Tumaini la Msichana Huyu ni Halisi
Mapema mwaka huu msichana wa shule ya masomo ya juu katika New Jersey alitayarishia shule insha fulani. Mgawo ulikuwa: “Kama ungesafiri kwenye wakati ujao, ungependa kufikia umbali gani? Taja mwaka wenyewe. Eleza jinsi ulimwengu ungekuwa. Eleza jinsi watu wangekuwa. Eleza namna zao za maisha; mambo wanayofanya kujitafutia riziki; vitu wanavyokula; n.k.” Msichana huyo wa miaka 15—mmoja wa Mashahidi wa Yehova—aliandika hivi:
“Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita. Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.”
“Kwa miaka mingi nimejifunza Biblia, na hasa kifungu hicho kimenisisimua sana. Mimi nimelifikiria kila neno la andiko hili na nyakati zote nimetaka kujua kama hali hizi zingeweza kweli kuwa duniani wakati ujao. Basi, nikatengeneza mashine ya wakati isiyopata kutengenezwa na mwanadamu mwingine ye yote, nikasafiri na kuingia katika wakati ujao.
“Uendeshaji wangu ulikuwa bila vizuizi. Nilisafiri mwendo wa miaka 10 kwa dakika moja. Nilipobaki mahali pamoja bila kusonga mbele wala nyuma, ulimwengu wenye kunizunguka ulibadilika sana. Nikaona mambo mabaya sana sana yakitukia: matetemeko ya dunia, vita, njaa kuu, ukosefu wa kufuata sheria, sawasawa na yanavyoelezwa katika Mathayo 24:6-8 katika Biblia. Lakini mambo haya yalitokea kwa ghafula nikayaona mbele yangu. Halafu, nikaona uharibifu kamili wa kila kitu chenye kunizunguka. Watu walikuwa wakiharibiwa na kitu fulani, si vyombo vyao wenyewe vya vita, bali na nguvu kubwa sana za maumbile zenye kutumiwa na mtu aliye mkubwa sana kuliko mwanadamu.
“Nikajaribu kusafiri ndani ya wakati pole-pole kidogo niweze kuyaona mambo haya ya kustaajabisha yakitukia. Halafu, nikaona watu wakifanya kazi kwa bidii wakisafisha, wakijenga na kutengeneza upya maumbo ya kila kitu. Kwa wazi wao hawakupatwa na uharibifu ule na kwa hiyo walikuwa wakiyaondolea mbali magofu yaliyoachwa. Wote walikuwa wakifanya kazi pamoja, kwa mapatano. Hayo yalipopita, nikaona wanaume na wanawake wengine wengi juu ya dunia. Mimi sikujua walikuwa wakitoka wapi. Nikatazama mpaka nikaona mwanamume mmoja aliyefanana na babu yangu—kusema kweli, alikuwa babu yangu kabisa. Yeye alikuwa amekufa mwaka 1972. Nikachunguza vifaa vyangu vyote katika mashine yangu nihakikishe kwamba sikuwa nikisafiri kurudi nyuma. Nikaona kwamba sikuwa nikirudi nyuma. Kwa uhakika nilikuwa nikisonga mbele, na bado nikawa nikiona watu waliokuwa wamekufa. Kisha, nikalikumbuka lile andiko lililo katika Biblia kwenye Matendo 24:15: ‘Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.’ Nilikuwa kwa kweli nikiuona ufufuo.
“Nikaongeza mwendo wangu wa kusafiri hata ikawa kwamba rangi na nuru hazikuonekana waziwazi tena, bali zilionekana kwa unyenyezi tu. Nikaamua kusimama. Bila shaka, mahali niliposimamia palikuwa mahali pale pale nilipoanzia, katika wakati ujao ulio karibu. . . .
“Kule mbali nikaweza kuona “kivulana akicheza na mnyama mkubwa. . . . alikuwa kabisa akicheza na SIMBA, weee! Nikataka kukimbia nikamwonye juu ya hatari yake, lakini jambo fulani likanizuia. Simba huyo alikuwa wa kufugwa, akawa akitenda kama paka aliye mikononi mwa mtoto. Nilipoendelea kusafiri kwa miguu, nikaona amani hii kwa wingi zaidi kati ya mwanadamu na wanyama, na kati ya wanyama wenyewe. Lakini upatano wenye kusisimua zaidi ulikuwa ule ulio kati ya wanadamu. Mbari zote za watu zilikuwe zikisema lugha ile ile na kupatana vizuri kama kwamba walikuwa ndugu na dada. . . . Nikaona kwamba watu hawa hawakuwa na makosa yo yote. Hawakuwa na maradhi, wala magonjwa. Wao walikuwa wakamilifu katika umbo. Halafu jambo fulani likanigutua. Walikuwa ni watu wale wale niliowaona miaka 400 iliyopita nilipokuwa katika safari yangu ya kwenda mahali mahali, lakini walionekana wenye umri ule ule. Hakuna aliyekuwa mgonjwa, hakuna aliyezeeka wala kufa. . . .
“Kwa kweli niliona furaha nyingi katika wakati huu mzuri ajabu wa siku za usoni. Sasa, mimi nipo nyumbani, nimeurudia wakati wangu mwenyewe. Ni vigumu kusadikisha mtu ye yote juu ya mambo niliyoyaona. Angalau kila jambo nililosoma katika Biblia sasa limekazika imara akilini mwangu. Ningependa kweli kurudi tena nikaishi huko milele pamoja na watu hao. Lakini nilifikiria kifungu kimoja katika Biblia kilichonihakikishia kwamba huenda nikapata utimizo wa mambo hayo, tena karibuni. Kifungu hicho kiko kwenye Zaburi 37:10, 11: ‘Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.’