Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 2/15 kur. 8-11
  • Wazazi Walindeni Salama Watoto Wenu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazazi Walindeni Salama Watoto Wenu!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtazamo wa Kiafrika Kuelekea Elimu ya Ngono
  • Kwa Nini Uwafundishe?
  • Uwasiliano Mzuri
  • Wenye Kulindwa na Wenye Furaha
  • Zungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Ninaweza Kufanya Nini Ili Kupinga Shinikizo la Kufanya Ngono?
    Vijana Huuliza
  • Ngono—Ni Shauri Gani Hasa Lihalofaa?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Ilinde Familia Yako Dhidi ya Mavutano Yaletayo Uharibifu
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 2/15 kur. 8-11

Wazazi Walindeni Salama Watoto Wenu!

KATIKA shule fulani ya upili ya Nigeria, msichana aliyekuwa mwenye sifa mbaya ya ukosefu wa adili katika ngono alipenda kuwashauri wanafunzi wenzake wa kike juu ya mambo ya ngono. Mojawapo ya maagizo yake juu ya utoaji-mimba lilikuwa kunywa pombe aina ya stout ikiwa imetiwa tumbaku nyingi sana. Hadithi zake, alizoteua kutoka katika fasihi ya kiponografia, ziliwavutia sana wengi wa wanafunzi wenzake. Baadhi yao walianza kujaribu-jaribu ngono, na mmoja wao akapata mimba. Ili atoe hiyo mimba, alikunywa mchanganyiko wa hiyo pombe aina ya stout na tumbaku. Katika muda wa saa chache, alianza kutapika damu. Siku kadhaa baadaye, alikufa akiwa hospitalini.

Katika ulimwengu wa leo, vijana wengi husema bila kukoma juu ya ngono, wakiwaletea uangamizo wasikilizaji wenye kuamini. Vijana wapaswa kugeukia nani ili kupata ujuzi sahihi utakaowalinda salama? Jinsi ilivyo vizuri wawezapo kutegemea wazazi wao wenye kumhofu Mungu, ambao wana daraka la kuwalea katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4.

Mtazamo wa Kiafrika Kuelekea Elimu ya Ngono

Ulimwenguni pote, wazazi wengi hulipata kuwa jambo gumu kuzungumza na watoto wao juu ya mambo ya ngono. Hilo hasa ni kweli katika Afrika. Donald, baba fulani katika Sierra Leone, asema hivi: “Mambo ya ngono hayazungumzwi kamwe. Si sehemu ya utamaduni wa Kiafrika kufanya hivyo.” Mwanamke Mnigeria aitwaye Confident akubali: “Wazazi wangu huona ngono kuwa jambo ambalo halipaswi kamwe kutajwa waziwazi; ni mwiko kitamaduni.”

Katika tamaduni nyingine za Kiafrika, yaonwa kuwa jambo la aibu kutaja maneno yahusianayo na ngono kama uume, shahawa, au hedhi. Mama mmoja Mkristo alimkataza binti yake kutumia neno “ngono,” ingawa alisema huyo binti angeweza kutumia neno “uasherati.” Tofauti na hilo, Neno la Mungu Biblia husema waziwazi juu ya ngono na viungo vya uzazi. (Mwanzo 17:11; 18:11; 30:16, 17; Mambo ya Walawi 15:2) Kusudi la jambo hilo si kushtua au kusisimua lakini ni kuwalinda na kuwafundisha watu wa Mungu.—2 Timotheo 3:16.

Zaidi ya miiko ya kitamaduni, sababu nyingine ifanyayo wazazi wasite ilionyeshwa na baba fulani Mnigeria: “Nikizungumza na watoto wangu juu ya ngono, jambo hilo lingeweza kuwachochea kuwa na ukosefu wa adili katika ngono.” Lakini je, habari yenye adhama juu ya ngono ambayo yategemea Biblia huwatia moyo watoto wakimbie kwenda kujaribu-jaribu? La, haifanyi hivyo. Kwa kweli, huenda ikawa kwamba kadiri vijana walivyo na ujuzi mdogo, ndivyo waelekeavyo kuingia matatani. “Hekima [itegemeayo ujuzi sahihi] ni ulinzi,” yataarifu Biblia.—Mhubiri 7:12.

Katika kielezi cha Yesu, mtu mwenye busara, akiona kimbele uwezekano wa dhoruba za wakati ujao, alijenga nyumba yake juu ya tungamo-mwamba huku mwanamume mpumbavu akijenga juu ya mchanga na kupatwa na msiba. (Mathayo 7:24-27) Vivyo hivyo, wazazi Wakristo wenye busara, wakijua kwamba watoto wao watakabili mikazo iliyo kama dhoruba ya kujipatanisha na viwango vilegevu vya kingono vya ulimwengu, huwatia nguvu watoto wao kwa ujuzi sahihi na uelewevu ambao utawasaidia kuendelea kuwa imara.

Sababu zaidi ifanyayo wazazi wengi wasizungumze na watoto wao juu ya ngono ilitajwa na mwanamke fulani Mwafrika: “Nilipokuwa kijana, wazazi wangu Mashahidi hawakuzungumza nami juu ya mambo ya ngono, kwa hiyo sifikirii kuzungumza na watoto wangu juu ya mambo hayo.” Hata hivyo, mikazo juu ya vijana wa leo ni mingi zaidi kuliko ilivyokuwa juu ya vijana miaka 10 au 20 iliyopita. Hilo halishangazi. Neno la Mungu lilitabiri kwamba “katika siku za mwisho . . . , watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi, wakiongoza vibaya na kuwa wenye kuongozwa vibaya.”—2 Timotheo 3:1, 13.

Wenye kuongezea hilo tatizo ni uhakika wa kwamba watoto wengi hawako tayari au hawawezi kuwafunulia wazazi wao mambo ya siri. Uwasiliano wa pande zote mbili si mzuri hata juu ya mambo ya kawaida. Kijana mwenye umri wa miaka 19 aliomboleza hivi: “Sizungumzi juu ya mambo na wazazi wangu. Hakuna uwasiliano mzuri kati yangu na baba yangu. Hasikilizi.”

Huenda vijana pia wakaogopa kwamba maulizo juu ya mambo ya ngono yataleta matokeo mabaya. Msichana mwenye umri wa miaka 16 alisema hivi: “Sizungumzi na wazazi wangu juu ya matatizo ya ngono kwa sababu ya njia ambayo wao huitikia mambo hayo. Wakati fulani uliopita dada yangu mwenye umri mkubwa zaidi aliuliza Mama maswali fulani kuhusu ngono. Badala ya Mama kumsaidia kutatua tatizo lake, alishuku makusudio yake. Mara nyingi Mama angeniita na kuuliza habari juu ya dada yangu, nyakati nyingine akisingizia mambo fulani juu ya maadili yake. Sitaki kupoteza kupendwa kwangu na Mama, hivyo sizungumzi naye juu ya matatizo yangu.”

Kwa Nini Uwafundishe?

Kuwafundisha watoto wetu vya kutosha juu ya mambo ya ngono si jambo lifaalo tu kufanya bali pia ni jambo la fadhili kufanya. Ikiwa wazazi hawatawafunza watoto wao juu ya ngono, wengine watafanya hivyo—kwa kawaida watafanya hivyo upesi zaidi kuliko vile wazazi wawezavyo kutazamia na kwa kutopatana kamwe na kanuni za kimungu. Msichana mwenye umri wa miaka 13 alifanya uasherati kwa sababu aliambiwa na mwenzake shuleni kwamba ikiwa hangeupoteza ubikira wake, angepatwa na maumivu makali wakati ujao. “Watakata kizinda chako kwa makasi,” akaambiwa. Alipoulizwa baadaye kwa nini hakumwambia mama yake Mkristo yale aliyokuwa amesikia, huyo msichana alijibu kwamba mambo hayo hayakuzungumzwa kamwe pamoja na watu wazima.

Msichana Mnigeria alisema hivi: “Marafiki wangu shuleni walijaribu kunisadikisha kwamba ngono ni kitu ambacho wanadamu wote wa kawaida lazima wafanye. Waliniambia kwamba ikiwa singeshiriki kufanya ngono sasa, wakati ambapo ningefika umri wa miaka 21, ningeanza kupatwa na ugonjwa ambao ungekuwa na matokeo yenye kuleta msiba juu ya uanauke wangu. Kwa sababu hiyo, ili kuepusha hatari hiyo mbaya, wakasema, ilikuwa vizuri kufanya ngono kabla ya ndoa.”

Akiwa amekuwa na uwasiliano mzuri na wazazi wake, alitambua mara moja hitilafiano na yale aliyokuwa amejifunza nyumbani. “Kama kawaida, nilirudi nyumbani na kumwambia mama yangu waliyokuwa wameniambia shuleni.” Mama yake aliweza kupinga hiyo habari isiyo ya kweli.—Linganisha Mithali 14:15.

Kwa kuwapa ujuzi uhitajiwao kuwasaidia watoto wafikie hekima ya kimungu katika mambo ya ngono, wazazi huwatayarisha kufahamu hali zilizo hatari na kutambua watu ambao hutaka kuwatumia ili kujifaidi. Ujuzi huo husaidia kuwalinda dhidi ya maumivu makali ya maradhi ya kupitishwa kingono na mimba isiyotakiwa. Huchangia kujistahi kwao na staha wapatayo kutoka kwa wengine. Huwaweka huru wasipate kuelewa mambo vibaya na wasiwe na hangaiko. Hukuza mtazamo mzuri na ulio chanya kuelekea ngono zifaazo, ukichangia furaha wakioa au kuolewa baadaye. Huo waweza kuwasaidia kudumisha msimamo uliokubaliwa pamoja na Mungu. Nao watoto waonapo hangaiko lenye upendo lionyeshwalo kwao, hilo laweza kuwachochea kuwastahi na kuwapenda wazazi wao hata zaidi.

Uwasiliano Mzuri

Ili wazazi wafanye shauri lao lifae mahitaji ya watoto wao, lazima kuwe na uwasiliano wa pande zote mbili. Wazazi wasipojua yale yaliyomo akilini na mioyoni mwa watoto wao, huenda hata shauri zuri likawa lenye manufaa kidogo sana, sawa na ikiwa daktari ajaribu kutoa agizo la dawa bila kujua asili ya ugonjwa wa mgonjwa. Ili wawe washauri wenye matokeo, lazima wazazi wajue yale ambayo watoto wao kwa kweli hufikiri na kuhisi. Wahitaji kuelewa mikazo na matatizo ambayo watoto wao wanakabili na maswali yanayowasumbua. Ni jambo la maana kuwasikiliza watoto kwa uangalifu, kuwa “[wepesi] sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema.”—Yakobo 1:19; Mithali 12:18; Mhubiri 7:8.

Inachukua wakati, subira, na jitihada kwa wazazi kukuza na kudumisha uhusiano wa karibu na watoto wao, uhusiano ambamo watoto wajihisi huru kufunua hisia zao za ndani kabisa. Lakini yapendeza kama nini jambo hilo lifanikiwapo! Baba fulani wa watoto watano kutoka Afrika Magharibi asema hivi: “Mimi ni baba na pia msiri. Watoto huzungumza nami habari zote kwa uhuru, kutia na ngono. Hata wasichana hunifunulia siri zao. Sisi huchukua wakati kuzungumza juu ya matatizo yao. Wao pia hushiriki shangwe zao pamoja nami.”

Bola, mmoja wa binti zake, asema hivi: “Simfichi baba yangu siri yoyote. Baba ni mwenye huruma na hisia-mwenzi. Yeye hatukandamizi au kututenda kwa ukali, hata wakati ambapo tumefanya kosa. Badala ya kukasirika, atachanganua hilo jambo na kutuonyesha tupaswalo kufanya au jambo ambalo hatukupaswa kufanya. Mara nyingi yeye hurejezea kitabu Ujana na kitabu Furaha ya Familia.”a

Iwezekanapo, ni vizuri wazazi kuanza kuzungumza na watoto wao juu ya ngono wakati ambapo hao watoto ni wachanga sana. Jambo hili huwekea msingi mazungumzo ya kuendelea katika miaka ya utineja ambayo mara nyingi ni migumu. Mazungumzo yasipoanzishwa mapema, nyakati nyingine si rahisi kuyaanzisha baadaye, lakini yawezekana. Mama mmoja wa watoto watano alisema hivi: “Nilijilazimisha kuzungumza juu ya ngono hadi mwishowe wala mimi wala mtoto hatukuona aibu tena.” Hali njema ya mtoto wako ikiwa hatarini, hapana shaka jitihada hizo zafaa.

Wenye Kulindwa na Wenye Furaha

Watoto huthamini wazazi ambao kwa upendo huwaandalia ujuzi utakaowalinda salama. Fikiria maelezo ya Mashahidi wa Yehova fulani Waafrika:

Akiwa na umri wa miaka 24 Mojisola alisema hivi: “Sikuzote nitakuwa mwenye shukrani kwa mama yangu. Alinipa elimu iliyohitajiwa juu ya ngono katika wakati ufaao. Ingawa niliona aibu alipokuwa akizungumza juu ya mambo hayo muda mrefu uliopita, sasa naona mambo mazuri ambayo mama yangu alinifanyia.”

Iniobong aliongeza: “Mimi ninafurahi sikuzote nikumbukapo na kufikiria yale ambayo Mama amenifanyia kwa kunipa mazoezi ya kutosha juu ya ngono. Jambo hilo limekuwa msaada muhimu sana katika kuniongoza kuingia katika uanauke. Naweka nadhiri kufanyia hayohayo watoto wangu wa wakati ujao.”

Kunle mwenye umri wa miaka 19 alisema hivi: “Wazazi wangu wamenisaidia kukinza mikazo ya wanawake wa ulimwengu wenye kutongoza. Isingekuwa kwa sababu ya mazoezi waliyonipa, ningefanya dhambi. Sikuzote nitathamini waliyofanya.”

Christiana alisema hivi: “Mimi hupata manufaa nyingi kutokana na kuwa na mazungumzo na mama yangu kuhusu ngono. Nimelindwa dhidi ya maradhi yenye kufisha na mimba isiyotakiwa, na nimeweza kuwawekea ndugu na dada zangu wenye umri mdogo kielelezo chema cha kufuata. Pia nimepata staha kutoka kwa watu, na mume wangu wa wakati ujao atanistahi pia. Jambo la maana zaidi ni kwamba nina uhusiano mzuri na Yehova Mungu kwa kushika amri yake.”

Bola, aliyetajwa mapema, alisema hivi: “Nilikuwa na mwanafunzi mwenzangu aliyesema kwamba ngono yapasa kufurahiwa bila uwajibikaji wowote wa ndoa. Kwake, lilikuwa jambo la kujifurahisha tu. Hata hivyo, alipata kuwa hilo halikuwa jambo la kujifurahisha alipopata mimba na kutoweza kufanya mtihani wa cheti cha shule pamoja nasi. Nisingekuwa na baba mzuri wa kuniongoza, labda ningeweza kuwa kama yeye, nikijifunza kupitia magumu.”

Ni baraka iliyoje wazazi Wakristo wawasaidiapo watoto wao wawe “wenye hekima kwa ajili ya wokovu” katika ulimwengu huu wenye kichaa cha ngono! (2 Timotheo 3:15) Mafundisho yao yenye kutegemea Biblia ni kama mkufu wenye thamani ambao huremba na kurembesha watoto machoni pa Mungu. (Mithali 1:8, 9) Watoto huhisi wakiwa salama, na wazazi huonea shangwe uradhi wenye kina. Baba fulani Mwafrika ambaye sikuzote hujitahidi kuweka njia za uwasiliano pamoja na vijana wake zikiwa wazi alisema hivi: “Tuna amani ya akili. Tu wenye hakika kwamba watoto wetu wajua kinachompendeza Yehova; hawawezi kuongozwa vibaya na watu wa nje. Tu wenye hakika kwamba hawatafanya mambo yatakayohuzunisha familia. Namshukuru Yehova kwamba wamethibitisha uhalali wa uhakika wetu.”

[Maelezo ya Chini]

a Vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Vijana Wakristo wapokeao habari yenye msingi wa Biblia kutoka kwa wazazi waweza kukataa hadithi zilizopotoka ambazo vijana wengine husimulia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki