Vijana Wauliza . . .
Kwa Nini Ni Lazima Niwe Kielelezo kwa Ndugu na Dada Zangu Wadogo Zaidi?
DARRYL ndiye mtoto mwenye umri mkubwa zaidi katika familia. Wakati wa kipindi fulani kigumu sana, aliruhusu maksi (viwango vya masomo) zake zishuke. Wazazi wake wakachukua kitendo cha haraka. Darryl akumbuka hivi: “Walinitia moyo nifanye maendeleo katika kazi yangu ya shule si kwa ajili yangu tu bali pia kwa ajili ya dada zangu wachanga zaidi, kuwaonyesha kwamba maksi nzuri ni za maana.”
Ikiwa wewe ndiwe mtoto mwenye umri mkubwa zaidi katika familia yenu, bila shaka wajua jinsi ilivyo kuambiwa kwamba, ‘Weka kielelezo chema kwa ndugu na dada zako wachanga zaidi!’ Ingawa hivyo, mara nyingi hilo husababisha kuona uchungu wa moyo. Katika kitabu chao Raising Siblings, Carole na Andrew Calladine husema hivi: “Wazaliwa wa kwanza pia hulalamika juu ya matarajio ya juu ambayo wazazi wao huwa nayo kwa kuwahusianisha na wengine. Wao huhisi wakibanwa na wazazi kwamba wafanye vizuri kuliko wengine, wafanikiwe mambo. Mifano ya maonyo ambayo wazaliwa wa kwanza hupewa ni kama hivi, ‘Umri wako umepita kiwango cha kufanya hivyo,’ ‘tumia akili.’”
Ingawa hivyo, kwa nini wazazi hutarajia mengi sana kwa mtoto aliye wa umri mkubwa zaidi? Je! labda wao huwa wakitarajia mengi mno?
Kwa Nini Ni Lazima Wewe Uwe Kielelezo
Kuanzia nyakati za mapema zaidi, watoto wazaliwa wa kwanza—hasa wana (wa kiume)—wamewekewa matarajio ya juu na wazazi. Wakiwa ndio mwanzo wa nguvu za uzazi za baba zao, mara nyingi wana wazaliwa wa kwanza katika nyakati za Biblia ndio waliopendwa sana hasa. (Mwanzo 49:3; Kumbukumbu 21:17) Naam, Yehova mwenyewe aliliita taifa la Israeli “mzaliwa wa kwanza” wake ili kuonyesha upendo wake wa kina kirefu kwao. (Kutoka 4:22) Ingawa hivyo, mengi yalitarajiwa kwa mwana mzaliwa wa kwanza kwa kuwa ndiye hatimaye angerithi baba yake akiwa kichwa cha familia.
Basi, haipasi kukushangaza kwamba bado wazazi huelekea kuwa na matarajio ya juu kwa mtoto wao aliye na umri mkubwa zaidi—nao wana sababu nzuri. Kwanza, ikiwa wewe ndiwe mwenye umri mkubwa zaidi, labda umepokea mazoezi mengi kuliko ndugu na dada zako katika kazi za nyumbani, thamani za kiadili, na kanuni za Biblia. Je! hupaswi kutarajiwa uwapokeze mambo ambayo umejifunza?
Hivyo mvulana mmoja wa miaka 14 aliambiwa na wazazi wake asaidie dada zake wachanga zaidi wajifunze kazi za nyumbani. Akumbuka hivi: “Wazazi wangu walieleza kwamba mimi nilikuwa mwenye mazoezi na ujuzi mwingi kuliko dada zangu kwa sababu nina umri mkubwa zaidi.”
Usaidizi wako katika kuzoeza ndugu na dada zako wadogo zaidi huenda ukahitajiwa kihususa kwa sababu ya mibano ya kiuchumi ambayo wazazi wengi waikabili sasa. Mara nyingi, huwa ni lazima akina mama na akina baba pia wafanye kazi za kimwili, wakibaki na wakati mchache nyumbani. Na ikiwa wewe waishi katika nyumba yenye mzazi mmoja, huenda mzazi wako akawa anataabika chini ya mkazo mkali wa kujaribu kutimiza madaraka ya wazazi wawili. Kuweka kwako kielelezo kwa walio wachanga zaidi katika nyumba hiyo kwaweza kupunguza sana mzigo huo. Zaidi ya hilo, mzazi wako ajua kwamba kuwawekea ndugu na dada zako wachanga kielelezo chema kutakusaidia ukue uwe mtu mzima mwenye kujali madaraka.
Kujali Madaraka Kuwaelekea
Ni kweli kwamba huenda usihisi ukistareheka juu ya kuwa kielelezo. Kama msichana mmoja alivyoweka wazo hilo: “Ni vigumu sana kuwa aliye wa umri mkubwa zaidi kwa sababu mimi hupata mapendeleo na madaraka mengi zaidi.” Lakini uhakika ni kwamba ndugu na dada zako huathiriwa na mwenendo wako. Mara nyingi wataiga usemi, mavazi, na mwenendo wako. Kama vile kijana mmoja alivyosema juu ya ndugu yake mkubwa: “Mimi hupenda yeye afanye mambo kwanza. Halafu naweza kuona jinsi yapasavyo kufanywa.” Kwa hiyo, ufanyayo na kusema ni ya maana sana! Kama vile watungaji wa Raising Siblings waonyesha wazi: “Kujali madaraka ndilo neno la kwanza ambalo wazazi huwaambia wazaliwa wa kwanza.”
Miriam, dada ya Musa mwenye umri mkubwa kuliko yeye, alikuwa kielelezo chema cha kuchukua daraka kuelekea ndugu yake mdogo. Utakumbuka kwamba wazazi wa Musa walikaidi agizo la mfalme kuchinja vitoto vyote vilivyozaliwa karibuni, wakaficha kitoto Musa katika kapu, au sanduku, la mafunjo. Miriamu alichungulia sanduku hilo lilipokuwa likielea kuteremka chini katika Mto Naili, naye akaliona likichukuliwa salama na binti ya Farao. Kwa ujasiri, Miriamu alimwendea na kupanga ili mama mwenyewe wa mtoto huyo amlee. Kwa sababu ya vitendo vyake vya ushujaa kwa ajili ya ndugu yake aliye kitoto, si kwamba Musa aliokoka tu bali pia alikua akawa ndiye mkombozi wa Israeli!—Kutoka 2:1-10.
Je! wewe wahisi daraka kama hilo kuelekea ndugu na dada zako? Badala ya kuwaonea uchungu wa moyo, je! wewe huwa unajaribu kuwa mwandamani na rafiki yao wa karibu? (Mithali 17:17) Kwa kielelezo, waweza kufanya mengi kwa kuwatolea msaada na ushauri katika kutatua matatizo. Labda ndugu au dada mmoja ashindwa kuchukuliana na mtu fulani shuleni. Huenda mwingine akawa na wasiwasi juu ya tukio fulani linalokuja—mhamo wa kwenda mahali papya, siku ya kwanza ya shule, safari ya kwenda kwa daktari—na huenda akahitaji kitia-moyo fulani na tegemezo. Mara nyingi, wewe huwa tayari umepatwa na hali kama hiyo na umo katika msimamo wa kushiriki maarifa na ujuzi wako. Kama vile msichana mmoja tineja alivyosema juu ya dada yake wa umri mkubwa zaidi: “Yeye ni kama mwongozi kwangu. Huelewa yanayonipata, kwa sababu tayari yeye mwenyewe amepatwa nayo.”
Hata hivyo, kuna hatari ya kupita kiasi.
Jua Mipaka Yako!
“Yeye hufikiri ndiye bwana-mamlaka,” akasema kijana mmoja wa miaka 15 kuhusu ndugu yake mwenye umri mkubwa zaidi. “Nikibishana naye, yeye hunyoosha mkono mezani na kunizaba kofi. Hatupatani hata kidogo.” Msichana tineja aripoti tatizo kama hilo katika kushughulika na dada zake wa umri mchanga zaidi. “Mimi nimeketi nao nikawaonyesha maandiko kadhaa,” ndivyo asimulia. “Lakini wao hukasirika! Nyakati fulani mabishano yetu huwa yenye jeuri sana hivi kwamba twaishia kupigana makonde.”
Kwa kusikitisha, nyakati fulani vijana hufikiri kimakosa kwamba kuwa kielelezo ni kuwa bwana-mkubwa. Ingawa waweza kuwa rafiki na mshauri wa ndugu na dada wachanga zaidi, hutakuwa kamwe mzazi wao! Yaelekea kabisa kwamba watayaonea uchungu majaribu yoyote ufanyayo ili kuwachukulia hatua kama vile kuwatia nidhamu au kuwashauri. Ni kazi ya wazazi wako ‘kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova’—si lako! (Waefeso 6:4, NW) Kwa hiyo ingawa ushauri fulani waweza kufaa, ukipingwa kwa kuutoa, labda lingekuwa jambo la hekima ujiondoe na kuacha wazazi wako washughulikie hilo.
Kujua mipaka yako katika jambo hilo kwaweza pia kukuzuia usipambane na wazazi wako. Huenda ndugu au dada mchanga zaidi akaomba sana ushauri wako juu ya jambo huwezi kulishughulikia kwa sababu limezidi ujuzi wako. Au huenda yeye akaungama kosa fulani ambalo wazazi wako wana haki ya kulijua. Badala ya kujaribu kushughulikia mambo wewe mwenyewe, kumbuka maneno ya Mithali 11:2: “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; bali hekima hukaa na wanyenyekevu [wenye kiasi, NW].” Ukiwa mwenye kiasi hakikisha kwamba wazazi wako wanawekwa chonjo juu ya hali hiyo; kwa kweli, ingekuwa vema kumtia moyo ndugu au dada yako awafikie yeye mwenyewe.
Kijana mmoja aonyesha eneo jingine bado ambamo ni lazima wewe ukumbuke mipaka yako, akisema hivi: “Mimi nafurahia kwamba ndimi mwenye umri mkubwa zaidi, lakini nyakati fulani ni vigumu kufanya kila jambo sawasawa.” Badala ya kuhisi ukiwa chini ya mzigo wa uonevu, ng’amua kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2, NW) Yesu Kristo tu ndiye kielelezo kikamilifu! (1 Petro 2:21) Kwa hiyo usijichukue kwa uzito mno.
Manufaa Zilizopo
Kujitahidi kuwawekea kielelezo ndugu na dada zako wachanga zaidi kuna matatizo, lakini kuna thawabu pia. Kwanza, kwa kujionyesha kuwa mwenye kujali madaraka, utakomaa upesi zaidi na bila shaka utajipatia mapendeleo ya ziada. (Luka 16:10) Utakuza uwezo mbalimbali na stadi zitakazokuwa za thamani kubwa sana baadaye, iwapo utakuwa na watoto wako mwenyewe. Lisilo la kusahauliwa, pia, ni tokeo ambalo kielelezo chako chaweza kuwa nalo juu ya ndugu na dada zako wachanga zaidi, kikiwasukuma wawe watu wazima wenye kumhofu Mungu, wenye kujali madaraka.
Kwa kuonyesha upendezi mchangamfu wenye upendo katika ndugu na dada zako, huenda ukawavuta wakupende na kukustahi daima. Ni kweli kwamba watakusumbua fikira mara kwa mara. Lakini kama vile msichana mmoja tineja akirivyo: “Kuna jambo moja ambalo mimi nashukuru kweli kweli kwalo, na hilo ni kuwa na dada wawili ambao huongea nami juu ya matatizo ya kibinafsi na kunipiga pambaja wakati ninapowahitaji.” Kifungo hiki cha upendo, kikiisha kuimarishwa, chaweza kuwa cha maisha yote. Kinaistahiki ile jitihada inayohusika katika kuweka kielelezo chema.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Saidia ndugu na dada wachanga zaidi wajifunze kufanya mambo
[Picha katika ukurasa wa 17]
Huenda dada mwenye umri mkubwa zaidi akaonewa uchungu wa moyo akitenda kama bwana-mkubwa