Je! Ni Enzi Mpya kwa Wayahudi na Wakristo?
“Mnyanyaso utakwisha wakati Papa aingiapo sinagogi.”—Mithali ya Kiyahudi.
KATIKA Aprili 13, 1986, Papa John Paul wa 2 alipata kuwa papa wa Kiroma wa kwanza aliyepata kutiwa katika rekodi kuwa ameingia katika nyumba ya ibada ya Kiyahudi. Huku akishangiliwa kwa kishindo, papa alithibitisha tena kwamba kanisa Katoliki “huchukizwa sana na chuki, minyanyaso na wonyesho wa kupinga Usemiti walioelekezewa Wayahudi wakati wowote na yeyote.” Alisema kwamba ‘ziara yake ilikusudiwa kushinda chuki za kale na kupata utambuzi mtimilifu zaidi wa urithi wa kiroho wa pamoja ulioko kati ya Wayahudi na Wakristo.’
Katika miaka ya karibuni dini nyinginezo za Jumuiya ya Wakristo zimetafuta kuziba lile pengo la muda mrefu sana lililoko kati yazo na Wayahudi. Katika Juni 1987 makanisa ya Kipresbiteri ya U.S. yalitoa hati yenye kuonyesha kutubia kujihusisha kwa muda mrefu kwa kanisa katika “mitazamo na matendo ya kupinga Wayahudi.” Kufuatia hatua hiyo, United Church of Christ lilipitisha azimio lalo lenyewe. Hilo lilijulisha wazi kwamba “mahali pa Uyuda hapakuchukuliwa na Ukristo” na kwamba “agano la Mungu na watu wa Kiyahudi halijafutwa.”
Jumuiya ya Wakristo na Lile Teketezo la Umati
Ni nini kusudi la jitihada hizo zenye kutokeza? Ni jitihada tu za Jumuiya ya Wakristo za kujiondoa katika lile Teketezo la Umati la Nazi. Katika miaka ya baada tu ya Vita ya Ulimwengu ya 2, walio wengi wa viongozi wa makanisa walijaribu kupuuza kwamba maogofyo makuu ya hilo Teketezo la Umati yalikuwa yametendwa na waliodai kuwa Wakristo. Hata hivyo, ukweli wa mambo hayo ya hakika yenye kusumbua haukusahauliwa na Wayahudi.
Kadiri miaka ilivyopita, waokokaji wa hilo Teketezo la Umati walianza kuteta. Vitabu, magazeti, na maonyesho ya sinema yalikabilisha ulimwengu na maogofyo makubwa ya kambi za mateso. Vilevile kujipigania kwa Taifa la Israeli ili lisalimike kulivuta fikira za ulimwengu kwenye Uyahudi. Kama tokeo, Jumuiya ya Wakristo imezidi kushutumiwa. Kama vile G. Peter Fleck alivyoandika katika The Christian Century: “Kuna kasoro fulani mbaya sana kwa . . . dini na ustaarabu ambao ungeweza kutokeza na kuvumilia chukizo [kama hilo Teketezo la Umati]. Na kanisa ambalo lingeweza kukaa karibu kimya kabisa na bila kutenda wakati wa hilo ogofyo kubwa lazima liwe na kasoro.”
Viongozi Wayahudi wakubali. Rabi Stuart E. Rosenberg huuliza kwa nini, baada ya Vita ya Ulimwengu ya 2, ‘ni makanisa machache sana au viongozi wayo waliona kwamba kulikuwako uhusiano kati ya historia ndefu na yenye kuendelea ya Ukristo kupinga Uyuda na tokeo la mwisho la Nazi—kuuawa kimakusudi kwa theluthi moja ya Wayahudi.’ Alitaja kwamba washiriki wengi wa kanisa “walificha nyuso zao, au, hata lililo baya zaidi, walikubali kwa kimya maangamizi ya wale milioni sita katika Ulaya ya Hitler kuwa hukumu ya kimungu kwa ‘[sababu ya] Wayahudi kumkataa Yesu.’”—The Christian Problem.
Na Elie Wiesel asema katika kitabu chake A Jew Today: “Mtu ataelezaje kwamba kanisa halikutenga na ushirika ama Hitler ama Himmler? Kwamba Pius wa 12 hakufikiria kushutumu Auschwitz na Treblinka kulihitajiwa kabisa, sembuse kuwa jambo la lazima? Kwamba miongoni mwa S.S. sehemu kubwa walikuwa waamini walioendelea kuwa waaminifu kwa mafungamano yao ya Kikristo mpaka mwisho? Kwamba walikuwako wauaji ambao walikwenda kuungama katikati ya machinjo yale? Na kwamba wote walitoka kwa familia za Kikristo na walikuwa wamepokea elimu ya Kikristo?”
Si ajabu, basi, kwamba viongozi wa makanisa wamelazimika kukadiria upya msimamo wao kuelekea Uyuda. Theolojia mpya inatokea ambayo katika hiyo Wayahudi hawasemwi tena kuwa ‘wauaji wa Kristo’ au kuwa ‘watu waliolaaniwa’ bali wanapewa utambuzi na heshima. Hata inasemwa kwamba Ukristo na Uyuda huenda vikatumika kuwa vijia mbalimbali vya kwenda kwa Mungu.’
Je, “Enzi Mpya” Inaanza?
Matukio hayo yameshangiliwa na wengine kuwa mwanzo wa “enzi mpya kabisa katika mahusiano” kati ya Wayahudi na Wakristo. Rabi Leon Klenicki hata alijulisha wazi kwamba Wayahudi wapaswa sasa “wafikirie maana ya Yesu na utume wa Ukristo kuwa njia ya kuipeleka jamii yote ya wanadamu kwa Mungu.” Aliongeza hivi: “Labda analotaka Mungu ni jitihada ya ushirikiano.”—The New York Times, Julai 24, 1988.
Lakini si wote walio na maoni ya kutazamia mema. Wanatheolojia Waevanjeliko katika Jumuiya ya Wakristo wanayaona maoni hayo mapya ya uvumilivu kuelekea Uyuda kuwa ni kuacha fundisho la msingi la Ukristo. Vilevile viongozi wengi Wayahudi wanatilia shaka semi hizo za kutaka amani, wakiziona kuwa zisizoeleweka na zenye kupingana au kuwa namna mpya tu ya ile hila ya kikale ya kutaka kuwaongoa Wayahudi.
Ili kuwe na mapatano ya kweli, viongozi Wayahudi waamini kwamba lazima Jumuiya ya Wakristo ikatae katakata bila masharti yoyote miongozo yayo ya kupinga Usemiti, kutia na daraka layo katika hilo Teketezo la Umati. Wanadai kwamba viongozi wa kanisa waondolee mbali kabisa lile wazo la kwamba Wayahudi wanalaumika kwa kifo cha Yesu. Wataka Uyuda utambuliwe kuwa njia halali ya wokovu, na si utangulizi tu wa Ukristo. Wataka Jumuiya ya Wakristo ikomeshe jitihada zote za kuwaongoa Wayahudi. Na hatimaye, wengi wanadai kwamba Jumuiya ya Wakristo itambue kikamili na kuunga mkono Taifa la Israeli.
Lakini kama vile makala inayofuata itakavyoonyesha, hata kama hatua hizo zisizo za kawaida zingechukuliwa, bado pengo kubwa lingebaki.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Jumuiya ya Wakristo haiwezi kukana lawama layo katika lile Teketezo la Umati
[Hisani]
Bundesarchiv Koblenz