Vijana Wauliza . . .
Wangewezaje Kunitendea Hivyo?
“Mimi nilimtegemea Gina dada yangu mwenye umri mkubwa awe kielelezo.a Alikuwa akinipeleka sinema na kunisaidia masomo yangu ya nyumbani. Sikujua alikuwa na matatizo mpaka usiku mmoja ilipotangazwa kwamba ameondoshwa katika kundi la Kikristo. Nilishtuka. Sikuweza kuamini. Yeye hakuniambia alikuwa na matatizo.”—Terry.
“Bill alikuwa ndugu yangu mwenye umri mkubwa. Mimi nilimtegemea sana awe kielelezo. Alikuwa mtu mwenye kupendeka sana—wa kufurahisha, wa kuchekesha. Familia yetu ilipokuwa ikila pamoja, yeye angeweza kutufanya tuangue kicheko kikubwa we! Lakini sikuzote Bill alikuwa mtu mwenye kasirani sana. Alianza kukaa-kaa nje na watoto fulani matajiri walioharibika na kuingilia dawa za kulevya. Hiyo ilimfanya awe na kasirani zaidi na zaidi. Muda si muda alianza hata kupigana na wazazi wetu. Wakati mmoja hata nilimwona akimsukuma Mama! Wiki moja tulipanga safari yetu ya kupiga kambi tukiwa familia. Mimi nilikuwa nikiitazamia kweli kweli! Ndipo Bill alipotoroka, bila kutudokezea amekwenda wapi. Nilihofu juu yake, nikaona wasiwasi. Lakini pia nilimwonea kasirani; nikamwonea kasirani kwa sababu Baba alilazimika kufuta safari hiyo, nikamwonea kasirani kwa sababu sikuzote Bill alikuwa akivuruga kila kitu.”—Don.
NI JAMBO lenye maumivu wakati ndugu au dada mwenye umri mkubwa awapo mwasi, atorokapo, akamatwapo, au aaibishapo jamaa yenu kwa njia fulani.
Mara nyingi wewe huwa umetegemea ndugu au dada huyo mwenye umri mkubwa awe kiolezo. Kumwona huyo akiacha kuwa mtu wa kutegemewa kwaweza kuvunja moyo sana. Huenda hata kukaamsha hofu kuhusu wewe mwenyewe. ‘Je! hili litanipata mimi?’
Hisia-moyo nyingine ambayo yaweza kuwa ya kushindana nayo huenda ikawa ni kuona uchungu. Wewe waona uchungu juu ya ndugu au dada yako kwa sababu ya umizo na umivu lote ambalo anasababisha kwako na jamaa yenu. “Mama na Baba walishindwa la kufanya,” akumbuka Don. “Walihuzunishwa kabisa na jambo hilo.” Huenda wewe ukaona uchungu zaidi kwamba ndugu au dada yako mpotovu amekuwa ndiye wa kukaziwa uangalifu wote wa wazazi wako—kana kwamba wewe haupo! Huenda hata ukashawishwa kufanya matata kidogo wewe mwenyewe ili uvute uangalifu wa wazazi wako kuelekea wewe.
Kwa upande ule mwingine, huenda wewe ukahisi uchungu pia kuelekea wazazi wako waanzapo kuchukua hatua kali ya kinidhamu kuelekea mwasi huyo. Wewe wajiuliza hivi kwa mshangao: ‘Je! ilikuwa lazima wawe wagumu hivyo kwake?’ Huenda pia ukachoka kusikia wazazi wako wakimkaripia. Vijana fulani hata huhisi kijicho kwa siri, wakijiuliza kama wangeweza kupata shangwe ya mtindo wa maisha ambao sasa ndugu au dada yao aonekana kuonea shangwe. Au huenda ukaona haya tu kulazimika kuwaeleza rafiki zako hali hiyo inayosononesha.
Basi, kwa nini ndugu na dada wenye umri mkubwa hutuaibisha nyakati nyingine? Nawe waweza kuzuiaje jambo hilo lisiathiri maisha yako isivyofaa?
Kwa Nini Ndugu au Dada Wenye Umri Mkubwa Hushindwa Nyakati Fulani
Biblia huelewesha wazi kwamba “wote”—hata ndugu na dada wenye kutegemewa sana—“wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Warumi 3:23) Na vijana hasa wanaweza kwa urahisi kupatwa na kosa, kwa maana mara nyingi wao huwa hawajajifunza kudhibiti hisia-moyo na misisimuko yao. Hivyo Biblia husema kwamba “ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto [au kijana].” (Mithali 22:15) Kwa hiyo ingawa bila shaka kushindwa kwao hukuumiza sana, labda hakuna sababu ya wewe kuamini kwamba kosa la ndugu au dada yako lilielekezwa moja kwa moja kwako binafsi kwa njia yoyote, wala hakuna sababu yoyote ya wewe kuona haya, kana kwamba kosa hilo lilikuwa lako mwenyewe.
Yawezekana kwamba kumekuwako kushindwa fulani upande wa wazazi wako katika kulea ndugu au dada yako. Labda wao walikuwa wenye kuachilia mambo mno na wakashindwa kumtia nidhamu ifaavyo. (Mithali 13:24; 29:15, 17) Labda, pia, kwa njia fulani walishindwa kuweka kielelezo kifaacho. Hata hivyo, ingekuwa ni kama kazi bure kujitia katika mabishano makali pamoja na wazazi wako, ukijaribu kukaza juu yao lawama la matatizo ya ndugu au dada yako.
Sana-sana haielekei kwamba kushindwa kumekuwa upande wa wazazi wako kuandaa mazoezi, bali kushindwa kumekuwa upande wa ndugu au dada yako kuitikia mazoezi ya wazazi.
Jinsi Wazazi Huhisi
Huenda hilo likakusaidia uthamini kwa nini kupotoka kwa ndugu au dada yako kunavunja sana hisia za wazazi wako. Wao wametumia wakati, jitihada, na hisia-moyo nyingi katika kulea ndugu au dada yako. Kwa kumwona huyo akifanya kosa, wao hawana la kufanya ila kujawa na shaka na hatia juu ya jinsi walivyomlea.
Basi, si ajabu kwamba wakati hiyo hali mbaya iwapo kwenye kilele chayo, huenda wazazi wako wakaonekana ni kama wanakosa kukujali. Kitabu How to Survive Your Child’s Rebellious Teens, kilichotungwa na Myron Brenton, hueleza hivi: “Mtoto mwasi ndiye hukaziwa sana fikira za wazazi na kuchukua kadiri kubwa ya nishati zao za kihisia-moyo hivi kwamba watoto wale wengine hawaangaliwi. ‘Mimi nilikosa sana ufahamu, nikakaza fikira sana juu ya binti huyo wa umri mkubwa hivi kwamba hata sikujua nilikuwa na binti mwingine au mume,’ ndivyo mama mmoja mwenye mtoto mzoelevu wa dawa za kulevya alivyoliweka wazo hilo.”
Yakubaliwa wazi kwamba haifai wazazi watende hivyo. Lakini je! si yaeleweka kwamba wangetenda hivyo? Biblia hutuambia kwamba Mfalme Daudi alivurugwa hisia sana na uasi wa Absalomu mwana wake halafu na kifo chake kilichofuata hivi kwamba kwa muda akapoteza usawaziko wake akawa hana la kufanya ila kupaaza kilio hiki: “Absalomu, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” (2 Samweli 19:4-6) Uwe na uhakikishio wa kwamba kadiri mambo yatuliavyo—na baada ya muda yatatulia—pole kwa pole wazazi wako watarudia usawaziko wao na wawe katika hali ya kutunza mahitaji yako vizuri zaidi.
‘Je! Mimi Nitafanya Hilo Hilo?’
Swali hili huhangaisha sana vijana wengi, hasa ikiwa wanajikuta wakidadisi juu ya ule “uhuru” ambao ndugu au dada yao mwenye umri mkubwa anaonja.
Kwanza kabisa, ng’amua kwamba ingawa huenda ukawa ulitegemea ndugu au dada yako mwenye umri mkubwa akuwekee kielelezo, bado wewe una daraka mbele za Mungu kufanya linalofaa. “Yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi,” yasema Yakobo 4:17. (Linganisha Wagalatia 6:5.) Ni upumbavu mtupu kuuonea kijicho ule ambao yaonekana kana kwamba ni uhuru alio nao. Kwa muda fulani mtunga zaburi Asafu alihisi kijicho hicho yeye mwenyewe. Lakini baada ya kuchunguza kwa uangalifu matokeo kwa watenda dhambi waasi, alikata shauri kwamba watu wa jinsi hiyo walikuwa “katika udongo wenye utelezi”—kwenye ukingo wa msiba! (Zaburi 73:18, NW) Wewe huhitaji kupatwa na kosa kibinafsi ili ujue kwamba hilo huongoza kwenye maumivu ya moyo tu.—Wagalatia 6:7, 8.
Ng’amua, pia, kwamba jambo ambalo ndugu au dada yako mkubwa afanya halitabiri kwa njia yoyote lile utakalofanya wewe. Kama vile Terry (aliyenukuliwa pale mwanzoni) alivyoweka wazo hilo: “Mimi sitafanya alilofanya dada yangu. Mimi sifanani naye hata kidogo. Sisi ni watu tofauti.”
Kwa kielelezo, fikiria usimulizi wa Biblia kuhusu Yosefu. Hakuna hata mmoja wa ndugu kumi za Yosefu wenye umri mkubwa waliomwandalia kielelezo chema cha kuiga. Hata hivyo Yosefu hakuacha kielelezo chao kibaya kimvute. Yeye alionyesha ujitoaji kwa kanuni za uadilifu na akawa “mmoja aliyechaguliwa pekee kutoka kwenye ndugu zake” ili apokee mapendeleo na mibaraka mingi.—Kumbukumbu 33:16; Mwanzo 49:26, NW.
Vivyo hivyo wewe waweza kujaribu ‘kuwa kielelezo kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi,’ bila kujali mwendo ambao ndugu au dada yako mwenye umri mkubwa amefuata. (1 Timotheo 4:12, NW) Jitihada zako za uaminifu huenda hata zikasukuma ndugu au dada yako mwenye umri mkubwa anyooshe maisha yake mwenyewe.
Jifunze Kutokana na Makosa Yao
Jaribu kupata manufaa fulani kutokana na hali ngumu hii. Kwa kielelezo, je! ndugu au dada yako alitafuta “mashirika mabaya”—vijana ambao hutumia usemi mbaya, hutumia dawa za kulevya, hutumia vinywaji kwa njia mbaya, au hujitia katika mwenendo wa ufisadi? (1 Wakorintho 15:33) Labda wewe wahitaji kutazama kwa ukaribu wale ambao wewe hushirikiana nao.
Fikiria, pia, njia ambayo ndugu au dada yako mwenye umri mkubwa aliitikia shauri kutoka kwa wazazi wako. Je! alikuwa mbishi-mbishi, mwenye kichwa kigumu, mwasi? Ikiwa ndivyo, je! wewe wajikuta pindi kwa pindi ukijibizana na wazazi wako au ukijikokota wakuambiapo utekeleze jambo fulani? Je! ungeweza kujali zaidi ‘kuheshimu baba yako na mama yako’?—Waefeso 6:2.
Haitakuwa rahisi, lakini wewe na jamaa yako mtaokoka tukio hilo lenye kuhuzunisha na labda mwone wema fulani ukitokana nalo. Kwa sasa, usipoteze tumaini kamwe kwamba ndugu au dada yako mwenye umri mkubwa atang’amua kosa la njia yake na achukue hatua za kubadilika. (Linganisha Luka 15:11-24.) Usisahau kamwe kwamba ingawa huenda washiriki wa jamaa wakakuaibisha, Yehova ‘hatakupungukia kabisa wala kukuacha’ kamwe. (Waebrania 13:5) Kwa hiyo ni lazima uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova uje kwanza. Tamaa yako kumpendeza itakusukuma uishi maisha safi yenye unyoofu—hata iwapo ndugu au dada mpendwa amechagua kufanya vingine.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mara nyingi ndugu au dada mwasi ndiye hasa huelekezewa hangaikio la wazazi. Tokeo ni kwamba huenda mtoto asiye na hatia akahisi kwamba yeye hana wa kumjali