Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 7 kur. 64-74
  • Ngono—Ni Shauri Gani Hasa Lihalofaa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ngono—Ni Shauri Gani Hasa Lihalofaa?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NGONO KABLA YA NDOA—SABABU GANI ZISIFANYWE?
  • MATOKEO—YENYE RAHA AU MAUMIVU?
  • NAMNA GANI UZINZI?
  • NGONO KATIKA MPANGO WA NDOA
  • Ninaweza Kufanya Nini Ili Kupinga Shinikizo la Kufanya Ngono?
    Vijana Huuliza
  • Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?
    Amkeni!—2004
  • Nitawaelezaje Wengine Msimamo Wangu Kuhusu Ngono?
    Vijana Huuliza
  • Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 7 kur. 64-74

Sura ya 7

Ngono​—Ni Shauri Gani Hasa Lihalofaa?

KAMA ungefanya uchunguzi wa kuuliza watu “Ni kitu gani kinacholeta furaha?” ungesikia majibu mengi yakitaja ngono. Hilo ni jambo la kutazamiwa, kwa sababu uchu na nyege za kutaka kufanya ngono ni tamaa zilizotiwa na Mungu ndani ya mwili wa kila mtu mwenye afya nzuri.

2 Siku hizi watu wanazungumza zaidi mambo ya ngono bila kuogopa, tofauti na watu wa vizazi vilivyopita. Pia, mwenendo unaohusu ngono umebadilika. Vijana zaidi na zaidi wanaanza ngono wakiwa na umri mdogo, hata wakiwa na umri wa miaka kumi na mitatu, minne hivi. Mamilioni ya watu, kutia ndani wengi waliostaafu, wanaishi pamoja na kufanya ngono bila ya kuoana. Kati ya watu waliooana, wengi wamejaribu ngono ya ushirika, wakabadilishana wake au wakajaribu “ndoa isiyo na masharti,” ambayo waliooana wanakubaliana kwamba kila mmoja wao ana uhuru wa kufanya ngono na mtu ye yote.

3 Habari hizo zinatokana na vyanzo vya habari vya namna mbalimbali. Mambo yanayoonwa leo na watu wengi kuwa yenye kupendeza yanafanywa kwa kutiwa moyo au angaa kwa kukubaliwa na madaktari wengi, washauri wa ndoa na viongozi wa kidini. Watu wengine wanapata mawazo yao kwenye vitabu au makala za magazeti zinazofundisha namna ya kufanya ngono. Na wengine wanapata mawazo yao kwenye mitaala inayofanywa shuleni kuwapa wanafunzi elimu ya ngono. Bado wengine wanapata mawazo yao kwenye vitabu vya hadithi za mapenzi, kwenye sinema na maonyesho ya televisheni yanayohusu ngono tu.

4 Kama watu walio wengi wanavyojua, Biblia pia inaizungumza habari hiyo. Sasa watu wengi wanaelekea kuepa viwango vya Biblia, wakiwa na maoni ya kwamba vinawakataza mambo mengi mno. Lakini hiyo ni kweli? Au kufuata maoni ya Biblia kunalinda mtu asipatwe na matatizo mengi yenye kuumiza moyo na kumwezesha afurahie zaidi maisha?

NGONO KABLA YA NDOA—SABABU GANI ZISIFANYWE?

5 Kwa kawaida nyege zinaamka na kuongezeka sana-sana wakati wa miaka ya utineja (13-19). Kwa hiyo muda wote wa historia vijana wengi wamefanya ngono kabla ya kuoa au kuolewa. (Mwanzo 34:1-4) Lakini katika miaka ya majuzi ngono za kabla ya ndoa zimezidi kufanywa kwa wingi. Mahali pengine ngono ni kama kawaida ya watu wote. Sababu gani?

6 Sababu moja iliyofanya ngono za kabla ya ndoa ziongezeke inahusiana na utangazaji wa ngono unaofanywa katika sinema na vitabu vya hadithi za mapenzi vinavyosomwa na watu wengi. Vijana wengi ni watafiti sana, wanataka kuonja. Basi, mikazo inafanya vijana wenzao pia watake kufanya hivyo. Kwa kuwa ngono kabla ya ndoa na ngono bila kuoana zimeenea sana, sasa viongozi wengi wa kidini wanasema zinaruhusika mradi watu wanaohusika ‘wanapendana.’ Basi hesabu inazidi kuongezeka ya watu wasiooa au kuolewa wanaokabili ulizo hili, ‘Sababu gani tusifanye ngono, hasa kama tunatumia vifaa vya kuzuia uzazi?’

7 Dakt. Saul Kapel, mwandikaji wa habari za magazeti ya tiba, alitaja sababu nyingine-nyingine zinazofanya watu wafanye ngono kabla ya ndoa, akatoa maoni juu ya matokeo yake:

‘Ngono inatumiwa vibaya kuwa njia ya kuasi wazazi. Inatumiwa vibaya kuvuta fikira za wengine, ikiwa ni kama namna ya “mwito wa kuomba msaada.” Inatumiwa vibaya kuwa njia ya ‘kuonyesha wengine’ kwamba mtu ni mwanamume au mwanamke. Watu wanaitumia vibaya ili waheshimiwe kwamba hata wao huifanya, lakini majaribio ya kufanya hivyo yamekuwa kazi bure.

‘Wakati ngono inapotumiwa vibaya namna hiyo, haiyatatui kamwe matatizo yanayoichochea. Kwa kawaida, inayafunika yasionekane.’

8 Hata sababu ya kufanya ngono kabla ya ndoa iwe nini, hata ngono iwe inafanywa na watu wengi namna gani, hata iwe inakubaliwa na washauri na viongozi wa kidini wengi namna gani, Biblia inatoa shauri hili:

“Hili ndilo Mungu analopenda, . . . mjiepushe na uasherati; . . . ili mtu ye yote asifikie hatua ya kuharibu na kuingilia haki za” mtu mwingine.—1 Wathesatonike 4:3-6, NW.

Huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba hapa Mungu anaweka kizuizi cha kupita kiasi. Lakini usisahau kwamba ngono ni zawadi kutoka kwa Yehova Mungu; yeye Ndiye aliyewaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa uzazi. (Mwanzo 1:28) Je! si jambo la akili nzuri kutazamia kwamba Mwanzishaji wa ngono za kibinadamu ana uwezo wa kutoa mashauri bora zaidi kuihusu, maoni yanayoweza kutukinga na huzuni nyingi?

MATOKEO—YENYE RAHA AU MAUMIVU?

9 Uvutano wa kufanya ngono na nyege unaweza kuwa na matokeo mazuri ukitumiwa katika hali zinazofaa. Tokeo moja ni watoto. Kisa cha kwanza kilichoandikwa juu ya ngono kinasema: “Sasa Adamu akafanya ngono pamoja na Hawa mke wake na mke huyo akapata mimba.” (Mwanzo 4:1, NW) Katika jamaa, watoto wanaozaliwa wanaweza kufurahisha sana. Lakini namna gani ikiwa ngono inafanywa na watu ambao wangali hawajafunga ndoa? Mara nyingi tokeo ni lile lile—mimba na watoto.

10 Wengi wanaofanya ngono kabla ya ndoa wana maoni ya kwamba hakuna haja ya kutiwa wasiwasi mwingi na jambo hilo. Wanaposema hivyo wanamaanisha wanaweza kuzuia kutungwa mimba kwa kutumia vifaa. Mahali fulani-fulani matineja (vijana) wanaweza kuvipata vifaa hivyo bila ya wazazi kuwa na habari. Hata hivyo, mimba za matineja ni chungu nzima hata kati ya vijana wanaojiona kuwa wajanja sana, wenye kusema, “Ah, hilo haliwezi kunipata mimi.” Habari kama zinazofuata zinahakikisha mimba ni nyingi:

“Zaidi ya kitoto kimoja kati ya kila vitoto vitano vilivyozaliwa New Zealand mwaka jana kilizaliwa na mzazi asiyeolewa.”

“Kati ya kila wanawake watatu Waingereza wa chini ya miaka 20 wenye kutamka nadhiri za ndoa wakati wa kuifunga, mmoja tayari ni mama mjamzito.”

“Mmoja kati ya wasichana watano matineja [katika U.S.A.] atakuwa mwenye mimba kabla hajahitimu shule ya masomo ya juu.”

11 Matokeo hayo yenye uchungu ya kufanya ngono kabla ya ndoa yameleta mkazo juu ya vijana wengi wa kike na wa kiume. Wengine wao wanajaribu kutoa mimba. Lakini watu ambao ni wepesi kuona huruma wanapata hangaiko kubwa sana wanapofikiria kuangamiza kitoto kinachoendelea kukua tumboni mwa mama yake. (Kutoka 20:13) Mawazo ya moyoni ya mwanarnke na dhamiri yake yanahusika pia. Mawazo hayo yanamkaza mtu sana hivi kwamba wengi ambao wamekubali kutoa mimba wamejuta sana sana baadaye.—Warumi 2:14, 15.

12 Mimba za wakati wa utineja zinaletea mama na mtoto hatari kubwa kuliko mimba za wanawake waliokomaa mwili. Kunakuwa na hatari kubwa zaidi ya kupatwa na anemia (upungufu wa damu), toksemia (sumu katika damu, inayotokeza matatizo mengi mwilini), kutokwa na damu isivyo kawaida, kuchukua mimba muda mrefu isivyo kawaida na kulazimishwa kujifungua maana mtoto hatoki kwa urahisi, na vilevile kufa wakati wa kujifungua. Kitoto kinachozaliwa na mama aliye chini ya miaka 16 kinaelekea maradufu kufa mwaka wa kwanza. Watoto haramu wanaletea wazazi matatizo mengi pia ya kibinafsi, ya kijamii na ya kiuchumi. Zaidi ya hilo, usalama na ukuzi wa mtoto unategemea sana kuwa na mazingira imara nyumbani. Watoto wanaonyimwa hali hiyo kwa sababu wamezaliwa kwa njia haramu huenda wakapata madhara (maumizo) ya maisha yote. Basi, je! wewe ungesema kwa ujumla matokeo ya kufanya ngono kabla ya ndoa ni yenye raha au ni yenye maumivu? Na je! unadhani shauri la Biblia linalosema, “Mjiepushe na uasherati,” ni ulinzi wenye hekima?

13 Kupuza maoni ya Biblia kumeletea watu wengi umizo jingine, yaani, ugonjwa. Wanawake walioanza maisha ya kufanya ngono na wanaume wengi wakiwa matineja ndio wanaoelekea zaidi kupatwa na kansa mlangoni pa tumbo la uzazi. Pia kuna hatari kubwa ya kupatwa na kaswende na kisonono. Watu wengine wanajidanganya wakidhani kwamba hayo ni magonjwa yanayoweza kuonekana upesi na kuponeshwa. Lakini watu wenye ujuzi, wa Shirika la Afya Ulimwenguni la Umoja wa Mataifa, wanasema viini fulani vya magonjwa hayo haviuawi na dawa. Madaktari wanaogopeshwa pia na ongezeko kubwa la uvimbe mwingi wenye majimaji katika viungo vya uzazi. Mara nyingi unaumiza watoto wanaozaliwa na wanawake wenye kuambukiwa na ugonjwa huo. Ndiyo, baada ya kupatwa na huzuni vijana wengi wameanza kujifunza kwamba onyo hili la Biblia linasema kweli:

“Kila dhambi nyingine ambayo huenda mtu akatenda iko nje ya mwili wake, lakini yeye azoeaye uasherati anatenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe.”—1 Wakorintho 6:18, NW.

14 Watu wengine wanadhani kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa kunampa mtu mazoezi ya mapema yatakayofanya iwe rahisi kujua kuifanya afungapondoa. Ni jambo la kawaida katika nchi fulani-fulani kwa akina baba wenye mali nyingi kupeleka wana wao kwa makahaba ili ‘wakaelimishwe.’ Huenda watu wengine wakadhani kufanya hivyo kunasaidia. Lakini kwa maoni ya Muumba wetu hakusaidii, naye amekuwa akiona matukio yote yaliyowapata wanadamu. Kuendeleza ubikira safi ndiko kunakowekea mtu msingi mzuri zaidi wa kuwa na ndoa yenye furaha. Uchunguzi mbalimbali uliofanywa na nchi ya Kanada ulionyesha wazi kwamba matineja waliofanya ngono mapema kabla ya ndoa wanaelekea kufanya uzinzi na wanawake au wanaume wengine baada ya ndoa. Lakini watu wanaoendeleza ubikira safi kabla ya ndoa wataelekea zaidi kuwa safi katika ndoa. Wataendelea kuheshimu na kustahi ndoa kama walivyofanya kabla ya siku yao ya arusi.

NAMNA GANI UZINZI?

15 Mashauri yanayotolewa kwa wingi siku hizi juu ya kufanya ngono yameongeza uzinzi pia. Habari zinazotoka Ulaya na Amerika ya Kaskazini zinaonyesha kwamba karibu nusu ya wanaume waliooa wanafanya uzinzi na wanawake wengine. Wanawake wengi wanazidi pia kuukubali uzinzi na kuushiriki, na mara nyingi tumaini lao ni kwamba wakifanya hivyo watakuwa na maisha yenye kupendeza zaidi.

16 Biblia inatoa shauri lililo wazi sana juu ya jambo hili: “Mume na ampe mkewe haki yake [ya ngono], na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake.” (1 Wakorintho 7:3) Unaweza pia kusoma Mithali 5:15-20, ambayo inatumia usemi wa mfano kwa kusema kwamba watu waliooana wanapaswa wajipatie raha ya ngono ndani ya mpango wa ndoa yao tu, si kwa mtu aliye nje ya mpango huo. Matukio ya karne zote yamethibitisha kwamba shauri hilo ni ulinzi. Linalinda mtu asipatwe na magonjwa na mimba za haramu. Linamlinda pia asipatwe na umizo na huzuni inayoletwa mara nyingi na uzinzi.

17 Wakati mwanamume na mwanamke wanapooana wanajifunga wajibu wa kushikamana mmoja na mwenzake. Inakuwaje wakati mmoja wao anapovunja amana hiyo kwa kufanya uzinzi? Uchunguzi uliofanywa kuhusu uzinzi unasema:

“Kunakuwa na hatia kubwa sana kwa sababu ya kushindwa kutimiza ahadi. Uzinzi ni uhalifu anaojitenda mtu binafsi, kwa sababu anajua kabisa kabisa anamsaliti au anamwumiza nani.”

Jambo hilo lilionekana wazi zaidi baada ya watu wengi waliooana kuyafuata maoni ya “ndoa isiyo na masharti,” ambayo wenye kuhusika walikuwa ati wamekubaliana kila mmoja afanye ngono na mtu ye yote anayemtaka. Baadaye wale wenye kutetea sana “ndoa isiyo na masharti” wakalazimika kubadili maoni yao. Matokeo yenye kuwahuzunisha yaliwalazimisha kukata kauli kwamba “uhakikisho wa kutofanya uzinzi ungali sifa ya maana na ya lazima katika ndoa nyingi zaidi.”

18 Uzinzi unaelekea kutokeza wivu na wasiwasi wa kukosa kutumaini mwenzako. Kwa hekima Mungu alitolea watu maoni ya kuwaeleza madhara yanayoletwa na uzinzi. (Mithali 14:30; 27:4) Hivyo, ingawa watu wengine wanajisikia wao ndio wanaojua zaidi na kwamba uzinzi ni sawa tu, mambo ya hakika yanathibitisha si sawa. Mshauri wa matatizo yanayohusiana na fikira, Dakt. Milton Matz ambaye ni msaikolojia, aliungama hivi waziwazi:

“Wengi wetu tunalemewa sana na huzuni nyingi wakati ngono inapofanywa nje ya mpango wa ndoa, iwe imefanywa na sisi au sisi tuwe ndio tumetendwa ubaya huo. . . .

“Uzinzi umenifunza kwamba unamchoma kila mmoja anayehusika kwa maumivu makali sana. Mtu akitaka dawa ya furaha, dawa hiyo si uzinzi.”

NGONO KATIKA MPANGO WA NDOA

19 Kwa habari ya ngono, Biblia haitushauri juu ya mambo tunayopaswa kuepuka tu. Bali inatutolea mashauri juu ya mema pia tunayoweza kutenda ili maisha yafurahishe sana.

20 Badala ya kuitaja ngono kuwa mwungano wa kuzaa watoto tu, Maandiko yanaonyesha vizuri kwamba ngono inaweza kufurahisha mume na mke. Biblia inasema juu ya ‘kushangilia’ na ‘kuchukuliwa na furaha’ ya mapenzi ya ngono katika mpango wa ndoa. (Mithali 5:19, NW) Kwa sababu ya kutoboa mambo wazi kwa njia hiyo, inaondosha hali ya kuona haya au aibu katika ngono yenye upendo na ya kiasili kati ya mume na mke.

21 Muumba anawashauri waume hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu na msiwe wenye hasira kali kwao.” (Wakolosai 3:19, NW) Ili ngono ifurahishe kweli kweli, lazima watu wawili waliooana waepuke kuoneana uchungu au kinyongo. Ndipo ngono katika ndoa inapoweza kufurahiwa kweli kweli kama inavyopasa, yaani, kuonyeshana upendo mwingi sana, kujiona kuwa na wajibu wa kushikamana na kuoneana huruma kwa mapenzi mengi.

22 Tena, Mungu anawahimiza waume wakae na wake zao “kwa akili.” (1 Petro 3:7) Kwa hiyo inampasa mume afikirie mawazo ya moyoni ya mkewe na vipindi vyake vya mabadiliko ya kimwili. Yeye akiwa mwepesi wa kujua maoni na mahitaji ya mke wake badala ya kumdai bila huruma, inaelekea kwamba hata mke atakuwa mwepesi zaidi kumtimizia mahitaji yake. Basi hapo wote wawili watatoshelezana.

23 Waume wengi wanalalamika wakisema wake zao ni baridi-baridi au hawaamki nyege. Jambo ambalo huenda likasababisha hali hiyo ni kwamba mume hajifanyi rafiki mkubwa wa mkewe, bali anajinyamazia tu au kuwa mkali isipokuwa nyakati zile tu anapotaka kufanya ngono. Lakini je! wewe hukubali kwamba mke ataelekea kumwitikia mumewe zaidi ikiwa mume huyo anamchangamkia na kumwonyesha mkewe urafiki nyakati zote? Ni jambo la kiasili zaidi mke kuitikia mume anayetii shauri analopewa kwamba ajivike “moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.”—Wakolosai 3:12, 13.

24 Biblia inasema hivi: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Jambo hilo linahusika katika njia nyingi, nalo limetumiwa katika ngono mpaka ikawa yenye kufurahisha sana. Namna gani? Hali ya mke ya kufurahia ngono inategemea sana hali aliyo nayo moyoni na akilini. Nyakati za majuzi wanawake wamesisitiziwa sana wahangaikie kujisisimua miili yao wenyewe na kujifurahisha, lakini bado wengi wao hawaridhiki. Walakini, Dakt. Marie Robinson, aliyelichunguza jambo hilo, alionyesha kwamba mke akisitawisha hali ya kuheshimu mumewe na kuiona ngono kuwa njia ya ‘kutoa’ badala ya kupokea, ataelekea kuridhika zaidi yeye mwenyewe. Daktari huyo alieleza hivi:

“Pole kwa pole [mke] anajikuta katika kumbatio la kufanya ngono likiwa na mapenzi na huruma nyingi ambazo ameanza kumwonyesha mumewe. Mke anaona na kuhisi mwilini mwake raha anayopata mumewe kwa sababu yeye mwenyewe amejitolea kumpa raha hiyo, na basi tendo hilo linazidi kuwa la kupeana raha, huku mume akizidi kumfurahisha mkewe kwa maana hata yeye anazidi kufurahishwa.”

Kwa hiyo shauri la Biblia linalosema tuwape wengine na kupendezwa nao linasaidia kuleta furaha, hata katika jambo hilo la unyumba.—Wafilipi 2:4.

25 Kutii shauri hilo kunatufaidi kwa njia nyingine pia. Maoni yetu kuhusu ngono, ambayo pia yanahusu uwezo wa kupitisha uhai, yanaweza kugeuza uhusiano wetu na Mungu, ambaye ndiye Mpaji-Uzima. Basi, ni hekima kuepuka uasherati na uzinzi, si kwa sababu tu tunapata faida za kimwili, za akilini na za moyoni, bali pia kwa sababu matendo hayo ni “dhambi juu ya Mungu.” (Mwanzo 39:9, NW) Na kwa habari ya kuepuka kumkosea mwenzi wa ndoa kwa kufanya uzinzi, Waebrania 13:4, NW, inasema hivi:

“Acheni ndoa iheshimike miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atahukumu waasherati na wazinzi.”

26 Tunapofikiria namna ngono inavyohusiana na furaha, tusiweke macho kwenye leo hii tu. Biblia imekusudiwa kutupatia hali njema ya milele kwa kutusaidia tufikirie matendo yetu yatakuwa na matokeo gani kwetu wenyewe na kwa wale wengine, kesho, mwaka kesho na maisha yetu yote.

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Kuna sababu gani sasa ya kufikiria shauri la Biblia juu ya ngono? (Mithali 2:6-12) (1-4)

Sababu gani ngono zinazidi kufanywa kabla ya ndoa? (5-7)

Maoni ya Mungu ni nini juu ya kufanya ngono kabla ya ndoa? (8)

Matokeo yanakuwa nini kwa kufanya ngono kabla ya ndoa? (9-12)

Wewe unaweza kutoa sababu gani nyingine za kuonyesha kwamba tunapaswa kuthamini mashauri ya Biblia juu ya ngono? (13, 14)

Ushuhuda unaonyesha nini juu ya shauri la Biblia kuhusu uzinzi? (15-18)

Biblia inatoa maelezo gani juu ya ngono katika mpango wa ndoa? (19-22)

Kufuata shauri hilo kunafaidi mtu kwa njia gani? (23-26)

[Sanduku katika ukurasa wa 70]

“Labda ule ‘uhuru wa kufanya ngono’ ulioanza majuzi ‘unafungua watu,’ . . . Lakini mambo ninayozidi kusikia, kila mahali, ni tofauti sana na hivyo. Mambo ninayozidi kusikia yanaonyesha kwamba kufanya ngono na mtu ye yote kunawatenda watu walio wengi jambo fulani. Kufanya ngono na mtu ye yote kunaumiza watu.”—Mwandikaji wa habari za magazetini, G. A Geyer, katika “The Oregonian.”

[Sanduku katika ukurasa wa 72]

“Uzinzi unaelekea kuleta hatia, maumivu, na kuoneana mashaka, na upande mwingine uaminifu unasitawisha hali ya kukaa bila wasiwasi na kuleta furaha nyingi sana.”—Dakt. C. B. Broderick, mkurugenzi wa kituo kinachohusu ndoa na mambo ya kijamaa.

[Picha katika ukurasa wa 69]

Mashauri ya Biblia yanasaidia watu wasipatwe na huzuni inayoletwa na uasherati—mimba zisizotakwa, magonjwa ya kaswende na kisonono

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki