Kitabu Kipya Chawasisimua Mamilioni
SEHEMU moja ya Mikusanyiko “Wapendao Uhuru” iliyoanza Juni uliopita ilikuwa ile hotuba “Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.” Jambo kuu layo lilikuwa kutolewa kwa kitabu chenye kichwa hicho hicho. Watu zaidi ya milioni sita ulimwenguni pote tayari wamehudhuria mfululizo huo wa mikusanyiko na kuisikia hotuba hiyo, inayotokea ikiwa na mabadiliko machache katika makala mbili za gazeti hili zinazotangulia makala hii.
Nakala zaidi ya milioni 12 za kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi zimechapwa katika lugha 60 hivi. Kinapatikana hata katika lugha za Ulaya Mashariki za Kialbania, Kikroashia, Kihungari, Kimakedonia, Kipolandi, Kirusi, Kiserbia, na Kislovenia. Wale zaidi ya 74,000 waliohudhuria mikusanyiko saba katika Urusi walipendezwa hasa kukipokea katika lugha ya Kirusi.
Chanzo cha Kitabu Hicho
Habari iliyo katika kitabu hicho ilikuwa imetokea katika namna ya mfululizo katika matoleo 149 yenye kufuatana ya Mnara wa Mlinzi, kuanzia toleo la Agosti 1 1985. Wasomaji wengi walisema kwamba walihuzunika wakati mfululizo huo ulipoisha kwa toleo la Juni 1, 1991. Melissa, mwenye umri wa miaka 12 katika Italia, alikuwa na machozi machoni pake aliposoma usimulizi wa mwisho katika Mnara wa Mlinzi. “Usiku kabla ya mkusanyiko wetu,” akasema, “Nilisali kwa Yehova nikimwomba kitabu kuhusu maisha ya Yesu. Kitabu hicho kilipotolewa, nilipiga makofi mpaka nikashindwa kupiga zaidi.”
Habari iliyotolewa kwa mfululizo katika Mnara wa Mlinzi ilihaririwa na kuingizwa katika kitabu kipya chenye picha zenye kupendeza cha kurasa 448 na sura 133. Jitihadi ilifanywa ili kutokeza kila hotuba ambayo Yesu alitoa na kila tukio lililorekodiwa katika maisha yake ya kidunia, kutia na mifano na miujiza yake yote. Kwa kadiri iwezekanavyo, kila jambo linasimuliwa katika taratibu ambalo lilitukia. Kwenye mwisho wa kila sura kuna orodha ya maandiko ya Biblia ambayo ndiyo msingi wa sura hiyo.
Mtu huenda akawa akifikiri, ‘Nimekwisha kusoma kitabu hicho kwa sababu nilisoma mfufulizo katika Mnara wa Mlinzi.’ Lakini wasomaji wa Mnara walipokea usimulizi wa maisha ya Yesu katika vipande vidogo vilivyotolewa katika makala zenye kutokea kila majuma mawili katika kipindi cha miaka zaidi ya sita. Hata ingawa makala hizo zilikuwa zenye kuarifu katika namna ya mfululizo, ebu fikiria ule msisimuko wa kusoma usimulizi huo wote katika wakati mfupi na kuona picha nzima ya yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi!
Chenye Kuimarisha Imani
“Nilimaliza kusoma kichapo hicho katika muda wa majuma mawili,” aripoti mwanamke mmoja kutoka Washington, D.C., U.S.A. “Nilipokuwa nikikisoma, machozi yalikuwa yakitiririka kutoka macho yangu. Nilikuwa nikiacha kusoma na kusali na kulia. Kilinifanya nihisi kana kwamba nilikuwa huko huko pamoja na Yesu, nikiteseka pamoja naye. Hata juma moja baada ya kukisoma kitabu hicho, machozi yalikuwa bado yakitoka machoni pangu nilipofikiria yale ambayo nilikuwa nimesoma. Nahisi nikiwa hata karibu zaidi na Yehova kwa ajili ya kule kutoa kwake Mwana wake.”
“Nilimaliza kile kitabu kuhusu Yesu leo,” mwanamke mmoja kutoka Pittsburgh, Pennsylvania, U.S.A., akaandika. “Kilikuwa kizuri ajabu. Nilikuwa na machozi machoni pangu nilipokuwa nikisoma sura chache za mwisho. Kukisoma kitabu hicho mfululizo kulikuwa jambo zuri sana. Siwezi kueleza kweli kweli jinsi ninavyohisi juu yacho—ni kwamba tu nilikipenda sana sana!”
Picha zenye kupendeza katika kitabu hicho zinachangia kuvutia hisia za mtu, kama vile msomaji mwenye uthamini aandikavyo: “Kinanifanya nihisi kana kwamba naweza karibu sana kusikia wakilia juu ya mtoto ambaye amekufa (sura 47) au kwamba twajua lile ambalo Yesu alikuwa akifikiria wakati mwanamke mwenye mtiririko wa damu alipomgusa na kuponywa (sura 46). Nyuso zao zaonyesha hisia sana hivi kwamba zatia uchungu. . . . Badala ya kusoma kuwe kazi ngumu, kitabu hiki hukufanya kuwe kama kitumbuizo zaidi au kuwe jambo lenye kupendeza mwisho mwa siku yangu. Namna kitabu hicho kilivyoandikwa kwa njia ya kuonyesha mielekeo na hisia haitoi habari tu juu ya lile ambalo Yesu alifanya bali pia yatuonyesha kwa ufupi lile alifikiria na kuhisi.”
Matumizi Yacho Mbalimbali
Wengi wameanza kukitumia kitabu hicho katika funzo la Biblia lao la familia. “Tuna watoto wachanga watatu,” wazazi kutoka Silverton, Oregon, U.S.A., waandika, “na kitabu hiki kinafaa kabisa kwa ajili ya ‘funzo letu la familia la kila usiku.’ Kwa kweli, inafaa kama nini kwamba tusome kwa uangalifu malezi ya Mfalme wetu mwenye upendo, Kristo Yesu.”
Tineja mmoja kutoka Japani aeleza hivi: “Baba yangu amekuwa akitusomea tunapokuwa tukipumzika baada ya chakula chetu cha jioni. Tukiwa familia, tunasoma kutoka mwanzo, lakini niliamua kusoma sura moja kila usiku kutoka mwisho wa kitabu kabla ya kulala usingizi. Hata hivyo, kitabu hicho chasisimua sana hivi kwamba mara nyingi inafika saa saba za usiku kabla sijatambua ni saa ngapi.”
Wengi wanashangaa juu ya wingi wa mambo madogo madogo yaliyotiwa ndani ya masimulizi hayo. “Nilijifunza mambo mengi sana ambayo sikuwa nimejua hata kidogo,” Shahidi mmoja akaandika. Barua kutoka California, U.S.A., ilisema hivi: “Mke wangu na mimi tumekuwa katika kweli kwa muda wa zaidi ya miaka 35, na twaweza kusema kwa unyofu kwamba hatujapata kuwa na kichapo ambacho kimekuwa chenye kusisimua sana kama hiki.”
Kitabu hicho chapasa kusaidia kukomesha ule uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova hawamwamini Yesu. Msomaji mmoja mwenye shukrani alieleza hivi: “Sikuweza kukiweka chini, kwani kilikuwa mkanyo mkubwa zaidi kwa ukosefu wa maarifa wa wale wasemao kwamba watu wa Yehova hawamwamini au kumheshimu Yesu Kristo. Jambo tu tupaswalo kufanya sasa ni kuwapa jibu hili kwa ukosefu wa maarifa wao.”
Kwa hakika kitabu hicho kitakuwa na mahali pa maana katika huduma ya Mashahidi wa Yehova. “Nilimpa mwanamke mmoja ninayejifunza Biblia naye nakala moja yacho,” akaandika Shahidi mmoja, “jinsi ambavyo kimemwathiri ni kana kwamba ni muujiza. Amekuwa akijifunza kwa muda wa mwaka mmoja, na nimekuwa na tatizo la kumfanya ahudhurie mikutano.” Mwanafunzi huyo aliposoma sura 45 za kitabu hicho kipya, Shahidi alieleza, “aliniambia kwamba angekuja kwenye mkutano Jumapili kwa sababu wakati ulikuwa umewadia wa kuchukua msimamo wake.”
Sehemu Zenye Thamani
Kwa kweli, Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi huandaa mafafanuzi juu ya zile Gospeli. Maelezo juu ya mambo mengi ambayo Yesu alisema na kufundisha yanaandaliwa, kwa hiyo kitabu hicho chaweza kutumiwa kuwa chombo cha uchunguzi chenye thamani, kwa kuwa kinashikamana kwa ukaribu na masimulizi ya Biblia.
Sehemu zuri hasa ni kwamba kwa msingi kila jambo linasimuliwa katika utaratibu wa wakati lilipotukia. Kugeuza kurasa tu kwa kukumbuka hilo kwaweza kuthibitika kuwa msaada wa kweli katika kutambulisha wakati mambo fulani yalipotukia, wakati wa huduma ya Yesu. Wasomaji wa zile Gospeli mara nyingi hukabili mambo yanayoonekana kupingana. Kitabu hicho kipya, bila uhitaji wa kuvuta fikira kwenye mambo hayo, huyapatanisha katika utoaji wacho.
Tukiwa Wakristo, kwa hakika hatupaswi kuacha funzo la uangalifu juu ya maisha ya Mfano wetu mwaminifu, Yesu Kristo. Kwa hiyo, acheni tufikirie kwa uangalifu masimulizi ya zile Gospeli tukiwa na msaada wa kitabu hiki kipya Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.