Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 10/22 uku. 10
  • Jinsi Unavyoweza Kuishi Milele

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Unavyoweza Kuishi Milele
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusudi la Mungu
  • Jinsi ya Kuishi Milele
  • Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kuishi Milele Si Ndoto Tu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Dunia?
    Mungu Anataka Tufanye Nini?
  • Twaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?
    Amkeni!—1990
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 10/22 uku. 10

Jinsi Unavyoweza Kuishi Milele

KWA kuwa mwili wa binadamu kwa wazi una uwezo wa kuishi maisha marefu zaidi kuliko yale waliyo nayo binadamu leo, wengine huweka tumaini lao katika sayansi igundue jinsi tunavyoweza kuishi milele. “Kadiri tupatavyo ujuzi kamili zaidi wa kemikali za mwili na jinsi zinavyoungana,” akaandika Dakt. Alvin Silverstein, “tutavumbua mambo yanayotatanisha ya uhai. Tutafahamu . . . jinsi mtu anavyozeeka.”

Kukiwa na matokeo gani? Itaongoza kwenye “muhula mpya katika historia ya binadamu,” akasema Silverstein. “Hakutakuwa tena na watu ‘wazee’ kwa kuwa ujuzi utakaoruhusu kushindwa kwa kifo utaleta pia ujana usio na mwisho.”

Je, binadamu watatimiza hilo? “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake,” yaonya Biblia. “Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:3, 4) Wanadamu wameshindwa kuonyesha, hata kushindwa kabisa kurekebisha kasoro ya kurithiwa ambayo hutokeza kuzeeka na kifo, kama tulivyoona. Ni Muumba wetu tu anayeweza kufanya hilo.

Hata hivyo, je, ni kusudi la Mungu kwelikweli kwamba binadamu waishi milele duniani?

Kusudi la Mungu

Yehova Mungu aliwaweka wapi mume na mke wa kwanza wa kibinadamu ili waishi? Ilikuwa katika paradiso ya kidunia. Na waliagizwa ‘wazaane na kuongezeka na kuijaza dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28) Ndiyo, kusudi la Mungu lilikuwa kwamba hatimaye, dunia yote ikaliwe na familia ya kibinadamu yenye uadilifu ikiishi pamoja kwa amani na furaha.—Isaya 45:18.

Ingawa hukumu ya kifo iliwekewa Adamu kwa sababu ya kutotii kwake, kusudi la Mungu la awali kwa binadamu kuishi milele katika Paradiso duniani halikubadilika. (Mwanzo 3:17-19) “Nimenena,” asema Mungu, “nami nitafanya.” (Isaya 46:11; 55:11) Mungu alionyesha kwamba kusudi lake kuhusu dunia halikuwa limebadilika aliposema hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.

Akiwa Muumba wetu, Mungu anaweza kurekebisha kasoro inayofanya binadamu wazeeke na kufa. Anafanya hilo kwa msingi gani? Kwa kuwa kasoro hiyo ilirithiwa kutoka mwanadamu wa kwanza, Adamu, Mungu ameandaa uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Mwana wake, Yesu Kristo kuwa dhabihu ya fidia, “ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16; Mathayo 20:28.

Kwa hiyo, Yesu Kristo, hasa, anachukua mahali pa Adamu wa awali akiwa baba yetu, au mpaji-uhai. Hiyo ndiyo sababu katika Biblia Yesu huitwa “Adamu wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:45) Kwa hiyo badala ya kuhukumiwa kifo wakiwa watoto wa mtenda-dhambi Adamu, binadamu watiifu wanaweza kuonwa kuwa wastahiki kupokea uhai udumuo milele wakiwa watoto wa “Baba [yao] wa Milele,” Yesu Kristo.—Isaya 9:6.

Bila shaka, “Mfalme wa umilele na “Baba yake Bwana wetu Yesu Kristo” ni Yehova Mungu. (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 15:3; Wakolosai 1:3) Licha ya Yesu Kristo kutolewa akiwa “Baba [yetu] wa Milele” na “Mwokozi,” yeye pia ni “Mwana-Mfalme wa Amani.” (Luka 2:11) Akiwa mwakilishi wa Baba yake, Kristo atatawala akiwa mwana mfalme ili kuleta amani duniani.—Zaburi 72:1-8; 110:1, 2; Waebrania 1:3, 4.

Chini ya utawala wa Yesu Kristo, Paradiso ya kidunia iliyopotea itapatikana tena. Yesu alisema hili litatokea wakati “Mwana wa Mtu atakapoketi katika kiti cha enzi cha utukufu wake katika ulimwengu mpya.” (Mathayo 19:28, HNWW) Wafuasi waaminifu wa Kristo—wote wakiwa 144,000—watatawala pamoja naye juu ya dunia iliyo Paradiso. (2 Timotheo 2:11, 12; Ufunuo 5:10; 14:1, 3) Mamilioni yatanufaika kutokana na utawala huo wa uadilifu kwa kufurahia maisha duniani katika Paradiso. Atakayekuwa miongoni mwao atakuwa yule mhalifu aliyekufa kando ya Yesu na ambaye Yesu alimwahidi hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:43, NW.

Hivyo, hata wafu wasio waadilifu watafufuliwa na kupewa fursa ya kustahili uhai udumuo milele duniani. (Matendo 24:15) Biblia hufafanua kwa njia nzuri sana kuondolewa kwa ugonjwa, kuzeeka, na kifo, isemapo hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.

Jinsi ya Kuishi Milele

Kwa kweli unataka kuwa miongoni mwa wale watakaorithi dunia na kukaa juu yake milele. Ikiwa ndivyo, ni lazima utimize matakwa ya kuishi milele katika Paradiso. Katika sala yake kwa Baba yake wa kimbingu, Yesu Kristo alitaja takwa la msingi, akisema: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kutwaa ujuzi huu wenye kutoa uhai. Waulize tu, nao, bila malipo yoyote, watakutembelea kwa wakati ufaao na kuzungumza nawe jinsi Mungu anavyokusudia kuinua jamii ya kibinadamu hadi ukamilifu wa kiroho na wa kimwili. Uwe na uhakika kwamba Muumba wetu mweza yote anaweza kurekebisha kikamili kasoro iliyorithiwa inayosababisha kuzeeka na kifo. Wakati unakuja, na uko karibu, ambapo maisha hayatakuwa mafupi mno tena. Yehova atabariki watu wake kwa “uhai usio na mwisho.”—Zaburi 133:3, HNWW.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Chini ya utawala wa mwana-mfalme, wa Kristo, kuzeeka na kifo zitashindwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki