Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 10/8 kur. 26-28
  • Kwa Nini Mimi Niwe Ndiye Kitindamimba?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Mimi Niwe Ndiye Kitindamimba?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vizuizi Katika Kuwa Kitindamimba
  • Kung’ang’ana na Walio Wakubwa
  • Manufaa
  • Kupata Manufaa Zote Katika Hali Yako
  • Nawezaje Kuwa Kiolezo kwa Ndugu na Dada Zangu Wachanga?
    Amkeni!—1992
  • Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?
    Amkeni!—2010
  • Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Kwa Nini Nifanye Amani na Ndugu na Dada Zangu?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 10/8 kur. 26-28

Vijana Wanauliza...

Kwa Nini Mimi Niwe Ndiye Kitindamimba?

Kitindamimba huelekea kuonwa kuwa “mtoto” wa familia.

“Ninachukia uhakika wa kwamba ninalazimika kulipia makosa yaliyofanywa na dada zangu wakubwa.”

“Ndugu yangu mkubwa hunipiga anapopata matatizo.”

‘MIMI ndiye kitindamimba kati ya watoto watano,’ aandika Lilia. ‘Na haipendezi sana. Huwa sishirikishwi sana katika mambo ya familia kwa sababu hakuna anayetaka kusumbuliwa na “mtoto.” Ndugu na dada zangu huchukia sana kunitunza. Nyakati zote mimi hujiona kuwa mzigo. Nyakati nyingine mimi hujihisi kama mtoto pekee kwa sababu wakati mwingi huwa ninacheza peke yangu.’

Kati ya watoto wanne, Faye alikuwa kitindamimba. Yeye akumbuka hivi: “Wazazi wangu waliamini sikuzote maneno ya wakubwa wangu kuliko maneno yangu. Na hao wakubwa wangu walikuwa na rafiki zao. Nikawa mpweke.”

Je! wewe ni kitindamimba katika familia yenu? Basi huenda ukawa na malalamiko kama hayo. Huenda wengine wakaona kuwa inapendeza kuwa wewe ni “mtoto” wa familia. Lakini kwa habari yako, kuwa kitindamimba hakupendezi.

Vizuizi Katika Kuwa Kitindamimba

Kwa mfano, je, unahisi kwamba dada au ndugu yako mkubwa hupewa mambo yote mazuri? Huenda ukawa na sababu ya kuhisi hivyo. Katika nyakati za Biblia mzaliwa wa kwanza alifurahia kupewa mapendeleo ya pekee; kitindamimba alikuwa anafuatia nyuma ulipokuwa wakati wa kupata mapendeleo au madaraka. (Linganisha Mwanzo 25:31; 43:33.) Leo, bado wazazi huelekea kuwa na matazamio mkubwa kwa mtoto wao wa kwanza. Si kwamba wanampenda kuliko watoto wao wengineo, lakini ni kwa sababu yeye akiwa mkubwa hivyo, anaweza kupewa daraka la kutunza wale watoto wadogo zaidi. Yeye ndiye wa kwanza kukua, na hivyo, mara nyingi hupewa mapendeleo na uhuru mbalimbali wenye kutamanika.

Hata hivyo, kitindamimba huonwa kuwa “mtoto” wa familia na anaweza kubembelezwa kwa shauku ya kimzazi! Mwanamke aliyenukuliwa katika kitabu Sibling Rivalry, cha Seymour V. Reit, akumbuka hivi: “Mimi nilikuwa kitindamimba katika familia yetu . . . Nilifanywa kuwa mtoto na kushughulikiwa sana, hata na watoto wakubwa katika familia. Bila shaka nilifurahia, lakini ninafikiri hilo lilinizuia kidogo. Huenda lilinizuia kukabiliana na magumu.”

Huenda wazazi wako wakapita kiasi pia katika kujaribu kukulinda. Huenda wakaruhusuwakubwa wako waende nje na rafiki zao lakini wakasisitiza kwamba ubaki nyumbani—au urudi mapema mno hivi kwamba unaona hakuna maana ya kwenda nje kwa vyovyote!

Ukiwa kitindamimba, huenda pia ukalinganishwa na wengine isivyofaa. “Ninapofanya kosa kubwa au ninapotenda kikosa tu nyumbani,” alalamika Karl mwenye miaka 16, “wazazi wangu watasema, ‘Alan huwa hafanyi hivyo’ au, ‘Kwa nini huwezi kunadhifisha chumba chako kama Alan?’” Na ikiwa mkubwa wako alikuwa na mwelekeo wa kuasi alipokuwa na umri wako, tahadhari! Huenda wazazi wako wakajitahidi kuzuia jambo hilo lisitukie tena. “Ninachukia uhakika wa kwamba ninalazimika kulipia makosa yaliyofanywa na dada zangu wakubwa,” alalamika msichana mmoja. “Eti tu kwa sababu dada yangu aliazima gari na kwenda asikotakiwa kwenda, mimi siwezi kuazima gari!”

Kung’ang’ana na Walio Wakubwa

Hata hivyo, huenda lalamiko lako lililo kubwa zaidi likawa jinsi unavyotendewa na wakubwa wako. Huenda wasiheshimu usiri wako au vitu vyako vya kibinafsi. Huenda wakakuchokoza-chokoza au wakakulaumu kwa makosa yao. “Ndugu yangu mkubwa hunipiga anapopata matatizo,” akalalamika mvulana mmoja mchanga.

Kijana Susannah aonyesha kile ambacho mara nyingi husababisha mahitilafiano hayo ya watoto. Yeye asema: “Mimi nafikiri vita vingi ni vya kung’ang’ania tu uwezo na kujua haki za mtu.” Ni jambo la kiasili tu kutaka kupendwa, kutambuliwa, na kukubaliwa na mzazi. Na kwa kuwa ni kama haiwezekani kwa wazazi kuwatendea watoto wote kwa usawa, mahitilafiano na chuki huenda yakazuka. Mzee wa ukoo Yakobo ‘alimpenda Yusufu kuliko wanawe wote.’ Wakubwa wake waliitikiaje? ‘Walimchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani.’ (Mwanzo 37:3, 4) Ukiwa kitindamimba, huenda pia ukapata kiasi kikubwa zaidi cha shauku na uangalifu wa wazazi wako. Ikiwa ndivyo, huenda wakubwa wako wakawa na uhasama kukuelekea. “Nilifikiri dada yangu mdogo alipata kila kitu alichotaka,” asema msichana tineja mzaliwa wa kwanza aitwaye Roseanna. “Nilitambua kuwa nilikuwa nikimwonea wivu.”

Manufaa

Hata hivyo, kuwa kitindamimba kuna manufaa kadhaa. Huenda wazazi wako wakawa wameinuka kifedha kuliko walipokuwa wazazi wapya. Hivyo, huenda ukafurahia faida za kimwili, kama vile kuwa na chumba chako mwenyewe, ambacho wakubwa wako hawakupata wakiwa umri wako. Na ingawa vijana fulani hawapendi kuvaa nguo zilizotumiwa na wakubwa wao, huenda nguo hizo zikakuwezesha kuwa na nguo nyingi kuliko baadhi ya marika wako!

Manufaa nyingine ni ujuzi ambao wazazi wako wamepata katika kulea watoto. (Linganisha Waebrania 5:14.) Yaani, wazazi wako walipata ujuzi kwa kuwalea ndugu na dada zako wakubwa. Wakiwa wamejifunza kutokana na makosa yao ya zamani, huenda wazazi wako wakawa wenye kustarehe na wenye uhakika zaidi katika majukumu yao mbalimbali, bila kushikilia mambo sana. Huenda ukawa na kiasi fulani cha uhuru ambacho wakubwa wako hawakupata walipokuwa umri wako.

Kuwa tu na ndugu na dada wakubwa ni kwenye manufaa pia. Kwa kufikiria uhasama ambao watoto mara nyingi huonyeshana, huenda hilo likawa gumu kwako kuamini. Hata hivyo, ni mara chache ambapo watoto huchukiana kikweli. Kwa kweli, msichana mmoja wa miaka 13 alikiri hivi: “Ndugu yangu hunisumbua nyakati zote. Lakini ninampenda sana kwa hisi zangu za ndani.” Ndugu na dada zako wakubwa wanaweza kuwa chanzo cha urafiki, ushirika, na ushauri. Huenda hata mkubwa wako akawa kiolezo kwako, hasa ikiwa yeye anamhofu Mungu. Je! unaanza mwaka wako wa kwanza wa sekondari? Huenda ndugu yako mkubwa akaweza kukusaidia ubadilikane. Je! wazazi wako wamekuruhusu hatimaye utumie virembeshi? Labda dada yako mkubwa anaweza kukuonyesha jinsi ya kuvitumia.

Kwa kupendeza, kitabu Sibling Rivalry chaendelea kusema hivi: “Vitindamimba . . . huelekea kuwa wenye urafiki na hupenda kukaa na wengine zaidi ya watoto wa kwanza au wa katikati na wanapendwa na watoto wengine. Kwa kuwa wanazoea kuwa pamoja na kushirikiana na marika tofauti, wanastarehe na marika wao nje ya familia.”

Kupata Manufaa Zote Katika Hali Yako

Je! bado unahisi kwamba kitindamimba hupata hasara? Basi, huenda ukapendezwa kujua kwamba mara nyingi watoto wa kwanza na wa katikati hulalamika sana kwamba hali yao ya maisha ndio mbaya zaidi! Hivyo, jambo kuu si ulizaliwa ukiwa wa ngapi, bali ni zile jitihada unazofanya za kutumia kanuni za Biblia.

Kwa mfano, ikiwa unahisi kwamba wazazi wako wanakulinda kupita kiasi, zungumza nao kikomavu. “Pasipo mashauri makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Kwa kuwa mwenye ‘kutaka amani na kutumia akili’ unaweza kushauriana nao na udokeze mapatano—badala ya kunung’unika wakati mambo hayakupendezi. (Yakobo 3:17, 18, NW) Iwapo unakosa kupewa pendeleo ambalo wakubwa wako wamepewa, usikasirike. Thibitisha kwamba unachukua mambo vizito na unayaweza kwa kufanya yote uwezayo katika migawo yoyote ambayo wazazi wako wanakupa.—Linganisha Luka 16:10.

Kanuni za Biblia zitakusaidia pia kuwa na amani na wakubwa wako. Je! unataka usiri? Basi tumia Kanuni ya Kidhahabu na ustahi usiri na vitu vyao. (Mathayo 7:12) Je! wewe huchukia kuchokozwa? Basi watendee wakubwa wako kwa “heshima” na uepuke kuwa wa kwanza kuwatukana. (Warumi 12:10) Je! umeudhika kwa sababu unahisi kwamba hawakujali au hawakushirikishi katika mambo? Usikate tamaa na kuwa mpweke. ‘Jitetee’ kwao, ukizungumzia mambo kwa njia iliyokomaa na yenye utulivu. (Mithali 25:9) Mara nyingi linalotakiwa tu ni kujifunza kusamehe. (Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13; 1 Petro 4:8) Lakini ukihisi kwamba mkubwa wako anakuumiza kimwili au kwa maneno, wajulishe wazazi wako yale yanayoendelea. Ni wakati huo tu ndipo wanaweza kufanya kazi yao ya ‘kurekebisha kiakili’ watoto wao.—Waefeso 6:4, NW.

La, kuwa kitindamimba hakukufanyi uwe “mtoto.” Wala hakuwezi kuzuia ukuzi wako wa kihisia-moyo au wa kiroho. Ukiwa kitindamimba, unaweza kusitawisha hisia-mwenzi, kutokuwa na ubinafsi, utayari wa kushiriki vitu, uwezo wa kuchukuliana na wengine—masomo yatakayokunufaisha katika miaka ijayo.

[Picha katika ukurasa wa 27]

“Kwa nini mimi sishirikishwi katika mambo yote yanayofurahisha?”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki