Kutatua Matatizo ya Vijana
Ifuatayo ni sehemu ya barua iliyopokewa katika afisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Ilikuwa imeandikwa na mama mwenye watoto wanne na mume asiyeamini. Kuhusu binti yake mwenye umri wa miaka 13, mama huyo aliandika hivi:
“Lazima nikiri kwamba sikumpa uangalizi wa kutosha . . .
“Nilianza kuona kwamba binti yangu alikuwa anapoa kwa habari ya kuhudhuria mikutano, mazungumzo ya jamaa ya Biblia na utumishi wa shambani. Nilipomwuliza tatizo lilikuwa nini, yeye alijibu, ‘Aa, hakuna.’ Halafu siku moja akaniambia kwamba yeye alikuwa akishiriki katika utendaji huo wa Kikristo kwa sababu alitakiwa tu afanye hivyo, wala si kwa sababu yeye alitaka. Yeye alisema kwamba hakutaka kuwa kama dada yake, kuwa na mvulana rafiki ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kuolewa ‘katika Bwana.’ Yeye alitaka namna ya maisha ambayo kila mtu mwingine alikuwa nayo. Ilikuwa vigumu kusadiki niliyosikia, kwa kuwa tunakuwa na nyakati za kufurahisha pamoja tukiwa jamaa.
“Nilipomkaza zaidi, alisema kwamba katika mazungumzo na rafikize shuleni angeweza kuona mambo ambayo ulimwengu unatoa. Na, kulingana nao, mimi nilikuwa mama asiye na fadhili na mwenye kudai mno. Kwa hiyo akaniomba nimpe miezi mitano bila yeye kufanya utendaji wo wote wa Kikristo ili ajiamulie ni jambo gani ambalo angependa maishani.
“Baada ya kulifikiria jambo hilo kwa muda fulani, nilipendekeza hivi: Kwamba badala ya mimi kumpa miezi mitano asifanye utendaji wo wote wa Kikristo, yeye anipe miezi mitano ya kufahamiana naye zaidi. Ningetembea pamoja naye kwenda na kutoka shuleni na yeye angekwenda pamoja nami kwenye mafunzo ya Biblia na ziara za kurudia. Ndiyo kusema, yeye angeshiriki kikamilifu zaidi pamoja nami katika utendaji wangu wa Kikristo.
“Yeye alikubali, na sasa miezi miwili imepita na matokeo yamekuwa mazuri sana. Yeye mwenyewe anakubali kwamba nia yake ilikuwa ya upumbavu wa kitoto tu. Kwa mara nyingine nauona mkono wa Yehova juu ya watoto wangu wote wanne. Hakika mimi ndiye mwenye kupendelewa. Katika sala zangu nimewatoa watoto wangu kwa Yehova, lakini mimi ndiye mwenye kupokea zawadi.”
Miezi minne baadaye msichana huyo mchanga alikuwa akishiriki tena kikamilifu na kwa hiari ya moyo wake mwenyewe katika utendaji wote wa Kikristo. Huenda ikawa kwamba pendekezo la mama huyo lingeweza kusaidia kutatua matatizo ambayo wengine wanayo katika kuwalea watoto wao.