Aliazimia Aishi Kulingana na Viwango vya Adili za Yehova
BIBLIA inaonyesha wazi kwamba mwanamume na mwanamke wakiishi pamoja bila haki ya kuwa wameoana kisheria wanafanya uasherati, nao hawataurithi ufalme wa Mungu wakiwa katika hali hiyo. (1 Wakorintho 6:9, 10) Jambo lililoonwa kutoka West Indies ya Uingereza linasimulia juu ya mwanamke kijana aliyejifunza ukweli huo.
Katika St. Lucia, wanawake wawili walio wahudumu Mashahidi wa Yehova walimfikia mwanamke huyo kijana, naye akaonyesha kupendezwa na Biblia. Basi, funzo la Biblia lilianzishwa pamoja naye. Alipofanya maendeleo katika ufahamu wake, aliona uhitaji wa kufanya marekebisho fulani ya kuhusu maadili. Ingawa alikuwa mama mwenye watoto wanne, hakuwa amefunga ndoa, bali alikuwa akiishi kinyumba tu na rafiki mwanamume. Yeye na pia mwanamume huyo walifanya bidii kujenga nyumba ndogo walimoishi wote sita.
Mwanamke huyo kijana alipotambua kwamba maisha yake hayakupatana na viwango vya uadilifu wa Yehova, alipiga moyo konde afanye mabadiliko. Uchaguzi ulikuwa ama alazimike kufunga ndoa na mwanamume aliyekuwa akiishi naye, ama ajitenge naye. Akazungumza naye jambo hilo, lakini mwanamume huyo hakutaka kumwoa. Yeye alitosheka tu na uhusiano ule wa kinyumba. Imani ya mwanamke yule ingemsukuma afanye nini? Alipaswa kufanya uamuzi fulani ikiwa alitaka kumpendeza Yehova, na baada ya kufikiria jambo hilo kwa sala akaamua kujitenga na mwanamume huyo. Lakini angeishi wapi na watoto wake wanne?
Baada ya kushauriana na mwanamume huyo, walifanya maafikiano mazuri—wagawane nyumba kila mmoja awe na nusu yake! Kupitia usaidizi wenye upendo wa akina ndugu, pamoja na mwanamume aliyekuwa akiachana naye, nyumba iligawanywa, nusu ikawa ya mwanamke huyo kijana na nusu ile nyingine ya mwanamume yule. Nusu ya nyumba ya mwanamke huyo ilihamishwa siku iyo hiyo ikapelekewa mahali pengine karibu kilometa nane kutoka ilipokuwa. Katika muda wa juma moja, ilijengwa upya ikawa na umbo tofauti kwa kufanywa makao yenye vyumba viwili vya kulala.
Alipokwisha kuchukua hatua zilizohitajiwa ili apatanishe maisha yake na viwango vya Yehova, bila kukawia alianza kushiriki utumishi wa shambani, akiwa ameambatana na watoto wake wanne. Aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa muda mfupi baada ya hapo. Ili aisherehekee pindi hiyo akajiandikisha kuwa painia msaidizi. Sasa amebarikiwa zaidi kwa sababu makao yake mapya yanatumiwa kuwa mahali pa Funzo la Kitabu la Kundi lenye hudhurio la wastani ya watu 17. Kweli Yehova amembariki kwa vile alivyoazimia awe mwabudu wake aliye safi.