Somo la 5
Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Dunia?
Kwa nini Yehova aliumba dunia? (1, 2)
Kwa nini dunia si paradiso sasa? (3)
Itakuwaje kwa watu waovu? (4)
Katika wakati ujao, Yesu atawafanyia nini wagonjwa? wazee-wazee? wafu? (5, 6)
Ili kushiriki katika baraka za wakati ujao, wewe wahitaji kufanya nini? (7)
1. Yehova aliumba dunia hii ili wanadamu waweze kufurahia kuishi juu yayo milele. Alitaka dunia ikaliwe sikuzote na watu waadilifu, wenye furaha. (Zaburi 115:16; Isaya 45:18) Dunia haitaharibiwa kamwe; itadumu milele.—Zaburi 104:5; Mhubiri 1:4.
2. Kabla ya Mungu kumfanya mwanadamu, Yeye alichagua sehemu ndogo moja ya dunia akaifanya iwe paradiso yenye kupendeza. Aliiita bustani ya Edeni. Hapa ndipo alipomweka mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa. Mungu aliwakusudia wawe na watoto na waijaze dunia nzima. Hatua kwa hatua wangalifanya dunia nzima iwe paradiso.—Mwanzo 1:28; 2:8, 15.
3. Adamu na Hawa walifanya dhambi kwa kuvunja sheria ya Mungu kimakusudi. Kwa hiyo Yehova aliwafukuza kutoka bustani ya Edeni. Paradiso ikapotezwa. (Mwanzo 3:1-6, 23) Lakini Yehova hakulisahau kusudi lake kuhusu dunia hii. Yeye aahidi kuifanya paradiso, ambako wanadamu wataishi milele. Yeye atafanyaje hivyo?—Zaburi 37:29.
4. Kabla ya dunia hii kuweza kuwa paradiso, ni lazima watu waovu waondolewe. (Zaburi 37:38) Hili litatendeka kwenye Har–Magedoni, ambayo ni vita ya Mungu ya kukomesha uovu. Halafu, Shetani atafungwa kwa miaka 1,000. Hili lamaanisha kwamba hakuna waovu watakaoachwa waiharibu dunia. Ni watu wa Mungu pekee watakaookoka.—Ufunuo 16:14, 16; 20:1-3.
5. Kisha Yesu Kristo atatawala akiwa Mfalme juu ya dunia hii kwa miaka 1,000. (Ufunuo 20:6) Yeye ataondoa dhambi kutoka katika akili na miili yetu hatua kwa hatua. Tutakuwa wanadamu wakamilifu kama vile Adamu na Hawa walivyokuwa kabla ya wao kufanya dhambi. Kisha hakutakuwa na ugonjwa, uzee, wala kifo tena. Watu wagonjwa wataponywa, na wazee watakuwa vijana tena.—Ayubu 33:25; Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4.
6. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu, wanadamu waaminifu watajitahidi kugeuza dunia nzima iwe paradiso. (Luka 23:43) Pia, mamilioni ya wafu watafufuliwa kwenye uhai wa kibinadamu duniani. (Matendo 24:15) Wakifanya yale ambayo Mungu ataka wafanye, wao wataendelea kuishi duniani milele. Wasipofanya hivyo, wataharibiwa milele.—Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:11-15.
7. Ndivyo kusudi la Mungu la kwanza kwa dunia litakavyofanikiwa. Je, ungependa kushiriki katika baraka hizo za wakati ujao? Ikiwa ndivyo, wewe wahitaji kuendelea kujifunza kumhusu Yehova na kuyatii matakwa yake. Kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu kutakusaidia ufanye hivyo.—Isaya 11:9; Waebrania 10:24, 25.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Paradiso iliyopotezwa
[Picha katika ukurasa wa 11]
Baada ya Har–Magedoni, dunia itafanywa iwe paradiso