Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 3/8 kur. 5-8
  • Je! Pengo Laweza Kuzibwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Pengo Laweza Kuzibwa?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vizuizi vya Patano
  • Sababu kwa Nini Patano Haliwezekani
  • Kukabiliana na Suala Halisi
  • Kusahihisha Kumbukumbu
  • Je! Ni Enzi Mpya kwa Wayahudi na Wakristo?
    Amkeni!—1992
  • Dini ya Kiyahudi—Jitihada ya Kutafuta Mungu Kupitia Andiko na Pokeo
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Kwa Nini Wayahudi Wengi Waliuawa? Kwa Nini Mungu Hakuzuia?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Mashahidi wa Yehova na Yale Maangamizi Makubwa ya Wayahudi—Biblia Inasema Nini?
    Habari Zaidi
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 3/8 kur. 5-8

Je! Pengo Laweza Kuzibwa?

LILE pengo lililopo kati ya Wayahudi na Wakristo ina kina kirefu zaidi ya lile Teketezo la Umati. Tangu mwanzo wenyewe, imani hizi mbili zimehitilafiana juu ya lile suala kuu: kama Yesu wa Nazareti alikuwa ndiye Mesiya aliyeahidiwa.

Katika karne ya kwanza, suala hilo la Kimesiya lilitokeza mnyanyaso wenye jeuri juu ya Wakristo. (Matendo 8:1) Hata hivyo, baadaye hali ikawa kinyume. Baada ya wakati, waliodai kuwa Wakristo wakapata kuwa wanyanyasi wa Wayahudi. Lakini zijapokuwa jitihada kubwa za Jumuiya ya Wakristo za kuongoa Wayahudi kwa kipindi cha karne nyingi, Wayahudi kwa ujumla hawajaacha hata kidogo msimamo wao wa kwanza.

Mwandikaji mmoja Myahudi alitaja kwamba ingawa Wayahudi hawana neno dhidi ya Yesu binafsi, yeye “siye yule Mesiya wa kisiasa ambaye sisi na wazazi wetu wa kale walimtamani sana.” Rabi Samuel Sandmel alilisema jambo hilo waziwazi zaidi: “Sisi hatujapata kuamini kama nyinyi [Wakristo] mnavyoamini; ni hivyo tu.” (We Jews and You Christians) Likiwa tokeo la tofauti hii ya maoni, kuna pengo la kidini kati ya Wayahudi na Wakristo ambayo ni kubwa zaidi ya vile wengi wanavyojua.

Vizuizi vya Patano

Kwa upande mmoja, fundisho la Ukristo haliachi nafasi hata kidogo kwa kijia cha wokovu pasipo Yesu. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” —Yohana 14:6; linganisha Matendo 4:12; 1 Timotheo 2:3-6.

Kwa upande mwingine, Uyuda huchukizwa na ibada ya sanamu inayojaa katika Jumuiya ya Wakristo. Fundisho la Utatu vilevile hudharauliwa na Wayahudi kuwa kipingamizi kilicho wazi cha “asili ya Uyuda”—fundisho la ibada ya Mungu mmoja linaloonyeshwa katika maneno haya, “SIKILIZA, EWE ISRAELI: BWANA MUNGU WETU, BWANA NI MMOJA.” (Kumbukumbu la Torati 6:4, The Soncino Chumash) Msomi Jakób Jocz alionelea hivi: “Ni kuanzia hapa kwamba pengo kati ya Kanisa na Sinagogi hufunguka mbele yetu kwa kina na umaana walo wote. . . . Lile fundisho la uungu wa Yesu Kristo ni kosa lisiloweza kusameheka machoni pa Uyuda.”—The Jewish People and Jesus Christ.

Pia Ukristo na Uyuda zina maoni tofauti kuhusu Sheria ya Musa na mapokeo yayo. Rabi Stuart E. Rosenberg alitoa hoja hivi: “Bila agano la Mungu hakuwezi kuwa taifa la Kiyahudi: Lilifanyiza mwanzo wao wenyewe, nao hawakuliachia mbali kamwe. . . . Lakini tangu mwanzo wenyewe, Wakristo wamekuwa na tatizo na agano la Israeli.” Kwa kweli, mtume Paulo alisema kwa habari ya Sheria ya Musa hivi: ‘Mungu aliifuta ile hati iliyoandikwa . . . , akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani [mti wa mateso, NW].’—Wakolosai 2:14.

Wanatheolojia wa makanisa wanaojaribu kupunguza mkazo wa fundisho la Ukristo kwa kutoa hoja kwamba agano la Musa lingali halali au kwamba kuna ‘vijia mbalimbali vya kwenda kwa Mungu’ hujipata wenyewe wakiwa katika tatizo lenye kuaibisha. Ili kupatanisha maoni yao na lile “Agano Jipya,” wanatheolojia wa kanisa lazima wajihusishe katika kile kinachokuwa kama mchezo wa ujanja wa kitheolojia: kudanganya, kupotosha, au hata kupuuza maandiko ya Biblia ya maana sana. Au huenda wakatoa hoja, kama vile wengine hufanya, kwamba kwanza kabisa yale maandiko yenye kutatiza si ya kweli, kwamba Yesu hakudai kamwe kuwa “njia na kweli na uhai,” kwamba maneno ya Petro kwenye Matendo 4:12, ambayo husema kwamba Yesu ndilo ‘jina pekee chini ya mbingu ambalo twapasa kuokolewa kwalo,’ yalibuniwa baadaye chini ya uvutano wa theolojia ya Paulo, na kadhalika. Lakini kwa kufanya hivyo, wanadhoofisha imani ya wafuasi wao wenyewe.

Hivyo Jakób Jocz alijumlisha mambo vizuri kwa kusema kwamba imani hizo mbili “hazina kiwango chochote kimoja kinachokubaliana ambacho kingeweza kutumiwa kuwa msingi wa ‘theolojia ya kupatanisha’. Zinaweza kuridhiana tu kwa kukubali kuacha kushikilia imani zao: ama Kanisa liwe Sinagogi ama Sinagogi liwe Kanisa.”

Sababu kwa Nini Patano Haliwezekani

Hata hivyo, kuna vizuizi visivyoshindika hata kwamba iwezekane kufikia uridhiano wowote wa namna hiyo wakati wowote. Kwa Wayahudi, wazo tu la wongofu wa kidini ni laana. Kwa vyovyote vile, dini za Jumuiya ya Wakristo zimefanya jambo gani linaloweza kuzipendekeza kwa Wayahudi? Rabi Samuel Sandmel huorodhesha baadhi ya mambo ya kuogopesha sana ya historia “yaliyotendwa na Wakristo dhidi ya Wakristo, kwa jina la Ukristo,” naye auliza: “Kwa msaada wayo, je, mwaweza kututarajia kupatana na akili nzuri tukubaliane na mkataa wa kwamba dini yenu ni bora zaidi ya yetu? Je! imetokeza watu bora zaidi? Je! imetatua masuala ya amani na vita na ufanisi na utulivu miongoni mwa mataifa ya Kikristo?”

Pia lile Teketezo la Umati limetokeza mbele lile suala la kusalimika kwa Wayahudi—wakiwa kikundi cha taifa, wakiwa dini, na wakiwa utamaduni. Hivyo Wayahudi wanaelekea kukuona kuongolewa, si kwamba tu ni kukubali fundisho la uzushi, bali kuwa tendo la usaliti. Jarida Journal of Jewish Communal Service liliomboleza hivi: “Sisi hatuwezi kukubali kupata hasara kwa kupoteza yeyote wa vijana walio watu wazima wa kizazi cha Kiyahudi. . . . Jambo ambalo Wanazi Walishindwa kwa lile Teketezo la Umati, bado laweza kutukia kupitia [wongofu wa kidini].”

Hivyo Rabi Henry Siegman hukata maneno hivi: “Kumbukumbu la wongofu wa kidini wa kutumia nguvu limeimarika sana katika dhamiri za Wayahudi na limekuwa ndicho kizuizi kigumu zaidi kushinda cha usitawi wa mahusiano kati ya Wakristo na Wayahudi.”

Kukabiliana na Suala Halisi

Hivyo hakuna patano la kweli kati ya Jumuiya ya Wakristo na Uyuda linaloonekana kuwa litatokea karibuni. Jitihada za kupata umoja huendelea kudhoofishwa na theolojia zisizoweza kupatanishwa, mapendezi ya kisiasa yenye kuhitilafiana, na kutotumainiana. Majadiliano ya kidini huelekea kuepuka lile suala ambalo lilitokeza mtengano mwanzoni kabisa, yaani, madai ya Yesu kuwa Mesiya. Wakati jambo hilo litakapotambuliwa na kushughulikiwa kwa unyofu ndipo tu baadhi ya vile vizuizi vya muda mrefu vya hofu na kutotumainiana vitakapoanza kubomoka.

Inakubalika kwamba Wayahudi walio wengi hawataki kuzungumza habari za Yesu. Kutotaka kwao ndilo jambo ambalo bila shaka hatimaye lilitokeza karne nyingi za kupinga Usemiti katika jina la Yesu. Ingawa hivyo, Yesu siye aliyeanzisha zile Krusedi, wala Yesu hakuanzisha lile Baraza la Kutesa Wazushi wala yeye hakutokeza lile Teketezo la Umati. Vitendo hivyo viovu sana vilitendwa na watu ambao hudai kwa uwongo kuwa Wakristo! Hilo ni wazi kutokana na maneno ya Yesu mwenyewe, ambaye, akinukuu maneno katika Sheria ya Musa, aliandaa mojawapo kanuni zenye kuongoza Ukristo wa kweli: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:39; Mambo ya Walawi 19:18) Maneno hayo yatumika kuwa shtaka kwa Jumuiya ya Wakristo. Kwa wazi, aina ya dini yayo ni mpotosho mbaya sana wa yale ambayo Yesu alifundisha hasa.

Kusahihisha Kumbukumbu

Mashahidi wa Yehova wataka Wayahudi waelewe kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo—wala si Ukristo wenyewe—ndiyo yamesababisha mateso mengi sana kwa Wayahudi. Wataka Wayahudi wasiwe na maoni ya chuki na yenye kupotoka juu ya Yesu bila kupata habari za kweli ili waweze kufanya uamuzi baada ya kupata habari kamili juu yake. Zaidi ya hilo, wanataka kushiriki pamoja na Wayahudi usadikisho wa kwamba ile Enzi ya Kimesiya, iliyotabiriwa na manabii zamani sana, imekaribia sana! Hata hivyo, kwa nini Myahudi akate kuwasikiliza Mashahidi wa Yehova?

Jambo moja ni kwamba, wao hawachukizi Wayahudi kwa kutumia sanamu katika ibada yao, wala wao hawaamini lile fundisho la Utatu—imani nyingine yenye kuchukiza sana Uyuda. Wao hulikataa fundisho hilo kuwa ni la kipagani na halipatani na Maandiko.a Kwa kweli, Mashahidi si sehemu ya Jumuiya ya Wakristo hata kidogo! Hivyo, wao hawabebi aibu ya lile Teketezo la Umati, sembuse ile historia yenye umwagaji damu ya kupinga Usemiti.

Kati ya dini zote ambazo hudai kuwa za Kikristo, wao peke yao ndio wamefuata amri ya Yesu kwenye Yohana 17:16, NW, ‘wasiwe sehemu ya ulimwengu.’ Hiyo yahusisha kudumisha kutokuwamo kamili kwa kisiasa. Wayahudi wajuao mambo ya hakika wajua kwamba wakati wa Vita ya Ulimwengu ya 2, Mashahidi Wajerumani zaidi ya elfu moja walikufa katika kambi za mateso za Hitler, wakikubali kuwa majeruhi wa lile Teketezo la Umati badala ya kuwa washiriki wanyamavu katika teketezo hilo.b Kusisitizia kwao bila hofu wadumishe kutokuwamo katika kukaidi mamlaka ya Nazi ni ushuhuda wenye kuangaza wa nguvu za Ukristo wa kweli. Kama Jumuiya ya Wakristo ingalifanya ivyo hivyo, hilo Teketezo la Umati halingalitukia kamwe.

Hivyo Mashahidi wa Yehova hupokewa kwa fadhili na Wayahudi wengi. Inakubalika kwamba, si wote huthamini ziara zao. Hata hivyo, Rabi Samuel Sandmel alikiri kwamba Wakristo huona lazima ya kuhubiria wengine. (Warumi 10:10) Yeye huwauliza Wakristo hivi: “Je! mwaweza kutekeleza kusudi lenu kwa njia ambayo haituvunjii heshima wala isiyoonyesha kwamba mmeachia mbali huu [utume wa kuhubiri] ambao mwauona kuwa wa maana kabisa?”—We Jews and You Christians.

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanya ivyo hivyo. Kwa staha, wao huwaomba majirani Wayahudi wafikirie lile suala ambalo limetenganisha Wakristo na Wayahudi kwa muda mrefu sana: Lile tumaini la Kimesiya. Ni jambo gani lililotokeza tumaini hilo? Maoni ya Wakristo na ya Wayahudi yalipataje kutofautiana sana kadiri hiyo? Ule upingaji Usemiti uliopo wenye kuongezeka katika sehemu fulani za ulimwengu huyafanya maswali kuhusu Yesu yafae zaidi sasa kuliko yalivyopata kuwa. Makala yetu inayofuata inajitahidi kuandaa majibu.

[Maelezo ya Chini]

a Ona broshua Je! Uamini Utatu?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Ona “Lile Teketezo la Umati—Majeruhi au Wafia-Imani?,” iliyotokea katika toleo la Amkeni! la Novemba 8, 1989.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Lile fundisho la uungu wa Yesu Kristo ni kosa lisiloweza kusameheka machoni pa Uyuda”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Vitendo vya waitwao Wakristo eti havikufanya lolote linaloweza kupendekeza Ukristo kuwa dini ya upendo

[Hisani]

U.S. Army

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ibada ya sanamu na fundisho la Utatu la Jumuiya ya Wakristo limewatenga mbali Wayahudi wengi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki