Kitabu Kinachosaidia Watu
KAZI iliyo kuu ya wanafunzi wa Kristo ni kufundisha wengine habari za Mungu na makusudi yake. (Mt. 28:10, 20; Matendo 1:8) Tangu kutolewa kwake mwaka wa 1978, kitabu My Book of Bible Stories kimekuwa msaada mkubwa sana katika kuifanya kazi hii. Kitabu hiki ni muhtasari ya Biblia iliyotolewa kwa usemi ulio mwepesi kufahamika. Picha zacho nyingi, zilizo kubwa na zenye rangi nzuri zinasaidia kwa njia bora zikiwa misaada ya kufundishia. Maono yafuatayo kutoka Berlin ya Magharibi yanaonyesha jinsi kitabu hiki kimekuwa chombo cha kusaidia watu.
“Kwa muda fulani tulinunua samaki sokoni kwa mume na mke vijana waliooana, wenye urafiki. Mara nyingi tulizungumza nao, hasa kwa sababu mwanamke huyo kijana alikuwa akitazamia kujifungua kitoto na sisi tuna mwana mdogo. Novemba 1979 kitoto chao kilizaliwa kisha sisi tukawapa kama zawadi nakala ya kitabu My Book of Bible Stories. Tuliandika maneno machache ya kuwatia moyo, tukawaomba wakichunguze wao wenyewe pia badala ya kumsomea mwana wao peke yake. Tukawaambia kitabu hicho kilieleza habari za Biblia kwa maneno yenye kufahamika kwa wepesi, na kwamba Biblia peke yake ndiyo inayoweza kutupa tumaini zuri ajabu kwa wakati ujao.
“Miezi miwili baadaye duka lao la samaki halikuonekana tena sokoni. Siku ya soko iliyofuata lilikuwapo tena nami nikauliza kama jamaa walikuwa wamekuwa wagonjwa. Mwanamume huyo akasema: ‘Wewe ulitupa sisi kitabu hicho, sivyo? Kwa kweli ulifanya jambo fulani lianze kutendeka.’ Halafu akaeleza kwamba wangeliacha duka lao la samaki kwa sababu ni vigumu sana mtu kuieleza ukweli afisi ya kodi ya mapato akiwa katika biashara hiyo. Baadaye tukajua mambo yafuatayo:
“Wazazi wa kijana huyo mwanamume walikuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova kwa miaka 30, lakini kijana huyo alikuwa amejiondoa kwenye tengenezo, hasa baada ya kukutana na mkewe aliyepinga imani zake. Lakini baada ya kukipokea kitabu Bible Stories, mke huyo alikuwa amekisoma bila kuacha, akafurahishwa sana na kutaka ajifunze Biblia.
“Moja kwa moja, mwanamke huyo kijana alisema na jirani yake mgeni habari alizokuwa akijifunza kisha akajua kwamba mwanamume huyo alikuwa amekuwa Shahidi hapo zamani. Walakini, baada ya kuhama hakuwa ameonana na Mashahidi wa Yehova. Halafu akakutana na mwanamke ambaye sasa alikuwa akiishi naye, naye mwanamke huyo alikuwa na maoni mabaya yasiyo na msingi juu ya Mashahidi. Lakini sasa mumewe aliamshwa akaanza kupendezwa tena, naye mwanamke aliyekuwa akiishi naye alipendezwa pia.
“Matokeo: Sasa yule mwanamume wa duka la samaki pamoja na mkewe wanajifunza Biblia na baba ya mwanamume mwenyewe, wakihudhuria mikutano na kufanya maendeleo mazuri. Namna gani jirani zao? Wao, pia, walianza kujifunza Biblia, wameandikisha kisheria ndoa yao na vilevile wanahudhuria mikutano na kufanya maendeleo mazuri.”
Katika nchi kadha waalimu wa shule wanatumia My Book of Bible Stories kama kitabu cha kufundishia madarasa yao. Mara nyingi imekuwa hivyo kwa sababu watoto wa shule wamechukua hatua ya kwanza kuonyesha shule zao kitabu hicho kwa busara, bila kuambiwa na mtu wafanye hivyo. Habari moja kutoka Uswedi inaeleza hivi:
“Madokezo yaliyotolewa kwenye makusanyiko ya mizunguko kwamba kitabu My Book of Bible Stories kichukuliwe na kupelekwa shuleni kikasomwe huko wakati wa mapumziko ili kuamsha kupendezwa kwa wanadarasa wengine yamefuatwa na Mashahidi wengi vijana. Wengine wameweza kuangushia wanadarasa wote wenzao kitabu hicho. Vilevile tumesikia maono juu ya waalimu waliokitumia kitabu hicho kama kitabu cha kufundishia, wakisoma kwa sauti sehemu zake katika darasa.
“Kwa mfano, kisichana chenye miaka minane kiliangushia mwalimu wacho kitabu hicho. Wanadarasa wenzacho wakatiwa moyo wachukue nakala ya kitabu hicho wakipeleke nyumbani kuwaonyesha wazazi wao. Wote waliruhusiwa kununua nakala, isipokuwa mmoja. Wakati mwalimu alipoanza kusoma habari za kitabu hicho darasani mwalimu mkuu wa shule alilalamika. Alilitaja jambo hilo kwenye mkutano uliofanywa pamoja na mwakilishi wa Baraza ya Elimu na wakuu wengine wa mwungano wa ualimu. Wao walipata nakala ya kitabu hicho, wakakisoma na kusema walikiona kuwa kizuri sana na chenye kuelimisha. Mwalimu yule alipewa ruhusa ya kukitumia tena kitabu hicho darasani.”
Katika Nigeria My Book of Bible Stories kimejulikana mahali pengine-pengine kama “Kile Kitabu.” Watu hata wanawajia Mashahidi wakikiomba. Shahidi mmoja wa huko anaandika hivi:
“Mapema katika Septemba, tulipopokea gawio letu la My Book of Bible Stories hapa Ilogbo, wale ambao kati yetu tuna watoto wenye kwenda shuleni tulimpa kila mmoja nakala. Watoto walipeleka vitabu vyao shuleni wakiwa na furaha nyingi. Walipokiona kitabu hicho, waalimu wote wakataka nakala. Halafu mwalimu mkuu akapata nakala yake, akaisoma na kupendekeza kitabu hicho kiwe kikitumiwa katika yale wanayoyaita madarasa ya Maarifa ya Biblia.
“Muda mfupi baada ya hapo, yeye alifanya iwe lazima kitabu hiki kiwe kikitumiwa katika shule yake, halafu nyumba zetu zikaanza kuzingirwa na watoto wa shule wenye kutaka nakala zao. Tukafanya agizo la vitabu 120. Kwa kuwa havikutosha kutimiza maagizo ya wenye kuvitaka, baadhi ya Mashahidi walianza kuangusha nakala zao za kibinafsi. Hata hivyo maagizo ya wenye kuvitaka hayakutimizwa yote. Tukaenda kwenye makundi ya karibu tupate vitabu zaidi, na, wakati wa kuandika habari hizi, vitabu 182 vimekwisha kuangushwa.
“Mara ya kwanza wazazi wenye kupinga njia ya Mashahidi wa Yehova ya kufundisha hawakutaka kununulia watoto wao vitabu hivi. Lakini wakapata habari kwamba hicho ndicho kitabu kilichochaguliwa kitumiwe kufundisha. Kwa upande wao, watoto wanafurahia masomo katika kitabu hicho. Kulingana na habari moja kutoka shule hiyo, kitabu My Book of Bible Stories kinatumiwa mara tatu kwa siku na sasa wanafanya Hadithi ya 62, ‘Matata Katika Nyumba ya Daudi.’ Waalimu wanasema kitabu hicho ndicho kitabu bora zaidi cha masomo ambacho wamepata kutumia katika kufundisha watoto Biblia.”
Kitabu hicho kimesaidia kwa njia mbalimbali. Habari moja kutoka Malaysia inakazia faida za kitabu hicho juu ya watoto wa shule katika sehemu hiyo ya ulimwengu.
“Mhudumu wa wakati wote anaeleza habari za mmoja wa wanafunzi wake wa Biblia, aliye mwalimu wa kike katika shule ya msingi ya Kichina, ambaye alifurahia sana kusoma My Book of Bible Stories kwa Kiingereza na Kichina pia hata akaamua kukitumia shuleni wakati wa mapumziko, akiagiza watoto wasome baadhi ya hadithi. Kukawa na matokeo yenye faida sana, kuwatuliza na kuwafanya wajifunze wao wenyewe, bila kuongozwa na mtu. Kwa kuruhusiwa na mwalimu mkuu na kukubaliwa na wazazi wa wanafunzi wake, mwalimu huyu alifurahia kuwaangushia wanafunzi hao nakala 33.”
Njia kuu ambayo Mashahidi wa Yehova wanatumia kufundisha wengine habari za Mungu na makusudi yake ni kuwaongoza katika mafunzo ya nyumbani ya Biblia yasiyo ya kulipiwa. Nacho kitabu My Book of Bible Stories kinatumiwa kwa matokeo mazuri katika mengi ya mafunzo haya. Shahidi mmoja wa Texas, katika United States, anatoa habari hii:
“Mke wangu nami tumechangamshwa sana na My Book of Bible Stories nasi tumejaribu kutumia njia tofauti kwa mafunzo yetu [wanafunzi wa Biblia] yenye watoto. Dakika 20 za kwanza tunajifunza pamoja na jamaa nzima katika kitabu hiki, nasi tunaona itikio lenye shauku nyingi sana tusiyopata kuona hapo kwanza. Jamaa moja ina watoto 11 na wote wanakuwa wamejitayarisha wakiwa na hamu ya kushiriki katika funzo, nyuso zao zikiwa na tabasamu. Halafu tunaingia moja kwa moja ndani ya lile funzo la kawaida kwa kukitumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, na wanaendeleza shauku yao hata kwenye funzo hilo pia. Kutokana na matokeo ambayo tumepata, tunaweza kuipendekeza kwa moyo njia hii ya kujifunza.”
Masomo yenye kuthaminika yanaweza mara nyingi kupatikana kwenye masimulizi ya Biblia. My Book of Bible Stories kinasaidia kufanya hivyo. Mwakilishi mwenye kusafiri wa Mashahidi wa Yehova katika Papua New Guinea anaeleza maono fulani katika nchi hiyo.
“Binti mkubwa zaidi nyumbani ni Maria. Yeye huithamini kweli ya Biblia, lakini nyakati nyingine hukataa kutii. Jioni moja wasichana wawili wadogo walimwita wakiwa barabarani kisha yeye akaenda pamoja nao. Kufikia saa tatu ya usiku hawakuwa wamerudi nyumbani, kwa hiyo mama yake akafunga mlango na kwenda kitandani, lakini si kulala. Karibu na saa sita ya usiku mama huyo akasikia kelele fulani mlangoni na kumwambia Maria aingie nyumbani na kuketi kwenye meza. Kwa utulivu mama akakichukua kitabu Bible Stories na kukifungua kwenye hadithi ya Dina kisha akamwuliza binti yake aisome. Alipomaliza, Maria alibubujika kwa machozi akaahidi kwamba asingejiingiza tena kamwe kwenye hali hiyo yenye hatari.”
Kwa wazi, My Book of Bible Stories ni kitabu kinachosaidia watu kote kote ulimwenguni. Je! wewe na rafiki zako, jirani na watu wa ukoo mna nakala? Ikiwa hamna, sababu gani wewe usijipatie nakala nyingi kisha umtolee kila mmoja wao kimoja? Huenda kikawasaidia wao pia.