Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • foa makala 6
  • Kuwa na Umoja Katika Nchi Iliyogawanyika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwa na Umoja Katika Nchi Iliyogawanyika
  • Hifadhi Yetu ya Vitu vya Kale
  • Vichwa vidogo
  • Kukabiliana na Hatari Zinazotokana na Migawanyiko
  • Kukutanika Pamoja Katika Nchi Iliyogawanyika
  • Kutoa Ushahidi Katika Maeneo Yaliyotengwa
  • Ingawa Walizungukwa na Chuki, Waliunganishwa na Upendo
Hifadhi Yetu ya Vitu vya Kale
foa makala 6
Milton Bartlett akiwa pamoja na baadhi ya akina ndugu weusi wakihubiri katika eneo la watu weusi wakati wa ubaguzi.

HIFADHI YETU YA VITU VYA KALE

Kuwa na Umoja Katika Nchi Iliyogawanyika

Kuanzia mwaka wa 1948 hadi miaka ya 1990, mfumo wa kisiasa nchini Afrika Kusini ulikuwa na ubaguzi wa rangi.a Katika kipindi hicho, wengi waliwatendea watu wa rangi tofauti isivyo haki. Wakati huo wa ubaguzi, Kallie alihesabiwa kwenye kundi la “machotara” (wazazi wake wametoka jamii mbili tofauti), naye anasema hivi: “Watu ambao hawakuwa weupe walikuwa wakibaguana wenyewe kwa wenyewe pia.”

Nchini Afrika Kusini Mashahidi wa Yehova wanatoka katika jamii na malezi mbalimbali. Walikabilianaje na ubaguzi? Tunajifunza nini kutokana na historia yao?

Kukabiliana na Hatari Zinazotokana na Migawanyiko

Baadhi ya watu waliopinga ubaguzi wa rangi walikuwa wakifanya maandamano nchini. Wengi kati ya wale waliopinga sera za serikali walifungwa, na baadhi yao waliuawa. Hivyo, wale waliopinga serikali wakawa na jeuri hata zaidi. Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova walitii sheria zilizowekwa na hawakujihusisha na maandamano au kujaribu kupindua serikali. Kwa njia hiyo, waliwaiga Wakristo wa karne ya kwanza ambao waliendelea “[kujitiisha] kwa mamlaka zilizo kubwa.”​—Waroma 13:1, 2.

Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova walishinikizwa wavunje msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Lakini, ikiwa wangeunga mkono upande fulani, hilo lingewafanya wajihusishe na migogoro ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea au hata wangejipata wakipigana na ndugu zao wa kiroho. Kwa mfano, Thembsie anaeleza hivi: “Mwaka 1976, wanafunzi wengi wa sekondari walilazimishwa kushiriki katika ghasia za kisiasa. Wanafunzi waliojihusisha katika ghasia hizo walienda kila mlango wakiwatafuta wanafunzi wengine ili wajiunge nao. Ikiwa mtu angekataa kujiunga nao, basi huenda wangechoma nyumba yake moto au hata wangempiga kufikia hatua ya kumwua.” Kiongozi mmoja wa chama cha upinzani alimwambia hivi Shahidi anayeitwa Theophilus, “Tukishamshinda mzungu, tutakuua kwa sababu hukupigana kwa ajili ya nchi yako.”

Kukutanika Pamoja Katika Nchi Iliyogawanyika

Licha ya magumu yaliyosababishwa na ubaguzi, Mashahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini waliendelea kukutana pamoja kwa ajili ya ibada. (Waebrania 10:24, 25) Baadhi ya makutaniko hayakuweza kujenga Majumba ya Ufalme kwa sababu watu wengi hawakuwa na uwezo wa kujikimu chini ya mfumo wa ubaguzi wa rangi.b Enver anasema hivi: “Kwa miaka mingi, tulilazimika kukodi majengo ambayo yalikuwa katika hali mbaya sana. Hivyo, baba yangu aliruhusu mikutano ya kutaniko ifanywe nyumbani kwetu. Nyumba yetu ilitumika kama Jumba la Ufalme mara mbili kwa juma. Pindi nyingine, nyumba yetu ilijaa watu hata zaidi ya watu 100. Baada ya mikutano, tulifurahia kuwaonyesha ukarimu wote waliohudhuria.”

Mashahidi weupe na weusi wakiwa wamekutanika pamoja, Aprili 1950

Mkutano wa watu wa rangi tofauti, katika Uwanja wa Rand, Johannesburg, mwaka 1980

Akina ndugu walitafuta njia za kushinda ubaguzi kwa werevu. Kwa mfano, katika Mkoa wa Limpopo, ndugu mweupe ambaye aliombwa atoe hotuba kwenye kusanyiko la mzunguko lililofanywa katika eneo la watu weusi hakuruhusiwa kuingia humo. Basi, alimwendea mtu mweupe aliyemiliki shamba lililopakana na eneo la watu weusi na kufanya makubaliano. Hivyo, kusanyiko lilifanywa huku msemaji akiwa ndani ya ua la shamba hilo na wahudhuriaji wakiwa upande wa pili.

Kutoa Ushahidi Katika Maeneo Yaliyotengwa

Wakati wa ubaguzi, watu wa jamii mbalimbali watenganishwa kulingana na rangi zao. Hata maeneo ya makutaniko yalipangwa kulingana na jamii ya watu walioishi katika eneo hilo. Kwa sababu ya ubaguzi Mashahidi walihitaji kubadilikana na hali walipopanga wahubiri kwa ajili ya utumishi wa shambani. Kwa mfano, haikuwa rahisi kuhubiri katika eneo ambalo halijagawiwa kutaniko. “Kwa kawaida hakukuwa na maeneo ambayo watu ambao si weupe waliruhusiwa kulala. Krish, ambaye wakati wa ubaguzi alihesabiwa kwenye kundi la “Wahindi” anasema: “Hivyo, tulilala ndani ya magari yetu au chini ya miti. Kisha asubuhi, tulienda kwenye kituo cha mafuta na kuoga chooni. Nyakati nyingine hata vyoo hivyo vilikuwa vimeandikwa ‘Weupe Pekee.’ Ingawa hivyo, wahubiri waliunga mkono utumishi na walifurahia sana kuwahubiria watu wengi waliopendezwa katika maeneo ya vijijini.”

Kikundi cha Mashahidi wa rangi tofauti wakihubiri katika eneo la vijijini, mwaka 1981

Licha ya magumu hayo, idadi ya watu wa Yehova iliendelea kuongezeka. Sera ya ubaguzi wa rangi ilipoanzishwa mwaka wa 1948, kulikuwa na wahubiri 4,831 Afrika Kusini. Lakini sera hiyo ilipokomeshwa mwaka wa 1994, idadi ya wahubiri ilikuwa imefikia watu 58,729. Idadi hiyo ya wahubiri imeendelea kuongezeka. Mwaka wa 2021, Afrika Kusini ilifikia kilele kipya cha wahubiri 100,112.

Ingawa Walizungukwa na Chuki, Waliunganishwa na Upendo

Ndugu mweupe akimhubiria mwanamke mweusi pamoja na mwana wake kijijini.

Wakati wa ubaguzi, Mashahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini walikuwa wakiishi katika nchi ambayo ilikuwa na sifa ya kuwalazimisha watu wawabague wengine. Katika hali hiyo, Mashahidi walifanya yote wanayoweza kusitawisha upendo na umoja kati ya watu wa rangi zote. Walifanya hivyo kwa kufundisha na kufuata kanuni za Biblia. (Matendo 10:34, 35) Ingawa walizungukwa na chuki, waliunganishwa na upendo.​—Yohana 13:34, 35.

Mwaka wa 1993, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko nchini Afrika Kusini lililokuwa na watu kutoka jamii mbalimbali. Kiongozi maarufu wa kisiasa aliwatazama Mashahidi wa Afrika Kusini wakiwasalimu kwa uchangamfu na kuwakaribisha wajumbe wa kimataifa walipowasili katika uwanja wa ndege. Kisha akasema hivi: “Kama tungekuwa na roho kama yenu, tungesuluhisha matatizo yetu kitambo.”

Milton Henschel, kutoka Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova, akizungumza katika kusanyiko kubwa la Mashahidi wa rangi tofauti, mwaka 1955

Ndugu mweupe na ndugu mweusi wakishirikiana kurekebisha gari.

