“Zawadi Iliyo Kubwa Zaidi”
WAZAZI ambao hufanya jitihada kulea watoto wao wawe na staha, watiifu kwa sheria, na wanaohofu Mungu hupendezwa sana wachanga wao waonyeshapo uthamini wao kwa ajili ya jitihada zao. Hili ni kweli hasa katika hizi “siku za mwisho” ambapo mmojapo ya ishara za nyakati hizi ni kuenea sana kwa ‘kutokutii wazazi.’—2 Timotheo 3:1, 2.
Nancy, mwanafunzi wa sekondari mwenye umri wa miaka 15, alilelewa na wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova. Siku moja mwalimu wake wa Kiingereza alipatia darasa mgawo wa kuandika juu ya zawadi iliyo kubwa zaidi ambayo wamepata kupokea. Inayofuata ni ile Nancy aliandika, chini ya kichwa “Zawadi Iliyo Kubwa Zaidi”:
“Kuna aina nyingi za zawadi na utoaji. Kuna zawadi za upendo, marafiki, na vipawa. Pia, kuna zawadi ambazo hautaki, kama vile chuki na umaskini. Kuna aina ya watoaji wengi. Wale ambao hutoa kichoyo na wale ambao hutoa kwa sababu wanataka. Zawadi iliyo bora ambayo nilipokea ni zawadi aliyonipa baba yangu, zawadi ya maarifa kumhusu Mungu.
“Zawadi hii ni ile itakayodumu maishani, si kama zawadi nyingine ambazo zitatupwa zichakaapo. Mambo niliyojifunza yatakaa ndani yangu maishani mwangu na kuchochea lolote nitakalofanya. Kwa kujifunza juu ya Mungu wa Biblia, nimepata kumjua kibinafsi akiwa rafiki, akiwa rafiki ninayemtegemea na kumheshimu.
“Hadi kifo cha baba yangu mwaka huu, nilikuwa nikimwendea kwa mwongozo. Wengine pia walifanya hivyo. Mara nyingi sikumwona baba yangu alipotoka kazini kwa kuwa aliwatembelea wengine na kuwapa msaada waliokuwa hospitalini. Sasa naweza kutambua jinsi kutoa wakati kwake kulivyokuwa. Ingawa hayuko pamoja nami sasa ili kunipa msaada na mwongozo ninaohitaji, naweza kumtegemea Baba yangu wa kimbingu kwa mambo ninayohitaji maishani mwangu.
“Naithamini zawadi hii sana, na namshukuru Mungu kwa kunipatia baba imara na mwaminifu kama huyo. Mfano wake utakuwa na athari ya milele kwangu. Kwa kufaa, nitaweza kuonyesha uthamini wangu ninapokuwa mkubwa na kufuata mfano ambao baba yangu aliniachia.
“Maarifa ya Mungu ndiyo zawadi ya thamani zaidi na itabaki kuwa hivyo wakati wote, na nawashukuru wazazi wangu wote wawili kwa kunipatia zawadi hii. Mfano wao mzuri wa uaminifu utabaki nami siku zote.”
Insha hii ilithaminiwa na mwalimu, ambaye alisema kwamba ilimgusa sana, na akaisomea darasa. Alisahihisha karatasi kwa alama mbili za A, moja ya yaliyomo, na nyingine ya sarufi na vituo.
Mama ya Nancy pia alithamini insha hiyo. Yeye alisema: “Ilinipendeza sana. Kutojua jinsi watoto wako huhisi wakati wote, kulinisaidia nielewe kwamba Nancy anafanya maendeleo na anakubali mambo kadiri awezavyo.”