeza masharti katika mipaka yake. Kwa sababu ya kuongezeka kwa uhuru wa kusafiri, ndugu zetu wa kaskazini mwa Yugoslavia walijitwika daraka la kupeleka vichapo vyetu katika nchi zilizozunguka Muungano wa Sovieti, ambako kazi ya kuhubiri ilikuwa bado imepigwa marufuku.

Kwanza, walileta vichapo Yugoslavia kutoka Ujerumani kwa magari-moshi ya mizigo. Ðuro Landić, anayetumika katika Halmashauri ya Tawi ya Kroatia, anakumbuka kwamba nyumba yao ilikuwa depo ya vichapo mpaka Muungano wa Sovieti ulipoporomoka. Ðuro anakumbuka: “Magari yetu ya familia yalikuwa na sehemu za kuficha vichapo upande wa chini na kwenye sehemu ya mbele. Tulijua kwamba tukinaswa, tutapoteza magari yetu na pia tutatupwa gerezani, lakini shangwe ambayo ndugu zetu walionyesha wakati walipopokea vichapo ilituchochea kufanya jitihada hizo.”

Dada Milosija Simić, ambaye alipeleka vichapo Bulgaria kutoka Serbia, anaeleza: “Sikujua ni nani ninayepelekea vichapo hivyo—nilipewa tu anwani. Pindi moja, nilitoka ndani ya basi na nikapata nyumba yenyewe, lakini hakuna mtu aliyekuwa nyumbani. Nilizunguka nyumba hiyo na kutokea upande mwingine na nikajaribu tena kufanya hivyo. Hata hivyo, sikuona mtu yeyote. Ili nisitokeze mashaka, nilizunguka nyumba hiyo kwa busara karibu mara kumi siku hiyo. Lakini sikupata mtu yeyote. Hiyo ilionekana kuwa baraka kwelikweli, kwa sababu baadaye nilipata habari kwamba haikuwa anwani sahihi.

“Kwa kuwa nilifanya kazi kwa bidii ili kunakili na kuandika upya vichapo, nilikabili tatizo. Singeweza kutupa tu vichapo hivyo. Hivyo, niliamua kuvirudisha Serbia ambako vingetumiwa vizuri. Hata hivyo, ingawa tikiti ambayo nilikata ilikuwa ya kwenda na kurudi, bado nilihitaji nauli ya kunipeleka kwenye kituo kingine. Kwa kawaida, nilipoacha vichapo, akina ndugu ambao walivipokea walinipa pesa za kukata tikiti ya kurudi. Tulifanya hivyo kwa sababu kulikuwa na sheria kuhusu kiasi cha pesa ambacho ningeweza kuingia nacho nchini. Nilipokaribia dirisha ili kukata tikiti nilisali kwamba niweze kumkuta mwanamke hapo. Nilipofika tu, mwanamume aliyekuwa hapo aliondoka na mwanamke akachukua mahali pake. Ili nipate tikiti, nilimwambia mwanamke huyo nitampa nguo tulizotumia kufunika vichapo. Alikubali, na nikapata tikiti yangu.”

Mwanzoni mwa miaka ya 1980, ndugu walitafsiri vichapo katika Kialbania na Kimakedonia kisha walituma nakala hizo zilizoandikwa kwa mkono kwenye ofisi ndogo huko Belgrade. Huko, Milosija alitumia taipureta na karatasi ya kaboni kutokeza nakala nane-nane. Ulikuwa mgawo mgumu kwa sababu habari ziliandikwa kwa mkono na hakujua lugha hiyo.

NDUGU VIJANA WANASIMAMA IMARA

Ingawa kirasmi tulikuwa na uhuru wa ibada, serikali iliona msimamo wetu wa kutokuwamo kuwa tishio kwa umoja wa Yugoslavia. Kwa sababu hiyo, akina ndugu walikabili upinzani. Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, wengi walibaki waaminifu mpaka kifo kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo. Lakini katika miaka 30 iliyofuata, si wote walioonyesha imani hiyohiyo yenye nguvu. Wengine walihudhuria mikutano ya Kikristo na kutegemeza kazi ya Ufalme; hata hivyo, walipoitwa kujiunga na jeshi, walipata visingizio vya kushiriki katika mazoezi ya kijeshi.

Ndugu vijana waliochukua msimamo wa kutojiunga na jeshi walihukumiwa kifungo cha mpaka miaka kumi. Kwa hiyo, walifungwa mara kadhaa kabla ya kufikia umri wa miaka 30. Baadhi ya wale waliokabili majaribu hayo ya utimilifu na kukataa kulegeza msimamo wao walikuwa wapya sana katika kweli. Kwa sasa wengi wao wana madaraka na ni waangalizi wa makutaniko.

KUSANYIKO LA KIMATAIFA LENYE KUSISIMUA

Mashahidi wa Yehova nchini Yugoslavia walikuwa hawajawahi kupata shangwe ya kupanga kusanyiko la kimataifa. Fikiria jinsi walivyosisimka mwaka wa 1991 Baraza Linaloongoza lilipotangaza kwamba moja ya makusanyiko ya kimataifa ya “Wapendao Uhuru” lingefanywa huko Zagreb, Kroatia!

Hata hivyo, kulikuwa na matatizo. Tangu Kroatia ilipotangaza uhuru wake kutoka kwa Yugoslavia, tishio la vita lilikuwa linakaribia zaidi na zaidi. Je, lingekuwa jambo la hekima kufanya kusanyiko? Usalama wa wajumbe kutoka nchi za kigeni na wenyeji ulikuwa ndilo jambo la maana zaidi. Baada ya kusali sana na kufikiria mambo yote, ndugu waliamua kuendelea na matayarisho ya kusanyiko hilo.

Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alienda Kroatia majuma machache kabla ya kusanyiko ili kusaidia katika matayarisho hayo. Kwa kuwa matukio mengine yote ya hadharani huko Zagreb yalikuwa yamefutwa, watu walitaka sana kujua kile ambacho kingetukia katika Uwanja wa Dinamo. Kadiri wakati wa kusanyiko ulivyokuwa ukikaribia, hali nchini iliendelea kuharibika. Kila siku ndugu walikadiria hatari, wakijiuliza swali lilelile tena na tena—Je, tunapaswa kuendelea na matayarisho, au kusanyiko linapaswa kufutwa? Ndugu waliendelea kusali kwa bidii kwa Yehova, wakiomba mwongozo wake. Jambo la kushangaza ni kwamba hali ya kisiasa ilitulia, na ndugu waliweza kufanya kusanyiko hilo toka Agosti (Mwezi wa 8) 16-18, 1991.

Kulikuwa na tofauti kubwa kama nini! Wakati nchi jirani zilipokuwa karibu kuanza vita vyenye jeuri, Mashahidi wa Yehova huko Kroatia walikuwa wakiwakaribisha maelfu ya wageni kwa ajili ya kusanyiko la kimataifa la “Wapendao Uhuru wa Kimungu.”b Wenyeji wengi walipokuwa wakikimbia kutoka nchini, ndugu na dada kutoka nchi 15 walikuwa wakikusanyika pamoja kwa upendo na uhuru. Wengi walikuja kwa ndege kutoka Marekani, Kanada, na nchi nyingine za Magharibi. Kwa sababu ya hali ya kijeshi, uwanja wa ndege wa Zagreb ulifungwa na ndege zilitua huko Ljubljana, Slovenia. Kutoka huko wajumbe walisafiri kwa basi mpaka Zagreb. Ujasiri wa ndugu wageni ulikuwa ushahidi mzuri kwa watu, na kuwapo kwao kuliwatia moyo sana ndugu wenyeji. Kundi lililokuwa kubwa zaidi lenye wajumbe 3,000 hivi lilitoka Italia. Ilionekana kwamba upendo na shauku yao ilifanya kusanyiko hilo liwe lenye kusisimua sana.—1 The. 5:19.

Lilikuwa jambo lenye kujenga imani hasa kutembelewa na washiriki watano wa Baraza Linaloongoza. Mpaka leo hii wengi wanakumbuka kwa shangwe hotuba zilizotolewa na Carey Barber, Lloyd Barry, Milton Henschel, Theodore Jaracz, na Lyman Swingle. Ndugu hao wenye uzoefu wa miaka mingi ambao hawatishwi na nyakati hizi zenye misukosuko, waliingia kwa ujasiri nchini ili kuwatia nguvu akina ndugu kupitia hotuba zao zenye kujenga.

Kwa sababu ya misukosuko ya kisiasa, wenye mamlaka waliogopa kwamba kungekuwa na vita vya kikabila kati ya wajumbe kutoka sehemu mbalimbali za Yugoslavia. Waliacha kuwa na wasiwasi walipoona wajumbe wakikusanyika pamoja kwa amani, na pia wakionyeshana shauku na upendo wa kindugu. Hesabu ya polisi waliokuja kusanyikoni ilipungua siku baada ya siku.

Kusanyiko hilo lisiloweza kusahauliwa lilionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wana undugu wa kweli wa ulimwenguni pote. Kutafakari juu ya kusanyiko hilo kungesaidia akina ndugu kudumisha umoja wakati wa majaribu yaliyokuwa mbele yao. Mabasi yaliyobeba wajumbe kutoka Serbia na Makedonia yalikuwa kati ya magari ya mwisho kuruhusiwa kurudi nyumbani kupitia kituo cha ukaguzi kati ya Kroatia na Serbia. Baada ya ndugu zetu kuvuka mpaka kwa usalama, mpaka ulifungwa. Watu wengi wanasema kuwa vita vilianza wakati huo.

Miezi na miaka iliyofuata, jamhuri ambazo zilikuwa hapo zamani sehemu ya Yugoslavia zilianza kujitenga na kuwa nchi huru zenye serikali. Katika vita hivyo, makumi ya maelfu ya watu walipoteza uhai wao na wengi waliteseka sana. Ni nini kingewapata ndugu zetu wakati huo wa msukosuko? Yehova amebariki jinsi gani kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ambayo imekuwa ikifanywa katika nchi hizo ambazo sasa ziko huru? Acheni tuone.

Historia ya Kisasa ya Bosnia na Herzegovina

“Mei 16, 1992 (16/5/1992), tukiwa watu 13, tulikusanyika pamoja katika nyumba fulani wakati makombora yaliporushwa huko Sarajevo. Makombora mawili yaligonga jengo ambamo tulikuwa tumekusanyikia. Ingawa wengine wetu walikuwa Wakroatia, Waserbia, na Wabosnia—makabila yaleyale matatu ambayo yalikuwa yakiuana kule nje—tuliunganishwa na ibada safi. Kufikia asubuhi, kulipokuwa na utulivu kidogo, tuliondoka kwenye nyumba hiyo na kutafuta mahali salama. Kama tulivyokuwa tumefanya usiku uliotangulia, tulimlilia Yehova kwa sauti katika sala, naye akatusikia.”—Halim Curi.

Sarajevo, ambalo lilikuwa na wakaaji zaidi ya 400,000, lilikabili mazingiwa ya muda mrefu zaidi na yenye kuogopesha zaidi katika historia ya leo. Ndugu na dada zetu wangeweza kukabiliana jinsi gani na mizozo yote ya kikabila na ya kidini iliyokuwa ikiigawanya nchi? Kabla hatujasimulia mambo yaliyowapata, acheni kwanza tupate habari zaidi kuhusu Bosnia na Herzegovina.

Nchi inayoitwa Bosnia na Herzegovina iko katikati ya nchi iliyoitwa Yugoslavia, nayo imezungukwa na Kroatia, Serbia, na Montenegro. Wakaaji wana uhusiano wa karibu wa kifamilia na wa kitamaduni, nao wanakazia sana ukarimu. Wanapenda kunywa kahawa fulani ya pekee na kwenda kwenye mikahawa inayoitwa kafići. Ingawa wakaaji wa Bosnia wanafanana sana, kuna Wabosnia, Waserbia, na Wakroatia. Wengi wao hawadai kuwa watu wanaofuata dini sana, hata hivyo, dini ndiyo imesababisha mgawanyiko. Wabosnia wengi ni Waislamu, Waserbia wengi ni wa Kanisa Othodoksi la Serbia, na Wakroatia wengi ni washiriki wa Kanisa Katoliki.

Chuki ya kidini na ya kikabila iliyoongezeka sana mapema katika miaka ya 1990 ilitokeza sera yenye kusikitisha ya kusafisha makabila. Majeshi yaliwafukuza raia—katika vijiji na majiji makubwa—ili kutenga maeneo yenye makabila fulani tu kwa ajili ya vikundi vyao vya kidini. Msimamo wa ndugu na dada zetu wa kutounga mkono upande wowote ulijaribiwa. Huko Bosnia, kama ilivyo katika nchi nyingine zilizokuwa sehemu ya Yugoslavia, watu wengi wanafuata dini ya wazazi wao, na kwa kawaida jina la familia linaonyesha dini inayofuatwa na familia. Watu wenye moyo mzuri wanapokuwa watumishi wa Yehova, huenda wakaonwa kuwa wameisaliti familia yao na utamaduni wao. Hata hivyo, ndugu zetu wamejifunza kwamba ushikamanifu kwa Yehova ni ulinzi.

JIJI LAZINGIRWA

Kama tulivyoona, ndugu wa Yugoslavia waliguswa moyo sana na upendo na umoja uliokuwepo katika kusanyiko la mwaka wa 1991 la “Wapendao Uhuru wa Kimungu” huko Zagreb, Kroatia. Kusanyiko hilo lisiloweza kusahaulika liliwatia nguvu kukabiliana na matatizo ambayo yangetokea baadaye. Wakati fulani, Wabosnia, Waserbia, na Wakroatia walikuwa wakiishi pamoja kwa amani huko Sarajevo. Kisha, jeshi likazingira jiji hilo na kila mtu akanaswa ndani—kutia ndani ndugu zetu. Ingawa kulikuwa na msukosuko wa kisiasa, hakuna aliyejua hali hiyo ingeendelea kwa muda gani.

Halim Curi, mzee wa kutaniko huko Sarajevo, alisema hivi: “Watu wanakufa njaa. Kila mwezi wanapewa kilo chache tu za unga, gramu 100 za sukari, na nusu lita ya mafuta. Wakipata kipande chochote kidogo cha ardhi jijini, wanakitumia kupandia mboga. Watu wanakata miti ya Sarajevo ili wapate kuni. Miti inapokwisha, wanabomoa sakafu za mbao za nyumba zao ili wazitumie kupikia na kupasha joto nyumba zao. Wanatumia chochote kinachoweza kuteketea, hata viatu vilivyochakaa.”

Jiji la Sarajevo lilipozingirwa, Ljiljana Ninković na mume wake Nenad walinaswa jijini na kutenganishwa na binti zao wawili. Ljiljana anasema: “Tulikuwa familia ya kawaida yenye watoto wawili, nasi tulikuwa na nyumba na gari. Halafu kwa ghafula, mambo yakabadilika kabisa.”

Lakini mara nyingi waliona mkono wa Yehova ukiwalinda. Ljiljana anaendelea kusimulia: “Nyumba yetu ililipuliwa kwa bomu mara mbili baada tu ya sisi kuondoka. Ingawa tulipata matatizo, tulifurahia mambo madogo-madogo. Kwa mfano, tulifurahia kwenda kwenye bustani kuchuna majani fulani (ya dandelion) ili kutengeneza saladi, hivyo hatukula wali mkavu. Tulijifunza kutosheka na vitu tulivyokuwa navyo na kutochezea kitu chochote.”

KUPATA MAANDALIZI YA KIMWILI NA YA KIROHO

Tatizo moja kubwa lilikuwa kupata maji. Nyumba hazikuwa na maji ya bomba. Iliwabidi watu watembee kilomita tano kupitia maeneo yenye wavamizi ili kupata maji. Na walipofika mahali pa kuteka maji, walipanga foleni kwa saa nyingi wakisubiri kujaza mitungi yao, halafu iliwabidi kuanza safari ndefu ya kurudi nyumbani wakiwa wamejitwika mitungi hiyo.

Halim anasema: “Imani yetu ilijaribiwa tuliposikia kwamba maji yangepatikana nyumbani kwa muda mfupi. Wakati huo kila mtu alioga, alifua nguo, na kuteka na kuhifadhi maji katika mitungi mingi iwezekanavyo. Lakini namna gani ikiwa maji yangepatikana wakati wa mkutano wa kutaniko? Ilitubidi tuamue—ama kwenda kwenye mkutano au kubaki nyumbani kuteka maji.”

Ingawa maandalizi ya kimwili yalihitajiwa sana, akina ndugu walithamini sana maandalizi ya kiroho. Kwenye mikutano, ndugu walipata chakula cha kiroho na pia habari kuhusu wale waliofungwa gerezani, wale walioumizwa, au hata wale waliouawa. Milutin Pajić, ambaye ni mzee wa kutaniko, anasema: “Tulikuwa kama familia. Tulipohudhuria mikutano, hatukutaka kuondoka. Baada ya mikutano mingi, tulibaki kwa saa nyingi tukizungumza kuhusu kweli.”

Maisha hayakuwa rahisi, na mara nyingi akina ndugu walihofia maisha yao. Lakini walitanguliza mambo ya kiroho. Ingawa vita vilizidi kuigawanya nchi, watu wa Yehova walifurahia uhusiano wa karibu hata zaidi kati yao na pamoja na Baba yao wa mbinguni. Watoto waliona ushikamanifu wa wazazi wao, na ukawachochea kuwa washikamanifu kabisa kwa Yehova.

Mji wa Bihać, ulio karibu na mpaka wa Kroatia, ulizingirwa kwa karibu miaka minne. Wakaaji hawangeweza kutoka nje, na misaada haingeweza kuingizwa ndani. Osman Šaćirbegović, ndugu pekee aliye katika mji huo, anasimulia: “Mwanzoni mwa vita, hali ilikuwa mbaya sana, si hasa kwa sababu ya hali ngumu lakini kwa sababu tulikuwa tukikabili jambo geni, jambo ambalo hatukuwa tumekabili awali. Inashangaza kwamba makombora yalipoanza kurushwa, wasiwasi ulipungua kwa sababu tulitambua kwamba si makombora yote yanayosababisha kifo. Makombora mengine hata hayalipuki.”

Kwa kuwa hakuna aliyejua mapigano hayo yangedumu kwa muda gani, Betheli za Zagreb, Kroatia, na Vienna, Austria zilishirikiana kuhifadhi misaada katika Majumba ya Ufalme na nyumba za Mashahidi huko Sarajevo, Zenica, Tuzla, Mostar, Travnik, na Bihać. Mapigano yalipoendelea, majiji yalizingirwa kwa ghafula na kutenganishwa. Kwa kuwa misaada haingeweza kusafirishwa, muda si muda maandalizi yalikwisha. Hata hivyo, ingawa miji mbalimbali ya Bosnia ilitenganishwa na maeneo mengine ya ulimwengu, umoja wa kindugu wa Mashahidi wa Yehova haukudhoofika kamwe. Hali hiyo ilikuwa tofauti kabisa na ile chuki ya kikabila na ya kidini iliyokuwa ikienea kama moto kotekote nchini.

WENYE BIDII LAKINI WAANGALIFU

Zaidi ya matatizo ya kupata vitu vya msingi vya kila siku, kulikuwa pia na hatari ya kushambuliwa na wavamizi waliokuwa kotekote Sarajevo, ambao walikuwa wakiwapiga risasi raia wowote wale. Pia, makombora yaliendelea kurushwa angani na kuwaua watu. Nyakati nyingine, ilikuwa hatari kutembea katika miji iliyozingirwa. Watu waliishi kwa woga. Lakini ndugu zetu walitumia hekima na ujasiri kwa usawaziko na kuendelea kuwahubiria habari njema ya Ufalme watu waliohitaji sana faraja.

