Sura ya 18
Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?
1-3. Watu wengi ulimwenguni wanaonaje kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa?
MAHALI pengi leo kuna mkazo wenye nguvu wa kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa. Sana sana ulimwengu umepatwa na kipindi cha ngono. Gazeti New York Daily News lilieleza hivi: “Sasa ngono pasipo kufunga ndoa zinakubaliwa mahali pote na wazazi, vyuo vikuu na jamii ya watu. Sasa uasherati unaachiliwa sana kana kwamba ingekuwa kazi bure kuzuia hali mpya isiyozuilika.”
2 Watu wengi wanadai uhuru wa kufanya ngono na mtu ye yote wanayetaka na kufanya kwa vyo vyote. Maoni hayo yanawatia watu wengi wasiwasi. Msichana wa chuo kikuu anasimulia habari ya tatizo (gumu) wakati wa kutembea na mvulana: “Yeye [mvulana] alisema, Kwa nini kutofanya? Nikatumia nusu ya muda wa matembezi hayo nikijaribu kumweleza ubora wa adili. Baada ya hapo nikawa nikijiuliza mwenyewe hivi, Kwa nini kutofanya?” Labda wewe vilevile, umeuliza “Kwa nini kutofanya?” Je! kweli ni busara kutofanya ngono kabla ya kufunga ndoa?
3 Vijana wengi wanadhani kwamba inawafaa kufanya ngono kwa sababu miili yao inaweza kufanya ngono, tena inasemekana kwamba kuna ‘raha nyingi.’ Lakini inawafaa kweli? Je! yafaa kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa? Je! kunasaidia kufanya maisha yawe yenye kufaa?
MATOKEO MEMA AU MABAYA?
4-7. (a) Ni mambo gani ya kawaida yanayotokana na kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba uasherati si adili “mpya” hata kidogo? (Waamuzi 19:22-25; Yuda 7) (c) Kwa sababu gani shauri lililo katika 1 Wakorintho 6:18 ni la maana sana? (Matendo 15:28, 29; 1 Wathesalonike 4:3, 7, 8)
4 Namna gani vile wengine wanavyodai kwamba uhuru wa kufanya ngono unamletea mtu furaha kubwa zaidi na ‘raha nyingi’? Jarida (gazeti) The Journal of the American Medical Association lilisema juu ya uamuzi huu wa kijana aliyekuwa amefanya ngono na wasichana wengi kabla ya kufunga ndoa: “Nimepata kujua kwamba kufanya hivyo hakukuniletea furaha.” Wasichana hasa hawaoni sana furaha kutokana na kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa. Mwanachuo kijana aliyekuwa akitiririka machozi alisema haya baada ya kufanya ngono: “Haikufaa hata—sikuona raha wakati huo, tangu wakati huo nimekuwa na wasiwasi.”
5 Mara nyingi wasiwasi huo una sababu fulani. Akitaja sababu moja, bwana afya mmoja alisema kwamba ugonjwa wa kisonono ulikuwa karibu kupata sehemu ya 50 kwa mia ya vijana wa United States katika muda wa miaka mitano tu! Nao matabibu (waganga) wanasema kwamba dawa za kisasa zinashindwa kuzuia kuongezeka kwa magonjwa ya kisonono na kaswende, ambayo ndiyo magonjwa makubwa yanayotokana na ngono. Kwa kawaida watu wanajua wamepatwa na magonjwa hayo wakiwa wamechelewa mno wasiweze kuepuka uharibifu mkubwa wa miili yao usioweza kuponywa. Je! ni busara kupata hasara yote hii ya daima, labda hata kuwa kipofu au kuwa tasa, kwa sababu ya uasherati?
6 Vilevile, haikosi msichana kuchukua mimba. Mamilioni ya wasichana wasioolewa wanachukua mimba. Wengi wao wanapatwa na hatari na masikitiko ya kutoa mimba. Wengine wanalazimika kufunga ndoa na watu wasiowafurahia. Hali wengine bado wanaona tatizo la muda mrefu na lenye kusikitisha la kulea mtoto haramu. Hivyo ni vyepesi kuona kwamba dawa za kuzuia kutungwa mimba hazimpi msichana uhakikisho wa kwamba hawezi kupata mimba, ijapokuwa dawa hizo zinaendelea kupatikana kwa vyepesi zaidi kwa vijana.
7 Kwa kweli, hakuna jambo lo lote jipya au la “kisasa” juu ya uasherati. Umekuwapo kwa muda mrefu sana. Watu wa Sodoma na Gomora waliuzoea zamani yapata miaka 2,000 kabla ya Yesu Kristo kuzaliwa. Ukiisoma historia ya Utawala wa Rumi wa zamani utaona kwamba ulikuwa na sifa mbaya sana ya uasherati wa namna zote kama ule unaofanywa leo. Kwa kweli utawala huo ulianguka kwa sababu ya ufisadi. Bila shaka, ni jambo la hekima kuitii amri ya Biblia inayosema, “ikimbieni zinaa [uasherati].”—1 Wakorintho 6:18.
JE! UADILIFU (MWENENDO MWEMA) NI ISHARA YA UDHAIFU?
8-11. (a) Sababu gani kutofanya ngono kabla ya kufunga ndoa kunataka uhodari? (b) Kama inavyosimuliwa katika Mithali sura ya 7, ni nini linaloonyesha kwamba kijana mwanamume aliyejitia katika uasherati hakuwa na akili? (c) Kushikamana sana na kanuni njema upande wa msichana mdogo wa Shunemu kunaonyeshwaje mfano?
8 Walakini, huenda ukashawishwa ufanye uasherati na, ukikataa kufanya, huenda wengine wakakuambia kwamba wewe ni goigoi tu. Mahali pengine uasherati umekuwa mazoea yaliyokubaliwa. Matabibu wawili wakiandika katika Medical Aspects of Human Sexuality wanasema hivi: “Vijana wamejiona kuwa wenye hatia kwa kukataa kufanya ngono wakati mvulana au msichana anapokubali kufanya, na mara nyingine wanawake vijana wameonyesha aibu kwa vile bado wangali mabikira wakiwa na umri wa miaka 25.” Je! ni ishara ya udhaifu kukataa kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa? Basi, ni jambo gani linalotaka uhodari—kuvutwa na nyege au kujiweza?
9 Hakika, goigoi ye yote anavutwa na nyege. Lakini “mwanamume” hodari (au “mwanamke” hodari) ni yule anayezuia nyege hizo mpaka atakapofunga ndoa. Uhodari watakiwa hata zaidi sasa kwa sababu watu wengi duniani pote wanafanya uasherati.
10 Kitabu cha Biblia cha Mithali kinatoa masimulizi yanayoonyesha jambo hilo. Kinasimulia namna kijana asiye na akili anayetoka “katikati ya wajinga,” anavyozurura-zurura katika njia kuu ya mjini kisha anakutana na malaya. Kwa sababu ya kukazwa na maneno yake ya werevu na ya kushawishi, kijana analainika, “huyo [anafuatana] naye mara hiyo, kama vile ng’ombe aendavyo machinjoni; au mpumbavu kuadhibiwa katika pingu.” (Mithali 7:6-23) Hakuweza kupinga ubembe huo.
11 Lakini mwanzoni mwa kitabu hiki tulisema habari za msichana mdogo mrembo wa Shunemu aliyepinga mambo yote yenye kushawishi ambayo Mfalme Sulemani mwenye mali nyingi angeweza kutoa, akiona afadhali kushikamana na mchungaji kijana ambaye alitazamia kuloewa naye. Ndiyo, badala ya kuwa “mlango” ambao ungeweza kufunguka vyepesi, aliwahakikishia kaka zake kwamba alikuwa imara kama “ukuta” katika uthabiti wake wa moyo wa kuendelea kuwa bikira kwa ajili ya mwanamume ambaye alikuwa akitazamia.—Wimbo Ulio Bora 8:8-10.
SABABU GANI NI BUSARA KUTOFANYA NGONO KABLA YA KUFUNGA NDOA
12-14. (a) Sababu gani ni jambo la busara kufuata kanuni za Mungu juu ya ngono? (b) Ni jambo gani ambalo Waebrania 13:4 na 1 Wakorintho 6:9, 10 yanasema litawapata waasherati wakati ujao? Uasherati maana yake nini?
12 Sababu kubwa inayoonyesha kwamba ni jambo la busara kutofanya ngono kabla ya kufunga ndoa ni kwa vile imeandikwa hivyo na Yeye anayejua mengi juu ya furaha ya wanadamu, yaani, Yehova Mungu. Ebu lifikirie hilo. Kwa upendo Yehova Mungu amefanya mpango wa kupitisha uhai wa kibinadamu kwa njia ya kufanya ngono, na hili ni jambo la ajabu na takatifu sana. Sisi sote tumepokea faida zake, kwa sababu tunaishi. Ikiwa tunakubali kuzipokea faida zake, je! hilo halitupi wajibu wa kukubali maongozi ya Mungu ya namna mpango wote unavyopaswa kuwa? Bila shaka, kwa kuwa Yehova Mungu ndiye Mpaji-Uzima wetu, anayo haki ya kuweka sheria za mwenendo juu ya kutumia viungo vyetu vya uzazi pamoja na nguvu za kupitishia uhai.
13 Mungu anatuambia kupitia kwa mtume Paulo hivi: “Ndoa iheshimiwe na watu wote, na kitanda kisiwe na uchafu: kwa sababu Mungu atahukumu waasherati na wazini.” (Waebrania 13:4, ZSB) Uasherati si kufanya ngono ovyo-ovyo na mtu ye yote tu, bali unatia ndani pia kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa, kati ya watu waliochumbiana lakini hawajafunga ndoa.
14 Neno la Mungu linalaumu waziwazi sana uasherati na mwenendo mwingine wa upotovu. Linasema kwamba watu wanaozoea mambo hayo hawatakuwa na shirika katika ufalme wa Mungu. Biblia inasema hivi: “Hamujui ya kama wazalimu hawatariti ufalme wa Mungu? Musidanganywe: waasherati, wala wenye kuabudu sanamu, wala wazini, wala wakike, wala wafiraji, wala wizi, wala wenye tamaa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyanganyi hawatariti ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10, ZSB.
15-19. (a) Sababu gani imetupasa tuchukie sana uasherati? (Zaburi 97:10) (b) Ni nini linaloweza kutusaidia tusitawishe chuki hiyo inayofaa?
15 Kweli sheria ya Mungu inasema hivyo kwa mkazo kwa faida yetu. Nyege zaweza kuzidi nguvu sana, hata maishani mwa watu wengi nyakati zinatokea inapokuwa vyepesi kushindwa na kishawishi. Kama sheria ya Mungu haingesema jambo hilo waziwazi au kwa mkazo, bila shaka isingetusaidia sana nyakati hizo. Lakini inatusaidia tuwe na akili, tukaze uadilifu wetu na, zaidi, inatusaidia tujifunze kuuchukia mwendo mbaya kwa sababu iko wazi sana na ina mkazo. Je! kweli wauchukia mwendo wa uasherati? Sababu gani uuchukie?
16 Ikiwa nyakati nyingine mwendo huo unaonekana kuwa wenye kuvutia, jiulize hivi: ‘Je! ningetaka wale wa jamaa yangu mwenyewe, wazazi wangu au ndugu na dada zangu wafanye uasherati? Je! ningetaka wazae watoto haramu? Je! hii ingenifanya nizidi kuwapenda na kuwaheshimu?’ Ikiwa sivyo, wewe huoni inafaa kuchukia mwendo huo? Bila shaka hungetaka ufanye uasherati uwe kama taulo (kitambaa cha kupanguzia maji) la watu wote ambalo mwanamume ye yote au mwanamke ye yote anaweza kujipanguza mikono yake.
17 Namna gani watoto wanaozaliwa katika uasherati? Kama wewe msichana ungezaa mtoto wa uasherati, nani angemwangalia? Je! angeangaliwa na mama yako na baba yako? Au wewe mwenyewe ungemwangalia? Ungemwangaliaje? Naye mtoto akikua na kujua namna alivyochukuliwa mimba, angeonaje? Au kama ungekataa kutwaa daraka hilo ukampeleka mtoto huyo kwa watu wengine ili wamlee, je! watu wengine wangekufikiriaje? Wewe mwenyewe ungejionaje? Labda utajaribu kuficha ili ionekane kama hukuzaa, kisha umfiche mtoto kwa kumkabidhi kwa wenye kulea watoto na kwa njia hiyo ujaribu kuepuka aibu na daraka. Lakini huwezi hata kidogo kujiepa mwenyewe, sivyo?
18 Kama wewe mvulana ungekuwa baba ya mtoto haramu, je! dhamiri yako ingetulia? Ebu ifikirie taabu na aibu yote juu ya mama mtoto na mtoto mwenyewe. Bila shaka hilo ni jambo la kuepuka.
19 Hasa ni faida gani ambayo imepata kutokana na uasherati? Ni kwa sababu gani mambo mengi mabaya yanahusiana (yanakamatana) nao, kutia ndani na magonjwa yenye kulemaza ya kisonono na kaswende, kutoa mimba, mapigano yenye wivu hata mauaji? Ni kwa sababu gani mara nyingi talaka zinaongezeka zaidi sana katika nchi zinazotoa “uhuru” mkubwa wa kufanya ngono? Je! talaka inamaanisha kufanikiwa au inaonyesha kutofanikiwa? Je! ni ishara ya furaha ya kweli au ni ya huzuni na masikitiko?
20, 21. Kuepuka uasherati kunawezaje kukuongezea matumaini ya kufanikiwa katika ndoa?
20 Kwa upande mwingine, ni jambo la busara kutofanya ngono kabla ya kufunga ndoa kwa sababu wale wasiofanya ngono kabla ya kufunga ndoa ndio wanaoelekea sana kuwa na ndoa yenye kufanikiwa. Ni kwa sababu wameheshimu sana ndoa, wakiheshimu mpango wa Mungu na kuheshimu wachumba wao na haki waliyo nayo wote ya kupokea mwenzi aliye safi katika ndoa.
21 Kadiri unavyokuwa mwangalifu zaidi katika kuepuka mwenendo mpotovu au kuepuka kufanya ngono wakati wa uchumba, ndivyo utakavyoelekea zaidi kufanikiwa katika ndoa yako. Ndipo wewe wala mwenzi wako hatakuwa na mashaka yenye kusumbua juu ya kama upendo wako au upendo wake ni wa kweli kwa kudhani kwamba kusudi la kuoana lilikuwa ni ngono tu. Kwa maana ndoa si mwungano tu wa miili miwili, bali ni mwungano wa watu wawili. Ili ndoa ilete furaha inayodumu (ya milele), ni lazima kila mmoja amheshimu na kumpenda mtu huyo mwenzake.
KUFANYA CHAGUO LA HEKIMA
22-24. (a) Ni onyo gani ambalo msichana aweza kupata kutokana na masimulizi ya Biblia juu ya Amnoni na Tamari? (b) Ni nini linaloonyesha kwamba zile nyege zilizoonyeshwa na mke wa Potifa hazikuwa upendo unaodumu (wa milele)?
22 Upendo unaotegemea nyege peke yake si upendo unaodumu (wa milele). Ni upendo wenye choyo na pupa. Upendo wa namna hiyo unatolewa mfano katika Biblia juu ya mmojawapo wa wana wa Daudi, anayeitwa Amnoni. “Akampenda” Tamari, dada yake mrembo. Ndipo alipofanya hila akafanya ngono naye kwa nguvu. Halafu ikawaje? Habari inatuambia hivi: “Kisha Amnoni akamchukia machukio makuu sana; kwa kuwa machukio aliyomchukia yakawa makuu kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza.” Akamfukuza aende zake. (2 Samweli 13:1-19) Basi, ikiwa wewe ni msichana, utakuwa mpumbavu udhani kwamba mvulana fulani anakupenda sana kwa sababu anakutamani akitaka ufanye ngono naye? Huenda akageuka akawa kama Amnoni.
23 Biblia yatuambia kwamba mke wa Potifa, mkuu wa serikali ya Misri, alipendezwa namna iyo hiyo na kijana Yusufu, aliyekuwa mtumishi katika nyumba yao. Yusufu alipovikataa vishawishi vyake vyote, hapo ndipo mwanamke huyo alipoonyesha jinsi alivyokuwa hasa. Alimsingizia Yusufu vibaya sana kwa mumewe, akafanya afungwe gerezani isivyo haki.—Mwanzo 39:7-20.
24 Ndiyo, ule unaoitwa “uhuru” wa kufanya ngono unageuza jambo linalopaswa kuwa lenye kupendezeka na safi likawa ovyo na lenye kuchukiza. Basi, wewe wataka nini, raha ya muda ya kufanya ngono isiyo halali pamoja na hatari zote na matatizo (magumu) yote yanayotokana nayo, au furaha ya kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na watu wote, pamoja na kujiheshimu kila siku?
25, 26. Ni mambo gani yatakayotusaidia tuepuke kujitia katika uasherati? (Waefeso 5:3, 4; Wafilipi 4:8)
25 Ikiwa wataka uepuke uasherati, basi jiepushe na vitu vinavyoongoza huko: mazungumzo ambayo sikuzote yanakuwa juu ya wanaume na wanawake, vilevile kusoma vitabu au kutazama sinema ambazo kusudi lake moja tu ni kuamsha nyege. Kaza akili zako, macho yako na ulimi wako juu ya mambo safi yenye kufaa, ukiilenga miradi inayofaa inayoleta faida zinazodumu (zinazoendelea) na zisizoleta aibu wala masikitiko.
26 Zaidi ya yote, ongeza maarifa yako kisha uzidi kumthamini Muumba wako pamoja na mafaa na hekima ya njia zake. Mwendee katika sala na kukaza moyo wako juu ya mambo anayowaahidia wale wanaomtumikia. Ukitaka sana, unaweza kujiepusha usifanye ngono kabla ya kufunga ndoa, maana Yehova Mungu na Mwanawe watakupa nguvu unayohitaji ili ufanye hivyo.