Sehemu ya 5
Uhai Una Kusudi Tukufu
1 Jinsi ambavyo dunia na viumbe hai vilivyomo vilifanyizwa huonyesha kwamba Muumba wao ni Mungu wa upendo anayejali kwelikweli. Na Neno lake, Biblia, huonyesha kwamba yeye hujali; hilo hutupatia majibu bora kabisa kuhusu maswali: Kwa nini sisi tupo hapa duniani? na, Sisi tunaelekea wapi?
2 Tunahitaji kutafuta katika Biblia tupate majibu hayo. Neno la Mungu husema: “Mkimtafuta ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi.” (2 Mambo ya Nyakati 15:2) Kwa hiyo basi, jitihada ya kutafuta katika Neno la Mungu hufunua nini kuhusu kusudi lake kwetu sisi?
Sababu kwa Nini Mungu Aliumba Wanadamu
3 Biblia huonyesha kwamba Mungu aliitayarisha dunia akiwafikiria wanadamu kihususa. Isaya 45:18 husema kuhusu dunia kwamba Mungu “hakuiumba ukiwa [bila kusudi], aliiumba ili ikaliwe na watu.” Naye aliandalia dunia kila kitu ambacho watu wangehitaji, si ili waishi tu, bali ili kufurahia maisha kikamili.—Mwanzo, sura 1 na 2.
4 Katika Neno lake, Mungu husema juu ya kuumba wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, na afunua yale yaliyokuwa akilini mwake kwa ajili ya familia ya kibinadamu. Yeye alisema hivi: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi.” (Mwanzo 1:26) Wanadamu wangekuwa wasimamizi wa ‘dunia yote’ na viumbe wanyama vyayo.
5 Mungu alifanyiza shamba kubwa lililo kama bustani katika sehemu iitwayo Edeni, iliyo katika Mashariki ya Kati. Kisha “akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” Ilikuwa paradiso ambayo ilikuwa na kila kitu ambacho wanadamu wa kwanza wangehitaji kula. Na hiyo ilitia ndani “kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa,” kutia na mimea mingine na aina mbalimbali za wanyama wenye kupendeza.—Mwanzo 2:7-9, 15.
6 Miili ya wanadamu wa kwanza iliumbwa ikiwa mikamilifu, kwa hiyo wao hawangekuwa wagonjwa, kuwa wazee, au kufa. Wao pia walipewa sifa nyinginezo, kama vile ile ya uhuru wa kuchagua. Jinsi walivyofanyizwa inaelezwa kwenye Mwanzo 1:27: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, hatukuumbwa tukiwa na sifa za kimwili na za kiakili tu bali pia zile za kiadili na kiroho, na ili tuwe wenye furaha kwelikweli, lazima sifa hizo zitoshelezwe. Mungu angeandaa njia ya kutimizia mahitaji hayo kutia na uhitaji wa chakula, maji, na hewa. Kama vile Yesu Kristo alivyosema, “mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.”—Mathayo 4:4.
7 Zaidi ya hiyo, Mungu aliwapa watu wawili wa kwanza agizo zuri ajabu walipokuwa katika Edeni: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.” (Mwanzo 1:28) Kwa hiyo wangeweza kuzaa na kuwa na watoto wakamilifu. Na kadiri ambavyo idadi ya watu ingeongezeka, wangekuwa na kazi yenye kufurahisha ya kupanua mipaka ya eneo la Edeni ya paradiso ya awali iliyo kama bustani. Hatimaye, dunia nzima ingesitawishwa kuwa paradiso, ikikaliwa na watu wakamilifu, wenye furaha ambao wangeweza kuishi milele. Biblia hutufahamisha kwamba baada ya kuanzisha mambo hayo yote, “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.”—Mwanzo 1:31; ona pia Zaburi 118:17.
8 Ni wazi kwamba wanadamu walipaswa kuitumia dunia iliyotiishwa kwa manufaa yao. Lakini hilo lilipaswa lifanywe kwa njia ya kujiona wana daraka. Wanadamu walipaswa wawe wasimamizi wastahifu wa dunia, si wenye kuiharibu. Kuharibiwa kwa dunia tunakoona leo ni kinyume cha mapenzi ya Mungu, na wale wanaokushiriki wanafanya kinyume cha kusudi la uhai duniani. Itawapasa wapate adhabu kwa kufanya hivyo, kwa kuwa Biblia husema kwamba Mungu ‘atawaharibu hao waiharibuo dunia.’—Ufunuo 11:18.
Bado ni Kusudi la Mungu
9 Hivyo, tangu mwanzo lilikuwa kusudi la Mungu kwa familia kamilifu ya kibinadamu iishi milele duniani katika paradiso. Na bado hilo ndilo kusudi lake! Kusudi hilo litatimizwa bila kushindwa. Biblia husema: “BWANA [Yehova, NW] wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile [n]ilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.” “Nimenena, nami nitatekeleza, nimekusudia, nami nitafanya.”—Isaya 14:24; 46:11.
10 Yesu Kristo alisema kuhusu kusudi la Mungu la kurudisha paradiso duniani alipomwambia hivi mtu fulani aliyetaka kuwa na tumaini la wakati ujao: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW) Mtume Petro pia alisema juu ya ulimwengu mpya unaokuja alipotabiri hivi: “Tunatazamia mbingu mpya [mpango mpya wa kiserikali ukitawala kutoka mbinguni] na nchi mpya [jamii mpya ya kidunia], ambayo haki [uadilifu, NW] yakaa ndani yake.”—2 Petro 3:13.
11 Mtunga zaburi Daudi pia aliandika kuhusu ulimwengu mpya unaokuja na huo ungedumu muda gani. Yeye alitabiri hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Hiyo ndiyo sababu Yesu aliahidi hivi: “Heri [wenye furaha, NW] wenye upole, kwa kuwa wao watairithi nchi.”—Mathayo 5:5.
12 Hilo ni taraja tukufu kama nini, kuishi milele katika dunia-paradiso isiyo na uovu, uhalifu, magonjwa, huzuni, na maumivu yote! Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Neno la kiunabii la Mungu hufanya muhtasari wa kusudi hilo tukufu kwa kujulisha hivi: “Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Hicho chaongeza hivi: “Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.”—Ufunuo 21:4, 5.
13 Naam, Mungu ana kusudi tukufu akilini. Hilo litakuwa ulimwengu mpya wenye uadilifu, paradiso ya milele, iliyotabiriwa na Yule ambaye aweza na atafanya yale anayoahidi, kwa kuwa “maneno [yake] ni amini na kweli.”
[Maswali ya Funzo]
1, 2. Tunaweza kujuaje kwamba Mungu hutujali sisi, na tunapaswa tupate wapi majibu ya maswali juu ya uhai?
3. Kwa nini Mungu aliumba dunia?
4. Kwa nini Mungu aliumba wanadamu wa kwanza?
5. Wanadamu wa kwanza waliwekwa wapi?
6. Wanadamu waliumbwa wakiwa na sifa gani za kiakili na kimwili?
7. Watu wawili wa kwanza walipewa agizo gani?
8. Wanadamu walipaswa kutunzaje dunia?
9. Kwa nini tuna uhakika kwamba kusudi la Mungu litatimizwa?
10, 11. Yesu, Petro, na mtunga zaburi Daudi walisemaje juu ya Paradiso?
12, 13. Fanya muhtasari wa kusudi tukufu la Mungu kwa ainabinadamu.
[Picha katika ukurasa wa 20, 21]
Mungu alikusudia kwamba wanadamu waishi milele juu ya dunia-paradiso. Hilo bado ndilo kusudi lake
[Picha katika ukurasa wa 22]
Mwenye nyumba aweza kuwataka wapangaji wanaoharibu nyumba yake watoe hesabu