Itikio la Wasomaji kwa Kitabu ”Young People Ask”
WENGINE walifikiri walikuwa tabaani. “Nilifikiri walitaka kutushauri juu ya mwenendo wetu,” akasema msichana mmoja mwenye miaka 15 aitwaye Shereda. Wengine walikuwa na wasiwasi tu. Mvulana mmoja Mwingereza mwenye miaka kumi aitwaye Timothy akumbuka hivi: “Nilipojua napaswa kuketi mbali na mama na baba, sikutaka kwenda.”
Ni nini kilichosababisha hangaiko hilo? Ni tangazo lililotolewa asubuhi ya Ijumaa ya 1989 “Ujitoaji Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehovaa kwamba vijana kati ya miaka 10 na 19 walipaswa kuketi katika kisehemu kilichowekwa kando. Woga wowote uliokuwapo ulitulizwa wakati kitabu Questions Young People Ask—Answers That Work kilipotolewa na kugawanywa bila malipo kwa vijana wote waliokuwapo. Maitikio yao yalikuwa nini? Yaliyofanywa ulimwenguni pote kuanzia Juni 1989.
“Nilikosa maneno ya kusema; machozi yakanitiririka usoni.”—Mike.
“Macho yangu yalikuwa na machozi nilipoona habari nzuri sana katika kitabu hiki. Uhakika wa kwamba tu kilikuwa ni zawadi iliyotolewa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kwa vijana ulikuwa ni kielelezo cha jinsi wanavyotujali sana.”—Margie, mwenye miaka kumi na minane.
Naomi mwenye miaka kumi, ambaye baba yake alikufa karibuni, alithamini hasa kupokea kitabu hicho. Yeye akumbuka hivi:
“Hilo ndilo kusanyiko kubwa la kwanza ambalo familia yetu ilienda pasipo baba yangu. Nilikuwa mwenye huzuni sana siku ya kwanza. Lakini ilinifurahisha kujua kwamba ndugu zetu na Baba yetu wa kimbingu, Yehova, wanatujali hadi tutakapompata tena baba yetu katika ulimwengu mpya.”
Kitabu hicho chazungumza, kwa namna iliyofupizwa, karibu nusu ya makala “Vijana Wauliza . . . ” ambazo zimetokea katika gazeti Amkeni! (Kiingereza) kuanzia 1982 hadi 1989. Kina sura 39, zilizopangwa katika vikundi-vikundi ikitegemea habari inayozungumzwa zikiwa ndani ya sehemu kumi. (Ona kisanduku ukurasa unaofuata.) Ni nini thamani ya kuwa na habari yote hiyo katika kitabu kimoja chenye kuchukulika? Kijana mmoja aeleza hivi: “Mara nyingi nilijua napaswa kuchunguza makala za ‘Vijana Wauliza . . . ’ zilizotangulia ili kunisaidia kwa tatizo, lakini nikawa sifikii kufanya hivyo kamwe. Sasa pana kichapo ninachoweza kuchukua wakati wowote ili nikitumie kuwa kiongozi.”
Kitabu Young People Ask pia kina uvutio wenye nguvu wa picha. “Mimi napenda picha zenye rangi nzuri,” asema Heather mwenye miaka 11. Picha hizo zaonyesha vijana kutoka ulimwenguni pote. Hivi ndivyo alivyosema kijana mmoja Mkanada: “Picha ni zenye kuvuta sana fikira na zawakilisha vizuri hisia zetu halisi tunapokabiliana na tatizo.” Basi, haishangazi sana kwamba vijana wengi walianza kusoma yaliyomo mara moja.
‘Sikuweza Kuacha Kukisoma’
Msichana mmoja mwenye miaka 17 aliandika, kwenye karatasi iliyotolewa na hoteli hivi:
“Tumemaliza nusu ya safari ya kwenda nyumbani kutoka mkusanyiko wetu na bado mbele yetu tuna saa nne za kusafiri kwa motokaa. Tayari nimesoma sura kumi.”