Ndugu mweupe na ndugu mweusi wakifanya kazi pamoja katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Afrika Kusini, mwaka 1986

Kikundi cha Mashahidi wa rangi tofauti wakipakua chakula katika kusanyiko, mwaka 1985

Kikundi cha Mashahidi wa rangi tofauti wakipakua chakula katika kusanyiko, mwaka 1985

Umati mkubwa wa Mashahidi wa rangi tofauti wakiwa wamekusanyika pamoja katika uwanja wa FNB, Johannesburg, mwaka 2011

a Mfumo wa sera ya ubaguzi wa rangi uliwalazimisha watu wa rangi tofauti kutengana. Rangi ya mtu iliamua elimu ambayo mtu angeweza kupata, kazi ya kimwili ambayo angeweza kufanya, mahali ambapo angeweza kuishi, na mtu ambaye angeweza kufunga ndoa naye. Ili kupata habari zaidi, ona makala “Sera ya Ubaguzi wa Rangi” kwenye 2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova.

b Tangu mwaka wa 1999, michango inayotolewa na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote imewawezesha kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme mahali palipo na uhitaji.

Kusitawisha Umoja Katika Nchi Iliyogawanyika

Tunaweza kuiga mfano mzuri wa Mashahidi waliokuwa waaminifu kwa Yehova chini ya sera ya ubaguzi wa rangi. Fikiria mambo yafuatayo:

Minki.

Shinda hisia za kuona jamii moja kuwa bora kuliko nyingine. (Wakolosai 3:10, 11)

Minki anasema, “Tulilelewa katika mazingira ambayo yalituchochea kuwaona watu weupe kuwa bora kuliko wengine.” Yeye na mume wake walijifunza kweli wakiwa watu wazima. “Tulijitolea kutumikia katika eneo ambalo halikuwa na watu weupe. Nasi tulijitahidi kushinda hisia zozote za ubaguzi na tulisali kihususa kuhusu tatizo hilo.” Minki na mume wake walifaulu kushinda hisia hizo za ubaguzi na hivyo wakabarikiwa. “Kwa muda wa miaka mitatu tu, kikundi hicho kidogo kilichokuwa katika eneo la mbali kikawa kutaniko, na zaidi ya watu 100 walikuwa wakihudhuria mikutano.”

Braaf.

“Usikasirike haraka.” (Mhubiri 7:9)

Braaf anasema hivi: “Shahidi mwenzangu anaposema au kufanya jambo ambalo linaonyesha ana mtazamo wenye ubaguzi, ninakumbuka kwamba Yehova ni mwenye subira. Inachukua muda kuvaa utu mpya.” (Waefeso 4:23, 24) “Ninasali kwa Yehova ili anisaidie kuiga subira yake na kuendelea kuonyesha upendo.”

Loyiso.

Epuka habari zilizokusudiwa kuchochea watu waunge mkono upande fulani wa kisiasa. (Yohana 17:16)

Loyiso anasema hivi: “Kulikuwa na magazeti mengi ambayo yalikuwa yakipinga sera ya ubaguzi wa rangi. Kwa kuwa sikutaka kuunga mkono upande wowote, niliepuka kusoma machapisho hayo.”

Ronnie.

Kazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu. (1 Yohana 2:17)

Ronnie anasema hivi: “Kuwa katika tengenezo la Yehova kumenisaidia kuwa na kusudi maishani na pia, ninahisi ninakubalika miongoni mwa watu wa Mungu. Kushiriki kwa bidii katika utumishi na utendaji mwingine wa kiroho kulinisaidia kuepuka kukazia fikira magumu niliyokabili maishani kwa sababu ya sera hiyo ya ubaguzi wa rangi.”

Ernest.

Fuata utaratibu wa kitheokrasi badala ya maoni ya ulimwengu. (Yakobo 3:13, 17, 18)

Ernest, aliyekuwa kwenye kikundi cha “machotara” chini ya sera ya ubaguzi anasema: “Nilianza kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko nilipokuwa na umri wa miaka 26. Baadhi ya makutaniko niliyotumikia yalikuwa na wazee weupe ambao walikuwa na umri wa kutosha kuwa baba yangu! Lakini, wazee hao hawakutenda kana kwamba wanahisi wao ni bora kuliko mimi. Walikubali kwa unyenyekevu mwongozo wowote wa tengenezo na ushauri niliowapa.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki