Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 10/8 kur. 22-25
  • Miaka Hiyo ya Utineja Yenye Msukosuko

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Miaka Hiyo ya Utineja Yenye Msukosuko
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wafundishe Kwamba Ubikira Una Thamani
  • Mfano Wako Mwenyewe
  • Bado Wewe Hujawafunza?
  • Zungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Ninaweza Kufanya Nini Ili Kupinga Shinikizo la Kufanya Ngono?
    Vijana Huuliza
  • Ngono—Ni Shauri Gani Hasa Lihalofaa?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Wazazi Walindeni Salama Watoto Wenu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 10/8 kur. 22-25

Miaka Hiyo ya Utineja Yenye Msukosuko

MATINEJA wamezungukwa na ujumbe mbalimbali wenye kuamsha nyege. Ngono huuza chochote kuanzia viatu hadi nguo za jins (jeans). Muziki wa ki-siku-hizi umejawa na maneno ya kingono. Kwenye televisheni watu wazima wenye kuvutia hutoka katika kisa kimoja cha utendaji ngono hadi kingine. Lakini Je! hilo linafaa?

Gazeti moja maarufu la Amerika lilisema kwamba “kuingizwa kwa mambo mengi ya kingono kwa wingi” wakati ambapo watu wengi wanatazama TV ni “mwendo wenye kutia wasiwasi usio wa kuchukua daraka kabisa.” Jarida The Journal of the American Medical Association liliuita “kutumiwa vibaya kwa vijana kwa faida za kibinafsi na watangazaji na watumbuizaji wa vyombo vya habari.”

Ni lazima uhakikishe kwamba watoto wako wanajua kwamba si kila mtu huishi hivyo. Hata ikiwa, kama inavyodaiwa, nusu ya wasichana Waamerika wa umri wa miaka 17 tayari wamefanya ngono, bado hilo lamaanisha kwamba nusu ile nyingine hawajafanya. Kama vile aliyekuwa Katibu Mkuu wa Elimu William J. Bennett alivyosema: “Si ‘kila mtu’ anayefanya hivyo, na huenda tukapenda kuwapa vijana hao—nusu ya wenye umri wa miaka kumi na saba—utegemezo wetu na kuwatia nguvu, pia.”

Alitaja kwamba katika uchunguzi uliofanywa katika Hospitali ya Ukumbusho wa Grady katika Atlanta, Georgia, U.S.A., wasichana 9 kati ya 10 walio chini ya umri wa miaka 16 “walitaka kujua jinsi ya kusema ‘la.’” Je! waweza kuwasaidia watoto wako wasadikishwe kwamba, itikio pekee kwa dokezo lolote la ukosefu wa adili, si kusema kwa udhaifu usio na uhakika, bali ni kusema la kwa njia chanya isiyokengeuka? Je! unaweza kuwasaidia wang’amue kwamba watu ambao wanafaa watawaheshimu kwa ajili ya hilo? Tineja aitwaye Emily aliliambia gazeti moja la California, U.S.A., kwamba: “Watu ambao huheshimiwa zaidi hawafanyi ngono.”

Unapaswa uwasaidie vijana wako watambue kwamba ngono ni kani yenye nguvu—yenye nguvu sana hivi kwamba imetokeza jamii nzima ya kibinadamu. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba haiwezi kudhibitiwa. Badala yake, inamaanisha kwamba kama vile gari lenye nguvu nyingi la mashindano, ni lazima litumiwe ifaavyo, kulingana na sheria za barabarani. Kupuuza sheria kwenye barabara ya milimani inayopinda kwaweza kuongoza kwa msiba. Kupuuza sheria zilizopewa na Mungu za tabia ya ngono kutakuwa na matokeo ayo hayo. Wewe waweza kusaidiaje watoto wako, unaowapenda sana, watambue jambo hilo?

Wafundishe Kwamba Ubikira Una Thamani

Zungumza pamoja na tineja wako mfano bora wa Biblia wa mwanamwali mzuri mchanga Mshulami. Yeye angeweza kusema kwa fahari: “Mimi nalikuwa ukuta, na maziwa yangu kama minara.” Kiadili yeye alikuwa kama ukuta usiopenyeka wa ngome yenye minara isiyopitika. Na machoni pa atazamiwaye kuwa mume wake, alikuwa kama “mtu aliyeipata amani.” Naam, amani ya akili isiyokatishwa na uchungu wa majuto ni faida kubwa ya ubikira.—Wimbo Ulio Bora 8:10.

Lakini kijana anaweza kuendeleaje kuwa imara kiadili, kama ukuta? Kabla mambo hayo hayajazuka, ni lazima uhakikishe kwamba mtoto wako anayekomaa anajua umaana wa kuchukua hadhari kwa kuepuka hali ambazo zaweza, na mara nyingi huongoza, kwenye ukosefu wa adili. Kwa mfano, wanapaswa kujua kwamba kama vile kunywa na kuendesha gari kunavyoongoza kwenye msiba, ndivyo msiba uwezavyo kupatikana katika karamu ya matineja ambapo wengine wameleta pombe au mahali ambapo hamna mtu mzima mwenye kuchukua daraka.

Vilevile, wasaidie wafahamu kwamba kuwa peke yao katika nyumba na kijana mwingine wa jinsia tofauti ni kujiweka kwenye jaribu. Vijana wanahitaji kufahamu waziwazi hatari ya kiadili ya kuruhusu mtu yeyote ambaye hawajaolewa naye kuweka mkono wake kwenye sehemu zao za siri, kutia na matiti. Waeleze kwamba ushawishi mara nyingi huanza na miguso ya viungo hivyo vya mwili yenye kuchochea kingono.—Linganisha 1 Wakorintho 7:1.

Ni lazima uwasaidie watoto wako wapendwa watambue kwamba upendo wa kweli humaanisha zaidi ya ngono kwa kiasi kikubwa na kwamba ngono nje ya ndoa ni kosa. Vijana wengine hufanya ngono kabla ya kufanya wajibu wa ndoa. Huenda wakafanya ngono na wenzi kadhaa bila kufunga ndoa kamwe. Halafu, kadiri miaka inavyosonga na wanatambua kwamba wanahitaji mwenzi wa ndoa kwelikweli, wanajipata wapweke na walioachwa. Ni kweli, hakuna yeyote aliyetaka wafanye wajibu, lakini pia hakuna yeyote aliyefanya wajibu nao kamwe.

Wana na binti zako wapaswa wajue kwamba ubikira wao ni wa thamani sana kuweza kutupwa kama maji machafu. Saidia mtoto wako afahamu kwamba furaha kamili ya ngono yaweza kupatikana tu katika mpango mtakatifu wa ndoa. Kwa maneno mazuri, ya kishairi, Biblia husema: “Unywe maji ya birika lako mwenyewe, na maji yenye kububujika katika kisima chako. Je! chemchemi zako zitawanyike mbali, na mito ya maji katika njia kuu? Chemchemi yako ibarikiwe; nawe umfurahie mke wa ujana wako.”—Mithali 5:15, 16, 18.

Mkiwa wazazi wenye upendo, ni lazima mfanye jitihada hususa ya kufunza mambo hayo hakika. Hilo ni tatizo la pekee leo, kwa maana mimba kati ya wale ambao hawajaolewa zinakubalika na wengi. Lillian, muuguzi wa uzalishaji watoto, asema kwamba siku hizi yeye hashtushwi kuona hofu kuu machoni pa baba mwenye umri wa miaka 15 ambaye hajaoa huku babu mzazi mwenye kuona fahari akimtupia mikononi kitoto kilichotoka kuzaliwa ambacho hajajitayarishia, hakitaki, wala hawezi kukikubali.

Mtangazaji mmoja wa televisheni alisema kwamba “wanawake wengi wachanga wasioolewa bado wenye watoto lakini bila waume” mara nyingi hushindwa kumaliza shule, kufanya kazi, au kulea watoto wao vema. Yeye alisema, mama hao matineja “wamenaswa katika mikasa yao wenyewe. . . . Umaskini karibu hauwezi kuepukika na hurudia-rudia katika mzunguko wenye kuhofisha.”

Mfano Wako Mwenyewe

Tabia yako mwenyewe itakuwa na uvutano wenye nguvu kwa watoto wako. Wakati mwingine hilo laweza kuwa kweli katika njia zenye hila zaidi kuliko vile unavyodhani. Ni nini hutendeka wakati baba anapotamani wanawake wengine? Au mama asemapo, “Mwanamume mwenye kuvutiaje!” wakati mtu mwenye kupendeza apitapo? Je! wazazi kama hao wanawatia moyo matineja wao wawe bikira? Ikiwa wewe huvutiwa hasa na umbo la mwili, je! unapaswa ushangae ikiwa watoto wako wanaweka mapendezi ya kimnofu mbele ya adili, fadhili, upendo wa kweli, au wakfu wa kibinafsi kwa Mungu?

Kwa hiyo kuwafunza watoto yale wanayohitaji kujua kuhusu ngono kunatia ndani mengi kuliko yale ambayo huenda ikawa ulifikiria. Kunatia ndani mwelekeo wako, roho unayokuza nyumbani, hiari yako ya kufunza watoto mapema, pamoja na mfano unaoweka. Bila shaka, yote hayo hutaka wakati na jitihada, lakini thawabu ni kubwa!

Bado Wewe Hujawafunza?

Lakini namna gani ikiwa watoto wako karibu wawe wakubwa, na bado wewe hujazungumzia mambo hayo nao? Waweza kusema tu: “Kwa kweli nilifanya kosa kungoja muda huo wote kuzungumza nanyi kuhusu mambo hayo, lakini ninataka sana mwe na maisha bora iwezekanavyo hivi kwamba ni lazima nijaribu sasa.”

Kwa hakika, ni afadhali kuzungumzia mambo hayo pamoja na watoto wako wakubwa kuliko kukosa kabisa. Maagizo ya kiadili ya watoto ni daraka la maana sana na ni pendeleo. Ron Moglia wa Chuo Kikuu cha New York alisema: “Mzazi yeyote anayeepa wajibu wa kuzungumza na mtoto wake kuhusu ngono anapoteza ono zuri ajabu analoweza kupata.”

Ikiwa hivi karibuni umepata kuthamini matakwa ya Mungu ya uadilifu na watoto wako wanajua kwamba wakati uliopita hukuishi kupatana nayo, hakikisha kwamba wanajua kwa nini umebadilika sasa. Unaweza kudokeza kwamba wasome gazeti hili halafu upange kuzungumzia habari hiyo. Usikatishwe tamaa na kijana asemaye: “Oh, mimi ninajua hayo yote!” Mwongozo ufaao wa maadili hauwezi kubadilishwa na hekaya za shuleni wala hadithi za vikundi vya marika wala hata maono na wastadi wa ngono. Ukweli ni kwamba kutokujua kwaweza kuongoza kwenye msiba.

Huenda kuzoeza watoto wako kukataka jitihada nyingi, lakini zawadi yaweza kuwa nzuri ajabu! Kama vile Biblia isemavyo: “Mwenye haki aendaye katika unyofu wake, watoto wake wabarikiwa baada yake.”—Mithali 20:7.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Televisheni hufunza nini kuhusu ngono?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kupuuza sheria za kuendesha gari mara nyingi huongoza kwenye matatizo makubwa, ndivyo ilivyo na kupuuza sheria za mwenendo safi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki