Je! Mwisho wa Uchafuzi U Karibu?
TAZAMIO la dunia safi lapendeza kweli kweli. Lakini je! ni la kihalisi? Ni ya kwamba, nchi fulani zinajaribu sana kuleta nafuu ya hali ihusuyo uchafuzi. Sasa upungufu wa uchafuzi wa hewa waripotiwa kwa sababu ya hatua kali za kudhibiti risasi iliyo katika vibomba vya kutolea moshi katika magari. Katika maeneo fulani, uchafuzi wa viwanda waonekana umepungua pia. Hata hivyo, hiyo haisababishwi sikuzote na hatua kali za udhibiti. Bali, nyakati fulani huwa ni tokeo la kuundwa upya kwa viwanda kwa sababu ya shida ya uchumi wa ulimwengu.
Dunia—Iliundwa Ijisafishe Yenyewe?
Kwa kuongezea, kuna taratibu za kiasili za usafishaji ambazo hufanya kazi. Kwa kielelezo, faitoplanktoni ni kimoja cha vitu vikuu ambavyo huzuia uchafuzi, kulingana na Dakt. Aubert wa Kitovu cha Tiba ya Viumbe wa bahari kuu katika Nice, Ufaransa. Vihai hivyo vidogo sana hutoa viuavijasumu ambavyo huharibu maambukizo. Ubaya ni kwamba, vihai hivyo vinazidiwa nguvu. Katika Italia, Venice na Bahari Adriati zinajawa sana na miani. Katika Bahari Adriati uchafuzi huo hutokeza “miani, [na] jelo inukayo yenye utelezi, ya kinjano, kihudhurungi, na kijivu, ambavyo huenea kusini kwa mamia ya kilometa” katika kiangazi. (The Globe and Mail, Toronto, Kanada) Jambo moja lenye kuchangia ni mitaro inayopitisha maji kutoka mto Po, “yenye kinyesi kibichi kutoka kwa watu zaidi ya milioni 15, takataka za kutoka viwanda vikubwa-vikubwa vingi vya Italia . . . na samadi ya nguruwe zaidi ya milioni tano.”
Namna gani uchafuzi wa udongo? Utafiti wa kampuni kubwa ya kemikali kwa kushirikiana na Idara ya United States ya Nishati ulifunua kuwapo kwa bakteria, kuvu, na amiba za namna nyingi katika ardhi, baadhi yazo zikifikia kiasi cha meta 260 chini ya ardhi. Dakt. David Balkwell wa Chuo Kikuu cha Mkoa wa Florida alieleza hivi: “Vihai hivi vya kina kirefu huenda hata vikawa vinatakasa mwamba-yavu [maji asili ya chini ardhini].” Ama, Dakt. Balkwell atumaini kwamba wahandisi wa kuunga chembe za urithi tabia wataweza kuchochea vihai hivi vya chini ya ardhi ‘viyeyushe vichafuzi fulani hususa.’
Ingawa hivyo, kwa uhakika ni lazima tukate shauri kwamba hali iliyopo haina dalili nzuri ya kwamba uchafu wa kihalisi wa dunia utamalizika mbio-mbio. Hata hivyo, twaweza kuwa na uhakika kwamba mwisho wa uchafuzi u karibu. Kwa nini?
Kuondoa Uchafuzi wa Kiadili
Ili sayari hii iwe makao safi kweli kweli kwa ajili ya ainabinadamu, ni lazima waakaji wayo wawe watu safi, kiadili na kimwili pia. Ni lazima wanadamu washinde ubinafsi wao wa msingi na wasitawishe sifa zisizo na ubinafsi, wakionyesha ufikirio kwa wanadamu wenzao na jirani zao wanyama. Je! hilo laweza kufanywa?
Muda wa miongo iliyopita, Mashahidi wa Yehova wamepata kwamba hilo laweza kufanywa. Wametahini nguvu za Biblia za kufinyanga utu, wakapata kwamba kitabu hicho kina nguvu za kubadili watu, kwa matokeo yenye mafaa juu ya mazingira. Kwa kielelezo, maofisa wa stediamu husisimukia utaratibu na usafi wa umati unaohudhuria mikusanyiko mikubwa ya Mashahidi wa Yehova. Elezo ambalo hutolewa mara nyingi ni kwamba ‘stediamu iliachwa ikiwa safi kuliko wakati ilipoingiwa na Mashahidi.’
Mshiriki wa wafanya kazi wa jengo-tata la michezo katika Lisbon, Ureno, alimweleza hivi mmoja wa Mashahidi wa Yehova: “Watu waniulizapo mimi naonaje juu yenu, siwezi kusema uwongo. Mimi huwaambia kwamba Mashahidi wa Yehova wana adabu njema sana, ni safi na hupanga mambo kitengenezo. . . . Mkichafua kitu kimoja, nyinyi husafisha 99!”
Usisitizo wa Mashahidi juu ya usafi wa kimwili wahusiana na kanuni zao bora za kiadili. Kanuni gani? Zile zilizopangiliwa katika Biblia, ambalo ni Neno la Mungu lililoandikwa. Kuhusu wenye kurudi nyuma, Biblia husema kwamba njia za Mungu ziko ‘juu kuliko njia zao, na mawazo yake kuliko mawazo yao.’ (Isaya 55:7-9) Hata hivyo, sisi twaweza kujifunza njia za Mungu kwa sababu Mungu mwenyewe hufanya sheria zake zipatikane kwa wale watakao kuishi kulingana nazo. Hii elimu ya kimungu ni muhimu kwa wakati ujao wetu.
Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova leo hujaribu kuishi kulingana na viwango hivi safi vya kiadili, nao hunufaika sana. Ingawa hivyo, kwa watu wengi hiyo imemaanisha kufanya mabadiliko makubwa katika mazoea na mitindo-maisha yao.
Dawa za Kulevya, Mapigo, na Ushindi
Chukua kisa cha Marie, mmoja wa familia ya washiriki 13 wa eneo lenye uhalifu mwingi katika jiji moja la Uingereza.
“Familia yetu ilijulikana sana kwa kuwa kali, nami nikiwa sawa na wenginewo wote, nilijulikana kuwa mchokozi. Nikiwa na miaka 15, mimba ilinitoka. Miaka miwili baadaye, binti yangu alizaliwa, nami nikaachwa nimtunze nikiwa peke yangu. Mvulana rafiki yangu alizuiliwa katika shule [ya kurekebisha tabia]. Alitoroka, nami nikashika mimba tena. Nilijaribu njia za aina zote ili kumaliza mimba hiyo na mwishowe nikafaulu, lakini karibu nipoteze uhai wangu.
“Mvulana rafiki yangu alianza kuvuta bangi na kuwa mwenye jeuri sana kwangu, hata ingawa nilikuwa na mimba tena. Mimi pia nikajihusisha, katika kulivuta gugu hilo na pia katika kuliuza. Kwa sasa niliishi katika nyumba iliyojaa malaya. Nilikuwa nikiwatunzia watoto wao.
“Nilipopendezwa na mvulana mwingine, mvulana rafiki yangu wa kwanza alikomesha uhusiano huo kwa kumdunga kisu mvulana huyo mwingine mara nane. Alikamatwa tena kwa sababu hiyo. Baada ya kufunguliwa kwake gerezani tulifunga ndoa na sote wawili tukaingilia tamasha ya dawa za kulevya kwa kishindo.”
Baada ya kuonana na Mashahidi wa Yehova na kujifunza nao Biblia, kijana huyu alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na badiliko likatokea pole kwa pole. Marie aeleza hivi:
“Mimi nilianza kung’amua kwamba uvutaji na utwaaji wa dawa za kulevya yalikuwa mambo mabaya. Baada ya mimi kumwambia mume wangu kwamba ningeacha yote hayo, yeye alikuwa akinipulizia usoni moshi wa sigareti yake ya bangi, akijaribu kunishawishi nirudie kutwaa dawa za kulevya. Nilishika mimba mara nyingine tena. Upesi baada ya hapo, mume wangu alianza kutorudi nyumbani usiku kucha.
“Miezi minane baadaye aliondoa vitu vyake vyote nyumbani na kuniacha. Nilisali kwa Yehova anisaidie kuvumilia hilo, naye akafanya hivyo. Halafu, baada ya miezi mitatu, mume wangu alirudi. Nilisali nipate imara ya kutenda yafaayo. Kwa mara nyingine nilijaribu kufanikisha ndoa yangu, lakini katika muda wa miezi sita nikawa nikiugua kutokana na nyuzi 14 nilizoshonwa kuzunguka jicho langu, likiwa ni tokeo la jeuri ya mume wangu; kipenzi chake cha kwanza kilikuwa kingali ni dawa za kulevya. Nyumba yetu ikawa ndilo bohari kuu la dawa za kulevya kwa eneo zima. Ilijaa ‘rafiki’ zake, wengi wao wakiwa walevi wa dawa za kulevya.
“Kwa msaada wa Yehova, nilijipa moyo mkuu nikawakabili wanaume hao. Niliwaomba kwa adabu waende nje ikiwa walitaka kuendelea kuvuta dawa zao za kulevya. Mume wangu aliposikia hilo, alikasirika, akaniita jikoni, akaanza kunigongesha kichwa ukutani. Mimi nilijikazania kumwambia nilihangaikia watoto na nilitaka kuwapa fursa ya kukua wakiwa katika mazingira safi, yenye hali njema. Mume wangu aliondoka kwa ghadhabu akawarudia rafiki zake. Nilingoja, nikisali. Aliingia jikoni tena, nikafikiri ataniua.
“Ingawa hivyo, tangu wakati huo mambo yalitulia sana. Baadaye tulihama. Wale wazoelevu wa dawa za kulevya walipokuja kuzuru, hawakuapa wala kuongea juu ya maisha zao zisizo za kiadili kama hapo kwanza. Ilionekana kwamba walikuwa na staha kwetu.”
Msimamo wa Marie upande wa maadili safi na maisha yasiyochafuzwa yaligusa moyo wa mume wake, na hatimaye yeye pia akajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Sasa wote wawili Marie na mume wake ni Mashahidi waliobatizwa na ni wenye shughuli wakisaidia wengine wasafishe maisha zao kwa msaada wa maarifa ya Biblia. Marie husema hivi:
“Nimsikiapo mume wangu akitoa sala, au nimsikiapo akieleza upendo wake kwa ajili ya Yehova, moyo wangu hudunda kama nini! Badiliko la sura yake hustaajabisha rafiki zake wa zamani. Sasa familia yetu imeungamana kweli kweli. Sijapata kamwe kuhisi nikiwa mwenye furaha jinsi hiyo, nami sijaacha kamwe kumshukuru Yehova kwa kutuondoa katika huu mfumo wa mambo uliochafuzwa.”
Mafanikio hayo katika kupambana na uchafuzi wa kiadili yafunua nguvu za Neno la Mungu. Zaidi ya hilo, yaonyesha tumaini la mwisho wa mapema kwa uchafuzi wa aina zote. Biblia yasema nini juu ya hilo?
Dunia Safi—Uhakika
Kuchunguza Biblia kwa uangalifu kwaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo wa mambo uliopo. (2 Timotheo 3:1-5) Hali ya mazingira ni sehemu moja tu ya kuthibitisha jambo hilo. Hiyo yamaanisha nini kuhusu tumaini letu la kuwa na dunia safi?
Yamaanisha kwamba karibuni Mungu ataingilia mambo ya kibinadamu. Karibuni atachukua hatua ya nguvu nyingi aondoe uchafuzi wote wa kiadili na kimwili kutoka kwenye sayari yetu. Katika kitabu cha Ufunuo yeye aahidi “kuwaangamiza wale wanaoangamiza dunia.”—Ufunuo 11:18, HNWW.
Kwa kweli, ni Mungu tu aliye na nguvu za kutokeza dunia safi isiyochafuzwa. Inasisimua kujua kwamba yeye akusudia kufanya hivyo hasa. Achukuapo hatua, hivi karibuni, itakuwa kama vile yeye mwenyewe asemavyo: “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya.” (Ufunuo 21:5) Halafu, mwishowe, sayari yetu itakuwa makao yenye kuwafaa watu safi wanyoofu, ambao wingi wayo utawapa shangwe milele.