Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 4/1 kur. 13-17
  • Jihadhari na Adui Yako, Ibilisi!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na Adui Yako, Ibilisi!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Shabaha na Makusudi ya Shetani
  • Udanganyifu Juu ya Kuwako Kwake
  • Hila ya Shetani ya Dini ya Uongo
  • Shetani Anatumia Kiburi cha Mtu
  • Shetani Anatumia Udhaifu wa Kibinadamu
  • Simama Imara!
  • Uwe Macho​—Shetani Anataka Kukumeza!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Adui wa Uzima wa Milele
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Shetani Ni Nani? Ni Kiumbe Halisi?
    Amkeni!—2007
  • Simama Imara Dhidi ya Hila za Shetani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 4/1 kur. 13-17

Jihadhari na Adui Yako, Ibilisi!

“Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”— 1 PETRO 5:8.

WEWE ni shahidi aliyejiweka wakfu bila masharti kwa Yehova Mungu? Ikiwa ndivyo, una adui mwenye hila, hasimu mwovu sana. Lakini, ajapokuwa anaweza kufanya mengi, mipango ya adui mjanja huyo inaweza kushindwa. Unaweza kuwa mwaminifu kwa Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova. Pasipo shaka, unaweza kushiriki kwa njia hiyo katika kuliondolea lawama jina lisilolinganika na jingine la Baba yako wa kimbingu. Kwa kweli, unaweza kufurahisha moyo wa Yehova na kumpa jibu la kumtolea yule Mdhihaki Mkuu. Ndiyo, na unaweza kupata zawadi ya uzima wa milele katika furaha ya kiparadiso.—Mithali 27:11; Luka 23:43; Ufunuo 2:7.

Ili ubaki mwaminifu kwa Mungu, ni lazima ujihadhari na adui yako mkuu. Juu yake, mtume Petro aliandika: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.” Lakini, mtu anaweza kujikinga na adui huyo, kwa maana mtume anaendelea kusema: “Mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika Imani . . . Mungu wa neema yote . . . mkiisha kuteswa kwa muda kidogo . . . atawatengeneza, na kuwathibitisha.” (1 Petro 5:8-10) Hasa maneno hayo yanawaletea faraja wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu Kristo. Hata hivyo, yana maana ya kweli kwa watumishi wa Yehova wanaotazamia kuishi milele katika paradiso ya kidunia.

Ili tujihadhari na Adui yetu, tunahitaji msaada, na pia maarifa ya kujua mbinu anazotumia. Wenye utayari na nia ya kutusaidia sote tudumishe ukamilifu ni Yehova Mungu, Yesu Kristo, malaika watakatifu na kundi la Kikristo. Kwa upande mwingine, tunapaswa kushindana na mwili wetu wenyewe usiokamilika, mfumo mbovu huu wa mambo na Shetani Ibilisi mwenyewe. Yeye anasukumwa na ukorofi na nyakati zote anakuwa tayari kutumia hao maadui wengine wetu wawili ili atimize makusudi yake mabovu.—Yohana 15:19; 1 Wakorintho 9:27.

Mitajo yenyewe ambayo Maandiko yanamwita Adui yetu yanatusaidia kufahamu njia zake, hila zake, kwa njia nzuri zaidi. Yeye anatajwa kuwa Shetani, Ibilisi, nyoka na joka. (Ufunuo 12:4, 9, 10) Jina lake Shetani linamaanisha “Mpingaji,” au “Adui.” (Ayubu 1:6; 2:1) “Ibilisi” maana yake ni “Mchongezi,” “Mshitaki,” au “Msingiziaji.” Shetani anaitwa “nyoka” pia kwa sababu alitumia nyoka kudanganya Hawa katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 3:1-7) Na anaitwa “joka” kwa sababu ya maelekeo yake ya kumeza.

Shabaha na Makusudi ya Shetani

Shetani Ibilisi, ambaye hapo mwanzo alikuwa mmoja wa wana wa kimbingu wa Mungu, aliangukia kupinga na kuchongea Yehova. Kusudi la Shetani lilikuwa kuondoa wanadamu kwa Mungu, ili watumikie makusudi ya kichoyo ya Shetani. Mwendo wa Ibilisi unaonyesha wazi kwamba alitia shaka juu ya kama Mungu ni msema kweli, na pia juu ya kama wanadamu wanahitaji kutegemea Yehova na kumtumaini ili waendelee kuwa na uhai na furaha. Mwendo wa Shetani ulielekea kuonyesha anatia shaka juu ya haki ya Mungu kutawala na njia yake ya kutawala. Yehova anajali sana kanuni ya kutawala kwa uadilifu na kutumikiwa na viumbe kwa nia inayoongozwa na kumpenda yeye na uadilifu. Kwa upande mwingine, Shetani ameshikilia maoni ya kwamba kupata faida ya kichoyo ndiyo shabaha ya kupendeza zaidi. Ndiyo kusema, anakazania kwamba viumbe wote wenye akili wanapaswa kuwa wachoyo kama yeye na ndivyo walivyo hata sasa.—Ayubu, sura 1 na 2.

Ili Shetani aanze kufuata mwendo wa namna hiyo, inaonyesha wazi aliacha nia isiyo na kiasi iwe tamaa kali sana na shabaha kubwa ya kujitakia makuu. Hilo linaonekana wazi kutokana na onyo la mtume Paulo linalopinga kuweka mwanamume aliyegeuzwa hivi karibuni kwenye cheo cha mwangalizi, “asije akajivuna akaanguka katika hukumu ya Ibilisi.” (1 Timotheo 3:6) Ulikuwa wonyesho wa majivuno makubwa sana Shetani kuthubutu kujilinganisha na Mwenye Nguvu Zote, yule Aliye Juu Zaidi, Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Mzima, Mfalme wa umilele, Yehova Mungu. (Mwanzo 17:1; 2 Samweli 7:28; Zaburi 83:18; 1 Timotheo 1: 17) Ibilisi alipomtolea Yesu Kristo “milki zote za ulimwengu” kama Yesu angekubali kumfanyia tendo moja la ibada, hiyo ilionyesha tamaa inayomtawala ni kujitukuza, kwamba aliona kijicho juu ya ibada ambayo viumbe wenye akili walikuwa wakimpa Yehova Mungu.—Mathayo 4:8, 9.

Bila shaka, Yehova Mungu angaliweza kuua Shetani na wale wanadamu wawili wa kwanza mara tu walipofanya kosa. Lakini kwa sababu ya masuala ambayo Shetani alikuwa ametokeza, na kwa kurehemu watoto wa Adamu wasiozaliwa bado, Mungu aliruhusu Ibilisi aishi kisha ajaribu kuthibitisha madai yake yenye majisifu yalikuwa ya kweli. Wakati ule ule, Yehova kwa njia hiyo aliwapa nafasi wale kati ya wanadamu walioitaka ili wajaribu kujitawala wenyewe bila kutegemea Mungu na kanuni zake za uadilifu.

Udanganyifu Juu ya Kuwako Kwake

Shetani anatumia njia nyingi za namna mbalimbali kuendeleza kusudi lake akiwa Adui ya Yehova Mungu na, ikiwezekana, aondoe wanadamu wote kwenye ibada inayompasa Muumba wao. Moja ya njia hizo ni kufanya watu waamini kwamba yeye hata hayuko! Jambo hilo linawezesha wanaswe naye vyepesi. Hivyo, leo, katika vikundi vingi vya kidini ni kawaida ya watu kuamini kwamba hakuna mtu kama Shetani Ibilisi. Kwa mfano, uchunguzi wa maoni ya watu uliofanywa na Makao ya Kuchunguza Miongozo katika Mji wa New York ulionyesha kwamba mwaka wa 1974 zaidi ya nusu ya Waamerika hawakuamini kwa ukamili kwamba kuna Ibilisi mwenye utu. Hata viongozi wa kidini wengi hawaamini Ibilisi ni mtu aliyeko.

Lakini Maandiko hayatuachii shaka lo lote juu ya kuwako kwa Ibilisi mwenye utu. Yanaonyesha kwamba mtu fulani alinena kupitia nyoka, akadanganya na kushawishi mwanamke wa kwanza, Hawa. Kitabu cha Ayubu kinathibitisha zaidi kwamba Shetani ni mtu aliyeko, kwa maana kinamtaja akinena na Yehova Mungu, akikana ukamilifu wa Ayubu mtumishi wa Mungu. Zaidi ya hilo, waandikaji wa masimulizi ya Injili Mathayo, Marko na Luka wanaandika kwamba Yesu Kristo alijaribiwa na Ibilisi. Kwamba majaribu ya namna hiyo yalimpata Yesu kwa kuletwa na chanzo cha nje inaonekana wazi kutokana na hali ya jaribu la tatu la Shetani, si kutokana na yale tu tunayojua juu ya ukamilifu wa Yesu na utu wake. Yesu angewezaje kusujudu na kufanya tendo la ibada mbele ya kanuni au wazo la uovu? Linalostahili kuangaliwa, pia, ni vile Yesu alivyorudia kumtaja-taja Shetani kuwa mtu na kuwa “mkuu wa ulimwengu huu.”—Yohana 12:31; 14:30; 16:11; 8:44; Mathayo 4: 1-10; 12:26; Luka 10:18.

Mitume wa Yesu pia walimtambulisha Ibilisi kuwa mtu. Paulo alionyesha kwamba Wakristo wa kweli hawakosi kuzijua “njia za werevu” anazotumia Shetani kisha mtume huyo akawaonya wajihadhari na “hila za Ibilisi.” (2 Wakorintho 2:11; Waefeso 6:11, NW ) Kama ilivyokwisha kuonwa, Petro alihimiza waamini wenzake wajihadhari na Adui yao, Ibilisi. Na mtume Yohana alishuhudia kwamba “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu” na “Ibilisi atawatupa baadhi [ya Wakristo] gerezani.” — 1 Yohana 5:19, NW; Ufunuo 2:10; 1 Petro 5:8.

Hila ya Shetani ya Dini ya Uongo

Njia ya werevu anayotumia Shetani kuweka watu katika upofu inahusu matumizi ya dini ya uongo. (2 Wakorintho 4:4) Mtu aliumbwa na Mungu akiwa na uhitaji wa kupashana habari na Muumba wake kupitia ibada. Shetani amepotosha tabia hiyo iliyo asili ya watu kwa kuwafanya wavutwe na choyo na kuwaweka katika hali ya kutokujua ibada safi. Ili kutimiza kusudi lake anaendelea ‘kujigeuza awe malaika wa nuru.’ (2 Wakorintho 11:14) Kwa sababu ya udanganyifu huo, wanadamu wanajitia katika maelfu ya namna zinazotofautiana za dini ya uongo.

Kwa kweli dini ya uongo yote imetokezwa na Shetani, kwa maana Paulo alisema: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu.” Yesu alisema: “Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya.” Tena, Kristo hakuyapa nafasi mambo ya kuchanganya pamoja imani mbalimbali, bali alisema: “Mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”—1 Wakorintho 10: 20; Mathayo 12:30; Yohana 14:6.

Shetani anatumia vibaya hamu ya mtu kutaka kujua mafumbo ya mambo yasiyoonekana na hali ya wafu. Kwa kutumia hila zinazopingana kabisa na Maandiko kama kusema na wafu, au kupashana habari na ulimwengu wa roho, kutabiria watu matukio yatakayowapata, kufanya unajimu na uchawi, amenasa watu wasiohesabika. Kwa kweli, leo watu wanaendelea kupendezwa nyakati zote na mambo kama hayo. Hilo limefikia hatua ya kupita kiasi hivi kwamba wengine wanamwabudu Ibilisi mwenyewe. —Kutoka 22:18; Mambo ya Walawi 19:26; 20:6; Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Shetani Anatumia Kiburi cha Mtu

Shetani alijiacha ashindwe na jaribu la kiburi. Kwa hiyo, aliamsha katika Hawa tamaa yenye kiburi na choyo ya kuwa kama Mungu Aliye Juu Zaidi, na hivyo akafaulu kugeuza wazazi wetu wa kwanza waache ibada ya Yehova Mungu. Bila shaka Shetani alitumia njia kama hiyo kwa habari ya Kaini. Alipoona Kaini akiwa na uchungu mwingi kwa sababu Habili ndugu yake alipokea ukubali wa kimungu, Ibilisi aliweza kuupepea uchungu huo ukawa kijicho chenye uuaji.—Mwanzo 4:3-8; 1 Yohana 3:11, 12.

Muda wote wa historia ya wanadamu, Shetani ameweza kuwatumia kama vyombo vyake watu walio na kiburi—watu kama Nimrodi, Farao wa Misri katika siku za Musa na Senakeribu Mfalme Mwashuri. (Mwanzo 10:8-12; Kutoka 5:2; Isaya 36:7-10, 16-20) Leo Shetani anashikilia halaiki ya watu katika uongozi wake kupitia kiburi: kiburi juu ya kabila, kiburi juu ya taifa, kiburi juu ya elimu, kiburi juu ya cheo cha mtu maishani, na mambo kama hayo. Yote hayo yanatimiza kusudi la Ibilisi kwa kufanya watu wazibe masikio wasiusikie ujumbe wa Mungu.

Chambo cha Pupa ya Vitu vya Kimwili

Hila nyingine anayotumia Shetani kunasa wanadamu ni utafutaji wa vitu vya kimwili, pupa, kupenda fedha, kiburi cha kujivunia mali. Kwa njia hiyo alinasa viongozi wa kidini wa siku za Yesu waliokuwa wapenda fedha wenye pupa. (Luka 16:14) Kwa kutumia chambo cha pupa ya utafutaji wa vitu vya kimwili, ‘Shetani alijaza moyo wa Anania kuiambia uongo roho takatifu.’ (Matendo 5:1-11) Na bila shaka Ibilisi alitumia upendo wa vitu vya kimwili na anasa za kilimwengu kupotoa Dema na Wakristo wengine watoke kwenye utumishi wa Yehova.—2 Timotheo 4:10.

Mfano unaoonyesha hasa namna Shetani alivyotumia pupa kwa njia mbaya sana kunasa mtu ni ule wa Yuda Iskariote. Si kwamba tu alikuja kuwa mwivi mwenye pupa, bali pia pupa ilihusika kumfanya Yuda asaliti Bwana wake. Kwamba akili yake ilielekea upande huo inaonyeshwa na kuteta kwake wakati Mariamu alipopaka miguu ya Yesu mafuta ya bei kubwa. (Yohana 12:4-6; Mathayo 26:14-16) Lo! tunapaswa kuwa na uangalifu ulioje Shetani asije akatupata kwa kutumia chambo cha pupa ya vitu vya kimwili!

Shetani Anatumia Udhaifu wa Kibinadamu

Kati ya udhaifu mbalimbali ambao Shetani anatumia kuvuta mtu ni kutaka sana kufurahisha tamaa za mwili kwa njia zilizokatazwa. Yehova Mungu alikusudia tufurahie mambo mengi, nayo yanapofurahiwa bila kuruka mipaka ya mapenzi yake kwetu, yanaweza kuleta faida nyingi na furaha. Lakini Shetani anajaribu wanadamu ili watangulize mambo hayo katika maisha yao na kuyafanya kwa njia za ufisadi zinazovunja sheria ya Mungu. Hivyo Shetani alisababisha Waisraeli 24,000 wakajiacha wavutwe na chambo chenye ushawishi cha Baali wa Peori. (Hesabu 25:1-9) Leo ulimwengu umepatwa na wazimu wa kufuatia sana mambo ya kufurahisha tamaa za mwili. Magazeti, sinema na vipindi vya televisheni vinavuta watu waziwazi kabisa wawe na tamaa za kufanya machafu. Lakini, sisi Wakristo wenye kuongozwa na roho ya Mungu lazima tuepuke vishawishi vya namna hiyo. —1 Wakorintho 14:20.

Hila nyingine ya Shetani ni kutumia tamaa ya msisimuko wenye kufurahisha ili kuvuta mtu. Hasa vijana Wakristo ndio wanaoweza kunaswa vyepesi katika mtego huo. Mara nyingi, wao wanajiingiza bila kujizuia katika namna mbalimbali za michezo, wakiwa watazamaji na washiriki pia. Lakini kufanya hivyo kungeweza kusababisha wawe “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:4) Vijana wengine kwa upande wao wanatosheleza tamaa yao ya kusisimuka kwa kugeukia namna za muziki na nyimbo zinazotukuza uasherati na jeuri. Kwa uhakika, kuna uhitaji mkubwa wa kujihadhari, kwa maana mambo kama hayo yanaweza kushawishi vijana Wakristo kwa kuwavuta waache njia ya unyofu na wema. —Zaburi 16:11; 2 Petro 2:20-22.

Pia Shetani anatumia mtego wa kuogopa wanadamu. Ni kawaida ya mtu kutokutaka kudhihakiwa na kujaribu kuepuka mateso. Woga huo umefanya wengi wakubaliane na matakwa ya watesi wao nyakati za mikazo. (Mithali 29:25; Waebrania 2:14, 15) Kwa kusaidiwa na Mungu hatutaruhusu kamwe jambo hilo litupate.

Njia nyingine ya werevu inayotumiwa na Shetani ni kujaribu kuwavunja moyo watumishi wa Mungu hata wakubali kushindwa. Ibilisi alijaribu kumtenda Ayubu hivyo, akamfanya aone ni afadhali kama angalikuwa mfu au hangalizaliwa kamwe. Shetani alijaribu kutumia njia hiyo kwa Musa. (Ayubu 3: 1-13; 14:13; Hesabu 11:10-15) Hakuna ye yote wa wanaume hao waaminifu aliyeshindwa na hali ya kuvunjika moyo. Bali, wao walifuata mapenzi ya kimungu. Kama hao, sisi hatuhitaji kuhuzunishwa mno na hali zo zote, kwa maana Yehova anaweza kutusaidia na hataruhusu kamwe mtu mwadilifu atikisike.—Zaburi 55:22.

Simama Imara!

Kwa sababu ya mafanikio ambayo Shetani amepata kutenga hesabu kubwa ya wanadamu wawe mbali na Yehova Mungu, ni lazima tufanye nini? Ni lazima sisi mashahidi hodari wa Yehova ‘tusimame imara kushindana na hila za Ibilisi,’ kushindana na njia zake za kushambulia kwa ujanja na werevu. (Waefeso 6:11, NW ) Kwa njia hiyo tunaweza kumthibitisha kuwa mwongo mpujufu na mwenye majisifu, kama alivyo kweli kweli.

Lakini, hatuwezi kusimama imara tushindane na Shetani kwa nguvu zetu wenyewe, kwa maana ana uwezo mkubwa zaidi, maarifa mapana zaidi na ujuzi mwingi sana kuliko sisi. Basi, ili tuweze kusimama imara kushindana naye tunahitaji kutumia kwa faida kamili misaada yote ambayo Yehova Mungu ametolea watu wake. Halafu tutashinda mipango ya adui huyo mwenye ujanja!

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mashahidi wa Yehova hawajiachi washindwe kwa kuogopa wanadamu

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Maneno Yanayochangamsha Moyo

DEBORA mwenye umri wa miaka minane aliulizwa na baba yake hivi: “Wewe unapelekea Yehova sala? ” Msichana huyo alijibu: “Ndiyo, sana.” “Wakati gani? ” “Ninapokuwa peke yangu.” “Kwa sababu gani wakati huo? ” “Ili mtu asinisumbue! ”

Mama mmoja aliuliza Laurent mwenye miaka sita hivi: “Unataka niache taa ikiwa imewaka chumbani mwako usiku wa Leo? ” (Laurent alikuwa akiogopa giza na alikuwa ameambiwa apelekee Yehova sala kuhusu jambo hilo.) “Hapana, sasa siogopi kwa sababu Yehova yuko pamoja nami.”

Msichana wa miaka sita alisema hivi katika sala: “Asante, Yehova, kwa tumaini la ufufuo. Ni wazo zuri sana hilo! ” katika sala nyingine, alisema: “Yehova wewe utakuwa na kazi nyingi ya kufanya hapa katika nchi yetu tutakapokuwa katika Paradiso kwa sababu hapa ni mahali penye mvua nyingi sana.”

Udo mwenye umri wa miaka mitatu alisali hivi: “Tafadhali, Yehova Mungu, mfanye baba yangu asoma Biblia ili asife wakati wa Har–Magedoni! ” Mlango wa chumba cha mvulana huyo ulikuwa wazi, naye baba yake akaisikia sala hiyo. Jambo hilo lilimaliza upinzani aliokuwa amebaki nao kuelekea ukweli, na leo yeye ni mtumishi mwaminifu wa Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki