Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 12/15 kur. 4-7
  • Je, Una Roho ya Kutoa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Una Roho ya Kutoa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Watafuta Kibali cha Mtu Fulani?
  • Je, Hiyo Zawadi Yatoka kwa Moyo wa Kupenda?
  • Hangaiko Lako Kubwa—Je, Ni Tukio? Au Ni Wonyesho wa Upendo?
  • Ukarimu wa Mwaka Mzima
  • Jitihada za Kutafuta Zawadi Bora
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • “Ilikuwa Zawadi Bora Niliyowahi Kupokea”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Zawadi Bora Zaidi ya Mungu​—Kwa Nini Ni Yenye Thamani Sana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • “Zawadi Iliyo Kubwa Zaidi”
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 12/15 kur. 4-7

Je, Una Roho ya Kutoa?

JE, UMEONA kwamba kuna zaidi ya roho moja ambayo husukuma watu kutoa? Zawadi huenda ikawa wonyesho wa upendo, wa ukarimu, na wa uthamini. Hata hivyo, je, hujaona kwamba zawadi huenda pia ikatokana na tamaa ya mtu ya kutaka kukubaliwa? Au huenda ikatolewa tu kwa sababu ya kuhisi daraka au kwa sababu mtoaji naye ataka kitu.

Zawadi hiyo huenda ikawekwa ndani ya furushi lililozungushiwa utepe wa rangi maridadi. Lakini je, si kweli kwamba zawadi nzuri huenda pia ikawa shada la maua, sahani ya chakula, au tendo la fadhili? Kwa kweli, zawadi ambazo huthaminiwa sana mara nyingi huhusisha kujitoa kwa mtu binafsi.

Je, Watafuta Kibali cha Mtu Fulani?

Ni jambo la kawaida kwa mtu fulani kumtolea zawadi yule ambaye kibali chake kinatafutwa. Katika nchi fulani mwanamume mchanga anayetafuta kumpata msichana anayetazamia kumuoa huenda akampelekea maua. Hata hivyo mwanamke mwenye hekima hufikiria mengi zaidi kuliko zawadi hiyo. Yeye hufikiria kama hiyo roho ya kutoa zawadi inayomsukuma huyo mwanamume kijana ni yenye upendo itakayomfanya pia awe mume mwema. Zawadi kama hiyo, ikionyesha roho ya kimungu, inaweza kuongoza kwenye furaha nyingi kwa mwenye kutoa na mwenye kupokea.

Biblia husema juu ya pindi moja ambapo Abigaili, mke wa Nabali, alitayarisha upesi zawadi ya ukarimu kwa Daudi, ambaye alimtambua kuwa aliyechaguliwa na Mungu kuwa mfalme wa Israeli wa wakati ujao. Abigaili pia alitafuta kibali. Mumeye alikuwa amemwonyesha Daudi madharau naye alikuwa amewagombeza vikali watu wa Daudi. Akiwa mkuu wa kikosi cha watu wenye silaha 400, Daudi alikuwa ameazimia kuangamiza Nabali na wote wa nyumba yake. Abigaili akaingilia mambo, akipeleka haraka zawadi ya ukarimu ya vyakula kwa Daudi na watu wake. Yeye mwenyewe akafika akiifuata zawadi hiyo, na baada ya kuomba msamaha kwa unyenyekevu kwa yale mume wake alikuwa amefanya, alidhihirisha uthibitisho wa kuwa mwenye ufahamu mwingi huku akisababu na Daudi.

Nia yake ilikuwa nzuri, nayo matokeo yalikuwa mazuri. Daudi alikubali zawadi yake akamwambia: “Haya! kwea kwa amani kwenda nyumbani kwako; tazama, nimeisikiliza sauti yako, nami nimeukubali uso wako.” Baadaye, baada ya kifo cha Nabali, Daudi hata akamposa Abigaili, naye akakubali kwa furaha.—1 Samweli 25:13-42.

Hata hivyo, katika hali fulani, kibali ambacho mtu hutafuta huenda kikahusisha wonyesho wa upendeleo, hata kupotosha haki. Katika hali hiyo, hiyo zawadi ni hongo. Mpaji hufikiri atafaidika, lakini yeye hujinyang’anya amani ya akili. Sikuzote kuna hatari ya kwamba wengine watapata kujua jambo hilo, na kwamba atahitaji kutoa sababu. Hata akipewa kibali kinachotamaniwa, yule aliyekitafuta huenda akaona kwamba sasa anatambuliwa kuwa mtu ambaye madhumuni yake yanatiliwa mashaka. Ikionyesha hekima ya kimungu, Biblia huonya dhidi ya kutoa zawadi kama hizo.—Kumbukumbu la Torati 16:19; Mhubiri 7:7.

Je, Hiyo Zawadi Yatoka kwa Moyo wa Kupenda?

Hakuna shaka kwamba kumpa zawadi mtu umpendaye kwa sababu unataka kufanya hivyo huleta shangwe nyingi zaidi kuliko kutoa kwa sababu wengine wanakufanya uhisi kwamba unapaswa kufanya hivyo.

Kuhusu kukusanywa kwa ugavi wa misaada kwa ajili ya Wakristo wenzake waliokuwa wenye uhitaji kimwili, mtume Paulo aliweka kanuni fulani nzuri sana za utoaji wa kimungu. “Kama nia ipo,” yeye akaandika, “hukubaliwa kwa kadiri ya alivyo navyo mtu, si kwa kadiri ya asivyo navyo.” Yeye aliongeza hivi: “Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.” (2 Wakorintho 8:12; 9:7) Hivyo, mengi yakutegemea. Badala ya kuingia katika deni kwa sababu ya utoaji wa zawadi uliopita kiasi, je, wewe hutumia pesa kulingana na bajeti yako? Badala ya kuhisi kwamba unalazimika kutoa kwa sababu tu ya mkazo wa kijamii au wa kibiashara, je wewe hufanya uliloazimia moyoni mwako? Kuhusu Wakristo wa mapema waliotumia kanuni kama hizo za kimungu, Paulo aliandika hivi: “Wakituomba sana pamoja na kutusihi kwa habari ya neema hii, na shirika hili la kuwahudumia watakatifu.”—2 Wakorintho 8:4.

Tofauti na hilo, Royal Bank Letter ya Novemba/Desemba 1994 ilisema hivi kuhusu majuma ambayo hutangulia Krismasi: “Hiyo pindi huenda ikaonekana kama hali ya msisimuko wa bandia wenye kuchochewa na faida za kibiashara ili kusihi wanunuaji wanunue vitu ambavyo kwa kawaida hawangenunua.” Ununuzi ukifanywa kwa mkopo, uradhi wowote ule uletwao na kutoa zawadi huenda upesi ukamalizwa wakati bili ni lazima zilipwe.

Hangaiko Lako Kubwa—Je, Ni Tukio? Au Ni Wonyesho wa Upendo?

Je, umeona kwamba wewe hutoa zawadi sanasana wakati pindi fulani huonekana kudai hivyo? Ikiwa ndivyo, huenda unakosa shangwe nyingi ambayo kutoa kwa moyo kwaweza kuleta.

Kuna watu wengi ambao hawapendezwi na matokeo ya kutoa zawadi katika siku hususa. Mama mmoja ambaye pia ni mwandikaji alikiri kwamba pupa ilionekana wazi katika watoto wake siku ilipokaribia ya kutoa zawadi zilizotarajiwa. Yeye alikubali kwamba kufurahia kwake mwenyewe zawadi yenye kupendeza iliharibiwa kwa sababu alikuwa ametumaini kitu kingine. Ripoti nyingi husema kwamba sikukuu zenye sherehe na kupeana zawadi vilevile ni nyakati ambapo wengi hushuka moyo na kutumia vibaya kileo.

Baada ya kutazama mkazo unaotiliwa kutoa zawadi wakati wa sikukuu nyakati nyingi huathiri watoto vibaya, profesa wa saikolojia aliyenukuliwa katika The New York Times apendekeza hivi: “Fikiria kutoa zawadi siku nyinginezo tofauti ili kupunguza mkazo.” Je, wafikiri hilo lingekuwa na matokeo mazuri?

Tammy, mwenye umri wa miaka 12 aliye katika familia isiyosherehekea Krismasi na siku za kuzaliwa, aliandika hivi: “Inafurahisha zaidi kupokea zawadi usipoitazamia.” Yeye alisema kwamba badala ya kutoa zawadi mara moja au mara mbili tu kwa mwaka, wazazi wake humpa yeye na ndugu yake zawadi wakati wowote wa mwaka. Lakini kuna kitu fulani ambacho ni muhimu hata zaidi kwake kuliko zawadi hizo. Kama asemavyo, “Nina maisha ya familia yenye furaha sana.”

Kitabu Secrets of Strong Families kilieleza hivi waziwazi: “Wengi wetu hutumia wakati mwingi na pesa nyingi mara kwa mara mwakani tukichagua zawadi bora kabisa za siku za kuzaliwa, makumbusho ya kila mwaka, au kwa sikukuu za watu tuwapendao. Zawadi bora zaidi ya zote haigharimu pesa. Nawe huhitaji kuifunga. Ikiwa unaamini, kama watu wengi wanavyoamini, kwamba uhai wako ndio kitu chenye thamani kabisa ulicho nacho, basi uhai wako ndio zawadi yenye thamani kabisa unayohitaji kutoa. Sisi hutoa zawadi hiyo yenye thamani kwa kadiri ya wakati tutoao kwa wapendwa wetu.”

Unaweza kufanya kutoa kuwe zaidi ya familia yako mwenyewe. Kutoa kwa moyo ili kujazia uhitaji ulio dhahiri wa wengine kwaweza kuleta uradhi wa pekee. Yesu Kristo alitusihi tuonyeshe upendo huo wenye hangaiko kwa walio maskini, viwete, na vipofu, akiongezea hivi: “Utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa.”—Luka 14:12-14.

Rockland Journal-News (Marekani) majuzi liliripoti mfano mmoja wa kutoa kwa aina hiyo. Wakati nyumba ya mwanamke fulani mzee-mzee aliye kipofu ilipoanguka, marafiki walimjengea nyumba mpya. Upaji ulitolewa na makampuni kadhaa ya sehemu hiyo, na upaji wa pesa ulitolewa na idara fulani ya sehemu hiyo ya serikali. “Hata hivyo, la muhimu kabisa,” hilo gazeti likasema, “wale watu wapatao 150, wengi wao wakiwa wahudhuriaji wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Haverstraw, walitoa wakati ili kujenga hiyo nyumba.”

Hiyo makala iliendelea kusema: “Kwenye mahali pa ujenzi kulikuwa na marundo ya vifaa kando ya meza zilizojaa chakula. Katika siku mbili wafanyakazi walikuwa wamejenga nyumba ya familia mbili, yenye orofa tatu. . . . Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa uwezo wao wa kujenga majengo upesi. . . . Ingawa hivyo, uharaka huo ni tofauti na udumifu wa utume wao: kuandaa udumifu katika kazi ya upendo. Bi. Blakely huenda asiweze kuona nyumba yake mpya, lakini mikono yake yaweza kuihisi, nao moyo wake unajua kina cha hisia ambazo zimesukuma tendo hilo la kujinyima.”

Ukarimu wa Mwaka Mzima

Wale walio wakarimu kwelikweli rohoni hawangoji siku za pekee. Maisha yao hayategemei ubinafsi tu. Wapokeapo kitu kizuri, wao hufurahia kukishiriki na wengine. Hilo halimaanishi kwamba wao wana ushurutisho wa kutoa zawadi. Hiyo haimaanishi kwamba wao hutoa kwa kiasi cha kwamba familia zao hubaki bila kitu. Haimaanishi kwamba wao hutoa bila kufikiria matokeo kwa mwenye kupokea. Hata hivyo, wao ni watu ambao ‘huzoea kutoa,’ kama vile Yesu alivyofundisha wanafunzi wake kufanya.—Luka 6:38, New World Translation.

Wao wanajua hali za marafiki na majirani walio wazee-wazee, walio wagonjwa, au wanaohitaji kitia-moyo. “Zawadi” yao huenda ikawa kwenda kununua vitu dukani au kusaidia katika kazi za nyumbani. Huenda ikawa kukata miti au kuondoa theluji kwa kolego. Yaweza kuwa bakuli la chakula kilichotayarishwa au muda wa saa moja wa kumtembelea huyo na kusoma pamoja naye. Maisha zao wenyewe huenda zikawa na shughuli nyingi lakini si zenye shughuli nyingi mno hata wasisaidie wengine. Wamejifunza kutokana na maono kwamba kwa kweli “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.

Bila shaka, Mtoaji aliye mkubwa zaidi ya wote, ni Muumba, Yehova Mungu. Yeye “ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Katika Biblia, yeye pia hutuandalia ufahamu wenye kina juu ya kusudi lake la kukomesha uovu, ugonjwa, na kifo, na kufanya dunia hii kuwa paradiso. (Zaburi 37:10, 11; Ufunuo 21:4, 5) Baada ya kujifunza juu ya hilo, wale wenye roho ya ukarimu hawanyamazi na hiyo habari njema. Jambo moja linalowapendeza zaidi ni kuishiriki na wengine. Kwa kweli wana roho ya kutoa ya kimungu. Je, hiyo ndiyo roho unayositawisha?

[Picha katika ukurasa wa7]

Baadhi ya zawadi zenye thamani sana hazigharimu pesa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki