Kuzuru Mgonjwa Jinsi ya Kusaidia
RAFIKI amelazwa hospitalini, na kwa kweli ungependa kumzuru. Unapaswa useme na kufanya nini? Ungeweza kuleta nini? Ni nini kingeweza kusaidia sana? Na je, kuna mambo ambayo unapaswa uepuke kusema au kufanya?
Unataka ziara yako iwe na ustahili, si kusema “Habari gani” tu, kusema “U hali gani?” ki-vivi-hivi halafu kusema kwa haraka “Tutaonana,” labda pamoja na kuacha kadi ya “Upate nafuu haraka” ili kuongezea hisani yako. Kwa hiyo unaweza kufanyaje?
Shauri la kwanza: Tumia utambuzi kuhusiana na wakati unapozuru. Unaweza kumwuliza mgonjwa au familia yake ni saa gani ingefaa zaidi, kwa mfano wakati hatakuwa akishughulika na wageni wengine au watu wa ukoo wa karibu. Labda yafaa zaidi kuzuru jioni ambayo ni kabla ya upasuaji wakati ambapo mgonjwa aweza kufaidika na mazungumzo yenye uchangamshi, yenye kuvuta fikira badala ya punde tu baada ya upasuaji, ambapo huenda akawa dhaifu na katika uchungu.
Maneno kwa na Kutoka kwa Wenye Hekima
Ingefaa tufikirie kifungu cha maneno hayo yasemayo ‘mazungumzo yenye uchangamshi.’ Wewe utazamie kuwa ndiye wa kwanza kuyaanzisha wakati wa ziara, na uyaendeleze bila kuacha. Mtu huyo aliye katika kitanda cha hospitali hapaswi kuhangaikia kuwa ndiye mkaribishaji mwema kwako. Wewe waweza kuchukua mzigo huo kwa mwenendo wa utulivu na mtazamo wa kirafiki. Sasa, ni yale upaswayo na usiyopaswa kusema.
Usije na uso wa majonzi au huzuni hata ikiwa hali ya mgonjwa si nzuri. “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri,” asema mwandikaji mwenye hekima wa mithali, “bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.” (Mithali 17:22) Kwa hiyo, kumbuka ni daraka lako kuendeleza mazungumzo yakiwa yenye kutia moyo na kupendeza.—Mithali 25:11; linganisha Isaya 41:13.
Habari za karibuni zaidi kutoka kwa familia au kundi la mgonjwa huenda zikapendeza na kujenga, hasa ikiwa una habari njema. Pia, usisahau tokeo ambalo kiasi fulani cha ucheshi huwa nalo juu ya kupona; tafuta fursa za kumfanya mgonjwa atabasamu au acheke. Usawaziko ni wa maana sana hapa. Wewe unatembea si ili uwe mfanya mzaha au mteremesha-baraza mwenye vichekesho vitupu bali ili uonyeshe hangaiko na huruma halisi.
Mgonjwa pia anahitaji uhakika. Hivyo, jihadhari usizungumze kwa njia hasi juu ya daktari au hospitali hiyo. Mara nyingi linakuwa jambo bora zaidi kutokulinganisha hali au tatizo la mgonjwa na jambo ambalo huenda wewe uliweza kupata au na wengine waliokuwa na tatizo kama hilo, isipokuwa tu ikiwa matokeo yalikuwa ya kufurahisha. Kila mtu ni tofauti, na hali ya kila mgonjwa ni ya namna yake.—Mithali 18:13.
Jambo la mwisho la kuangaliwa kuhusu mazungumzo yako: Je! umeshapata ono lenye kulemea na kuchosha la kuwa na mtu ambaye maneno yake hutoka kama risasi za mmiminiko, kama mabubujiko ya maji yanayoanguka kwenye poromoko la maji? Ilikuchosha, sivyo? Kwa hiyo tafadhali usiwe hivyo unapomzuru rafiki yako au mtu wa ukoo aliyelazwa hospitalini. Hali maongezi yako yakiwa yenye ufurahifu na yenye kutia moyo, dhibiti wingi na mwendo wayo. Hakuna haja ya kuhisi wasiwasi, kama kwamba ni lazima ujaze kila sekunde kwa maneno. Wakati wenye kimya mkiwa pamoja waweza kuwa wenye kufariji pia. Ndiyo, uwe mwangalifu usichangie uchovu wa mgonjwa kwa tiririko lisilokwisha la wageni wanaofanya alazimike kusikia tiririko lililo kubwa hata zaidi la maneno.
Kuzuru kwa Muda Gani?
Katika sehemu fulani za ulimwengu, ni kama familia huishi pamoja na mgonjwa hospitalini. Wao wanatazamiwa kumtunza mgonjwa kwa kumwosha na kuandaa chakula, hivi kwamba ziara hiyo huenda ikarefushwa. Lakini katika hospitali zilizo nyingi, saa za kuzuru zina kikomo ili mgonjwa asichoshwe mno na ili wafanya kazi wa hospitali waweze kufanya kazi yao. Hivyo, mara nyingi ziara yako haipasi kuzidi saa moja ikiwa wewe ni mtu wa ukoo au rafiki wa karibu sana wa mgonjwa, na nusu saa ikiwa mnafahamiana tu. Namna gani ikiwa mgonjwa anakuuliza ukae zaidi? Bado ingekuwa vema kufupiza ziara yako, kwa sababu huenda akawa amechoka na akawa na uamuzi usio mwema. Bila shaka, ni lazima utumie utambuzi wako mwenyewe, lakini jambo lenyewe ni, usikawie zaidi baada ya kukaribishwa.
Shauri hilo lahitaji mkazo wa pekee ikiwa mgonjwa tayari anaonekana akiwa na wenye kuzuru wengi kuliko ilivyo vema kwake au kwa mpango wa hospitali. Kwa kweli, kufanya kwako ziara kadhaa fupi ni afadhali na kwaonyesha hangaikio lako kuliko ziara moja ndefu. Kumbuka, pia, uhitaji wa busara ikiwa mgonjwa ana watu wa ukoo ambao wanaonekana ni kama wenye uhasama au hata wanachukizwa na kuwapo kwako.—Linganisha Mithali 25:17.
Msaada Wako Wenye Kutumika
Hata kabla ya kuondoka kwenda ziara yako, aina nyingine ya matayarisho ya mapema itasaidia. Je, kuna kitu chochote cha maana ambacho waweza kuleta? Namna gani kitu kipya cha kusoma? Labda siku hiyo hiyo ulipokea toleo la karibuni zaidi la gazeti ambalo hata mgonjwa huonea shangwe. Mgonjwa huenda akaguswa moyo kwa kuona utayari wako wa kushiriki toleo lako jipya unalothamini. Ungeweza hata kujitolea kumsomea nakala moja au mbili ulizoona kuwa zapendeza hasa.
Ungeweza kuleta vitu gani vingine? Kikumbusho kidogo kama maua au matunda kingeweza kuiangazia siku. Kifariji kingine kingeweza kuwa ni peremende ambazo anapendelea zaidi au hata chakula kilichotayarishiwa nyumbani—ikiwa hilo laruhusiwa. Ungeweza kuchunguza na familia yake kuhusu aina hiyo ya chakula au uwaulize wauguzi kabla ya kukileta ndani ya chumba.
Pia ungeweza kumwuliza daktari au wauguzi kama kuna kitu kingine ambacho waweza kumletea mgonjwa au ambacho unaweza kumfanyia ambacho kitarahisisha mzigo wao au kimfanye astareheke zaidi. Huenda wakakaribisha msaada wako.
Je! wapenda kusaidia katika njia nyinginezo? Mwulize mgonjwa juu ya mambo madogo yenye kutumika. Ni nani anachukua au kumletea barua zake? Je! ungeweza kujitoa kuchunguza nyumba yake, labda hata kuisafisha pamoja na rafiki fulani kabla mgonjwa hajarudi nyumbani? Je! mtu fulani anahitajiwa kufagia uchafu uliokusanyika kwenye njia ya nyumba yake, anyunyizie mimea maji, au achukue hatua ili nyumba yake ionekane kama inakaliwa na watu, na hivyo isivutie wavunja-nyumba? Je! yeye anahangaishwa na utunzi wa mnyama kipenzi? Hayo na mambo mengine huenda yakawa akilini mwa mgonjwa lakini hayawezi kutokezwa kama hujayauliza. Udadisi wako wenye rehema pia utasaidia kukazia kwamba kwa kweli unajali.
Yafaa neno lisemwe juu ya kuvalia ifaavyo wakati wa kuzuru hospitali. La kushangaza ni kwamba, jinsi unavyovalia na kutenda yaweza kuathiri jinsi mgonjwa anavyotendewa na wafanya kazi wa hospitali. Wanaweza kuvutiwa sana ikiwa wanaona mgonjwa akipokea wageni ambao wamevalia kinadhifu. Wakati baadhi ya wageni hao wanapoonekana wakiulizia hali ya mgonjwa, wafanya kazi huenda wakakata kauli kwamba mgonjwa huyo lazima awe ni mtu wa kustahiwa, na ndivyo alivyo. Biblia hutaja juu ya mtu kujipamba ‘kama iwapasavyo wanaoukiri uchaji wa Mungu,’ na kwa kufanya hivyo, unaweza kuwatia moyo wafanya kazi kumtendea vema.—1 Timotheo 2:9, 10.
Kama Kuna Tatizo Zito
Mara kwa mara, mgonjwa unayezuru huenda akawa ana tatizo zito katika kuwasiliana na wafanya kazi wa hospitali. Swali zuri la kuwa nalo tayari bila kuingilia mambo ya kibinafsi ya mgonjwa ni, “Daktari anafikiri unaendeleaje?” Ikiwa mambo hayaendi vema, na wewe ndiwe mshiriki wa famili au mhudumu mwenye daraka, labda unaweza kuandaa msaada. Kwa ajili ya hali njema ya mgonjwa, huenda ukahitaji kuchukua hatua ya kwanza katika kupata habari zaidi kutoka kwa wafanya kazi wa hospitali. Au labda ungeweza kujitoa kuandamana na familia, ambao kwa sababu fulani huenda wakasita kuzungumza na daktari.
Ikiwa hivyo, jambo la maana kuweka akilini ni kwamba usihofishwe na mpangilio wa hospitali au na wafanya kazi. Mgonjwa huenda hata akawa yumo katika sehemu ya kutunzia wagonjwa mahututi, akiwa amezungukwa na aina zote za mashine na watu wagonjwa sana. Wafanya kazi huenda wakaonekana kuwa na shughuli sana au labda wenye maneno makavu. Mwelekeo ni kuhofu kuwakatiza, sembuse kusema jambo ambalo lingeweza kuonekana kama ushindani. Lakini ikiwa kwa haki wewe ndiwe mtetezi wa mgonjwa, wewe (na yeye) mwastahili majibu ya wazi na kujua njia za badala ambazo zingeweza kufuatwa. Usikubali kukatizwa mpaka jitihada yako ifaulu. Hali ukitunza kwamba usiwe chukizo, kumbuka kwamba katika kielezi kimoja hata Yesu alikazia kwamba wakati mwingine inalazimu kuendelea kuuliza ili kupata utunzi au habari ambayo mtu ana haki ya kuipata.—Luka 18:1-6.
Kutazama Nyuma Kwenye Ziara Yako
Baada ya wewe kumaliza ziara yako, na kuondoka ukiwa mwenye furaha, unaweza kupitia yale uliyoyasema na kufanya. Kuwazia huko kunaweza kukusaidia kufahamu jinsi ziara yako itakayofuata, kwa mgonjwa huyu au kwa mwingine, iwezavyo kuwa na mafanikio na yenye kuridhisha hata zaidi.
Kwa ujumla, kuna mengi uwezayo kutimiza kwa ziara ya hospitali. Kumbuka kujitayarisha na kuwa na tamaa ya kusaidia. Kwa kuitumia fursa kwa faida, unaweza kutimiza mengi sana na uthibitike kuwa “rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.”—Mithali 18:24.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Ziara Yako Yenye Msaada kwa Mgonjwa
1. Uwe tayari.
2. Fikiria hali ya mgonjwa. Usirefushe mno ziara yako.
3. Valia ifaavyo.
4. Ongoza katika maongezi, lakini fupisha maneno yako.
5. Uwe mwenye msaada katika uletacho au ujitoleacho kuleta.
6. Uwe mchangamfu na mwenye kujenga.
7. Rudi kwa ajili ya ziara fupi nyingine.