Jinsi Ukweli Ulivyonibadili Nisiwe Mhalifu Niwe Mkristo
MIMI nilikulia katika mji mdogo mmoja katika Maine. Sikuzote nilielekea kuwa katika fujo ndogo ya namna fulani. Baba yangu aliponishika na vijikosa hivyo, nilicharazwa sana. Nyakati fulani nilikuwa mpweke, hasa baada ya baba kufa—yeye alikufa siku ile niliyotimu miaka 11 tangu kuzaliwa kwangu.
Nilipohamia mji mkubwa zaidi, nilihusika katika yaliyokuwa ni zaidi ya vijikosa tu, mambo mazito zaidi kama kuiba vitu madukani na pia kuyavunja na kuingia ndani. Nilikuwa nikivunja duka la bidhaa za chuma ili tu nione kama ningeweza. Si sikuzote nilipochukua kiasi kikubwa sana. Nilifanya hivyo kwa ajili ya msisimuko hasa. Sasa nitazamapo nyuma, nafikiri sehemu kubwa ya jambo hilo ilisababishwa na kuona televisheni kupita kiasi—nilielekea kuvutiwa na maonyesho yenye jeuri.
Visa vya uhalifu wangu vilizidi kuwa vibaya hatua kwa hatua. Kadiri nilivyoponyoka zaidi, ndivyo nilivyothubutu zaidi. Ndipo nikashikwa. Nilikuwa na miaka 15 au 16 hivi, nikiiba ndani ya duka la bidhaa za namna nyingi saa nane ya usiku—huo ukiwa sio wakati ufaao kamwe kwa jambo hilo. Kwa kuwa nilikuwa mtoto mvunja sheria, niliwekwa chini ya muda wa kujaribiwa kwa miezi sita. Sikujifunza lolote kutokana na ono hilo; wizi wangu wa kudokoadokoa uliendelea.
Nilipofikia miaka 21, haukuwa tena mdogo. Usiku mmoja kazimaisha yangu katika uhalifu ilifikia upeo kwa kuua kimakusudi. Baada ya kuiba katika duka la mchanganyiko wa bidhaa za chuma na la vyakula vya wanyama, nilipakia vitu nilivyozoa nyuma ya moja la malori yao, nikalipiga stati haraka, nikatimka. Nilipokuwa nikitoroka, nilikuwa nikiwaza nilivyofanya jambo la maana. Duka hilo lilikuwa limeibiwa mara nyingi, na mwenyewe alikuwa amelifanya likawa ngome. Hakuna mtu angeweza kamwe kujipenyeza humo tena. Lakini mimi nilipenyeza! Lo, nilikuwa bingwa kweli kweli!
Lakini si kwa muda mrefu. Lori lilikwama, kwa hiyo nikaliacha nikaenda nyumba moja kutafuta usafiri mwingine. Mwanamume mmoja katika nyumba hiyo aliniona nikinyemelea-nyemelea akatisha kuwaita polisi. Singeweza kukubali waje, kwa kuwa nilikuwa ndiyo sasa tu nimetoka kuiba katika duka lile. Nilibabaika, nikatoa bastola yangu, nikampiga risasi. Mwisho wa kabiliano hilo ukawa ni kufa na mimi kuwa mtoro.
Mitonotono ya jasho ikanitoka. Niliogopa sana. Nikafa ganzi. Kwanza niliendesha gari kwenda Augusta, nikaliacha gari hilo la kuiba, nikaanza kutembea kuvuka darajani. Niliyatazama maji kule chini. ‘Je! niruke ndani?’ nikawaza. Wazo la kujiua lilipita katika akili yangu mara kadhaa siku zilizofuata, lakini sikuweza kujipa moyo wa kufanya hivyo. Kwa hiyo nikaendelea kuwa mtoro kwa miaka miwili.
Mwishowe nilipanda basi kwenda Boston. Kufikia sasa polisi walikuwa wameacha kunitafuta, lakini nilikuwa na woga bado. Ndani ya basi, watu wenye yunifomu walikuwa wakiingia, nami ningebabaika. Kufikia wakati huu nilikuwa nimeitupilia mbali bunduki ile. Baada ya kuua mwanamume huyo, sikutaka uhusiano wowote nayo. Nilipofika Boston, nilitangatanga wakati wa mchana na usiku nikalala katika majaa au katika viwanja vya ujenzi. Muda si muda pesa kidogo nilizokuwa nazo zikamalizika kwa chakula. Niligeukia kuiba dukani mara moja mbili hivi, lakini sasa sikutaka tena mambo hayo. Ile roho ya kuthubutu mambo, ule msisimuko, kule kubiri kuiba na kuponyoka—sasa yote hayo yalikuwa yameisha.
Nilitafuta kazi, nikapata chumba cha bei rahisi, nikatumia jina la kujibandika, nami nikawa na wasiwasi kila wakati nilipoona polisi. Nilipoona mmoja akija, ningefuata njia ile nyingine. Sikuzote nilikuwa mwangalifu sana, hata sikutembea kiholela tu kwa kupitanapitana na watu, kwa kuhofu ningebambwa. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwangu, mwizi yule mwenye kutafuta msisimuko hapo kwanza, sasa akawa mtoro mwenye kulemewa na hatia.
Nilikuwa na kitabu kidogo cha mithali, na nyakati fulani nilisoma ndani yacho. Ndipo nikakumbuka kitabu cha Mithali katika Biblia. Nilipata Biblia na kuanza kusoma ndani. Sijui ni kwa nini. Sisi hatukupata kamwe kuwa jamaa ya kidini. Nilipokuwa na miaka 13, mama yangu alienda kwenye mikutano michache kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Mimi sikutaka uhusiano wowote nayo, wala yeye hakuendelea nayo.
Hata sasa, kwa kusoma kidogo katika Biblia, sikuwa nikifikiria kupata dini. Lakini nilikuwa nikichoshwa na kukimbia-kimbia, kulazimika kuangalia-angalia nyuma kwa wasiwasi, nikijiuliza kama wenye mamlaka walikuwa wakingojea kwenye kona iliyofuata ili wanikamate. Nadhani kwa kina kirefu ndani yangu nilikuwa nikitafuta kitu fulani, ingawa sikujua ni kitu gani.
Nilikuwa nikisoma mambo yaliyonifanya mdadisi. Nilitaka kuelewa. Maswali yalikuwa yakisongamana katika akili yangu, nami sikujua pa kwenda nikapate majibu. Nadhani ni kwa sababu mama yangu alikuwa ameenda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, mimi niliamua kwenda huko. Sikuwa na uhakika ningepata upokezi gani, lakini nilienda. Upokezi ulikuwa mchangamfu. Wengi walinikaribisha; Shahidi mmoja alianza funzo la Biblia pamoja nami.
Katika miezi iliyofuata, dhamiri yangu ilifufuliwa. Kadiri nilivyozidi kujifunza, ndivyo nilivyozidi kuwaza, ‘Siwezi kuendelea hivi. Ni lazima jambo fulani lifanyike. Ama niache kujifunza Biblia ama nijipeleke nikajishtaki mwenyewe.’ Muda si muda niling’amua kwamba singeweza kuacha funzo langu la Biblia, lakini chaguo jingine hilo liliogopesha. Sikulitaka. Sikutaka kwenda gerezani.
Ulikuwa ndio uamuzi mgumu zaidi niliopata kufanya wakati wowote, lakini niliufanya. Nikiwa na umri wa miaka 24, niliendea mmoja wa wazee katika kundi, Willard Stargell. Nilimwambia kwamba nilikuwa nimeua mwanamume na kwamba ningejipeleka kujishtaki mwenyewe.
“Je! una uhakika wataka kufanya hivyo?” yeye akauliza.
“Nina uhakika.”
“Mimi nitasaidia kwa njia yoyote niwezayo. Ungependa niende nawe kwenye kituo cha polisi?”
“Ningependa.”
“Basi, kuna kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova mwishojuma huu,” yeye akanikumbusha. “Tungeweza kulihudhuria, kisha twende kwenye kituo cha polisi asubuhi ya Jumatatu.”
Nilipenda wazo hilo. Nilitaka kuhudhuria kusanyiko hilo, lakini pia nilitetemekea wazo la kwenda kwenye kituo cha polisi. Nilirukia nafasi hiyo ya kuahirisha. Kwa hiyo nikaenda naye kwenye kusanyiko na kulionea shangwe. Asubuhi ya Jumatatu tulienda kwenye kituo cha polisi, nami nikajipeleka kujishtaki mwenyewe.
Polisi hawakuweza kuamini. Si watu wengi hujipeleka kujishtaki wenyewe—kwa kuua kimakusudi! Waliwapigia polisi katika Bangor, Maine, ili kuhakikisha. Siku iliyofuata Shahidi wa hapo alinizuru. Kesi ilipofanywa, Stargell alikuja Maine kuwa shahidi kwa ajili yangu. Huko nikaungama kuiba na kuua kimakusudi; kichwa kikuu chenye kutangaza uamuzi kilinena juu yangu kuwa “Mwenye Utulivu Hakimu Amhukumupo Kifungo cha Maisha.” Mwezi mmoja baadaye nilikuwa katika gereza la serikali la Maine, nikitumikia miaka 15 hadi maisha. Huko Mashahidi walikuja pia kunizuru.
Upokezi niliopewa na wafungwa ulitofautiana. Wao walinidhihaki kwa ‘kuwa mpumbavu vya kutosha kujipeleka nikajishtaki mwenyewe,’ hasa kwa kuwa polisi walikuwa wameacha kunitafuta. Walipojua kwamba nilifanya hivyo kwa sababu ya kujifunza Biblia, walichekacheka, wakiniita ‘kondoo miongoni mwa majibwa-mwitu.’ Mabaya waliyonitenda yalikuwa ya maneno sikuzote, si ya kimwili kamwe. Sana-sana, nilikaa kwa kujitenga na wafungwa.
Ukweli ukawa kingasalama kwangu. Baada ya muda wakang’amua kwamba ‘jamaa huyu ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Yeye ni asiyekuwamo. Hatahusika na wowote wa mizozano hii ya kindani.’ Pia, walijua ya kutosha wasije kuniuzia dawa za kulevya wala kuniomba niibe kitu kwa ajili yao. Pia maofisa wa usimamizi waling’amua kwamba singezivunja sheria. Hiyo iliweka rekodi yangu bila waa na kuniruhusu niwe na uhuru zaidi.
Wakati mmoja katika kipindi hiki, nilivutwa fikira kando zikatoka kwenye ufuatiaji wangu wa ukweli wa Biblia. Si kwamba niliamua kimakusudi nisiendelee nao. Ilikuwa kwa kushindwa kutii Waebrania 2:1, ambapo twaonywa ‘tusipeperuke kamwe.’ (NW) Hata hivyo, mimi nilifanya hivyo. Hata katika gereza, ufuatiaji wa vitu vya kimwili waweza kukutia mtegoni! Fursa moja ilifunguka ambapo ningeweza kufanyiza bidhaa za unamnanamna ili ziwekwe katika chumba cha wonyesho gerezani. Wenye kuzuru wangenunua bidhaa hizi, na sehemu kubwa ya pesa iliendea wanagereza waliokuwa wamezifanyiza. Kwa hiyo nikahusika katika kutafuta pesa, na funzo langu la kibinafsi likahasirika.
Ndipo nikaanza kujiwazia hivi: ‘Kwa nini ulijipeleka kujishtaki mwenyewe? Kwa nini ukarudi na kwenda gerezani? Na sasa wewe unaacha mafunzo yako ya Biblia? Hilo si jambo la akili! Ingalikuwa vema kama usingalijitokeza.’ Sehemu ya tatizo langu ilikuwa kwamba nilitatizika kuamini kwamba Yehova alikuwa amenisamehe kikweli kwa kuua mwanamume. Mmoja wa walinzi alikuwa Shahidi, naye akaona kwamba nilishuka moyo juu ya jambo hilo. Kwa hiyo akanisimulia baadhi ya mambo aliyokuwa amefanya alipokuwa akitumikia katika Vietnam kabla ya kuwa Shahidi.
“Jambo gani likufanye wewe uwe maalumu mno?” akauliza. “Ebu tazama maisha yote ya raia ambayo mimi nachukua lawama yake. Wakati kikosi chetu kiliposhambulia vijiji vya Vietnam, tulifyeka madazani ya watu, wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto wasio na hatia. Je! wewe wafikiri hayo hayanisumbui mimi sasa? Siwezi kuyasahau! Hata hivyo nahisi kwamba Yehova, Mungu wa rehema isiyo na kikomo, amenisamehe. Ulilofanya halikukaribia kuwa baya kama nililofanya mimi. Wewe uliua mwanamume mmoja; mimi hata siwezi kujua ni wangapi niliua!”
Hilo ndilo nilihitaji. Lilinifanya nifikirie rehema na msamaha wa Yehova kwa wale wenye kutubu kikweli. Kwa hiyo hatimaye niliacha shughuli zangu za ufuatiaji wa vitu vya kimwili nikarudia ratiba yangu ya funzo la Biblia. Na imekuwa hivyo tangu wakati huo.
Hatimaye, funzo la Biblia la kila juma liliongozwa pamoja nami, na mara moja kwa mwezi nikaruhusiwa kwenda nje pamoja na Mashahidi kwa ajili ya makusanyiko ya nje. Wakati mmoja, wanagereza wengine kadhaa na mimi tulikuwa tukijifunza Biblia. Tuliaminiwa zaidi na kuruhusiwa mapendeleo zaidi. Maofisa walijua kwamba hawakulazimika kufuliza kutulinda kwa ukaribu. Wakati mmoja tuliruhusiwa kwenda seli kwa seli tukitoa trakti, pamoja na mialiko kwenye wonyesho wa slaidi wa Mashahidi wa Yehova. Zaidi ya 20 walihudhuria.
Nimesaidiwa kufuliza kusonga mbele na Yehova, chakula cha kiroho kupitia tengenezo lake, na msaada wenye upendo wa ndugu wenye imani. Nikiwa gerezani nilipokea kadi na barua nyingi zenye kunitia moyo kutoka kwa Mashahidi, na hiki kilikuwa kiamsha-nishati cha kiroho ambacho kilichangamsha roho yangu. Yote haya yakaongoza kwenye ubatizo wangu kwa kuzamishwa katika maji katika 1983 ili nifananishe wakfu wangu kufanya mapenzi ya Yehova—baada ya miaka saba katika gereza la serikali la Maine la ulinzi kamili kabisa.
Miaka miwili baadaye, baada ya miaka tisa katika ulinzi kamili kabisa, nilihamishwa nikapelekwa gereza la karibu la ulinzi kidogo. Mwaka mmoja na nusu baadaye, nilihamishwa nikapelekwa mahali pa kutuma wafanya kazi katika Bangor. Huko wanagereza hupelekwa nje kwenye miradi ya kazi, nao hurudi mahali hapo mwishoni mwa siku. Miezi sita baadaye nilikuja kwa ajili ya kusikizwa kwa ombi langu la kwanza la msamaha. Hakuna yeyote wa walinzi au wafungwa aliyefikiri ningefaulu. “Hakuna mtu ambaye hufaulu mara ya kwanza,” wakasema. “Hakuna!”
Lakini mimi nilifaulu. Ni kweli, ni wachache sana waliofaulu mara ya kwanza. Mfungwa wa kawaida husema uwongo na kujaribu kuhadaa baraza la kutoa msamaha, lakini wao wamepata kusikia yote hayo hapo zamani. Wao huona wanapohadaliwa. Mimi nilienda tu mbele yao nikasema, ‘Hivi ndivyo nilivyo, hivi ndivyo nimefanya, hivi ndivyo nimebadilika, na hivi ndivyo napanga kufanya.’ Nikawaambia juu ya kujifunza kwangu Biblia, juu ya mabadiliko ambayo kulifanyiza ndani yangu, na juu ya kuwa kwangu mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wangeweza kuona mabadiliko hayo.
Nadhani uhakika wa kwamba nililazimika kujipeleka nikajishtaki mimi mwenyewe, kwamba rekodi ya mwenendo na kazi yangu ilikuwa nzuri, na kwamba kanuni za Biblia nilizokuwa nimejifunza zilionekana katika mwelekeo na mwenendo wangu—yote hayo yalinena kwa ajili yangu. Kuongezea hilo nilisali kwa Yehova na kumwegemea. Mimi hupenda kufikiri kwamba huenda yeye akawa alikuwa na uhusiano fulani na jambo hili, nami natumaini kwamba sijitangulizi kwa kufikiri hivyo. Vyovyote vile, baraza liliruhusu ombi langu la msamaha. Katika Februari 1987, baada ya miaka 12 katika gereza, nikawa huru kwenda.
Siku ya Aprili 30, 1988, nilioa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Yeye ana watoto watatu wa ndoa ya wakati uliotangulia. Tukiwa jamaa, sisi huwa na funzo letu la Biblia la kila juma. Sisi huhudhuria mikutano yote kwenye Jumba la Ufalme. Sisi huhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu nyumba kwa nyumba. Sisi hufanya ziara za kurudia wote wenye kupendezwa, nasi huongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia na wale wenye kutamani hivyo. Baada ya miaka kadhaa ya mahubiri yenye mipaka gerezani na kuwa ni kama hakuna kabisa uhudhuriaji wowote wa mikutano, ni vizuri ajabu kushiriki “kwa uhuru wa uneni ulio mkubwa zaidi” katika utendaji wa Kikristo wa Mashahidi wa Yehova!—Matendo 28:31, NW.
Yote haya yaliwezekana kwa sababu maarifa sahihi ya Neno la Mungu yaliniwezesha nivulie mbali utu wangu wa kale wa uhalifu na kuvaa wa Kikristo ulio mpya wenye kufuatishwa kigezo cha mfano na ufanano wa Yehova Mungu.—Wakolosai 3:9, 10.
Kwa uhakika, katika kisa changu ‘neno la Mungu lilikuwa kali na lenye nguvu’ kunitenganisha na wakati wangu uliopita na kutengeneza tabia zangu niwe mshiriki mfuata-sheria katika jamii ya watu na mhubiri wa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Waebrania 4:12) Sifa yote iwe kwa Yehova, “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3, NW.—Jina halikutajwa kufuatia ombi hilo.
[Blabu katika ukurasa wa 21]
Usiku mmoja kazimaisha yangu katika uhalifu ilifikia upeo kwa kuua kimakusudi
[Blabu katika ukurasa wa 22]
Ama niache kujifunza Biblia ama nijipeleke kujishtaki mwenyewe
[Blabu katika ukurasa wa 23]
Polisi hawakuweza kuamini. Si watu wengi hujipeleka kujishtaki wenyewe—kwa kuua kimakusudi!
[Blabu katika ukurasa wa 24]
Tuliruhusiwa kwenda seli kwa seli tukitoa trakti