Simama Imara Dhidi ya Hila za Shetani
“Vaeni ile suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili kwamba ninyi mpate kuweza kusimama imara dhidi ya hila [Kigiriki, “vitendo vya kiufundi”] vya Ibilisi.”—WAEFESO 6:11, NW.
1. Ni ithibati gani ya kwamba Shetani yuko inayoandaliwa na vishawishi vya Yesu?
JE! KWELI Shetani yuko? Watu fulani wanabisha kwamba katika Biblia, neno “Shetani” linarejeza kwenye uovu tu ulio ndani ya mwanadamu. Wao wanakana kuwako kwake akiwa kiumbe. Lakini Maandiko yanatuambia nini? Masimulizi ya Injili ya Mathayo na Luka yanaonyesha kwamba Kristo Yesu alishawishwa mara tatu na Shetani, na kila mara Yesu alimkataa yeye, akitumia Andiko. Kwa nini Yesu alimjibu kutokana na Maandiko ya Kiebrania? Kwa sababu Shetani alimjia akitumia kimakosa Maandiko hayo hayo ili kumfanya atende dhambi na kupungukiwa kuwa Mwana wa Mungu, ile Mbegu iliyoahidiwa.—Mathayo 4:1-11; Luka 4:1-13.
2. Ni jinsi gani sisi tunajua kwamba Yesu hakuwazia tu mikabiliano yake pamoja na Shetani?
2 Ni wazi kwamba Yesu, aliyekuwa mwanadamu mkamilifu, hakuiwazia tu mikabiliano hiyo. (Waebrania 4:15; 7:26) Yeye alikabiliwa na yule yule aliyekuwa nguvu iliyomchochea nyoka katika Edeni, ambaye hapo kwanza alikuwa ndugu yake mwenyewe wa kimalaika aliyekuwa ameasi muda mrefu sana kabla ya hapo na sasa akawa amejitokeza ili apotoshe utimizo wa Mwanzo 3:15. Shetani alitaka kuvunja ukamilifu wa Mbegu iliyoahidiwa. Akiwa mwenye hekima kuona vitendo vyake vya kiufundi. Yesu alimkataa Mshawishi kwa uthabiti. Itikizo la Shetani lilikuwa nini? “Kwa hiyo Ibilisi, akiwa amemaliza kishawishi chote, akajiuzulu akamwacha mpaka wakati mwingine wenye kufaa.” Kwa uwazi, Yesu hakujiuzulu kwa kujiacha yeye mwenyewe! Kwa kuvurugika fikira, Shetani alimwacha, “na, tazama! malaika wakaja na kuanza kuhudumia [Yesu].”—Luka 4:13; Mathayo 4:11, NW.
3. Mwanahistoria mmoja anasema nini juu ya umaana wa kuwapo kwa Ibilisi kuhusiana na Ukristo?
3 Kwa kadiri inayofaa, mwanahistoria mmoja anaeleza hivi: “Kukana kuwako kwa Ibilisi na sehemu kuu aliyo nayo katika Ukristo ni kwenda kinyume cha fundisho la kimitume na cha mwendeleo-endeleo wa kihistoria wa fundisho la Kikristo. Kwa kuwa ni kazi ya bure kabisa kuufafanua Ukristo kwa njia zilizo tofauti na hizi, ni jambo lisilopatanika kiakili kutokeza ubishi kwa kutetea Ukristo usiomhusisha ndani Ibilisi. Ikiwa Ibilisi hayuko, basi tangu pale mwanzo Ukristo umekuwa wenye makosa kabisa kabisa kuhusiana na jambo hili lililo la umaana mkubwa.”a Kukata shauri hivyo kunatokeza mwito wa ushindani kwa kila mtu aliye duniani leo. Je! wewe unatambua kuwako kwa adui asiyeonekana ambaye amejitokeza kabisa apindue enzi kuu ya Mungu na utii mshikamanifu wa mwanadamu?
Utambulisho Halisi wa Shetani
4. Ni jinsi gani kiumbe roho aliye mkamilifu alikuja kuwa Shetani?
4 Shetani ni kiumbe roho mwenye nguvu nyingi, ambaye hapo awali aliumbwa na Mungu akiwa malaika, mwana roho aliyekuwa na ruhusu ya kuingia katika ua wa Yehova wa kimbingu. (Ayubu 1:6) Hata hivyo, Shetani alijizoeza uchaguzi wake wa hiari katika kumpinga Mungu; kwa ujanja akaongoza Hawa na, kupitia kwa huyo, Adamu ndani ya kutotii na kifo. (2 Wakorintho 11:3) Hivyo, yeye akawa Shetani, maana yake “Mpinzani”—mwasi, roho mbaya, mwuaji, na mwongo. (Yohana 8:44) Unafaa kama nini usemi wa Paulo kwamba “Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru,” na hali kwa uhakika yeye ni ‘mtawala wa giza hili’! (2 Wakorintho 6:14; 11:14; Waefeso 6:12) Kwa kushawishi malaika wengine kuasi, yeye aliwaongoza kutoka kwenye nuru ya Mungu na kuwaingiza ndani ya giza lake mwenyewe. Yeye akawa ndiye “mtawala wa roho wabaya.” Yesu pia alimtambulisha kuwa ndiye “mtawala wa ulimwengu huu.” Ni wazi kwamba, ili awe mtawala, ni lazima awepo akiwa mtu roho aliyeumbwa.—Mathayo 9:34; 12:24-28; Yohana 16:11, NW.
5. Shetani anatambulishwa kwa uwazi gani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?
5 Ingawa Shetani anatajwa kwa uhaba katika Maandiko ya Kiebrania, roho takatifu ya Mungu ilihakikisha kwamba yeye anafichuliwa kikamili katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo—sana sana hivi kwamba sisi tunakuta humo jina hilo Shetani mara 36 na neno Ibilisi mara 33. (Ona Comprehensive Concordance of the New World Translation of the Holy Scriptures.) Yeye anatambulishwa pia akiwa chini ya majina na mitajo mingine ya cheo. Mawili ya hayo yalitumiwa na Yohana kwenye Ufunuo 12:9, NW; “Kwa hiyo chini likavurumishwa lile joka kuu, yule nyoka wa awali, yule mmoja anayeitwa Ibilisi na Shetani, ambaye anaongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.”—Ona pia Mathayo 12:24-27; 2 Wakorintho 6:14 15, NW.
6. Ni nini maana ya neno “Ibilisi”?
6 Humu katika Ufunuo linaonekana neno la Kigiriki di·aʹbo·los, lililotafsiriwa kuwa “Ibilisi.” Kulingana na mwanachuo Mgiriki J. H. Thayer, neno hilo kwa uhalisi linamaanisha “mkashifu, mshtaki bandia, mchongezi.” (Linganisha 1 Timotheo 3:11; 2 Timotheo 3:3, Kingdom Interlinear.) W. E. Vine anamsimulia Ibilisi kuwa “akiwa yule adui habithi kabisa wa Mungu na mwanadamu.”b
7. Kwa nini Shetani anaweza kuelekeza jitihada zake juu ya watu wa Yehova hasa?
7 Huyo Mpinzani mkuu hakai kitako tu bila la kufanya. (1 Petro 5:8) Labda hiyo ndiyo sababu mithali moja inasema, “Ibilisi huitafutia kazi mikono isiyo na la kufanya.” Yeye amejitokeza kabisa kupindua Wakristo wote wa kweli. (2 Timotheo 3:12) Na anaweza kukaza fikira zake juu ya watu wa Yehova kwa sababu moja rahisi—tayari sehemu ile nyingine yote ya ulimwengu imo katika nguvu zake! (1 Yohana 5:19) Ulimwengu wa leo ni ulimwengu wa Shetani. Yeye ndiye mtawala na mungu wao, hata kama watu wanatambua au hawatambui jambo hilo. (Yohana 12:31; 2 Wakorintho 4:4) Tokeo ni kwamba, yeye atageukia utumizi wa kila kitendo au dokezo la kiufundi au la werevu sana ili apindue watu wa Yehova, ama mmoja mmoja ama wote kwa ujumla. Acheni tuchunguze baadhi ya njia anazotumia kuendesha kazi.—Marko 4:14, 15; Luka 8:12.
Vitendo vya Werevu na Vyenye Ufundi vya Shetani
8. Shetani anaweza kuwa akifanya kazi dhidi yetu akiwa na kitu gani cha kutuzidi sisi?
8 Shetani amekuwa na muda mrefu wa kujifunza akili za kibinadamu, kuchanganua asili ya kibinadamu pamoja na kasoro zayo zote. Yeye anajua jinsi ya kutumia udhaifu wetu mbalimbali na ubatili wetu. Sasa, hali ikoje ikiwa adui yako anajua udhaifu wako mbalimbali na wewe mwenyewe unakosa kuutambua? Hapo basi unakuwa hujajitayarisha vizuri kwa vifaa vya kujikinga mwenyewe, kwa kuwa huna habari ya vitobotobo vilivyo katika deraya yako ya kiroho. (1 Wakorintho 10:12; Waebrania 12:12, 13) Yanafaa kama nini yale maneno ya mshairi Mskochi: ‘Laiti nguvu fulani ingetujalia sisi tujione binafsi kama wengine watuonavyo sisi! Hiyo ingetutia uhuruni bila makosa mengi ya kiupuzi.’
9. Tokeo lisilo la kufurahisha huenda likawa nini ikiwa sisi tunashindwa kujichanganua wenyewe na kubadilika?
9 Je! sisi tuna nia ya kujiona wenyewe kama vile wengine wanavyotuona sisi—hasa kama vile huenda Mungu au Shetani akawa anatuona sisi? Hiyo inataka kufuata haki katika kujichanganua na kujikadiria binafsi na nia ya kufanya badiliko. Ni rahisi sana kujidanganya wenyewe. (Yakobo 1:23, 24) Nyakati nyingine sisi hujipunguzia-punguzia malawama kama nini ili kutetea mwendo wetu wa kitendo! (Linganisha 1 Samweli 15:13-15, 20, 21, 24.) Tena ni rahisi kama nini kusema, “A-ah, hakuna mtu mkamilifu!” Hilo hasa ndilo jambo ambalo Shetani anajua, na yeye anatumia kwa faida yake mwenyewe hali yetu ya kutokamilika. (2 Samweli 11:2-27) Ni huzuni kama nini mtu kufikia umri wa makamo hivi halafu aje kung’amua kwamba kwa sababu ya njia yake ya kutumia mabavu, isiyo ya kiutu, au isiyo ya fadhili ambayo ameshughulika na wengine muda wa miaka iliyopita, amekuwa asiye na rafiki; au aje kung’amua kwamba amefanya mambo machache sana au hakufanya lo lote la kufurahisha watu wengine. Labda Shetani ametuongoza kwa werevu sana maishani akitumia ubinafsi wetu tuliozaliwa nao ili kutupofusha. Tumeshindwa kukipata kile kiini halisi cha akili ya Kristo—upendo, huruma, na fadhili.—1 Yohana 4:8, 11, 20.
10. Ni maswali gani ambayo tunaweza kujiuliza wenyewe, na kwa nini?
10 Kwa hiyo, ili kumkinza Shetani, ni lazima sisi tujichunguze wenyewe. Je! wewe una udhaifu fulani ambao Shetani angeweza kutumia au ambao anatumia sasa hivi kwa manufaa yake mwenyewe? Je! wewe una tatizo la kujifikiria mno? Je! ni lazima wewe uwe ndiwe namba moja sikuzote? Je! kiburi chako ndiyo kani iliyofichika ambayo inakusukuma? Je! wivu, husuda, au upendo wa pesa hupotoa utu wako? Je! wewe ni mtu wa matata-matata? Je! wewe ni baridi-baridi na mwenye madharau? Au wewe ni mwenye kunyeta mno unapotolewa madokezo au uchambuzi? Je! wewe unaonea mashauri uchungu au hata kuyakataa? Ikiwa sisi tunajijua wenyewe, tunaweza kurekebisha matatizo hayo, mradi sisi ni wanyenyekevu. Ama sivyo, tunajiacha tukiwa wazi tuingiliwe na Shetani.—1 Timotheo 3:6, 7; Waebrania 12:7, 11; 1 Petro 5:6-8.
11. Huenda Shetani akajaribu kufukua hali yetu ya kiroho kwa kutumia njia gani ya werevu sana?
11 Shetani anaweza pia kufukua hali yetu ya kiroho kwa njia ya werevu sana, yenye hila. Labda sisi tunaudhika kwa jinsi mambo yanavyofanywa katika kundi au tengenezo. Mara nyingi huwa kwamba hatuna mambo yote ya uhakika, lakini kwa urahisi tunarukia kukata mashauri. Ikiwa uhusiano wetu pamoja na Yehova ni dhaifu, basi hiyo ni hatua fupi ya kuingilia fikira na mashaka ya mwelekeo hasi juu ya ukweli. Huenda watu fulani wakatafuta njia ya kutetea haki yao ya kuepa madaraka ambayo ukweli unahusisha ndani. Ndipo Shetani anapotia ukosefu wa ushikamanifu na usaliti ndani ya mioyo yao. Baada ya muda mfupi wanakuwa majeruhi wa uasi-imani, na Shetani anashangilia.—Luka 22:3-6; Yohana 13:2, 27; 2 Yohana 9-11.
12. (a) Watu fulani wamejasirishwa na Shetani jinsi gani? (b) Ni jinsi gani Shetani anatega wengi kuwaingiza katika ukosefu wa adili?
12 Wengine wanajasirishwa na Shetani si kutenda dhambi nzito tu zinazostahiki kufanya watengwe na ushirika bali hata wanageukia kusema mambo ya uwongo na kudanganya ili wajaribu kupumbaza wazee wa kundi. Kama vile Anania na Safira, wao wanafikiri wanaweza kuwadanganya malaika na roho takatifu ya Mungu. (Matendo 5:1-10) Maelfu wengi katika miaka ya majuzi wameanguka ndani ya mtego wa Shetani wa ukosefu wa adili. Ibilisi anajua kwamba misisimuko ya ngono ya aina ya wanadamu ina nguvu nyingi, na kupitia mfumo wake wa ulimwengu, yeye anakazia, anapotosha, na kugeuza kusudi la ngono. (Hesabu 25:1-3) Huenda Wakristo wasiofunga ndoa wakashawishwa kuingia katika uasherati au matumizi mengine mabaya ya ngono. (Mithali 7:6-23) Ikiwa Wakristo waliofunga ndoa wanaruhusu akili na mioyo yao itange-tange, wanaweza kwa urahisi kuanguka ndani ya mwenendo wa usaliti, wakisaliti mwenzi wa ndoa ambaye waliweka nadhiri ya kumtendea uaminifu.—1 Wakorintho 6:18; 7:1-5; Waebrania 13:4.
13. (a) Televisheni inafanyiza kufikiri kwetu kuwe jinsi gani? (b) Ni jinsi gani sisi tunaweza kukinza uvutano huo?
13 Sisi tunaishi katika ulimwengu ambamo uwongo, udanganyifu, na hasira yenye jeuri ni mambo ya kawaida. Shetani anavitumia kikamili vyombo vya habari ili kupitishia watu akili hiyo ya upujufu. Mifululizo ya vitimbi vya televisheni inaonyesha watu wenye sura za kuvutia wakiishi katika maisha ya kudanganyana. Sisi tukiruhusu kufikiri kwa jinsi hiyo kutuathiri, baada ya muda mfupi tunaweza kuanza kuziachia nafasi dhambi “ndogo-ndogo,” zinazokuwa mwanzo mdogo wa kuangulia zilizo “kubwa-kubwa.” Madokezo ya Shetani yaliyo ya werevu sana yanajipenyeza polepole na kwa urahisi ndani ya kufikiri kwetu. Ni jinsi gani sisi tunaweza kukinza mavutano hayo? ‘Usiruhusu kamwe nafasi kwa ajili ya Ibilisi,’ kama vile Paulo alivyoshauri. Hiyo inamaanisha pia kudhibiti ni nani utamruhusu aingie ndani ya maskani yako kupitia televisheni. Je! haitupasi tukirihi kujidukiza kwa watu wenye jeuri, wasio na adili, walio na vinywa vichafu—ambao wanaleta uchafu ndani ya sebule yetu?—Waefeso 4:23-32, NW.
Ni Jinsi Gani Tunaweza Kukinza Shetani na Kubaki Waaminifu kwa Mungu?
14. Ni azimio gani lenye sehemu mbili linalohitajiwa ili kukinza Shetani, na hiyo inataka nini?
14 Kwa kuwa adui huyo aliye na nguvu nyingi kuliko binadamu amejipanga dhidi yetu sisi viumbe wanadamu wasiokamilika, tunaweza jinsi gani kuendeleza ukamilifu wetu? Ufunguo unapatikana katika maneno ya Yakobo: “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7) Angalia kwamba shauri la Yakobo linahusu sehemu mbili. Ingawa sisi tunapinga Ibilisi na mapenzi yake, ni lazima tujitiishe wenyewe kwa mapenzi ya Mungu. Hiyo inahusisha ndani kupenda mapenzi ya Mungu na kuchukia ya Shetani. (Warumi 12:9) Hivyo, Yakobo anasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.” (Yakobo 4:8) Ndiyo, katika ukinzano wetu kwa Shetani, hakuna nafasi ya moyo nusunusu wala ya kubaki bila uamuzi. Hatuwezi kuthubutu kujasirisha ukamilifu wetu kwa kujaribu kuona ni kwa kadiri gani tunaweza kuja karibu na mpaka uliowekwa. Ni lazima “tuchukie [kabisa kabisa] lililo baya.”—Zaburi 97:10, NW.
15. Kwa nini “ile suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu” ni ya maana sana? Toa kielezi.
15 Shauri la kutokeza juu ya kumkinza Shetani linapatikana katika Waefeso sura ya 6. Paulo anasema tunaweza jinsi gani kukinza “ufundi,” “njama,” au “mbinu” za Shetani? (Waefeso 6:11, Phillips, New International Version, The Jerusalem Bible) “Vaeni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,” yeye anashauri. Usemi huu “suti kamili” hauachii nafasi mwelekeo wa kizembe kuhusu Ukristo, kama vile tu askari Mroma hangeweza kuthubutu kuwa mzembe wakati ya kujitayarishia pigano. Mambo yangekuwaje kwa askari huyo ikiwa alijitayarisha akiwa na suti nzima yote ya silaha isipokuwa ngao na lile bamba la chuma la kifuani? Yeye angaliweza kufikiri kwamba, ‘Hiyo ni ngao kubwa kweli kweli, na lile bamba la chuma la kifuani ni zito sana. Vitu hivyo ni vizito sana, na kwa kweli mimi sivihitaji.’ Wazia hali hiyo—askari Mroma akiwa na silaha za kupigana lakini bila vitu vyake vikuu vya kujikingia.—Waefeso 6:16, 17.
16. (a) Ni lazima sisi tufuate kielelezo cha Yesu jinsi gani katika kutumia “upanga” wetu? (b) Ni jinsi gani sisi tunaweza kuendelea kuwa macho dhidi ya “makombora yanayowaka moto” ya Shetani, na kwa tokeo gani?
16 Wazia, pia, askari akiwa bila upanga wake. Ule “upanga wa roho” ni kinga nzuri sana, kwa kuwa unatumiwa kukatilia-katilia mbali silaha ambazo Shetani analeta dhidi ya Mkristo. “Upanga” wetu unapasa kuwa tayari nyakati zote. Utakuwa hivyo ikiwa sisi hatukosi kujali funzo letu la kibinafsi na funzo la Biblia la kijamaa. Lakini hasa, huu “upanga . . . Neno la Mungu” ni chombo chetu cha kushambulia. Yesu aliutumia kwa njia zote mbili. (Mathayo 4:6, 7, 10; 22:41-46) Lazima sisi pia tuutumie hivyo. Ni lazima tuendelee kunoa uthamini wetu juu ya ukweli. Hatuwezi kudumisha hali yetu ya kiroho kwa msingi wa mambo tuliyojifunza katika miezi au miaka yetu michache ya kwanza katika ukweli. Kama tungeshindwa kuifanya upya mikondo ya kani za kiroho zenye kuzunguka katika akili yetu, njozi yetu ya kiroho ingefifia. Bidii yetu kwa ajili ya ibada ya kweli ya Yehova ingepungua sana. Tungekuwa wanyong’onyevu kiroho. Tungekuwa hatuwezi tena kuondosha mashambulizi ya watu wa ukoo, marafiki, waandamani, na waasi-imani ambao huenda wakarundika madharau juu ya itikadi zetu. Lakini Mungu atatuokoa kutoka kwa Ibilisi na ‘makombora yake yanayowaka moto’ ikiwa sisi tunaendelea kujitayarisha wenyewe kwa vifaa vya “ile suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.”—Isaya 35:3, 4, NW.
17, 18. Pigano letu ni dhidi ya nani, na ni jinsi gani sisi tunaweza kushinda?
17 Ndiyo, Paulo alikazia ile hatari inayohusika katika pigano la Kikristo wakati alipoandika hivi: “Kwa maana pigano letu si dhidi ya adui za kibinadamu, bali dhidi ya nguvu za kikosmosi, dhidi ya mamlaka na wawezaji-wakuu wa ulimwengu huu wenye giza, dhidi ya kani za uovu katika mbingu ambazo zina nguvu nyingi kuliko zile za kibinadamu.” (Waefeso 6:12, The New English Bible) Ni jinsi gani sisi wanadamu duni tunaweza kukinza na kushinda katika pigano hilo la kutumia nguvu zisizolingana? Paulo anarudia wazo lake: “Kwa sababu hii chukueni ile suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili ninyi mpate kuweza kukinza katika ile siku ya uovu na, baada ya ninyi kuwa mmefanya mambo yote kweli kweli, kusimama kwa imara.” (Waefeso 6:13, NW) Maneno makuu ni: “Baada ya ninyi kuwa mmefanya mambo yote kweli kweli.” Hapa tena nafasi haiachwi kwa ajili ya Ukristo wa moyo nusunusu au wenye kuelekeza fikira upande usiofaa.—1 Yohana 2:15-17.
18 Kwa hiyo, acheni tusimame kwa uthabiti katika ukweli, tukipenda uadilifu wa Yehova, tukihubiri zile habari njema za amani, tukishikamana sana kuwa na imani imara katika wokovu ambao Yehova anatoa kupitia Kristo Yesu, huku sisi tukitegemea Neno la Mungu kuwa nguzo yetu kuu. (Waefeso 6:14-17) Kumbuka, Mungu anatujali sisi, na atatusaidia tupate shangwe ya kushinda majaribu na wasiwasi ambao unatujia sisi katika mfumo wa mambo wa Shetani. Sisi sote na tutii onyo hili: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.” Ndiyo, “mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani.”—1 Petro 5:6-9.
19. (a) Ni uandalizi gani zaidi ulio wa maana sana ambao ni lazima sisi tuutumie ili kukinza Shetani? (b) Ni nini litakalopata Shetani mwishowe?
19 Tusisahau ile nyongeza ya maana sana ya Paulo kwenye “suti ya silaha.” Yeye anasema: “Huku kwa kila namna ya sala na dua mkiendelea kutoa sala kila pindi katika roho. Na kwa kusudi hilo endeleeni kuwa wenye kuamka kwa uendelevu wote na kwa dua kwa ajili ya watakatifu wote.” (Waefeso 6:18, NW) Adui yetu asiyeonekana ni mwenye nguvu sana hivi kwamba tunahitaji “kila namna ya sala na dua.” Basi, ni lazima sala zetu ziwe za kweli sana na za namna-namna! Ni jambo muhimu kumtegemea Yehova kabisa ndipo tushinde lile pigano na kudumisha ukamilifu. Ni yeye peke yake anayeweza kugawa “nguvu inayopita ile iliyo ya kikawaida” ambayo itatuwezesha kukinza Mpinzani wetu asiyepunguza ukali wake. Ni faraja kama nini kujua kwamba karibuni Mpinzani wetu mkuu atatiwa katika shimo lisilo na kikomo na hatimaye aangamizwe kabisa milele!—2 Wakorintho 4:7, NW; Ufunuo 20:1-3, 10.
[Maelezo ya Chini]
a Satan—The Early Christian Tradition, kilichotungwa na Jeffrey Burton Russell, ukurasa 25.
b An Expository Dictionary of New Testament Words.
Je! Wewe Unaweza Kujibu?
◻ Ni jinsi gani sisi tunajua kwamba Shetani ni mtu halisi?
◻ Kwa nini majina na mitajo ile mingine ya vyeo vya Shetani inafaa?
◻ Ni uchanganuzi gani wa kibinafsi unaweza kutusaidia tukinze mashambulizi ya Shetani yaliyo ya werevu sana?
◻ Ni shauri gani litatusaidia katika kumshinda Shetani, na kwa nini?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Njia moja ya kukinza uvutano wa Shetani ni kuwa mwenye kujitokeza kuonyesha watu urafiki, kuwa mwenye msaada, mwenye upendo
[Picha katika ukurasa wa 16]
Inatupasa sisi tujilinde dhidi ya kuwa kama Anania na Safira, ambao walimpa Shetani nafasi
[Picha katika ukurasa wa 17]
Ili kuondosha makombora ya Shetani, hatuwezi kuacha nje sehemu yo yote ya deraya yetu ya kiroho