Saidia Wengine Wajifunze Juu ya Yule Mtu Mkuu Zaidi
1 Wengi ambao wamesoma kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi wameonyesha uthamini wa moyo mweupe juu ya matokeo ambayo kimefanyia maisha zao. Mtu mmoja aliandika hivi: “Nilipofika mwisho wa kitabu hicho, nilihisi kana kwamba nimekaribishwa na Yesu kushirikiana naye, kuishi kando yake, kushiriki mateso yake, hisia-moyo zake, kila upande wa huduma yake. . . . Kukisoma kitabu hicho ni kama kutazama sinema ya maisha ya Yesu.”
2 Kile kitabu Mtu Mkuu Zaidi kinatusaidia tufahamiane vizuri zaidi si na Yesu tu bali pia na Yehova. (Yn. 14:9) Mtoto mmoja wa umri wa miaka 12 alisema hivi kuhusu kitabu hiki: “Kilinifariji sana hivi kwamba nikasali kwa Yehova nikiwa na machozi ya shangwe mara tu nilipokisoma. Ndani yangu kabisa, nilihakikishiwa kujua kwamba Yehova na Yesu wanatuangalia.” Yesu alisema, kama ilivyorekodiwa kwenye Yohana 17:3, kwamba uhai wa milele wamaanisha sisi kumjua Yehova na Mwana wake. Kujifunza kitabu hiki kuhusu maisha ya Yesu kwatupatia mwono-ndani wa kipekee wa utu wa Yehova kwa sababu Yesu “ni chapa ya nafsi yake.”—Ebr. 1:3.
3 Zaidi ya nakala milioni 19 za kitabu Mtu Mkuu Zaidi zimechapwa katika lugha zaidi ya 70. Hilo laonyesha jinsi hicho kitabu kinavyopokelewa vema. Wengi walikisoma kitabu chote kizima mara baada ya kukipokea. Mtu mmoja mwenye kupendezwa alikisoma kwa majuma mawili baada ya kukipata. Kasisi aliyepokea kitabu hicho alisema: “Siwezi kukiweka chini kitabu hicho. Mke wangu na mimi hukisoma kila usiku kabla ya kwenda kulala.”
4 Ushahidi wa Vivi-Hivi: Ndugu mmoja alionyesha watu wa mahali pake pa kazi kitabu Mtu Mkuu Zaidi. Fununu zilienea kwamba alikuwa na kitabu hiki, na ripoti zikaenea kuhusu habari kilichokuwa nazo. Wafanyakazi wenzake wakampa orodha ya wale waliotaka nakala moja. Aliangusha vitabu 461! Watano kati ya wale waliokipokea wanajifunza. Dada mmoja, alipokuwa akisafiri kwa ndege, alimwangushia kitabu Mtu Mkuu Zaidi kasisi mmoja aliyekuwa akienda kuhudhuria kuwekewa mikono kwa kardinali mpya. Kasisi huyo amekuwa kwenye Vatikani kwa miaka 40. Sisi sote twapaswa kutumia ifaavyo fursa za kukipendekeza kitabu hiki kwa wengine.
5 Vijana Wanakithamini: Vijana wanaonyesha kupendezwa kwingi na hicho kitabu. Kijana mmoja wa miaka tisa aliandika: “Kichapo changu nikipendacho sana ni Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi kwa sababu ninajifunza mengi kutokana nacho.” Tukutapo vijana katika utumishi wa shambani, kama wazazi wao wanakubali, twapaswa kutumia wakati kuwaonyesha vijana kitabu hicho na kupitia baadhi ya mambo yacho makuu na picha zacho. Huenda tukaweza kuwaangushia vijana hao vitabu. Vijana wakipewa fursa ya kujua juu ya Yesu leo, wanaweza kufungamanishwa kwake. Yesu alikuwa mtu anayeweza kufikiwa.—Mt. 19:14, 15.
6 Kusoma kitabu Mtu Mkuu Zaidi kwaweza kubadili maisha za watu. Jaribu kuwajulisha watu wengi uwezavyo yaliyomo katika kitabu hicho. Tumia habari iliyo kwenye ukurasa wa mwisho wa utangulizi wa kitabu hicho, chini ya kichwa kidogo “Faidika kwa Kujifunza Juu Yake.” Habari hii itasaidia watu wakazie fikira juu ya wanaloweza kupata kwa kusoma kitabu hicho. Huenda wengi katika eneo lenu wakapaaza sauti ya mshangao kama alivyofanya mtu mmoja baada ya kusoma kitabu hicho: “Ndicho kitabu kizuri zaidi ambacho nimepata kukisoma! Kilibadili maisha yangu.”