Wengine walinaswa na jedwali ya yaliyomo:
“Niliposoma jedwali ya yaliyomo, ilikuwa ni kama kutazama maisha yangu mwenyewe. Mengi sana ya maswali yalikuwa yale niliyokuwa nimejiuliza wakati mmoja au mwingine.”—Kathy mwenye miaka kumi na sita.
Hata wengine “wasio wasomaji” walivutwa:
“Mimi sipendi kusoma sana, lakini kitabu hiki ni kizuri sana hivi kwamba nianzapo kukisoma, siwezi kukiacha. Nimesoma karibu kitabu chote katika siku tatu.”—Jennifer mwenye miaka kumi na mitano.
“Mimi si msomaji mzuri sana na huwa sisomi sana. Baada ya kufika nyumbani kutoka kwa mkusanyiko, nilikuwa nimechoka na ilikuwa shida kuendelea kufungua macho yangu. Lakini nilifungua kurasa za kichapo hiki, nikaanza kusoma, na nikasoma sura nzima! Tangu wakati huo, nimesoma sura moja kila siku, hadi kufikia usiku huu—nimesoma mbili!”—Tiffany mwenye miaka kumi na saba.
Na kulikuwako wengine wenye kutia shaka:
“Nilidhani ningekuwa mwenye umri mkubwa zaidi nisisome sehemu fulani za kitabu hiki. Kwa hiyo nilianza kusoma Sehemu 6, ‘Ngono na Maadili.’ Hiyo ilinisaidia sana katika kufanya maamuzi fulani makubwa. Hakuna mtu aliye mwenye umri mkubwa sana asisome kitabu hiki.”—Sabrina mwenye miaka kumi na tisa.
Kwa kweli, baada ya kukimaliza, wengi huhisi kwamba kukisoma mara moja hakutoshi:
“Nilibatizwa mwaka mmoja uliopita, lakini mambo yakawa magumu, nami nikashuka moyo. Pindi moja hata nilitoroka nyumbani! Kwa hiyo nilipopokea kitabu hiki kipya, nilihisi kwamba Yehova alijua nilichohitaji hasa. Ni kizuri we! Tayari nimekisoma mara mbili.”—J.S.
“Ninaandika kila andiko neno kwa neno ndani ya kitabu ili iwe rahisi zaidi kwangu kusoma kitabu hiki nirudiapo mara ya pili. Bila kutia chumvi: Kitabu hiki kimenifanya kuwa mtu bora zaidi.”—Aida mwenye miaka kumi na minane.
‘Huhisi Kamwe Unaambiwa Upaswayo Kufanya’
Zaidi ya mwaka mmoja umepita tangu kutolewa kwa kitabu Young People Ask, lakini bado maelezo yenye uthamini yaendelea kupokewa. Bila shaka, kwa sehemu, sababu ya kufanikiwa ni kwamba ijapokuwa kimeelekezwa kwa vijana, kitabu hicho si cha kitoto; wala hakikuandikwa katika njia inayofanya wasomaji wacho wahisi kwamba wanahubiriwa. Vijana fulani wanalisema hilo hivi:
“Kitabu hiki hata kina ucheshi. Kikiwa chaungwa mkono na Neno la Mungu, Biblia, chafaa zaidi ya gazeti lolote la vijana.”
“Huhisi kamwe kwamba unaambiwa upaswayo kufanya; badala yake, unatahadharishwa juu ya uwezekano mbalimbali na matokeo ya kila mmoja. Daima maoni ya Yehova yanaonyeshwa waziwazi na kutegemezwa Kimaandiko.”
Wengi walionyesha uthamini kwa lugha iliyotumiwa kuandika na mwono-ndani kilioonyesha katika hisia zao.
“Baba yangu hajapata kunionyesha namna yoyote ya shauku, lakini shauri lililomo katika kitabu hiki lilionekana latoka kwa baba apendaye ambaye hutushauri kwa ajili ya faida yetu.”—Stefano, Italia.
“Hisia niliyopata mara moja ilikuwa ile ya kuongea na mtu fulani aliyenijua vizuri sana wala si ile ya kusoma kitabu.”—Myriam, Italia.
“Vielelezo vingi vilivyotumiwa vilifanana sana na nyumbani. Nilivielewa kabisa.”—Msichana kijana.
“Najua hakuna vijana kwenye Baraza Linaloongoza. Hata hivyo, yote mnayoandika juu ya vijana ni sahihi sana; ni kama kuongeleshwa na Yehova mwenyewe moja kwa moja.”—Aubree mwenye miaka kumi na mitano.
Si kwa Ajili ya Vijana Tu
Sura nyingi zatoa mwono-ndani katika matatizo wanayokabili Wakristo walio watu wazima, matatizo kama vile haya, kushuka moyo, upweke, na kukosa kuajiriwa. Basi, haishangazi watu wazima wengi wameonyesha uthamini pia kwa ajili ya kitabu hicho. Alisema hivi mke wa mhudumu asafiriye wa Mashahidi wa Yehova:
“Mume wangu nami hatuna watoto wowote wetu. Hata hivyo, niliona njia ambayo habari hiyo inatolewa ni yenye thamani kwetu pia. Kitabu hicho kingeweza kwa urahisi kuitwa ‘Maswali Ambayo Watu Wauliza—Majibu Yafanyayo Kazi!’”
Watu wazima wengine wakubali kwa moyo:
“Kuna matungo, vifungu vya maneno, na kanuni ambazo zimekuwa zenye faida sana kwa maisha yangu ya ujana ya miaka 41.”
“Hungeweza kufikiri kitabu kilichoandikwa kwa ajili ya vijana kingeweza kusaidia mwanamke wa miaka 61. Lakini kilinisaidia nifikiri kwa kufaa juu ya wakati uliopita na kuacha kinyongo ambacho nimekuwa nikifungia wazazi wangu.”
“Nilikuta kwamba ‘watu wa umri mkubwa zaidi huuliza’ pia. Hakuna chochote katika miaka mingi yangu nikiwa Mkristo kimepata kunisaidia nijielewe. Kama ilivyo, mimi ni kijana wa miaka 74.”
Pia barua zimepokewa kutoka wazazi wengi Wakristo:
“Nina vijana watatu, na kitabu hiki kilikuwa ni jibu kwa sala zangu. Asanteni kwa kuwa hapo kwa ajili yetu. Shetani ajaribu kila jambo kuvuta watoto wangu. Lakini sasa nimetayarishwa kufanya kwa ustadi yote niwezayo, shukrani kwa ajili ya kitabu hiki cha wakati ufaao.”
“Mfumo huu hutuchakaza siku kwa siku. Mtoto wangu mchanga zaidi ya wote ana miaka 12, na kupendezwa kwake na mambo ya kiroho kumeshambuliwa sana wakati wa mwaka mmoja uliopita. Siwezi kuwaambia jinsi ilivyo vizuri kuona kwamba anajitahidi kuelekea ubatizo likiwa ni tokeo la mkusanyiko na kitabu kipya hiki.”
“Machozi yalikuja machoni pangu watoto wangu walipopokea nakala zao. Hakuna matengenezo mengineyo ya kidini yanayojali vijana wao!”
“Mimi ni mzazi asiye na mwenzi, nami huhisi woga sana na kutostahili vya kutosha nyakati nyingine nikiwa mzazi. Mwana wangu aliye mkubwa wa wote ana miaka 11 na ana mwalimu asiyempenda. Ilifariji kama nini kuona sura katika kitabu Young People Ask iliyoshughulika na hali hiyo!”
Wengi walishuhudia juu ya kufaa sana kwa sehemu inayoitwa “Maswali kwa Ajili ya Mazungumzo” inayotokea mwishoni mwa kila sura:
“Sisi husoma kitabu hicho pamoja ikiwa sehemu ya kawaida ya funzo la Biblia la familia yetu. Kimetuvuta sote tukakaribiana. Naona kwamba watoto wanastareheshwa na maswali hayo, na kinasaidia kweli kweli kueleza hisia ambazo huenda zisiwe rahisi kuzieleza.”
Majibu Yafanyayo Kazi Kweli Kweli!
Bila shaka, uthibitisho wa thamani ya kitabu hiki si umaarufu wacho bali kuwa kwacho chenye kutumika. Kwa maneno mengine, je! majibu yacho yanafanya kazi kikweli? Vijana wengi wanahakikisha kwa shauku kwamba ndivyo:
“Kabla sijasoma kitabu hiki, nilikuwa nikijikokota tu kwenda kwenye Jumba la Ufalme pamoja na mama yangu na dada yangu kwa sababu singeweza kukaa nyumbani peke yangu. Nilikuwa nikiishi maisha maradufu. Sasa mambo hayo yote yamebadilika sana yakawa bora zaidi.”
“Waweza kuuacha ukweli, lakini huo haukuachi kamwe. Nikiwa na miaka 27, nilijaribu kurejea kwenye Jumba la Ufalme—nikiwa peke yangu, mwenye kuogopa, na mwenye kutubu. Nilikuwa na tabia mbaya sana na nilihisi kwamba Mungu hangeweza kunisamehe kamwe. Lakini dada mmoja mwenye umri mkubwa zaidi alinipa kitabu kipya Young People Ask. Nilipata kwamba kilizungumza juu ya matatizo yangu yote na kikaeleza jinsi ya kushughulika nayo. Nililia. Siwezi kueleza uthamini wangu wa kutosha kwa ajili ya kitabu hiki. Majibu yafanyayo kazi—kabisa!!!”
“Kitabu hicho kilinifanya nifikiri kwa uzito. Hapo kwanza sikujifikiria kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa na rafiki msichana. Nilikuwa nikitembea-tembea na watu wa ulimwengu. Hata nilikuwa nikiiba. Lakini baada ya kukisoma kitabu hiki, nikatambua nilikuwa nikifanya jambo lenye kosa maishani mwangu. Nilisali kwa Yehova kwamba anisamehe na nikamshukuru kwa kunipa kitabu hiki kipya kizuri.”
Huo ni mwonjo tu wa mamia ya barua zilizopokewa. Twatiwa moyo na kuchochewa sana na itikio zuri la nyinyi vijana. Ni wazi, mwataka kufanya yaliyo haki, nanyi mwathamini mwelekezo anaotoa Yehova kwa upendo katika Neno lake. Ni wazi pia kwamba majibu kutoka Neno la Mungu hufanya kazi kikweli!
Kwa hiyo mtafurahi sana kujua kwamba mfululizo wa “Vijana Wauliza . . . ” katika Amkeni! utaendelea kutoa ushauri timamu, wenye kutegemea Biblia juu ya habari zinazowahusu. Usikose makala hata moja! Na iwapo ungali hujafanya hivyo, soma—na usome tena—kichapo Questions Young People Ask—Answers That Work.b Kishiriki pamoja na wanadarasa wako. Fungua maandiko yaliyotajwa. Zungumza sura hizo pamoja na wazazi wako. Fuata shauri lacho. Na bila shaka utakubaliana na Kent mwenye miaka 16, aliyesema hivi: “Ni kama kuwa na kitabu cha mkononi cha kurejezea ili kunisaidia kuipitia ile miaka ya unyumbufu zaidi ya maisha yangu.”
[Maelezo ya Chini]
a Yaliyofanywa ulimwenguni pote kuanzia Juni 1989.
b Chapatikana kwa kuandikia watangazaji wa gazeti hili.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]
Yaliyomo
Sehemu 1
Upande wa Nyumbani:
Kushughulika na Washiriki wa Familia
Sura Ukurasa
1 11 Sababu Gani ‘Niheshimu Baba Yangu na Mama Yangu!?’
2 18 Mbona Wazazi Wangu Hawanielewi?
3 26 Niwafanyeje Wazazi Wangu Wanipe Uhuru Zaidi?
4 34 Kwa Nini Baba na Mama Waliachana?
5 42 Naweza Kushughulikiaje Kufungwa Upya kwa Ndoa ya Mzazi Wangu?
6 50 Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kusikilizana na Ndugu na Dada Yangu?
7 56 Je! Niondoke Nyumbani?
Sehemu 2
Wewe na Marika Wako
Sura Ukurasa
8 65 Naweza Kufanyaje Marafiki wa Kweli?
9 73 Naweza Kukabilianaje Na Msongo wa Marika?
Sehemu 3
Kuangalia Jinsi Unavyoonekana
Sura Ukurasa
10 82 Sura Ni ya Maana Kadiri Gani?
11 90 Je! Mavazi Yangu Yanifunua Nilivyo Hasa?
Sehemu 4
Kwa Nini Mimi Nahisi Hivi?
Sura Ukurasa
12 98 Kwa Nini Mimi Sijipendi?
13 104 Kwa Nini Ninashuka Moyo Sana?
14 115 Naweza Kufanyaje Upweke Wangu Uniondoke?
15 121 Kwa Nini Mimi ni Mwenye Haya Sana?
16 127 Je! Ni Kawaida Kuwa na Kihoro Kama Mimi?
Sehemu 5
Shule na Kazi
Sura Ukurasa
17 134 Je! Niache Shule?
18 140 Naweza Kufanyaje Maksi Zangu Ziwe Nzuri?
19 150 Kwa Nini Watoto Hawaniachi Tu?
20 158 Naweza Kusikilizanaje na Mwalimu Wangu?
21 166 Naweza Kupataje Kazi (na Kuidumisha!)?
22 174 Nichague Kazi-Maisha Gani?
Sehemu 6
Ngono na Maadili
Sura Ukurasa
23 181 Vipi Ngono Kabla ya Ndoa?
24 192 Naweza Kukataaje Ngono Kabla ya Ndoa?
25 198 Kupiga Punyeto —Kuna Uzito Gani?
26 205 Kupiga Punyeto—Naweza Kushindaje Hima Hiyo?
27 212 Haki—Je! Kweli Ndiyo Sera Bora Zaidi?
Sehemu 7
Urafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti, Upendo na Jinsia Tofauti
Sura Ukurasa
28 219 Naweza Kushindaje Upendo wa Kupumbazwa?
29 225 Je! Niko Tayari Kufanya Urafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti?
30 236 Je! Niko Tayari kwa Ajili ya Ndoa?
31 242 Nijueje Kama Ni Upendo Halisi?
32 252 Naweza Kufanikishaje Utafutaji wa Mapenzi?
Sehemu 8
Mtego wa Madawa ya Kulevya na Alkoholi
Sura Ukurasa
33 262 Kunywa—Kwa Nini Kutokunywa?
34 272 Kwa Nini Ukatae Madawa ya Kulevya?
Sehemu 9
Wasaa
Sura Ukurasa
35 283 Je! Haidhuru Hata Nisome Nini?
36 289 Naweza Kudhibitije Mazoea Yangu ya Kutazama TV?
37 296 Kwa Nini Nisijifurahishe Pindi Moja Moja?
Sehemu 10
Wakati Ujao Wako
Sura Ukurasa
38 305 Wakati Ujao Umeniwekea Nini?
39 311 Naweza Kumkaribiaje Mungu?
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Upande wa Nyumbani: “Dada yangu nami hugombana sikuzote. Lakini kitabu hiki kimenisaidia niwe mwema kwa dada yangu. Na iwapo tunagombana, sisi husema pole na kwamba hatukukusudia tuliyosema.”
“Nilikuwa nikifikiri kwamba dada yangu alipata kila kitu alichotaka, lakini sasa natambua nilikuwa namwonea wivu. Natambua, pia, kwamba wazazi wangu hawapendelei bali wanajaribu tu yote wawezayo ili kueneza upendo wao kotekote.”
“Ilinisaidia kujua kwamba mama na baba yangu hawakuachana kwa sababu yangu.”
Wewe na Marika Wako: “Ilinisaidia kuelewa kwamba nikitaka rafiki, lazima mimi niwe mmoja. Pia, nilijifunza kutotembea-tembea na watoto ambao ni mashirika mabaya.”
Kuangalia Jinsi Unavyoonekana: “Nilidhani nilikuwa na uzani mkubwa mno, nami nikawa karibu sili kitu kwa siku nyingi. Lakini ningekula mno siku iliyofuata na kuongeza uzani tena. Nikaamua kuwa nilikuwa mwenye sura mbaya na asiyevutia. Rafiki mpendwa mmoja aliniambia niisome ile sehemu juu ya ‘sura.’ Machozi yalitiririka usoni pangu nilipoisoma. Sasa nimejua mambo yangu yaliyo ya kutangulizwa, nami nakaza fikira juu ya utumishi kwa Mungu—si ninavyoonekana.”
Kwa Nini Mimi Nahisi Hivi?: “Nilishuka moyo sana, kufikia hatua ya kuwa na mawazo yenye nguvu sana ya kujiua. Sasa nimeanza kujaribu kukabili hofu zangu na nimepokea msaada wa kitaalamu. Nilitulia sana kusoma kutakuwako na mwisho wa hili ‘ogofyo la daima.’”
Shule na Kazi: “Nimekuwa nikitatizwa na maksi zangu na kuchokozwa-chokozwa shuleni. Napanga kutumia shauri hilo shuleni.”
Ngono na Maadili: “Kuna misongo mingi inayowekelewa vijana ili wafanye mabaya, lakini kwa kutumia kanuni za Biblia, naweza kupinga marika wangu.”
“Nina tatizo la kupiga punyeto, nalo lanihuzunisha sana. Lakini nitafanya jitihada kubwa ya kutumia shauri hili na kujaribu kuwa kijana bora zaidi niwezaye kuwa kwa Baba yangu wa kimbingu.”
Urafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti, Upendo, na Jinsia Tofauti: “Nimekuwa na upendo wa kupumbazwa kuelekea msichana mmoja kwa wakati fulani sasa. Sifanyi upumbavu wala kujiaibisha mbele yake. Hata hivyo, nilikuwa na zile hisia mlizoeleza. Kitabu hiki kilinisaidia nitambue hiyo ilikuwa ni shauku ya kipumbavu na kwamba bado sikuwa na umri wa kutosha kutafuta mapenzi.”
Mtego wa Madawa ya Kulevya na Alkoholi: “Mimi ni mpya katika shule ya upili, na tayari wamenipa madawa ya kulevya. Kitabu hiki hunisaidia kukataa.”
Wasaa: “Nilikuwa nikitazama TV Jumatatu hadi Ijumaa. Kitabu hiki kilinisaidia nipunguze utazamaji wangu wa TV—kuwa Jumapili na Ijumaa peke yake!”
Wakati Ujao Wako: “Nilikuwa nikifikiri kwamba Biblia ilikuwa yenye kuchosha—lakini sivyo tena! Mimi hujaribu kuisoma dakika 15 kila siku!”
“Imenisaidia sana katika sala zangu. Sasa naweza kuongea na Yehova kama vile rafiki wa karibu sana.”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Kikundi cha vijana kutoka Ufaransa kilipeleka picha hii
(kulia) kuwa wonyesho wa ‘ulinzi na tegemezo lenye upendo’ la Yehova na tengenezo lake katika kutoa kitabu Young People Ask