Macho Kusaidia Wengine
AKIWA anafanya kazi katika Jengo la Manispaa ya Dade la Mahakama ya Uhalifu wa Waendesha Magari, mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika Miami, Florida, amepata fursa ya kutoa msaada wa kiroho kwa wafanya kazi wenzake. “Siku moja,” Rafael akaandika, “bibi mmoja ambaye alikuwa akipokea nakala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida kutoka kwangu alisema kwamba mchuuzi mmoja alikuwa amempa ensaiklopidia ya Biblia kwa ajili ya mtoto wake wa miaka 8 kwa dola 500 lakini kwamba hakuweza kuigharimia. Mara moja nikamwahidi kumletea lile buku moja la Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Siku iliyofuata nikakileta, naye akapendezwa na vielezi na kusifu kile kitabu.
“Aliweka kitabu hicho juu ya dawati lake na akaendelea kufanya kazi. Kwa muda usiozidi dakika 15 baadaye, mfanya kazi mwingine akaja kwenye dawati langu akiwa na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia mikononi mwake; alitaka kujua nilikipata wapi. Nikamwelezea kwamba Watch Tower Society hukichapisha. Alitaka nakala tatu kwa ajili ya watoto wake. Yeye hufundisha katika shule ya Jumapili na alihisi kwamba kitabu hiki kingesitawisha darasa lake. Alisema kwamba angenijulisha baadaye ni nakala ngapi zaidi angehitaji.
“Nusu saa hivi baadaye, mfanya-kazi-mwenzi mwingine tena akaja kwangu akiwa na kitabu kile mikononi mwake, akitaka kujua kama angepata nakala tatu za kitabu hicho. Upesi wengine wakawa wanaomba vitabu, na kabla sijajua, nilikuwa nimepata maagizo 12 kwa nakala za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Wale wanawake hata walinikasirikia kwa kutokuwaambia juu ya kile kitabu kabla ya hapo! Siku ya kazi iliyofuata, nilivileta vile vitabu ofisini na kuwakabidhi wale waliokuwa wameviomba.
“Juma lililofuata yule mwalimu wa shule ya Jumapili alisema angehitaji vitabu 15 kwa ajili ya wanafunzi wake. Alikuwa amekuwa akingoja kupata kibali cha kasisi na pia msimamizi wa shule. Yule kasisi, akasema yule mwanamke, alikipenda kile kitabu na akasifu vidokezi vyacho. Alitoa kibali cha kuvipata vitabu vile.
“Yule mwalimu wa shule ya Jumapili alitaka kuwapa watoto hao vitabu kama zawadi ya Krismasi. Alisema kwamba alijua kwamba mimi sisherehekei Krismasi, lakini kitabu hiki kingekuwa zawadi nzuri ya Krismasi. Aliniambia jinsi ilivyokuwa rahisi kuwafanya watoto wasikilize alipowasomea kutokana na kile kitabu.
“Mfanya kazi mwenzi mmoja aliniambia kwamba yeye huwasomea watoto wake kile kitabu kila usiku na kwamba hata yeye anajifunza mambo. Kwa mfano, hakujua kwamba kwa kweli kulikuwa na watu wakubwa mno waliopata kuishi duniani wakati wa Noa. Mfanya-kazi-mwenzi mwingine alisema kwamba lazima iwe ni mtu mwenye akili sana aliyevifanya vielezi katika kitabu. Vinaonekana vikiwa halisi sana. ‘Kitabu hicho ni kito cha thamani,’ akasema.
“Kwa ujumla, kwa muda wa siku chache tu, niliangusha nakala 32 za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kazini, na idadi hiyo inazidi kukua. Wakati wowote ninapomwonyesha mtu kitabu hicho, swali linaulizwa, ‘Ulikipata wapi?’”
Je, wewe uko macho kuridhisha mahitaji ya kiroho ya wengine? Rafael, sasa akiwa mzee wa Kikristo katika kundi fulani la Miami la Mashahidi wa Yehova, amalizia hivi: “Ono hili limenifunza somo kuhusu ushahidi wa vivi hivi na utayari wa kusaidia wengine.”