Twaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?
“WATU WENGI walio hai leo watakuwa na fursa ya kuwa na maisha marefu zaidi. Hata hali ya kutokufa yaonekana ni kama yawezekana.”
“Mamilioni Walio Hai Sasa Huenda Wasife Kamwe.”
Tofauti ni nini kati ya taarifa mbili hizo? Ya kwanza ni taarifa ya Dakt. Lawrence E. Lamb, mwanasafu wa habari za tiba na profesa, iliyo katika kitabu chake Get Ready for Immortality, kilichochapishwa katika 1975. Ile ya pili ni kichwa cha mhadhara ambao ulifuatishwa kuwa kitabu kwa kutolewa na kutungwa na J. F. Rutherford, msimamizi wa pili wa Watch Tower Society. Mhadhara huo ulitolewa kwanza katika Los Angeles, Kalifornia, katika 1918.
Hata hivyo, taarifa hizo mbili ambazo zaonekana kuwa zafanana zilitofautiana sana katika fikira za kusababu mambo na utafiti ulioongoza kwazo. Maneno ya Dakt. Lamb ni mfano halisi wa wengi wa wale waitwao wasiokufa eti. Watu hawa huhisi kwamba maendeleo katika sayansi ya kitiba, kutia na utafiti juu ya kuzeeka, yatafumbua karibuni lile fumbo la sababu ya sisi kuzeeka na hatimaye yashinde kifo chenyewe. Hata hivyo, yajapokuwako mambo ambayo sayansi ya ki-siku-hizi imetimiza katika kurefusha tarajio la maisha ya wastani na katika kusaidia wengi waone shangwe ya maisha bora, matabiri ya kuwako hali ya kutokufa yamebaki hivyo hivyo yalivyo tu—mabashiri ya kutazamia mema.
J. F. Rutherford, kwa upande mwingine, hakuwa akifanya matabiri yenye msingi wa sayansi au tiba. Msingi wa zungumzio lake ulikuwa Biblia. Kwa njia ya unabii wa Biblia wenye kutimizwa alionyesha kwamba ulimwengu wa ainabinadamu ulikuwa umeingia katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Halafu akaelekeza kwenye lile tumaini lenye msingi wa Biblia kwamba kama vile Noa na jamaa yake walivyookoka mwisho wa ulimwengu katika siku yao, mamilioni wataokoka uharibifu wa ulimwengu huu waishi ndani ya ulimwengu mpya wenye uadilifu ili waone shangwe ya uhai wa milele katika dunia-paradiso.—Mathayo 24:37-39; Ufunuo 21:3, 4.
Kwa wengi wa wale walio kati ya wasikilizaji wake, hotuba ya Rutherford ilikuwa ya kugutusha. Hata leo, watu wengi huona maongeo juu ya kuishi milele duniani chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu kuwa yasiyo halisi na magumu kuaminiwa. (Zaburi 37:10, 11, 29) Lakini je! kweli mambo ambayo Biblia husema juu ya sababu ya sisi kuzeeka na kufa ni yasiyoaminika kwa kadiri hiyo? Kwa uhakika, Biblia husema nini juu ya habari hiyo?
Kafanywa Ili Kuishi, Si Kufa
Kwa kufaa, Biblia huanza kwa usimulizi wa mwanzo wa uhai wa kibinadamu. Katika sura ya kwanza ya Mwanzo, twasoma kwamba baada ya kuumba jozi ya kwanza ya kibinadamu, “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”—Mwanzo 1:28.
Ili jozi ya kwanza ya kibinadamu, Adamu na Hawa, itekeleze mgawo huo, hiyo ingemaanisha kwamba ingekuwa sharti waishi kwa muda mrefu sana, ndivyo na wazao wao. Lakini muda mrefu kadiri gani? Tuendeleapo kusoma katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo, hatuoni Adamu na Hawa wakiagiziwa urefu wowote wa maisha. Hata hivyo, kulikuwako sharti moja ambalo ingewalazimu kutimiza ikiwa walitaka waendelee kuishi. Mungu alisema hivi kwa Adamu: “Walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”—Mwanzo 2:17.
Hivyo, kifo kingewajilia ikiwa tu hawangetii amri ya Mungu. Au sivyo, walikuwa na tazamio la kuendelea kuishi kwa wakati usio dhahiri katika Paradiso hiyo ya kidunia yenye kuitwa Edeni. Kwa wazi, wanadamu walifanywa ili waishi, si kufa.
Hata hivyo usimulizi wa Mwanzo huendelea kueleza kwamba jozi ya kwanza ya kibinadamu ilichagua kupuuza amri ya Mungu iliyotaarifiwa wazi na kwa njia hiyo ikatenda dhambi. Mwendo wao wa kutotii uliwaletea wao, na baadaye wazao wao, laana kali ya kifo. Karne kadhaa baadaye, mtume Paulo alieleza hivi: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”—Warumi 5:12.
Sheria ya urithi ni ya kwamba Adamu na Hawa wangeweza kupitishia wazao wao kitu kile tu ambacho wao wenyewe walikuwa nacho. Wakiwa kama walivyoumbwa, walikuwa na uwezo wa kupitishia vizazi vya wakati ujao maisha makamilifu yasiyo na mwisho. Lakini kwa kuwa sasa maisha zao wenyewe zilikuwa zimeumbuliwa na dhambi na kifo, hawangeweza tena kurithisha urithi huo bora. Dhambi, kutokamilika, na kifo vimekuwa fungu la ainabinadamu yote muda wote wa tangu hapo, zijapokuwako jitihada za kurefusha muda wa maisha ya kibinadamu.
Katika maana fulani, hiyo yaweza kufananishwa na programu ya kompyuta ambamo mna kasoro, au kipingamizi. Kipingamizi hicho kisipotambulikana wazi na kusahihishwa, programu haitafanya kazi vizuri, na huenda matokeo yakawa yenye msiba. Mwanadamu hajaweza kutambua wazi, sembuse kusahihisha, kasoro ya urithi ambayo hutokea katika utendaji mbaya wa miili yetu ya kibinadamu, ikitokeza kuzeeka na kufa. Hata hivyo, Muumba wa binadamu, Yehova Mungu, amefanya mipango ya kuisahihisha. Utatuzi wake ni nini?
Mungu ameandaa uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Mwana wake, Yesu Kristo, “Adamu wa mwisho,” ambaye kwa njia hiyo huchukua mahali pa Adamu wa awali akiwa baba yetu na mpaji-uhai. Kwa hiyo, badala ya kulaaniwa vikali wafe wakiwa watoto wa Adamu mtenda dhambi, huenda wanadamu watiifu wakahesabiwa kuwa wastahili kupokea uhai wa milele wakiwa watoto wa “Baba wa milele,” Yesu Kristo. Yesu mwenyewe alieleza hivi: “Mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini [kujizoeza imani katika, NW] yeye, awe na uzima wa milele.”—1 Wakorintho 15:45; Isaya 9:6; Yohana 3:16; 6:40.
Kwenye umalizio wa huduma yake ya kidunia, katika sala kwa Baba yake wa kimbingu, Yesu Kristo alijulisha rasmi takwa la msingi la kupata thawabu hii bora ya uhai kwa kusema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.
“Kama Siku za Mti”
Ebu fikiria kupanda mbegu ya mti-sekwaya na kuutazama ukikua uwe na urefu wa meta nyingi angani, ukionea shangwe ukuzi wao muda wote mti huo uishipo. Halafu wazia ukiuona ukikua na kupanda mwingine maelfu ya miaka baadaye na halafu tena uonee shangwe ukuzi na uzuri wao.
Je! wazo la jinsi hiyo ni halisi? Kwa kweli ndivyo lilivyo, kwa maana msingi walo ni ahadi ya Muumba wa binadamu, Yehova Mungu, asemaye hivi: “Kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu.” (Isaya 65:22) Ahadi hii husaidia kujibu swali hili, Binadamu aweza kuishi muda mrefu kadiri gani? Jibu ni: kuendelea mpaka wakati ujao usio dhahiri, naam, milele hasa.—Zaburi 133:3.
Mwaliko unatolewa sasa, yaani: “Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” (Ufunuo 22:17) Huu ni mwaliko ambao Yehova Mungu anatolea wote wenye mioyo ya kufuata haki. Mwaliko huo ni wa kutumia kwa faida maandalizi ya kiroho ya Mungu kwa uhai wa milele katika dunia-paradiso.
Je! wewe utachagua kukubali mwaliko huo? Matazamio yako ya maisha marefu zaidi, uhai wa milele, hutegemea chaguo lako sasa!
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
TARAJIO LA MAISHA
Mtu aliyezaliwa mwishoni mwa karne ya 18 katika Amerika ya Kaskazini au Ulaya ya Magharibi angeweza kutarajia kuishi awe na umri wa miaka 35 au 40. Leo, katika United States wanaume wanaweza kutarajia kuishi karibu miaka 71 na wanawake 78, na usitawi kama huo umefanywa katika nchi nyinginezo. Tunang’amua zaidi uwezekano wa urefu wa maisha yetu. Lakini je! kuna mpaka fulani wa kadiri ambavyo tarajio la maisha laweza kurefushwa?
Hakuna mtu yeyote katika historia ya majuzi ambaye ameishi au ametarajia kuishi miaka 500, 300, au hata 200. Yajapokuwako maendeleo ya sayansi ya kitiba, tarajio la maisha leo lingali chini ya miaka 80. Hata hivyo kuna ripoti juu ya watu mmoja mmoja wenye kuishi kufikia umri wa miaka 140 au hata 150. Na nyakati za Biblia, watu waliishi wakawe na umri wa mamia ya miaka. Je! hiyo ni hadithi au hekaya tu?
Kwa kupendeza, The New Encyclopædia Britannica hutaarifu kwamba “muda hususa wa maisha ya kibinadamu haujulikani.” Kama vile kichapo hicho kielezavyo, ikichukuliwa kwamba mtu fulani aliishi akawa na miaka 150, “hakuna sababu halali ya kukataa uwezekano wa kwamba huenda mtu fulani mwingine akaishi miaka 150 na dakika moja. Na hiyo miaka 150 na dakika moja ikikubaliwa, kwa nini miaka 150 na dakika mbili isikubaliwe, na hivyo hivyo?” Kichapo hicho chaendelea kusema: “Kwa msingi wa maarifa yaliyopo juu ya urefu wa maisha, tarakimu hususa kabisa kwa muda wa maisha ya kibinadamu haiwezi kutolewa.”
Twaweza kukata shauri gani kutokana na hilo? Kwa usahili ni kwamba, msingi wa mambo ambayo sayansi ya kitiba imejifunza juu ya kuzeeka na kufa ni hali ya kibinadamu kama tuionavyo leo. Swali lililo la maana ni kama hali ya kibinadamu imekuwa hivyo hivyo sikuzote au kama itabakia hivyo hivyo sikuzote. Ahadi ya Mungu ni hii: “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya.” Katika ulimwengu mpya unaokaribia kasi, yeye “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4, 5.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
‘Mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ulikuwa ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu.’—Ufunuo 22:1