Shetani Kavaa Kificha-Sura
LEO, Shetani anaelekezewa uangalifu ulimwenguni pote. Habari nyingi sana zimeandikwa katika karatasi-habari, magazeti, na trakti za kidini juu yake. Programu za redio na televisheni zimetumiwa kwa dini yenye jina lake.
Neno “Shetani,” likiwa limeandikwa kwa herufi za kwenda mbele na za kurudi nyuma, laweza kuonwa juu ya benchi (vikalio) za utumizi wa watu wote, likiwa limechorwa juu ya madaraja na kuta za majengo yaliyoachwa na mbele ya maduka, na kupakwa kwa chokaa juu ya madirisha ya kioo. Kumekuwa na ongezeko kubwa ajabu la watu, hasa vijana, wenye kushawishwa halafu kunaswa waingie katika dini iliyo na jina Shetani.
Hata hivyo, ijapokuwa habari za Shetani zimetangazwa kotekote, kuna maoni tofauti-tofauti yeye ni nani hasa. Kwa watu wengi, kutia na wafuasi wake wenye kujitoa sana, Shetani hajulikani vizuri alivyo. “Kuna maoni ya kila namna,” asema profesa mmoja wa dini, “kuanzia ncha moja ya watu waaminio katika mtu halisi aliye Shetani hadi ncha nyingine ya wale waaminio kwamba huo ni usemi wa kitamathali na kulipuuza kabisa wazo hilo.”
Profesa mwingine wa dini kwenye seminari ya kitheolojia ya Baptisti alipompa Shetani sifa ya kuwa ‘mtumishi wa Mungu,’ badala ya kuwa ndiye adui mkuu Wake, hiyo ilifyatusha kasirani kali ya kidini. Simu nyingi na barua kwa kampuni ya uchapishaji ya kanisa ziliteta juu ya fasiri hiyo. Mhudumu mmoja Mbaptisti asiyekubali maoni mapya alisema, “Ikiwa Shetani akubaliwa kuwa mtumishi wa Mungu, basi hiyo yamfanya Mungu awe hasimu wetu.” Hata hivyo, mhudumu mwingine Mbaptisti aliye profesa wa dini alipinga hilo kwa maoni ya kwamba washiriki wa baraza la Kibaptisti “hawajapiga kura waone ni nini msimamo rasmi wa Wabaptisti” kuhusu Shetani.
Kwa kweli, washiriki wa makanisa mengi hawajui vile dini yao hufundisha juu ya Shetani. Mwandikaji mmoja wa karatasi-habari alionelea hivi: “Ni makanisa machache yenye fundisho linalotaarifu mambo ambayo washiriki wao wapaswa kuamini juu ya Shetani, kwa hiyo habari hiyo huwa ya kibinafsi kabisa.” Baadhi yayo hata hufundisha kwamba Ibilisi huwakilisha uovu tu ulio ndani yetu. Kwa kielelezo, mhudumu Mpresbiteri A. D. Ellison adai kwamba Yesu alishawishwa jangwani, si na mhai fulani wa kishetani aliye na nguvu zisizo za kiasili, bali na ubinafsi wake mwenyewe.
Si ajabu kwamba washiriki wa kanisa wamo katika shaka juu ya utambulisho wa Shetani, kwa kuwa viongozi wao wa kidini wamo katika shaka pia.
Kile Alicho
Hata hivyo, Maandiko huonyesha wazi sana na kutia mkazo kuhusu kile alicho Shetani. Mungu Mweza Yote aliumba viumbe-roho wengi walio na idhini ya kumfikia yeye katika mbingu na walio watumishi wake. Biblia hufunua kwamba Mungu ‘alipoiweka misingi ya dunia,’ akiiumba ili ikaliwe na wanadamu wakati ujao, “wana wote wa Mungu [viumbe-roho wa kimalaika] walianza kupaaza sauti kwa kupiga makofi.” (Ayubu 38:4, 7, NW) Baada ya muda, mmoja wa malaika hawa aligeuka dhidi ya Muumba wake, akiwa mwasi, mpinzani.
Mpinzani huyu wa awali, au Shetani (linalomaanisha “Mkinzani”), ndiye aliyetumia nyoka kuwa msemaji wakati aliponena na Hawa ili kumvuta asitii Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Ndiyo yeye huitwa pia “nyoka wa zamani.” (Ufunuo 12:9) Yesu mwenyewe alisema hivi juu ya Shetani: “Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake.” (Yohana 8:44; 1 Yohana 3:8) Hivyo Yesu alimtambulisha Shetani kuwa yeye ambaye wakati mmoja aliona shangwe ya upendeleo wa Mungu lakini akaasi dhidi ya Yehova Mungu.
Ingawa watu fulani husema kwamba Ibilisi humaanisha tu kanuni isiyogusika ya uovu, sifa na vitendo ambavyo huhesabiwa Shetani katika Biblia vyaweza kuhesabiwa kwa mtu peke yake. Kwa kweli, Biblia huonyesha kwamba Shetani ni mtu-roho wa halisi asiyeonekana ambaye ameapa kugeuza ainabinadamu wasimtumikie Muumba, Yehova Mungu. Shetani alipomshawishi Yesu jangwani, Yesu asingaliweza kuwa alishawishwa na sifa tu ya uovu wala na ‘ubinafsi wake mwenyewe.’ Kwa maana uovu, au ubinafsi, usingeweza kukaa ndani ya Yesu, kwa kuwa Biblia huonyesha wazi kwamba Yesu alikuwa “asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji.”—Waebrania 7:26; Luka 4:1-13.
Utafutaji wa Mamlaka
Shetani aliasi dhidi ya Mungu katika utafutaji wa mamlaka, akiwa na tamaa ya kutawala wengine, kuwa mungu wao, kuabudiwa. (2 Wakorintho 4:4) Alitolea Adamu na Hawa mamlaka na uhuru—‘kuwa kama Mungu’ katika kufanya maamuzi yao wenyewe juu ya mema na mabaya, yafaayo na yasiyofaa. (Mwanzo 3:5) Mamlaka na uhuru yangali ndiyo mambo ambayo Shetani hutolea waabudu wake.
Hivyo, mwabudu wa Shetani aliye tineja jina lake Sean, aliyekuwa ndiyo sasa tu ameua wazazi wake na mhanga wa tatu, aliandika hivi: “Mimi niko huru. Naweza kuua bila masikitiko.” Wakati mwingine aliandika hivi kwa damu yake mwenyewe: “Mimi namkana Mungu, namkana Kristo, nitatumikia Shetani peke yake . . . Shetani juu.”
Randy Shores, tineja na mshiriki wa hapo zamani wa kiibada cha kishetani alieleza hivi: “Wakati huo lilikuwa jambo bora, mtu kuhisi ana mamlaka yote.” Shores alikazia kwamba ‘mamlaka ilikuwa ndicho chambo [uvutio wenye kunasa], mamlaka itokayo kwa kikundi kukulinda, kutoka kwenye zile desturi za ibada na maneno ya kunuizwa yasemwayo ili kudhuru mtu mwingine, na kutoka kwenye ule usiri.’
Ndiyo, kuna imani miongoni mwa wengi wa waabudu wa Shetani kwamba atawaandalia mamlaka wale wafuatao mafundisho yake. Na uelewevu wa baadhi ya waabudu wa kishetani ni kwamba hiyo humaanisha mamlaka ya kuua bila kupatilizwa kisasi. Visa vya kuua vyenye kutangazwa na waabudu wa Shetani hufunua kwamba kweli wao huamini ya kuwa kwa kuua wanaweza kujipendekeza kwa Ibilisi. Kwa hiyo kuna uhitaji wa kuuchukua kwa uzito ule usumbufu wenye kuongezeka wa ibada ya kishetani.
Usidanganywe
Kumbuka, Shetani ni halisi. Yeye si uwazio wa mtu fulani. Upendezi wake mkubwa kabisa ni kuondolea Mungu na Neno Lake, Biblia, sifa na kunasa wengi awezavyo katika tandabui lake la uharibifu. Lakini tayari Mungu ameanzisha kitendo dhidi ya Shetani, akitoa mamlaka ya kumwondoa kwenye mbingu awe kwenye mipaka ya dunia. Bila shaka kuzuiliwa kwa Shetani katika mipaka ya dunia kumekuwa kisababishi kimoja cha kuhuishwa kwa Ushetani hivi majuzi.—Ufunuo 12:7-12.
Wazazi wanahitaji kuwa wasikivu. Katika visa vingi ambapo watoto wamekubali kwa moyo kuufuata Ushetani, hiyo ilikuwa kwa sababu wazazi wao hawakuwapa upendo na uangalifu waliouhitaji. Watoto waliona uchungu juu ya hali hiyo iliyoonekana kuwa ya kuachiliwa mbali nao wakawa windo rahisi kwa wenye kutafuta washiriki wapya wa ushetani.
Hata hivyo, la kufurahisha ni kwamba mwisho wa Shetani na uvutano wake uko karibu. Karibuni yeye na wafuasi wake watapata ushinde na uharibifu kamili. Mungu mkubwa, Yehova, ambaye Shetani na roho waovu wake wamemkaidi kwa majisifu, atatumia Shujaa-Mfalme wake, Yesu Kristo, kuwaondolea mbali watu waovu hawa. (1 Yohana 3:8; Ufunuo 20:1-3, 10) Kwa sasa, wewe na uwe miongoni mwa wale wenye kumkinza Shetani na kupata ulinzi katika udugu wenye upendo wa waabudu waliopangwa kitengenezo wa Mungu wa kweli, Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 17]
Chanzo cha Ulinzi wa Kweli
Katika barua moja kwa The Times Herald Record la Middletown, New York, mwanamume mmoja alieleza jinsi alivyokuja kuhusika katika nguvu za mafumbo ya kiroho. Alikuwa ameshawishwa na miandiko ya watabibu wawili wa kisaikolojia waliokuwa wamekusanya jawabu la kupata nguvu hizo. Mwanamume huyo alieleza kwamba, “Mimi nilifuata jawabu hilo kwa hamu nyingi lakini nikapata hasara ya kuwa na hofu nyingi kila usiku kwa muda wa majuma sita.
“Kwa nasibu,” yeye aendelea kusema, “wawili [wa] Mashahidi wa Yehova walinishauri, miongoni mwa mambo mengine, nisali kwa Yehova nami nikafanya hivyo kila usiku nilipoanza kupatwa na hisia za kiajabu-ajabu.” Matokeo yalikuwa nini?
Yeye alisema kwamba, “usiku wa mwisho wa kuwa na hofu nyingi chochote kile kilichokuwa kikinipagaa kiliacha kunishika . . . Baada ya hapo, sijapatwa na mabaya yoyote tena.” Mtu huyu alijifunza, kama alivyoandikia karatasi-habari hiyo, kwamba “Mungu hulaani vikali wenye kushiriki katika mazoea ya mafumbo ya kiroho (Kumbukumbu 18:10-13).”—Februari 27, 1988.
Andiko hilo (katika NW) husema hivi kwa sehemu: “Hapaswi kupatikana ndani yako . . . yeyote ambaye hutumia uaguzi, mzoea mizungu au yeyote ambaye hutafuta ishara au mlozi, au mmoja ambaye hutafuta shauri kwa chombo cha kuwasiliana na ulimwengu wa roho au mtabiri kikazi wa matukio au yeyote ambaye huulizia habari za wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo haya ni kitu chenye kukirihika kwa Yehova.”
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
Wazazi, Iweni Macho Kuziona Ishara
Kwa sababu ibada ya Ibilisi huvutia vijana, wazazi wapaswa kuwa macho kuziona ishara za kwamba huenda watoto wao wakawa wanahusika. Mwenye mamlaka moja juu ya viibada vya kishetani, Evon Peterson, alishauri hivi:
“Wao (vijana) huhitaji mtu fulani wa kuwaamini. . . . Wanataka sana kuwe na mtu fulani wa kuwapa uangalifu . . . kuwasikiliza. Viibada hivyo ni stadi sana kwa kusikiliza. Ikiwa wazazi hawapatikani, wenye viibada hivyo wapatikana.”
Angelo Pierri, mshauri katika New Jersey, aonya hivi: “Mimi najua kwamba labda wewe unasema, ‘huo ni mtindo unaopita tu,’ lakini hivyo ndivyo waabudu wa Shetani wangetaka wewe ufikiri. Hawataki kufichuliwa. Hawataki nuru iangazwe juu ya utendaji wao mbalimbali.”
Hasa ni muhimu kuangalia muziki ambao vijana husikiliza. Mwingi wa muziki wa leo wa roki yenye fujo-fujo umekolezwa jumbe na maneno ya ufananisho wa kishetani. “Umepotoshwa kabisa kabisa,” asema Peterson, “ukiwa na jumbe za kuua na kuumiza. Hujaza mahitaji ya mtoto ili atende kwa jeuri.”
Mwaka wa juzi kijana mmoja wa New Jersey mwenye umri wa miaka 14 aliua mama yake kwa kumdunga kisu halafu akajiua mwenyewe. Vibandiko vya wanamuziki wenye roki yenye fujo-fujo vilifunika kuta za chumba chake. Baba ya mvulana huyo alisihi hivi baadaye: “Ambieni wazazi wawe macho juu ya muziki ambao watoto wao husikiliza.” Alisema kwamba juma zima kabla ya visa hivyo vya kuua, mwana wake alikuwa ameimba wimbo wa roki “juu ya damu na kuua mama yako.”
Kwa kweli, Ushetani ni usumbufu hatari unaoongezeka. Hatua ya kwanza katika kupambana nao ni kuwa na habari. Halafu ukabili. Ndiyo, Biblia ni sahihi isemapo kwamba sisi tuna pigano “dhidi ya majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12, NW) Shetani na roho waovu wake wako kikweli, na ndio walio nyuma ya mazoea yote haya ya kiibilisi.