Mzee mmoja anasema hivi: “Wakati wa mashambulizi makali zaidi huko Sarajevo, maelfu ya makombora yalilipuka kwa siku moja tu. Jumamosi hiyo asubuhi, akina ndugu waliwapigia simu wazee na kuwauliza, ‘Mkutano wa utumishi wa shambani utakuwa wapi?’”

Dada mmoja alisema hivi: “Niliona kwamba watu wanahitaji sana kweli. Hilo hasa ndilo jambo lililonisaidia kuvumilia na kupata shangwe wakati wa hali ngumu.”

Wakaaji wengi walitambua kwamba walihitaji tumaini la Biblia. Ndugu mmoja alisema hivi: “Watu wanatutafuta ili wapate msaada wa kiroho, badala ya sisi kuwatafuta. Wanakuja kwenye Jumba la Ufalme na kuomba funzo.”

Mafanikio mengi katika kazi ya kuhubiri wakati wa vita yalichangiwa na umoja ulio katika undugu wetu wa Kikristo, ambao watu waliuona waziwazi. Nada Bešker, dada ambaye amekuwa akitumika akiwa painia wa pekee kwa miaka mingi, anasimulia hivi: “Ulikuwa ushahidi mkubwa. Watu wengi waliona ndugu Wabosnia na Waserbia wakihubiri pamoja. Na walipomwona dada Mkroatia pamoja na dada ambaye zamani alikuwa Mwislamu wakijifunza pamoja na Mserbia, walitambua waziwazi kwamba sisi ni tofauti.”

Matokeo ya bidii ya akina ndugu yanaweza kuonekana mpaka leo hii kwa sababu wengi ambao wanamtumikia Yehova sasa walikubali kweli wakati wa vita. Kwa mfano, kutaniko la huko Banja Luka liliongezeka mara mbili, hata ingawa wahubiri 100 walihamia makutaniko mengine.

FAMILIA YENYE UAMINIFU

Ndugu zetu walikuwa waangalifu sana nyakati zote. Hata hivyo, wengine walipatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa” kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa. (Mhu. 9:11) Božo Ðorem, ambaye ni Mserbia, alibatizwa kwenye kusanyiko la kimataifa huko Zagreb mwaka wa 1991. Baada ya kurudi Sarajevo, alifungwa gerezani mara kadhaa, na akiwa huko alitendewa vibaya sana kwa sababu ya msimamo wake wa kutounga mkono upande wowote. Mwaka wa 1994, alifungwa gerezani kwa miezi 14. Tatizo kubwa ni kwamba hangeweza kuwa pamoja na mke wake, Hena, na binti yao mwenye umri wa miaka mitano, Magdalena.

Muda mfupi baada ya Božo kuwekwa huru kutoka gerezani, msiba ulitokea. Alasiri moja yenye utulivu, wote watatu walienda kuongoza funzo la Biblia karibu na nyumba yao. Walipokuwa njiani, utulivu ulivurugwa na mlipuko wa kombora. Hena na Magdalena walikufa papo hapo, na Božo alikufa baadaye hospitalini.

MSIMAMO WA KIKRISTO WA KUTOUNGA MKONO UPANDE WOWOTE

Kwa kuwa ubaguzi ulikuwa ukienea sana, watu walilazimishwa kuunga mkono upande fulani. Huko Banja Luka, kutaniko lilikuwa na ndugu wengi vijana ambao wanajeshi walitaka kuwatumia katika vita. Kwa sababu hawakuunga mkono upande wowote, walipigwa viboko.

Osman Šaćirbegović anakumbuka hili: “Polisi walituhoji mara nyingi na kutuita waoga kwa kuwa hatukupigana ili kulinda familia zetu.”

Osman alikuwa akiwaambia polisi hivi: “Bunduki zenu zinawalinda, sivyo?”

Kisha polisi wangejibu, “Bila shaka.”

“Je, mnaweza kukubali kubadilisha bunduki zenu kwa mizinga ili mwe salama zaidi?”

“Ndiyo.”

“Je, mnaweza kukubali kubadilisha mizinga kwa vifaru?”

“Bila shaka.”

Kisha Osman aliwaambia: “Mngefanya yote hayo ili mwe salama zaidi. Mimi ninalindwa na Yehova, Mungu mweza-yote, Muumba wa ulimwengu wote. Je, kuna ulinzi bora zaidi kuliko huo?” Jibu lilikuwa wazi, na baada ya hapo polisi wangemwacha.

MISAADA YAFIKA

Ingawa ndugu katika nchi za karibu walijua kwamba Mashahidi Wabosnia walikuwa wakiteseka, kwa muda fulani ilikuwa vigumu kuwapelekea misaada ndugu zetu wenye uhitaji. Kisha, mnamo Oktoba 1993, wenye mamlaka walisema kwamba misaada hiyo inaweza kusafirishwa. Ijapokuwa kulikuwa na hatari, ndugu zetu waliamua kutumia nafasi hiyo vizuri. Mnamo Oktoba 26, malori matano yalianza safari ya kwenda Bosnia kutoka Vienna, Austria, yakiwa na tani 16 za chakula na kuni. Msafara huo ungepita jinsi gani katika maeneo mengi yaliyokuwa bado na mapigano makali?c

Nyakati fulani katika safari hiyo akina ndugu walikabili hatari kubwa. Dereva mmoja anakumbuka hivi: “Nilianza safari nikiwa nimechelewa asubuhi hiyo, nami nikajipata nyuma ya malori mengine yaliyokuwa yakipeleka misaada. Nilipokaribia kituo kimoja cha ukaguzi, malori yote yalisimama ili maofisa wakague vibali. Kwa ghafula, nikasikia mlio wa risasi za mvamizi, kisha tukaona dereva ambaye si Shahidi akiwa amepigwa risasi.”

Ni madereva tu walioruhusiwa kuingia Sarajevo wakiwa na malori yao, hivyo iliwabidi ndugu wengine waliosafiri pamoja nao wasubiri nje ya jiji. Lakini kwa kuwa walitaka sana kuwatia moyo ndugu zao wenyeji, walitafuta simu, wakawapigia simu wahubiri huko Sarajevo, na kuwatolea hotuba ya watu wote yenye kutia moyo. Mara nyingi wakati wa vita, waangalizi wanaosafiri, Wanabetheli, na washiriki wa Halmashauri ya Nchi walihatarisha maisha yao ili kuwasaidia ndugu zao kupata vitu vya kimwili na kuendelea kuwa imara kiroho.

Kwa karibu miaka minne, bidhaa hazingeweza kuwafikia ndugu zetu huko Bihać. Ingawa chakula cha kimwili hakikuruhusiwa kuvuka vizuizi vilivyotenganisha mji, ndugu zetu waliweza kupata chakula cha kiroho. Jinsi gani? Walipata laini ya simu na mashini ya faksi, ambayo iliwawezesha kupata mara kwa mara Huduma Yetu ya Ufalme na nakala za Mnara wa Mlinzi. Walichapa tena vichapo hivyo na kugawia kila familia nakala moja. Vita vilipoanza, kulikuwa na kikundi kidogo tu cha wahubiri watatu waliobatizwa. Pia, kulikuwa na wahubiri wengine 12 ambao walisubiri kwa miaka miwili pindi inayofaa ili wabatizwe katika maji ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova.

Haikuwa rahisi kutenganishwa kwa miaka mingi hivyo. Osman anasema: “Wanafunzi wangu wa Biblia hawakuwa wamewahi kuhudhuria kusanyiko wala mikutano wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Tulizungumza mara nyingi kuhusu wakati ambapo tutaweza kufurahia undugu wetu.”

Hebu wazia jinsi akina ndugu walivyofurahi Agosti 11, 1995, wakati magari mawili yaliyoandikwa “Misaada ya Mashahidi wa Yehova” yalipoingia Bihać. Yalikuwa magari ya kwanza ya kibinafsi kufaulu kuleta misaada tangu jiji lilipozingirwa! Nayo yalifika wakati tu akina ndugu walipoanza kuhisi kwamba wamedhoofika sana, kimwili na kiakili.

Majirani huko Bihać waliona jinsi akina ndugu walivyotunzana, kama vile kwa kurekebisha madirisha yaliyovunjika. Osman anasema: “Jambo hilo liliwavutia majirani wangu, kwa kuwa walijua hatuna pesa. Ulikuwa ushahidi mkubwa sana, na bado wanauzungumzia.” Sasa kuna kutaniko lenye bidii lenye wahubiri 34 na mapainia 5 katika mji wa Bihać.

SAFARI ISIYOSAHAULIKA!

Akina ndugu zetu walihatarisha maisha yao mara nyingi ili kupeleka chakula na vitabu katika miji yenye vita huko Bosnia. Lakini safari ya Juni 7, 1994 ilikuwa tofauti. Msafara wa malori matatu yaliyobeba washiriki wa Halmashauri ya Nchi na wafanyakazi wengine yaliondoka Zagreb, Kroatia, mapema asubuhi hiyo. Walikusudia kufikisha misaada na kufanya kusanyiko la pekee lililofupishwa, la kwanza katika muda wa miaka mitatu!

Jiji la Tuzla ni moja ya maeneo yaliyokuwa yamechaguliwa kwa ajili ya programu hiyo ya pekee. Mwanzoni mwa vita, kulikuwa na wahubiri 20 hivi tu waliobatizwa katika kutaniko. Ilishangaza kama nini kuona watu zaidi ya 200 wakiwa wamekusanyika kusikiliza programu ya kusanyiko! Watu 30 walibatizwa. Leo, jiji la Tuzla lina makutaniko matatu na wahubiri zaidi ya 300.

Huko Zenica, akina ndugu walipata mahali pazuri pa kukutania, lakini walishindwa kupata kidimbwi cha ubatizo. Mwishowe, baada ya jitihada nyingi, walipata pipa ambalo lingeweza kutumiwa. Lakini tatizo ni kwamba pipa hilo lilikuwa linanuka, kwa kuwa zamani lilitumiwa kuwekea samaki! Hata hivyo, waliotaka kubatizwa ambao walikuwa wameukubali mwaliko wa Yesu wa kuwa “wavuvi wa watu,” hawakuogopa. (Mt. 4:19) Herbert Frenzel, ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Kroatia, alikuwepo ili kutoa hotuba ya ubatizo. Anaripoti hivi: “Wale waliotaka kubatizwa walikuwa wamesubiri kwa muda mrefu sana ili wabatizwe hivi kwamba hakuna jambo ambalo lingewazuia! Baada ya kubatizwa walihisi ni kana kwamba wamepata ushindi!” Leo, kuna kutaniko lenye bidii lenye wahubiri 68 huko Zenica.

Huko Sarajevo, programu ingeweza kufanyiwa tu kwenye makutano ya barabara ambapo wavamizi walikuwa wakiwashambulia watu kwa risasi. Akina ndugu walipofika salama kwenye kusanyiko, walikabili tatizo la kupata mahali pa ubatizo na njia ya kuhifadhi maji, ambayo yalipatikana kwa shida. Ili kuhakikisha kwamba kuna maji ya kutosha kwa ajili ya ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa waliambiwa wapange foleni kulingana na ukubwa wao, nao wakabatizwa kuanzia yule mdogo zaidi mpaka yule mkubwa zaidi!

Ilikuwa siku yenye furaha kama nini kwa ndugu na dada zetu! Hawakuruhusu matukio yoyote yenye kuogopesha yawanyang’anye shangwe yao kubwa ya kuabudu pamoja. Leo, kuna makutaniko matatu imara katika jiji la Sarajevo.

BAADA YA VITA

Njia za kuingiza bidhaa zilipofunguliwa, maisha yakawa rahisi zaidi kwa ndugu na dada zetu. Hata hivyo, sera ya kusafisha makabila iliendelea, na watu wakaendelea kufukuzwa makwao. Ivica Arabadžić, mzee anayetumika Kroatia, anakumbuka akitimuliwa kwenye nyumba ya familia yao huko Banja Luka. “Mtu mmoja alikuja na bunduki na kutuambia tuondoke, akisema kwamba sasa hiyo ni nyumba yake. Alikuwa amefukuzwa kwenye nyumba yake huko Šibenik, Kroatia, kwa sababu alikuwa Mserbia. Sasa alitaka tuondoke. Polisi mmoja wa jeshi niliyejifunza naye aliingilia kati kutusaidia. Ingawa hatungeweza kuendelea kumiliki nyumba yetu, tulikubaliana na Mserbia huyo tubadilishane nyumba—yeye akachukua yetu nasi tukachukua yake. Haikuwa rahisi kwetu kuhama nyumba yetu na kutaniko lililotusaidia kujifunza kweli, lakini hatukuwa na lingine la kufanya. Tulichukua vitu vichache na kuhamia nyumba yetu ‘mpya’ huko Kroatia. Lakini tulipofika Šibenik, mtu mwingine alikuwa tayari ameingia katika nyumba hiyo yetu. Sasa tungefanya nini? Ndugu zetu walitukaribisha mara moja, na mzee fulani akaturuhusu tuishi katika nyumba yake kwa mwaka mmoja mpaka tuliposuluhisha tatizo hilo la nyumba.”

Bado kuna msukosuko wa kisiasa hata leo, lakini kweli inaendelea kusitawi huko Bosnia na Herzegovina, ambako karibu asilimia 40 ya watu wanadai kuwa Waislamu. Tangu vita vilipokwisha, ndugu zetu wamejenga Majumba ya Ufalme mapya. Jumba moja hasa, huko Banja Luka, ni zaidi ya mahali pa kukutania. Jumba hilo linawakilisha ushindi wa kisheria. Kwa miaka mingi, ndugu zetu walijaribu kupata ruhusa ya kujenga Jumba la Ufalme katika eneo hilo ambako Kanisa la Othodoksi la Serbia lina uvutano mkubwa. Baada ya vita, ingawa ndugu zetu huko Bosnia walitambuliwa kisheria, walinyimwa ruhusa ya kujenga Jumba la Ufalme huko Banja Luka. Mwishowe, baada ya kusali sana na kujitahidi sana, akina ndugu walipewa ruhusa ya kujenga. Ushindi huo umeweka msingi wa kisheria unaoweza kutumiwa kupata ruhusa ya kujenga Majumba mengine ya Ufalme katika eneo hilo la Bosnia na Herzegovina.

Uhuru huo wa ibada umewawezesha mapainia wa pekee 32, wengi wao wakiwa wametoka nchi nyingine, wasaidie kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji mkubwa. Bidii yao katika huduma na ushikamanifu wao kwa miongozo ya kitheokrasi ni baraka kubwa.

Sasa makusanyiko yanafanywa kwa amani katika jiji la Sarajevo, ambako ndugu zetu walishambuliwa mara nyingi na wavamizi wenye kufyatua risasi miaka 10 tu iliyopita. Makusanyiko hayo yanahudhuriwa na wajumbe kutoka nchi zote zilizokuwa sehemu ya Yugoslavia. Ingawa vita vya karne iliyopita vimeharibu nchi hiyo maridadi yenye milima, watu wa Yehova wamezidi kuwa na uhusiano wa karibu wakiwa wameunganishwa na “upendo wa kindugu usio na unafiki.” (1 Pet. 1:22) Leo, makutaniko 16 yenye wahubiri 1,163 huko Bosnia na Herzegovina yanamsifu kwa umoja Mungu wa kweli, Yehova.

Historia ya Kisasa ya Kroatia

Baada ya kusanyiko la kimataifa huko Zagreb mwaka wa 1991, kwa ghafula mpaka wa Kroatia na Serbia ulifungwa. Wanajeshi waliharibu au kuweka vizuizi kwenye barabara kuu na madaraja, na watu wengi waliohudhuria kusanyiko kutoka sehemu ya mashariki ya Kroatia hawangeweza kurudi makwao. Wakichochewa na upendo mwingi wa kindugu, Mashahidi wengi kutoka sehemu nyingine za nchi walijitolea kuwapa makao ndugu hao, hata ingawa wao wenyewe hawakuwa na pesa nyingi.

Huko Zagreb, ving’ora vililia usiku na mchana vikionya kuhusu mashambulizi ya mabomu. Watu walikimbilia usalama, na wengine wao walibaki ndani ya nyumba kwa majuma au miezi mingi. Kwa sababu chumba cha chini cha Betheli kilikuwa mahali salama, wenye mamlaka wa jiji hilo walikiteua kuwa mahali pa kujificha kutoka kwa mabomu. Hali hiyo ilitokeza nafasi nzuri sana za kuhubiri, na watu walipata faida nyingine zaidi mbali na kujikinga. Kwa mfano, siku moja ving’ora vililia, na kama kawaida, watu wakashuka haraka kutoka kwenye gari-moshi na kukimbilia ndani ya kile chumba cha chini cha Betheli. Kila mtu alipokuwa akisubiri kwa wasiwasi, mzee anayetumika Betheli aliuliza ikiwa wangependa kutazama picha za slaidi za kusanyiko la kimataifa lililofanywa Zagreb miezi kadhaa mapema. Wote walikubali na baadaye wakashukuru kwa onyesho hilo.

Kwa sababu ya mapigano, haikuwa rahisi kufika kwenye mikutano, na inasikitisha kwamba Majumba ya Ufalme fulani yaliharibiwa kwa risasi au makombora. Hata hivyo, ndugu walithamini sana chakula cha kiroho, na ndugu hao wapendwa ‘hawakuacha kukusanyika pamoja.’ (Ebr. 10:25) Kwa mfano, makombora ya roketi yalirushwa kwenye eneo la Šibenik kwa miezi sita, hivyo akina ndugu hawangeweza kukutana kwenye Jumba la Ufalme. Mzee mmoja anaeleza hivi: “Tuliishi nje ya jiji, na tulikuwa tukikutana kwenye nyumba yangu kwa ajili ya funzo la kitabu na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Lakini tujapokabili hali hizo, hatukupunguza bidii ya kuhubiri. Tulihubiri katika ujirani wetu na katika vijiji vya karibu. Kila mtu alitambua kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova. Walijua sisi ni tofauti.”

UPENDO WA KINDUGU WAKATI WA VITA

Ndugu wengi waliopoteza makao yao walikaa pamoja na wengine, na makutaniko yalifanya jambo lolote lililohitajiwa ili kuwasaidia. Kwa mfano, kwenye Jumba la Ufalme huko Osijek, Kroatia, akina ndugu waliisalimia kwa uchangamfu familia mpya iliyokuwa imekimbia Tuzla, Bosnia, chini ya hali ngumu sana. Kutaniko hilo lilifurahi kujua kwamba mke ni dada yao wa kiroho.

Wenye mamlaka walikubali familia hiyo iishi katika nyumba fulani, lakini nyumba hiyo ilikuwa imezeeka na kuharibika sana. Akina ndugu walipoona kwamba nyumba hiyo imeharibika sana, walitoa msaada. Mmoja wao alileta stovu, mwingine akaleta dirisha, na wengine wakaleta mlango na kitanda. Wengine walileta vifaa vya ujenzi, na wengine chakula na kuni. Kufikia siku inayofuata, chumba kimoja kilikuwa tayari. Hata hivyo, nyumba hiyo haingeweza kuikinga vya kutosha familia hiyo wakati wa baridi kali. Kwa hiyo, kutaniko liliandika orodha ya vitu ambavyo bado vilihitajiwa, na wahubiri walileta chochote ambacho wangeweza kutoa. Ingawa wahubiri hao ni maskini, walileta kila kitu kilichohitajiwa, kuanzia vijiko mpaka vifaa vya kujengea paa.

Vita vilipoendelea, vyakula vilipungua haraka sana, na ofisi ya tawi ilijitahidi sana kushughulikia mahitaji ya kimwili na ya kiroho ya ndugu zetu. Ofisi ya tawi ilishirikiana na Baraza Linaloongoza kufanya mpango wa kukusanya chakula, mavazi, viatu, na dawa. Mwanzoni, msaada ulitoka hasa kwa ndugu wenyeji, lakini hawangeweza kutimiza mengi sana kwa sababu ya hali yao ngumu. Wakati huohuo, ndugu huko Austria, Italia, Ujerumani, na Uswisi walichanga kwa ukarimu mavazi na dawa na vitabu vinavyozungumzia Biblia. Malori yalifika usiku na mchana yakiendeshwa na wajitoleaji ambao walitanguliza mahitaji ya ndugu zao Wakroatia kuliko usalama wao. Vitu hivyo vilipelekwa kwenye makutaniko yenye uhitaji kutoka kwenye kituo cha kuhifadhia misaada huko Zagreb.

Ndugu wa Kroatia walikuwa wamepokea msaada, lakini sasa wangewasaidia jinsi gani ndugu zao huko Bosnia? Malori yaliyopakiwa tani 16 za chakula na kuni yalielekea kwenye mpaka wa Bosnia. Safari hiyo ilikuwa hatari kwa kuwa kulikuwa na ripoti nyingi kwamba vikundi fulani vya kijeshi vinawashambulia watu. Wale wanaosafirisha misaada wangeuawa au hata kunyang’anywa misaada hiyo ikiwa wangekutana na vikundi hivyo.

Ndugu mmoja anasimulia hivi: “Tuliendesha malori kupitia misitu na kupita kituo kimoja cha ukaguzi baada ya kingine, na nyakati nyingine tulipita kwenye maeneo ya mapigano. Ingawa tulikabili hatari hizo, tulifika salama huko Travnik, Bosnia. Mwanajeshi fulani aliyesikia kwamba tumefika alikimbia kwenye nyumba ambayo ndugu zetu walikuwa wamekusanyika. Kisha akasema kwa sauti: ‘Watu wenu wamekuja kwa malori yao.’ Wazia shangwe ambayo ndugu walikuwa nayo! Tulibeba vyakula na kuviingiza ndani ya nyumba, tukaongea kwa ufupi, na kuondoka haraka. Bado tulihitaji kupeleka misaada sehemu nyingine pia.”

Ndugu wengi waliiandikia Betheli ya Zagreb kushukuru kwa msaada waliopata. Kutaniko moja liliandika hivi: “Asanteni sana kwa jitihada nyingi mnazofanya ili tupate chakula chote cha kiroho kwa ukawaida. Asanteni pia kwa misaada tuliyopata; akina ndugu waliihitaji sana. Tunawashukuru kutoka moyoni kwa jitihada zenu zote na kwa kutuhangaikia kwa upendo.”

Barua nyingine ilisema: “Ndugu fulani ni wakimbizi, na wengine wao hawana kazi. Walipopokea misaada na kuona jinsi ilivyokuwa mingi sana, walitokwa na machozi. Walivutiwa na kutiwa moyo sana kwa maana ndugu zao waliwahangaikia kwa upendo na kuwaonyesha ukarimu bila ubinafsi.”

Katika nyakati hizo ngumu, jitihada za pekee zilifanywa ili kuwagawia akina ndugu chakula cha kiroho chenye kujenga imani. Pia, ilikuwa wazi kwamba roho ya Yehova iliwasaidia sana, si kuvumilia tu hali hizo ngumu bali pia kuendelea kuwa na nguvu zaidi za kiroho.—Yak. 1:2-4.

UJUMBE WA TUMAINI WENYE KUTIA NGUVU

Ingawa mashirika ya misaada yalitoa misaada, ni Mashahidi wa Yehova tu waliotoa msaada ulioleta kitulizo cha kudumu. Badala ya kuketi kitako wakisubiri vita vikwishe, ndugu zetu walifanya yote waliyoweza kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme.

Huko Vukovar, karibu na mpaka wa Serbia, ambako uharibifu mkubwa ulitukia, idadi kubwa ya watu, kutia ndani ndugu zetu, walilazimika kukimbia kutoka jijini. Hata hivyo, dada mmoja anayeitwa Marija hakukimbia. Kwa miaka minne, akina ndugu huko Kroatia hawakujua alipo, lakini aliendelea kuwahubiria kwa bidii watu wachache waliobaki ndani ya jiji. Na alipata baraka nyingi kwa sababu ya bidii yake! Hebu wazia jinsi akina ndugu Wakroatia walivyoshangaa kuona kikundi cha watu 20 kutoka Vukovar wakihudhuria kusanyiko la wilaya la 1996!

Pia, ujumbe wetu wa tumaini una nguvu za kubadili maisha ya watu. Mwanzoni mwa vita, mwanajeshi mmoja kijana alipandishwa cheo haraka katika kikosi fulani cha juu cha jeshi la Kroatia. Mwaka wa 1994, alipokuwa akisubiri gari-moshi, alipata trakti yenye kichwa Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu? Alipokuwa akisoma trakti hiyo kwa uangalifu, alijifunza kwamba Shetani ndiye anayesababisha wanadamu watendewe kwa jeuri bali si Yehova Mungu. Ukweli huo ulimvutia sana. Sababu moja iliyomchochea awe mwanajeshi ni kwamba alitaka kulipiza kisasi kuuawa kwa dada yake mwenye umri wa miaka 19 na watu wengine wawili wa familia waliouawa wakati wa vita. Ingawa alikuwa amefanya mipango ya kwenda kwenye kijiji cha wauaji hao, trakti hiyo ilimsaidia kufikiri. Alianza kujifunza Biblia, na baada ya kujitahidi kwa miaka kadhaa kuboresha utu wake, alibatizwa mwaka wa 1997. Mwishowe, alienda kwenye kijiji ambamo wauaji wa familia yake waliishi. Lakini badala ya kulipiza kisasi, alifurahia kuwahubiria habari njema ya Ufalme wa Mungu watu waliohitaji kujifunza kuhusu rehema ya Mungu.

Bidii ya wahubiri katika huduma, hata wakati wa mizozo mikali zaidi, ilichangia ongezeko lenye kusisimua nchini Kroatia. Kuanzia mwanzo wa vita mwaka wa 1991 mpaka mwisho wa vita mwaka wa 1995, idadi ya mapainia iliongezeka kwa asilimia 132. Mafunzo ya Biblia yaliongezeka kwa asilimia 63, na idadi ya wahubiri iliongezeka kwa asilimia 35. Ndiyo, akina ndugu wenyeji walihubiri Neno la Mungu kwa ujasiri, na Yehova alibariki sana jitihada zao.

WAFANYAKAZI WALIOJIDHABIHU

Muda mfupi kabla ya kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1991, wamishonari wa kwanza waliozoezwa Gileadi, Daniel na Helen Nizan, kutoka Kanada, walifika nchini. Zaidi ya hayo, wenzi wa ndoa kutoka nchi nyingine za Ulaya ambao walikuwa wamejifunza lugha ya eneo hilo walialikwa watumikie Kroatia.

Wenzi fulani wa ndoa, Heinz na Elke Polach, kutoka Austria, walikuwa mapainia wa pekee huko Denmark katika eneo lenye watu wa Yugoslavia, walipoalikwa kutumika Kroatia mwaka wa 1991. Vita vilianza walipokuwa tu wanaanza kazi ya kutembelea makutaniko. Mzunguko wao wa kwanza ulitia ndani maeneo ya pwani ya Dalmatia na sehemu fulani za Bosnia, na maeneo yote hayo yalikumbwa na vita. Heinz alisema hivi: “Ilikuwa vigumu kutembelea Bosnia wakati wa vita. Kwa sababu ya hatari, hatungeweza kutumia gari letu la kibinafsi, kwa hiyo ilitubidi tutumie mabasi ambayo hayakutegemeka. Hatungeweza kubeba vitu vingi, tulibeba mifuko michache na taipureta tu.

“Tulihitaji kutumia akili ili tufanikiwe. Wakati fulani, tulipokuwa tukisafiri kati ya Tuzla na Zenica, wanajeshi walisimamisha basi letu. Walituambia ni hatari sana kuendelea na safari. Ilimbidi kila mtu katika basi ashuke. Lakini tulijua kwamba ndugu zetu huko Zenica wanatusubiri, kwa hiyo tulianza kuwaomba watu wengine watupeleke huko. Mwishowe, msafara wa malori ya mafuta yaliyokuwa na kibali yalikubali kutubeba. Tulipokuwa njiani tulimhubiria dereva, akatusikiliza sana.

“Kwa mara nyingine, tulilazimika kusimama njiani kwa sababu ya vita, na ilitubidi tutumie barabara za kandokando. Barabara hizo zilikuwa mbovu, na theluji ilifanya safari iwe ngumu hata zaidi. Tulisimama mara nyingi ili kusukuma malori mengine yaliyokwama. Katika eneo fulani, tulishambuliwa na ilibidi tukimbie. Tulifika Vareš, kilomita 50 hivi kutoka mahali tulipokuwa tukienda, tukasimamisha safari yetu hapo usiku huo.

“Dereva alilala kwenye viti, nami na Elke tukalala tukiwa tumejikunja nyuma ya kiti cha dereva tukijaribu kupata joto. Ni kana kwamba muda ulijikokota sana usiku huo! Hata hivyo, siku iliyofuata, tulipofika mwishowe Zenica, ndugu walifurahi sana kutuona! Safari yetu haikuwa ya bure! Ingawa hawakuwa na maji ya bomba wala umeme, walijitahidi wawezavyo kututendea kwa ukarimu. Ingawa walikuwa maskini kimwili, walikuwa tajiri kiroho nao walionyesha kwamba wanaipenda sana kweli.”

Tangu wakati wa vita, mapainia wa pekee karibu 50 wametumwa Kroatia kutoka Austria, Italia, Ujerumani, na nchi nyingine. Baadaye, tengenezo la Yehova lilituma wamishonari zaidi ili kuwaimarisha na kuwatia moyo akina ndugu. Watumishi hao wa wakati wote wenye bidii wamesaidia sana shambani na katika makutaniko.

“SIAMINI KWAMBA NIMEIONA SIKU HII!”

Mpaka mwishoni mwa miaka ya 1980, akina ndugu wanaoishi nje ya Betheli walikuwa wakitafsiri toleo la kila mwezi la Mnara wa Mlinzi katika Kikroatia kutoka Kijerumani. Kisha, mwaka wa 1991, kazi ya kutafsiri ikaanza kufanywa na kikundi cha watafsiri katika Betheli. Baada ya muda, Baraza Linaloongoza lilitoa kibali cha kutafsiri Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kufikia wakati huo, akina ndugu walikuwa wakitumia Biblia iliyotafsiriwa miaka 150 kabla ya hapo, yenye lugha iliyopitwa na wakati na yenye maneno mengi magumu. Kikundi cha watafsiri wa lugha ya Kikroatia kiliongoza katika kazi hiyo, na kilishirikiana kwa ukaribu na vikundi vya watafsiri wa Kiserbia na Kimakedonia. Wote walifaidika kutokana na ushirikiano huo na kazi ya kila mmoja.

Ijumaa, Julai 23, 1999, ni siku itakayokumbukwa kwa muda mrefu na Mashahidi wa Yehova huko Kroatia, vilevile Bosnia na Herzegovina, Montenegro, Serbia, na Makedonia. Kwenye Makusanyiko yote manne ya Wilaya ya “Neno la Mungu la Kiunabii,” Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kikroatia na Kiserbia, na wahudhuriaji wakaambiwa kwamba kazi ya kutafsiri Biblia ya Kimakedonia inaendelea vizuri. Wahudhuriaji walipiga makofi kwa dakika kadhaa na ikawabidi wasemaji wanyamaze kimya. Wahudhuriaji walishangilia sana, na wengi wao hawangeweza kuzuia machozi yao ya furaha. Mzee mmoja wa kutaniko ambaye ametumika kwa muda mrefu alisema: “Siamini kwamba nimeiona siku hii!” Biblia yote nzima ilitolewa katika mwaka wa 2006 katika lugha hizo tatu.

Kufikia mwaka wa 1996, Halmashauri ya Nchi, chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Austria, ilisimamia shughuli za Mashahidi wa Yehova huko Kroatia na katika Bosnia na Herzegovina. Mwaka wa 1996, Halmashauri ya Tawi yenye washiriki wanne iliwekwa rasmi kusimamia kazi ya kuhubiri katika maeneo hayo, na imeonekana wazi kwamba Yehova amebariki mpango huo.

MAJENGO MAPYA YA OFISI YA TAWI NA MAJUMBA YA UFALME

Sawa na inavyokuwa katika sehemu nyingine, familia ya Betheli huko Zagreb, Kroatia, ilianza kujionea matokeo ya ukuzi wa kiroho. Idadi ya familia ya Betheli iliongezeka kutoka watu 10 mpaka karibu 50. Lakini kwa kuwa Makao ya Betheli yalikusudiwa wenzi wa ndoa wanne au watano tu, ilibidi nyumba nyingine zilizo karibu zikodiwe.

Muda mfupi baada ya Halmashauri ya Tawi kuundwa, Baraza Linaloongoza liliagiza halmashauri hiyo inunue uwanja huko Zagreb kwa ajili ya ujenzi wa Makao mapya ya Betheli. Baada ya muda mfupi, wajitoleaji wenyeji na watumishi wa kimataifa walijenga majengo maridadi ambayo yangesaidia kuendeleza mambo ya Ufalme kwa miaka mingi. Majengo hayo mapya ya ofisi ya tawi na Jumba la Ufalme yaliwekwa wakfu Jumamosi, Oktoba 23, 1999, kutia ndani jengo lenye Majumba mawili ya Ufalme ambalo liko katikati ya Zagreb. Wajumbe kutoka nchi 15 walihudhuria, kutia ndani Ndugu Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza, ambaye alitoa hotuba ya wakfu. Siku iliyofuata, watu 4,886 walikusanyika kwa ajili ya programu ya kiroho yenye kufurahisha katika ukumbi mkubwa wa michezo. Hiyo ilikuwa siku isiyoweza kusahaulika kwa watu wa Yehova nchini Kroatia—na wengi wao walikuwa wamemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka 50 au zaidi huku wakivumilia hali zenye kuogopesha sana katika historia ya kisasa!

Pia, programu ya kujenga Majumba mapya ya Ufalme imekuwa ikiendelea. Kufikia mwaka wa 1990, makutaniko mengi yalikutana ndani ya vyumba vya chini ya ardhi au nyumba za watu. Kwa mfano, kwa miaka 20, kutaniko fulani huko Split lilikutana ndani ya chumba kidogo katika nyumba ya mtu binafsi. Ingawa kulikuwa na viti 50 tu, nyakati nyingine wahudhuriaji walikuwa zaidi ya mara mbili ya idadi ya viti, na iliwabidi wengi wao wasimame nje. Makusanyiko yalifanyiwa hapohapo, na watu 150 au zaidi walihudhuria. Leo, kuna makutaniko manne huko Split ambayo yanatumia Majumba mawili maridadi ya Ufalme. Kwa sababu ya ongezeko la wahubiri, ukumbi wa mikutano wa hoteli fulani unatumiwa kwa ajili ya makusanyiko. Dawati la Ujenzi wa Majumba ya Ufalme, linalosimamiwa na Ofisi ya Uhandisi ya Kimkoa huko Selters, Ujerumani, linaendelea kupangia ujenzi wa Majumba ya Ufalme yanayofaa na yenye kuvutia.

Vijana na wazee ambao wamejitolea kwa ajili ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme wamefanya kazi nyingi sana. Kufikia sasa, Majumba ya Ufalme mapya 25 yamejengwa na mengine 7 yamefanyiwa ukarabati. Jambo hilo limechangia ukuzi wa kazi ya Ufalme, na hivyo kumletea Yehova sifa.

KAZI YA UFALME INASONGA MBELE

Mwaka wa 1991, Kroatia ilipopata uhuru, wenye mamlaka waliendelea kutekeleza sheria zilizokuwepo kuhusu dini mpaka sheria mpya zilipopitishwa. Nchi mpya ilipoanzishwa, asilimia 90 hivi ya raia walikuwa Wakatoliki. Hivyo, makasisi walikuwa na uvutano mkubwa katika serikali. Hata hivyo, kwa sababu Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria zamani na kwa sababu ndugu zetu walikuwa na sifa nzuri, mnamo Oktoba 13, 2003, Wizara ya Haki ilitangaza kwamba sasa Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa kuwa kikundi cha kidini huko Kroatia. Baada ya kupitia magumu kwa miaka mingi, watumishi wa Yehova walifurahi kama nini kutambuliwa kisheria nchini Kroatia!

Mapema katika miaka ya 1990, nchi zote ambazo hapo zamani zilikuwa sehemu ya Yugoslavia zilikuwa na Shule moja tu ya Mapainia; sasa katika nchi ya Kroatia pekee, shule nyingi zinafanywa kila mwaka. Mnamo Septemba 2008, Kroatia ilifurahia kuwa na wahubiri 5,451 wanaoshirikiana na makutaniko 69. Na ilisisimua sana kuwa na hudhurio la Ukumbusho la watu 9,728! Yote hayo yanaonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa ukuzi zaidi.

Hata ingawa chuki ya kidini imeenea na matatizo ya maisha yanaongezeka, watumishi wote wa Yehova katika eneo hili wameazimia kuliko wakati mwingine wowote kuendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu hata Shetani achochewe na hasira yake kufanya nini. (Ufu. 12:12) Watu wengi wanaona jitihada za kupata riziki kuwa jambo la maana zaidi maishani. Lakini, miongoni mwa watu hao, kuna wale wanaougua kwa sababu ya maadili mapotovu yaliyo ulimwenguni na wanaotambua kwamba wana njaa ya kiroho. (Eze. 9:3, 4; Mt. 5:6) Watu hao wanapatikana na wanasaidiwa kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli na kusema: “Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova, kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.”—Isa. 2:3.

Historia ya Kisasa ya Makedonia

“Vuka uingie Makedonia utusaidie,” hivyo ndivyo mwanamume fulani alivyomwambia mtume Paulo katika maono katika karne ya kwanza. (Mdo. 16:8-10) Paulo na wahubiri wenzake walikubali mwaliko huo kwa kuwa walikata kauli kwamba Mungu alikuwa akiwaongoza wahubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika eneo hilo lisilohubiriwa. Muda si muda, Ukristo ulianza kusitawi katika eneo hilo. Ibada ya kweli imesitawi jinsi gani katika Makedonia ya leo, ambayo iko katika eneo dogo upande wa kaskazini wa Makedonia ya zamani?

Baada ya vita vya pili vya ulimwengu, Makedonia ilikuwa jamhuri ya kusini kabisa ya nchi ya Yugoslavia. Ilipata uhuru mwaka wa 1991. Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1993, Mashahidi wa Yehova walishangilia sana walipoandikishwa rasmi katika nchi hiyo mpya. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ingeweza kuanzishwa huko Makedonia chini ya usimamizi wa Halmashauri ya Tawi ya Austria. Hivyo basi, katika mwaka wa 1993, nyumba ilinunuliwa kwenye Barabara ya Alžirska, huko Skopje, na kikundi cha kutafsiri vichapo vya Kimakedonia kikahamia kwenye Betheli hiyo mpya kutoka Zagreb, Kroatia.

Michael na Dina Schieben kutoka Ujerumani walikuja kufanya kazi ya mzunguko, na Daniel na Helen Nizan, kutoka Kanada, ambao walikuwa wakitumika huko Serbia, walitumwa Makedonia. Halmashauri ya Nchi ilianzishwa, na Betheli ikaanza kufanya kazi.

VICHAPO VINAZUIWA

Ingawa Mashahidi wa Yehova walikuwa wameandikishwa rasmi, ilikuwa vigumu kuingiza vichapo nchini humo. Kuanzia mwaka wa 1994 mpaka 1998, serikali iliweka sheria iliyomruhusu kila mhubiri kupata gazeti moja peke yake. Kwa hiyo, ndugu walilazimika kufanya nakala za makala za funzo za Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya wanafunzi wao wa Biblia. Akina ndugu walitumiwa pia magazeti kutoka katika nchi nyingine, na wageni waliokuja Makedonia waliruhusiwa kubeba kiasi fulani cha magazeti. Mwishowe, baada ya kesi kusikizwa kwa miaka mingi, mahakama kuu ilifanya uamuzi uliowatetea Mashahidi, hivyo wakaruhusiwa kuingiza nchini vichapo vingi kadiri walivyotaka.

Mnamo Agosti, mwaka wa 2000, hesabu ya wahubiri ilifikia 1,024. Ilikuwa mara ya kwanza kwa wahubiri zaidi ya 1,000 kushiriki katika utumishi wa shambani! Huku vichapo vingi zaidi vikichapishwa katika Kimakedonia na wahubiri wakiongezeka, jengo walilotumia kwenye Barabara ya Alžirska halikutosha tena familia ya Betheli iliyokuwa ikiongezeka. Mwaka uliofuata, nyumba nyingine tatu zilizo karibu zilinunuliwa na kubomolewa ili majengo mawili mapya yajengwe. Leo, washiriki 34 wa familia ya Betheli ya Makedonia wanafanya kazi na kuishi katika majengo matatu yenye vifaa vingi. Walifurahi wakati Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza alipowatembelea wakati wa programu ya kuweka wakfu majengo hayo mnamo Mei 17, 2003.

UJENZI WA MAJUMBA YA UFALME

Ndugu na dada katika nchi yote ya Makedonia wamethamini sana mpango wa kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi maskini. Kikundi cha ujenzi chenye ndugu watano kilipewa mgawo wa kusaidia makutaniko kujenga Majumba ya Ufalme nchini; na kati ya 2001 na 2007, Majumba tisa mapya ya Ufalme yalijengwa. Kikundi hicho cha ujenzi chenye wafanyakazi wanaotoka nchi mbalimbali kimetoa ushahidi mzuri kwa kufanya kazi kwa amani na umoja bila ubaguzi wa kikabila. Mfanyabiashara mmoja aliyefika kwenye Jumba la Ufalme lililokamilika aliona kwamba lilijengwa kwa ufundi wa hali ya juu sana, akasema, “Kwa kweli jengo hili lilijengwa kwa upendo.”

Kikundi cha ujenzi kilipokuwa kikijenga Jumba jipya la Ufalme katika mji wa Štip, jirani mmoja alifikiri kwamba mradi huo haungeweza kufanikiwa kwa sababu wajenzi walionekana vijana wasio na uzoefu. Hata hivyo, ujenzi ulipokamilika, alikuja kwenye jumba hilo akiwa amebeba ramani ya nyumba yake akawasihi ndugu hao vijana wamjengee nyumba hiyo. Alivutiwa sana na ubora wa kazi yao hivi kwamba alijitolea kuwalipa pesa nyingi. Alishangaa akina ndugu walipomwambia kwamba walikuwa wakijenga Jumba la Ufalme kwa sababu wanampenda Mungu na jirani, bali si kwa sababu ya kuchuma pesa.

TAFSIRI YA ULIMWENGU MPYA

Wakati huohuo, kikundi kingine cha wanaume na wanawake waliojitolea walikuwa wakifanya kazi tofauti, kazi ya kutafsiri Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kimakedonia. Yehova alibariki kazi yao ngumu; na katika muda wa miaka mitano tu, walitafsiri Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Wajumbe walifurahi kama nini katika Kusanyiko la Wilaya la 2006 la “Ukombozi Unakaribia!” huko Skopje wakati mshiriki wa Baraza Linaloongoza Gerrit Lösch alipotangaza kutolewa kwa tafsiri hiyo mpya ya Biblia iliyo bora. Walipiga makofi kwa msisimuko sana na kwa muda mrefu, na wengi wao walitiririkwa na machozi. Baadhi yao walipopokea Biblia hiyo wakati wa chakula cha mchana waliketi chini mara moja na kuanza kuisoma tafsiri hiyo ya pekee ya Neno la Mungu katika lugha yao.

Wamakedonia wengi wanaiheshimu sana Biblia. Kwa mfano, Orhan alianza kujifunza Biblia miaka sita iliyopita. Hakujua kusoma wala kuandika, hata hivyo, alifundishwa kusoma na kuandika na ndugu aliyekuwa akijifunza naye. Tangu alipobatizwa miaka mitatu iliyopita, ameisoma Biblia yote mara sita!

Kwa muda fulani, Orhan ndiye aliyekuwa Shahidi pekee katika mji wa Resen. Hata hivyo, wengi walimsifu mtu huyo ambaye mwanzoni hakujua kusoma wala kuandika, na wazazi fulani waliwaomba akina ndugu wajifunze na watoto wao ili wawe kama Orhan. Wengi walianza kupendezwa na kweli, na mwishowe Funzo la Kitabu la Kutaniko la kila juma likaanzishwa katika mji huo. Mtu mmoja aliyependezwa alifikia kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, na sasa Orhan ni painia wa kawaida na mtumishi wa huduma.

KUVUKA KUINGIA MAKEDONIA

Katika mwezi wa Julai mwaka wa 2004, mume mmoja na mke wake ambao ni mapainia wa pekee kutoka Albania walikuja Makedonia ili kuwahubiria watu wanaozungumza Kialbania, ambao ni asilimia 25 ya watu wote nchini. Muda si muda, ilikuwa wazi kwamba wenzi hao wa ndoa walihitaji msaada kwa sababu walikuwa peke yao na walihitaji kuwahubiria watu zaidi ya nusu milioni wanaozungumza Kialbania. Kwa hiyo, mwaka mmoja baadaye wenzi wengine wa ndoa walitumwa kutoka Albania ili wajiunge nao, na mapainia hao wanne wa pekee walianza kuwatia moyo watu saba wenye kupendezwa wa kikundi kidogo katika mji wa Kičevo, ulio katikati ya eneo lenye Waalbania wengi nchini Makedonia. Katika maadhimisho yaliyofuata ya Ukumbusho, kikundi hicho kidogo kilifurahi sana kuona watu 61 wakihudhuria hotuba ya Ukumbusho, ambayo ilitolewa katika Kialbania na Kimakedonia. Kuanzia wakati huo, kikundi hicho kimekuwa na wahubiri 17 wenye bidii, na kwa wastani watu 30 au zaidi wanahudhuria mikutano.

Ili eneo lote la Makedonia liweze kuhubiriwa, Baraza Linaloongoza lilikubali kampeni ya pekee ifanywe kuanzia Aprili mpaka Julai 2007. Kusudi lilikuwa kuhubiri eneo ambalo halikuwa limehubiriwa na kueneza habari njema kwa watu wanaozungumza Kialbania.

Ndugu na dada 337 kutoka katika nchi saba walifurahi sana kujitolea kusaidia. Walipata matokeo gani? Habari njema ilihubiriwa katika maeneo zaidi ya 200 kotekote Makedonia. Watu 400,000 hivi walihubiriwa, na ilikuwa mara ya kwanza kwa wengi wao kusikia ujumbe huo. Watu waliachiwa vitabu na broshua zaidi ya 25,000 na magazeti zaidi ya 40,000 wakati wa kampeni hiyo ya miezi minne. Wahubiri walitumia saa 25,000 katika huduma, wakaanzisha mafunzo ya Biblia zaidi ya 200.

“Watu fulani walitokwa na machozi tulipowaambia tulikotoka na sababu ya kuwatembelea,” akaripoti ndugu mmoja. “Wengine wao waliguswa moyo na mambo waliyosoma katika Neno la Mungu, wakatiririkwa na machozi.”

Wahubiri walioshiriki katika kampeni hiyo walieleza sana jinsi walivyothamini kutoka moyoni kampeni hiyo. Dada mmoja aliandika hivi: “Mwalimu mmoja alituambia hivi: ‘Mungu awabariki. Mnafanya kazi nzuri kabisa. Mambo mnayozungumzia yameniburudisha kwelikweli!’”

Mhubiri fulani alisema hivi: “Ni vigumu kuacha eneo hilo ambalo linafaa kabisa umishonari. Tuliona jinsi watu walivyohitaji sana kweli, na tulihuzunika kuwaaga wanafunzi wetu wa Biblia tulipokuwa tukiondoka.”

Wenzi fulani wa ndoa walisema: “Tunasikitika kwamba hatukuchukua siku zaidi za likizo, kwa sababu sasa tunaona jinsi uhitaji ulivyo mkubwa.”

Wengi walihisi kama mhubiri aliyesema hivi: “Sidhani kuna wakati wowote ambapo tulifurahi sana tukiwa familia kama wakati huo.”

Kwenye milima iliyo karibu na mji wa Tetovo, kikundi cha wahubiri kilikuwa kikihubiri katika kijiji kimoja ambacho hakikuwa kimewahi kuhubiriwa na yeyote. Wahubiri wawili walianza kuhubiri upande wa kushoto wa barabara, na wawili upande wa kulia. Kabla hawajamaliza kuhubiri nyumba tatu tu, habari zilienea katika mtaa wote kwamba Mashahidi wa Yehova wanahubiri. Punde si punde, habari hizo zilienea katika kijiji chote, na kundi kubwa la wanawake wenye kupendezwa liliwazunguka akina dada. Mbele kidogo barabarani, kikundi cha wanaume 16 kilikuwa kikiwangojea kwa hamu akina ndugu. Wenye nyumba walileta mara moja viti vinne ili wahubiri waketi, na mwanamume mmoja akawatayarishia kahawa. Wahubiri walimpa kila mtu kitabu, wakaitumia kabisa Biblia kuufundisha umati huo kweli.

Wengi waliuliza maswali, na wote walisikiliza kwa makini. Wahubiri walipomaliza mazungumzo yao, wanakijiji wengi waliwaaga kibinafsi. Hata hivyo, ndugu hao walishtuka wakati mama mmoja mzee alipowakaribia akiwa ameinua bakora yake juu. “Nitawatwanga kwa bakora hii!” akasema, huku akiwanyooshea bakora hiyo. Wahubiri hao walikuwa wamemtendea nini mama huyo? “Mlimpa kila mtu kitabu lakini mimi hamkunipa!” akasema mama huyo. “Ninataka kile kitabu kikubwa cha manjano,” akasema, huku akionyesha kitabu cha Hadithi za Biblia ambacho jirani yake alikuwa amepewa. Bila kukawia, ndugu hao walimpa kitabu cha mwisho walichokuwa nacho.

KUWAHUBIRIA WAROMANI

Huko Makedonia, kuna Waromani wengi wanaozungumza Kimakedonia lakini lugha yao ni lugha ya Kiromani iliyochanganywa na lugha nyingine kadhaa za Kiromani. Inasemekana kwamba mji mkuu, Skopje, ambao una eneo kubwa zaidi la Waromani huko Ulaya, una wakaaji 30,000 hivi. Jengo lenye Majumba mawili ya Ufalme katika eneo linaloitwa Šuto Orizari linatumiwa na makutaniko matatu ya Kiromani yaliyo huko. Wahubiri 200 walio huko wanafurahia eneo lao lenye matokeo mazuri, kila mhubiri anahitaji kuwahubiria watu 150, mojawapo ya idadi ndogo zaidi ya watu katika nchi hiyo. Watu 708 waliohudhuria Ukumbusho mwaka wa 2008 wanathibitisha kwamba wengi wanaitikia huko Romani!

Ni jitihada gani zinazofanywa ili kuwasaidia Waromani ambao ni wanyenyekevu na wenye njaa ya kweli ili wajifunze kuhusu kusudi la Mungu katika lugha yao? Muhtasari wa hotuba ya pekee ya mwaka wa 2007 ulitafsiriwa katika Kiromani, na watu 506 walisikiliza kwa makini sana mzee Mromani alipokuwa akitoa hotuba hiyo. Wahubiri wa makabila mbalimbali, kama vile, Waromani, Wamakedonia, na Waalbania, walifurahi sana wakati broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? ilipotolewa katika Kiromani katika kusanyiko la wilaya la 2007. Kabla ya wakati huo, mara nyingi wahubiri waliongoza mafunzo ya Biblia katika lugha yao wenyewe wakitumia vichapo vya Kimakedonia. Sasa wanafanikiwa kabisa kugusa mioyo ya Waromani wanyoofu kwa kutumia broshua Anataka ya Kiromani.

Leo wahubiri 1,277 walio katika makutaniko 21 huko Makedonia wanahubiri kwa bidii sana wakifuata mfano ambao mtume Paulo aliweka katika karne ya kwanza. Itikio zuri la Wamakedonia wengi wanaotafuta kweli linaonyesha umuhimu wa kampeni ya kisasa ya ‘kuvuka kuingia Makedonia.’

Historia ya Kisasa ya Serbia

Nchi ya Serbia ambayo iko katikati ya eneo la Balkani, ina watu wa mataifa na tamaduni mbalimbali. Ofisi ya tawi ilianzishwa katika mji wa Belgrade, nchini Serbia, mwaka wa 1935 ili kushughulikia maeneo ya nchi iliyokuwa ikiitwa Yugoslavia, kukawa na ongezeko kubwa la kitheokrasi. Katika nyakati za karibuni, ndugu katika nchi ya Serbia wamesaidia jinsi gani nchi mpya zilizoundwa katika eneo hilo?

Mipaka ya nchi hizo ilipokuwa ikifungwa na chuki ya kidini na ya kijamii kuenea, ndugu wa mataifa mbalimbali walikuwa wakifanya kazi pamoja kwa amani katika ofisi ya tawi huko Zagreb, Kroatia. Mwishowe, ndugu zetu Waserbia walilazimika kuondoka kwa sababu chuki ya kijamii na ya kitaifa ilikuwa imepamba moto katika maeneo yaliyozunguka Betheli. Mwaka wa 1992, vichapo vya Kiserbia vilianza tena kutafsiriwa huko Belgrade, Serbia, kama ilivyokuwa miaka 50 hivi iliyopita. Hatua hiyo ilithibitika kuwa ya hekima na ya wakati unaofaa.

Watu wengi sana walihitaji misaada huko Bosnia, ambako vita vikali vilikuwa vikiendelea. Kwa upendo, ofisi ya tawi ya Austria ilikuwa imepanga kupeleka misaada, na ndugu wa Serbia wangeweza kupeleka kwa urahisi misaada hiyo katika maeneo ya Bosnia yaliyotawaliwa na Waserbia.

Ingawa vita havikufika Serbia, nchi hiyo ilipatwa na matokeo ya vita hivyo. Vikwazo vya kiuchumi vilifanya iwe vigumu kupata vichapo kutoka Ujerumani ambako vilichapishiwa. Makutaniko yalipokosa magazeti mapya, ndugu zetu walijifunza magazeti ya zamani mpaka magazeti mapya yalipofika. Hata hivyo, mwishowe ndugu zetu hawakukosa kamwe gazeti lolote.

‘MSAADA WENYE KUTIA NGUVU’

Daniel Nizan, aliyehitimu Shule ya Gileadi alisema hivi: “Tulipofika Serbia mwaka wa 1991, nchi hiyo ilikuwa na msukosuko mkubwa wa kisiasa. Tulivutiwa na bidii ambayo ndugu walionyesha hata ingawa waliishi katika hali ngumu sana. Ninakumbuka jinsi tulivyoshangaa kuona watu wapya 50 wakisimama ili wabatizwe katika kusanyiko la kwanza la pekee ambalo mimi na mke wangu tulihudhuria. Hilo lilitutia moyo sana.”

Ndugu na Dada Nizan walisaidia sana kupanga kazi katika ofisi mpya huko Belgrade. Ofisi ya kwanza, ambayo ilitoshea watu kumi, ilikuwa kwenye Barabara ya Milorada Mitrovića. Pia, Jumba la Ufalme lilikuwa sehemu ya chini ya jengo hilo. Nafasi zaidi zilihitajiwa kwa ajili ya watafsiri waliokuwa wakiongezeka. Mwishowe, uwanja ulipatikana na ujenzi ukaanza. Mwishoni mwa mwaka wa 1995, familia ya Betheli ilihamia makao mapya.

Matatizo yaliyokuwa yakiongezeka yaliwachochea watu zaidi wakubali kweli, na kadiri hesabu ya wahubiri ilivyoongezeka ndivyo kulivyokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa waangalizi wenye upendo. Mapainia wa pekee kutoka Italia walikuja kusaidia—watumishi wa wakati wote wenye bidii na wenye kujidhabihu ambao walijitolea kwa kupenda. Ingawa haikuwa rahisi kujifunza lugha mpya na kuzoea utamaduni mpya wakati wa vita, mapainia hao walikuwa ‘msaada wenye kuwatia nguvu’ ndugu zetu huko Serbia.—Kol. 4:11.

Mapainia kutoka nchi nyingine walisaidia katika njia nyingi, lakini njia ya maana zaidi ni kwamba “walikuwa na uzoefu wa mambo ya kitengenezo,” akasema Rainer Scholz, mratibu wa Halmashauri ya Nchi huko Serbia. Leo, kuna makutaniko 55 nchini Serbia ambayo yanasaidiwa na mapainia wa pekee 70.

HALI MBAYA SANA YA KUONGEZEKA KWA BEI KUPITA KIASI

Serbia ilikumbwa na hali mbaya sana ya kiuchumi iliyosababishwa na vita, hasa kuongezeka kwa bei kupita kiasi. Gazeti moja linaripoti hivi: “Katika muda wa siku 116 kati ya Oktoba 1993 na Januari 24, 1994, bei za vitu ziliongezeka kwa asilimia trilioni 500.” Mira Blagojević, ambaye amefanya kazi Betheli tangu 1982, anakumbuka kwamba alihitaji kubeba gunia lililojaa pesa ili kwenda kununua mboga chache sokoni.

Dada mwingine, Gordana Siriški, anasema kwamba mama yake alipoenda kuchukua malipo yake ya uzeeni ya mwezi mmoja, angeweza kununua karatasi moja tu ya chooni. Gordana alisema: “Ni vigumu sana kuelewa jinsi watu walivyoishi kwa kuwa kila kitu walichokuwa nacho kilipoteza thamani kwa ghafula. Ndugu zetu wa ulimwenguni pote walituletea misaada. Kadiri watu walivyokatishwa tamaa na benki na serikali, ndivyo wengi walivyoanza kumwamini Mungu, na akina ndugu walisitawisha uhusiano wa karibu zaidi.”

KUTAFSIRI BIBLIA

Kwa miaka mingi vikundi vya kutafsiri nchini Yugoslavia vilifanya kazi mahali pamoja huko Zagreb, Kroatia. Baada ya vita, kila kikundi cha kutafsiri kilihamia nchi yao lakini, bado waliendelea kuwasiliana na kikundi cha kutafsiri kilichokuwa Zagreb. Hatua hiyo ilisaidia sana hasa wakati kikundi cha Kiserbia kilipoanza kutafsiri Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Walikusudia itolewe kwenye kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova la 1999.

Hata hivyo, watafsiri walipokuwa wakimalizia kazi ya kutafsiri Biblia, nchi ilikuwa ikijitayarisha kwa ajili ya vita. Kwa kuwa mabomu yangeangushwa, na mawasiliano ya simu kukatizwa, ingekuwa vigumu kwa watafsiri kutuma habari kutoka Belgrade mpaka kwenye kiwanda cha uchapishaji nchini Ujerumani. Mnamo Jumanne, Machi 23, huku mashambulizi ya hewani yakitarajiwa, akina ndugu walifanya kazi usiku wote na wakafaulu kutuma faili za elektroniki mpaka Ujerumani mapema asubuhi. Saa chache baadaye, mabomu yalianza kuangushwa na watafsiri wakakimbilia mahali salama, huku wakishangilia! Walishangilia hata zaidi wakati Biblia iliyochapishwa ilipotolewa miezi minne baadaye kwenye kusanyiko lililofanyiwa Belgrade. Akina ndugu waliendelea kutafsiri vichapo vingine ijapokuwa walikabili mashambulizi hayo na ukosefu wa umeme. Lakini mara nyingi iliwabidi waache kazi na kukimbilia mahali salama. Kwa kweli, ulikuwa wakati mgumu, lakini wote walifurahia kushiriki kutayarisha chakula cha kiroho kilichohitajiwa sana.

Kupitia kazi nyingi ngumu na baraka za Yehova, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kiserbia mnamo Julai 1999. Wajumbe walithamini na kushangilia sana kwa sababu ya kupata tafsiri hiyo katika lugha yao wenyewe. Mwishowe, kwenye makusanyiko ya 2006, Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika maandishi ya Kisiriliki na Kilatini.

UPINZANI WA KIDINI UNAONGEZEKA

Kwa kuwa Kanisa Othodoksi la Kiserbia ndiyo dini kuu nchini, watu wengi wanafikiri Waserbia wote ni Waothodoksi. Wanahisi kwamba mtu ambaye si mfuasi wa Kanisa Othodoksi si Mserbia. Hata hivyo, ujumbe wetu wa tumaini kutoka katika Biblia ulikubaliwa na watu wengi katika miaka ya 1990. Vita vilipokuwa vikikaribia kwisha mwaka wa 1999, hesabu ya wahubiri ilikuwa imeongezeka karibu mara mbili, na kufikia kilele cha wahubiri 4,026.

Kanisa Othodoksi liliwakasirikia watu wa Yehova kwa sababu ya ufanisi wao wa kiroho. Kwa kuwachochea watu wawe wazalendo, kanisa hilo lilijaribu kukomesha kazi yetu ya Kikristo ya kuhubiri. Wapinzani walijaribu kuwavunja moyo ndugu zetu kwa kuwatesa na kwa kutumia sheria vibaya. Kwa mfano, ndugu zetu 21 walifungwa gerezani kwa sababu ya kutounga mkono vita. Wengi wao waliachiliwa huru muda mfupi baada ya vita, na walifurahi kwamba Yehova alitia nguvu imani yao wakati huo mgumu.

Kwa ghafula, mnamo Aprili 9, 2001, Wizara ya Mambo ya Ndani ilipiga marufuku kuleta vichapo vyetu nchini. Kwa nini? Walidai kwamba vichapo vyetu vingewapotosha vijana wa nchi hiyo. Orodha ya vichapo vilivyopigwa marufuku ilitia ndani Biblia!

Televisheni na magazeti yalieneza ripoti za uwongo kuhusu kazi yetu, na nyakati nyingine ripoti hizo ziliwafanya wenye nyumba fulani watutendee kwa jeuri. Painia mmoja wa pekee alisema hivi: “Walitupiga ngumi au makofi tulipohubiri nyumba kwa nyumba, na nyakati nyingine waliturushia mawe.” Kwa kuongezea, Majumba fulani ya Ufalme yaliporwa na kuharibiwa. Leo, ndugu zetu nchini Serbia wanaruhusiwa kisheria kukutana pamoja ingawa wanahitaji kufanya hivyo kwa busara.

Ndugu wanaendelea kuhubiri kwa bidii. Wanaonyesha kwamba watu wa Yehova hawana maoni yasiyofaa kuelekea watu na kwamba wana upendo wa kweli kama wa Kristo. Kampeni zenye mafanikio za kuhubiri zimepangwa katika miaka ya karibuni, na akina ndugu kutoka katika nchi nyingine za Ulaya wametumia likizo yao kusaidia kuhubiri maeneo ambayo hayajahubiriwa nchini Serbia na Montenegro. Hata hivyo, bado wana kazi nyingi ya kuwahubiria watu karibu milioni tatu wanaoishi katika maeneo hayo.

Leo Betheli ya Belgrade ina majengo matatu yaliyo katika bustani yenye kuvutia. Washiriki watatu wa Halmashauri ya Nchi wanasimamia kazi nchini Serbia na pia Montenegro. Yehova amewabariki watu wake katika eneo hilo lililokuwa na vita hivi kwamba jina Serbia sasa linatukumbusha bidii na azimio la Mashahidi wa Yehova.

Historia ya Kisasa ya Kosovo

Chuki kati ya Waserbia na Waalbania huko Kosovo miaka ya 1980 ilisababisha vita vikali katika miaka ya 1990, na watu waliteseka sana na kuumia. Chini ya hali hiyo, ndugu na dada zetu waliwaonyesha waamini wenzao wa makabila yote “upendo wa kindugu usio na unafiki.” (1 Pet. 1:22) Kwa kuongezea, wametii amri ya Kristo ya ‘kuwapenda adui zao na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa.’ (Mt. 5:43-48) Hata hivyo, nyakati nyingine imekuwa vigumu kufanya hivyo.

Saliu Abazi, anayezungumza Kialbania, na ambaye alikuwa Mwislamu zamani anasema: “Ndugu waliokuwa Waislamu zamani hawatendewi sikuzote kwa fadhili na Waislamu, na watu wa familia zetu wanafikiri kimakosa kwamba tumewaacha kwa sababu tumechagua dini nyingine. Pia, kwa sababu ya chuki ya kikabila kati ya Waalbania na Waserbia, mara nyingi inakuwa vigumu kwa wale waliokuwa Waislamu kuwahubiria Waserbia.”

Hata hivyo, kikundi cha watu 30 wa makabila mbalimbali kilikuwa kikikutana katika nyumba ya Saliu. “Katika miaka hiyo,” anakumbuka Saliu, “mikutano ilifanywa katika Kiserbia, na tulipata vitabu kutoka Belgrade. Siku moja polisi walikuja kwa ghafula katika nyumba yangu. Wakati huo akina ndugu kutoka Belgrade walikuwa tu wameleta vitabu, na sote tulikuwa tukifurahia ushirika. Nilipowaambia polisi kwamba hao walikuwa ndugu zangu, hawangeweza kuelewa jinsi Waserbia na Waalbania wanavyoweza kuwa ndugu.” Mwaka wa 1998, kikundi hicho cha wahubiri kilikodi mahali pa kutumia kama Jumba la Ufalme, katika mji mkubwa zaidi wa Kosovo, Priština.

Katika majira ya masika ya 1999, chuki ya kikabila na roho ya utaifa ilipamba moto sana. Saliu anasema: “Jirani yangu alitisha kwamba ikiwa mimi na mwanangu hatungeshiriki katika vita, nyumba yetu ingeteketezwa kabisa. Hali ya kisiasa iliwachochea vibaya watu. Kwa sababu watu walipinga serikali iliyokuwa ikitawala Serbia, sheria hazingeweza kutekelezwa, watu walikuwa wajeuri, nao walifanya walichotaka.”

Waserbia walioishi Kosovo walikabili hali ngumu zaidi kadiri hali ya kisiasa ilivyozidi kuzorota. Katika vita vya mwaka wa 1999, maelfu ya Waserbia na Waalbania walilazimika kukimbilia nchi nyingine jirani. Hata hivyo, ingawa kulikuwa na chuki kali sana ya kikabila, Saliu alihatarisha uhai wake kwa kuwaruhusu ndugu zake Waserbia wakimbilie katika nyumba yake.

KUFINYANGWA NA MAONI YA YEHOVA

Dada mmoja alisema hivi: “Chuki kati ya Waserbia na Waalbania ilikuwa kali sana. Tulijifunza kuwachukia tangu utotoni. Si rahisi kuacha chuki hiyo hata baada ya kujifunza kweli. Wengi wetu tulilazimika kufanya mabadiliko makubwa ili tufuate maoni ya Yehova. Kwa sababu ya chuki hiyo, hata nilipokuwa nikijifunza kwamba Yehova ni upendo, nilikuwa nikimwepuka dada fulani katika kutaniko kwa sababu tu ni Mserbia. Hata hivyo, nilipoendelea kujifunza nilianza kutambua kwamba kweli ya Neno la Yehova inawaunganisha watu, lakini mafundisho ya dini nyingine yanawagawanya watu.” Je, nguvu za Neno la Mungu za kuwabadili watu zimemsaidia dada huyo kuvaa utu mpya wa Kikristo? Anasema hivi: “Sasa, ninafurahi kutumikia katika kutaniko moja na ndugu na dada zangu Waserbia.”—Kol. 3:7-11; Ebr. 4:12.

Umoja wa kweli wa Kikristo unaonekana wazi katika ulimwengu huu uliogawanyika kidini. Wakati watu walipokuwa wakiteketeza nyumba na kurusha guruneti kwa sababu ya roho ya utaifa, ndugu zetu walikuwa wakisafiri kwenda Belgrade, Serbia, kwa ajili ya kusanyiko mwezi wa Julai 1998. Waalbania, Wakroatia, Wamakedonia, na Waromani walisafiri pamoja katika mabasi kwa amani. Dashurie Gashi, ambaye alikuwa akienda kubatizwa kwenye kusanyiko hilo, anasema hivi: “Askari-jeshi walipolisimamisha basi, nyuso zao zilionyesha kwamba walikuwa wameshtuka. Hata ingawa kulikuwa na chuki kali ya kikabila katika nchi hizo, tulikuwa kikundi kimoja chenye umoja—watu wa Yehova.”

Mwanamke mmoja kijana Mromani alijifunza kweli akiwa mtoto kutoka kwa mashangazi wake walioishi katika nchi nyingine. Kizuizi kimoja alichohitaji kushinda ni kujua kusoma na kuandika. Akichochewa na upendo kwa Yehova, alijifunza kusoma na kuandika katika muda wa miaka mitatu aliyokuwa akijifunza Biblia. Kizuizi cha pili kilikuwa babu yake, ambaye aliishi naye. Mwanamke huyo anasema hivi: “Nilijificha nilipokuwa nikienda kwenye mikutano.” Lakini babu yake aliporudi, alimpiga. Anasema hivi: “Niliteseka sana kimwili kwa sababu ya kweli, lakini sikukata tamaa. Nilitafakari kuhusu mateso yote ya mwanamume mwaminifu Ayubu. Nilimpenda sana Yehova, na niliazimia kutoacha kujifunza.” Hivi sasa anatumikia akiwa painia, naye anajifunza Biblia pamoja na wasichana wawili wasiojua kusoma na kuandika. Ingawa hakuenda katika shule ya kilimwengu, anathamini jinsi ambavyo Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imemzoeza kuwafundisha wengine.

Adem Grajçevci alikuwa Mwislamu kabla ya kujifunza kweli mwaka wa 1993 huko Ujerumani. Kisha mwaka wa 1999, alirudi katika nchi yao ya Kosovo na kama Mashahidi wengine wapya, alikabiliana na chuki na upinzani kutoka kwa watu wa jamaa yake. Adem anakumbuka hivi: “Nilipokuwa nikijifunza kweli, nilifurahi sana kujua kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu na kwamba ndiye anayesababisha jeuri yote iliyopo.” Baba ya Adem hakupendezwa na imani mpya ya Kikristo ya mwana wake, hivyo akamwambia achague kati ya Yehova na familia yao. Adem alimchagua Yehova, akaendelea kufanya maendeleo ya kiroho, na sasa anatumikia akiwa mzee Mkristo. Inafurahisha kwamba baada ya miaka mingi kupita, baba ya Adem hana chuki tena, naye sasa anaheshimu zaidi uamuzi ambao Adem alifanya.

Adnan, mwana wa Adem, hakupendezwa hata kidogo na dini alipokuwa mtoto. Alijihusisha sana na mchezo fulani kama wa karate na wenzake walimbandika jina, Muuaji. Hata hivyo, mwishowe kweli ilipogusa moyo wake aliacha kabisa mchezo huo. Alifanya maendeleo makubwa naye akabatizwa. Alisema hivi: “Muda mfupi baada ya kubatizwa nililazimika kufanya uamuzi. Nilikuwa na kazi nzuri, na vilevile pesa nyingi. Lakini nilikuwa mgonjwa kiroho na sikuwa na wakati wa kuhubiri. Niliamua kufanya mabadiliko, hivyo niliacha kazi yangu.” Alianza kufanya upainia, akawekwa kuwa mtumishi wa huduma, na baadaye akaalikwa kuhudhuria darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma huko Albania. Sasa, Adnan ni mzee wa kutaniko, naye ni painia wa pekee pamoja na mke wake, Hedije. Anahisi namna gani kuhusu uamuzi aliofanya? Anasema: “Nimepata furaha isiyo na kifani. Sijuti kamwe kwamba nilichagua huduma ya wakati wote.”

UMOJA KATIKA IBADA NA MAFUNDISHO

Leo makutaniko yote sita nchini Kosovo yamekodi majengo ya kutumia kama Majumba ya Ufalme. Makutaniko mengine ni madogo, kama lile lililo katika mji wa Peć, ambalo lina wahubiri 28. Kwa kuwa kuna upungufu wa ndugu waliowekwa rasmi, makutaniko fulani hayawezi kuwa na hotuba ya watu wote kila juma. Hata hivyo, kama ndugu na dada zao wa mji wa Peć, wanakutana kwa uaminifu kila juma kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na mikutano mingine ya kutaniko.

Kwa miaka mingi Halmashauri ya Nchi ya Serbia iliwafanyia uchungaji wenye upendo ndugu wa Kosovo walipokuwa wakikabili hali ngumu sana. Ili kutimiza mahitaji yanayobadilika ya ndugu hao, Baraza Linaloongoza lilichagua ofisi ya tawi ya Albania isimamie kazi ya kuhubiri nchini Kosovo kuanzia mwaka wa 2000.

Kwa muda mrefu, Mashahidi wengi wa Yehova nchini Kosovo walikuwa Waserbia, kwa hiyo mikutano ilifanywa katika Kiserbia, na ndugu walifurahi kuwasaidia watu waliozungumza Kialbania kuelewa mikutano. Sasa hali imebadilika. Ndugu wengi nchini Kosovo ni Waalbania. Makutaniko yote yanatumia Kialbania isipokuwa kutaniko moja ndilo linalotumia Kiserbia, na ndugu wanafurahi kutafsiri hotuba ili ndugu Waserbia waelewe mikutano. Makusanyiko yote yanafanywa katika lugha zote mbili. Kwa mfano, programu yote ya kusanyiko la wilaya la 2008 ilifanywa katika Kialbania na ikatafsiriwa katika Kiserbia, na hotuba kuu zilitolewa katika Kiserbia na wazee wa Kosovo. Ndugu mmoja anaeleza hivi: “Ingawa watu wengine wanachukiana huko nje, ndani ya jumba sisi ni familia moja.”

Ijapokuwa watu wengi huko Kosovo ni Waislamu, wanaiheshimu Biblia, na wengi wao wako tayari kuzungumzia mambo ya dini. Ndugu wa Kosovo walifurahi sana kupata kilele kipya cha wahubiri 164 katika 2008. Huku wakimtegemea Yehova kikamili, wameazimia kuendelea kujitahidi kabisa kuhubiri eneo lao, na kuwatangazia watu wa mataifa yote habari njema.

Historia ya Kisasa ya Montenegro

Lulu hii iliyojificha ya Mediterania ni nchi ndogo maridadi kwenye Pwani ya Adriatiki. Nchi ya Montenegro ambayo ina mandhari mbalimbali zenye kuvutia sana imezungukwa na Albania, Kosovo, Serbia, na Bosnia na Herzegovina. Nchi hiyo ina ufuo maridadi sana kwenye Bahari ya Adriatiki, wenye urefu wa kilomita 293 hivi. Korongo la Mto Tara ni moja ya makorongo yenye kina zaidi na marefu zaidi huko Ulaya. Ziwa Scutari ndilo ziwa refu zaidi huko Balkani na lina mojawapo ya hifadhi kubwa zaidi za ndege huko Ulaya. Vitu hivyo vyote vinapatikana katika eneo ambalo ni karibu nusu ya eneo la nchi ya Burundi!

Hata hivyo, kwa miaka mingi nchi hiyo imekumbwa na vita, misukosuko, na mateso. Kwa hiyo, hali ambazo watu wa Montenegro wamekabili zimekuwa na uvutano juu ya desturi, mtazamo, na utamaduni wao. Utamaduni wao unakazia hasa sifa kama ujasiri, unyoofu, heshima, unyenyekevu, kujinyima, na kuwaheshimu wengine. Wamontenegro ni wastahimilivu na wengi wao wamekubali habari njema ya Ufalme na wanatetea kweli ya Biblia kwa ushikamanifu.

UKUZI WA KIROHO

Watu wote waliohudhuria kusanyiko la kihistoria la mwaka wa 1991 lililofanyiwa Zagreb, Kroatia, hawawezi kamwe kusahau umoja na upendo wa akina ndugu waliokusanyika huko kutoka sehemu zote za ile iliyokuwa Yugoslavia. Savo Čeprnjić, ambaye alikuwa ameanza kujifunza Biblia anakumbuka hivi: “Ilikuwa hatari sana kusafiri kutoka Montenegro kwenda Kroatia kwa kuwa vita vilikuwa karibu kufyatuka. Nilishangaa kuona mabasi mengi sana yakifika kwenye kusanyiko bila tatizo. Nilivutiwa zaidi na amani na umoja wa Mashahidi. Siku ya kwanza, mamia ya polisi walikuja, lakini walipoona kwamba sisi ni watu wenye amani, ni polisi wachache tu waliokuja kulinda usalama siku zilizofuata.”

Kabla ya vita kuanza, wenzi fulani wa ndoa walisafiri mara nyingi kati ya Kroatia na Montenegro ili kumfundisha Savo. Baada ya mipaka kufungwa, Savo angeendelea jinsi gani kujifunza Biblia?

Savo anaeleza: “Watu waliopendezwa ambao walikuwa wamefanya maendeleo katika funzo lao walilazimika kuwafundisha wengine. Ndugu fulani aliyebatizwa alikuwa akijifunza pamoja nami kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Lakini aliposhindwa kuendelea, mhubiri mwingine ambaye hajabatizwa aliendelea kujifunza pamoja nami. Kufikia mwaka wa 1992, kikundi kilichokutana kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko na Funzo la Mnara wa Mlinzi katika mji wa Herceg Novi kiliongezeka na kuwa na watu 15.” Savo, pamoja na mke wake na binti, waliendelea kufanya maendeleo wakabatizwa mwaka wa 1993. Leo kuna Jumba la Ufalme lenye wahubiri 25 katika mji huo wa pwani wenye kuvutia sana.

Mwanzoni mwa miaka ya 1990, kikundi cha wahubiri kilikutana katika mji mkuu wa Podgorica. Kikundi hicho kiliendelea kukua, na katika mwaka wa 1997 mipango ilifanywa ya kununua uwanja wa kujenga Jumba la Ufalme. Uwanja ambao ndugu walinunua ulizungukwa na ukuta, na hivyo ndugu wakaamua kutoubomoa ili wawe na faragha. Lakini ofisa wa polisi aliyeishi katika chumba cha chini katika jengo jirani aliwaomba wabomoe ukuta huo ili mwangaza ufike kwenye chumba chake chenye giza. Ili wawe na uhusiano mzuri na jirani huyo, akina ndugu walikubali kuubomoa ukuta huo na kuweka ua. Walibarikiwa sana kwa sababu ya kumwonyesha jirani yao upendo!

Wapangaji wengine wa jengo hilo walipoanza kuwasumbua akina ndugu, ofisa huyo wa polisi aliwaonya kwamba angehakikisha wameshtakiwa ikiwa wangevamia Jumba la Ufalme. Sasa akina ndugu wana Jumba zuri sana la Ufalme, vilevile nyumba ya mapainia wa pekee, na kibanda kikubwa cha kuegesha magari ambacho kinaweza pia kutumiwa kwa ajili ya makusanyiko.

Hata hivyo, akina ndugu katika mji wa Nikšić walipata matatizo. Walinunua uwanja mwaka wa 1996, lakini majirani wao walikataa kabisa Jumba la Ufalme lisijengwe. Ndugu walilinda jengo hilo usiku na mchana, wakiogopa kwamba majirani wao wangejaribu kuliharibu. Siku moja, kasisi wa eneo hilo alikusanya umati wa watu 200, wakavamia jengo hilo wakiwa wamebeba bunduki na fimbo. Walifyatua risasi hewani na kuanza kubomoa Jumba la Ufalme, jiwe kwa jiwe. Polisi walisimama kando tu bila kuchukua hatua yoyote.

Ndugu waliposhindwa kusuluhisha tatizo hilo kwa amani, walitafuta jengo lingine. Miaka minne baadaye, walipata jengo lingine, wakalirekebisha na kulifanya kuwa Jumba la Ufalme. Mwanzoni, ilionekana kwamba majirani hawakuwa na tatizo, lakini baada ya miezi michache, Jumba hilo la Ufalme liliteketezwa na watu wasiojulikana. Hata hivyo, ndugu zetu waliazimia kuendelea na hawakukata tamaa. Walijitahidi sana wakajenga upya jumba hilo. Tangu wakati huo hawajasumbuliwa tena.

Makutaniko manne yaliyo nchini Montenegro yanasimamiwa na Halmashauri ya Nchi ya Serbia. Kila mhubiri anahitaji kuwahubiria watu 2,967, na wahubiri 201 walio katika nchi hiyo wanathamini msaada wa mapainia wa pekee 6. Kwa ujumla, watu wa Montenegro wanahisi kwamba dini inategemea sana desturi badala ya kusoma Biblia. Lakini ndugu na dada zetu katika nchi ya Montenegro wanaendelea kwa ushikamanifu kuhubiri habari njema kwa ujasiri.

Historia ya Kisasa ya Slovenia

Kabla ya Slovenia kupata uhuru mwaka wa 1991, ilikuwa sehemu ya kaskazini-magharibi ya Yugoslavia. Baada ya Slovenia kupata uhuru, uchumi wake ulisitawi sana, ikajiunga na Muungano wa Ulaya mwaka wa 2004. Ingawa Slovenia ni nchi ndogo, ina mandhari mbalimbali zenye kuvutia. Ina milima mirefu iliyochongoka, maziwa yaliyo milimani, misitu mikubwa, mapango makubwa sana ya chokaa, na eneo maridadi sana la kitalii la pwani. Kwa muda wa saa moja hivi, unaweza kushuka kwenye miteremko yenye kuvutia sana ya milima na kufika kwenye mashamba yanayonukia vizuri ya mizeituni na mizabibu kwenye Pwani ya Adriatiki. Zaidi ya hayo, unaweza kujifunza mengi sana katika maeneo ya kitamaduni na ya kihistoria ya Slovenia. Hata hivyo, nchi hiyo ndogo ina uzuri mwingine zaidi ya uzuri wa mbuga za kitaifa na miji ya kihistoria. Slovenia ina utajiri mwingi sana wa kiroho.

MAJUMBA YA UFALME NA MAPAINIA

Bila shaka, unakumbuka kwamba Maribor ndio mji ambamo wale “vinyozi wanaoamini Biblia” walihubiri kuhusu imani yao mpya. Mkahawa fulani, ambao baadaye uliitwa kwa kufaa Novi Svet (Ulimwengu Mpya), ulikuwa mahali pazuri sana pa kukutania pa kikundi kidogo kilichoanzishwa huko. Leo, Mashahidi wa Slovenia wanamshukuru Yehova kwa sababu ya Majumba maridadi ya Ufalme ambamo wanakutania ili kuabudu na kufundishwa. Kwa sababu ya kuongezeka kwa idadi ya wahubiri, na kuboreka kwa hali katika miaka ya 1990, Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa ilianzishwa. Kwa msaada wa wajitoleaji zaidi ya 100 na michango kutoka nchi nyingine, makutaniko yamejenga au kurekebisha Majumba ya Ufalme 14 tangu 1995.

Hesabu ya wahubiri iliongezeka na pia hesabu ya mapainia wa kawaida, kutoka mapainia 10 mwaka wa 1990 mpaka 107 mwaka wa 2000. Anica Kristan alikuwa mmoja wa mapainia hao wenye bidii, na kabla ya kukubali kweli alijihusisha sana na siasa.

Ndugu na dada waliokuja kutumika nchini Slovenia kutoka katika nchi nyingine wamechangia sana ukuzi wa kazi ya kuhubiri. Mwaka wa 1992, wamishonari wa kwanza walifika Slovenia, Franco na Debbie Dagostini. Franco na Debbie walipopewa mgawo wa kwenda Afrika, wamishonari wawili wapya, Daniel na Karin Friedl kutoka Austria walitumwa Slovenia. Na hivi karibuni zaidi, wamishonari wa Gileadi, Geoffrey na Tonia Powell na Jochen na Michaela Fischer walitumwa Slovenia. Wamishonari hao pamoja na mapainia wa pekee kutoka Austria, Italia, na Poland, ambao wanampenda sana Yehova, wanatamani sana kuwasaidia watu.

HALMASHAURI ZA UHUSIANO NA HOSPITALI

Mnamo mwaka wa 1994, Dawati la Habari za Hospitali lilifunguliwa Betheli, na Halmashauri mbili za Uhusiano na Hospitali zikaanzishwa. Ndugu fulani waliowekwa rasmi katika halmashauri hizo walikutana na waziri wa afya, ambaye alipanga mkutano pamoja na wakurugenzi wa hospitali zote nchini Slovenia. Ndugu hao walieleza kazi ya Halmashauri za Uhusiano na Hospitali na kwa nini Mashahidi wa Yehova wanakataa kutiwa damu mishipani. Mkutano huo umesaidia madaktari kushirikiana vizuri na wagonjwa wanaokataa kutiwa damu mishipani, na zaidi ya hilo, makala zinazoeleza kuhusu matibabu bila damu zimechapishwa katika magazeti ya kitiba.

Mwaka wa 1995, madaktari wa Slovenia walifanya upasuaji wa kwanza wa moyo bila kutumia damu. Vyombo vya habari viliripoti kwamba upasuaji huo ulifanikiwa, na daktari na mtaalamu wa unusukaputi waliohusika wakaandika makala ya pekee kuhusu upasuaji huo. Hivyo, wagonjwa wanaweza kutibiwa bila kutiwa damu, na madaktari wengi zaidi wako tayari kuheshimu uamuzi wa Mashahidi wa Yehova wa matibabu yasiyohusisha damu.

KUTOSHELEZA MAHITAJI YA HESABU INAYOONGEZEKA YA WAHUBIRI

Baada ya mabadiliko ya kisiasa mwaka wa 1991, Baraza Linaloongoza liliamua kwamba ofisi inapaswa kufunguliwa huko Slovenia ili isimamie vizuri kazi ya Ufalme. Jengo la ghorofa moja lilinunuliwa katikati ya mji mkuu wa Slovenia, Ljubljana. Jengo hilo lilirekebishwa, na mnamo Julai 1, 1993 lilimalizika na Wanabetheli wakajitayarisha kuhamia humo. Mwanzoni, familia ya Betheli ilikuwa na washiriki 10, lakini katika muda wa miaka 10 hesabu yao iliongezeka kufikia 35. Kwa hiyo, jengo la karibu lilikodiwa, nalo lilikuwa na mahali pa kupikia, pa kulia vyakula, na pa kufulia nguo. Wakati huohuo, Wanabetheli walihamia nyumba nyingine za karibu ili kuwe na nafasi zaidi ya ofisi. Mwaka wa 1997, ofisi ya Slovenia ilianza kufanya kazi ikiwa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova.

Baraza Linaloongoza lilipotoa idhini ya kujenga ofisi mpya ya tawi nchini Slovenia, akina ndugu walianza kutafuta uwanja unaofaa. Baada ya kuchunguza viwanja karibu 40, ndugu walichagua uwanja ulio karibu na mji wa Kamnik, kilomita 20 kutoka kwenye mji mkuu, chini ya safu yenye kuvutia ya milima. Muda si muda, walitimiza matakwa yote ya ujenzi, wakapata vibali vya ujenzi, uwanja ukanunuliwa, wakafanya makubaliano pamoja na kampuni ya ujenzi, kisha watumishi wa kimataifa wakaitwa ili washiriki katika ujenzi huo. Walikuwa tayari kabisa kuanza ujenzi.

Hata hivyo, habari kuhusu mradi huo zilipoenea, majirani waliandamana haraka ili kupinga ujenzi huo. Siku ya kuanza ujenzi ilipofika, watu waliandamana na kufunga njia ya kuingia kwenye uwanja huo. Kisha wakabeba mabango ya kupinga mradi huo. Siku sita baadaye, karibu saa sita mchana, polisi 30 hivi walikuja kuwalinda wafanyakazi wa baraza la jiji waliotumwa kuondoa vizuizi vya waandamanaji; waandamanaji hao waliwatukana polisi. Kazi ya ujenzi ilikuwa imeahirishwa, basi hakuna ndugu wala mfanyakazi yeyote wa kampuni ya ujenzi aliyefika mahali pa ujenzi siku hiyo. Upinzani ulianza kupungua baada ya ujenzi kuahirishwa, na ndugu zetu walijaribu kusuluhisha tatizo hilo kwa amani.

Ua wa uwanja huo ulikuwa umebomolewa mara tatu na wapinzani, lakini mwishowe kazi ya ujenzi ilianza tena baada ya mwezi na kuendelea bila kuvurugwa. Kwa kweli, hatua hiyo ya kuwashambulia watu wa Yehova mwishowe ilileta baraka kwa sababu ilitangazwa sana na vyombo vya habari. Ripoti zaidi ya 150 kuhusu ujenzi huo zilitangazwa kwenye televisheni na redio na katika magazeti. Ujenzi ulikamilika baada ya miezi 11, na mnamo Agosti 2005, familia ya Betheli ilihamia majengo hayo mapya.

Tangu wakati huo, uhusiano kati ya ndugu na majirani wao umebadilika kabisa. Majirani wengi wametembelea ofisi ya tawi. Mtu mmoja aliyekuwa mpinzani baadaye alipendezwa sana na ujenzi huo. Alituuliza sisi ni nani na ni kazi gani itakayofanywa katika ofisi hiyo. Alipotembelea ofisi ya tawi, alivutiwa sana kuona akikaribishwa kwa urafiki na alivutiwa pia na usafi wa jengo hilo. Aliwaambia hivi akina ndugu: “Majirani wananiuliza ikiwa sasa nimejiunga nanyi. Nami ninawajibu hivi: ‘Hata ingawa niliwapinga vikali Mashahidi wa Yehova mwanzoni, sasa ninawaunga mkono kwa sababu ni watu wazuri.’”

Agosti 12, 2006 ilikuwa siku yenye furaha kwa sababu Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya wakfu iliyosikilizwa na watu 144 kutoka katika nchi 20 hivi. Katika mkutano wa pekee huko Ljubljana, aliwahutubia wasikilizaji 3,097 kutoka sehemu mbalimbali za Slovenia, na pia kutoka Kroatia na Bosnia na Herzegovina.

WAKATI UJAO MZURI

Mashahidi wa Yehova nchini Slovenia wana tumaini zuri la wakati ujao wakiwa na uhakika kwamba Baba yao wa mbinguni atawaongoza na kuwabariki. Katika kusanyiko la wilaya la 2004, walifurahi sana kupata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kislovenia. Sasa, kwa kuwa wana ofisi mpya ya tawi yenye vifaa na wengi wao wanajitahidi wakiwa mapainia, wameazimia kutimiza mgawo wao wa kuhubiri na kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.

Nchi ya Slovenia ina Wakatoliki wengi, lakini enzi ya Ukomunisti iliwafanya watu wengi waamini kwamba hakuna Mungu. Kwa kuongezea, watu wengi wanalemewa na mahangaiko ya maisha au wanavutiwa na tamaa ya vitu vya kimwili. Wengine wanapendezwa zaidi na michezo au burudani. Hata hivyo, bado kuna watu wenye mioyo minyoofu wanaovutiwa na ahadi za Mungu zilizo katika Biblia.

Kazi imeendelea kusitawi. Slovenia ilifikia kilele cha wahubiri 1,935 katika mwezi wa Agosti 2008, na karibu robo ya wahubiri walishiriki katika utumishi mbalimbali wa upainia. Maeneo ya lugha za kigeni yanatia ndani maeneo yanayotumia Kialbania, Kichina, Kikroatia, Kiingereza, na Kiserbia, vilevile Lugha ya Ishara ya Slovenia. Tofauti na mwanzo mdogo wa kazi ya kuhubiri katika Slovenia, kulipokuwa na vinyozi wawili tu waliohubiri habari njema, sasa kuna umati mkubwa wa wahubiri wenye bidii kutoka katika mataifa mbalimbali wanaowatafuta watu wanaostahili ambao wanataka kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.—Mt. 10:11.

Eneo la Balkan ambalo lilikuwa likiitwa Yugoslavia limekumbwa na misukosuko, huzuni, na mateso mengi. Hata hivyo, ingawa kuna upinzani kuelekea dini na chuki ya kikabila, upendo wa watu wa Yehova umewatambulisha kuwa wanafunzi wa kweli wa Kristo na umethibitisha kwamba ibada ya kweli ya Yehova ni bora kuliko mambo ya ulimwengu huu. Upendo huo wa kimungu umewavutia watu wengi zaidi katika ibada safi, na umewasaidia ndugu zetu kubaki thabiti na kuazimia kuendelea kumtumikia Yehova kwa umoja milele.—Isa. 2:2-4; Yoh. 13:35.

[Maelezo ya Chini]

a Kikundi cha Ustaše kilikuwa kikundi cha kimapinduzi cha Kifashisti ambacho kiliungwa mkono na Kanisa Katoliki katika kupigania uhuru wa Kroatia. Wanajeshi wa kikundi hicho walijulikana sana kwa sababu ya ukatili wao.

b Kwa sababu ya hali ya kisiasa, neno “Kimungu” liliongezwa kwenye kichwa cha kusanyiko ili kuonyesha uhuru ambao akina ndugu walikuwa wakitafuta.

c Ona makala “Kusaidia Familia Yetu ya Waamini Katika Bosnia,” katika Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1994, ukurasa wa 23-27.

[Blabu katika ukurasa wa 165]

Chuki ya kitaifa na ya kidini ilipokuwa ikisitawi Yugoslavia, ndugu zetu walikuwa na umoja

[Blabu katika ukurasa wa 173]

‘Je, niko hapa ili nimpendeze mwanadamu? Hapana! Je, uhai wangu unategemea yale ambayo wengine huenda wakasema, kufikiri, au kufanya? Hapana!’

[Sanduku katika ukurasa wa 144]

Hali Tofauti-Tofauti Katika Ile Iliyokuwa Yugoslavia

Ukiwauliza watu kadhaa wakueleze hali tofauti zilizokuwa katika ile iliyokuwa nchi ya Yugoslavia, inaelekea kwamba utapata majibu mbalimbali. Huenda wote wakakubaliana kwamba kulikuwa na makabila saba yaliyofuata dini tofauti-tofauti na hata yalizungumza lugha tofauti zenye alfabeti tofauti. Kila kabila lina dini yake. Miaka zaidi ya 1,000 iliyopita, dini zinazodai kuwa za Kikristo zilikuwa zimegawanyika katika makundi mawili, dini ya Kikatoliki na dini ya Othodoksi. Nchi iliyoitwa Yugoslavia imegawanyika katikati kabisa kulingana na dini hizo mbili. Watu wengi wanaoishi Kroatia na Slovenia ni Wakatoliki, na wengi wa wale wanaoishi huko Serbia na Makedonia ni Waothodoksi. Nchi ya Bosnia ina mchanganyiko wa Waislamu, Wakatoliki, na Waothodoksi.

Dini imewagawanya watu kama vile lugha zilivyowagawanya. Watu wengi katika ile iliyokuwa Yugoslavia, isipokuwa Kosovo, wanazungumza lugha ya Kislavi ya Kusini. Ingawa kila nchi ina lugha yake, Waserbia, Wakroatia, Wabosnia, na Wamontenegro wanaweza kuwasiliana na kuelewana kwa sababu wanatumia maneno mengi yanayofanana. Lakini hali ni tofauti katika Kosovo, Makedonia, na Slovenia. Mwishoni mwa karne ya 19, jitihada zilifanywa za kuunganisha lugha zinazofanana, lakini nchi ya Yugoslavia iliposambaratika mwaka wa 1991, jitihada hizo zilifikia kikomo. Katika miaka kumi ambayo imepita, nchi zote zimejitahidi sana kuwa tofauti na nchi nyingine kwa kutumia maneno fulani na kuepuka mengine.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 148]

Fundi wa Saa Aeneza Kweli Huko Slavonia

Katika miaka ya 1930, Antun Abramović alisafiri kutoka kijiji mpaka kijiji huko Kroatia, akirekebisha saa. Alipata kijitabu chetu kimoja katika hoteli moja. Alipokisoma, alitambua mara moja kwamba kilifundisha kweli, na moyo wake ukaguswa. Hilo lilimchochea kuandika barua akiomba ofisi ya tawi imtumie vichapo zaidi. Muda si muda, alijiweka wakfu na kuwa mtumishi wa Yehova. Baada ya hapo, aliposafiri kijiji kwa kijiji, hakurekebisha tu saa za watu bali pia aliwahubiria. Kwa kuwa kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku, lilikuwa jambo la busara kuhubiri kisiri-siri huku akirekebisha saa. Katika mji mdogo unaoitwa Privlaka, alikutana na watu fulani ambao walikubali kweli kwa moyo wote. Baada ya muda, kutaniko dogo lilianzishwa. Kuanzia huko, kweli ilienea mpaka Vinkovci na maeneo ya karibu.

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Ndugu Abramović alisaidia kuchapisha kisiri-siri vichapo ambavyo vilisambazwa kotekote Yugoslavia. Kwa sababu ya bidii yake, alikuwa kati ya ndugu 14 waliohukumiwa vifungo virefu gerezani mwaka wa 1947. Baada ya kuachiliwa huru kutoka gerezani, alitumikia akiwa mwangalizi anayesafiri. Aliendelea kumtumikia Yehova kwa bidii maisha yake yote.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 151]

Kiongozi wa Bendi Anakuwa Painia

Miaka mingi iliyopita katika nchi inayoitwa leo Bosnia na Herzegovina, kiongozi wa Bendi ya Royal Guards, Alfred Tuček, alipewa vichapo vinavyozungumzia Biblia na mfanyakazi mwenzake Fritz Gröger. Alfred aliwasiliana na shirika la Lighthouse Society labda mwishoni mwa miaka ya 1920, huko Maribor, akasema kwamba alitaka kuwa painia wa kawaida. Muda si muda, akawa kati ya mapainia wa kwanza nchini Yugoslavia. Hata ingawa alikuwa na kazi yenye mshahara mnono akiwa kiongozi wa bendi ya jeshi, upendo wake kwa Yehova ulimsukuma aache kazi hiyo na akaamua ‘kutotazama mambo yaliyo nyuma.’ (Luka 9:62) Mwanzoni mwa miaka ya 1930, alisafiri pamoja na ndugu mapainia kutoka Ujerumani na kuwaonyesha watu sinema ya “Photo-Drama of Creation.” Pia, alisaidia sana kuchora ramani za maeneo na kupanga kazi ya kuhubiri nchini Yugoslavia. Mwaka wa 1934, alimwoa Frida, mmoja wa mapainia waliotoka Ujerumani. Mgawo wao wa kwanza ulikuwa Sarajevo, Bosnia. Baadaye, walihubiri habari njema katika sehemu fulani za Makedonia, Montenegro, Kroatia, na Serbia. Mwanzoni walisafiri sana kwa baiskeli, lakini baadaye walitumia pikipiki. Ingawa watu hawakukubali habari njema mara moja wakati huo na kwamba kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku, walitambua umuhimu wa kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 155, 156]

Akiwa Mgonjwa na Akiwa na Afya Nzuri

Martin Poetzinger alitumikia katika nchi kadhaa za Ulaya ya Kati kabla ya kupewa mgawo wa kusimamia kikundi fulani cha mapainia huko Yugoslavia. Huko ndiko alikokutana na Gertrud Mende, dada painia mwenye bidii kutoka Ujerumani, ambaye alimwoa baadaye. Mapainia walihitaji kumtegemea kabisa Yehova ilipohusu afya yao. Ingawa hakukuwa na bima ya matibabu, sikuzote walipata msaada waliohitaji. Nyakati nyingine hali ilipokuwa mbaya, Yehova aliwasaidia kupitia watu wenye mwelekeo unaofaa. Kwa mfano, Ndugu Poetzinger alipokuwa mgonjwa sana huko Zagreb, Dada Mende alimsaidia.

Gertrud anakumbuka hivi: “Katikati ya miaka ya 1930, mimi na Martin tulitumwa Sarajevo. Lakini mambo hayakuwa jinsi tulivyotarajia. Martin alikuwa mgonjwa jioni moja, na wakati wa usiku akapata homa na joto lake la mwili likafikia karibu nyuzi 40 Selsiasi. Asubuhi iliyofuata nilipoenda mahali alipokuwa akiishi ili kumjulia hali, bibi aliyemiliki nyumba hizo alikuwa na wasiwasi sana kuhusu hali yake. Mimi na bibi huyo tulijaribu kumtibu kwa dawa ya kienyeji iliyotengenezwa kwa divai iliyochemshwa na kutiwa sukari nyingi sana. Hata hivyo, hakupata nafuu. Niliwapigia simu madaktari fulani ambao nilipata majina yao katika kitabu cha nambari za simu, lakini hakuna yeyote aliyekuwa na nafasi ya kuja haraka. Wote walitoa visababu.

“Bibi aliyemiliki nyumba zile alipendekeza tupigie hospitali simu, kwa hiyo nilimpigia simu msimamizi wa hospitali na kumwambia kwamba Martin alikuwa kitandani akiwa na homa kali na joto la mwili wake lilikuwa limepanda mpaka nyuzi 40 Selsiasi. Mtu huyo alikuwa mwenye urafiki sana na akatuma gari la wagonjwa. Martin alipoingizwa ndani ya gari hilo, yule bibi aliniambia, ‘Hutamwona tena.’

“Nilifadhaika sana na zaidi ya hilo sikuwa na pesa. Sisi mapainia hatukuwa na pesa za kutosheleza mahitaji yetu kwa sababu pesa tulizotumia ni zile zilizotolewa kama michango ya vitabu. Hatukujua jambo la kufanya, na hatukujua matibabu yangegharimu pesa ngapi. Dakt. Thaler alimchunguza Martin na kusema hivi: ‘Mapafu ya Martin yamevimba, anahitaji upasuaji. Itamchukua muda mrefu kupona.’

“Inaonekana Dakt. Thaler aliona kwamba hatukuwa na pesa kwa sababu alisema, ‘Ninataka kuwasaidia watu wenye imani kama yenu,’ na hivyo hakumwomba Martin amlipe pesa za upasuaji. Yehova alitusaidia kukabiliana na hali hiyo ngumu. Kwa sababu ya ugonjwa wa Martin, hatungeweza kwenda Sarajevo, tulilazimika kurudi Ujerumani.”

[Picha]

Martin Poetzinger akiwa Ujerumani, mwaka wa 1931

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 161, 162]

Alifanya Kazi Mchana, na Kuchapisha Usiku

LINA BABIĆ

ALIZALIWA 1925

ALIBATIZWA 1946

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Ametumika Betheli tangu 1953, kazi ilipohalalishwa. Alisaidia katika kuchapisha na kusambaza magazeti na vijitabu. Leo anatumika kwa uaminifu katika Betheli huko Zagreb.

BAADA ya akina ndugu kuachiliwa huru kutoka gerezani, mipango ya kuchapisha magazeti ilifanywa haraka. Lakini ndugu walikuwa wachache, na kazi ilikuwa nyingi. Nilipoona uhitaji huo, niliamua kujitolea, hata ingawa nilikuwa na kazi ya kimwili. Hata hivyo, nilitaka kusaidia. Kwa hiyo, nilifanya kazi yangu ya kimwili mchana kutwa, na karibu usiku wote nilifanya kazi ya kuchapisha magazeti.

Wakati huo, hatukuwa na majengo ya ofisi ya tawi. Hivyo, wenzi wa ndoa waliozeeka, Petar na Jelena Jelić, waliruhusu nyumba yao yenye chumba kimoja itumiwe kwa kazi ya kuchapisha magazeti. Chumba hicho kilikuwa na upana wa mita 4.5 hivi kila upande. Makaratasi yaliyochapishwa yaliwekwa kwenye kitambaa cha kitani kilichotandazwa juu ya fremu ya mbao. Fremu hiyo iliwekwa juu ya kitanda. Mashini ya kuchapishia iliyoendeshwa kwa mikono iliwekwa juu ya meza kando ya kitanda. Tulichapisha kurasa 800 hivi kwa saa. Tulichapisha nakala chache sana ukilinganisha na nakala zinazochapishwa na mashini za kisasa, lakini tulitosheka kwamba kwa subira na jitihada nyingi sana tulichapisha vichapo vyote tulivyohitaji.

Tuliguswa moyo sana kuona ndugu na dada Jelić wakingoja kwa subira mpaka tulipomaliza kufanya kazi na kuondoa vichapo tulivyochapisha ili waweze kulala. Hawakulalamika kamwe. Badala yake, walifurahi, na macho yao yaling’aa kwa shangwe kwa sababu walitegemeza kazi ya Ufalme kwa njia hiyo. Jelena pamoja na dada wengine waliozeeka, walisaidia kukusanya, kuunganisha, na kukunja kurasa zilizochapishwa. Msaada wao ulikuwa muhimu sana.

Mwaka wa 1958, tulinunua mashini ya kuchapishia inayotumia umeme, hivyo, kazi ya kuchapisha ikawa rahisi zaidi. Mwaka wa 1931 tulikuwa tukichapisha magazeti 20 tu, na kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1960, tulikuwa tukichapisha magazeti 2,400 katika lugha tatu, Kikroatia, Kiserbia (Kisirili), na Kislovenia. Hata ingawa hatungeweza kuchapisha vitabu, tulichapisha vijitabu vingi. Mwaka wa 1966, tulifanya kazi kubwa ya kuchapisha kuliko wakati mwingine wowote. Mchapishaji mmoja alichapisha kitabu “Mambo Asiyoweza Mungu Kusema Uongo” katika vijitabu 12. Kila kitabu kilikuwa na seti ya vijitabu 12. Tulilazimika kuchapisha vijitabu 600,000 katika lugha tatu, yaani, vitabu 50,000.

Leo ninatumika katika Betheli ya Zagreb. Ninafurahi ninapokumbuka miaka yangu ya utumishi na kuona jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi katika nchi zote zilizokuwa sehemu ya Yugoslavia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 176, 177]

“Kesho Kila Kitu Kinaweza Kubadilika”

IVICA ZEMLJAN

ALIZALIWA 1948

ALIBATIZWA 1961

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifungwa gerezani mara tano kwa sababu ya msimamo wake wa kutojihusisha na siasa. Baadaye, alitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko mwishoni mwa juma, na leo anatumika akiwa mzee wa kutaniko moja la huko Zagreb.

WAZAZI wangu walikuwa katika kweli, na nyumbani tulizungumza kuhusu kweli. Nilipoitwa ili nijiunge na jeshi, nilienda nikawaambia kwa nini singeweza kufanya kazi hiyo. Baada ya kuwaeleza msimamo wangu wa kutojihusisha na vita, nilihukumiwa kifungo cha miezi tisa. Nilipoachiliwa huru, mwito mwingine wa kunitaka nijiunge na jeshi ulikuwa ukiningojea. Nilishikwa na kuhukumiwa tena, mara hii nilihukumiwa kifungo cha mwaka mmoja. Nilipoachiliwa huru, mwito wa tatu wa kunitaka nijiunge na jeshi ulikuwa ukiningojea, na nikahukumiwa tena. Mara hii nilihukumiwa kifungo cha miezi 15. Mara ya nne, nilihukumiwa kifungo cha miezi 20; na mara ya tano, kifungo cha miaka miwili—kwa ujumla nilifungwa gerezani kwa miaka zaidi ya sita. Mambo yote hayo yalitukia kati ya mwaka wa 1966 na 1980.

Mara mbili nilifungiwa huko Goli Otok kwenye Bahari ya Adriatic. Kisiwa chote kilikuwa gereza la wafungwa wa kisiasa. Nilitendewa kama wafungwa wa kisiasa. Kazi yetu ilikuwa “kujaza mawe baharini.” Tulibeba mawe katika sanduku la mbao kutoka upande mmoja wa kisiwa mpaka upande mwingine, kisha tuliyatupa baharini. Kila sanduku lenye mawe lilikuwa na uzito wa zaidi ya kilo 100. Kisha, tulirudi tena kubeba mawe mengine, na tulifanya kazi hiyo isiyo na maana tena na tena kwa siku nzima.

Nilipofungiwa kwa mara ya pili huko Goli Otok, kulikuwa na zoea la kumweka kila mfungwa mpya katika kifungo cha upweke kwa muda wa mwezi mmoja. Lilikuwa jambo lenye kutisha sana kufungiwa ndani ya jela na kuachwa humo peke yako. Katika pindi hizo nilisali sana kuliko wakati mwingine wowote. Sikuwa na Biblia wala vichapo vya Biblia. Kutengwa kabisa na wengine lilikuwa jaribu kali sana kwangu. Nilitiwa moyo tu na barua kutoka kwa wazazi wangu. Hapo ndipo nilipotambua ukweli wa maneno haya ya mtume Paulo: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.” (2 Kor. 12:10) Nilikuwa mwenye furaha na nguvu kama nini nilipoachiliwa huru kisha nikapata kazi!

Katika gereza lingine, niliombwa niende kumwona daktari mmoja wa magonjwa ya akili aliyekuwa mkali sana na aliyenitukana kwelikweli. Alinifokea, na kuniambia kwamba sikuwa na akili timamu. Sikuruhusiwa kusema neno lolote ili kujitetea. Siku iliyofuata daktari huyohuyo aliniita tena na kuzungumza nami kwa sauti tofauti kabisa na kusema: “Nilikufikiria sana, na ninafikiri kwamba hustahili kukaa gerezani. Nitakutafutia kazi nje ya gereza hili.” Na jambo la kushangaza ni kwamba, alifanya jinsi alivyoahidi. Sijui ni nini kilichomfanya abadili maoni yake, lakini jambo hilo lilinionyesha kwamba hatuhitaji kamwe kuogopa au kufikiri kwamba mambo hayawezi kubadilika. Kesho kila kitu kinaweza kubadilika. Ninamshukuru Yehova kwa mambo yote hayo niliyopitia maishani ambayo yamenisaidia nimkaribie zaidi.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 179]

“Je, Watu Wanaruhusiwa Kuzungumza Kuhusu Mchezo wa Kandanda?”

HENRIK KOVAČIĆ

ALIZALIWA 1944

ALIBATIZWA 1962

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alitumika mwaka wa 1973 akiwa mwangalizi anayesafiri mwishoni mwa juma, na baadaye kuanzia mwaka wa 1974 mpaka 1976, aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi anayesafiri wa wakati wote. kwa sasa yeye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Kroatia.

HATUKUJUA kamwe ikiwa tungeweza kurudi nyumbani kutoka katika huduma. Mara nyingi, polisi walitukamata na kutuhoji. Kwa kawaida, watu walikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu kazi yetu.

Pindi moja kwenye kituo cha polisi, niliambiwa kwamba tuliruhusiwa tu kuzungumza kuhusu Mungu mahali fulani palipochaguliwa kwa ajili ya kusudi hilo na si barabarani wala nyumba kwa nyumba. Kama Nehemia, nilitoa sala fupi ili kumwomba Yehova anisaidie kupata maneno yanayofaa. Kisha, nikamuuliza mchunguzi huyo, “Je, watu wanaruhusiwa kuzungumza kuhusu mchezo wa kandanda wakiwa uwanjani tu au wanaweza kufanya hivyo mahali pengine pia?” Alijibu kwamba watu wanaweza kufanya hivyo mahali popote pale. Nikamwambia hivi: “Hivyo, basi, unaweza pia kuzungumza kuhusu Mungu mahali popote pale, si kanisani tu au mahali fulani pa ibada.” Ingawa tulihojiwa kwa muda wa saa tano, mimi na mwenzangu tuliachiliwa huru.

Mimi na mke wangu, Ana, tunapokumbuka miaka 40 ya utumishi, tunaweza kusema kwamba hatuwezi kuacha utumishi huo kwa ajili ya kitu kingine chochote ulimwenguni. Mimi na mke wangu tumepata pendeleo la kuwasaidia watu 70 hivi kujifunza kweli. Kila mgawo ambao Yehova anataka tufanye unaboresha tu maisha yetu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 195, 196]

Tuliahidi Kurudi

HALIM CURI

ALIZALIWA 1968

ALIBATIZWA 1988

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alisaidia kupanga na kusambaza misaada huko Sarajevo. Sasa anatumika akiwa mzee, mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali, na wakili wa Mashahidi wa Yehova huko Bosnia na Herzegovina.

MWAKA wa 1992, jiji la Sarajevo lilizingirwa na wanajeshi. Tulipokosa kupata magazeti mapya, tulijifunza magazeti ya zamani. Akina ndugu walitumia taipureta nzee kunakili makala za funzo zilizopatikana. Ingawa kulikuwa na wahubiri 52 tu, watu zaidi ya 200 walihudhuria mikutano yetu, nasi tuliongoza mafunzo ya Biblia 240 hivi.

Mnamo Novemba 1993, wakati vita vilipokuwa vimepamba moto, binti yetu, Arijana, alizaliwa. Haikuwa rahisi hata kidogo kumlea mtoto wakati huo. Nyakati nyingine, hatukuwa na maji ya bomba wala umeme kwa majuma mengi. Tulipata kuni kwa kupasua vyombo vya nyumbani vya mbao, nasi tulipitia maeneo hatari ili kufika kwenye mikutano. Wavamizi walifyatua risasi kiholela, hivyo ilitubidi tukimbie ili kuvuka barabara fulani na vizuizi.

Siku moja yenye utulivu, tulipokuwa tukirudi nyumbani kutoka kwenye mkutano pamoja na mke wangu na mtoto wetu na Ndugu Dražen Radišić, risasi zilianza kufyatuliwa ghafula. Tulilala chini barabarani, lakini nilipigwa risasi tumboni. Nilikuwa na maumivu makali sana. Watu wengi waliona kilichotukia kupitia madirisha ya nyumba zao, na vijana fulani wenye ujasiri walitoka nje ya nyumba haraka na kutupeleka mahali salama. Nilikimbizwa hospitalini, ambako walitaka kunitia damu mishipani haraka. Nilimweleza daktari kwamba dhamiri yangu haiwezi kuniruhusu nitiwe damu mishipani. Walinishinikiza nifikirie tena jambo hilo; lakini niliazimia kusimama imara na nilikuwa tayari kwa matokeo yoyote yale. Nilifanyiwa upasuaji kwa muda wa saa mbili na nusu, na nilipata nafuu bila kutiwa damu mishipani.

Baada ya upasuaji, nilihitaji kupumzika, lakini ilikuwa vigumu kufanya hivyo kwa sababu ya vita. Tuliamua kutembelea familia yetu huko Austria. Hata hivyo, njia pekee ya kutoka Sarajevo ilipitia chini ya uwanja wa ndege. Njia hiyo ilikuwa na urefu wa mita 900 na kimo cha sentimita 120 hivi. Mke wangu alimbeba mtoto, nami nikajaribu kubeba mizigo. Lakini kwa sababu ya upasuaji, ilibidi mke wangu anisaidie.

Tulifurahia sana kukaa Austria. Tulipokuwa tukiondoka Sarajevo, tuliwaahidi ndugu zetu na Muumba wetu kwamba tutarudi. Haikuwa rahisi hata kidogo kuiacha familia yetu huko Austria, hasa mama yangu. Lakini tuliwaeleza kwamba tulikuwa tumemwahidi Mungu tutarudi Sarajevo ikiwa angetusaidia kutoka huko na kupumzika kidogo. Sasa je, kweli tungeweza kumwambia Mungu: “Asante kwa kutusaidia kufika huku. Tunafurahia sana kuwa huku, na sasa tungependa kukaa huku”? Pia, akina ndugu wa Sarajevo walituhitaji. Mke wangu, Amra, alinitegemeza sana katika mambo yote hayo.

Hivyo, Desemba 1994, tulifika kwenye ile njia ya chini ya ardhi huko Sarajevo. Wakati huu tulikuwa tukiingia Sarajevo kutoka nje. Watu walipotuona tukirudi kupitia mfereji huo, walituuliza: “Mnafanya nini? Kila mtu anataka kuondoka, lakini ninyi mnarudi katika jiji lililozingirwa?” Siwezi kueleza kikamili shangwe tuliyokuwa nayo tulipokutana tena na ndugu zetu kwenye Jumba la Ufalme la Sarajevo. Hatujawahi kamwe kujuta kwamba tulirudi.

[Sanduku katika ukurasa wa 210]

Visiwa vya Kroatia

Ukanda wa pwani wa Kroatia wenye urefu wa kilomita 1,778 una visiwa zaidi ya 1,000, na visiwa 50 hivi kati yake vinakaliwa na watu. Visiwa hivyo vina ukubwa mbalimbali, kuanzia chini ya kilomita moja ya mraba mpaka kilomita 400 za mraba.

Wakaaji wa visiwa hivyo wanafanya hasa kazi ya uvuvi, wanakuza mizeituni, na wanatunza mashamba ya mizabibu na mabustani yao. Unaweza kufurahia kupiga mbizi katika Mbuga ya Kitaifa ya Kornati, ambayo ina visiwa na miamba 140. Katika visiwa vya Krapanj na Zlarin, wakaaji hupiga mbizi ili kupata matumbawe na wanyama wa baharini wanaoitwa sifongo. Urujuani, asali, na mafuta ya mmea wa rosemary yanazalishwa katika kisiwa cha Hvar. Wakaaji wa kisiwa cha Pag chenye ukame, wanatumia maziwa ya kondoo wanaokula majani na nyasi zenye chumvi za kisiwa hicho ili kutengeneza jibini fulani inayopendwa sana.

Mashahidi wa Yehova wanajitahidi sana kuwahubiria wakaaji wote. Wengine wanavuka daraja tu ili kufika kwenye kisiwa, na inawabidi wengine kupanda feri. Vikundi vya Mashahidi vinapenda kupanga kampeni za pekee za kuhubiri katika kisiwa fulani kwa siku chache. Hata hivyo, ni vigumu kuzungumza na wakaaji wa visiwa hivyo kwa sababu wana lahaja ya pekee ambayo haieleweki kwa urahisi na wakaaji wa bara.

Kwa kupendeza, wakaaji wa visiwa wanakubali habari njema, na kisiwa cha Korčula kina kutaniko la wahubiri 52. Kwa kuwa kutaniko hilo liko mbali, wasemaji wanaokuja kutoa hotuba za watu wote wanapata ugumu wanaposafiri. Lakini jitihada zao zinasaidia kutaniko hilo la mbali kuendelea kuunganishwa na undugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote.—1 Pet. 5:9.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 224]

“Nilienda Gerezani Siku 11 Mapema”

PAVLINA BOGOEVSKA

ALIZALIWA 1938

ALIBATIZWA 1972

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alianza kufanya upainia mwaka wa 1975 naye akawa painia wa pekee wa kwanza huko Makedonia mwaka wa 1977. Amewasaidia watu 80 kujifunza kweli.

MARA nyingi nilipokuwa nikihubiri, watu waliniripoti kwa polisi, ambao walinishika na kunipeleka kwenye kituo cha polisi ambako nilihojiwa, nyakati nyingine kwa saa nyingi. Nilitozwa faini mara nyingi. Katika mahakama, nilishtakiwa kimakosa kwamba nilikuwa adui wa kisiasa wa Serikali na kwamba nilikuwa nikieneza propaganda za Ulaya na Marekani. Pindi moja nilihukumiwa kifungo cha siku 20 gerezani, na pindi nyingine kifungo cha siku 30.

Nilipaswa kuwa katika kifungo cha siku 20 wakati uleule ambapo kusanyiko la wilaya lingefanywa. Niliomba mahakama iahirishe hukumu yangu; lakini ombi langu lilikataliwa, kwa hiyo nikaamua kwenda gerezani siku 11 mapema. Maofisa wa gereza walishangaa kuniona. Hawakuamini kwamba mtu anaweza kuomba kufungwa gerezani haraka iwezekanavyo. Nilipata nafasi ya kutoa ushahidi, nao wakaniahidi kwamba wangejitahidi sana kunitunza. Siku 11 baadaye, ofisa wa polisi alikuja gerezani kuona ikiwa nilikuwa nimefika. Hebu wazia jinsi alivyoshangaa alipojulishwa na maofisa wa gereza kwamba tayari nilikuwa nimekaa gerezani kwa siku 11! Mwishowe, niliweza kuhudhuria kusanyiko.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 232]

‘Walinihudumia kwa Njia Bora Kabisa’

ŠANDOR PALFI

ALIZALIWA 1933

ALIBATIZWA 1964

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Wazazi wake walijifunza kweli katika kambi iliyoanzishwa na kikundi cha Wakomunisti muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Alikuwa mwangalizi anayesafiri mwishoni mwa juma na sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Serbia.

KWA sababu familia yangu ilizaliwa Hungaria, tulipelekwa kwa muda mfupi katika kambi iliyoanzishwa na kikundi cha Wakomunisti. Hatua hiyo ilituletea baraka, kwa sababu wazazi wangu walijifunza kweli katika kambi hiyo. Nikiwa kijana, sikupendezwa sana na kweli. Lakini Ndugu Franz Brand aliyeishi katika nyumba yetu kwa miaka kadhaa alinisaidia sana kubadili maoni yangu. Nilidhani kwamba nilikuwa nikimsaidia tu nilipokubali ombi lake la kutafsiri kichapo cha Kihungaria katika Kiserbia. Baadaye niligundua kwamba hakikuhitaji kutafsiriwa; alitaka tu kuhakikisha kwamba nimesoma kichapo hicho. Mbinu yake ilifanya kazi, na punde si punde, nikabatizwa mwaka wa 1964.

Jambo moja lililoniletea shangwe kubwa sana lilikuwa kutumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri. Haikuwa rahisi sikuzote kwa sababu akina ndugu walikuwa maskini. Mara nyingi nililala pamoja na familia nzima katika chumba kimoja. Kujidhabihu kwa njia hizo zote kulileta faida. Nilifurahi sana kuona shangwe ya akina ndugu, ambao walikuwa wakingojea kwa hamu ziara yangu. Walijitahidi kadiri wawezavyo kunihudumia kwa njia bora kabisa. Sikuwa na sababu yoyote ya kulalamika.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 236, 237]

“Ninaweza Kuwapata Wapi Watu Hawa?”

AGRON BASHOTA

ALIZALIWA 1973

ALIBATIZWA 2002

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa mwanajeshi katika Jeshi la Ukombozi la Kosovo na sasa anatumika akiwa painia wa kawaida na mtumishi wa huduma.

NILIPOONA mambo mabaya sana yaliyofanywa wakati wa vita, kama vile kuwaua watoto wadogo, nilikata kauli kwamba hakuna Mungu. Nilifikiri hivi: ‘Ikiwa yupo, kwa nini hakomeshi mateso haya yote?’ Imani yangu ilidhoofika zaidi nilipoona jinsi viongozi wa dini ya Kiislamu walivyounga mkono vita dhidi ya Waserbia. Kabla ya vita, nilikuwa Mwislamu, hata hivyo, vita vilipokwisha, sikuamini tena kwamba kuna Mungu, na nilijiunga na Jeshi la Ukombozi la Kosovo. Ingawa nilikuwa katika jeshi hilo kwa muda mfupi tu, niliheshimiwa sana na nilipata mapendeleo mengi. Hilo lilinifanya niwe mkali na mwenye kiburi kwa sababu watu walifanya nilivyoagiza.

Inasikitisha kwamba nilimtendea mke wangu kwa njia hiyohiyo. Nilifikiri kwamba anapaswa kufanya kila jambo ninalomwambia na kutii maagizo yangu yote. Mke wangu, Merita, alikuwa amekutana na Mashahidi wakati wa vita na alikuwa na vitabu vyao vichache. Usiku mmoja kabla ya kwenda kulala, alisema hivi: “Chukua vitabu hivi usome. Vina habari kumhusu Mungu.” Nilikasirika kwamba alifikiri angenifundisha kumhusu Mungu. Ili kuepuka ugomvi, Merita alienda kulala.

Nilibaki na vitabu hivyo, nikaamua kusoma broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Kisha nikasoma kijitabu Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli. Nikiwa Mwislamu, nilishangaa kuona kwamba kilinukuu Kurani. Halafu nikasoma magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baadaye usiku huohuo, nilienda katika chumba cha kulala na kumwamsha mke wangu. Nilimuuliza: “Ni nani aliyekupa vitabu hivi? Ninaweza kuwapata wapi watu hawa?”

Niliguswa moyo sana na mambo niliyosoma, lakini mke wangu alikuwa na shaka na aliogopa kwa kuwa hakujua nilichokusudia kufanya. Hata hivyo, usiku huo tulimpigia simu Shahidi mmoja, akatujulisha wakati na mahali ambapo wangefanyia mkutano wao. Asubuhi iliyofuata tulihudhuria mkutano huo. Nilivutiwa sana kuona jinsi ndugu walivyotukaribisha kwa fadhili! Sikufikiri kamwe kwamba kuna watu kama hao duniani. Niliona wazi kwamba walikuwa tofauti. Wakati wa mkutano nilikuwa na swali ambalo nilitaka sana lijibiwe, hata niliinua mkono wangu ili niulize swali hilo. Wazee walikuwa na wasiwasi kidogo kwa sababu hawakujua kwa nini nilitaka sana kuzungumza nao. Bila shaka, walifurahi sana walipotambua kwamba nilitaka tu kujua nilichopaswa kufanya ili niwe Shahidi wa Yehova.

Nilianza kujifunza Biblia siku hiyohiyo. Nilitaka kuboresha sana utu wangu, na haingekuwa rahisi kufanya hivyo. Nilitaka kuacha kuvuta sigara, na nilihisi kwamba nilihitaji kuvunja uhusiano na marafiki wangu wa zamani. Kusali na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kulinisaidia kutubu mwenendo wangu wa zamani wa maisha na kuvaa utu mpya. Kweli imebadili kabisa maisha yangu na ya familia yangu! Sasa mimi na mke wangu tunatumikia tukiwa mapainia wa kawaida, na mwaka wa 2006, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. Sasa ninaweza kuwasaidia wengine kuelewa kwa nini watu wanateseka na jinsi Yehova atakavyotatua matatizo yetu yote hivi karibuni.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 249, 259]

“Ni Kana Kwamba Yehova Aliwafumba Macho”

JANEZ NOVAK

ALIZALIWA 1964

ALIBATIZWA 1983

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikaa gerezani kwa miaka mitatu kwa sababu ya imani yake na sasa yeye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Slovenia.

MNAMO Desemba 1984, wakuu wa jeshi waliniagiza tena na tena nijiunge na jeshi. Walipobandika kwenye mlango wangu taarifa ya kuniita katika jeshi na kutisha kwamba askari-jeshi wangekuja kunichukua, niliamua kwenda kwenye kambi ya jeshi ili nieleze msimamo wangu. Sikufaulu, hivyo wakaamua kufanya yote wanayoweza ili kunilazimisha kuwa mwanajeshi. Walininyoa kichwa, wakachukua nguo zangu za raia, na kunipa nguo za wanajeshi. Nilipokataa nguo hizo, walinivisha kwa nguvu, kisha wakajaribu kunilazimisha kushika kalamu na kutia sahihi ya kukubali kujiunga na jeshi. Nilikataa.

Pia nilikataa kufanya mazoezi ya asubuhi na kuisalimu bendera. Wanajeshi wanne waliponipeleka uwanjani na kuniamuru nifanye mazoezi, nilikataa kuinua mikono yangu. Walijaribu kuinua mikono yangu lakini wakaona kwamba ni jambo la kipumbavu sana kujaribu kuniinua mikono. Walinielekezea bunduki na kutisha kuniua. Nyakati nyingine walijaribu kunihonga kwa kunipa kahawa na keki.

Wanajeshi wengine walilia walipoona azimio langu. Wengine walikasirika nilipokataa kuitemea mate picha ya Jemadari Tito ambayo waliiweka mbele ya uso wangu. Baada ya siku kadhaa, walijaribu kunilazimisha kubeba silaha, nikakataa pia. Hilo lilionwa kuwa kosa la kijeshi, hivyo nikafungiwa kambini kwa mwezi mmoja. Halafu nilikaa gerezani huko Zagreb, Kroatia, kwa majuma kadhaa, nikingojea uamuzi. Taa nyekundu iliwashwa kwenye chumba changu cha gereza usiku mzima, na niliruhusiwa kwenda chooni ikiwa tu askari aliyekuwa kwenye zamu alikuwa na furaha siku hiyo.

Mwishowe, nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu gerezani kwenye kisiwa cha Adriatiki kinachoitwa Goli Otok, ambako wafungwa hatari sana walipelekwa. Walinipeleka kwenye gereza hilo ambalo lilikuwa na wafungwa wakatili sana. Walinifunga mikono kwa minyororo kwa sababu nilikataa kupigana vita. Katika gereza hilo nilikutana na Mashahidi wengine wanne ambao walifungwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono vita.

Hatukuruhusiwa kuwa na Biblia au kitabu kingine chochote. Hata hivyo, tayari kulikuwa na Biblia moja gerezani. Watu wangu wa ukoo walinitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi ndani ya sanduku lenye sehemu iliyojificha. Walinzi hawakupata kamwe vichapo vyetu wala hawakugundua kamwe kwamba tulikuwa tukifanya mikutano ya Kikristo. Nyakati nyingine, walinzi walipokuja, vichapo vilivyosahauliwa vilikuwa mbele yao tu, lakini ni kana kwamba Yehova aliwafumba macho kwa sababu hawakuviona hata kidogo.

Baada ya mwaka mmoja, nilipelekwa Slovenia ili nimalizie kifungo changu huko. Nilimwoa Rahela nilipokuwa gerezani. Nilipoachiliwa huru, nilianza kufanya upainia pamoja na mke wangu, na tangu 1993 tumekuwa tukitumikia katika Betheli ya Slovenia.

[Chati/Grafu katika ukurasa wa 244, 245]

MFUATANO WA MATUKIO—Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia

Miaka ya 1920 Kikundi kidogo chakutana huko Maribor, Slovenia, kuzungumzia Biblia.

Miaka ya 1930 Mapainia wanaozungumza Kijerumani watumwa Yugoslavia.

1935 Ofisi ya tawi yaanzishwa huko Belgrade, Serbia, ili kusimamia kazi.

1940

1941 Jeshi la Ujerumani lavamia, kisha upinzani mkali waanza.

1950

1953 Mashahidi wa Yehova waandikishwa kisheria; hata hivyo, kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba inazuiwa.

1960

1969 Kusanyiko la kimataifa lafanywa katika uwanja huu huko Nuremberg, Ujerumani.

1970

1990

1991 Kusanyiko la kwanza la kimataifa lafanywa huko Zagreb, Kroatia. Wamishonari wa kwanza waliozoezwa Gileadi wafika. Ofisi yafunguliwa huko Slovenia chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Austria. Vita vyaanza.

1993 Mashahidi wa Yehova waandikishwa huko Makedonia.

1994 Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali yaanzishwa huko Slovenia.

2000

2003 Mashahidi wa Yehova watambuliwa kisheria huko Kroatia. Betheli mpya yawekwa wakfu huko Makedonia.

2004 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yatolewa katika Kislovenia.

2006 Ofisi mpya ya tawi yawekwa wakfu huko Slovenia. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa nzima yatolewa katika Kikroatia, Kiserbia, na Kimakedonia. Kikundi cha Kichina chaanzishwa huko Belgrade, Serbia.

2007 Hotuba ya pekee yatolewa kwa mara ya kwanza kabisa katika lugha ya Kiromani huko Makedonia. Kichapo cha kwanza cha Kiromani chatolewa.

2010

[Grafu]

(See publication)

Jumla ya Wahubiri

Jumla ya Mapainia

14,000

10,500

7,000

3,500

1940 1950 1960 1970 1990 2000 2010

[Ramani katika ukurasa wa 147]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

JAMHURI YA CHEKI

AUSTRIA

VIENNA

SLOVAKIA

BRATISLAVA

HUNGARIA

BUDAPEST

RUMANIA

BULGARIA

UGIRIKI

ALBANIA

TIRANË

BAHARI YA IONIA

ITALIA

BAHARI YA ADRIATIKI

ILE ILIYOKUWA YUGOSLAVIA

SLOVENIA

LJUBLJANA

Maribor

Kamnik

KROATIA

ZAGREB

SLAVONIA

Osijek

Vukovar

Vinkovci

Privlaka

Jasenovac

Šibenik

Split

PWANI YA DALMATIA

Goli Otok

Pag

Kornat

Zlarin

Krapanj

Hvar

Korčula

BOSNIA NA HERZEGOVINA

SARAJEVO

Bihać

Banja Luka

Tuzla

Travnik

Zenica

Vareš

Mostar

SERBIA

BELGRADE

VOJVODINA

Bor

MONTENEGRO

PODGORICA

Nikšić

Herceg Novi

Tara

Ziwa Scutari

KOSOVO

Peć

Priština

MAKEDONIA

SKOPJE

Tetovo

Kočani

Štip

Kičevo

Strumica

Resen

Taarifa: Shirika la Umoja wa Mataifa liliripoti kwamba “Kosovo ilijitangaza kuwa huru kutoka chini ya Serbia mnamo Februari [2008].” Ili kujaribu kutatua mzozo kuhusu hali ya kisiasa ya Kosovo, Baraza Kuu la UM linatafuta “maoni kutoka katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki.”

[Picha katika ukurasa wa 142]

[Picha katika ukurasa wa 145]

Franz Brand

[Picha katika ukurasa wa 146]

Rudolf Kalle, na moja ya taipureta zake

[Picha katika ukurasa wa 149]

Ndugu wakihubiri huko Slovenia wakitumia lori ambalo walikodi

[Picha katika ukurasa wa 154]

Mapainia wa zamani walikabili matatizo mengi

[Picha katika ukurasa wa 157]

Alfred na Frida Tuček wakiwa na baiskeli zao

[Picha katika ukurasa wa 158]

Rudolf Kalle akiwa mbele ya Betheli ya Belgrade, Serbia

[Picha katika ukurasa wa 168]

Franc Drozg, na nakala ya barua yake

[Picha katika ukurasa wa 180]

Kulia: Nyumba ya farasi ambayo iligeuzwa kuwa Jumba la Ufalme, Ljubljana, Slovenia

[Picha katika ukurasa wa 180]

Chini: Moja kati ya Majumba ya kwanza ya Ufalme huko Zagreb, Kroatia

[Picha katika ukurasa wa 182]

Stojan Bogatinov

[Picha katika ukurasa wa 184, 185]

Nyuma: Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” la mwaka wa 1969, Nuremberg, Ujerumani; kushoto: gari-moshi la wajumbe wa kusanyiko kutoka Yugoslavia; kulia: Nathan Knorr

[Picha katika ukurasa wa 188]

Ðuro Landić

[Picha katika ukurasa wa 192]

Milton Henschel akitoa hotuba, na chini, ubatizo kwenye Kusanyiko la Kimataifa la “Wapendao Uhuru wa Kimungu” mwaka wa 1991, Zagreb, Kroatia

[Picha katika ukurasa wa 197]

Ljiljana akiwa na binti zake

[Picha katika ukurasa wa 199]

Misaada ilisafirishwa kwa lori kutoka Austria

[Picha katika ukurasa wa 200]

Familia ya Ðorem, 1991

[Picha katika ukurasa wa 204]

Ubatizo katika pipa la samaki huko Zenica, 1994

[Picha katika ukurasa wa 209]

Misaada ilihifadhiwa Zagreb, Kroatia

[Picha katika ukurasa wa 215]

Elke na Heinz Polach

[Picha katika ukurasa wa 216]

Halmashauri ya Tawi ya Kroatia, na ofisi ya tawi

[Picha katika ukurasa wa 228]

Kupeleka misaada huko Bosnia

[Picha katika ukurasa wa 233]

Halmashauri ya Nchi ya Serbia, na majengo ya Betheli huko Belgrade

[Picha katika ukurasa wa 235]

Saliu Abazi

[Picha katika ukurasa wa 243]

Kuhubiri huko Podgorica; Jumba la Ufalme huko Podgorica

[Picha katika ukurasa wa 247]

Mji wa kale wa Piran, Slovenia

[Picha katika ukurasa wa 251]

Ofisi ya tawi ya zamani huko Ljubljana, Slovenia, 2002

[Picha katika ukurasa wa 253]

Ofisi ya tawi huko Kamnik, Slovenia, 2006

[Picha katika ukurasa wa 254]

Halmashauri ya Tawi ya Slovenia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki