Vijana Wanauliza . . .
Nawezaje Kuwa Kiolezo kwa Ndugu na Dada Zangu Wachanga?
PAUL alijua ni kwa kadiri gani ndugu yake mchanga alifurahia kutazama televisheni. Kwa hiyo alishangaa siku moja kumwona akiizima wakati programu ilipokuwa inaendelea. Sababu ilikuwa nini? Ndugu ya Paul akaeleza: “Hakikuwa kipindi kinachofaa. Nilijua wewe ungeliizima, kwa hiyo mimi mwenyewe nikaizima.”
Bila hata kutambua, Paul alikuwa ameweka kiolezo kwa ndugu yake mchanga kufuata—na kilikuwa kiolezo kizuri. Je! wewe una ndugu au dada wachanga? Basi unalosema na unalofanya laweza pia kuwaathiri. Kitabu Sibling Rivalry, kilichoandikwa na Seymour V. Reit chasema: “Msukumo wa kuiga ndugu au dada wakubwa kwa umri ni wenye nguvu ajabu na huongoza matendo mengi ya mtoto. Kwa kawaida, ndugu au dada wakubwa huwa violezo.”
Kwa hiyo, upende usipende, kwa sababu wewe ni mkubwa na mwenye madaraka mengi zaidi, ndugu na dada zako huenda wakakuiga. Huenda wakajaribu kuiga jinsi unavyosema na kufanya mambo. Ni kweli, kuwa kiolezo nyakati zote kwa ndugu na dada zako huenda kukaonekana kuwa mzigo nyakati nyingine.a “Mimi ndiye kiolezo kwa kila mmoja,” alalamika msichana tineja aitwaye Linda. “Hivyo mama yangu huniambia hiyo ndiyo sababu napaswa kufanya vizuri shuleni . . . Kwa kweli nina madaraka mengi zaidi.” Mbano waweza kuwa mkubwa hasa ikiwa unaishi katika nyumba ya mzazi mmoja. “Kimatendo mimi ndiye baba yao,” akaandika mvulana mmoja kuhusu ndugu zake wachanga.
Ingawa hivyo, kuwa ndugu au dada mkubwa kuna manufaa yake. Jambo moja, inakuruhusu uwe na uongozi mwema wa maisha ya ndugu na dada zako wachanga. Acha tuone ni jinsi gani hivyo.
Nyumbani
Mithali ya kale husema: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa ufahamu huthibitika.” (Mithali 24:3) Bila shaka, ni daraka la wazazi wako kujenga nyumba yenu, kuifanya mahali pa amani na upendezi. Lakini kwa kuonyesha hekima na utambuzi, unaweza kuchangia zaidi furaha katika familia yenu.
Kwa mfano, wewe huitikiaje wakati Mama au Baba anapokuuliza ukatupe takataka au usafishe chumba chako? Je! unaonyesha ushirikiano? Unatii? Au unapinga au unajibu bila heshima? Ikiwa ni hivyo, usishangae ikiwa ndugu zako wachanga wanaanza kurudisha maneno vivyo hivyo. Jambo la hekima na lenye utambuzi kufanya ni kufuata maneno ya Mithali 1:8: “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako.”
Ingawa hivyo, unaweza kuwa na sababu halali ya kulalamika. Akaomboleza msichana mmoja wa miaka 18: “Sifikiri mama yangu huwapa ndugu zangu wawili daraka la kutosha. Daraka huwa langu kwa kila kitu: kazi ya nyumba, kuweka violezo, kila kitu.” Unaweza kuwajulisha jinsi unavyohisi na lile ambalo unafikiri litarekebisha mambo. Kwa kuwasiliana kwa wazi na kwa uhuru pamoja na wazazi wako, si kwamba tu unafanya maisha yawe mazuri kwako lakini pia unafundisha ndugu zako wachanga njia ya ukomavu ya kutatua kutoelewana.
Hata hivyo, baada ya kuongea mambo pamoja na wazazi wako, kumbuka, wao ndio wenye uamuzi wa mwisho kuhusu jambo hilo. Kwa hiyo uwe mwenye furaha kwa uamuzi wao. Katika njia hii pia utakuwa unaweka kiolezo chema kwa ndugu zako.
Mabishano makali juu ya kazi za nyumbani yaweza kuepukwa ikiwa utachukua hatua. Kwa upande mwingine, je! ni lazima kila wakati uambiwe usiache nguo zako kwenye sakafu, au huwa unarekebisha mambo bila kusukumwa? Mfano wako mtulivu katika upande huu waweza kusaidia sana ndugu na dada zako wachanga kujifunza kwamba katika familia kila mmoja lazima abebe furushi lake mwenyewe ikiwa mambo yatakuwa mazuri.—Linganisha Wagalatia 6:5.
Shuleni
‘Nachukia shule.’ ‘Sioni ni kwa nini napaswa kuenda huko. Sijifunzi chochote.’ ‘Mara tu ikiwezekana, nitaacha shule.’ Vijana wengi mara nyingi husikiwa wakieleza maoni yasiofaa kuhusu shule. Lakini je, ndugu zako wachanga wanakusikia ukiongea jinsi hiyo? Je, wanakuona ukikosa shule na vipindi vya masomo? Hilo laweza kuathiri upesi mtazamo wao kuelekea shule.
Kuweka kiolezo kizuri humaanisha kukuza mwelekeo chanya, unaofaa kuhusu shule. Hilo huenda lisiwe rahisi. Lakini kumbuka: Kuenda kwako shuleni kunaweza kukusaidia kimwili hata kiroho. Wakati uleule, kunaweza kukusaidia uwe na stadi zitakazokusaidia wewe siku moja ukiwa mtu mzima. Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kina sehemu iliyo na kichwa “Shule na Kazi.”b Hiki kina habari inayoweza kutumika inayoweza kusaidia mwelekeo wako kuhusu kujifunza.
Mtazamo wako mzuri kuelekea shule kwa hakika utaambukia ndugu na dada zako wachanga. Na kwa kuwa na upendezi wa kibinafsi kwa maksi zao na masomo yao ya nyumbani—ukijitolea kuwasaidia mara kwa mara—unaweza kukuza maendeleo yao ya kielimu. Lakini vipi juu ya jinsi unavyojiendesha shuleni? Unawaonaje walimu, washauri, na wakuu wa shule? Je, wewe ni mchokozi na mwenye mabishano, au unaweka kiolezo chema kwa kuonyesha heshima kwa mamlaka yao?—Linganisha Tito 3:1, 2.
Ndugu zako pia watachunguza ni aina gani ya marafiki ambao unachagua. Ikiwa utaanza kujiingiza na umati wa “kisasa,” upesi utajipata kwamba “unakataliwa” na Mungu. Laonya andiko lenye kunukuliwa mara kwa mara katika 1 Wakorintho 15:33: “Msidanganyike; mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema.” Wakati huo huo unaweza kuweka kiolezo kibaya kwa ndugu zako. Kijana mmoja ambaye alilelewa na mama Mkristo alichagua kukataa njia za Mungu na akaanza kushirikiana na kikundi cha vijana wa kutumia dawa za kulevya. Upesi akawa mwenye kutumia dawa za kulevya. Akiogopa kwamba ndugu yake mchanga angefuata hatua zake, alimwonya: “Usianze kutumia dawa za kulevya!” Lakini matendo yake yalikuwa na shawishi kuliko maneno yake, na ndugu yake upesi akajiunga na kikundi hicho. Kwa kweli, haungependa dhamiri yako ilemewe kwa kujua kwamba umekuwa kisababishi cha kikwazo kwa ndugu na dada yako!—Linganisha Mathayo 18:7.
Kuweka Kiolezo Katika Ibada
Kwa vijana Wakristo ni jambo la maana kuweka kiolezo katika mambo yanayohusiana na ibada. Uzito wako, kicho, na maongezi yenye kujenga hayatafanya tu moyo wa Baba yako wa kimbingu kufurahi bali yatafanya uvutio wenye kudumu kwa ndugu na dada zako wachanga.—Mithali 27:11.
Kutoa kielelezo: Kwa vijana wengine miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, kuhubiri peupe ni vigumu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kama vile Yeremia wa zamani, vijana wengine wanahisi kwamba hawastahili. (Linganisha Yeremia 1:6) Wengine huenda wakaaibikia kuonekana na marafiki zao wanapojishughulisha katika kazi hii yenye kuokoa uhai. Je, huenda ikawa ndugu zako wanazuiwa na mielekeo kama hiyo isiyofaa? Ikiwa ndivyo, jaribu kuwa na mwelekeo unaofaa juu ya kazi ya kuhubiri. Fanya iwe kawaida yako kwenda pamoja na familia yenu katika kazi ya kuhubiri. Ndugu zako waonapo ukipata shangwe na utimilifu katika kazi hii, huenda wakataka kuiga imani yako.—Linganisha Waebrania 13:7.
Fikiria, kwa mfano, msichana tineja aitwaye Crystal. Yeye anaelezea: “Mradi wangu ni kutumia angalau miezi miwili kila mwaka nikiwa painia msaidizi wakati wa kiangazi.”c Bidii yake imekuwa na tokeo gani kwa ndugu yake mchanga? Asema Crystal: “Ndugu yangu wa miaka 12 ameanza kutumia wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri tangu nianze kufanya hivyo.”
Mikutano ya Kikristo huwa na nafasi nyingine ya kuweka kiolezo chema. Kuhudhuria kwa ukawaida ni takwa la Kimaandiko. (Waebrania 10:24, 25) Kwa nini usiwafundishe ndugu zako kuwa na utaratibu na nidhamu ili wafanye kazi yao ya shule mapema na wahudhurie mikutano? Wanaweza pia kufurahia mikutano zaidi ikiwa wanakuona ukitayarisha vizuri kila mara na wafanya jitihada ya kushiriki.
Kuishi kulingana na matakwa ya Mungu si rahisi. Lakini vijana wote Wakristo wanatakiwa na Mungu kuwa “kielelezo . . . katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi” wawe wana ndugu au hawana. (1 Timotheo 4:12) Kwa nini usianzie nyumbani? Kufanya hivyo huenda kukafanya kuwe na tofauti kubwa—kwa maisha za ndugu na dada zako wachanga na maisha yako pia!
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Kwa Nini Ni Lazima Niwe Kielelezo kwa Ndugu na Dada Zangu Wachanga Zaidi?” katika toleo la Amkeni! la Agosti 8, 1990.
b Kilichotangazwa na Watch Tower Bible and Tract Society of New York Inc.
c Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, painia msaidizi hutoa saa 60 kwa mwezi huo katika kazi ya evanjeli.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Jinsi unavyotendea wazazi wako kwaweza kuathiri jinsi ndugu zako wachanga watakavyowatendea